-
Shikamana na Tengenezo la YehovaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
una kazi ya kufanya katika kukamilisha utu wetu wa Kikristo na kutufanya tuwe wenye kukubalika kabisa mbele za Mungu. Naam, uvumilivu wetu huongezeka siku baada ya siku tunapokabiliana na kushinda majaribu. Nao, uvumilivu hutokeza sifa nyingine zenye kupendeza tunazohitaji.
9 Uvumilivu wetu unampendeza Yehova; utamchochea atupe thawabu ya uzima wa milele. Yakobo alisema hivi pia: “Mwenye furaha ni yule anayeendelea kuvumilia jaribu, kwa sababu atakapokubaliwa atapokea taji la uzima, ambalo Yehova aliwaahidi wale wanaoendelea kumpenda.” (Yak. 1:12) Naam, tunachochewa kuvumilia kwa sababu tunatarajia kupata uzima. Tusipovumilia, hatuwezi kuendelea kuwa katika kweli. Tukishindwa na mikazo ya ulimwengu, tutarudi katika ulimwengu. Tusipovumilia, hatutaendelea kuwa na roho ya Yehova, na hivyo, hatutaweza kuzaa tunda la roho yake maishani mwetu.
10 Ili tuendelee kuvumilia katika nyakati hizi ngumu, tunahitaji kuwa na maoni yanayofaa kuhusu kuteseka tukiwa Wakristo. Kumbuka kwamba Yakobo aliandika hivi: “Oneni yote kuwa shangwe.” Huenda isiwe rahisi kudumisha shangwe tunapoteseka kimwili au kiakili. Hata hivyo, kumbuka kwamba uhai wetu wa wakati ujao unahusika. Mfano wa mitume unatusaidia kuona jinsi tunavyoweza kushangilia tunapoteseka. Simulizi moja linapatikana katika kitabu cha Matendo, na linasema hivi: “Wakawaita mitume, wakawapiga viboko, na kuwaagiza waache kusema kwa msingi wa jina la Yesu, kisha wakawaacha waende. Basi wakatoka mbele ya Sanhedrini, wakishangilia kwa sababu walikuwa wamestahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake.” (Mdo. 5:40, 41) Walielewa kwamba mateso yao ni uthibitisho wa kwamba wanatii amri ya Yesu na kwamba wana kibali cha Yehova. Miaka kadhaa baadaye, alipokuwa akiandika barua yake ya kwanza iliyoongozwa na roho, Petro alitaja faida za kuteseka kwa ajili ya uadilifu.—1 Pet. 4:12-16.
11 Mfano mwingine ni ule wa Paulo na Sila. Walipokuwa katika kazi ya umishonari huko Filipi, walikamatwa na kushtakiwa kwa kulisumbua jiji na kutangaza desturi zisizo halali. Matokeo ni kwamba walipigwa vibaya na kutupwa gerezani. Simulizi hilo la Biblia linatuambia kwamba walipokuwa gerezani wakiwa bado na majeraha, “karibu katikati ya usiku, Paulo na Sila walikuwa wakisali na kumsifu Mungu kwa wimbo, nao wafungwa walikuwa wakiwasikiliza.” (Mdo. 16:16-25) Paulo na mwenzake waliyaona mateso yao kwa ajili ya Kristo kuwa uthibitisho wa utimilifu wao mbele za Mungu na wanadamu, na vilevile kuwa njia ya kutoa ushahidi zaidi kwa wale ambao huenda wakawa na mwelekeo wa kusikiliza habari njema. Uhai wa wengine ulihusika. Usiku huohuo, mlinzi wa jela na watu wa nyumbani mwake walisikiliza na kuwa wanafunzi. (Mdo. 16:26-34) Paulo na Sila walimtumaini Yehova, nguvu zake, na nia yake ya kuwategemeza katika mateso yao. Hawakukata tamaa.
12 Leo pia, Yehova ametuandalia yote tunayohitaji ili kututegemeza nyakati za majaribu. Anataka tuvumilie. Ametupa Neno lake lililoongozwa na roho ambamo tunapata ujuzi sahihi kuhusu kusudi lake. Hilo huimarisha imani yetu. Tuna fursa za kushirikiana na waamini wenzetu, na kufanya utumishi mtakatifu. Pia tuna pendeleo la kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova mwenyewe kupitia sala. Yeye husikiliza tunapomsifu na kumwomba kwa bidii atusaidie kudumisha msimamo safi mbele zake. (Flp. 4:13) Hatuwezi pia kupuuza nguvu tunazopata kwa kutafakari tumaini lililowekwa mbele yetu.—Mt. 24:13; Ebr. 6:13; Ufu. 21:1-4.
KUVUMILIA MAJARIBU MBALIMBALI
13 Majaribu tunayokabili leo ni kama yale ambayo wanafunzi wa Yesu Kristo wa karne ya kwanza walikabili. Leo, Mashahidi wa Yehova wametukanwa na kuteswa na wapinzani ambao wameambiwa habari za uwongo kuwahusu. Kama ilivyokuwa katika siku za mitume, upinzani mwingi huchochewa na wafuasi sugu wa dini ambazo mafundisho na mazoea yake ya uwongo hushutumiwa katika Neno la Mungu. (Mdo. 17:5-9, 13) Nyakati nyingine, watu wa Yehova hupata kitulizo kwa kudai haki za kisheria zilizowekwa na serikali za kisiasa. (Mdo. 22:25; 25:11) Hata hivyo, watawala pia wamepiga marufuku kazi yetu, wakijaribu kukomesha huduma yetu ya Kikristo. (Zab. 2:1-3) Chini ya hali kama hizo, sisi hufuata kwa ujasiri mfano wa mitume waaminifu na kuendelea ‘kumtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.’—Mdo. 5:29.
14 Kadiri roho ya uzalendo inavyozidi kuongezeka duniani pote, ndivyo wahubiri wa habari njema wanavyoshinikizwa zaidi waache huduma yao waliyopewa na Mungu. Watumishi wote wa Mungu wanafahamu vizuri zaidi onyo lililo kwenye Ufunuo 14:9-12 kuhusu kumwabudu “yule mnyama wa mwituni na sanamu yake.” Tunaelewa umuhimu wa maneno haya ya Yohana: “Hapa ndipo watakatifu wanapohitaji uvumilivu, wale wanaoshika amri za Mungu na kushika imara imani kwa Yesu.”
15 Majaribu yanayosababishwa na vita, mapinduzi, au mateso na marufuku yanaweza kufanya iwe vigumu kuendelea na ibada ya Kikristo hadharani. Huenda msiweze kufanya mikutano mkiwa kutaniko. Huenda msiweze kuwasiliana na ofisi ya tawi. Huenda ziara za waangalizi wa mzunguko zikakatishwa. Huenda machapisho yasifike. Lolote kati ya mambo hayo likitokea, mtafanya nini?
16 Jibu ni, fanyeni mambo mnayoweza kufanya kadiri hali zenu zinavyoruhusu. Huenda isiwe vigumu kujifunza kibinafsi. Kwa kawaida vikundi vidogo vinaweza kukutana katika nyumba za akina ndugu ili kujifunza. Biblia na machapisho tuliyojifunza wakati uliopita yanaweza kutumiwa katika mikutano hiyo. Usiogope wala kuwa na wasiwasi. Kwa vyovyote vile, Baraza Linaloongoza litatafuta haraka njia ya kuwasiliana na ndugu wenye madaraka.
17 Hata ukiwa mbali na ndugu zako Wakristo, kumbuka kwamba Yehova na Mwana wake, Yesu Kristo hawako mbali nawe. Tumaini lako linaweza kuendelea kuwa imara. Bado Yehova anaweza kusikia sala zako na kukuimarisha kwa roho yake. Mtegemee akuongoze. Kumbuka kwamba wewe ni mtumishi wa Yehova na mwanafunzi wa Yesu Kristo. Kwa hiyo, tumia vizuri fursa za kuhubiri unazopata. Yehova atabariki jitihada zako, na muda si muda, huenda wengine wakajiunga nawe katika ibada ya kweli.—Mdo. 4:13-31; 5: 27-42; Flp. 1: 27-30; 4: 6, 7; 2 Tim. 4:16-18.
18 Hata unapokabili kifo kama mitume na wengine, mtumaini “Mungu ambaye huwafufua wafu.” (2 Kor. 1:8-10) Kuamini tumaini la ufufuo kunaweza kukusaidia kuvumilia hata upinzani mkali sana. (Luka 21:19) Kristo Yesu alituwekea mfano; alijua kwamba uaminifu wake chini ya jaribu ungewaimarisha wengine ili wavumilie. Unaweza kuwaimarisha ndugu zako kwa njia hiyohiyo.—Yoh. 16:33; Ebr. 12:2, 3; 1 Pet. 2:21.
19 Mbali na mateso na upinzani, huenda ukalazimika kuvumilia hali nyingine ngumu. Kwa mfano, wengine wamevunjika moyo kwa sababu watu katika eneo lao hawapendezwi na habari njema. Wengine wamepambana na magonjwa ya kimwili au kihisia au kuvumilia hali nyingine zinazosababishwa na udhaifu wa kibinadamu. Nyakati nyingine mtume Paulo alivumilia jaribu fulani lililoathiri au kufanya utumishi wake uwe mgumu. (2 Kor. 12:7) Pia, Epafrodito, Mkristo katika karne ya kwanza kutoka Filipi, ‘alihuzunika kwa sababu rafiki zake walisikia alikuwa mgonjwa.’ (Flp. 2:25-27) Kutokamilika kwetu na kwa wengine kunaweza pia kusababisha matatizo ambayo si rahisi kuyavumilia. Kutoelewana kunaweza kutokea kati yetu na Wakristo wenzetu au watu wa familia. Hata hivyo, kufuata shauri la Neno la Yehova kunaweza kutusaidia kuvumilia na kushinda matatizo kama hayo.—Eze. 2:3-5; 1 Kor. 9:27; 13:8; Kol. 3:12-14; 1 Pet. 4:8.
AZIMIA KUENDELEA KUWA MWAMINIFU
20 Ni lazima tushikamane na yule ambaye Yehova amemweka rasmi kuwa Kichwa cha kutaniko, Kristo Yesu. (Kol. 2:18, 19) Tunahitaji kushirikiana na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” na pia wale waliowekwa rasmi kuwa waangalizi. (Ebr. 13:7, 17) Tukifuata kwa ukaribu mipango ya kitheokrasi na kushirikiana na wale wanaoongoza, tutakuwa tayari kufanya mapenzi ya Yehova. Tunahitaji kutumia kikamili pendeleo la sala. Kumbuka kwamba kuta za gereza wala kifungo cha upweke hakiwezi kutuzuia kuwasiliana na Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo wala kuvuruga umoja uliopo kati yetu na waamini wenzetu.
21 Kwa uvumilivu, na tuazimie kufanya yote tunayoweza ili kutimiza utume wetu wa kuhubiri, tukidumu katika kazi ambayo Yesu Kristo aliyefufuliwa aliwaagiza wafuasi wake wafanye: “Basi, nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru. Na tazama! mimi nipo pamoja nanyi sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:19, 20) Kama Yesu, natuvumilie. Acheni tukazie macho tumaini la Ufalme na tarajio la uzima wa milele lililo mbele yetu. (Ebr. 12:2) Tukiwa wanafunzi waliobatizwa wa Kristo, tuna pendeleo la kushiriki kutimiza unabii wa Yesu kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo.” Alisema hivi: “Habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:3, 14) Tukifanya kazi hiyo kwa moyo wetu wote wakati huu, tutafurahia uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Yehova wenye uadilifu!
-
-
NyongezaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
Nyongeza
Ujumbe kwa Wazazi Wakristo:
Ukiwa mzazi, ungependa kuwasaidia watoto wako wapendwa wampende Yehova na kujiweka wakfu kwake. Unaweza kufanya nini ili uwasaidie wajitayarishe kwa ajili ya ubatizo? Utajuaje kwamba wako tayari kwa ajili ya hatua hiyo muhimu?
Yesu aliwaagiza wanafunzi wake hivi: ‘Fanyeni wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, na kuwabatiza.’ (Mt. 28:19) Kulingana na agizo hilo, takwa la msingi ili mtu astahili kubatizwa ni kuwa mwanafunzi, yaani, anapaswa kuelewa, kuamini, na kujitahidi kuishi kupatana na mafundisho ya Yesu. Hata watoto wanaweza kutimiza jambo hilo.
Wawekee watoto wako kielelezo chema, na ukazie sheria za Yehova mioyoni mwao. (Kum. 6:6-9) Unaweza kutumia habari zilizo katika kitabu Furahia Maisha Milele! ili kuwafundisha kweli za msingi na jinsi ya kuishi kulingana na kanuni za Biblia. Wasaidie watoto wako wajue jinsi ya kueleza mambo wanayoamini kwa maneno yao wenyewe wanapoongea na wengine. (1 Pet. 3:15) Kitia-moyo na ujuzi wanaopokea kutoka kwako pamoja na mambo wanayojifunza kibinafsi, ibada ya familia, mikutano ya kutaniko, na marafiki wazuri, yatawasaidia kufikia ubatizo na kufanya maendeleo zaidi. Wasaidie wajiwekee miradi ya kiroho.
-