Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Unaweza Kupata Wapi Elimu Bora Zaidi?
    Amkeni!—2000 | Desemba 22
    • Leo kazi isiyo na kifani ya kutoa elimu ya Biblia inaendeshwa ulimwenguni pote na jamii ya Kikristo ya Mashahidi wa Yehova. Elimu hiyo inatia ndani mengi zaidi ya kufundisha kusoma na kuandika tu. Inatokeza maendeleo ya kiakili na ya kiadili. Inaathiri mtazamo wa watu kuhusu wakati ujao kwa njia yenye kujenga, na kuandaa msingi wa kuwa na tumaini lifaalo la wakati ujao la kwamba hali ya wakati ujao itakuwa bora kuliko ya wakati uliopita.

      Tafadhali jifunze kuhusu programu hiyo ya elimu inayoongoza kwenye uhai kwa kusoma makala ifuatayo.

  • Programu ya Elimu Yenye Matokeo Makubwa
    Amkeni!—2000 | Desemba 22
    • Programu ya Elimu Yenye Matokeo Makubwa

      “Walioelimika tu ndio walio huru.”—Epictetus, karibu na mwaka wa 100 W.K.

      MWANAHARAKATI wa kupinga utumwa William H. Seward aliyeishi karne ya 19, aliamini kwamba “tumaini lote la maendeleo ya wanadamu lategemea uvutano unaoongezeka wa Biblia.”

      Mashahidi wa Yehova pia wanaiheshimu sana Biblia. Wanasadiki kwamba wale wanaotumia kanuni zake huwa waume bora, wake bora, watoto bora—naam, watu bora zaidi ulimwenguni. Kwa hiyo wao hutii amri hii ya Yesu Kristo: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . [na] kuwafundisha.”—Mathayo 28:19, 20.

      Ili kutimiza lengo hilo la kuwafundisha watu Biblia, Mashahidi wa Yehova wanatekeleza ile inayoweza kuwa kampeni ya elimu iliyoenea sana katika historia yote ya wanadamu. Ina matokeo makubwa kadiri gani?

      Kazi ya Uchapishaji ya Ulimwenguni Pote

      Katika huduma yao ya peupe, Mashahidi hutumia tafsiri za Biblia zinazopatikana katika mamia ya lugha. Lakini wamechapisha pia New World Translation of the Holy Scriptures katika lugha 21 na Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo (yale yanayoitwa Agano Jipya) katika lugha nyingine 16. Pia, bado wanaendelea kutafsiri Biblia hiyo katika lugha 11 zaidi. Mashahidi pia huchapisha vichapo vinavyositawisha uthamini kuelekea Biblia na kuchangia uelewevu bora wa Biblia.

      Kwa mfano, jarida hili la Amkeni! huchapishwa katika lugha 82, na wastani wa zaidi ya nakala 20,380,000 za kila toleo huchapishwa. Gazeti-jenzi lake, Mnara wa Mlinzi, huchapishwa kwa wastani nakala 22,398,000 za kila toleo katika lugha 137. Jumla ya nakala zaidi ya bilioni moja za magazeti hayo huchapishwa kila mwaka! Isitoshe, Mnara wa Mlinzi huchapishwa sambamba katika lugha 124 na Amkeni! katika lugha 58. Hivyo basi, habari zilizo katika majarida hayo husomwa ulimwenguni pote na watu wa lugha nyingi mbalimbali wakati uleule katika lugha zao.

      Kwa kuongezea, katika miongo ya karibuni Mashahidi wa Yehova wamechapisha mamia ya mamilioni ya nakala za vichapo vya kujifunzia Biblia. Nakala zaidi ya milioni 107 za kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele zilichapishwa. Baadaye, nakala zaidi ya milioni 81 za kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani zilichapishwa, na hivi karibuni, zaidi ya nakala milioni 75 za kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele zimechapishwa katika lugha 146. Pia, zaidi ya nakala milioni 113 za broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? yenye kurasa 32 zimechapishwa katika lugha 240.

      Vitabu vingine vimechapishwa ili kutimiza mahitaji mahususi. Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, kinachokusudiwa watoto, kimechapishwa kwa zaidi ya nakala milioni 51. Vitabu viwili vilivyotayarishwa hususan kwa ajili ya vijana, Kupata Faida Zote za Ujana Wako na Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, vimechapishwa kwa zaidi ya nakala milioni 53 kwa ujumla. Na kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, ambacho kimesaidia mamilioni ya familia kukabiliana na matatizo yao, kimechapishwa katika lugha 115.

      Jumla ya zaidi ya nakala milioni 117 za vichapo vingine vinne vilivyotolewa tangu mwaka wa 1985 ambavyo hujenga imani hasa katika Muumba, Mwanaye, na katika Biblia vimechapishwa. Vichapo hivyo ni Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation?, Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi, Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?, na Je, Kuna Muumba Anayekujali?

      Leo vichapo vinavyotegemea Biblia vinavyochapishwa na Mashahidi wa Yehova vinapatikana katika lugha 353, na baadhi yake vitatolewa hivi karibuni katika lugha nyingine 38. Kwa kweli, Mashahidi wa Yehova wamechapisha vitabu, vijitabu, broshua, na magazeti zaidi ya bilioni 20 tangu mwaka wa 1970! Isitoshe, takriban walimu milioni sita wanajitahidi kueneza ujuzi wa Biblia katika nchi zaidi ya 230. Lakini yote hayo yamewezekanaje, na maisha ya watu yameathiriwaje?

      Kwa Nini Viwe Katika Lugha Yao Wenyewe?

      Kama uwezavyo kuwazia, ili kuchapisha sambamba vichapo vya hali ya juu katika lugha zaidi ya mia moja, jitihada na utaratibu mkubwa unahitajika. Vikundi vya watafsiri, ambao wamedhabihu wakati wao na ujuzi wao, hutumia mifumo ya kompyuta ili kuweza kufanya kazi bora sana iliyo sahihi na kwa mwendo wa kasi. Kwa hiyo, hata lugha ambazo zina watafsiri wachache, vichapo hutayarishwa haraka. Hivi sasa, zaidi ya wanaume na wanawake 1,950 hufanya kazi hii ya kutafsiri ya ulimwenguni pote bila malipo. Lakini kwa nini jitihada hiyo hufanywa? Je, jitihada hizo zafaa, kwa kuwa watu wengi wanaosema lugha zisizojulikana sana wanajua angalau lugha moja maarufu?

      Mashahidi wa Yehova wamegundua kwamba jitihada zao zinafaa kikweli kupatana na sababu iliyotajwa na William Tyndale, mtafsiri maarufu wa Biblia wa karne ya 16. Aliandika hivi: “Nilithibitisha mwenyewe kwamba haingewezekana kuwasaidia watu wa kawaida kufahamu mafundisho ya kweli ya Biblia, isipokuwa waandaliwe maandiko ili wajisomee wenyewe moja kwa moja katika lugha yao ya mama, na kupata kuelewa somo kuu, mpangilio, na maana ya maandiko hayo.”

      Ni kweli kwamba sikuzote haiwezekani kwa watu kupata vichapo vya Biblia katika lugha yao ya mama. Lakini wanapopata vichapo hivyo, kweli za Biblia hugusa mioyo yao upesi zaidi na hupenya zaidi. Hilo limeonekana katika nchi za ule uliokuwa Muungano wa Sovieti ambako wakazi wa huko huzungumza lugha nyingi za kienyeji. Mwanzoni mwa karne iliyopita, wengi kati yao walifanywa kuwa sehemu ya Muungano wa Sovieti na kufundishwa—na kulazimika kutumia—lugha ya Kirusi. Hivyo, walisoma na kuandika Kirusi na, wakati huohuo, walizungumza lugha yao ya kienyeji.

      Hasa tangu kuporomoka kwa Muungano wa Sovieti mwaka wa 1991, wengi wao wanapenda kutumia lugha yao ya mama. Ndivyo ilivyo kwa wale ambao lugha yao ya kienyeji ni Kiadige, Kialtai, Kibelorusi, Kigeorgia, Kikirghizi, Kikomi, Kioseti, Kituvinia, au lugha yoyote ile kati ya nyingine nyingi. Ijapokuwa wengi wao wanaweza kuzungumza Kirusi, vichapo vya Biblia vya Kirusi havigusi mioyo yao kwa wepesi. Kwa upande mwingine, vichapo vya lugha zao za kienyeji huweza kuvutia watu wengi. “Ni vyema kwamba mmeanza kuchapisha vichapo katika lugha yetu,” akasema mtu mmoja aliyepokea trakti ya Biblia ya Kialtai.

      Mfano mwingine ni Greenland, kisiwa cha Aktiki chenye takriban watu 60,000 tu. Mnara wa Mlinzi na Amkeni! huchapishwa katika lugha ya Greenland, na magazeti hayo yanapendwa sana—sawa na vichapo vingine vinavyochapishwa na Mashahidi wa Yehova katika lugha ya Greenland. Kwa kweli, vichapo hivyo vyaweza kupatikana katika nyumba nyingi katika vijiji vilivyo mbali sana kisiwani.

      Kusini ya Pasifiki, watu wapatao 7,000 huzungumza Kinauru, 4,500 Kitokelau, na 12,000 Kirotuma. Sasa Mashahidi huchapisha trakti za Biblia na broshua katika lugha hizo na vilevile matoleo ya kila mwezi ya Mnara wa Mlinzi katika Kiniue, lugha inayozungumzwa na watu 8,000 hivi, na Kituvalu, kinachozungumzwa na watu wapatao 11,000. Kwa kweli, Mashahidi wa Yehova ni mojawapo wa wachapishaji wakuu zaidi wa vichapo katika lugha zisizojulikana sana, wanachapisha vichapo vya Biblia katika lugha kama vile Kibislama, Kihiri Motu, Kipapiamento, Kikreoli cha Mauritius, Kipijini cha New Guinea, Kikreoli cha Shelisheli, Kipijini cha Visiwa vya Solomon, na lugha nyinginezo nyingi.

      Mara nyingi kadiri watu wazungumzao lugha fulani walivyo wachache, ndivyo jamii zao zinavyokuwa maskini zaidi na kuishi maeneo yaliyojitenga sana. Lakini idadi ya wanaojua kusoma na kuandika katika maeneo hayo yaweza kuwa kubwa sana. Na kwa kawaida Biblia ya lugha za wenyeji huwa mojawapo ya vichapo vichache sana vinavyopatikana kwa wakazi wenyeji. Kwa kweli, hakuna gazeti hata moja linalochapishwa katika baadhi ya lugha hizo, kwa kuwa kuchapisha gazeti lolote lile hakuwezi kuleta faida kibiashara.

      Kinachofanya Kazi Hiyo Ithaminiwe

      Watu wengi husifu jitihada za kutafsiri za Mashahidi wa Yehova kwa sababu wao huandaa vichapo vinavyoboresha maisha ya watu. Linda Crowl, mfanyakazi katika Taasisi ya Pacific Studies, iliyo katika Chuo Kikuu cha South Pacific huko Suva, Fiji, alisema kwamba kazi ya kutafsiri ya Mashahidi ndilo “jambo lenye kuvutia zaidi linalofanywa katika Pasifiki.” Anapendekeza vichapo vyao kwa sababu ya ubora wake wa hali ya juu.

      Wakati matoleo ya baada ya kila miezi mitatu ya Amkeni! yalipoanza kuchapishwa katika lugha ya Kisamoa, magazeti ya habari vilevile kituo cha taifa cha televisheni kilitangaza habari hizo. Wakati wa matangazo hayo jalada la Amkeni! lilionyeshwa, na kila makala ya gazeti hilo ilionyeshwa. Kisha makala hizo zikazungumziwa moja baada ya nyingine.

      Jambo la kutokeza ni kwamba katika nchi fulani taasisi za lugha huwasiliana kwa ukawaida na watafsiri wa vichapo vya Mashahidi kuhusiana na sarufi, tahajia, utohozi wa istilahi mpya, na kadhalika. Kwa wazi, kazi ya kutoa elimu ya bure inayofanywa na Mashahidi wa Yehova imeathiri maisha ya watu wengi zaidi ya wale ambao wamekuja kuwa washiriki wenye bidii wa makutaniko yao.

      Na bado, kama ilivyotajwa kwenye makala iliyotangulia, takriban watu wazima bilioni moja—karibu moja kwa sita ya watu wote ulimwenguni—hawajui kusoma wala kuandika. Ni hatua gani imechukuliwa ili kuwasaidia watu hao wanufaike na ujumbe muhimu unaopatikana kupitia kusoma na kujifunza?

      Kutimiza Mahitaji ya Msingi ya Elimu

      Katika nchi nyingi Mashahidi wamepanga programu za kuwafunza watu kujua kusoma na kuandika bila malipo. Hata wamechapisha vijitabu vyao wenyewe vya maagizo, kama vile kichapo Apply Yourself to Reading and Writing, ambacho kimechapishwa katika lugha 28. Maelfu ya watu, kutia ndani wanawake na wazeewazee, wamesaidiwa kujua kusoma na kuandika kupitia kwa madarasa hayo.

      Nchini Burundi, Mashahidi wa Yehova wameendesha madarasa ya kujua kusoma na kuandika ambayo yamesaidia mamia ya watu kujua kusoma na kuandika. Baada ya kupitia matokeo mazuri ya programu hiyo, Idara ya Taifa ya Shule za Ngumbaru nchini humo ziliwapa walimu wanne Mashahidi tuzo wakati wa Siku ya Kimataifa ya Kujua Kusoma na Kuandika, Septemba 8, 1999.

      Ripoti ifuatayo ilipokewa kuhusu madarasa ya kujua kusoma na kuandika katika makutaniko 700 ya Mashahidi wa Yehova nchini Msumbiji: “Kwa muda wa miaka minne iliyopita, wanafunzi 5,089 wamehitimu, na hivi sasa wanafunzi 4,000 wamejiandikisha.” Mwanafunzi mmoja aliandika hivi: “Ningependa kuonyesha uthamini wangu wa kutoka moyoni kwa ajili ya shule hiyo . . . Mimi sikujua chochote. Lakini shule hiyo imenisaidia kujua kusoma, na ijapokuwa ningali nahitaji kufanya mazoezi, naweza kuandika.”

      Tangu mwaka wa 1946, rekodi zilipoanza kuhifadhiwa huko Mexico, zaidi ya watu 143,000 nchini humo wamefundishwa kusoma na kuandika katika shule za pekee zilizoanzishwa kwa kusudi hilo. Mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 63 aliandika hivi: “Ninawashukuru sana Mashahidi wa Yehova, walionifunza kusoma na kuandika. Maisha yangu yalikuwa magumu sana. Hata hivyo, sasa naweza kusoma Biblia na kupata ushauri, na ujumbe wake umeniletea furaha.”

      Katika nchi ya Brazili huko Amerika Kusini, Mashahidi wamewafunza maelfu ya watu kusoma na kuandika. “Kujifunza kusoma kulikuwa kama kuwekwa huru kutokana na minyororo baada ya miaka mingi,” akasema mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 64. “Sasa naweza kusoma habari mbalimbali. Jambo la muhimu zaidi ni kwamba kusoma na kujifunza Biblia kumeniweka huru kutokana na mafundisho bandia.”

      Kwa kawaida walimu wa Biblia walio Mashahidi wa Yehova huwasaidia wanafunzi wao wakiwa mmoja-mmoja kujua kusoma. Nchini Filipino, Martina alikuwa na umri wa miaka 80 hivi alipotembelewa na Shahidi mmoja. Martina alitaka funzo la Biblia la kawaida, lakini hakujua kusoma. Kwa msaada wa mwalimu wake wa Biblia, pamoja na mazoezi ya ziada aliyopokea kutanikoni, Martina alifanya maendeleo na akastahili kuwafunza wengine Biblia. Leo yeye ni mwalimu wa Biblia wa wakati wote anayejua kusoma na kuandika.

      Ni dhahiri kwamba watu wote wana uwezo wa kujua kusoma na kuandika. Lakini twaweza kuuliza hivi, Je, ujuzi wa Biblia kuhusu Mungu na makusudi yake unawafaidi watu kwelikweli? Makala ya mwisho ya mfululizo huu itajibu swali hilo.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

      “Maneno Hayatoshi . . . ”

      Wenye mamlaka katika serikali, wana-taaluma, na watu wa kawaida wote wameona jitihada za Mashahidi wa Yehova za kuwaelimisha watu kotekote ulimwenguni. Haya ni baadhi ya maoni yao:

      “Serikali yangu na hususan mimi nimefurahi kwa sababu kitabu hiki [Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, katika Kituvalu] kimekuwa kifaa kingine cha ziada katika ‘urithi’ muhimu wa Tuvalu. Mwapaswa kuonea fahari fungu mlilotimiza—fungu bora katika kujenga hali ya kiroho ya watu wa taifa hili. Naamini kwamba kazi hiyo itaandikwa katika historia ya uchapishaji wa vitabu vya kielimu ya Tuvalu.”—Dakt. T. Puapua, aliyekuwa waziri mkuu wa Tuvalu, Pasifiki Kusini.

      “Mashahidi wa Yehova wana programu kabambe ya uchapishaji, inayotumia tekinolojia ya kisasa zaidi katika Pasifiki Kusini. . . . Kazi hiyo kubwa ya uchapishaji ni yenye kutokeza sana mtu afikiriapo hali hafifu ya mawasiliano . . . katika Visiwa vya Pasifiki.”—Linda Crowl, Chuo Kikuu cha Pasifiki Kusini, Suva, Fiji.

      “Kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia katika lugha ya Isoko ni kizuri na chenye uvutano kama nini! Twawashukuru wajitoleaji wanaotafsiri lugha ya Isoko kwa kutusaidia kuelewa kikamili kitabu hicho.”—C.O.A., Nigeria.

      “Siwezi kueleza jinsi nilivyo mwenye shukrani kwa ajili ya tafsiri hii ya Biblia [New World Translation katika Kiserbia], ambayo inaeleweka kwa urahisi. Hapo zamani, nilijaribu kusoma Biblia nzima, lakini sikuzote nilijikuta nikishindwa upesi kwa sababu sikuweza kuelewa lugha. Sasa naweza kusoma tafsiri hii ya pekee na kuielewa!”—J. A., Yugoslavia.

      “Asanteni kwa ajili ya vichapo vizuri, vyenye kufundisha, na vyenye kujenga vilivyotafsiriwa katika lugha ya Tiv. Kwa kweli, maneno hayatoshi kueleza manufaa yote na kitia-moyo kinachotokana na vitabu na broshua hizi. Vichapo hivyo vimefikia maelfu ya watu.”—P.T.S., Nigeria.

      [Picha]

      Nakala milioni 36 katika lugha 115

      [Picha katika ukurasa wa 4, 5]

      Zaidi ya nakala milioni 100 za “New World Translation” zimechapishwa katika lugha 37

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Ulimwenguni pote takriban watafsiri 2,000 hushiriki kutafsiri vichapo vya Mashahidi wa Yehova. (Watafsiri wa lugha ya Kizulu huko Afrika Kusini, kushoto; na mtafsiri Mjapani, chini)

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Zaidi ya magazeti bilioni moja ya “Mnara wa Mlinzi” na “Amkeni!” huchapishwa kila mwaka

      [Picha katika ukurasa wa 8]

      Madarasa ya kujua kusoma na kuandika huendeshwa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote (Mexico, kulia; na Burundi, chini. Ghana imeonyeshwa kwenye jalada letu)

  • Elimu Inayoongoza Kwenye Uhai
    Amkeni!—2000 | Desemba 22
    • Elimu Inayoongoza Kwenye Uhai

      “Biblia [ni] kiongozi bora zaidi katika ujuzi wa maisha.”—Thomas Tiplady, 1924.

      SI KUTILIA chumvi kusema kwamba elimu inayotegemea Biblia inaweza kugeuza maisha. Imewapa kusudi na tumaini wale waliokuwa wapweke na waliotamauka. Mzazi mmoja mwenye watoto kutoka nchini Namibia aliandikia ofisi ya tawi ya Afrika Kusini ya Mashahidi wa Yehova:

      “Nina umri wa miaka 29, nami nilisoma kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi kwa siku mbili tu. Kiligusa moyo wangu sana kwa sababu mimi ni mpweke kwelikweli. Rafiki yangu wa kiume alikufa kwenye aksidenti ya gari na kuniacha nikiwa na watoto wawili. Tunateseka sana. Nyakati nyingine nilikuwa nikiwaza kwamba ingekuwa heri kuwaua na kisha kujiua. Lakini nilipopokea kitabu hicho, nilibadili mawazo yangu. Tafadhali nisaidieni kupitia funzo la Biblia bila malipo.”

      Biblia ni kiongozi kinachoweza kuwasaidia watu wafanikiwe katika nyanja zote za maisha—katika mahusiano na familia zao, wafanyakazi wenzi, na watu katika jamii. (Zaburi 19:7; 2 Timotheo 3:16) Huandaa mwelekezo unaofaa kuhusu namna ya kufuatia lililo jema na kuepuka lililo baya. Ni kitabu kinachoshughulikia maisha kwa njia halisi. Unapoisoma, utagundua kwamba ina masimulizi chungu nzima ya watu halisi. Utaona kile kilichofanya maisha ya baadhi yao yawe yenye furaha na yenye kuthawabisha na ya wengine yawe machungu na yenye taabu. Hivyo utaelewa kinagaubaga mambo yanayofaa na yale yasiyofaa.

      Elimu Inayoongoza Kwenye Uhai Yatolewa Sasa

      Biblia hukazia umuhimu wa hekima inayotumika. Inasema: “Bora hekima, basi jipatie hekima.” (Mithali 4:7) Inakiri pia kwamba mara nyingi wanadamu hukosa hekima, na hivyo inaonya hivi kwa upole: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, acheni afulize kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu.”—Yakobo 1:5.

      Muumba wetu, Yehova Mungu, hupaje watu hekima kwa ukarimu? Yeye hufanya hivyo kupitia Neno lake, Biblia, na yeye hututia moyo tuisome. Mungu anasihi hivi: “Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; hata ukatega sikio lako kusikia hekima . . . , ndipo utakapofahamu kumcha BWANA, na kupata kumjua Mungu. Kwa kuwa BWANA huwapa watu hekima.” (Mithali 2:1, 2, 5, 6) Tunapotumia shauri lililo katika Neno la Mungu na kuona jinsi linavyotumika, tunang’amua kwamba kwa kweli linadhihirisha hekima ya kimungu.

      Mathalani, fikiria tatizo la kukabiliana na umaskini. Biblia inapendekeza bidii ya kazi na kuonya dhidi ya utendaji unaotapanya mali chache alizo nazo mtu. Hivyo basi, mazoea mabaya kama vile utumiaji wa tumbaku na kunywa vileo kupita kiasi kwa wazi hupingana na kanuni za Biblia.—Mithali 6:6-11; 10:26; 23:19-21; 2 Wakorintho 7:1.

      Marafiki wetu wanawezaje kuathiri maisha yetu? Biblia husema: “Enenda pamoja na wenye hekima nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.” (Mithali 13:20) Je, umeona kwamba msongo wa marika mara nyingi umewatumbukiza watu—wachanga kwa wazee—katika ulevi, matumizi mabaya ya dawa za kulevya, na ukosefu wa adili? Naam, tukishirikiana na watu wanaozoea mambo hayo, tutakuwa kama wao, ni kama Biblia inavyosema: “Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.”—1 Wakorintho 15:33.

      Bila shaka, sote tunataka kuwa wenye furaha. Lakini inawezekanaje? Je, unajua Biblia husema kwamba furaha yetu haitegemei vitu lakini, badala yake, hutegemea mitazamo na mahusiano yanayofaa, hasa uhusiano mzuri pamoja na Mungu? (1 Timotheo 6:6-10) Yesu Kristo, kwenye Mahubiri yake maarufu ya Mlimani, alisema kwamba walio na furaha kikweli ni wale “wenye kuona uhitaji wao wa kiroho,” “wenye tabia-pole,” “walio na kiu kwa ajili ya uadilifu,” “wenye rehema,” “wenye kutakata moyoni,” na “wenye kufanya amani.”—Mathayo 5:1-9.

      Unapofikiria kwa uzito kuhusu mafundisho ya Biblia, utathamini namna ambavyo yanaweza kutusaidia kuelekeza maisha yetu. Biblia ni chanzo cha pekee sana cha kutoa ushauri. Shauri lake hunufaisha sikuzote—si la kinadharia tu na haliwezi kamwe kutudhuru. Wale wanaotumia mashauri ya Biblia hunufaika daima.

      Elimu Inayoongoza Kwenye Uhai

      Kwa kuongezea, pamoja na kutunufaisha sasa hivi, Biblia huandaa tumaini la uhai wakati ujao. Hueleza kuhusu kuondolewa kwa uchafu wote duniani na kugeuzwa kwake kuwa makao maridadi sana kwa ajili ya wale wanaomtumikia Mungu. Zingatia maelezo haya yenye kuchangamsha moyo kuhusu wakati ujao: “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa vikundi vya watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:3, 4; Mithali 2:21, 22.

      Hebu wazia: Watoto wagonjwa-wagonjwa hawatakuwako tena, njaa haitakuwako tena, magonjwa hatari yanayodhoofisha mwili hayatakuwako tena, maumivu makali hayatakuwako tena! Machozi ya kuvunjika moyo, kukata tamaa, na huzuni yatatoweka, kwa kuwa hali zinazosababisha mambo hayo zitabadilishwa au kuondolewa. Kwa kuwa watu wanaofanya maovu kimakusudi wataangamizwa na jeshi la Mungu la malaika, wezi, wauaji, waongo, na wengineo wanaofanya maisha yasiwe salama hawatakuwako tena. Watu wataweza kuwa na nyumba zao nao wataishi humo kwa usalama.—Isaya 25:8, 9; 33:24; 65:17-25.

      Je, mambo hayo yanakuvutia? Je, ungependa kujifunza mengi zaidi kuhusu kutumia kanuni za Biblia ili uweze kujinufaisha sasa na hata wakati ujao? Ikiwa ndivyo, tafadhali wasiliana na Mashahidi wa Yehova, nao watafurahia kukuhusisha wewe na familia yako katika programu yao ya ulimwenguni pote ya “elimu inayoongoza kwenye uhai.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki