-
‘Aliendelea Kukua Akiwa na Yehova’Mnara wa Mlinzi—2010 | Oktoba 1
-
-
Samweli Hakuathiriwa na Upotovu Uliomzunguka
Alipokuwa na umri mdogo, Samweli alijionea upotovu na uovu mkubwa uliofanywa waziwazi. Eli alikuwa na wana wawili, Hofni na Finehasi. Simulizi la Samweli linasema: “Wana wa Eli walikuwa watu wasiofaa kitu; hawakumtambua Yehova.” (1 Samweli 2:12) Mawazo mawili yaliyo katika mstari huo yanapatana. Hofni na Finehasi walikuwa “watu wasiofaa kitu” kwa kuwa hawakumheshimu Yehova. Hawakufikiria kamwe kanuni na sheria zake za uadilifu. Jambo hilo lilikuwa chanzo kikuu cha dhambi walizotenda.
Sheria ya Mungu ilitaja waziwazi kazi za makuhani na jinsi walivyopaswa kutoa dhabihu katika madhabahu. Mungu alifanya hivyo kwa sababu nzuri! Dhabihu hizo ziliwakilisha mpango wa Mungu wa kusamehe dhambi ili watu wawe safi machoni pake, na kustahili kupata baraka na mwongozo wake. Lakini Hofni na Finehasi waliwaongoza makuhani wenzao kutoheshimu dhabihu zilizokuwa zikitolewa.c
Hebu wazia jinsi kijana Samweli alivyotazama uovu huo mkubwa uliokuwa ukiendelea bila kurekebishwa. Aliona watu wangapi—kutia ndani watu wapole, maskini, na waliokandamizwa—wakija katika hema takatifu la kukutania huku wakitumaini kufarijiwa na kutiwa moyo, lakini badala yake kuondoka wakiwa wamevunjika moyo, wameumia, au kuaibishwa? Na wazia jinsi alivyohisi alipotambua kuwa Hofni na Finehasi hawakutii sheria za Yehova kuhusu ngono, kwa kuwa walikuwa na uhusiano wa kingono na wanawake fulani waliokuwa wakitumika katika hema la kukutania? (1 Samweli 2:22) Huenda alitazamia Eli angechukua hatua fulani kuhusu jambo hilo.
Eli alikuwa na uwezo wa kutatua tatizo hilo lililokuwa linazidi kuwa baya. Akiwa kuhani mkuu, alikuwa na jukumu la kusimamia kila kitu kilichokuwa kikitendeka katika hema la kukutania. Pia akiwa baba, alikuwa na jukumu la kuwarekebisha watoto wake. Mambo hayo mabaya yaliwaumiza wao wenyewe na watu wengine wengi katika nchi hiyo. Hata hivyo, Eli alishindwa kutimiza majukumu yake, akiwa baba na akiwa kuhani mkuu. Aliwakaripia watoto wake kwa unyonge tu. (1 Samweli 2:23-25) Lakini watoto wake walihitaji nidhamu kali zaidi. Walikuwa wakitenda dhambi zilizostahili kifo!
Hali hiyo ilizidi kuwa mbaya mpaka Yehova akatuma ujumbe mzito wa hukumu kwa Eli kupitia “mtu wa Mungu,” yaani, nabii fulani ambaye hatajwi jina. Yehova alimwambia Eli hivi: “Unaendelea kuwaheshimu wana wako kuliko mimi.” Hivyo, Mungu akatabiri kuwa wana waovu wa Eli wangekufa wote wawili siku moja na familia ya Eli ingeteseka sana, na hata kupoteza pendeleo la kuwa makuhani. Je, onyo hilo kali lilileta badiliko lolote katika familia hiyo? Simulizi hilo linaonyesha kwamba familia ya Eli haikubadilika.—1 Samweli 2:27–3:1.
-
-
‘Aliendelea Kukua Akiwa na Yehova’Mnara wa Mlinzi—2010 | Oktoba 1
-
-
c Simulizi hilo linatoa mifano miwili inayoonyesha jinsi walivyokosa heshima. Kwanza, Sheria ilitaja kihususa vipande vya nyama vilivyotolewa dhabihu ambavyo makuhani waliruhusiwa kula. (Kumbukumbu la Torati 18:3) Lakini katika hema la kukutania, makuhani hao waovu walifanya jambo tofauti kabisa. Waliwalazimisha wahudumu wao kuingiza uma mkubwa ndani ya chungu cha kupikia ambacho kilikuwa na nyama zilizokuwa zikitokota, na kutoa kipande chochote kizuri walichopata! Pia, watu walipoleta dhabihu zao ili ziteketezwe juu ya madhabahu, makuhani hao waovu waliwatuma wahudumu wao kuwasumbua watu walioleta dhabihu kwa kuwaambia wawape nyama mbichi kabla ya kumtolea Yehova dhabihu ya sehemu ya mafuta.—Mambo ya Walawi 3:3-5; 1 Samweli 2:13-17.
-