Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Viumbe Vingi Tofauti-tofauti vya Dunia Vilikujaje Kuwapo?
    Amkeni!—1997 | Mei 8
    • Viumbe Vingi Tofauti-tofauti vya Dunia Vilikujaje Kuwapo?

      KATI ya zaidi ya spishi milioni 1.5 za wanyama ambao wanasayansi wametambua kufikia sasa, karibu milioni moja ni wadudu. Ingehitaji kurasa 6,000 za ensaiklopedia kuorodhesha wadudu wote wanaojulikana! Viumbe hivyo vilianzaje kuwapo? Kwa nini kuna viumbe vingi tofauti-tofauti? Je, vilitokana na nasibu tu, ya asili kupata “bahati nzuri” mara mamilioni? Au ni kwa ubuni?

      Kwanza, ebu tuchunguze kifupi baadhi ya viumbe tofauti-tofauti vinavyopatikana katika dunia yetu.

      Ndege wa Kustaajabisha

      Vipi juu ya zaidi ya spishi 9,000 za ndege waliobuniwa kwa njia ya ajabu sana? Ndege-wavumi fulani ni wadogo sana kama nyuki wakubwa, lakini wao huruka kwa ustadi na kwa madaha kuliko helikopta za hali ya juu zaidi. Ndege wengine huhama maelfu ya kilometa kila mwaka, kama vile membe wa aktiki, ambaye husafiri kufikia kilometa 35,000 za kwenda na kurudi. Hana kompyuta, hana zana za kumwongoza, lakini bila kukosea yeye hufika anakoenda. Je, uwezo huo wa asili wa ndege huyo ulitukia kwa nasibu au kwa ubuni?

      Mimea Tofauti-Tofauti Yenye Kuvutia

      Kwa kuongezea, kuna mimea tofauti-tofauti na yenye umaridadi—zaidi ya spishi 350,000 za mimea. Mimea ipatayo 250,000 kati ya mimea yote hutoa maua! Vitu vyenye uhai vilivyo vikubwa zaidi duniani—miti ya sekuia iliyo mikubwa mno—ni mimea.

      Ni aina ngapi za maua tofauti-tofauti zinazokua katika bustani yako au katika eneo lenu? Umaridadi, muundo wenye kupatana, na mara nyingi manukato ya maua hayo—tokea ua dogo zaidi la jangwa, kibibi, au kombetindi hadi okidi za aina mbalimbali zenye kupendeza—hustaajabisha. Tena, twauliza: Hayo yalikujaje kuwapo? Kwa nasibu au kwa ubuni?

      Bahari-Kuu Zilizojaa Viumbe

      Na vipi juu ya viumbe vinavyopatikana katika mito, maziwa, na bahari-kuu za ulimwengu? Wanasayansi wasema kwamba kuna spishi zipatazo 8,400 za samaki wa maji yasiyo ya chumvi zinazojulikana na karibu spishi 13,300 za samaki wa bahari-kuu. Aliye mdogo zaidi kati ya hao ni gobi ambaye anapatikana katika Bahari-Kuu ya Hindi. Ana urefu wa karibu sentimeta moja tu. Aliye mkubwa zaidi ya wote ni nyangumi-papa, ambaye aweza kufikia urefu wa meta 18. Tarakimu hizo za spishi bado hazijatia ndani wanyama wasio na uti wa mgongo au spishi ambazo bado hazijagunduliwa!

      Ubongo Wenye Kustaajabisha

      Zaidi ya yote, ubongo wa binadamu—wenye angalau nyuroni bilioni kumi, kila moja labda ikiwa na sinapsi zaidi ya 1,000, au vidaraja vya kuunganisha na chembe nyinginezo za mishipa—ni wa kustaajabisha sana. Mtaalamu wa mfumo mkuu wa neva Dakt. Richard Restak asema: “Jumla ya viunganishi vilivyo katika mfumo mkubwa sana wa mfumo wa neva wa ubongo kwa kweli ni vingi mno.” (The Brain) Yeye aongezea: “Inawezekana kwamba kuna sinapsi kati ya trilioni kumi hadi trilioni 100 katika ubongo.” Kisha yeye auliza swali lenye kuhusika kabisa: “Kiungo kama ubongo, ambacho kina kati ya chembe bilioni kumi na bilioni 100, kitawezaje kukua kutoka kwa chembe moja tu, yai?” Je, ubongo ni tokeo la aksidenti tu na nasibu za asili? Au kuna mbuni mwenye akili aliyeufanyiza?

      Ndiyo, viumbe hivi vingi tofauti-tofauti vinavyoonekana kana kwamba havina mwisho na ubuni vilikujaje kuwapo? Je, umefundishwa kwamba hivyo vilisababishwa na nasibu tu, ya kujaribu na kukosea na ya kiholela ya kamari ya kimageuzi isiyoongozwa? Basi endelea kusoma uone maswali ambayo wanasayansi fulani, kwa ufuatiaji wa haki kabisa, wanauliza kuhusu nadharia ya mageuzi, ambayo imeitwa msingi wa sayansi zote za biolojia.

  • Je, Msingi wa Mageuzi Wakosekana?
    Amkeni!—1997 | Mei 8
    • Je, Msingi wa Mageuzi Wakosekana?

      NI NINI kiini cha nadharia ya Darwin ya mageuzi? “Ikifafanuliwa kabisa, kibiolojia, . . . mageuzi yamaanisha njia ambayo uhai ulianza kutokana na kitu kisicho na uhai na kuendelea kujikuza kwa njia za asili pekee.” Mageuzi ya Darwin yadai kwamba “uhai wote, au angalau sehemu zao zote zenye kupendeza, zilitokana na uteuzi asilia ambao ulitokeza kiholela viumbe tofauti-tofauti.”—Darwin’s Black Box—The Biochemical Challenge to Evolution,a cha Michael Behe, profesa-mshiriki wa biokemia katika Chuo Kikuu cha Lehigh, Pennsylvania, Marekani.

      Mfumo-Tegemeano—Je, Ni Kizuizi cha Mageuzi?

      Darwin alipositawisha nadharia yake, wanasayansi hawakujua jinsi chembe-hai ilivyo tata sana. Biokemia ya kisasa, ambayo ni kuchunguza uhai katika kiwango cha molekuli, imefunua baadhi ya utata huo. Pia imezusha maswali mazito na shaka juu ya nadharia ya Darwin.

      Sehemu za chembe zimefanyizwa kwa molekuli. Chembe ndizo vitu vyenye kujenga viumbe hai vyote. Profesa Behe ni mfuasi wa Katoliki ya Kiroma naye anaamini katika mageuzi katika kueleza maendeleo ya baadaye ya wanyama. Hata hivyo, yeye anazusha shaka nzito kama kweli mageuzi yaweza kueleza jinsi chembe ilivyopata kuwapo. Yeye asema juu ya mashine za molekuli ambazo “hutoa mizigo kutoka mahali fulani hadi fulani katika chembe hiyo kupitia ‘barabara kuu’ zilizofanyizwa kwa molekuli nyinginezo . . . Chembe husafiri kwa kutumia mashine, hujinakili kwa kutumia mashine, humeng’enya chakula kwa kutumia mashine. Kwa ufupi, mashine za hali ya juu sana za molekuli huongoza kila utendaji wa chembe. Kwa hiyo kila kijambo kidogo cha uhai kimefanyizwa kwa njia bora zaidi, na mashine ya uhai ni tata sana.”

      Sasa, utendaji huu wote unatukia katika nafasi inayotoshanaje? Chembe ya kawaida ina upana wa milimeta 0.03 pekee! Katika nafasi hiyo ndogo sana, kuna utendaji tata ambao ni muhimu kwa uhai. (Ona picha, ukurasa wa 8-9.) Si ajabu kwamba imesemwa: “Jambo kuu ni kwamba chembe—ambayo ni msingi wenyewe wa uhai—ni tata sana.”

      Behe abisha kwamba chembe inaweza kutenda ikiwa tu ina sehemu zayo zote. Kwa hiyo, haiwezi kutenda inapobadilika polepole na hatua kwa hatua kupitia mageuzi. Yeye atumia mfano wa mtego wa panya. Chombo hiki sahili chaweza tu kufanya kazi ikiwa sehemu zacho zote zimewekwa. Kila sehemu ikiwa peke yayo—kikanyagio, spring’i, kishikilio, kipigio, kishikio—si mtego wa panya nao hauwezi kufanya kazi. Sehemu zote zinahitajika wakati uleule na lazima zote ziwekwe mahali pazo ndipo zifanyize mtego wa panya ufanyao kazi. Hali kadhalika, chembe yaweza tu kufanya kazi wakati sehemu zayo zote zipo. Yeye atumia mfano huo kueleza kile anachokiita “mfumo-tegemeano.”b

      Jambo hilo hutokeza tatizo kubwa kwa hatua za mageuzi, ambazo huhusisha kutokea kitaratibu kwa sehemu fulani-fulani zenye mafaa. Darwin alijua kwamba nadharia yake ya mageuzi ya kitaratibu kupitia uteuzi asilia ilikabili tatizo kubwa aliposema: “Ikiwa inaweza kuthibitishwa kwamba kuna kiungo chochote tata, ambacho hakiwezekani kufanyizwa kwa marekebisho madogo-madogo ya mfululizo, nadharia yangu ingeambulia patupu.”—Origin of Species.

      Chembe ya mfumo-tegemeano ni kizuizi kikuu kwa kuitikadi nadharia ya Darwin. Kwanza, mageuzi hayawezi kueleza jinsi vitu visivyo na uhai vilivyopata kuwa hai. Kisha, kuna tatizo la chembe ya kwanza iliyo tata, ambayo ni lazima ingetokea kwa ghafula ikiwa na kila sehemu. Yaani, chembe (au, mtego wa panya) ni lazima ijitokeze yenyewe, ikiwa na kila sehemu na kufanya kazi!

      Mfumo-Tegemeano wa Kuganda kwa Damu

      Kielelezo kingine cha mfumo-tegemeano ni utendaji ambao sisi huchukua kivivi-hivi—kuganda kwa damu. Kwa kawaida, maji yoyote yale yatavuja mahali ambapo pana tundu nayo yataendelea kuvuja mpaka kiwekeo hicho kiwe kitupu. Lakini, sisi tunapotoboa au kukata ngozi yetu, mvujo huo huzibwa haraka kwa mgando wa damu. Na kama madaktari wajuavyo, “kuganda kwa damu ni mfumo tata sana na wenye mambo mengi ambao una sehemu nyingi za protini zinazotegemeana.” Hizo huchochea kile kiitwacho mfululizo wa kuganda. Hatua hiyo tata ya kupona “hutegemea sana wakati na mwendo ambao utendanaji tofauti-tofauti hutukia.” La, sivyo, mtu aweza kuganda damu yote na kuwa ngumu, au kwa upande mwingine, anaweza kuvuja damu hadi afe. Wakati na mwendo ni muhimu sana.

      Uchunguzi wa kibiokemia umeonyesha kwamba kuganda kwa damu hutia ndani mambo mengi sana, ambayo hata moja haliwezi kukosa ili damu igande. Behe auliza: “Mara damu ianzapo kuganda, ni nini kinachoifanya isiendelee kuganda hadi damu yote . . . iwe ngumu?” Yeye aeleza kwamba “mfanyizo, vizuizi, uimarisho, na kuondolewa kwa mgando wa damu” ni sehemu zinazotegemeana za mfumo wa kibiolojia. Sehemu yoyote ikishindwa, basi mfumo wote utashindwa kufanya kazi.

      Russell Doolittle, ambaye ni mwanamageuzi na profesa wa biokemia katika Chuo Kikuu cha California, auliza: “Mfumo huu tata na wenye usawaziko ulifanyizwaje kupitia mageuzi? . . . Yaani, ikiwa kila protini ilitegemea kutendeshwa na nyingine, basi mfumo huo wa mgando wa damu ungeanzaje kuwapo? Ama sehemu yoyote ile ingetumikaje bila sehemu nyinginezo zote?” Akitumia hoja za kimageuzi, Doolittle ajaribu kueleza chanzo cha mfumo huo. Hata hivyo, Profesa Behe ataja kwamba “bahati kubwa sana inahitajika kuweka jeni zifaazo katika sehemu zifaazo.” Aonyesha kwamba maelezo ya Doolittle na lugha yake rahisi yaficha magumu mengi sana.

      Kwa hiyo, mojawapo mambo makuu yenye kupinga mageuzi ni kizuizi kikubwa sana cha mfumo-tendeano. Behe asema: “Nakazia kwamba uteuzi wa asili, ambalo ndilo jambo kuu la nadharia ya Darwin, unafaulu tu ikiwa kuna kitu cha kuteua—kitu ambacho kina manufaa sasa hivi, wala si kwa wakati ujao.”

      “Ukimya Sana Wenye Kutisha”

      Profesa Behe asema kwamba baadhi ya wanasayansi wamechunguza “violezo vya hisabati za mageuzi au njia mpya za hisabati za kulinganisha na kusoma mfululizo wa DNA.” Hata hivyo, yeye afikia mkataa huu: “Hisabati hizo hudhani kwamba mageuzi halisi ni ya kitaratibu na kiholela; haziyathibitishi (nazo haziwezi) kuyathibitisha.” (Italiki za fungu la mwisho ni zetu.) Mapema alikuwa amesema: “Ukitafuta fasihi za kisayansi juu ya mageuzi, na ukikazia akili kutafuta maswali ya jinsi mashine za molekuli—ambazo ndizo msingi wa uhai—zilivyositawi, utapata ukimya sana wenye kutisha. Utata wa msingi wa uhai umezuia jaribio la sayansi kuufafanua; mashine za molekuli zimeweka kizuizi ambacho bado hakijavunjwa na mweneo wa nadharia ya Darwin.”

      Hilo lazusha mfululizo wa maswali kwa wanasayansi wanyoofu kufikiria: “Kitovu cha utendanaji wa usanidimwanga kilianzaje? Usafiri wa ndani ya molekuli ulianzaje? Ile biosynthesis ya kolesteroli ilianzaje? Ile retinal ilianzaje kuhusika na uwezo wa kuona? Njia za ishara za phosphoprotein zilianzaje?”c Behe aongezea: “Uhakika wa kwamba hakuna hata moja ya matatizo hayo yanayojadiliwa, acha kusuluhishwa, ni dhihirisho kubwa kwamba nadharia ya Darwin haiwezi kueleza chanzo cha mifumo mingi ya kibiokemia.”

      Ikiwa nadharia ya Darwin haiwezi kufafanua msingi wa chembe za molekuli, basi itawezaje kufafanua vizuri kuwapo kwa mamilioni ya spishi yanayoishi katika dunia hii? Kwani, mageuzi hata hayawezi kutokeza aina mpya za familia kwa kuziba mapengo yaliyo kati ya familia moja na nyingine.—Mwanzo 1:11, 21, 24.

      Matatizo ya Kuanza kwa Uhai

      Hata nadharia ya Darwin ya mageuzi iwe yenye kukubalika machoni pa wanasayansi kama nini, hatimaye ni lazima wakabili swali hili, Hata tukisema kwamba aina nyingi za vitu vyenye uhai vilikuja kupitia uteuzi asilia, uhai wenyewe ulianzaje? Yaani, tatizo si kusalimika kwa viumbe bora, bali kuwasili kwa kiumbe bora na cha kwanza! Hata hivyo, kama ionyeshwavyo na maneno ya Darwin juu ya mageuzi ya macho, yeye hakuhangaikia tatizo la jinsi uhai ulivyoanza. Yeye aliandika: “Jinsi neva ipatavyo kuwa nyetivu kwa nuru ni jambo lisilotuhangaisha sawa na tusivyohangaika na jinsi uhai ulivyoanza.”

      Mwandikaji wa mambo ya sayansi wa Ufaransa Philippe Chambon aliandika: “Darwin mwenyewe alijiuliza jinsi asili ilivyoteua vitu vilivyotokea kabla ya vitu hivyo kuanza kuwa vyenye utendaji kabisa. Orodha ya mambo yasiyoweza kufafanuliwa na mageuzi haina kikomo. Na wanabiolojia wa leo ni lazima wakubaliane kwa unyenyekevu na Profesa Jean Génermont wa Chuo Kikuu cha South Paris katika Orsay, kwamba ‘nadharia bandia ya mageuzi haiwezi kufafanua kwa utayari chanzo cha viungo tata vya mwili.’”

      Kwa kufikiria jinsi mageuzi hayawezi kabisa kutokeza viumbe tata mbalimbali, je, wewe huona ugumu wa kukubali kwamba kila kitu kilikuja kupitia mageuzi kwa njia ifaayo kwa nasibu tu? Je, unajiuliza ni vipi viumbe vyovyote vingesalimika katika vita vya kusalimika kwa viumbe bora wakati ambapo bado macho yavyo yalikuwa yanapitia mageuzi? Au wakati ambapo inasemekana eti vilikuwa vinafanyiza vidole hafifu kwenye mwili ulio nusu binadamu? Je, unajiuliza jinsi chembe zilivyosalimika zikiwa katika hali ya nusu-nusu na za kutofaa?

      Robert Naeye, mwandikaji wa gazeti Astronomy aliye pia mwanamageuzi, aliandika kwamba uhai duniani umetokana na “mfululizo mrefu wa matukio yasiyowezekana [ambayo] yalitukia kwa njia sawa tu na kutufanya tuwepo, kana kwamba tumeshinda bahati-nasibu ya mamilioni ya dola mara milioni moja mfululizo.” Kuwaza kwa njia hiyo labda kwaweza kutumiwa katika kila kiumbe-hai kilichopo leo. Haiwezekani kabisa. Na bado tunatazamiwa kuamini kwamba kwa nasibu mageuzi pia yalitokeza wa kiume na wa kike kwa wakati uleule ili spishi mpya iendelezwe. Na kufanya jambo hilo hata lisiwezekane zaidi, ni lazima pia tuamini kwamba wa kiume na wa kike hawakupitia mageuzi wakati uleule tu bali pia mahali palepale! Kama hawangekuja pamoja basi kuzaana hakungekuwapo!

      Kwa hakika, ni ujinga mkubwa sana kuamini kwamba uhai uliopo katika mamilioni ya viumbe kamili ulitokana na mamilioni ya kamari zilizofanikiwa.

      Kwa Nini Watu Wengi Zaidi Wanaamini Mageuzi?

      Kwa nini mageuzi yanapendwa sana na kukubaliwa na watu wengi sana kuwa ndiyo maelezo ya pekee ya jinsi uhai ulivyoanza duniani? Sababu moja ni kwamba hayo ndiyo maoni ya kawaida yanayofundishwa shuleni na katika vyuo vikuu, na ni ole wako ukijaribu kuyatilia shaka. Behe aeleza: “Wanafunzi wengi hujifunza kutokana na vitabu vyao vya mafunzo jinsi ya kuona ulimwengu kupitia mageuzi. Lakini, wao hawajifunzi jinsi mageuzi ya Darwin yangetokeza mifumo yoyote tata ya kibiokemia ambayo vitabu hivyo hufafanua.” Yeye aongezea: “Ili kuelewa mafanikio ya nadharia ya Darwin kuwa maoni ya kawaida na kushindwa kwayo kuwa sayansi kwenye kiwango cha molekuli, ni lazima tuchunguze vitabu vya mafundisho ambavyo vinatumiwa kufundisha wale wanaotaka kuwa wanasayansi.”

      “Kama wanasayansi wote ulimwenguni wangeulizwa, wengi zaidi wangesema wao waamini nadharia ya Darwin kuwa kweli. Lakini, wanasayansi, kama ilivyo na kila mtu, hutegemeza maoni yao kwenye maoni ya watu wengine. . . . Pia, kwa ubaya, mara nyingi uchambuzi hutupiliwa mbali na jamii ya kisayansi kwa kuogopa kwamba itawapa nguvu creationists. Ni jambo la kushangaza kwamba kwa sababu ya kulinda sayansi, uchambuzi halali wa kisayansi dhidi ya uteuzi asilia umepuuzwa.”d

      Kuna jambo gani lifaalo na lenye kutegemeka badala ya nadharia ya Darwin ya mageuzi? Makala yetu ya mwisho katika mfululizo huu itazungumzia suala hilo.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ambacho kimerejezewa kuanzia hapa na kuendelea kuwa (Darwin’s Black Box)

      b “Mfumo-tegemeano” hufafanua “mfumo mmoja wenye sehemu kadhaa zinazofaana na kupatana ambazo huchangia utendaji sahili, na sehemu yoyote ikiondolewa mfumo huo hushindwa kabisa kufanya kazi.”

      c Usanidimwanga ni utendaji ambamo chembe za mmea, kwa kutumia nuru na chanikiwiti, hufanyiza wanga kutokana na kaboni dioksidi na maji. Huo huitwa na wengine kuwa utendanaji muhimu zaidi unaotukia katika hali ya asili. Ile Biosynthesis ni utendaji ambamo chembe-hai zinatengeneza misombo tata ya kemia. Ile retinal inahusika na mfumo tata wa macho. Njia za kupeleka ishara za phosphoprotein ni sehemu muhimu za utendaji wa chembe.

      d Creationism hutia ndani itikadi ya kwamba dunia iliumbwa kwa siku sita halisi au, katika hali fulani, kwamba dunia ilifanyizwa kwa miaka 10,000 hivi pekee iliyopita. Ingawa Mashahidi wa Yehova wanaamini uumbaji, wao si creationists. Wao waamini kwamba masimulizi ya kitabu cha Mwanzo cha Biblia yaruhusu dunia iwe na mamilioni ya miaka.

      [Blabu katika ukurasa wa 6]

      “Ikiwa inaweza kuthibitishwa kwamba kuna kiungo chochote tata, ambacho hakiwezekani kufanyizwa kwa marekebisho madogo-madogo ya mfululizo, nadharia yangu ingeambulia patupu.”

      [Blurbs katika ukurasa wa 10]

      Ndani ya chembe, mna “Ulimwengu wa tekinolojia ya hali ya juu sana na yenye utata wa ajabu.”—Evolution: A Theory in Crisis

      Maagizo yaliko katika DNA ya chembe, ”kama yangeandikwa, yangejaza vitabu 1,000 vyenye kurasa 600 kila kimoja.”—National Geographic

      [Blabu katika ukurasa wa 11]

      “Hisabati hizo hudhani kwamba mageuzi halisi ni ya kitaratibu na kiholela; haziyathibitishi (nazo haziwezi) kuyathibitisha.”

      [Blabu katika ukurasa wa 12]

      “Ni jambo la kushangaza kwamba kwa sababu ya kulinda sayansi, uchambuzi halali wa kisayansi dhidi ya uteuzi asilia umepuuzwa.”

      [Sanduku katika ukurasa wa 8]

      Molekuli na Chembe

      Biokemia—“uchunguzi wa msingi halisi wa uhai: molekuli ambazo hufanyiza chembe na tishu, ambazo huchochea utendanaji wa kemikali wa umeng’enyaji, usanidimwanga, kinga, na nyinginezo nyingi.”—Darwin’s Black Box.

      Molekuli—“sehemu ndogo zaidi ambayo elementi au msombo waweza kugawanywa bila kubadili hali zayo za kemikali na sura; kikundi cha atomu zinazofanana au zilizo tofauti ambazo zimeshikanishwa pamoja na kani za kemikali.”—The American Heritage Dictionary of the English Language.

      Chembe—kifanyizo cha msingi cha viumbe hai. “Kila chembe ni kitu ambacho kimejipanga kwa hali ya juu sana na ambacho kinasababisha muundo wa kiumbe na utendanaji wacho.” Ni chembe ngapi ambazo hufanyiza mtu mzima? Trilioni 100 (100,000,000,000,000)! Tuna karibu chembe 155,000 kwa kila sentimeta moja ya mraba kwenye ngozi, na ubongo wa binadamu una kati ya nyuroni bilioni 10 hadi bilioni 100. “Chembe ndiyo jambo kuu la uhai kwa sababu ni katika chembe ambamo maji, chumvi, molekuli kubwa-kubwa, na tando zinatokeza uhai.”—Biology.

      [Sanduku katika ukurasa wa 9]

      ‘Utata Usio na Kifani’ wa Chembe

      “Ili kufahamu uhalisi wa uhai kama ambavyo umeonyeshwa na biolojia ya molekuli, ni lazima tupanue chembe mara milioni 1,000 mpaka chembe iwe na kipenyo cha kilometa 20 na kufanana na ndege kubwa sana iwezayo kufunika jiji kubwa kama London au New York. Kile ambacho tungeona sasa kingekuwa kitu ambacho ni tata kisicho na kifani na chenye ubuni unaopatana. Nje kwenye chembe tungeona mamilioni ya matundu, yaliyo kama madirisha ya ndege kubwa sana, yakijifunga na kujifungua ili kupitisha vifaa vinavyoingia na kutoka. Kama tungaliingia mojawapo matundu hayo tungalijikuta katika ulimwengu wa tekinolojia ya hali ya juu sana na yenye utata wa ajabu. Tungeona vijia vingi sana vilivyopangwa kwa utaratibu sana na mahandaki yanayotoka nje yanayoingia katika kila sehemu ya chembe, mengine yakielekea kwenye kitovu cha kumbukumbu katika kiini na mengine yakienda kwenye viwanda na sehemu za utendanishaji wa vitu. Kiini chenyewe kingekuwa chumba kikubwa sana cha mviringo chenye kipenyo cha zaidi ya kilometa moja, kikifanana na kuba laini ambamo ndani yacho tungeona kilometa nyingi sana za minyororo ya molekuli za DNA zikiwa zimewekwa kinadhifu kwa utaratibu mzuri. Vitu vingi tofauti-tofauti na mali-ghafi zingepitishwa katika mahandaki mengi kwa utaratibu sana zikienda na kutoka kwenye viwanda kadhaa vilivyo katika sehemu za nje za chembe.

      “Tungeshangaa kwa jinsi miendo ya vitu vingi vinavyodhibitiwa katika mahandaki mengi sana yasiyoonekana, yote yakifanya kazi katika muungano mkamilifu. Tungeona kotekote kutuzunguka, katika kila mahali tutazamapo, kila aina ya mashine zinazofanana na roboti. Tungeona kwamba sehemu sahili zaidi inayofanya kazi ya chembe, zile molekuli za protini, ni mashine zilizo tata ajabu za molekuli, kila moja ikiwa na atomu 3,000 zikiwa zimejipanga katika muundo wa kuonekana kwa pande tatu. Tungeshangaa hata zaidi tutazamapo utendaji ambao hatuujui wenye kusudi fulani wa mashine hizo za kiajabu za molekuli, hasa tutambuapo kwamba, japo ujuzi wetu mwingi wa fizikia na kemia, kubuni mashine moja kama hiyo ya molekuli—yaani protini moja tu inayofanya kazi—kungetushinda kabisa kwa wakati huu na hata labda hakutaweza kufanywa mpaka angalau mwanzo wa karne ifuatayo. Na bado uhai wa chembe wategemea maelfu ya utendaji mwingi wenye kupatana, kwa hakika hata makumi ya maelfu, na labda mamia ya maelfu ya aina mbalimbali za molekuli za protini.”—Evolution: A Theory in Crisis.

      [Sanduku katika ukurasa wa 10]

      Mambo ya Hakika na Hekaya

      “Kwa mtu ambaye anaona yuko huru kutafuta visababishi vyenye hekima, uamuzi wa mara moja ni kwamba mifumo mingi ya kibiokemia ilibuniwa. Haikubuniwa na sheria za asili, wala na nasibu na uhitaji; bali, ilipangwa. . . . Uhai duniani kwenye kiwango cha chini kabisa, katika sehemu zao muhimu kabisa, ni tokeo la utendaji wenye akili.”—Darwin’s Black Box.

      “Hakuna shaka kwamba baada ya karne moja ya jitihada zenye bidii wanabiolojia wameshindwa kutetea [nadharia ya Darwin ya mageuzi] katika jambo lolote kubwa. Jambo la hakika ni kwamba asili haijatokeza mfululizo wa viumbe vinavyohusiana kwa ukaribu ambao nadharia ya Darwin yadai, wala ustahili wa nasibu kuwa chanzo cha uhai haujathibitishwa.”—Evolution: A Theory in Crisis.

      “Uvutano wa nadharia ya mageuzi kwenye nyanja zilizo tofauti sana na biolojia ni mojawapo mifano bora zaidi katika historia ya jinsi wazo la kudhaniwa tu ambalo halina uthibitisho mzuri wa kisayansi linavyoweza kubadili kufikiri kwa jumuiya nzima na kudhibiti mtazamo wa kizazi fulani cha watu.”—Evolution: A Theory in Crisis.

      “Sayansi yoyote iliyopita . . . ambayo haitii ndani uwezekano wa ubuni au uumbaji kutokana na uthibitisho haitafuti kweli, nayo ni mtumishi (au mtumwa) wa fundisho la kifalsafa lenye matatizo, yaani, naturalism.”—Origins Research.

      “Ni hekaya . . . kwamba Charles Darwin alisuluhisha tatizo la chanzo cha utata wa kibiolojia. Ni hekaya kwamba tunafahamu au hata kufahamu vizuri chanzo cha uhai, au kwamba maelezo yafaayo yarejezea tu vile viitwavyo eti visababishi vya asili. Kwa hakika, hekaya hizo na nyinginezo za naturalism za kifalsafa zinapendwa kwa kadiri fulani. Huwezi kuzishutumu sana miongoni mwa wangwana. Lakini hupaswi vilevile kuzikubali bila kuzichambua.”—Origins Research. “Faraghani wanasayansi wengi hukiri kwamba sayansi haifafanui chanzo cha uhai. . . . Darwin hakupata kuwazia utata mkubwa sana uliopo hata katika hali za chini kabisa za uhai.”—Darwin’s Black Box.

      “Mageuzi ya molekuli hayategemei mamlaka ya kisayansi. . . . Kuna madai kwamba mageuzi kama hayo yalitukia, lakini hakuna hata moja linaloungwa mkono na majaribio au hesabu. Kwa kuwa hakuna mtu ambaye amepata kuona mageuzi ya molekuli, na kwa kuwa hakuna uthibitisho wa kuunga mkono ujuzi huo, yaweza kusemwa kwa hakika kwamba . . . sisitizo la nadharia ya Darwin ya mageuzi ya molekuli ni majivuno tu.”—Darwin’s Black Box.

      [Sanduku katika ukurasa wa 12]

      Mageuzi—“Mchezo wa Nasibu”

      Nadharia ya mageuzi hakika ni ndoto ya mcheza-kamari. Kwa nini? Kwa sababu kulingana na mwanamageuzi huyo, hiyo hushinda hata kama haiwezi kamwe kushinda.

      Robert Naeye aandika: “Kwa sababu mageuzi hasa ni mchezo wa nasibu, tukio lolote lionekanalo kuwa dogo sana lingetukia kwa njia tofauti kidogo, jambo ambalo lingekomesha mwendo wa mageuzi kabla ya kugeuka kwa wanadamu.” Lakini la, tunatakiwa tuamini kwamba kila kamari ilishinda, mara mamilioni. Naeye akiri: “Mfululizo wa matatizo hudhihirisha kwamba ni vigumu zaidi kwa uhai wenye akili kutokea kuliko vile wanasayansi walivyodhani pindi moja. Labda kuna vizuizi vingi ambavyo wanasayansi hawajapata kuona bado.”

  • Mungu—Je, Ni Mcheza-kamari au Muumba?
    Amkeni!—1997 | Mei 8
    • Mungu—Je, Ni Mcheza-kamari au Muumba?

      “HAKUNA shaka kwamba wanasayansi wengi wanapinga kabisa hoja za kuwapo kwa nguvu zenye kupita uwezo wa wanadamu. Wao wanapuuza wazo la kwamba huenda Mungu yupo, au hata kuwapo kwa chanzo fulani chenye uwezo wa kuumba . . . Mimi binafsi sikubaliani na dhihaka zao.” Ndivyo asemavyo Paul Davies, profesa wa fizikia ya hisabati katika Chuo Kikuu cha Adelaide, Australia Kusini, katika kitabu chake The Mind of God.

      Pia Davies asema: “Uchunguzi wenye uangalifu waonyesha kwamba sheria za ulimwengu wote mzima zafaa kabisa kutokea kwa viumbe vingi tofauti-tofauti. Kwa habari ya viumbe hai, kuwapo kwao yaonekana hutegemea matukio kadhaa mazuri ambayo baadhi ya wanasayansi na wanafalsafa wamedai kuwa ya ajabu mno.”

      Yeye aendelea kusema: “Utafutaji wa kisayansi ni safari ya kwenda kusikojulikana. . . . Na katika utafutaji huo wote kuna jambo lilelile la akili na utaratibu. Tutaona kwamba utaratibu huo mzuri wa ulimwengu unaungwa mkono na sheria fulani hususa za hisabati ambazo hupatana na kufanyiza muungano usioonekana lakini wenye umoja. Sheria hizo ni sahili sana.”

      Davies amalizia kwa kusema: “Sababu hasa inayofanya binadamu ndiye awe na akili ya kufahamu ulimwengu wote mzima, ni fumbo kubwa sana. . . . Siwezi kuamini kwamba kuwapo kwetu katika ulimwengu wote mzima kulitukia tu kwenyewe, kukiwa aksidenti fulani tu katika historia na kasoro fulani katika matukio ya ulimwengu wote mzima. Tumehusika sana na ulimwengu. . . . Hakika tumekusudiwa kuwa hapa.” Lakini, Davies hafikii mkataa wa kwamba kuna Mbuni, Mungu. Lakini wewe wafikia mkataa upi? Je, ilikusudiwa wanadamu wawepo? Ikiwa ndivyo, ni nani aliyekusudia tuwepo?

      Funguo za “Fumbo”

      Katika Biblia mtume Paulo atoa dokezo la kuelewa kile Davies akiitacho “fumbo kubwa sana.” Paulo aonyesha jinsi Mungu amejifunua: “Kwa sababu lile liwezalo kujulikana juu ya Mungu ni dhahiri miongoni mwao [“watu wanaokandamiza kweli”], kwa maana Mungu alilifanya dhahiri kwao. Kwa maana sifa zake zisizoonekana zaonwa waziwazi tangu uumbaji wa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zafahamiwa kwa vitu vilivyofanywa, hata nguvu zake za milele na Uungu, hivi kwamba hawana sababu ya kujitetea.” (Waroma 1:18-20)a Ndiyo, aina nyingi sana za uhai, utata wao ajabu sana, ubuni wao bora zaidi, wapaswa kufanya mtu ambaye ni mnyenyekevu na wa kimungu atambue kwamba kuna uwezo mkuu zaidi na akili, ipitayo kitu chochote ambacho mwanadamu amepata kujua.—Zaburi 8:3, 4.

      Maneno zaidi ya Paulo kuhusu wale wanaomkataa Mungu hufanya mtu atue na kufikiri: “Ijapokuwa walisisitiza kuwa ni wenye hekima, wakawa wapumbavu . . . , hata wale walioibadili kweli ya Mungu kwa uwongo nao waliheshimu mno na kutoa utumishi mtakatifu kwa kiumbe badala ya Yeye aliyeumba, ambaye abarikiwa milele. Ameni.” (Waroma 1:22, 25) Wale wanaoheshimu “asili” na kumkataa Mungu kwa hakika si wenye hekima kwa maoni ya Yehova. Wakiwa wamekwama katika nadharia nyingi zenye kupingana za mageuzi, wao hawatambui Muumba na vilevile utata na ubuni wa uumbaji wake.

      “Mfululizo wa Aksidenti Kubwa-Kubwa”

      Paulo aliandika pia: “Bila imani haiwezekani kumpendeza [Mungu] vema, kwa maana amkaribiaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Imani inayotegemea ujuzi sahihi, wala si kukubali mambo bila msingi, yaweza kufanya tuelewe ni kwa nini tupo. (Wakolosai 1:9, 10) Kwa hakika, kukubali mambo bila msingi hutokea wakati wanasayansi fulani wanataka tuamini kwamba uhai upo kwa sababu ni “kana kwamba tumeshinda bahati nasibu ya dola milioni moja mara mamilioni mfululizo.”

      Mwanasayansi wa Uingereza Fred Hoyle alinadharia kwamba utendanaji wa nyuklia ambao ulitokeza mfanyizo wa elementi mbili zilizo muhimu kwa uhai, yaani kaboni na oksijeni, ulitokeza kiasi chenye usawaziko cha elementi hizo kwa aksidenti nzuri.

      Yeye atoa mfano mwingine: “Kama jumla ya protoni na elektroni zingeongezeka kidogo tu zaidi badala ya kupungua kidogo zaidi kuliko jumla ya nutroni, matokeo yangekuwa mabaya zaidi. . . . Kotekote katika Ulimwengu Wote Mzima atomu zote za hidrojeni zingevunjika-vunjika mara moja ili kufanyiza nutroni na nutrinosi. Bila fueli yalo ya nyuklia, Jua lingefifia na kuporomoka.” Na ndivyo ingekuwa na mabilioni ya nyota nyinginezo katika ulimwengu wote mzima.

      Hoyle alifikia mkataa huu: “Orodha ya . . . zile zionekanazo kuwa aksidenti za asili zisizo za kibiolojia bila kaboni na hivyo uhai wa kibinadamu usiweze kuwapo, ni kubwa na kustaajabisha.” Yeye asema: “Mambo hayo [muhimu kwa uhai] yaonekana yameshikamana na ulimwengu wa asili kama mfululizo wa aksidenti nzuri. Lakini kuna matukio hayo yasiyo ya kawaida mengi yaliyo muhimu kwa uhai hivi kwamba twahitaji yafafanuliwe.”—Italiki ni zetu.

      Pia alitaja: “Tatizo ni kuamua kama matukio hayo ya kiaksidenti kwa kweli yalikuwa aksidenti au la, na basi kama uhai ulitukia kwa aksidenti au la. Hakuna mwanasayansi apendaye kuuliza swali kama hilo, lakini ni lazima swali hilo liulizwe. Je, yawezekana kwamba matukio hayo yanafanywa na akili fulani?”

      Paul Davies aandika: “Hoyle alivutiwa sana na ‘mfululizo wa aksidenti kubwa-kubwa,’ mpaka akasema ilikuwa kana kwamba ‘sheria za fizikia zimebuniwa kwa kufikiria matokeo yazo ndani ya nyota.’” Ni nani au ni nini kimesababisha “mfululizo wa aksidenti [nzuri] kubwa-kubwa”? Ni nani au ni nini kilichotokeza sayari hii ndogo sana, iliyojaa mamilioni ya viumbe na mimea iliyo tofauti-tofauti?

      Jibu la Biblia

      Mtunga-zaburi aliandika kwa staha sana miaka ipatayo 3,000 iliyopita: “Ee BWANA, jinsi yalivyo mengi matendo yako! Kwa hekima umevifanya vyote pia. Dunia imejaa mali zako. Bahari iko kule, kubwa na upana, ndimo mlimo viendavyo visivyohesabika, viumbe hai vidogo kwa vikubwa.”—Zaburi 104:24, 25.

      Mtume Yohana alisema: “Wewe wastahili, Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako na vikaumbwa.” (Ufunuo 4:11) Uhai si tokeo la nasibu tu, la bahati nasibu ambayo ilitukia kutokeza washindi wa mamilioni ya aina za uhai.

      Ukweli ni kwamba Mungu ‘aliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yake vilikuwapo na kuumbwa.’ Yesu Kristo mwenyewe aliwaambia Mafarisayo: “Je, hamkusoma kwamba yeye aliyewaumba wao kutoka mwanzo aliwafanya wa kiume na wa kike?” Yesu alijua Muumba! Akiwa Mfanyakazi Stadi wa Yehova, alikuwa pamoja na Yeye wakati wa uumbaji.—Mathayo 19:4; Mithali 8:22-31.

      Hata hivyo, inahitaji imani na unyenyekevu kuona na kukubali kweli ya msingi kuhusu Muumba. Imani hiyo si kuamini tu mambo bila msingi. Inategemea uthibitisho uonekanao. Ndiyo, “Sifa [za Mungu] zisizoonekana zaonwa waziwazi tangu uumbaji wa ulimwengu na kuendelea.”—Waroma 1:20.

      Kwa ujuzi wetu kidogo wa sasa juu ya mambo ya kisayansi, hatuwezi kueleza jinsi Mungu alivyoumba. Basi, twapaswa kutambua kwamba kwa wakati huu hatuwezi kujua wala kuelewa kila kitu kuhusu mwanzo wa uhai. Twakumbushwa jambo hili tusomapo maneno ya Yehova: “Mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu . . . Kwa maana kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.”—Isaya 55:8, 9.

      Chaguo ni lako: ama uamini mambo ya mageuzi yasiyo na msingi, zile kamari nyingi sana ambazo zasemekana eti zilikuwa na matokeo mazuri, ama uamini katika Mkusudiaji-Muumba-Mbuni, Yehova Mungu. Nabii aliyepuliziwa alisema hivi kwa usahihi: “Yeye Mungu wa milele, BWANA, Muumba miisho ya dunia, hazimii, wala hachoki; akili zake hazichunguziki.”—Isaya 40:28.

      Basi, utaamini nini? Uamuzi wako utafanyiza tofauti kubwa sana katika matazamio yako ya wakati ujao. Kama mageuzi yangekuwa kweli, basi kifo kingemaanisha utupu kabisa, japo hoja zisizo za kweli za theolojia za Katoliki, ambazo zinajaribu kuingiza “nafsi” katika mageuzi.b Mwanadamu hana nafsi isiyoweza kufa iwezayo kupunguza pigo la kifo.—Mwanzo 2:7; Ezekieli 18:4, 20.

      Tukikubali kwamba Biblia ni kweli na kwamba Mungu aishiye ni Muumba, basi kuna ahadi ya ufufuo kwenye uhai udumuo milele, uhai mkamilifu, katika dunia iliyorekebishwa kwenye hali yayo ya awali ya usawaziko na upatano. (Yohana 5:28, 29) Utaweka imani yako wapi? Katika kamari isiyoweza kuaminiwa ya nadharia ya Darwin ya mageuzi? Au katika Muumba, ambaye ametenda kwa kusudi na aendelea kufanya hivyo?c

      [Maelezo ya Chini]

      a “Tangu Mungu aumbe ulimwengu uwezo wake na uungu wake wa milele—hata kama hauonekani—umekuwapo tuuone kwa akili katika vitu ambavyo ameumba.”—Waroma 1:20, Jerusalem Bible.

      b Ona “Kuutazama Ulimwengu,” ukurasa wa 28, “Papa Ahakikisha Tena Mageuzi.”

      c Kwa mazungumzo marefu juu ya jambo hili, ona kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation?, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

      [Blabu katika ukurasa wa 14]

      Wanamageuzi fulani wasema kwamba kuwapo kwetu duniani ni “kana kwamba tumeshinda bahati nasibu ya dola milioni moja mara mamilioni mfululizo.”

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 15]

      Viumbe Vingi Sana vya Aina na Ubuni Mbalimbali

      Wadudu “Wanasayansi hugundua spishi mpya 7,000 hadi 10,000 za wadudu kila mwaka,” yasema The World Book Encyclopedia. Na bado, “yawezekana kwamba kuna spishi milioni 1 hadi milioni 10 ambazo hazijagunduliwa.” Gazeti la habari la Ufaransa Le Monde, kama lilivyonukuliwa katika Guardian Weekly, katika makala moja iliyoandikwa na Catherine Vincent, lasema juu ya spishi ambazo zimejulikana kuwa “idadi ndogo sana kwa kulinganisha na idadi halisi . . . inayokadiriwa kuwa kati ya milioni 5 na, kwa kushangaza sana, milioni 50.”

      Fikiria ulimwengu wa wadudu wa ajabu—nyuki, chungu, manyigu, vipepeo, mende, bibiarusi, vimulimuli, mchwa, nondo, nzi, kereng’ende, mbu, silverfish, panzi, chawa, chenene, viroboto—kwa kutaja wachache tu! Orodha yaonekana kuwa ndefu sana!

      Ndege Twaweza kusema nini kuhusu ndege ambaye ana uzito unaopungua gramu 14? “Ebu mfikirie akihama zaidi ya kilometa 16,000 kwa mwaka kutoka misitu ya Alaska hadi misitu ya mvua ya Amerika Kusini na kurudi, akipita juu ya vilele vya milima vyenye misitu, orofa ndefu za majiji, na kuvuka upana mkubwa sana wa Bahari-kuu ya Atlantiki na Ghuba ya Mexico.” Ndege huyo wa ajabu ni yupi? “Ni blackpoll warbler [Dendroica striata], ndege mwenye nguvu ambaye umahiri wake wa kusafiri hauna kifani miongoni mwa ndege wa bara la Amerika Kaskazini.” (Book of North American Birds) Tena twajiuliza: Je, hilo ni tokeo la aksidenti nyingi za asili ambazo zimetukia tu zenyewe? Au je, ni ajabu ya ubuni wa akili?

      Ongezea mifano hiyo ndege wanaoonekana kuwa na orodha ndefu isiyo na mwisho ya nyimbo: nightingale, ajulikanaye kotekote Ulaya na sehemu za Afrika na Asia kwa nyimbo zake tamu; mockingbird wa Amerika Kaskazini, ndege ambaye ni “mwigaji stadi ambaye huimba pia mafungu ya maneno aliyokariri katika wimbo wake”; lyrebird aliye stadi sana wa Australia, mwenye “wimbo wa hali ya juu sana, na mwenye uwezo sana wa kuiga.”—Birds of the World.

      Kwa kuongezea, rangi kamili na ubuni wa mabawa na manyoya ya ndege wengi sana hustaajabisha. Ongezea uwezo wao wa kufuma na kutengeneza viota, ardhini, magengeni, au mitini. Akili hiyo ya asili ni lazima ivutie wanyenyekevu. Walikujaje kuwapo? Kwa nasibu au kwa ubuni?

      Ubongo wa Kibinadamu “Inawezekana kwamba kuna sinapsi kati ya trilioni kumi hadi trilioni 100 katika ubongo, na kila moja hutenda kama kikokotozi kidogo sana ambacho huhesabu ishara zinazofika kwa njia ya mipwito ya elektroni.” (The Brain) Tuna mwelekeo wa kupuuza ubongo, lakini ni kama ulimwengu wote mzima uliowekwa na kulindwa na fuvu. Sisi tulipataje kuwa na kiungo hicho ambacho hufanya wanadamu wafikiri, wasababu, na kusema maelfu ya lugha? Je, ni kupitia mamilioni ya kamari zenye bahati nzuri? Au ni kupitia ubuni wenye akili?

      [Mchoro katika ukurasa wa 16, 17]

      Mchoro Sahili wa Sehemu ya Nje ya Ubongo

      Koteksi ya fahamu

      Huchanganua mipwito ya fahamu inayotoka mwilini kote

      Occipital lobe

      Huchakata ishara za kuona

      Ubongo-kati

      Hudhibiti usawaziko na uratibu wa mwili

      Sehemu ya mbele ya koteksi

      Hudhibiti uratibu wa misuli

      Koteksi ya miendo ya neva

      Husaidia kudhibiti miendo ya mwili

      Frontal lobe

      Husaidia kudhibiti kusababu, hisia, usemi, miendo

      Temporal lobe

      Huchakata sauti; huongoza hali ya kujifunza, kumbukumbu, lugha, hisia

      [Mchoro katika ukurasa wa 16]

      Kituo cha aksoni

      Vipitisha-neva

      Dendira

      Sinapsi

      [Mchoro katika ukurasa wa 16, 17]

      Nyuroni

      Dendira

      Aksoni

      Dendira

      Sinapsi

      Nyuroni

      Aksoni

      “Inawezekana kwamba kuna sinapsi kati ya trilioni kumi hadi trilioni 100 katika ubongo, na kila moja hutenda kama kikokotozi kidogo sana ambacho huhesabu jumla ya ishara zinazofika kwa njia ya mipwito ya elektroni.”—THE BRAIN

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki