Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ezekieli—II
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Agosti 1
    • “UWEKE MOYO WAKO JUU YA YOTE NINAYOKUONYESHA”

      (Ezekieli 40:1–48:35)

      Ni mwaka wa 14 tangu jiji la Yerusalemu lilipoangushwa. (Ezekieli 40:1) Bado kuna miaka mingine 56 ya uhamisho. (Yeremia 29:10) Sasa Ezekieli anakaribia umri wa miaka 50. Katika maono, analetwa katika nchi ya Israeli. Anaambiwa hivi: “Mwana wa binadamu, ona kwa macho yako, na kwa masikio yako usikie, na uweke moyo wako juu ya yote ninayokuonyesha.” (Ezekieli 40:2-4) Ezekieli anasisimuka kama nini kupokea maono ya hekalu jipya!

      Hekalu tukufu ambalo Ezekieli anaona lina malango 6, vyumba 30 vya kulia chakula, Patakatifu, Patakatifu Zaidi, madhabahu ya mbao, na madhabahu ya matoleo ya kuteketezwa. Maji ‘yaliyokuwa yakitoka’ hekaluni yaliongezeka na kuwa mto. (Ezekieli 47:1) Ezekieli anapewa pia maono ya migawo ya nchi kwa ajili ya makabila—kila kabila likigawiwa sehemu ya nchi kuelekea mashariki au magharibi huku kukiwa na sehemu ya nchi kati ya Yuda na Benyamini iliyotengwa kwa ajili ya shughuli za usimamizi. “Patakatifu pa Yehova” na “jiji” linaloitwa Yehova-Shama liko katika sehemu hiyo iliyotengwa.—Ezekieli 48:9, 10, 15, 35.

      Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

      40:3–47:12—Hekalu la maono ya Ezekieli linafananisha nini? Kwa kweli, hekalu hilo kubwa sana ambalo Ezekieli anaona katika maono halikujengwa kamwe. Linafananisha Hekalu la kiroho la Mungu—mpango wake ulio kama hekalu kwa ajili ya ibada safi katika siku zetu. (Ezekieli 40:2; Mika 4:1; Waebrania 8:2; 9:23, 24) Maono ya hekalu yanatimizwa katika “siku za mwisho” wakati ambapo ukuhani unasifishwa. (2 Timotheo 3:1; Ezekieli 44:10-16; Malaki 3:1-3) Hata hivyo, utimizo wa mwisho wa maono hayo utakuwa katika Paradiso. Hekalu la maono ya Ezekieli liliwapa Wayahudi waliohamishwa ahadi ya kwamba ibada safi itarudishwa na kwamba kila familia ya Kiyahudi itapata urithi wake katika nchi.

      40:3–43:17—Kupima hekalu kunamaanisha nini? Kupimwa kwa hekalu ni ishara ya kwamba kusudi la Yehova kuhusu ibada safi litatimizwa hakika.

      43:2-4, 7, 9—Ni nini iliyokuwa “mizoga ya wafalme wao” ambayo ilipaswa kuondolewa hekaluni? Kwa wazi mizoga hiyo ilifananisha sanamu. Watawala wa Yerusalemu na wakaaji wake walikuwa wamelichafua hekalu la Mungu kwa sanamu, na hivyo wakazifanya kuwa wafalme wao.

      43:13-20—Madhabahu ambayo Ezekieli aliona katika maono inafananisha nini? Madhabahu hiyo inafananisha mapenzi ya Mungu kuhusiana na dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. Kwa sababu ya uandalizi huo, watiwa-mafuta wanatangazwa kuwa waadilifu, nao “umati mkubwa” una msimamo safi machoni pa Mungu. (Ufunuo 7:9-14; Waroma 5:1, 2) Labda hiyo ndiyo sababu “bahari ya kuyeyushwa” ya hekalu la Sulemani, yaani, beseni kubwa la maji ambalo makuhani walitumia kuoga, haiko katika hekalu hilo la maono.—1 Wafalme 7:23-26.

      44:10-16—Ni nani wanaofananishwa na jamii ya kikuhani? Jamii ya kikuhani ilionyesha kimbele kikundi cha Wakristo watiwa-mafuta katika siku zetu. Walisafishwa mnamo 1918 Yehova alipoketi “kama msafishaji na mtakasaji” katika hekalu la kiroho. (Malaki 3:1-5) Wale waliokuwa safi au waliotubu wangedumisha pendeleo lao la utumishi. Baada ya hilo, walihitaji kujitahidi sana kuendelea kujitunza “bila doa kutokana na ulimwengu,” na hivyo kuuwekea mfano “umati mkubwa,” unaofananishwa na makabila yasiyo ya kikuhani.—Yakobo 1:27; Ufunuo 7:9, 10.

      45:1; 47:13–48:29—“Nchi” na kugawanywa kwa nchi kunafananisha nini? Nchi inafananisha eneo la utendaji la watu wa Mungu. Haidhuru anaishi wapi, mwabudu wa Yehova yumo katika nchi iliyorudishwa mradi tu anaunga mkono ibada ya kweli. Kugawanywa kwa nchi kutatimizwa mara ya mwisho katika ulimwengu mpya wakati kila mtu mwaminifu atakapopewa urithi wake.—Isaya 65:17, 21.

      Ezekieli 45:7, 16—Ni nini kinachoonyeshwa na mchango ambao watu wanatoa kwa ajili ya jamii ya kikuhani na kwa mkuu? Katika hekalu la kiroho, hilo hasa linaonyesha utegemezo wa kiroho, yaani, kutoa msaada na kuonyesha roho ya ushirikiano.

      47:1-5—Ni nini kinachofananishwa na maji ya mto ambao Ezekieli anaona katika maono? Maji hayo yanafananisha uandalizi wa Yehova kwa ajili ya uzima, kutia ndani dhabihu ya fidia ya Kristo Yesu na ujuzi juu ya Mungu unaopatikana katika Biblia. (Yeremia 2:13; Yohana 4:7-26; Waefeso 5:25-27) Kina cha mto huo kinazidi kuongezeka ili wapya wanaokubali ibada ya kweli wapate nafasi humo. (Isaya 60:22) Maji ya uzima ya mto huo yatatiririka kwa nguvu zaidi wakati wa ile Miaka Elfu, nayo yatatia ndani uelewaji zaidi unaotegemea vile “vitabu vya kukunja” vitakavyofunguliwa wakati huo.—Ufunuo 20:12; 22:1, 2.

      47:12—Miti ya matunda inafananisha nini? Miti hiyo ya mfano inafananisha maandalizi ya kiroho ya Mungu ya kuwarudisha wanadamu kwenye ukamilifu.

      48:15-19, 30-35—Jiji katika maono ya Ezekieli linafananisha nini? Jiji la “Yehova-Shama” liko katika nchi “najisi,” na hilo linaonyesha kwamba linafananisha jambo fulani la kidunia. Inaelekea kwamba jiji hilo linafananisha usimamizi wa kidunia ambao unawafaidi wote watakaofanyiza “dunia mpya” yenye uadilifu. (2 Petro 3:13) Kuwa na malango kila upande kunaonyesha kwamba linaweza kuingiwa kwa urahisi. Waangalizi miongoni mwa watu wa Mungu wanapaswa kuwa wenye kufikika.

      Mambo Tunayojifunza:

      40:14, 16, 22, 26. Michongo ya miti ya mitende iliyokuwa kwenye miingilio ya hekalu hilo inaonyesha kwamba wale tu walio wanyoofu kiadili ndio wanaoruhusiwa kuingia. (Zaburi 92:12) Hilo linatufundisha kwamba ibada yetu inakubalika kwa Yehova ikiwa tu sisi ni wanyoofu.

      44:23. Tunashukuru kama nini kwa ajili ya utumishi unaotolewa na jamii ya kikuhani leo! “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anaongoza katika kuandaa chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa, chakula ambacho kinatusaidia kutambua tofauti kati ya kitu safi na kisicho safi machoni pa Yehova.—Mathayo 24:45.

      47:9, 11. Ujuzi, ambao ni sehemu muhimu ya maji ya mfano, umekuwa ukiponya kwa njia ya ajabu katika siku zetu. Ujuzi huo unawapa uhai wa kiroho watu wanaoupata. (Yohana 17:3) Kwa upande mwingine, wale wasiokubali maji yanayoleta uzima ‘wataachwa kwenye chumvi,’ yaani, wataharibiwa milele. Ni muhimu kama nini ‘tufanye kabisa yote tunayoweza ili tulitumie sawasawa neno la kweli’!—2 Timotheo 2:15.

  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ezekieli—II
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Agosti 1
    • [Picha katika ukurasa wa 9]

      Hekalu tukufu la maono ya Ezekieli

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki