-
Nimepata Mambo Mengi MazuriMnara wa Mlinzi—2011 | Aprili 15
-
-
Kisha, jambo lingine zuri likafanyika mwaka wa 1958: Tulipewa mgawo wa kufanya kazi ya mzunguko.
Wakati huo, kulikuwa na mizunguko miwili tu midogo katika nchi yote. Kwa hiyo, zaidi ya kutembelea makutaniko, tulitumia majuma mengi katika mwaka tukihubiri katika miji midogo ya Wahindi ambayo haikuwa na Mashahidi. Kwa kawaida wageni waliotembelea miji hiyo (pueblos) waliishi katika vyumba vidogo visivyo na madirisha vyenye kitanda kimoja bila kitu kingine chochote. Tulibeba sanduku la mbao ambalo lilikuwa na jiko linalotumia mafuta ya taa, lilikuwa pia na sufuria, sahani, beseni, mashuka, chandarua cha mbu, nguo, magazeti ya zamani, na vitu vingine. Tulitumia magazeti hayo kuziba mashimo kwenye ukuta ili iwe vigumu kwa panya kuingia.
Ingawa vyumba hivyo vilikuwa vichafu na vyenye giza, tunakumbuka vizuri mazungumzo tuliyokuwa nayo wakati wa usiku tukiwa tumeketi kwenye kitanda, tukila chakula chepesi tulichokuwa tumekipika kwa jiko letu la mafuta. Kwa sababu kiasili mimi ni mtu mwenye msisimko, mara nyingi nilizungumza kabla ya kufikiri, nyakati nyingine mke wangu angetumia pindi hizo zenye utulivu kunitajia njia za busara ambazo ningetumia ili kujieleza vizuri kwa ndugu tuliowatembelea. Nilimsikiliza na hivyo ziara zangu zikawa zenye kutia moyo zaidi. Pia, nilipozungumza vibaya kuhusu mtu fulani bila kufikiri, mke wangu alikataa kushiriki katika mazungumzo hayo. Hivyo, nilijifunza kuwa na mtazamo unaofaa kuwaelekea ndugu zangu. Ingawa hivyo, mara nyingi mazungumzo yetu wakati wa usiku yalihusu mambo ambayo tulikuwa tumejifunza katika gazeti la Mnara wa Mlinzi na mambo ambayo tulikuwa tumejionea katika utumishi wa shambani siku hiyo. Kwa kweli, tulijionea mambo yenye kusisimua kama nini!
Jinsi Tulivyompata Carlos
Katika mji wa Jipijapa, magharibi mwa Ekuado, tulipewa jina la mtu anayependezwa—jina peke yake, Carlos Mejía, lakini hatukuambiwa mahali anapoishi. Tulipoondoka kwenye chumba chetu cha kukodi asubuhi hiyo, hatukujua tungeanzia wapi kumtafuta, kwa hiyo tulianza tu kutembea. Tulilazimika kuruka mashimo mengi yenye matope kwenye barabara za udongo kwa sababu ya mvua kubwa iliyokuwa imenyesha usiku uliotangulia. Nilikuwa nikitembea mbele ya mke wangu wakati niliposikia kwa ghafula mtu akilia nyuma yangu kwa sauti na kuniomba msaada, “Art!” Niligeuka na kumwona Edie akiwa ametumbukia ndani ya matope meusi yaliyofika kwenye magoti yake. Jambo hilo lilikuwa la kuchekesha sana hivi kwamba ningecheka lakini sikucheka kwa sababu machozi yalikuwa yakimlenga-lenga.
Nilifanikiwa kumvuta Edie kutoka ndani ya shimo hilo, lakini viatu vyake vilibaki ndani ya matope hayo. Kando yetu kulikuwa na mvulana na msichana ambao walikuwa wakitutazama, hivyo nikawaambia: “Nitawapa pesa ikiwa mtatoa viatu vilivyo ndani ya matope.” Papo hapo wakavitoa viatu hivyo, lakini Edie alihitaji mahali pa kusafisha miguu yake. Mama ya watoto hao alikuwa akitazama kilichokuwa kikiendelea na akatukaribisha ndani ya nyumba yake, ambako alimsaidia mke wangu kusafisha miguu yake huku watoto wakisafisha vile viatu vichafu. Kabla hatujaondoka, jambo zuri lilitokea. Nilimuuliza mwanamke huyo ikiwa alijua mahali ambapo tungempata mwanamume anayeitwa Carlos Mejía. Alisema hivi kwa mshangao: “Yeye ni mume wangu.” Baada ya muda tulianzisha funzo la Biblia, na mwishowe washiriki wote wa familia hiyo wakabatizwa. Miaka mingi baadaye, Carlos, mke wake, na wawili kati ya watoto wao wakawa mapainia wa pekee.
Safari Ngumu—Ukarimu Wenye Kugusa Moyo
Tulipambana na hali ngumu katika kazi ya kusafiri. Tulisafiri kwa mabasi, magari-moshi, malori, mitumbwi au boti, na ndege ndogo. Wakati mmoja tulienda kuhubiri kwenye vijiji vya wavuvi vilivyo karibu na mpaka wa Kolombia pamoja na John McLenachan, aliyekuwa mwangalizi wa wilaya, na mke wake, Dorothy. Tulisafiri kwa mtumbwi wenye injini. Samaki wanaoitwa papa waliokuwa wakubwa kama mtumbwi wetu walikuwa wakiogelea kando yetu! Hata mwendeshaji-mtumbwi hodari tuliyekuwa naye alishtuka alipoona ukubwa wa papa hao na akaelekeza haraka mtumbwi karibu na ufuo.
Hata hivyo, tulipata matokeo mazuri sana hata ingawa tulikabili magumu katika kazi ya mzunguko. Tuliwafahamu ndugu wazuri sana, wenye ukarimu. Mara nyingi familia ambazo tuliishi nazo zilisisitiza kwamba tule chakula mara tatu kwa siku huku wao wakila mlo mmoja tu. Au walitukaribisha tulale kwenye kitanda kimoja tu katika nyumba yao, huku wao wakilala kwenye sakafu. Mara nyingi mke wangu aliniambia, “Ndugu na dada hawa wapendwa wananisaidia kuona kwamba kwa kweli tunahitaji vitu vichache maishani.”
-
-
Nimepata Mambo Mengi MazuriMnara wa Mlinzi—2011 | Aprili 15
-
-
Mwanzoni mwa miaka ya 1970, hali yangu ya afya ilikuwa nzuri zaidi na tukarudia kazi ya mzunguko. Mji wa Ibarra ulikuwa katika mzunguko wetu. Tulipotembelea mji huo mwishoni mwa miaka ya 1950 kulikuwa na Mashahidi wawili tu, yaani, mmishonari mmoja na ndugu mmoja mwenyeji. Kwa hiyo, tulitamani sana kukutana na watu wengi wapya ambao walikuwa wamejiunga na kutaniko hilo.
Katika mkutano wetu wa kwanza huko, Ndugu Rodrigo Vaca alisimama jukwaani na akaongoza sehemu ambayo ilihusisha mazungumzo pamoja na wasikilizaji. Kila alipouliza swali, wasikilizaji walisema kwa sauti “Yo, yo!” (“Mimi, mimi!”) badala ya kuinua mikono yao. Mimi na Edith tuliangaliana kwa mshangao. Nilijiuliza, ‘Ni nini kinachoendelea hapa?’ Baadaye tuliambiwa kwamba Ndugu Vaca ni kipofu lakini anatambua sauti za washiriki wa kutaniko wanaposema kwa sauti. Yeye ni mchungaji ambaye kwa kweli anawajua kondoo wake! Hilo lilitukumbusha maelezo ya Yesu katika andiko la Yohana 10:3, 4, 14 kuhusu jinsi Mchungaji Mwema anavyowajua vizuri sana kondoo na jinsi wanavyomjua. Leo, mji wa Ibarra una makutaniko sita yanayozungumza Kihispania, kutaniko moja la lugha ya Quichua, na kutaniko moja la lugha ya ishara. Ndugu Vaca anaendelea kutumika kwa uaminifu akiwa mzee na painia wa pekee.a
-
-
Nimepata Mambo Mengi MazuriMnara wa Mlinzi—2011 | Aprili 15
-
-
[Picha katika ukurasa wa 31]
Kutembelea familia ya Mashahidi tulipokuwa tunafanya kazi ya mzunguko, 1959
-