-
Ayubu—Mtu Mvumilivu na MtimilifuMnara wa Mlinzi—2006 | Agosti 15
-
-
Ayubu—Mtu Mvumilivu na Mtimilifu
“Je, umeuweka moyo wako juu ya mtumishi wangu Ayubu, kwamba hakuna yeyote aliye kama yeye duniani, mtu asiye na lawama na mnyoofu, mwenye kumwogopa Mungu na kujiepusha na ubaya?”—AYUBU 1:8.
1, 2. (a) Ayubu alipatwa na misiba gani? (b) Eleza jinsi maisha ya Ayubu yalivyokuwa kabla ya misiba hiyo.
MTU fulani alikuwa na vitu vingi vizuri, yaani, mali, umashuhuri, afya nzuri, na familia yenye furaha. Kisha, akapatwa na misiba mara tatu mfululizo. Alipoteza mali zake zote kwa ghafula. Baadaye, dhoruba isiyo ya kawaida ilisababisha kifo cha watoto wake wote. Muda mfupi baada ya hapo, akaugua ugonjwa wenye kudhoofisha uliotokeza majipu yenye maumivu makali kwenye mwili wake wote. Huenda unajua kwamba mtu huyo alikuwa Ayubu, anayezungumziwa hasa katika kitabu cha Biblia kinachoitwa kwa jina lake.—Ayubu, sura ya 1 na ya 2.
2 Ayubu aliomboleza hivi: “Laiti ningekuwa kama nilivyokuwa katika miezi ya zamani.” (Ayubu 3:3; 29:2) Msiba unapotokea, kila mtu hutamani siku zilizopita. Ayubu aliishi maisha mazuri kana kwamba alikuwa amelindwa kutokana na mabaya. Watu mashuhuri walimheshimu na kutafuta mashauri kutoka kwake. (Ayubu 29:5-11) Ingawa alikuwa tajiri, alikuwa na maoni yanayofaa kuhusu pesa. (Ayubu 31:24, 25, 28) Aliwasaidia wajane na mayatima waliokuwa na uhitaji. (Ayubu 29:12-16) Naye alikuwa mwaminifu kwa mke wake.—Ayubu 31:1, 9, 11.
3. Yehova alimwonaje Ayubu?
3 Ayubu hakuwa na lawama kwa sababu alimwabudu Mungu. “Hakuna yeyote aliye kama yeye duniani,” Yehova akasema, “mtu asiye na lawama na mnyoofu, mwenye kumwogopa Mungu na kujiepusha na ubaya.” (Ayubu 1:1, 8) Lakini, ingawa Ayubu alifuata maadili, misiba ilisambaratisha maisha yake. Kila kitu alichokuwa nacho kilitoweka, na sifa zake zilijaribiwa na uchungu mwingi aliohisi, maumivu yake ya kihisia, na kuvunjika moyo.
4. Kwa nini tutafaidika kwa kuchunguza majaribu ambayo Ayubu alikabili?
4 Bila shaka, kuna wengi miongoni mwa watumishi wa Mungu ambao wameteseka kama Ayubu. Leo, Wakristo wengi wanateseka, na hivyo wanaweza kuelewa hali iliyompata Ayubu. Hivyo, tunapaswa kufikiria maswali haya mawili: Kuchunguza majaribu ambayo Ayubu alikabili kunaweza kutusaidiaje tunapokabili msiba? Na majaribu hayo yanaweza kutusaidiaje kuwahurumia wengine wanapoteseka?
Suala la Ushikamanifu na Jaribu la Utimilifu
5. Shetani alidai kwamba Ayubu alimtumikia Mungu kwa sababu gani?
5 Kisa cha Ayubu kilikuwa cha pekee. Bila Ayubu kujua, Ibilisi alikuwa ametilia shaka kusudi la Ayubu la kumtumikia Mungu. Katika mkutano uliofanyiwa mbinguni, Yehova alitaja sifa nzuri za Ayubu, naye Shetani akajibu hivi: “Je, wewe hukuweka ukuta kumzunguka yeye na kuzunguka nyumba yake na kuzunguka kila kitu alicho nacho pande zote?” Hivyo, Shetani alidai kwamba Ayubu alichochewa na ubinafsi, na hivyo dai hilo likatia ndani watumishi wengine wote wa Mungu. Shetani alimwambia Yehova hivi: “Tafadhali nyoosha mkono wako, uguse kila kitu alicho nacho, uone kama hatakulaani wewe mbele za uso wako.”—Ayubu 1:8-11.
6. Shetani alizusha suala gani muhimu?
6 Hilo lilikuwa suala muhimu. Shetani alitilia shaka njia ya Yehova ya kutawala. Je, kweli inawezekana Mungu autawale ulimwengu kwa upendo? Au kama vile Shetani alivyodokeza, je, sikuzote ubinafsi utafanikiwa? Yehova alimruhusu Ibilisi amjaribu Ayubu huku akiwa na uhakika kwamba mtumishi Wake angedumisha utimilifu na ushikamanifu, na jaribu hilo likawa mfano. Hivyo, Shetani ndiye aliyesababisha matatizo yaliyompata Ayubu kwa mfululizo. Shetani aliposhindwa katika mashambulizi yake ya kwanza, alimpiga Ayubu kwa ugonjwa wenye maumivu makali. Ibilisi alidai hivi: “Ngozi kwa ngozi, na kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake.”—Ayubu 2:4.
7. Ni kwa njia gani watumishi wa Mungu leo hukabili majaribu kama ya Ayubu?
7 Ingawa Wakristo wengi leo hawateseki kama Ayubu, wanakabili dhiki za aina mbalimbali. Wengi wao hukabili mateso au matatizo ya familia. Pia, matatizo ya kiuchumi au magonjwa yanaweza kulemea. Baadhi yao wamekufa kwa sababu ya imani yao. Bila shaka, hatupaswi kufikiri kwamba kila tatizo tunalokabili husababishwa na Shetani. Huenda matatizo mengine yakasababishwa na makosa yetu au hali tuliyorithi. (Wagalatia 6:7) Sisi sote huathiriwa na uzee na misiba ya asili. Biblia inaeleza waziwazi kwamba leo Yehova hawalindi kimuujiza watumishi wake wasipatwe na matatizo hayo.—Mhubiri 9:11.
8. Shetani anaweza kutumiaje matatizo tunayokabili?
8 Hata hivyo, huenda Shetani akatumia matatizo tunayokabili ili kudhoofisha imani yetu. Mtume Paulo alitaja kwamba alisumbuliwa na “mwiba katika mwili, malaika wa Shetani,” aliyeendelea kumpiga “kofi.” (2 Wakorintho 12:7) Iwe alikuwa na matatizo ya afya, kama vile matatizo ya macho au tatizo lingine, Paulo alijua kwamba Shetani angetumia matatizo hayo na matokeo yake ili kumnyang’anya shangwe na utimilifu wake. (Methali 24:10) Leo, huenda Shetani akawachochea watu wa familia, wanashule, au hata serikali za kimabavu kuwatesa watumishi wa Mungu kwa njia fulani.
9. Kwa nini hatupaswi kushangaa sana tunapokabili shida au mateso?
9 Tunaweza kukabilianaje na matatizo hayo kwa mafanikio? Tunaweza kufanikiwa tukiyaona kuwa njia ya kuthibitisha kwamba tunampenda Yehova na tunajitiisha chini ya utawala wake. (Yakobo 1:2-4) Hata matatizo yetu yawe yanasababishwa na nini, kuelewa maana ya kuwa mshikamanifu kwa Mungu kutatusaidia tuendelee kuwa thabiti kiroho. Mtume Petro aliwaandikia Wakristo hivi: “Wapendwa, msishangazwe juu ya moto unaowaka katikati yenu, unaowapata ninyi ili kuwa jaribu, kana kwamba jambo geni linawapata.” (1 Petro 4:12) Naye Paulo akaeleza hivi: “Wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Timotheo 3:12) Bado Shetani anatilia shaka utimilifu wa Mashahidi wa Yehova, kama alivyofanya katika kisa cha Ayubu. Biblia inaonyesha kwamba Shetani amezidisha mashambulizi yake juu ya watu wa Mungu hasa katika hizi siku za mwisho.—Ufunuo 12:9, 17.
Kutoelewa Mambo na Mashauri Mabaya
10. Ayubu alikabili tatizo gani?
10 Ayubu alikabili tatizo ambalo hatuhitaji kukabili. Hakujua kwa nini alipatwa na misiba. Ayubu alikata kauli kimakosa kwamba “Yehova [alitoa], na Yehova [alichukua].” (Ayubu 1:21) Huenda Shetani alijaribu kimakusudi kumfanya Ayubu aamini kwamba Mungu ndiye aliyesababisha mateso yake.
11. Eleza jinsi Ayubu alivyotenda alipoteseka.
11 Ayubu alivunjika moyo sana, lakini alikataa kumlaani Mungu kama mke wake alivyomsihi afanye. (Ayubu 2:9, 10) Alisema hivi: ‘Waovu wanafanikiwa sana kuliko mimi.’ (Ayubu 21:7-9) Haikosi aliwaza hivi: ‘Kwa nini Mungu ananiadhibu?’ Wakati mwingine alitamani kufa. Alisema hivi: “Laiti ungenificha katika Kaburi, kwamba ungenificha mpaka hasira yako igeuke!”—Ayubu 14:13.
12, 13. Maneno ya wale marafiki watatu wa Ayubu yalimwathirije?
12 Marafiki watatu walimtembelea Ayubu ili ‘wamsikitikie na kumfariji.’ (Ayubu 2:11) Lakini, walithibitika kuwa “wafariji wasumbufu.” (Ayubu 16:2) Huenda Ayubu angefaidika ikiwa angepata marafiki ambao angewaeleza matatizo yake, lakini wafariji hao watatu walimfanya Ayubu achanganyikiwe hata zaidi na kukata tamaa zaidi.—Ayubu 19:2; 26:2.
13 Huenda Ayubu alijiuliza hivi: ‘Kwa nini mimi niteseke? Nimefanya nini ili niteseke hivi?’ Marafiki wake walimpa majibu yenye kupotosha kabisa. Waliwazia kwamba Ayubu alikuwa ametenda dhambi fulani nzito na ndiyo sababu alikuwa anateseka. “Je, ni nani aliyepata kuangamia bila hatia?” Elifazi akauliza. “Kulingana na yale ambayo nimeona, wale wanaotunga madhara na wale wanaopanda taabu wataivuna wenyewe.”—Ayubu 4:7, 8.
14. Kwa nini hatupaswi kuhusianisha kuteseka na mwenendo usiofaa?
14 Ni kweli kwamba matatizo yanaweza kutokea ikiwa tunapanda kwa mwili badala ya kupanda kwa roho. (Wagalatia 6:7, 8) Hata hivyo, katika mfumo huu wa sasa, tunaweza kupatwa na matatizo hata mwenendo wetu uweje. Isitoshe, hatuwezi kusema kwamba wasio na hatia hawawezi kupatwa na msiba. Ingawa Yesu Kristo hakuwa na ‘unajisi na alitengwa kutoka kwa watenda-dhambi,’ bado alikufa kwa maumivu juu ya mti wa mateso, na mtume Yakobo alifia imani. (Waebrania 7:26; Matendo 12:1, 2) Elifazi na marafiki wake wawili walifikiri kimakosa na hivyo kumfanya Ayubu ajitetee na kusisitiza kwamba hakuwa na hatia. Lakini, huenda madai yao ya ukaidi kwamba Ayubu alistahili kuteseka yaliathiri maoni yake kuhusu haki ya Mungu.—Ayubu 34:5; 35:2.
Kutafuta Msaada Tunapokabili Dhiki
15. Tunapoteseka, inafaa tuwe na maoni gani?
15 Tunajifunza nini kutokana na yaliyompata Ayubu? Huenda tukahisi kwamba hatustahili kupatwa na misiba, magonjwa, au mateso. Ni kana kwamba watu wengine hawateseki. (Zaburi 73:3-12) Wakati mwingine, huenda tukahitaji kujiuliza maswali haya muhimu: ‘Je, upendo wangu kwa Mungu unanichochea nimtumikie hata hali ziweje? Je, ninatamani kumpa Yehova “jibu kwa yule anayemdhihaki?”’ (Methali 27:11; Mathayo 22:37) Tusiruhusu kamwe mambo ambayo watu wanasema bila kufikiri yatufanye tumtilie shaka Baba yetu wa mbinguni. Dada mmoja mwaminifu aliyeugua ugonjwa wa kudumu kwa miaka mingi alisema hivi wakati fulani: “Najua kwamba ninaweza kuvumilia chochote ambacho Yehova anaruhusu. Najua atanipa nguvu ninazohitaji. Sikuzote amenipa nguvu.”
16. Neno la Mungu huwasaidiaje wale walio na matatizo?
16 Tofauti na Ayubu, sisi tunaelewa vizuri zaidi ujanja wa Shetani. “Hatukosi kuzijua mbinu zake,” au hila zake mbovu. (2 Wakorintho 2:11) Isitoshe, tuna chanzo cha hekima nyingi. Katika Biblia, tunapata masimulizi ya wanaume na wanawake waaminifu waliovumilia matatizo ya aina yote. Mtume Paulo, aliyeteseka zaidi kuliko wengine wengi, aliandika hivi: “Kwa maana mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” (Waroma 15:4) Shahidi mmoja huko Ulaya ambaye alifungwa kwa sababu ya imani yake wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, alitoa chakula chake cha siku tatu ili apate Biblia. Anasema: “Nilifaidika sana kwa kufanya hivyo! Licha ya njaa ya kimwili, nilipokea chakula cha kiroho kilichoniimarisha mimi pamoja na wengine katika majaribu yetu wakati huo wa taabu. Nimeitunza Biblia hiyo mpaka leo.”
17. Ni maandalizi gani kutoka kwa Mungu yanayoweza kutusaidia kuvumilia?
17 Mbali na faraja kutoka katika Maandiko, tuna vifaa vingi vinavyotusaidia kuielewa Biblia na vinavyotoa mwongozo unaofaa ili kukabiliana na shida. Ukitumia Watch Tower Publications Index, yaelekea utapata masimulizi ya Mkristo ambaye amepatwa na jaribu kama lako. (1 Petro 5:9) Pia, unaweza kufaidika ukiwaeleza wazee wenye huruma au Wakristo wengine wakomavu kuhusu hali yako. Zaidi ya yote, unaposali, unaweza kupata msaada kutoka kwa Yehova na roho yake takatifu. Paulo aliyakabilije ‘makofi’ ya Shetani? Kwa kujifunza kutegemea nguvu za Mungu. (2 Wakorintho 12:9, 10) Aliandika hivi: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.”—Wafilipi 4:13.
18. Wakristo wenzetu wanaweza kututiaje moyo sana?
18 Kwa hiyo, kuna msaada, nawe usisite kuutafuta. Methali moja inasema: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” (Methali 24:10) Kama vile mchwa wanavyoweza kuiangusha nyumba ya mbao, ndivyo kuvunjika moyo kunavyoweza kudhoofisha utimilifu wa Mkristo. Ili kushinda hatari hiyo, Yehova anatuandalia msaada kupitia watumishi wenzetu. Usiku ambao Yesu alikamatwa, malaika alimtokea na kumtia nguvu. (Luka 22:43) Akisafiri kuelekea Roma akiwa mfungwa, Paulo ‘alimshukuru Mungu na kujipa moyo’ alipokutana na akina ndugu katika Soko la Apio na Mikahawa Mitatu. (Matendo 28:15) Shahidi mmoja Mjerumani bado anakumbuka msaada aliopata alipofika katika kambi ya mateso ya Ravensbrück akiwa kijana mwoga mwenye umri wa chini ya miaka 20. Anasema hivi: “Mkristo mwenzangu aliniona mara moja na kunikaribisha kwa uchangamfu. Dada mwingine mwaminifu alinitunza, naye akawa kama mama yangu wa kiroho.”
“Uwe Mwaminifu”
19. Ni nini kilichomsaidia Ayubu kupinga jitihada za Shetani?
19 Yehova alimtaja Ayubu kuwa mtu ‘aliyeshikilia sana utimilifu wake.’ (Ayubu 2:3) Licha ya kuvunjika moyo na kutoelewa chanzo cha matatizo yake, Ayubu aliendelea kuwa imara kuhusiana na suala muhimu la ushikamanifu. Ayubu alikataa kuacha utimilifu wake. Alisisitiza hivi: “Mpaka nitakapokata pumzi, sitajiondolea utimilifu wangu!”—Ayubu 27:5.
20. Kwa nini sifa ya uvumilivu ni muhimu?
20 Azimio kama hilo litatusaidia kudumisha utimilifu wetu chini ya hali zozote, tuwe tunakabili vishawishi, upinzani, au taabu. Yesu aliliambia kutaniko la Smirna hivi: “Usiogope mateso ambayo yanakaribia kukupata. Tazama! Ibilisi ataendelea kuwatupa gerezani baadhi yenu ili mjaribiwe kwa ukamili, na ili muwe na dhiki [shida, taabu, au uonevu] siku kumi. Uwe mwaminifu hata kufikia kifo, nami nitakupa taji la uzima.”—Ufunuo 2:10.
21, 22. Tunapovumilia dhiki, tunaweza kupata faraja kwa kujua jambo gani?
21 Uvumilivu na utimilifu wetu utajaribiwa katika mfumo huu unaotawaliwa na Shetani. Hata hivyo, Yesu anatuhakikishia kwamba hatuna sababu ya kuogopa tunapoendelea kutarajia wakati ujao. Jambo muhimu ni kuwa waaminifu. “Dhiki ni ya dakika,” akasema Paulo, lakini “utukufu” au zawadi ambayo Yehova anatuahidi ‘ni yenye uzito mkubwa zaidi na zaidi na ni ya milele.’ (2 Wakorintho 4:17, 18) Hata dhiki ya Ayubu ilikuwa ya dakika ikilinganishwa na furaha aliyokuwa nayo kwa miaka mingi kabla na baada ya jaribu hilo.—Ayubu 42:16.
22 Lakini, huenda wakati fulani maishani tukahisi kwamba majaribu yetu hayaishi na kwamba hatuwezi kuvumilia mateso tunayokabili. Katika makala inayofuata, tutazungumzia jinsi kisa cha Ayubu kinavyoweza kutufundisha mengi zaidi kuhusu uvumilivu. Pia, tutajifunza jinsi ya kuwaimarisha wale wanaokabili matatizo.
-
-
“Mmesikia Juu ya Uvumilivu wa Ayubu”Mnara wa Mlinzi—2006 | Agosti 15
-
-
“Mmesikia Juu ya Uvumilivu wa Ayubu”
“Mmesikia juu ya uvumilivu wa Ayubu nanyi mmeona matokeo ambayo Yehova alileta, kwamba Yehova ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema.”—YAKOBO 5:11.
1, 2. Wenzi fulani wa ndoa huko Poland walikabili jaribu gani?
HARALD ABT alikuwa Shahidi wa Yehova kwa muda usiozidi mwaka mmoja wakati majeshi ya Hitler yalipoteka jiji la Danzig (ambalo sasa ni Gdańsk) kaskazini mwa Poland. Kisha, hali ikawa mbaya na hatari kwa Wakristo wa kweli waliokuwa huko. Polisi wa siri wa Nazi walijaribu kumlazimisha Harald atie sahihi hati ya kukana imani yake, lakini alikataa. Baada ya majuma kadhaa gerezani, Harald alipelekwa katika kambi ya mateso ya Sachsenhausen, ambapo alitishwa na kupigwa mara nyingi. Ofisa mmoja alimwonyesha Harald bomba la kutolea moshi la mahali pa kuteketeza maiti na akamwambia hivi: “Ukiendelea kushikilia imani yako, baada ya siku 14 utateketezwa na kupanda kwa Yehova wako kupitia lile bomba.”
2 Wakati Harald alipokamatwa, mke wake, Elsa, alikuwa bado anamnyonyesha binti yao mwenye umri wa miezi kumi. Lakini, polisi wa siri wa Nazi hawakumwacha Elsa. Muda mfupi baadaye, mtoto wake alichukuliwa, naye Elsa akapelekwa katika kambi ya maangamizi ya Auschwitz. Hata hivyo, yeye pia aliendelea kuvumilia kwa miaka mingi kama Harald. Unaweza kusoma habari zaidi kuhusu jinsi walivyovumilia katika gazeti la Kiingereza la Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 1980. Harald aliandika hivi: “Kwa jumla, nilitumia miaka 14 ya maisha yangu katika kambi za mateso na gerezani kwa sababu ya kumwamini Mungu. Nimewahi kuulizwa hivi: ‘Je, mke wako alikusaidia kuvumilia mateso hayo?’ Bila shaka! Nilijua tangu mwanzo kwamba hataacha imani yake kamwe, na kujua hivyo kuliniimarisha sana. Nilijua angependa nife nikiwa mwaminifu kuliko kuachiliwa kwa sababu ya kukana imani. . . . Kwa miaka yote aliyokuwa katika kambi za mateso huko Ujerumani, Elsa alivumilia mateso mengi.”
3, 4. (a) Ni vielelezo vya akina nani vinavyoweza kuwatia moyo Wakristo kuvumilia? (b) Kwa nini Biblia inatusihi tuchunguze kisa cha Ayubu?
3 Mashahidi wengi wanaweza kuthibitisha kwamba si rahisi mtu kuvumilia anapoteseka. Kwa hiyo, Biblia inawashauri Wakristo wote hivi: “Wachukueni manabii kuwa kielelezo cha kupatwa na uovu na kuonyesha subira, wale waliosema katika jina la Yehova.” (Yakobo 5:10) Kwa karne nyingi, watumishi wengi wa Mungu wameteswa bila sababu. Vielelezo vya hilo ‘wingu kubwa la mashahidi’ vinaweza kututia moyo tuendelee kukimbia kwa uvumilivu shindano letu la Kikristo.—Waebrania 11:32-38; 12:1.
4 Katika Biblia, Ayubu anatajwa kuwa kielelezo cha uvumilivu. Yakobo aliandika hivi: “Tazama! Tunawatangaza kuwa wenye furaha wale ambao wamevumilia. Mmesikia juu ya uvumilivu wa Ayubu nanyi mmeona matokeo ambayo Yehova alileta, kwamba Yehova ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema.” (Yakobo 5:11) Kisa cha Ayubu kinatuonyesha thawabu ambayo waaminifu wanatarajia kutoka kwa Yehova ambaye huwabariki. Zaidi ya hilo, kinafunua kweli zitakazotunufaisha wakati wa shida. Kitabu cha Ayubu kinatusaidia kujibu maswali haya: Tunapojaribiwa, kwa nini ni muhimu kuelewa masuala muhimu yanayohusika? Ni sifa na mitazamo gani ambayo hutusaidia kuvumilia? Tunaweza kuwaimarishaje Wakristo wenzetu wanaoteseka?
Kuelewa Mambo Yote Yanayohusika
5. Ni suala gani kuu tunalopaswa kukumbuka tunapokabili majaribu au vishawishi?
5 Ili kuendelea kuwa thabiti kiroho tunapokabili matatizo, tunahitaji kuelewa masuala yanayohusika. Tusipofanya hivyo, matatizo tunayokabili yanaweza kutukengeusha kiroho. Suala la ushikamanifu kwa Mungu ni muhimu sana. Baba yetu wa mbinguni anatusihi tufanye jambo ambalo kila mmoja wetu anapaswa kufikiria kwa uzito: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.” (Methali 27:11) Hilo ni pendeleo la pekee! Ingawa sisi ni dhaifu na hatujakamilika, tunaweza kumfanya Muumba wetu ashangilie. Tunafanya hivyo wakati upendo wetu kwa Yehova unapotuwezesha kustahimili majaribu na vishawishi. Upendo wa kweli wa Kikristo huvumilia mambo yote. Haushindwi kamwe.—1 Wakorintho 13:7, 8.
6. Shetani humdhihaki Yehova jinsi gani, naye hufanya hivyo kwa kadiri gani?
6 Kitabu cha Ayubu kinamtambulisha waziwazi Shetani kuwa ndiye anayemdhihaki Yehova. Pia, kinafunua mwelekeo mbovu wa adui huyo asiyeonekana na tamaa yake ya kuharibu uhusiano wetu pamoja na Mungu. Kama inavyoonyeshwa katika kisa cha Ayubu, Shetani anamshtaki kila mtumishi wa Yehova kuwa anachochewa na ubinafsi na anajaribu kuonyesha kwamba upendo wao kwa Mungu unaweza kupoa. Amemdhihaki Mungu kwa maelfu ya miaka. Shetani alipotupwa chini kutoka mbinguni, sauti kutoka mbinguni ilimtaja kuwa “mshtaki wa ndugu zetu” na ikasema kwamba yeye huwashtaki “mchana na usiku mbele za Mungu wetu.” (Ufunuo 12:10) Kwa kuvumilia kwa uaminifu, tunaweza kuthibitisha kwamba mashtaka yake hayana msingi.
7. Ni njia gani bora ya kushinda udhaifu wa kimwili?
7 Tunapaswa kukumbuka kwamba Ibilisi atatumia dhiki yoyote tunayokabili ili kujaribu kuharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova. Shetani alimjaribu Yesu wakati gani? Ni wakati Yesu alipoona njaa baada ya kufunga kwa siku nyingi. (Luka 4:1-3) Hata hivyo, nguvu za kiroho zilimwezesha Yesu kukataa katakata vishawishi vya Ibilisi. Ni muhimu sana tushinde udhaifu wowote wa kimwili, uwe umesababishwa na ugonjwa au uzee, kwa kutumia nguvu za kiroho! Ingawa “mtu tuliye kwa nje anachakaa,” hatukati tamaa kwa sababu “mtu tuliye kwa ndani anafanywa upya siku baada ya siku.”—2 Wakorintho 4:16.
8. (a) Hisia zisizofaa zinaweza kutudhoofishaje? (b) Yesu alikuwa na mtazamo gani?
8 Isitoshe, hisia zisizofaa zinaweza kuharibu hali yetu ya kiroho. Huenda mtu akajiuliza, ‘Kwa nini Yehova anaruhusu hali hii?’ Baada ya kutendewa isivyofaa, huenda mwingine akauliza, ‘Ndugu anawezaje kunitendea hivi?’ Hisia hizo zinaweza kutufanya tupuuze masuala muhimu na kukazia fikira hali zetu tu. Mfadhaiko ambao Ayubu alipata kwa sababu ya marafiki wake watatu ambao walisema mambo yaliyopotoka ulimuumiza sana kihisia kama vile ugonjwa wake ulivyomdhoofisha kimwili. (Ayubu 16:20; 19:2) Vilevile, mtume Paulo alionyesha kwamba hasira ya muda mrefu inaweza ‘kumpa Ibilisi nafasi.’ (Waefeso 4:26, 27) Badala ya kuzungumza na wengine kwa hasira au kufikiria sana hali fulani isiyofaa, Wakristo watafaidika wakimwiga Yesu kwa ‘kuendelea kujiweka mkononi mwa yule ambaye anahukumu kwa uadilifu,’ Yehova Mungu. (1 Petro 2:21-23) Kuwa na ‘mwelekeo wa akili’ wa Yesu kunaweza kutulinda sana dhidi ya mashambulizi ya Shetani.—1 Petro 4:1.
9. Mungu anatupa uhakikisho gani kuhusu mizigo tunayobeba na vishawishi tunavyokabili?
9 Zaidi ya yote, tusione kamwe matatizo kuwa uthibitisho wa kwamba Mungu hapendezwi nasi. Hali hiyo ya kutoelewa mambo ilimuumiza Ayubu wakati aliposhambuliwa kwa maneno makali ya watu waliodai kumfariji. (Ayubu 19:21, 22) Biblia inatupa uhakikisho huu: “Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13) Mbali na hilo, Yehova anaahidi kutusaidia kubeba mzigo wowote unaotulemea na kutuandalia njia ya kushinda kishawishi chochote tunachokabili. (Zaburi 55:22; 1 Wakorintho 10:13) Kwa kumkaribia Mungu wakati wa shida, tunaweza kuona mambo kwa njia inayofaa na kufanikiwa kumpinga Ibilisi.—Yakobo 4:7, 8.
Mambo ya Kutusaidia Kuvumilia
10, 11. (a) Ni nini kilichomsaidia Ayubu kuvumilia? (b) Kuwa na dhamiri nzuri kulimsaidiaje Ayubu?
10 Ayubu alishikilia utimilifu wake licha ya hali yake mbaya, kutukanwa na watu waliodai kuwa wafariji wake, na kutojua chanzo cha misiba yake. Tunaweza kujifunza nini kutokana na uvumilivu wake? Bila shaka, uaminifu wake kwa Yehova ndio uliomwezesha kuvumilia. ‘Alimwogopa Mungu na kujiepusha na ubaya.’ (Ayubu 1:1) Hiyo ilikuwa njia yake ya maisha. Hata wakati ambapo hakuelewa kilichofanya mambo yaharibike kwa ghafula, Ayubu alikataa kumkana Yehova. Ayubu aliamini kwamba anapaswa kumtumikia Mungu wakati hali ni nzuri au mbaya.—Ayubu 1:21; 2:10.
11 Pia, kuwa na dhamiri nzuri kulimfariji Ayubu. Ilipoonekana wazi kwamba atakufa, alipata faraja kwa kujua alikuwa amefanya yote awezayo kuwasaidia wengine, alikuwa ameshika viwango vya uadilifu vya Yehova, na kujiepusha na kila namna ya ibada ya uwongo.—Ayubu 31:4-11, 26-28.
12. Ayubu alitendaje baada ya kusaidiwa na Elihu?
12 Ni kweli kwamba Ayubu alihitaji msaada ili kurekebisha maoni yake kuhusu mambo fulani. Ayubu alikubali msaada huo kwa unyenyekevu, na hivyo akavumilia. Elihu alitoa shauri la hekima, naye Ayubu alilisikiliza kwa heshima na kukubali kurekebishwa na Yehova. “Nilisema, lakini sikuwa ninaelewa,” akasema. “Ninayatangua niliyosema, nami ninatubu katika mavumbi na majivu.” (Ayubu 42:3, 6) Licha ya ugonjwa uliokuwa unamsumbua, Ayubu alifurahi kujua kwamba kurekebisha maoni yake kwa njia hiyo kulimsaidia amkaribie Mungu. Ayubu alisema: “Nimepata kujua kwamba [Yehova] unaweza kufanya mambo yote.” (Ayubu 42:2) Kwa sababu Yehova alimfafanulia Ayubu ukuu Wake, Ayubu alielewa wazi zaidi kuwa yeye ni duni sana akilinganishwa na Muumba wake.
13. Ayubu alifaidikaje kwa kuwa mwenye rehema?
13 Hatimaye, Ayubu ni mfano mzuri wa rehema. Wafariji wake wa uwongo walimuumiza sana kihisia, lakini wakati Yehova alipomwomba asali kwa ajili yao, alifanya hivyo. Baadaye, Yehova akamponya Ayubu. (Ayubu 42:8, 10) Ni wazi kwamba kinyongo hakitatusaidia kuvumilia, lakini upendo na rehema zitatusaidia. Tusipoweka kinyongo tunaburudika kiroho, na Yehova hutubariki.—Marko 11:25.
Washauri Wenye Hekima Wanaotusaidia Kuvumilia
14, 15. (a) Mshauri anahitaji kuwa na sifa gani ili aweze kuwafariji wengine? (b) Eleza mambo yaliyomwezesha Elihu afaulu kumsaidia Ayubu.
14 Jambo lingine tunaloweza kujifunza kutokana na kisa cha Ayubu ni umuhimu wa washauri wenye hekima. Hao ni ndugu ‘waliozaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.’ (Methali 17:17) Hata hivyo, kama tunavyoona katika kisa cha Ayubu, washauri wengine wanaweza kuumiza badala ya kufariji. Mshauri mzuri anapaswa kuonyesha hisia-mwenzi, heshima, na fadhili, kama Elihu. Wazee na Wakristo wengine wakomavu wanaweza kuwasaidia akina ndugu waliolemewa na matatizo warekebishe maoni yao, na kwa kufanya hivyo wanaweza kujifunza mengi kutokana na kitabu cha Ayubu.—Wagalatia 6:1; Waebrania 12:12, 13.
15 Kuna mambo mengi mazuri tunayojifunza kutokana na jinsi Elihu alivyoshughulikia hali hiyo. Alisikiliza kwa makini kabla ya kujibu maoni yenye kasoro ya marafiki watatu wa Ayubu. (Ayubu 32:11; Methali 18:13) Elihu alimwita Ayubu kwa jina na kumsihi kama rafiki. (Ayubu 33:1) Tofauti na wale wafariji watatu wa uwongo, Elihu hakujiona kuwa bora kuliko Ayubu. Alisema hivi: “Mimi pia niliumbwa kutoka kwenye udongo.” Hakutaka kumuumiza Ayubu zaidi kwa kuzungumza bila kufikiri. (Ayubu 33:6, 7; Methali 12:18) Badala ya kumchambua Ayubu kwa sababu ya matendo yake ya awali, Elihu alimpongeza kwa uadilifu wake. (Ayubu 33:32) La muhimu hata zaidi ni kwamba Elihu alikuwa na maoni kama ya Mungu kuhusu mambo, naye alimsaidia Ayubu kujua kwamba kamwe Yehova hawezi kutenda isivyo haki. (Ayubu 34:10-12) Alimtia moyo Ayubu amngojee Yehova badala ya kujaribu kujionyesha kuwa mwadilifu. (Ayubu 35:2; 37:14, 23) Bila shaka, wazee Wakristo na wengine wanaweza kufaidika kutokana na mambo hayo.
16. Wafariji watatu wa Ayubu walitumiwaje na Shetani?
16 Shauri la hekima la Elihu lilikuwa tofauti kabisa na maneno yenye kuumiza ya Elifazi, Bildadi, na Sofari. Yehova aliwaambia hivi: “Ninyi hamkusema mambo ya kweli kunihusu.” (Ayubu 42:7) Hata kama walidai kuwa na makusudi mazuri, walitumiwa na Shetani badala ya kuwa marafiki waaminifu. Tangu mwanzo, wote watatu walidai kwamba Ayubu ndiye aliyepaswa kulaumiwa kwa matatizo yaliyompata. (Ayubu 4:7, 8; 8:6; 20:22, 29) Kulingana na Elifazi, Mungu hana imani na watumishi wake, wala hajali ikiwa sisi ni waadilifu au la. (Ayubu 15:15; 22:2, 3) Elifazi hata alimshtaki Ayubu kwa makosa ambayo hakutenda. (Ayubu 22:5, 9) Kwa upande mwingine, Elihu alimsaidia Ayubu kwa njia ya kiroho, na hilo ndilo lengo la kila mshauri mwenye upendo.
17. Tunapaswa kukumbuka nini tunapojaribiwa?
17 Tunaweza kujifunza jambo lingine kuhusu uvumilivu katika kitabu cha Ayubu. Mungu wetu mwenye upendo huona hali yetu na anataka na anaweza kutusaidia kwa njia mbalimbali. Mwanzoni tulisoma kuhusu kisa cha Elsa Abt. Ona mkataa aliofikia: “Kabla ya kukamatwa, nilisoma barua ya dada mmoja aliyeandika kwamba wakati wa majaribu makali, roho ya Yehova hututuliza sana. Nilifikiri kwamba alitia chumvi kidogo. Lakini nilipokabili majaribu, nilitambua kwamba yale aliyosema ni kweli. Kwa hakika, hivyo ndivyo mambo yanavyokuwa. Si rahisi kuwazia hivyo ikiwa hujapata majaribu. Lakini ilikuwa hivyo kwangu. Yehova husaidia.” Elsa hakuwa anazungumzia mambo ambayo Yehova anaweza kufanya au aliwahi kufanya zamani katika siku za Ayubu. Alikuwa anazungumzia wakati wetu. Naam, “Yehova husaidia!”
Mwenye Furaha Ni Mtu Anayevumilia
18. Ayubu alipata faida gani kwa kuvumilia?
18 Wengi wetu hatutakabili matatizo makali kama yale ambayo Ayubu alikabili. Hata tupate majaribu gani katika mfumo huu, tuna sababu nzuri za kudumisha utimilifu wetu kama Ayubu. Kwa kweli, uvumilivu uliboresha maisha ya Ayubu. Ulimfanya awe kamili. (Yakobo 1:2-4) Uliimarisha uhusiano wake na Mungu. Ayubu alisema hivi: “Nimesikia habari zako kwa fununu, lakini sasa jicho langu mwenyewe linakuona wewe.” (Ayubu 42:5) Ayubu alishikilia utimilifu wake na hivyo kumthibitisha Shetani kuwa mwongo. Miaka mingi baadaye, Yehova bado alimtaja Ayubu, mtumishi wake, kuwa kielelezo cha uadilifu. (Ezekieli 14:14) Utimilifu na uvumilivu wake huwachochea watu wa Mungu hata leo.
19. Kwa nini unahisi kwamba uvumilivu ni muhimu?
19 Yakobo alipowaandikia Wakristo wa karne ya kwanza kuhusu uvumilivu, alitaja uradhi unaotokana na kuvumilia. Naye alitumia mfano wa Ayubu kuwakumbusha kwamba Yehova huwapa thawabu watumishi wake waaminifu. (Yakobo 5:11) Tunasoma hivi kwenye Ayubu 42:12: “Naye Yehova akaubariki mwisho wa Ayubu baadaye kuliko mwanzo wake.” Mungu alimpa Ayubu mara mbili ya vitu alivyopoteza, naye akaishi miaka mingi na yenye furaha. (Ayubu 42:16, 17) Vivyo hivyo, maumivu, mateso, au huzuni yoyote ambayo huenda tukavumilia wakati wa mwisho wa mfumo huu wa mambo, itaondolewa na kusahauliwa katika ulimwengu mpya wa Mungu. (Isaya 65:17; Ufunuo 21:4) Tumesikia kuhusu uvumilivu wa Ayubu, na kwa msaada wa Yehova, tumeazimia kumwiga Ayubu. Biblia inaahidi hivi: “Mwenye furaha ni mtu anayeendelea kuvumilia jaribu, kwa sababu akiisha kukubaliwa atapokea taji la uzima, ambalo Yehova aliwaahidi wale wanaoendelea kumpenda.”—Yakobo 1:12.
-