-
Watu Wengi Wanaogopa Nini Hasa?Mnara wa Mlinzi—2010 | Agosti 1
-
-
Watu Wengi Wanaogopa Nini Hasa?
“Si wanadini tu wanaoamini kwamba karibuni wanadamu watakabili msiba mkubwa.”—STEPHEN O’LEARY, PROFESA MSAIDIZI WA CHUO KIKUU CHA SOUTHERN CALIFORNIA.a
JE, UNAKUBALIANA na maoni hayo? Sehemu zifuatazo zinaonyesha baadhi ya sababu zinazofanya watu waogope mambo yatakayotukia wakati ujao. Pia, zinaonyesha kwa nini unaweza kuwa na hakika kwamba uhai hautakoma duniani. Ijapokuwa habari zinazofuata ni zenye kushtua, kuna sababu nzuri za kutarajia mema.
Bado kuna uwezekano mkubwa wa vita vya nyuklia kuzuka. Mwaka wa 2007, wanasayansi walionya katika gazeti lao la Bulletin of the Atomic Scientists kwamba mwaka huo ulimwengu ulikuwa ukikabili maamuzi hatari kama yale uliokabili wakati ambapo mabomu ya kwanza ya atomiki yaliangushwa jijini Hiroshima na Nagasaki. Kwa nini kuna wasiwasi huo? Gazeti la Bulletin lilisema kwamba katika mwaka wa 2007, bado kulikuwa na silaha 27,000 hivi za nyuklia, na 2,000 kati ya hizo “zilikuwa zimewekwa tayari, na zingeweza kutumiwa wakati wowote.” Hata kama silaha chache tu kati ya hizo zingelipuliwa, bado zingesababisha uharibifu mkubwa sana!
Je, uwezekano wa kuzuka kwa vita vya nyuklia umepungua tangu wakati huo? Kitabu cha Mwaka cha SIPRI cha 2009 (cha Kiingereza)bc kinasema kwamba nchi tano zenye silaha nyingi sana za nyuklia, yaani, China, Marekani, Ufaransa, Uingereza, na Urusi, “zinaendelea kuweka silaha za nyuklia ziwe tayari kutumiwa, au zinakusudia kufanya hivyo.” Lakini kitabu hicho cha mwaka kinasema kwamba si nchi hizo tu ambazo zina silaha za nyuklia. Watafiti wanakadiria kwamba kila moja kati ya nchi ya India, Pakistan, na Israeli, ina mabomu 60 hadi 80 ya nyuklia. Wanasema pia kwamba duniani kote kuna silaha 8,392 za nyuklia ambazo ziko tayari kutumiwa!
Huenda mabadiliko ya hali ya hewa yakaleta msiba. Gazeti la wanasayansi linalotajwa hapo juu linasema kwamba “madhara ambayo huenda yakasababishwa na mabadiliko ya hali ya hewa, yanaweza kuwa mabaya kama tu madhara ambayo silaha za nyuklia zinaweza kusababisha.” Wanasayansi wanaoheshimiwa, kama vile Stephen Hawking ambaye ni profesa aliyestaafu wa hisabati kwenye Chuo Kikuu cha Cambridge, na Bwana Martin Rees, Mkuu wa Chuo cha Trinity kwenye Chuo Kikuu cha Cambridge, wanatoa maonyo kama hayo yenye kutia hofu. Wanaamini kwamba huenda maisha duniani yakabadilika kabisa au hata ustaarabu ukakoma kwa sababu wanadamu wametumia tekinolojia bila kufikiria matokeo ya baadaye, na utendaji wao umesababisha mabadiliko ya mazingira.
Utabiri kuhusu siku ya maangamizi unawatia watu wengi hofu. Chapa maneno “mwisho wa ulimwengu” kwa Kiingereza, na mwaka wa “2012” kwenye kituo fulani cha Intaneti, na utapata habari nyingi sana kuhusu makisio ya watu wanaoamini kwamba mwisho utakuja mwaka huo. Kwa nini? Mwaka wa 2012 umekadiriwa kuwa mwaka wa mwisho katika kalenda fulani ya kale ya Wamaya. Watu wengi wanahofu kwamba mwaka huo ustaarabu uliopo utakwisha kwa njia moja au nyingine.
Wanadini wengi wanaamini kwamba Biblia inafundisha kuwa dunia halisi itaharibiwa. Wengine wanaamini kwamba watu wote waaminifu wataenda mbinguni, na wanadamu wengine wataachwa wakiteseka kwenye dunia yenye msukosuko au kutupwa motoni.
Je, Biblia inasema kwamba hali duniani zitaharibika kabisa au dunia yenyewe itaharibiwa? Mtume Yohana alionya: “Msiamini kila neno lililoongozwa na roho, lakini yajaribuni maneno yaliyoongozwa na roho ili kuona kama yanatokana na Mungu.” (1 Yohana 4:1) Badala ya kuamini tu maneno ya watu wengine, fungua Biblia yako na ujisomee mambo ambayo inasema kuhusu mwisho wa ulimwengu. Huenda ukashangaa unapoona mambo inayofundisha.
[Maelezo ya Chini]
a Maneno haya yamenukuliwa kutoka katika makala “Misiba ya Hivi Karibuni Inawachochea Watu Watabiri Siku ya Maangamizi.” Makala hii ilipatikana kwenye kituo cha Intaneti cha MSNBC, Oktoba 19, 2005 (19/10/2005).
b SIPRI ni kifupisho cha Taasisi ya Utafiti Kuhusu Amani ya Kimataifa ya Stockholm.
c Ripoti hiyo katika Kitabu cha Mwaka cha SIPRI cha 2009 iliandikwa na Shannon N. Kile, mtafiti mkuu na msimamizi wa mradi wa silaha za nyuklia wa Kitengo cha SIPRI cha Kudhibiti na Kuzuia Kuenea kwa Silaha; Vitaly Fedchenko, mtafiti wa Kitengo cha Kudhibiti na Kuzuia Kuenea kwa Silaha; na Hans M. Kristensen, mkurugenzi wa mradi wa kutoa habari za mambo ya nyuklia wa Shirika la Wanasayansi wa Marekani.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]
Mushroom cloud: U.S. National Archives photo; hurricane photos: WHO/League of Red Cross and U.S. National Archives photo
-
-
Maswali Manne Kuhusu Mwisho YajibiwaMnara wa Mlinzi—2010 | Agosti 1
-
-
Maswali Manne Kuhusu Mwisho Yajibiwa
YESU KRISTO alitabiri kwamba ‘mwisho utakuja.’ Alisema hivi alipozungumzia mwisho huo: “Ndipo kutakapokuwa na dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatukia tena.”—Mathayo 24:14, 21.
Maneno ya Yesu kuhusu mwisho, na maandiko mengine ya Biblia yanayozungumzia habari hii, yanazusha maswali kadhaa muhimu. Ebu fungua Biblia yako na uone jinsi inavyojibu maswali hayo.
1 Ni Mwisho wa Nini?
Biblia haifundishi kwamba dunia yenyewe itaharibiwa. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “[Mungu] ameiwekea dunia msingi juu ya mahali pake palipofanywa imara; haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.” (Zaburi 104:5) Wala Biblia haifundishi kwamba viumbe wote duniani watateketezwa kwa moto. (Isaya 45:18) Yesu mwenyewe alisema kwamba kuna watu ambao wataokoka mwisho. (Mathayo 24:21, 22) Basi, Biblia inaonyesha mwisho huo ni mwisho wa nini?
Mwisho wa serikali za wanadamu ambazo zimepungukiwa. Mungu alimwongoza nabii Danieli kuandika hivi: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Danieli 2:44.
Mwisho wa vita na uchafuzi wa mazingira. Andiko la Zaburi 46:9 linaonyesha mambo ambayo Mungu atafanya: “Anakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia. Upinde anauvunja na kuukata mkuki vipande-vipande; magari ya kukokotwa anayateketeza motoni.” Biblia inafundisha pia kwamba Mungu ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’—Ufunuo 11:18.
Mwisho wa uhalifu na ukosefu wa haki. Neno la Mungu linaahidi: “Wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake. Nao waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani; nao wenye hila, watang’olewa kutoka ndani yake.”a—Methali 2:21, 22.
2 Mwisho Utakuja Lini?
Yehova Mungu ‘ameweka wakati’ ambapo atakomesha maovu na wakati Ufalme wake utakapoanza kutawala dunia nzima. (Marko 13:33) Lakini Biblia inaonyesha wazi kwamba hatuwezi kujua tarehe hususa ya mwisho. Yesu alisema hivi: “Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.” (Mathayo 24:36) Hata hivyo, Yesu na wanafunzi wake walitabiri jinsi ambavyo hali zingekuwa duniani kabla ya Mungu kuleta mwisho. Mwisho unakaribia wakati ambapo matukio yote yanayotajwa hapa chini yanatukia kotekote duniani, kwa wakati uleule.
Matatizo ya mazingira, ya kisiasa, na ya kijamii, yanaongezeka sana kuliko wakati mwingine wowote. Yesu alipojibu maswali ya wanafunzi wake kuhusu mwisho, alisema hivi: “Taifa litasimama kupigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme, kutakuwa na matetemeko ya nchi mahali pamoja baada ya pengine, kutakuwa na upungufu wa chakula. Hayo ni mwanzo wa maumivu ya taabu.” (Marko 13:8) Mtume Paulo aliandika: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.”—2 Timotheo 3:1-5.
Habari njema zinahubiriwa katika lugha nyingi duniani kote. Yesu alisema hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.
3 Ni Nini Kitakachotukia Baada ya Mwisho?
Biblia haifundishi kwamba watu wote wema watachukuliwa kutoka duniani ili waishi milele mbinguni kwa furaha. Badala yake, Yesu alifundisha kwamba kusudi la awali la Mungu kuwahusu wanadamu litatimizwa. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mathayo 5:5; 6:9, 10) Biblia inaahidi kwamba wale wanaokufa kabla ya mwisho, watafufuliwa wakati ujao.—Ayubu 14:14, 15; Yohana 5:28, 29.
Yesu ambaye ni Mfalme wa Ufalme wa Mungu, atatawala dunia akiwa mbinguni. Nabii Danieli aliandika hivi: “Nikaendelea kuona katika maono ya usiku, na, tazama! mtu fulani kama mwana wa binadamu [Yesu baada ya kufufuliwa] alikuwa anakuja na mawingu ya mbingu; naye akaja kwa Mzee wa Siku [Yehova Mungu], nao wakamleta karibu mbele zake Yule. Naye [Yesu] akapewa utawala na heshima na ufalme, ili vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha vimtumikie yeye. Utawala wake ni utawala unaodumu mpaka wakati usio na kipimo ambao hautapitilia mbali, na ufalme wake ni ufalme ambao hautaharibiwa.”—Danieli 7:13, 14; Luka 1:31, 32; Yohana 3:13-16.
Raia wa Ufalme wa Mungu watakuwa na afya bora, usalama wa kudumu, na uzima wa milele. Nabii Isaya aliandika: “Hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake; hawatapanda na mtu mwingine ale.” (Isaya 65:21-23) Mtume Yohana naye aliandika hivi kuhusu wakati huo: “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:3, 4.
4 Ni Lazima Ufanye Nini ili Uokoke Mwisho?
Mtume Petro alitambua kwamba baadhi ya watu ambao wangeishi katika siku za mwisho wangedhihaki na kusema kwamba Mungu hataingilia shughuli za wanadamu ili kukomesha maovu duniani. (2 Petro 3:3, 4) Basi, Petro anawahimiza watu wanaoishi katika siku zetu wachukue hatua zinazotajwa hapa chini.
Jifunze kutokana na historia. Petro aliandika kwamba Mungu “hakujizuia kuuadhibu ulimwengu wa kale, bali alimlinda Noa, mhubiri wa uadilifu, akiwa salama pamoja na wengine saba alipoleta gharika juu ya ulimwengu wa watu wasiomwogopa Mungu.” (2 Petro 2:5) Pia, aliandika hivi kuwahusu wadhihaki: “Kulingana na kupenda kwao, wao hawalioni jambo hili, kwamba mbingu zilikuwapo tangu zamani za kale na dunia ikisimama imara kutoka katika maji na katikati ya maji kwa neno la Mungu; na kwa njia hizo ulimwengu wa wakati huo uliangamia kwa gharika ya maji. Lakini kwa neno hilohilo mbingu na duniab za sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto nazo zinahifadhiwa mpaka ile siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.”—2 Petro 3:5-7.
Ishi kupatana na kanuni za maadili za Mungu. Mtume Petro aliandika kwamba watu ambao wanataka kuokoka mwisho wangekuwa na “matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu.” (2 Petro 3:11) Ona kwamba Petro anakazia “matendo matakatifu ya mwenendo” na “vitendo vya ujitoaji-kimungu.” Kwa hiyo, haitoshi tu kudai kuwa na imani, wala kumkimbilia Mungu dakika ya mwisho.
Mungu anakubali matendo na vitendo gani hususa? Tunakualika ulinganishe mambo unayojua na kile ambacho Biblia inasema kuhusu habari hii. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia. Waombe wakuonyeshe jinsi Biblia yako inavyounga mkono majibu yao. Huenda jambo hilo likakusaidia kuwa na matumaini na moyo mkuu unapokabili mambo yatakayokuja wakati ujao, ijapokuwa kuna mambo mengi yanayotutisha wakati huu.
[Maelezo ya Chini]
a Ona pia makala yenye kichwa “Je, Watu Wote Wana Nafasi Sawa za Kupata Kumjua Mungu?” kwenye ukurasa wa 22 wa gazeti hili.
b Katika andiko hilo Petro anazungumzia dunia ya mfano. Musa, mwandikaji mwingine wa Biblia, alizungumzia pia dunia ya mfano. Aliandika hivi: “Dunia yote iliendelea kuwa na lugha moja.” (Mwanzo 11:1) Dunia halisi haiwezi kuzungumza “lugha moja,” hali kadhalika, si dunia halisi itakayoharibiwa. Lakini kama Petro anavyosema, ni watu wasiomwogopa Mungu watakaoangamizwa.
[Blabu katika ukurasa wa 7]
Dunia haitaharibiwa, bali watu ambao wanaiharibu wataangamizwa
-