-
Ujumbe Wenye Tumaini kwa Mateka Walioshuka MoyoUnabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
1. Eleza jinsi hali ya wahamishwa Wayahudi ilivyokuwa huko Babiloni.
GIZA la huzuni lilikuwa limeingia katika historia ya Yuda. Watu wa agano la Mungu walikuwa wameng’olewa katika nchi yao na sasa walikuwa wakiteseka utekwani Babiloni. Ni kweli kwamba walipewa uhuru wa kiasi fulani ili kuendeleza shughuli zao za kila siku. (Yeremia 29:4-7) Wengine walijifunza ufundi wa mambo mbalimbali na wengine wakafanya biashara.a (Nehemia 3:8, 31, 32) Hata hivyo, maisha ya mateka Wayahudi hayakuwa rahisi. Walikuwa utumwani kimwili na kiroho. Acheni tuone ilikuwaje.
2, 3. Uhamisho ulikuwa na matokeo gani juu ya ibada ambayo Wayahudi walimtolea Yehova?
2 Wakati majeshi ya Babiloni yalipoangamiza Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K., yaliipiga ibada ya kweli pigo kali, licha ya kufanya taifa hilo ukiwa. Yalisomba vyombo vyote vya hekalu la Yehova na kuliangamiza, yakauharibu kabisa mpangilio wa ukuhani kwa kuteka baadhi ya watu wa kabila la Lawi na kuua wengine. Bila nyumba ya ibada, bila madhabahu, na bila mpangilio mzuri wa ukuhani, haikuwezekana Wayahudi wamtolee Mungu wa kweli dhabihu kwa njia iliyoagizwa na Sheria.
3 Bado Wayahudi waaminifu wangeweza kudumisha utambulisho wao wa kidini kwa kufuata tohara na kufuata Sheria kwa kadiri ilivyowezekana. Kwa mfano, wangeweza kuepuka vyakula vilivyokatazwa na pia kuishika Sabato. Lakini kwa kufanya hivyo, wangeweza kudhihakiwa na watekaji wao kwa maana Wababiloni waliziona desturi za kidini za Wayahudi kuwa upumbavu. Kuonyesha kwamba wahamishwa hao walishuka moyo, maneno ya mtunga-zaburi yanasema hivi: “Kando ya mito ya Babeli ndiko tulikoketi, tukalia tulipoikumbuka Sayuni. Katika miti iliyo katikati yake tulivitundika vinubi vyetu. Maana huko waliotuchukua mateka walitaka tuwaimbie; na waliotuonea walitaka furaha; tuimbieni baadhi ya nyimbo za Sayuni.”—Zaburi 137:1-3.
4. Kwa nini ingekuwa kazi bure ikiwa Wayahudi wangetegemea mataifa mengine ili kupata ukombozi, lakini wangeweza kugeukia nani awasaidie?
4 Basi, mateka Wayahudi wangeweza kupata faraja kwa kugeukia nani? Wokovu wao ungetoka wapi? Ni wazi haungetoka kwa mataifa yaliyowazunguka! Mataifa hayo yote yalikuwa hoi mbele ya majeshi ya Babiloni, na mengi yaliwachukia Wayahudi. Hata hivyo kulikuwa na tumaini. Yehova, ambaye walikuwa wamemwasi wakiwa watu huru, aliwakaribisha kwa uchangamfu ingawa walikuwa uhamishoni.
-
-
Ujumbe Wenye Tumaini kwa Mateka Walioshuka MoyoUnabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
a Majina mengi ya Kiyahudi yamepatikana katika maandishi ya kibiashara ya Babiloni ya kale.
-