Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Huu Ndio Wakati Tunaopaswa Kuwa Wenye Kulinda Zaidi
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Desemba 15
    • Huu Ndio Wakati Tunaopaswa Kuwa Wenye Kulinda Zaidi

      “Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja.”—MATHAYO 24:42.

      1, 2. Ni nini kinachoonyesha kwamba tunaishi katika umalizio wa mfumo huu wa mambo?

      “KARNE ya ishirini iliathiriwa sana na vita,” anasema mwandishi Bill Emmott. Ingawa anakiri kwamba kumekuwa na vita na jeuri katika historia yote ya mwanadamu, Emmott anaendelea kusema: “Karne ya ishirini imekuwa tofauti na karne nyingine kwa kuwa imekuwa na vita vingi zaidi. Ilikuwa karne ambayo vita vilivyohusisha ulimwengu mzima vilipiganwa kwa mara ya kwanza . . . Isitoshe, katika karne hiyohiyo, vita vingine vilivyohusisha ulimwengu mzima vilipiganwa pia.”

      2 Yesu Kristo alitabiri kwamba kungekuwa na vita ambavyo ‘taifa lingepigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme.’ Hata hivyo, vita hivyo ni sehemu moja tu ya ile ‘ishara ya kuwapo kwa Kristo na ya umalizio wa mfumo wa mambo.’ Katika unabii huu muhimu, Yesu pia alitaja njaa kali, tauni, na matetemeko ya nchi. (Mathayo 24:3, 7, 8; Luka 21:6, 7, 10, 11) Katika njia nyingi, maafa hayo yameongezeka na kuwa mabaya zaidi. Uovu wa mwanadamu umeongezeka, kama inavyoonyeshwa na mtazamo wake kuelekea Mungu na wanadamu wenzake. Pia maadili yanazidi kuzorota na uhalifu na jeuri vimeongezeka. Watu wamekuwa wenye kupenda fedha kuliko kumpenda Mungu, wakijishughulisha sana na anasa. Mambo hayo yote yanathibitisha kwamba tunaishi katika “nyakati za hatari.”—2 Timotheo 3:1-5.

      3. “Ishara za nyakati” zinapaswa kuwa na matokeo gani juu yetu?

      3 Unaonaje mwelekeo wa wanadamu ambao unazidi kuwa mbaya? Wengi hawajali, na hata wamekuwa wagumu kuhusiana na matukio ya sasa yenye kuhuzunisha. Watu mashuhuri na wasomi wa ulimwengu hawatambui maana ya “ishara za nyakati”; wala viongozi wa kidini hawatoi mwongozo unaofaa kuhusiana na jambo hilo. (Mathayo 16:1-3) Lakini Yesu aliwashauri hivi wafuasi wake: “Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja.” (Mathayo 24:42) Katika andiko hilo Yesu anatutia moyo tuwe wenye kulinda na pia ‘tuendelee kukesha.’ Ili kuendelea kukesha, ni lazima tudumu tukiwa macho. Kufanya hivyo kunahusisha mengi zaidi ya kutambua kwamba tunaishi katika siku za mwisho, na kwamba hali ni ngumu. Ni lazima tusadiki kabisa kwamba “mwisho wa mambo yote umekaribia.” (1 Petro 4:7) Tukiwa na usadikisho huo, tutaweza kuwa wenye kulinda na kutambua uharaka wa nyakati. Kwa hiyo, tunapaswa kutafakari swali hili: ‘Ni nini kitakachotusaidia kuimarisha usadikisho wetu kwamba mwisho uko karibu?’

      4, 5. (a) Ni nini kitakachoimarisha usadikisho wetu kwamba mwisho wa mfumo huu mwovu uko karibu, na kwa nini? (b) Taja ufanani mmoja uliopo kati ya siku za Noa na kuwapo kwa Mwana wa binadamu?

      4 Fikiria jinsi hali zilivyokuwa kabla tu ya tukio la kipekee katika historia ya mwanadamu, yaani, ile Gharika kuu ya siku za Noa. Watu walikuwa wabaya sana hivi kwamba Yehova ‘aliumia moyoni mwake.’ Alisema: “Nitawafutilia mbali kutoka usoni pa nchi wanadamu ambao nimeumba.” (Mwanzo 6:6, 7) Naye akafanya vivyo hivyo. Yesu alilinganisha siku hizo na wakati wetu na kusema: “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.”—Mathayo 24:37.

      5 Ni jambo linalopatana na akili kusema kwamba Yehova anahisi kuhusu ulimwengu wa sasa kama alivyohisi kuhusu ulimwengu wa kabla ya Gharika. Kwa kuwa aliangamiza ulimwengu usiomwogopa wa siku za Noa, bila shaka ataharibu ulimwengu mwovu wa sasa. Tukielewa vizuri ufanani uliopo kati ya siku hizo na siku zetu tutaimarisha usadikisho wetu kwamba mwisho wa ulimwengu wa sasa uko karibu. Hivyo basi, ni mambo gani yanayofanana? Kuna angalau mambo matano. Kwanza, onyo kuhusu kuja kwa uharibifu linatolewa waziwazi.

      Walionywa Kuhusu “Mambo Ambayo Yalikuwa Bado Hayajaonekana”

      6. Yehova aliamua kufanya nini katika siku za Noa?

      6 Katika siku za Noa, Yehova alisema hivi: “Roho yangu haitavumiliana sikuzote na mwanadamu kwa kuwa yeye pia ni mwili. Kwa hiyo siku zake zitakuwa miaka 120.” (Mwanzo 6:3) Kutolewa kwa amri hiyo ya Mungu katika mwaka wa 2490 K.W.K. kulionyesha kwamba mwisho wa ulimwengu huo usiomwogopa Mungu ulikuwa umeanza. Wazia kilichomaanishwa na amri hiyo kwa watu walioishi siku hizo! Ni miaka 120 tu iliyokuwa imebaki kabla ya Yehova kuleta “gharika ya maji duniani ili kuharibu kutoka chini ya mbingu wote wenye mwili walio na nguvu za uhai ndani yao.”—Mwanzo 6:17.

      7. (a) Noa aliitikiaje onyo kuhusu Gharika? (b) Tunapaswa kuitikiaje maonyo kuhusu mwisho wa mfumo huu?

      7 Noa alipokea onyo kuhusu kuja kwa uharibifu huo miaka mingi mapema, naye alitumia kwa hekima muda huo kujitayarisha kwa ajili ya kuokoka. “Baada ya kupewa onyo la kimungu la mambo ambayo yalikuwa bado hayajaonekana,” asema mtume Paulo, “[Noa] alionyesha woga wa kimungu na kujenga safina kwa ajili ya kuiokoa nyumba yake.” (Waebrania 11:7) Namna gani sisi? Miaka 90 hivi imepita tangu siku za mwisho za mfumo huu wa mambo zianze mwaka wa 1914. Hakika tunaishi katika “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) Tunapaswa kuitikiaje maonyo ambayo tumepewa? Biblia inasema: “Yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:17) Sasa ndio wakati wa kufanya mapenzi ya Yehova huku tukitambua uharaka wa nyakati.

      8, 9. Ni maonyo gani ambayo Yehova ametoa leo, nayo yanatangazwaje?

      8 Katika nyakati zetu, wanafunzi wanyoofu wa Biblia wamejifunza katika Maandiko yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu kwamba mfumo huu utaharibiwa. Je, tunaamini hayo? Ona yale Yesu Kristo aliyosema waziwazi: “Ndipo kutakapokuwa na dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatukia tena.” (Mathayo 24:21) Yesu alisema pia kwamba angekuja akiwa Hakimu aliyewekwa rasmi na Mungu naye angetenganisha watu kama vile mchungaji hutenganisha kondoo na mbuzi. Wale ambao wangepatikana hawastahili ‘wangekatiliwa mbali milele, lakini waadilifu wangeingia katika uzima wa milele.’—Mathayo 25:31-33, 46.

      9 Yehova ameendelea kufanya watu wake watambue maonyo hayo kwa njia ya vikumbusho vya wakati unaofaa kupitia chakula cha kiroho kinachoandaliwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45-47) Isitoshe, kila taifa, kabila, lugha, na watu wanahimizwa ‘wamwogope Mungu na kumpa utukufu, kwa sababu saa ya hukumu yake imefika.’ (Ufunuo 14:6, 7) Sehemu muhimu ya ujumbe wa Ufalme ambao unahubiriwa duniani pote na Mashahidi wa Yehova ni onyo kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utaondoa utawala wa kibinadamu. (Danieli 2:44) Onyo hilo linapaswa kuchukuliwa kwa uzito. Mungu Mweza Yote hutimiza ahadi zake sikuzote. (Isaya 55:10, 11) Alifanya hivyo katika siku za Noa, na atafanya vivyo hivyo leo.—2 Petro 3:3-7.

      Upotovu wa Kingono Waenea Sana

      10. Upotovu wa kingono ulikuwa umeenea kadiri gani siku za Noa?

      10 Wakati wetu unafanana na siku za Noa katika njia nyingine. Yehova alikuwa amemwamuru mwanamume na mwanamke wa kwanza ‘waijaze dunia’ na wanadamu, wakitumia kwa heshima uwezo wa kingono waliopewa na Mungu ndani ya mpango wa ndoa. (Mwanzo 1:28) Katika siku za Noa, malaika wasiotii waliwachafua wanadamu kwa ngono zisizo za asili. Walishuka duniani, wakajivika miili ya kibinadamu, wakafanya ngono na wanawake warembo, na kuzaa watoto ambao walikuwa nusu-binadamu, nusu-mashetani, yaani Wanefili. (Mwanzo 6:2, 4) Dhambi ya malaika hao wenye tamaa ya ngono inafananishwa na upotovu wa Sodoma na Gomora. (Yuda 6, 7) Hivyo, upotovu wa kingono ukaenea sana siku hizo.

      11. Ni hali gani za kiadili ambazo zinafanya wakati wetu ufanane na siku za Noa?

      11 Namna gani hali ya kiadili leo? Watu wengi katika siku hizi za mwisho wanajishughulisha sana na mambo ya ngono. Kuhusu watu hao, Paulo anaeleza waziwazi kwamba ‘wameishiwa na ufahamu wote wa maadili’; wengi wamejitoa wenyewe “ili kuwa na mwenendo mpotovu na kufanya ukosefu wa usafi wa kila namna kwa pupa.” (Waefeso 4:19) Ponografia, ngono kabla ya ndoa, kutendea watoto vibaya kingono, na ngono za watu wa jinsia moja ni mambo ambayo yameneea sana. Tayari wengine ‘wanapokea ndani yao wenyewe malipo kamili’ kwa kupata magonjwa yanayoambukizwa kupitia ngono, kuvunjika kwa familia, na matatizo mengine ya kijamii.—Waroma 1:26, 27.

      12. Kwa nini tunapaswa kusitawisha chuki kwa mambo mabaya?

      12 Katika siku za Noa, Yehova alileta Gharika kuu na kukomesha ulimwengu huo uliokuwa na kichaa cha ngono. Hatupaswi kamwe kusahau kwamba kwa kweli siku hizi ni kama siku za Noa. “Dhiki kuu” inayokuja itaondoa duniani ‘waasherati, wazinzi, wanaume wanaowekwa kwa ajili ya makusudi yasiyo ya asili, na wanaume wanaolala na wanaume.’ (Mathayo 24:21; 1 Wakorintho 6:9, 10; Ufunuo 21:8) Ni jambo la haraka kama nini kusitawisha chuki kwa mambo mabaya na kuepuka kabisa hali zinazoweza kutuingiza katika uasherati!—Zaburi 97:10; 1 Wakorintho 6:18.

      Dunia ‘Yajaa Jeuri’

      13. Kwa nini dunia “ilijaa jeuri” katika siku za Noa?

      13 Inapotaja hali nyingine inayofanana na ya siku za Noa, Biblia inasema: “Dunia ikaharibika machoni pa Mungu wa kweli, dunia ikajaa jeuri.” (Mwanzo 6:11) Kwa kweli, jeuri haikuwa jambo jipya. Kaini, mwana wa Adamu alimuua ndugu yake aliyekuwa mwadilifu. (Mwanzo 4:8) Akionyesha roho ya jeuri ya siku hizo, Lameki alitunga shairi akijigamba kuhusu jinsi alivyomuua mwanamume mmoja kijana, kwa dai la kujitetea. (Mwanzo 4:23, 24) Kilichokuwa tofauti katika siku za Noa ni kiwango cha jeuri. Wakati wana wa Mungu wa kimalaika wasiotii walipooa wanawake duniani na kuzaa Wanefili, jeuri iliongezeka kwa kiwango kisicho na kifani. Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inaonyesha kwamba neno la awali la Kiebrania linalorejelea majitu hao linamaanisha ‘Waangushaji’, yaani, “watu wenye kuwaangusha wengine.” (Mwanzo 6:4) Kwa sababu hiyo, dunia ‘ilijaa jeuri.’ (Mwanzo 6:13) Wazia matatizo ambayo lazima Noa alikabiliana nayo kulea watoto katika mazingira hayo! Hata hivyo, Noa alionekana kuwa ‘mwadilifu mbele za Yehova kati ya kizazi hicho.’—Mwanzo 7:1.

      14. Leo ulimwengu ‘umejaa jeuri’ kwa kadiri gani?

      14 Kumekuwa na jeuri katika historia yote ya mwanadamu. Lakini kama ilivyokuwa katika siku za Noa, wakati wetu pia umekuwa na jeuri isiyo na kifani. Mara nyingi tunasikia juu ya jeuri ya nyumbani, vitendo vya ugaidi, kampeni za maangamizi ya watu wengi, au mauaji ya watu wengi yanayofanywa na majambazi bila kusudi hususa. Isitoshe, kuna umwagikaji wa damu unaosababishwa na vita. Dunia imejaa jeuri tena. Kwa nini? Ni nini ambacho kimesababisha ongezeko hilo? Jibu linaonyesha hali nyingine inayofanana na ya siku za Noa.

      15. (a) Ni nini kimefanya jeuri iongezeke siku hizi za mwisho? (b) Tunaweza kutazamia nini kwa uhakika?

      15 Ufalme wa Kimasihi wa Mungu ulipoanzishwa mbinguni mwaka wa 1914, Mfalme aliyetawazwa, Yesu Kristo, alichukua hatua muhimu sana. Shetani Ibilisi na roho wake waovu walitupwa kutoka mbinguni hadi kwenye ujirani wa dunia. (Ufunuo 12:9-12) Kabla ya Gharika, malaika wasiotii waliacha kwa hiari makao yao mbinguni; lakini nyakati za sasa wamefukuzwa kwa nguvu. Isitoshe, sasa hawawezi kujivika miili ya kibinadamu duniani ili kufurahia anasa haramu za kimwili. Kwa hiyo, wakiwa wamekata tamaa, wenye hasira, na wenye kuogopa hukumu inayokuja, wao huchochea wanadamu na matengenezo mbalimbali kutenda uhalifu na jeuri ya kinyama na ya kiwango kikubwa hata zaidi kuliko ile ya siku za Noa. Yehova aliufutilia mbali ulimwengu wa kabla ya Gharika baada ya malaika wasiotii na wazao wao kujaza uovu duniani. Uwe na hakika kwamba atafanya vivyo hivyo katika siku zetu! (Zaburi 37:10) Hata hivyo, leo wale wanaolinda wanajua kwamba ukombozi wao uko karibu.

      Ujumbe Unahubiriwa

      16, 17. Ni ufanani gani wa nne uliopo kati ya siku za Noa na siku zetu?

      16 Jambo la nne linaloonyesha ufanani kati ya siku zetu na za kabla ya Gharika linaonekana katika kazi ambayo Noa aliagizwa kufanya. Noa alijenga safina kubwa. Pia alikuwa “mhubiri.” (2 Petro 2:5) Alihubiri ujumbe gani? Yaonekana katika mahubiri yake Noa aliwasihi watu watubu na kuwaonya kuhusu uharibifu uliokuwa unakuja. Yesu alisema kwamba watu wa siku za Noa “hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.”—Mathayo 24:38, 39.

      17 Vivyo hivyo, Mashahidi wa Yehova wanapofanya kwa bidii kazi yao ya kuhubiri, ujumbe wa Ufalme wa Mungu unahubiriwa duniani pote. Karibu kila mahali duniani watu wanaweza kusikia na kusoma ujumbe wa Ufalme katika lugha yao wenyewe. Nakala zaidi ya 25,000,000 za Mnara wa Mlinzi, unaotangaza Ufalme wa Yehova, huchapishwa katika lugha zaidi ya 140. Kwa kweli, habari njema ya Ufalme wa Mungu inahubiriwa “katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” Bila shaka, mwisho utakuja Mungu atakaporidhika kwamba kazi hiyo imekamilika.—Mathayo 24:14.

      18. Itikio la wengi kwa kazi yetu ya kuhubiri linafananaje na la watu wengi katika siku za Noa?

      18 Kwa kufikiria hali ya kutopendezwa kabisa na mambo ya kiroho na ukosefu wa maadili kabla ya Gharika, tunaweza kuelewa ni kwa nini familia ya Noa ilichekelewa, ikatukanwa, na kudhihakiwa na majirani wasioamini. Hata hivyo, mwisho ulikuja. Vivyo hivyo, “wadhihaki na dhihaka zao” wamekuwa wengi siku hizi za mwisho. “Lakini siku ya Yehova itakuja kama mwizi,” Biblia inasema. (2 Petro 3:3, 4, 10) Na bila shaka itakuja wakati uliowekwa. Haitachelewa. (Habakuki 2:3) Ni jambo la hekima kama nini kuwa wenye kulinda!

      Wachache Tu Ndio Wanaookoka

      19, 20. Tunaweza kuona ufanani gani kati ya Gharika na uharibifu wa mfumo huu wa mambo?

      19 Ufanani kati ya siku za Noa na siku zetu hauhusu tu uovu wa watu na kuharibiwa kwao. Kama vile kulivyokuwa na watu waliookoka Gharika, pia kutakuwa na watu watakaookoka mwisho wa mfumo huu wa mambo. Watu waliookoka Gharika walikuwa wanyenyekevu na maisha yao yalikuwa tofauti na ya watu wengine kwa ujumla. Walitii onyo la Mungu na wakajitenga na ulimwengu mwovu wa wakati huo. Biblia inasema, ‘Noa alipata kibali machoni pa Yehova.’ Naye “alionekana kuwa mtu asiye na kosa kati ya watu wa siku zake.” (Mwanzo 6:8, 9) Kati ya wanadamu wote, familia moja, “watu wachache, yaani, nafsi nane, walichukuliwa salama kupitia maji.” (1 Petro 3:20) Naye Yehova Mungu aliwaamuru hivi: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia.”—Mwanzo 9:1.

      20 Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba ‘umati mkubwa utatoka katika ile dhiki kuu.’ (Ufunuo 7:9, 14) Umati mkubwa utakuwa na watu wangapi? Yesu mwenyewe alisema: “Lango ni jembamba na barabara inayoongoza kwenye uzima ina nafasi ndogo, na wachache ndio wanaoipata.” (Mathayo 7:13, 14) Kwa kulinganishwa na mabilioni ya watu wanaoishi duniani sasa, waokokaji wa dhiki kuu inayokuja watakuwa wachache. Lakini huenda wakawa na pendeleo kama lile la waokokaji wa Gharika. Huenda waokokaji hao wakaruhusiwa kuzaa watoto kwa muda fulani ambao watakuwa sehemu ya jamii mpya ya kidunia.—Isaya 65:23.

      “Endeleeni Kukesha”

      21, 22. (a) Umenufaikaje kwa kuchunguza masimulizi kuhusu Gharika? (b) Andiko la mwaka wa 2004 ni gani, na kwa nini tunapaswa kutii shauri la andiko hilo?

      21 Ingawa Gharika inaonekana kana kwamba haihusiani na wakati wetu, kwa wazi inatoa onyo tusilopaswa kupuuza. (Waroma 15:4) Mambo yanayofanana kati ya siku za Noa na siku zetu yanapaswa kufanya tutambue umuhimu wa matukio ya sasa na kufanya tuwe macho kuhusu kuja kwa Yesu kama mwizi ili kutekeleza hukumu juu ya waovu.

      22 Leo, Yesu Kristo anaongoza kazi kubwa sana ya ujenzi wa kiroho. Waabudu wa kweli wanaokolewa na kupata usalama katika paradiso ya kiroho iliyo kama safina. (2 Wakorintho 12:3, 4) Ili kuhifadhiwa wakati wa dhiki hiyo kuu, ni lazima tubaki katika paradiso hiyo. Nje ya paradiso hiyo ya kiroho kuna ulimwengu wa Shetani ambao uko tayari kummeza yeyote anayesinzia kiroho. Kwa hiyo, ni muhimu kwamba ‘tuendelee kukesha’ na kuwa tayari kwa ajili ya siku ya Yehova.—Mathayo 24:42, 44.

  • Uwe Tayari kwa Ajili ya Siku ya Yehova
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Desemba 15
    • Uwe Tayari kwa Ajili ya Siku ya Yehova

      “Iweni tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyofikiria.”—MATHAYO 24:44.

      1. Kwa nini tuifikirie siku ya Yehova?

      ITAKUWA siku ya pigano na ghadhabu, ya taabu na maumivu makali, ya giza na ukiwa. Hapana shaka kwamba ‘siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha’ itakuja juu ya mfumo huu mwovu wa mambo, kama vile Gharika ilivyowaangamiza waovu katika siku za Noa. Haitakosa kuja. Hata hivyo, “kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokoka.” (Yoeli 2:30-32; Amosi 5:18-20) Mungu ataharibu maadui wake na kuwaokoa watu wake. Kwa kutambua uharaka wa nyakati, nabii Sefania anasema: “Ile siku kuu ya Yehova iko karibu. Iko karibu, nayo inaharakisha sana.” (Sefania 1:14) Hata hivyo, hukumu hiyo ya Mungu itatekelezwa wakati gani?

      2, 3. Kwa nini ni muhimu tuwe tayari kwa ajili ya siku ya Yehova?

      2 Yesu alisema: “Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.” (Mathayo 24:36) Kwa kuwa hatujui wakati barabara, ni muhimu tutii maneno ya andiko la mwaka wa 2004: “Endeleeni kukesha . . . Iweni tayari.”—Mathayo 24:42, 44.

      3 Akionyesha jinsi wale walio tayari watakavyokusanywa haraka mahali penye usalama huku wengine wakiachwa, Yesu alisema: “Watu wawili watakuwa shambani: mmoja atachukuliwa na mwingine ataachwa; wanawake wawili watakuwa wakisaga kwenye jiwe la kusagia: mmoja atachukuliwa na mwingine ataachwa.” (Mathayo 24:40, 41) Hali yetu binafsi itakuwaje wakati huo muhimu? Je, tutakuwa tayari, au siku hiyo itatupata ghafula? Mengi yanategemea hatua tunazochukua sasa. Ili tuwe tayari kwa ajili ya siku ya Yehova tunahitaji kuepuka mtazamo fulani ambao umeenea sana leo, tukatae kujiingiza katika hali fulani ya kiroho, na kuepuka mitindo fulani ya maisha.

      Epuka Mtazamo wa Kutojali

      4. Watu wa siku za Noa walikuwa na mtazamo gani?

      4 Fikiria siku za Noa. Biblia inasema: “Kwa imani Noa, baada ya kupewa onyo la kimungu la mambo ambayo yalikuwa bado hayajaonekana, alionyesha woga wa kimungu na kujenga safina kwa ajili ya kuiokoa nyumba yake.” (Waebrania 11:7) Safina ingekuwa kitu kisicho cha kawaida na chenye kuonekana waziwazi. Isitoshe, Noa alikuwa “mhubiri wa uadilifu.” (2 Petro 2:5) Watu wa siku za Noa hawakubadili mwenendo wao hata walipohubiriwa na kuona safina ikijengwa. Kwa nini? Kwa sababu walikuwa “wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa.” Watu ambao Noa alihubiria walijishughulisha sana na mambo ya kibinafsi na anasa hivi kwamba “hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.”—Mathayo 24:38, 39.

      5. Wakaaji wa Sodoma katika siku za Loti walikuwa na maoni gani?

      5 Hali ilikuwa vivyo hivyo katika siku za Loti. Maandiko yanatuambia: “Walikuwa wakila, walikuwa wakinywa, walikuwa wakinunua, walikuwa wakiuza, walikuwa wakipanda, walikuwa wakijenga. Lakini siku ambayo Loti alitoka Sodoma kulinyesha moto na kiberiti kutoka mbinguni na kuwaangamiza wote.” (Luka 17:28, 29) Baada ya malaika kumwonya Loti kuhusu uharibifu uliokuwa unakaribia, Loti alizungumza na wakwe zake kuhusu yale ambayo yangetokea. Lakini, machoni pao “alionekana kama mtu aliyekuwa anafanya mzaha.”—Mwanzo 19:14.

      6. Tunapaswa kuepuka mtazamo gani?

      6 Kama ilivyokuwa katika siku za Noa na Loti “ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu” kutakavyokuwa, akasema Yesu. (Mathayo 24:39; Luka 17:30) Kwa kweli, watu wengi leo wana mtazamo wa kutojali. Ni lazima tujihadhari tusiathiriwe na mtazamo kama huo. Hakuna ubaya kufurahia chakula na kinywaji kizuri kwa kiasi. Vivyo hivyo, ndoa ni mpango wa Mungu. Hata hivyo, ikiwa mambo hayo yamekuwa muhimu zaidi maishani mwetu na hivyo kutufanya tupuuze mambo ya kiroho, je, kweli tuko tayari kwa ajili ya siku ya Yehova yenye kuogopesha?

      7. Ni swali gani muhimu tunalopaswa kujiuliza kabla ya kuchukua hatua fulani, na kwa nini?

      7 “Wakati uliobaki umepungua,” akasema mtume Paulo. “Tangu sasa wale walio na wake na wawe kana kwamba hawana.” (1 Wakorintho 7:29-31) Ni wakati mchache tu unaobaki ili tumalize kazi tuliyopewa na Mungu ya kuhubiri juu ya Ufalme. (Mathayo 24:14) Paulo anawashauri hata watu waliofunga ndoa wasijishughulishe sana na wenzi wao na hivyo kutotanguliza mambo ya Ufalme maishani mwao. Bila shaka, mtazamo wa kiakili ambao Paulo alipendekeza ni kinyume na ule wa kutojali. Yesu alisema: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu [wa Mungu].” (Mathayo 6:33) Unapofanya uamuzi wowote au kabla ya kuchukua hatua fulani, unapaswa kujiuliza swali hili, ‘Jambo hili litanizuia nisitangulize Ufalme maishani mwangu katika njia gani?’

      8. Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunahangaikia sana mambo ya kawaida maishani?

      8 Namna gani tukitambua kwamba tayari tunahangaikia sana mambo ya kawaida maishani, hivi kwamba hatupati nafasi kwa ajili ya mambo ya kiroho? Je, kuna tofauti kati ya mtindo wetu wa maisha na ule wa majirani ambao hawana ujuzi sahihi wa Maandiko na si watangazaji wa Ufalme? Ikiwa hakuna tofauti yoyote, basi tunahitaji kusali kuhusu jambo hilo. Yehova anaweza kutusaidia kuwa na mtazamo unaofaa wa akili. (Waroma 15:5; Wafilipi 3:15) Anaweza kutusaidia kutanguliza mambo yanayohusu Ufalme, kufanya yaliyo sawa, na kutimiza wajibu wetu kwake.—Waroma 12:2; 2 Wakorintho 13:7.

      Epuka Kusinzia Kiroho

      9. Kulingana na andiko la Ufunuo 16:14-16, kwa nini ni muhimu kuepuka kusinzia kiroho?

      9 Ule unabii unaotaja ‘vita ya siku kuu ya Mungu Mweza-Yote’ inayokuja kwenye Har-Magedoni, unaonya kwamba huenda wengine wasiendelee kukesha. “Tazama! Ninakuja kama mwizi,” Bwana Yesu Kristo anasema. “Mwenye furaha ni yule anayekaa macho na kutunza mavazi yake ya nje, ili asipate kutembea akiwa uchi na watu waitazame aibu yake.” (Ufunuo 16:14-16) Mavazi ya nje yanayotajwa hapa yanamaanisha mambo yanayotutambulisha kuwa Mashahidi wa Kikristo wa Yehova. Hayo yanatia ndani kazi yetu tukiwa watangazaji wa Ufalme na pia mwenendo wetu wa Kikristo. Tukijikuta katika hali ya kutotenda, huenda tukavuliwa mavazi yetu yanayotutambulisha kuwa Wakristo. Hilo ni jambo lenye aibu na hatari. Lazima tuepuke kusinzia na kuchoka kiroho. Tunawezaje kuepuka mwelekeo huo?

      10. Kwa nini kusoma Biblia kila siku hutusaidia tubaki macho kiroho?

      10 Biblia hukazia mara kwa mara uhitaji wa kuendelea kukesha na kutunza akili zetu. Kwa mfano, masimulizi ya Injili hutukumbusha hivi: “Endeleeni kukesha” (Mathayo 24:42; 25:13; Marko 13:35, 37); “iweni tayari” (Mathayo 24:44); “endeleeni kutazama, endeleeni kukesha,” (Marko 13:33); “endeleeni kuwa tayari” (Luka 12:40). Baada ya kusema kwamba siku ya Yehova itakuja bila kutazamiwa juu ya ulimwengu huu, mtume Paulo anawahimiza waamini wenzake hivi: “Basi, na tusiendelee kulala usingizi kama wengine, bali na tukae macho na kutunza akili zetu.” (1 Wathesalonike 5:6) Katika kitabu cha mwisho cha Biblia, Yesu Kristo aliyetukuzwa anakazia jinsi atakavyokuja kwa ghafula, anaposema: “Mimi ninakuja upesi.” (Ufunuo 3:11; 22:7, 12, 20) Manabii wengi Waebrania walieleza na kuonya pia kuhusu siku kuu ya Yehova ya hukumu. (Isaya 2:12, 17; Yeremia 30:7; Yoeli 2:11; Sefania 3:8) Kusoma Neno la Mungu, Biblia, kila siku na kutafakari mambo tunayosoma kutatusaidia sana kubaki macho kiroho.

      11. Kwa nini funzo la Biblia la kibinafsi ni muhimu ili kuendelea kulinda kiroho?

      11 Kwa kweli, kujifunza Maandiko kibinafsi kwa bidii tukitumia vichapo vinavyozungumzia Biblia ambavyo huandaliwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” kutatuchochea kuendelea kulinda. (Mathayo 24:45-47) Hata hivyo, funzo la kibinafsi hunufaisha tu linapofanywa kwa kuendelea na kwa ukawaida. (Waebrania 5:14–6:3) Tunapaswa kula chakula kigumu cha kiroho kwa ukawaida. Huenda leo ikawa vigumu kupata wakati wa kujifunza. (Waefeso 5:15, 16) Hata hivyo, kusoma Biblia na vichapo vinavyozungumzia Biblia wakati tu tuna nafasi hakutoshi. Funzo la kibinafsi la ukawaida ni muhimu ili tubaki wenye “afya katika imani” na kuendelea kukesha.—Tito 1:13.

      12. Mikutano ya Kikristo na makusanyiko hutusaidiaje kupambana ili tusisinzie kiroho?

      12 Mikutano ya Kikristo na makusanyiko hutusaidia pia kupambana ili tusisinzie kiroho. Jinsi gani? Kupitia maagizo tunayopokea. Kwenye mikutano hiyo tunakumbushwa kwa ukawaida kuhusu kukaribia kwa siku ya Yehova. Mikutano ya Kikristo ya kila juma hutupa pia nafasi za “kuchocheana katika upendo na matendo mazuri.” Kuchochewa huko hutusaidia tuendelee kuwa macho kiroho. Kwa hiyo, haishangazi kwamba tunaamriwa kukutana kwa ukawaida ‘kwa kadiri tunavyoona siku ile kuwa inakaribia.’—Waebrania 10:24, 25.

      13. Huduma ya Kikristo hutusaidiaje kuendelea kukesha kiroho?

      13 Tunasaidiwa pia kuwa macho tunaposhiriki kwa moyo wote katika huduma ya Kikristo. Njia bora zaidi ya kutambua ishara za nyakati na maana yake ni kuzungumza na wengine kuhusu habari hiyo. Na tunapoona wale tunaojifunza Biblia pamoja nao wakifanya maendeleo na kuanza kutenda kulingana na yale wanayojifunza, kutambua kwetu uharaka wa nyakati kunaongezeka. “Kazeni akili zenu kwa ajili ya utendaji,” akasema mtume Petro, “tunzeni akili zenu kikamili.” (1 Petro 1:13) Njia bora ya kuepuka uchovu wa kiroho ni ‘sikuzote kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’—1 Wakorintho 15:58.

      Epuka Mitindo ya Maisha Yenye Kudhuru Kiroho

      14. Kama inavyoelezwa katika Luka 21:34-36, Yesu anatoa onyo gani kuhusu mitindo fulani ya maisha?

      14 Katika unabii wake muhimu kuhusu ishara ya kuwapo kwake, Yesu alitoa onyo lingine. Alisema: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mtego. Kwa maana itakuja juu ya wale wote wanaokaa juu ya uso wa dunia yote. Basi, endeleeni kukesha wakati wote mkiomba dua ili mpate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia, na kusimama mbele ya Mwana wa binadamu.” (Luka 21:34-36) Yesu alieleza kwa usahihi mitindo ya maisha ambayo watu kwa ujumla wangefuatia: kula kupita kiasi, ulevi, na maisha yanayoleta mahangaiko.

      15. Kwa nini tunapaswa kuepuka kula na kunywa kupita kiasi?

      15 Kula kupita kiasi na kunywa sana hakupatani na kanuni za Biblia na kwapaswa kuepukwa. Biblia inasema: “Usiwe kati ya watu wanaokunywa divai mno, kati ya watu wanaokula nyama kwa ulafi.” (Methali 23:20) Hata hivyo, si lazima mtu ale au anywe kupita kiasi ili kuhatarisha hali yake ya kiroho. Kula na kunywa kunaweza kufanya mtu asinzie na awe mvivu hata kabla ya kuwa mlafi na mlevi. “Mvivu anajionyesha kutamani,” inasema methali ya Biblia, “lakini nafsi yake haina chochote.” (Methali 13:4) Mtu kama huyo anaweza kutaka kufanya mapenzi ya Mungu, lakini hawezi kutimiza tamaa yake kwa sababu ya uzembe.

      16. Tunawezaje kuepuka kulemewa na mahangaiko kuhusu familia zetu?

      16 Yesu alionya kuhusu mahangaiko gani ya maisha? Hayo yanatia ndani mahangaiko ya kibinafsi, kuiandalia familia mahitaji yake, na kadhalika. Si jambo la hekima kuacha mambo hayo yatulemee. Yesu aliuliza: “Ni nani kati yenu kwa kuhangaika anaweza kuongeza kipimo cha mkono mmoja kwenye uhai wake?” Aliwashauri hivi wasikilizaji wake: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote.” Kutanguliza mambo yanayohusu Ufalme maishani mwetu na kuwa na hakika kwamba Yehova atatuandalia mahitaji yetu kutatuepusha na mahangaiko na kutusaidia kuendelea kukesha.—Mathayo 6:25-34.

      17. Kufuatia vitu vya kimwili kunawezaje kuleta mahangaiko?

      17 Mahangaiko yanaweza pia kusababishwa na kufuatia vitu vya kimwili. Kwa mfano, watu fulani hufanya maisha yao yawe magumu kwa kununua vitu wasivyoweza kugharimia. Wengine wameshawishiwa na mipango inayokusudiwa kufanya mtu atajirike haraka na pia vitega-uchumi ambavyo ni hatari. Nao wengine, hunaswa katika mtego wa kufuatia elimu ili wafanikiwe kifedha. Ni kweli kwamba, kiwango fulani cha elimu kinaweza kumsaidia mtu kupata kazi. Hata hivyo, ukweli ni kwamba wengine wamepatwa na madhara ya kiroho kwa kutumia wakati mwingi wakifuatia elimu ya juu. Ni hatari sana kujikuta katika hali hiyo siku ya Yehova inapokaribia. Biblia inatoa onyo hili: “Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu.”—1 Timotheo 6:9.

      18. Tunapaswa kusitawisha uwezo gani ili tusishawishiwe kufuatia vitu vya kimwili?

      18 Jambo muhimu linaloweza kutuzuia tusishawishiwe kufuatia vitu vya kimwili ni kusitawisha uwezo wa kupambanua yaliyo sawa na yaliyo makosa tunapofanya maamuzi. Tunasitawisha uwezo huo kwa kula kwa ukawaida ‘chakula kigumu cha kiroho cha watu wakomavu,’ na kwa ‘kuzoeza nguvu zetu za ufahamu kwa kuzitumia.’ (Waebrania 5:13, 14) Kuhakikisha “mambo yaliyo ya maana zaidi” tunapopanga mambo ya kutangulizwa kutatulinda pia tusifanye maamuzi mabaya.—Wafilipi 1:10.

      19. Tunapaswa kufanya nini tunapotambua kwamba hatuna wakati wa kutosha kufuatia mambo ya kiroho?

      19 Maisha ya kufuatia vitu vya kimwili yanaweza kutupofusha na kufanya tusiwe na wakati wa kutosha au tukose kabisa wakati wa kufuatia mambo ya kiroho. Tunawezaje kujichunguza na kuepuka kunaswa na maisha kama hayo? Tunahitaji kufikiria kwa sala ni kwa njia gani na kadiri gani tunaweza kufanya maisha yetu yawe rahisi. Mfalme Sulemani wa Israeli la kale alisema: “Usingizi wa mtumishi ni mtamu, bila kujali kama anakula kidogo au kingi; lakini wingi alio nao tajiri haumruhusu kulala.” (Mhubiri 5:12) Je, tunatumia nguvu na wakati mwingi kutunza vitu vya kimwili visivyo vya lazima? Kadiri tunavyokuwa na vitu vingi, ndivyo tunavyotumia pesa nyingi kuvitunza, kuvilipia bima, na kuvilinda. Je, tunaweza kunufaika kwa kufanya maisha yetu yawe rahisi kwa kuondoa vitu fulani?

      Hakikisha Kwamba Uko Tayari

      20, 21. (a) Mtume Petro anatoa uhakikisho gani kuhusu siku ya Yehova? (b) Ni matendo na vitendo gani tunavyopaswa kuendelea kufanya huku tukiwa tayari kwa ajili ya siku ya Yehova?

      20 Ulimwengu wa siku za Noa ulifikia mwisho wake, nao mfumo huu wa mambo pia utafikia mwisho. Mtume Petro anatuhakikishia hivi: “Siku ya Yehova itakuja kama mwizi, ambayo katika hiyo mbingu zitapitilia mbali kwa kelele ya kuvuma, lakini vitu vyake vya msingi vikiwa moto sana vitayeyushwa, na dunia na kazi zilizo ndani yake zitafunuliwa.” Mbingu za mfano, yaani serikali mbovu, na dunia ya mfano, yaani wanadamu waliotengwa na Mungu, havitaokoka hasira kali ya Mungu inayowaka. Akionyesha jinsi tunavyoweza kuwa tayari kwa ajili ya siku hiyo, Petro anasema: “Kwa kuwa hivyo vitu vyote vitayeyushwa jinsi hiyo, ninyi mnapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu, mkingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova!”—2 Petro 3:10-12.

      21 Baadhi ya matendo na vitendo vya ujitoaji kimungu ni kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida na kushiriki katika kuhubiri habari njema. Na tufanye mambo hayo kwa kujitoa kwa Mungu kwa moyo wote huku tukisubiri siku kuu ya Yehova. Acheni ‘tufanye yote tuwezayo ili mwishowe Mungu atupate tukiwa bila doa na bila dosari na tukiwa katika amani.’—2 Petro 3:14.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki