-
Uwe na Maoni Yenye Usawaziko Kuhusu KaziAmkeni!—2010 | Januari
-
-
Uwe na Maoni Yenye Usawaziko Kuhusu Kazi
KATIKA kipindi hiki chenye matatizo mengi ya kiuchumi, kila mtu anahangaikia kuwa na kazi inayotegemeka, yenye mapato ambayo yatatosheleza mahitaji ya familia yake. Si rahisi kufanya hivyo, hasa wakati maelfu ya watu wanaachishwa kazi. Ikiwa wewe ni mmoja wa wale ambao wameachishwa kazi ghafula, kibarua kigumu sasa ni kujitahidi kutafuta kazi nyingine.—Ona masanduku kwenye ukurasa wa 8 na 9.
Lakini, bado kuna mambo mengine muhimu maishani zaidi ya kufanya kazi kwa bidii. Glenn, mwanamume mwenye familia anayeishi Australia, anasema hivi: “Ukweli wa mambo ni kwamba hakuna mtu ambaye husema hivi anapokaribia kufa, ‘Laiti ningetumia wakati mwingi zaidi kazini.’” Pasipo shaka, maisha yenye kuridhisha na yaliyo na kusudi yanatia ndani kufanya kazi ya kimwili. Lakini si hayo tu. Yanatia ndani pia kutenga wakati wa kuwa pamoja na familia, kuwa na burudani, na kushughulikia mahitaji ya kiroho. Unaweza kutengaje wakati wa kushughulikia mambo hayo muhimu maishani kwa usawaziko?
Wakati wa Kazi, Wakati wa Kupumzika
Biblia inatuambia tufanye kazi kwa bidii ili kuandalia familia mahitaji yake. (Waefeso 4:28) Hata hivyo, inatuhimiza pia ‘tule, tunywe na kuona mema kwa ajili ya kazi yetu yote iliyo ngumu.’ (Mhubiri 3:13) Kwa kweli, kufanya kazi kwa saa nyingi bila kupumzika vya kutosha au kuwa na burudani kunaweza kufanya tukose kufurahia mambo mengi maishani. Kunaweza pia kusababisha matatizo mabaya ya afya.
Kufanya kazi kupita kiasi kwa muda mrefu kumehusianishwa na kuwa mnene kupita kiasi, uraibu wa kileo, ugonjwa wa moyo, aksidenti kazini, matumizi mabaya ya dawa, wasiwasi, uchovu, kushuka moyo, na matatizo mengine mengi yanayohusiana na mfadhaiko. Kufanya kazi kupita kiasi kunaweza pia kusababisha kifo. Ripoti moja inakadiria kwamba nchini Japani, karibu watu 10,000 hufa kila mwaka kwa sababu ya kufanya kazi kupita kiasi, idadi ambayo inalingana na ya wale wanaokufa kutokana na aksidenti za barabarani kila mwaka nchini humo. Tatizo hilo ambalo limeitwa karoshi, yaani, “kufa kutokana na kufanya kazi kupita kiasi,” limeenea katika nchi nyingine pia.
Ona kwamba Biblia inashauri hivi kwa hekima: “Konzi moja ya pumziko ni afadhali kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kufuatilia upepo.” (Mhubiri 4:6) Kuwa na usawaziko ni muhimu sana. Usiruhusu kazi iwe uraibu wako. Tunza afya yako ya kiakili, kimwili, na kihisia kwa kutenga wakati wa kupumzika na kufurahia matunda ya kazi yako.
“Tunapaswa kufanya kazi ili tujiruzuku, si kufanya kazi kuwa ndilo jambo la maana maishani,” anasema Andrew, ambaye ana mke na watoto watatu. Kuwa na usawaziko kuhusu kazi na kuwa na pindi za kupumzika na burudani kutakusaidia pia kushughulikia mahitaji ya familia yako. Lakini si rahisi kufanya hivyo, hasa ikiwa una mahitaji ya kifedha.
Kusawazisha Kazi na Maisha ya Familia
Leo familia nyingi zina shughuli nyingi kupita kiasi na hazina wakati wa kuwa pamoja. Mwanamke mmoja huko Uingereza analalamika hivi: “Kazi huchukua nguvu zangu nyingi na watoto wangu hupata masalio.” Huko Marekani, kijana 1 kati ya 5 waliohojiwa alitaja kwamba “kutokuwa na wakati wa kutosha pamoja na wazazi” ndilo jambo linalowahangaisha sana vijana. Uchunguzi mwingine uliofanywa Marekani unaripoti kwamba, kwa wastani, wenzi wa ndoa ambao wanafanya kazi huzungumza pamoja kwa dakika 12 tu kwa siku.
Watu wengi sasa wanachunguza tena mambo wanayotanguliza na kufanya mabadiliko kwa kuwa wamechoshwa na mkazo wa kufanya kazi. Timothy, aliye na mke na watoto wawili wadogo, anasema hivi: “Nilikuwa nikifanya kazi baada ya saa za kazi, na mke wangu alikuwa akifanya kazi Jumamosi [Siku ya Posho] na Jumapili [Siku ya Yenga]. Tulionana mara chache sana. Mwishowe, tulichunguza tena maisha yetu na kubadili muda tuliotumia kazini. Sasa tuna furaha zaidi.” Brian, ambaye ni meneja wa duka anasema: “Kwa kuwa tulikuwa tukitarajia mtoto wetu wa pili, nilitafuta kazi ambayo ingefaa familia yangu. Nilikubali kazi ambayo ningelipwa mshahara unaopungua ule niliokuwa nikipata kwa dola 10,000 kwa mwaka, lakini kufanya hivyo kuliniruhusu nifanye kazi saa zinazofaa.” Melina aliacha kufanya kazi alipojifungua binti yake wa kwanza. Anasema: “Ilikuwa vigumu kutegemea mshahara mmoja tu, lakini mimi na mume wangu tuliona ingefaa nikae nyumbani na Emily badala ya kumpeleka kwenye kituo cha kuwatunzia watoto.”
Ingawa hivyo, lazima tutambue kwamba ni vigumu kwa familia nyingi kulipia gharama za kila mwezi. Wenzi fulani wa ndoa huwa na kazi mbili ili tu waweze kulipia gharama za lazima, na katika visa vingine, wazazi wote wawili hufanya kazi, na hivyo wao huwaacha watoto watunzwe na babu na nyanya yao au wanawaacha kwenye kituo cha kuwatunzia watoto.
Unaweza kupata njia nyingine za kusawazisha majukumu kazini na ya familia. Jambo muhimu ni hili: Usikose kufurahia maisha ya familia kwa sababu ya kukazia fikira sana kazi yako.
Uwe na hakika kwamba ukiwa na usawaziko kuhusu kazi yako, burudani, na mahitaji ya familia yako, utapata baraka nyingi. Katika makala ya mwisho ya mfululizo huu, tutazungumzia jambo muhimu zaidi ambalo litatusaidia kuwa na maisha rahisi yaliyo na usawaziko.
-
-
Ishi Maisha Rahisi, Yenye UsawazikoAmkeni!—2010 | Januari
-
-
Ishi Maisha Rahisi, Yenye Usawaziko
KUISHI maisha rahisi, yenye usawaziko kunathawabisha kwelikweli. Lakini hilo linahusisha nini? Kwanza, huenda ukahitaji kufikiria mambo unayotanguliza. Unaweza kufanyaje hivyo?
Jiulize: ‘Nimetimiza nini kufikia sasa? Ni mambo gani yanahitaji kufanywa?’ Andika miradi yako muhimu hapa chini:
1. ․․․․․
2. ․․․․․
3. ․․․․․
Leo watu wengi wana mtazamo wa kufuatilia vitu vya kimwili kwa kuwa hawafikirii wakati ujao. Ni kana kwamba wanasema: “Na tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.” (1 Wakorintho 15:32) Wanaamini kwamba maisha bora zaidi ni kufanya kazi na kununua vitu. Hata hivyo, Biblia inapinga maoni hayo.
Katika moja ya mifano yake, Yesu alizungumza kuhusu mtu ambaye alijikusanyia vitu lakini akafa kabla ya kuvifurahia. “Hivyo ndivyo huwa kwa mtu anayejikusanyia mwenyewe hazina lakini si tajiri kwa Mungu.” (Luka 12:16-21) Je, mtu huyo alifanya makosa kwa kufanya kazi kwa bidii ili kujiruzuku? Hapana. Tatizo lake lilikuwa kukazia fikira sana vitu vya kimwili. Hakufikiria maoni ya Mungu alipofanya mipango yake. Kwa sababu hiyo, mali yake yote—kila kitu alichokuwa amefanyia kazi—haingemfaidi mwishowe. Inasikitisha kama nini!—Mhubiri 2:17-21; Mathayo 16:26.
Tofauti na hilo, Yesu anatuambia tufanye kazi ili tupate zawadi ya milele. “Fanyeni kazi, si kwa ajili ya chakula ambacho huharibika,” akahimiza, “bali kwa ajili ya chakula ambacho hudumu kufikia uzima wa milele.” (Yohana 6:27) Mapema Yesu alikuwa amesema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Hiyo ni zawadi nzuri kama nini!
Unaweza Kukabilianaje na Mahangaiko?
Yesu alitambua kwamba wanadamu wana mwelekeo wa kuhangaikia vitu vya kimwili. Kwa hiyo, aliwahimiza wanafunzi wake hivi: “Acheni kutafuta mnachoweza kula na mnachoweza kunywa, na acheni kuhangaika kwa wasiwasi; kwa maana mataifa ya ulimwengu yanafuatilia kwa bidii mambo yote hayo, lakini Baba yenu anajua mnahitaji mambo hayo. Hata hivyo, utafuteni ufalme wake sikuzote, na mambo hayo mtaongezewa.”—Luka 12:29-31.
Maneno hayo yenye kutia moyo yamewachochea Wakristo wengi kurahisisha maisha yao. Juliet, anayeishi nchini Malasia anasema hivi: “Kazi yangu ilinifanya nijihisi mchovu na nikate tamaa. Kwa hiyo mimi na mume wangu tulisali Yehova atusaidie kurahisisha maisha yetu. Alijibu haraka. Kabla ya mwezi mmoja kwisha, nilipata kazi ambayo haikuwa ya wakati wote ya kuwafundisha watoto walemavu.” Steve, ambaye hufanya kazi ya kuezeka paa huko Australia, alirekebisha ratiba yake ya kazi ili aweze kutumia wakati mwingi zaidi pamoja na familia yake katika utendaji wa kiroho. Mke wake, Maureen, anaeleza hivi: “Sasa sisi sote tuna furaha zaidi. Watoto wanafurahia sana mpango huo! Mimi pia ninaufurahia! Ukifanya maisha yako yawe rahisi, familia yote itasitawi.”
Hata hivyo, ikiwa umepoteza kazi na unakaribia kupoteza nyumba yako, unahitaji imani yenye nguvu kufuata himizo hilo la Yesu. Lakini, ukitanguliza mambo ya kiroho na kumtegemea Mungu, wewe pia unaweza kuishi maisha rahisi, yenye usawaziko. Kufanya hivyo kutakusaidia kufikia “uzima ulio wa kweli,” yaani, uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu, ambamo kazi yote itafurahisha na haitakuwa ya bure.—1 Timotheo 6:17-19; Isaya 65:21-23.
-