Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Imani ya Kikristo Itajaribiwa
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Mei 15
    • Imani ya Kikristo Itajaribiwa

      “Imani si miliki ya watu wote.”—2 WATHESALONIKE 3:2.

      1. Historia imeonyeshaje kwamba si watu wote walio na imani ya kweli?

      KATIKA historia yote, kumekuwa na wanaume, wanawake, na watoto wenye imani ya kweli. Kivumishi “kweli” chafaa kwa sababu mamilioni ya watu wengine wameonyesha namna ya imani ambayo imekuwa kama wepesi wa kuamini bila ushuhuda, utayari wa kuamini bila msingi au sababu halali. Imani hiyo mara nyingi imehusisha miungu ya uwongo au njia za ibada zisizopatana na Yehova, Mweza Yote, na pia Neno lake lililofunuliwa. Kwa hiyo, mtume Paulo aliandika hivi: “Imani si miliki ya watu wote.”—2 Wathesalonike 3:2.

      2. Kwa nini ni muhimu kuchunguza imani yetu wenyewe?

      2 Lakini taarifa ya Paulo yadokeza kwamba, wakati huo baadhi ya watu walikuwa na imani ya kweli na, sawa na wakati huo, baadhi ya watu leo wana imani ya kweli. Wasomaji walio wengi wa jarida hili hutamani kuwa na imani ya kweli kama hiyo, na kuizidisha—imani ipatanayo na ujuzi sahihi wa kweli ya kimungu. (Yohana 18:37; Waebrania 11:6) Je, ndivyo ilivyo kwako? Basi, ni jambo la lazima kwamba utambue na ujitayarishe kwa sababu ya uhakika wa kwamba, imani yako itajaribiwa. Kwa nini yaweza kusemwa hivyo?

      3, 4. Kwa nini yatupasa kumtazama Yesu kwa habari ya majaribu ya imani?

      3 Yatupasa tukubali kwamba Yesu Kristo ni wa maana katika imani yetu. Kwa kweli, Biblia humtaja kuwa Mkamilishaji wa imani yetu. Humtaja hivyo kwa sababu ya yale Yesu aliyosema na kufanya, hasa kwa sababu ya jinsi alivyoutimiza unabii. Aliimarisha msingi ambao juu yake wanadamu waweza kujenga imani ya kweli. (Waebrania 12:2; Ufunuo 1:1, 2) Hata hivyo, twasoma kwamba Yesu “[ali]jaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini asiye na dhambi.” (Waebrania 4:15) Naam, imani ya Yesu ilijaribiwa. Jambo hilo lapaswa kutufariji, badala ya kutuvunja moyo au kututia wasiwasi.

      4 Yesu “alijifunza utii” kwa kupatwa na majaribu makubwa hata kufikia hatua ya kufa kwenye mti. (Waebrania 5:8) Alithibitisha kwamba wanadamu waweza kuishi kulingana na imani ya kweli, licha ya majaribu ambayo huenda yakawapata. Jambo hilo hupata maana mahususi tufikiriapo yale Yesu aliyosema kuhusu wafuasi wake: “Zingatieni akilini neno nililowaambia, Mtumwa si mkubwa zaidi kuliko bwana-mkubwa wake.” (Yohana 15:20) Kwa kweli, kwa habari ya wafuasi wake katika wakati wetu, Yesu alitabiri hivi: “Nanyi mtakuwa vitu vya kuchukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.”—Mathayo 24:9.

      5. Maandiko yanaonyeshaje kwamba tutakabili majaribu?

      5 Mapema katika karne hii, hukumu ilianza na nyumba ya Mungu. Maandiko yalitabiri hivi: “Ni wakati uliowekwa rasmi kwa hukumu kuanza na nyumba ya Mungu. Sasa ikiwa yaanza na sisi kwanza, utakuwa nini mwisho wa wale wasio watiifu kwa habari njema ya Mungu? ‘Na ikiwa ni kwa shida mtu mwadilifu anaokolewa, mtu asiyemwogopa Mungu na mtenda-dhambi wataonekana wapi?’”—1 Petro 4:17, 18.

      Imani Yajaribiwa—Kwa Nini?

      6. Kwa nini imani ambayo imejaribiwa ni yenye thamani kubwa?

      6 Katika maana fulani, imani ambayo haijajaribiwa imekosa thamani iliyothibitishwa, na ubora wake hubaki bila kujulikana. Waweza kuilinganisha na hundi ambayo fedha zake hazijalipwa. Huenda ukawa ulipokea hundi ikiwa malipo ya kazi uliyofanya, bidhaa ulizoandaa, au hata ikiwa zawadi. Huenda hiyo hundi ikaonekana kuwa halali, lakini ndivyo ilivyo? Je, ungeweza kupata fedha zilizo sawa na zile zinazoonyeshwa kwenye hundi hiyo? Vivyo hivyo, imani yetu haipaswi kuwa wonyesho tu wa nje au kujidai tu. Lazima ijaribiwe ikiwa tutathibitisha kwamba ina umaana na ubora halisi. Imani yetu ijaribiwapo, huenda tukagundua kwamba ni yenye nguvu na yenye thamani pia. Huenda jaribu pia likafunua maeneo yoyote ambayo imani yetu yahitaji kutakaswa au kuimarishwa.

      7, 8. Majaribu ya imani yetu hutokana na chanzo gani?

      7 Mungu huruhusu mnyanyaso au majaribu mengine ya imani yatupate. Twasoma hivi: “Wakati yuko chini ya jaribu, acheni yeyote asiseme: ‘Mimi ninajaribiwa na Mungu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13) Je, ni nani, au ni nini ambacho huleta majaribu hayo? Ni Shetani, ulimwengu, na mwili wetu usio mkamilifu.

      8 Huenda tukakubali kwamba Shetani hutumia uvutano wenye nguvu juu ya ulimwengu, juu ya kufikiri kwa huo ulimwengu na juu ya njia zake. (1 Yohana 5:19) Na labda twajua kwamba yeye huchochea mnyanyaso dhidi ya Wakristo. (Ufunuo 12:17) Lakini je, twasadikishwa hivyohivyo kwamba Shetani hujaribu kutuongoza vibaya kwa kutushawishi kwa kutumia mwili wetu usio mkamilifu, akitushawishi kwa vivutio vya kilimwengu, akitumaini kwamba atatunasa, tukose kumtii Mungu, na mwishowe tukose kibali cha Yehova? Bila shaka, njia za Shetani hazipaswi kutushangaza, kwa sababu alitumia mbinu hizohizo alipokuwa akijaribu kumshawishi Yesu.—Mathayo 4:1-11.

      9. Twaweza kunufaikaje na vielelezo vya imani?

      9 Kupitia Neno lake na kutaniko la Kikristo, Yehova hutuandalia vielelezo halisi vya imani ambavyo twaweza kuiga. Paulo alionya kwa upole hivi: “Kwa muungano iweni waigaji wangu, akina ndugu, na fulizeni kuwaangalia wale wanaotembea katika njia ilinganayo na kielelezo mlicho nacho katika sisi.” (Wafilipi 3:17) Akiwa mmoja wa watumishi wa Mungu wa karne ya kwanza waliotiwa mafuta, Paulo aliongoza katika kufanya kazi za imani licha ya kupatwa na majaribu makubwa. Hadi kufikia mwisho wa karne ya 20, tuna vielelezo vya imani viwezavyo kulinganishwa na hivyo vya karne ya kwanza. Maneno ya Waebrania 13:7 yatumika sasa kwa nguvu sawa na vile yalivyotumika wakati Paulo alipoyaandika: “Kumbukeni wale ambao wanaongoza miongoni mwenu, ambao wamelisema neno la Mungu kwenu, nanyi mfikiriapo jinsi mwisho wa mwenendo wao upatavyo kuwa, igeni imani yao.”

      10. Tumekuwa na vielelezo gani mahususi vya imani katika nyakati za majuzi?

      10 Onyo hilo la upole ni lenye nguvu mahususi tuchunguzapo jinsi ambavyo mwendo wa mabaki watiwa-mafuta umethibitika kuwa. Twaweza kufikiria kwa makini kielelezo chao na kuiga imani yao. Wao wana imani ya kweli ambayo imetakaswa na majaribu. Kwa mianzo midogo huko nyuma miaka ya 1870, udugu wa Kikristo wa ulimwenguni pote ulisitawi. Wakiwa matunda ya imani na uvumilivu wa watiwa-mafuta ya tangu wakati huo na kuendelea, Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni tano na nusu sasa wanahubiri na kufundisha juu ya Ufalme wa Mungu. Kutaniko la kisasa la tufeni pote la waabudu wa kweli na wenye bidii, ni ithibati dhahiri ya imani ambayo imejaribiwa.—Tito 2:14.

      Imani Yajaribiwa Kuhusiana na Mwaka wa 1914

      11. Mwaka wa 1914 ulikuwaje wenye maana kwa C. T. Russell na washiriki wake?

      11 Miaka mingi kabla ya kuzuka kwa vita ya ulimwengu ya kwanza, mabaki watiwa-mafuta walikuwa wakipiga mbiu kwamba, mwaka wa 1914 ungekuwa tarehe yenye maana katika unabii wa Biblia. Hata hivyo, baadhi ya matarajio yao yalikuwa ya kabla ya wakati, na maoni yao juu ya yale ambayo yangetukia hayakuwa sahihi kabisa. Kwa kielelezo, C. T. Russell, msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Society, na washiriki wake, wangeweza kuona kwamba kazi kubwa mno ya kuhubiri ilihitajika. Walisoma hivi: “Gospeli ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14, King James Version) Ingawa hivyo, ni jinsi gani hesabu yao iliyokuwa ndogo kwa kulinganishwa, ingeweza kwa vyovyote kufanya hivyo?

      12. Mmoja wa washiriki wa Russell aliitikiaje kweli ya Biblia?

      12 Fikiria jinsi jambo hilo lilivyomwathiri A. H. Macmillan, mshiriki wa Russell. Macmillan, aliyezaliwa Kanada, hakuwa amefikia umri wa miaka 20 alipopata kitabu cha Russell kiitwacho The Plan of the Ages (1886). (Kitabu hicho ambacho pia kiliitwa The Divine Plan of the Ages, kilipata kuwa Buku la 1 la seti iitwayo Studies in the Scriptures, iliyogawanywa kwa wingi mno. Buku la 2 liitwalo, The Time Is at Hand [1889], lilionyesha mwaka wa 1914 kuwa mwisho wa “nyakati za Wasio Wayahudi.” [Luka 21:24, KJ]) Usiku uleule Macmillan alipoanza kukisoma, aliwaza hivi: “Hiyo yasikika kuwa kweli!” Katika kiangazi cha mwaka wa 1900, alikutana na Russell kwenye mkusanyiko wa Wanafunzi wa Biblia, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Punde si punde, Macmillan akabatizwa na kuanza kufanya kazi pamoja na Ndugu Russell kwenye makao makuu ya Sosaiti huko New York.

      13. Macmillan na wengineo waliona tatizo gani kuhusiana na utimizo wa Mathayo 24:14?

      13 Kwa kutegemea usomaji wao wa Biblia, hao Wakristo watiwa-mafuta walionyesha mwaka wa 1914 kuwa wakati wa badiliko la maana katika kusudi la Mungu. Lakini Macmillan na wengineo walijiuliza jinsi ambavyo huko kuyahubiri mataifa kulikotabiriwa kwenye Mathayo 24:14 kungeweza kutimizwa katika wakati mfupi uliobaki. Baadaye alisema hivi: “Nakumbuka nikizungumzia jambo hilo pamoja na Ndugu Russell mara nyingi, na alikuwa akisema, ‘Ndugu, hapahapa katika New York tuna Wayahudi wengi zaidi kuliko walioko Yerusalemu. Tuna watu wengi zaidi kutoka Ireland kuliko walioko Dublin. Na tuna Waitalia wengi zaidi kuliko walioko Roma. Sasa ikiwa tutawafikia wakiwa hapa, hiyo itakuwa kuufikia ulimwengu kwa ule ujumbe.’ Lakini hilo halikuelekea kutosheleza akili zetu. Kwa hiyo basi, tukafikiria kutokeza ‘Photo-Drama’ [Drama-Picha].”

      14. Ni mradi gani wenye kutokeza ambao ulianzishwa kabla ya mwaka wa 1914?

      14 Hiyo “Photo-Drama of Creation” (Drama-Picha ya Uumbaji) ilikuwa jambo lenye kutokeza kama nini! Ilikuwa ni muunganisho wa sinema na slaidi za rangi, ambazo ziliambatanishwa na hotuba za Biblia na muziki uliochezwa kwa kutumia sahani za santuri. Mwaka wa 1913, gazeti la Mnara wa Mlinzi lilisema hivi kuhusu mkusanyiko uliokuwa Arkansas, Marekani: “Iliamuliwa kwa kauli moja kwamba, wakati umefika wa kutumia sinema katika kuifundisha kweli ya Biblia. . . [Russell] alieleza kwamba alikuwa akishughulikia mpango huohuo kwa miaka mitatu na sasa alikuwa na mamia ya picha nzuri zilizokuwa zinakaribia kuwa tayari, ambazo bila shaka zingevutia umati mkubwa na kuitangaza Gospeli, na kusaidia umma kurudisha imani yao katika Mungu.”

      15. Ile “Photo-Drama” ilikuwa na matokeo ya aina gani?

      15 Ile “Photo-Drama” ilitimiza jambo hilohilo baada ya kuonyeshwa mara ya kwanza katika Januari 1914. Zifuatazo ni ripoti kutoka katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la mwaka wa 1914 (la Kiingereza):

      Aprili 1: “Baada ya kutazama sehemu mbili, kasisi mmoja alisema hivi: ‘Nimetazama sehemu moja na nusu tu ya PHOTO-DRAMA OF CREATION, lakini kutoka kwayo, tayari nimejifunza mambo mengi zaidi kuhusu Biblia kushinda yale niliyojifunza katika mtaala wangu wa miaka mitatu katika seminari ya theolojia.’ Baada ya kuitazama, Myahudi mmoja alisema, ‘Naenda zangu nikiwa Myahudi bora zaidi ya vile nilivyokuwa nilipoingia.’ Makasisi na watawa wa kike kadhaa wamekuja kuitazama hiyo DRAMA na wameonyesha uthamini mkubwa. . . . Ni seti kumi na mbili tu za hiyo DRAMA ambazo zimekamilika . . . Hata hivyo tayari tumeyafikia na tunayatumikia majiji thelathini na moja . . . Watu zaidi ya thelathini na tano elfu kwa siku, wanatazama, kusikia, kushangilia, na kufikiri, nao wanabarikiwa.”

      Juni 15: “Hizo picha zimenifanya niwe na bidii zaidi kuieneza Kweli, na imeongeza upendo wangu kwa Baba wa Kimbingu na Ndugu yetu Mkubwa mpendwa, Yesu. Mimi husali kila siku ili Mungu abariki sana hiyo PHOTO-DRAMA OF CREATION na wote wanaoshiriki kuionyesha. . . . Ni mimi mtumishi wenu katika Yeye, F. W. KNOCHE.—Iowa.”

      Julai 15: “Twapendezwa kuona uvutio mzuri ajabu ambao hizo picha zimekuwa nao katika jiji hili, na tumepata uhakikisho wa kwamba, ushahidi huo unaotolewa ulimwengu pia unatumiwa kukusanya wengi wanaothibitika kuwa vito vyenye kuchaguliwa na Bwana. Twajua juu ya hesabu kubwa ya wanafunzi wa Biblia ambao sasa wanashirikiana na Darasa hapa kwa sababu ya hiyo kazi ya Photo-Drama. . . . Dada yenu katika Bwana, EMMA L. BRICKER.”

      Novemba 15: “Tuna hakika kwamba mtaterema kusikia juu ya ushahidi mzuri ambao unatolewa kupitia PHOTO-DRAMA OF CREATION kwenye jumba liitwalo The London Opera House, Kingsway. Mkono wenye kuongoza wa Bwana umedhihirishwa vizuri ajabu katika kila shughuli ya maonyesho hayo hivi kwamba, ndugu wanashangilia sana . . . Watazamaji wetu walikuwa watu wa matabaka yote na aina zote; tumewaona makasisi wengi kati ya wahudhuriaji. Kasisi mmoja . . . aliomba apewe tikiti ili yeye na mke wake waweze kuja na kuiona tena. Kasisi fulani wa Kanisa la Uingereza, ameitazama hiyo DRAMA mara kadhaa, na . . . amewaleta rafiki zake wengi ili kuishuhudia. Maaskofu wawili wamekuwapo, na watu kadhaa wenye vyeo.”

      Desemba 1: “Mke wangu nami twamshukuru Baba yetu wa Kimbingu kwa kweli, kwa sababu ya baraka kubwa na yenye thamani sana ambayo imetujia kupitia kwako. Tuliielewa na kuikubali Kweli kwa sababu ya PHOTO-DRAMA yenu nzuri . . . Tuna mabuku yako sita ya STUDIES IN THE SCRIPTURES. Yanatusaidia sana.”

      Kuitikia Majaribu Wakati Huo

      16. Kwa nini mwaka wa 1914 ulileta majaribu ya imani?

      16 Ingawa hivyo, ilikuwaje wakati ambapo hao Wakristo wenye moyo mweupe na wenye kujitoa waligundua kwamba tarajio lao la kujiunga pamoja na Bwana mwaka wa 1914 halikutimizwa? Watiwa-mafuta hao walipatwa na kipindi chenye majaribu yasiyo na kifani. Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1914, (la Kiingereza) lilitangaza hivi: “Na tukumbuke kwamba tuko katika majira ya majaribu.” Juu ya hilo, kitabu Mashahidi wa Yehova Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu (1997) chataarifu hivi: “Miaka ya kutoka 1914 hadi 1918, ilithibitika kwelikweli kuwa ‘majira ya kutahini [kujaribiwa]’ kwa Wanafunzi wa Biblia.” Je, wangeruhusu imani yao itakaswe na kufikiri kwao kurekebishwe ili waweze kuchukua daraka la kufanya kazi kubwa iliyokuwa mbele yao?

      17. Watiwa-mafuta waaminifu waliitikiaje kubaki duniani baada ya mwaka wa 1914?

      17 Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1916, (la Kiingereza) lilisema hivi: “Tuliwaza kwamba kazi ya Uvunaji ya kukusanya Kanisa [watiwa-mafuta], ingetimizwa kabla ya mwisho wa Nyakati za Wasio Wayahudi; lakini Biblia haikusema jambo lolote kama hilo. . . . Je, tunajuta kwamba kazi ya Uvunaji inaendelea? . . . Ndugu wapendwa, mtazamo wetu wa sasa wapaswa kuwa wa kuonyesha shukrani kubwa kwa Mungu, wa kuonyesha uthamini wenye kuongezeka wa Kweli nzuri ambayo Ametupa pendeleo la kuielewa na kutambulishwa kwayo, na wa kuwa na bidii yenye kuongezeka katika kusaidia kupelekea wengine ujuzi wa hiyo Kweli.” Imani yao ilikuwa imejaribiwa, hata hivyo walikabili jaribu hilo kwa mafanikio. Lakini yatupasa sisi Wakristo tujue kwamba, majaribu ya imani yaweza kuwa mengi na ya aina mbalimbali.

      18, 19. Baada ya kifo cha Ndugu Russell, ni majaribu gani mengine ya imani yaliyofuata kwa watu wa Mungu?

      18 Kwa kielelezo, punde baada ya Ndugu Charles T. Russell kufa, aina nyingine ya jaribu iliwapata mabaki. Hilo lilikuwa jaribu la uaminifu-mshikamanifu wao na imani yao. Ni nani ‘aliyekuwa mtumwa mwaminifu’ wa Mathayo 24:45? Baadhi yao walihisi kwamba huyo mtumwa mwaminifu alikuwa Ndugu Russell mwenyewe, nao walisita kushirikiana na mipango mipya ya kitengenezo. Ikiwa alikuwa amekuwa huyo mtumwa, ndugu wangefanya nini kwa kuwa sasa alikuwa amekufa? Je, iliwapasa wafuate mtu fulani aliyechaguliwa karibuni, au sasa ulikuwa wakati wa kutambua kwamba Yehova alikuwa akitumia, si mtu mmoja tu, bali kikundi chote cha Wakristo kikiwa mtumishi, au jamii ya mtumwa?

      19 Jaribu la ziada liliwapata Wakristo wa kweli mwaka wa 1918, wakati ambapo wenye mamlaka wa kilimwengu, wakichochewa na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo, ‘walitunga madhara kwa njia ya sheria’ dhidi ya tengenezo la Yehova. (Zaburi 94:20, KJ) Mnyanyaso wenye jeuri ulioongezeka ulianzishwa dhidi ya Wanafunzi wa Biblia katika Amerika Kaskazini na Ulaya. Upinzani uliochochewa na makasisi ulifikia upeo katika Mei 7, 1918, wakati ambapo waranti za serikali ya muungano ya Marekani zilitolewa ili kumkamata J. F. Rutherford na washiriki kadhaa wa karibu, kutia na A. H. Macmillan. Walishtakiwa isivyo kweli kuwa wachochezi, na wenye mamlaka walipuuza maombi yao ya kutokuwa na hatia.

      20, 21. Kama ilivyotabiriwa kwenye Malaki 3:1-3, ni kazi gani iliyofanywa miongoni mwa watiwa-mafuta?

      20 Ingawa haikutambuliwa hivyo wakati huo, kazi ya kutakasa ilikuwa ikiendelea, kama ifafanuliwavyo kwenye Malaki 3:1-3: “Ni nani atakayestahimili siku ya kuja kwake? au ni nani atakayesimama atakapoonekana yeye? Kwa maana yeye [mjumbe wa agano] ni mfano wa moto wa mtu asafishaye fedha, ni mfano wa sabuni ya mtu afuaye nguo; naye ataketi kama asafishaye fedha na kuitakasa, naye atawatakasa wana wa Lawi, atawasafisha kama dhahabu na fedha; nao watamtolea BWANA dhabihu katika haki.”

      21 Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilipokaribia kwisha, baadhi ya Wanafunzi wa Biblia walikabili jaribu jingine la imani—kama wangedumisha kutokuwamo kabisa kuhusiana na mambo ya kijeshi ya kilimwengu. (Yohana 17:16; 18:36) Baadhi yao hawakufanya hivyo. Kwa hiyo mwaka wa 1918, Yehova alimtuma “mjumbe wa agano,” Kristo Yesu, kwenye mpango Wake wa hekalu la kiroho ili kukitakasa kikundi kidogo cha waabudu Wake kisiwe na mawaa ya kilimwengu. Waliokubali wajibu wa kuonyesha imani ya kweli walijifunza kutokana na jambo hilo lililowapata na kusonga mbele, wakiendelea kuhubiri kwa bidii.

      22. Kuhusiana na majaribu ya imani, ni mambo gani ambayo yabaki kuchunguzwa?

      22 Yale ambayo tumechunguza si mambo yenye upendezi wa kijuujuu tu wa kihistoria. Yanahusika moja kwa moja na hali ya kiroho ya sasa ya kutaniko la ulimwenguni pote la Yehova. Lakini acheni tuchunguze katika makala inayofuata baadhi ya majaribu ya imani ambayo watu wa Mungu leo wanakabili, na tuone jinsi tuwezavyo kuyashinda kwa mafanikio.

  • Ubora wa Imani Yako—Wajaribiwa Sasa
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Mei 15
    • Ubora wa Imani Yako—Wajaribiwa Sasa

      “Fikirieni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, mkutanapo na majaribu ya namna mbalimbali, kama mjuavyo kwamba ubora huu uliojaribiwa wa imani yenu hutokeza uvumilivu.”—YAKOBO 1:2, 3.

      1. Kwa nini Wakristo watarajie majaribu ya imani yao?

      WAKRISTO wa kweli hawatamani kuteseka, wala hawafurahii maumivu au kutwezwa. Hata hivyo, wao hukumbuka maneno yaliyo juu ambayo yaliandikwa na Yakobo, ndugu-nusu ya Yesu. Kristo aliwaeleza wanafunzi wake wazi kwamba, wangeweza kutarajia mnyanyaso na magumu mengineyo kwa sababu ya kushikamana sana kwao na viwango vya Mungu. (Mathayo 10:34; 24:9-13; Yohana 16:33) Hata hivyo, shangwe yaweza kutokezwa na majaribu hayo. Jinsi gani?

      2. (a) Majaribu ya imani yetu yaweza kutokezaje shangwe? (b) Ni jinsi gani uvumilivu waweza kuwa na kazi yao ikiwa kamili katika hali yetu?

      2 Sababu kuu itufanyayo tupate shangwe tunapokuwa chini ya majaribu au mitihani ya imani ni kwamba, majaribu hayo hutokeza matunda mazuri. Kama vile Yakobo asemavyo, kustahimili tunapokabiliwa na majaribu au magumu, “hutokeza uvumilivu.” Twaweza kunufaika kwa kusitawisha sifa hiyo ya Kikristo yenye thamani. Yakobo aliandika hivi: “Acheni uvumilivu uwe na kazi yao ikiwa kamili, ili nyinyi mpate kuwa kamili na timamu katika mambo yote, bila ukosefu katika kitu chochote.” (Yakobo 1:4) Uvumilivu una kazi ya kufanya, “kazi” fulani. Mgawo wake ni kutufanya tuwe kamili katika mambo yote, ukitusaidia kuwa Wakristo wenye usawaziko na wenye kukomaa. Kwa sababu hiyo, kwa kuruhusu majaribu yaendelee hadi mwisho wake, bila kujaribu kwa vyovyote kutumia njia zisizo za Kimaandiko ili kuyakomesha upesi, imani yetu inajaribiwa na kutakaswa. Ikiwa tulikuwa tumekosa subira, huruma, fadhili, au upendo katika kushughulika na hali au na wanadamu wenzetu, uvumilivu waweza kutufanya tuwe kamili zaidi. Naam, huu ndio mfuatano wa mambo: Majaribu hutokeza uvumilivu; uvumilivu huongeza sifa za Kikristo; hizo hutokeza shangwe.—1 Petro 4:14; 2 Petro 1:5-8.

      3. Kwa nini haitupasi kurudi nyuma kwa kuogopa majaribu au mitihani ya imani yetu?

      3 Mtume Petro pia alikazia ni kwa nini hatuhitaji kuhofu wala kurudi nyuma kutoka kwenye majaribu ya imani yetu. Aliandika hivi: “Katika uhakika huu mnashangilia sana, ingawa kwa muda kidogo mmetiwa kihoro wakati wa sasa, ikiwa ni lazima, kwa namna mbalimbali za majaribu, ili ubora wa imani yenu uliojaribiwa, ulio na thamani kubwa zaidi sana kuliko dhahabu ambayo huharibika ijapokuwa kuthibitishwa kwayo na moto, upatikane kuwa sababu ya sifa na utukufu na heshima wakati wa ufunuo wa Yesu Kristo.” (1 Petro 1:6, 7) Maneno hayo hasa ni yenye kutia moyo sasa, kwa sababu “dhiki kubwa”—wakati wa sifa, utukufu, heshima, na wa kuokoka—iko karibu zaidi kuliko vile ambavyo wengine huenda wakafikiri, na iko karibu zaidi kuliko tulipopata kuwa waamini.—Mathayo 24:21; Waroma 13:11, 12.

      4. Ndugu mmoja alihisije juu ya majaribu ambayo yeye na Wakristo wengine watiwa-mafuta walipatwa nayo?

      4 Katika makala iliyotangulia, tulichunguza majaribu ambayo mabaki watiwa-mafuta walikabili kuanzia mwaka wa 1914 na kuendelea. Je, hayo yalikuwa msingi wa kuwa na shangwe? A. H. Macmillan alitoa maoni haya kwa kukumbuka wakati uliopita: “Nimeona majaribu makali yakilipata tengenezo na majaribu ya imani ya wale waliomo ndani yake. Kwa msaada wa roho ya Mungu, tengenezo liliokoka na kuendelea kusitawi. Nimeona hekima ya kumngojea Yehova kwa subira ili aboreshe uelewevu wetu wa mambo ya Kimaandiko, badala ya kukasirika kwa sababu ya wazo jipya. . . . Hata iwe pindi kwa pindi tutalazimika kufanya marekebisho gani katika maoni yetu, jambo hilo halingebadili maandalizi yenye rehema ya fidia na ahadi ya Mungu ya uhai wa milele. Kwa hiyo hakukuwa na uhitaji wa kuruhusu imani yetu idhoofishwe na matarajio ambayo hayakutimizwa au mabadiliko katika maoni.”—Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 1966, ukurasa wa 504 (la Kiingereza).

      5. (a) Ni manufaa zipi zilizotokezwa na kupatwa na majaribu kwa mabaki? (b) Kwa nini jambo hilo la kujaribiwa litupendeze sasa?

      5 Wakristo watiwa-mafuta waliookoka kipindi cha majaribu cha 1914-1919 waliwekwa huru na uvutano wenye kudhibiti wa ulimwengu, na mazoea ya kidini ya Kibabiloni. Mabaki walisonga mbele wakiwa watu waliosafishwa na kutakaswa, wakitoa kwa utayari dhabihu za sifa kwa Mungu na wakiwa na uhakikisho kwamba, walikuwa kikundi cha watu waliokubalika kwake. (Isaya 52:11; 2 Wakorintho 6:14-18) Hukumu ilikuwa imeanza na nyumba ya Mungu, lakini haingekamilishwa katika kipindi kimoja kilichowekwa. Kujaribiwa na kupepetwa kwa watu wa Mungu kwaendelea. Imani ya wale watumainio kuokoka “dhiki kubwa” inayokaribia, inajaribiwa pia. (Ufunuo 7:9, 14) Inajaribiwa katika njia sawa na vile imani ya watiwa-mafuta ilivyojaribiwa, na vilevile katika njia nyinginezo.

      Huenda Wewe Ukajaribiwaje?

      6. Ni aina gani ya jaribu kali ambayo imewapata watu wengi?

      6 Wakristo wengi wamefikiria ugumu wa kukinza majaribu ya namna ya mashambulizi ya moja kwa moja. Wao hukumbuka ripoti hii: “[Viongozi wa Kiyahudi] wakawaita mitume, wakawapiga viboko, na kuwaagiza wakome kusema juu ya msingi wa jina la Yesu, na kuwaacha waende zao. Kwa hiyo, hawa wakashika njia yao kwenda kutoka mbele ya Sanhedrini, wakishangilia kwa sababu walikuwa wamehesabiwa wenye kustahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake.” (Matendo 5:40, 41) Na historia ya kisasa ya watu wa Mungu, hasa wakati wa vita vya ulimwengu, huonyesha wazi kwamba wengi wa Mashahidi wa Yehova kwa kweli walipigwa na kutendwa hata vibaya zaidi na wanyanyasaji.

      7. Ni kwa kadiri gani Wakristo wa siku ya kisasa wameonyesha imani?

      7 Kuhusiana na Wakristo kuwa watu wa kunyanyaswa, ulimwengu hautofautishi watiwa-mafuta na umati mkubwa wa “kondoo wengine.” (Yohana 10:16) Kwa miaka ambayo imepita, washiriki wa vikundi vyote viwili wamejaribiwa vikali kwa kutiwa gerezani na hata kufia-imani kwa sababu ya upendo wao kwa Mungu na imani yao katika yeye. Vikundi vyote viwili vimehitaji roho ya Mungu, hata viwe na tumaini gani. (Linganisha gazeti la Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 1996, ukurasa wa 31.) Wakati wa miaka ya 1930 na 1940 katika Ujerumani ya Nazi, wengi wa watumishi wa Yehova, kutia na watoto, walionyesha imani isiyo na kifani, na wengi wao walijaribiwa kufikia upeo. Katika nyakati za majuzi zaidi, watu wa Yehova wamekabili jaribu la mnyanyaso katika nchi kama Burundi, Eritrea, Ethiopia, Malawi, Msumbiji, Rwanda, Singapore, na Zaire. Na majaribu ya aina hiyo yanaendelea.

      8. Maelezo ya ndugu mmoja Mwafrika yaonyeshaje kwamba mengi zaidi yahusika katika kujaribiwa kwa imani yetu kuliko kuvumilia tu mnyanyaso katika njia ya kuchapwa?

      8 Hata hivyo, kama ilivyotajwa tayari, imani yetu pia inajaribiwa katika njia zenye hila zaidi. Baadhi ya hayo majaribu si ya moja kwa moja sana na hayatambuliki kwa urahisi. Fikiria jinsi ambavyo ungeitikia baadhi ya majaribu yanayofuata. Ndugu kutoka Angola aliyekuwa na watoto kumi, alikuwa katika kutaniko ambalo kwa muda fulani, lilikuwa halina njia yoyote ya kuwasiliana na ndugu wenye madaraka. Baadaye, wengine waliweza kulizuru hilo kutaniko. Aliulizwa jinsi alivyofaulu kulisha familia yake. Halikuwa swali rahisi kwake kujibu, na angeweza tu kusema kwamba hali ilikuwa ngumu. Je, alikuwa na uwezo wa kulisha familia yake angalau mlo mmoja kwa siku? Alijibu hivi: “Ni vigumu. Tumejifunza kuishi kwa kile tulicho nacho.” Kisha kwa sauti iliyojaa usadikisho, akasema hivi: “Je, hatutarajii hali kama hizi katika siku hizi za mwisho?” Imani kama hiyo ni yenye kutokeza katika ulimwengu, lakini ni ya kawaida miongoni mwa Wakristo waaminifu-washikamanifu, walio na uhakika kamili kwamba, ahadi za Ufalme zitatimizwa.

      9. Tunajaribiwaje kuhusiana na 1 Wakorintho 11:3?

      9 Umati mkubwa pia unajaribiwa kuhusiana na utaratibu wa kitheokrasi. Kutaniko la Kikristo la ulimwenguni pote huongozwa kulingana na kanuni za kimungu na viwango vya kitheokrasi. Hilo humaanisha kwanza kabisa kumtambua Yesu kuwa Kiongozi wa kutaniko. (1 Wakorintho 11:3) Kujitiisha kwake na kwa Baba yake kwa utayari, huonyeshwa kupitia imani yetu katika mapendeleo na maamuzi ya kitheokrasi yahusianayo na kufanya kwetu mapenzi ya Yehova kwa muungano. Zaidi ya hayo, katika kila kutaniko la kwenu, kuna wanaume waliowekwa rasmi kuongoza. Hao ni wanaume wasio wakamilifu, ambao huenda tukaona makosa yao kwa urahisi; hata hivyo, twahimizwa tustahi waangalizi kama hao na kuwa wenye kunyenyekea. (Waebrania 13:7, 17) Je, nyakati nyingine unapata jambo hilo kuwa gumu? Je, kwa kweli hilo ni jaribu kwako? Ikiwa ndivyo, je, unanufaika kutokana na jaribu hilo la imani yako?

      10. Tunakabili jaribu gani kwa habari ya huduma ya shambani?

      10 Tunajaribiwa pia kuhusiana na pendeleo na takwa la kushiriki kwa ukawaida katika huduma ya shambani. Ili tuweze kushinda jaribu hilo, ni lazima tung’amue kwamba, kushiriki kikamili katika huduma huhusisha mengi zaidi ya kuhubiri kwa kiwango kidogo tu, au kufanya hivyo kama wonyesho tu. Kumbuka maoni ya Yesu yenye kibali kuhusu yule mjane maskini aliyetoa vyote alivyokuwa navyo. (Marko 12:41-44) Huenda tukajiuliza wenyewe, ‘Je, ninajitoa vivyo hivyo kuhusiana na huduma yangu ya shambani?’ Sisi sote twapaswa kuwa Mashahidi wa Yehova nyakati zote, tukiwa tayari kuacha nuru yetu ing’ae kwenye kila fursa.—Mathayo 5:16.

      11. Ni jinsi gani mabadiliko katika uelewevu au shauri juu ya mwenendo yaweza kuwa jaribu la imani?

      11 Jaribu jingine ambalo huenda tukakabili lahusiana na kiwango chetu cha uthamini wa nuru inayoongezeka ambayo inamulika kweli ya Biblia, na shauri liandaliwalo na jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. (Mathayo 24:45) Nyakati nyingine, hilo hutaka marekebisho katika mwenendo wa kibinafsi, kama wakati ambapo ilijulikana wazi kwamba wale wenye kutumia tumbaku wangelazimika kuiacha ikiwa walitaka kubaki kutanikoni.a (2 Wakorintho 7:1) Au huenda tukajaribiwa katika kukubali kwetu uhitaji wa kubadili uchaguzi wetu wa muziki au aina nyinginezo za vitumbuizo.b Je, tutashuku hekima ya shauri lenye kutolewa? Au tutairuhusu roho ya Mungu iongoze kufikiri kwetu na itusaidie kuvaa utu wa Kikristo?—Waefeso 4:20-24; 5:3-5.

      12. Ni nini kinachohitajiwa ili kuimarisha imani baada ya mmoja kubatizwa?

      12 Kwa miongo mingi, idadi ya wale wa umati mkubwa imekuwa ikiongezeka, na baada ya ubatizo wao, wanaendelea kuimarisha uhusiano wao na Yehova. Hilo lahusisha mengi zaidi ya kuhudhuria kusanyiko la Kikristo, kuhudhuria mikutano fulani kwenye Jumba la Ufalme, au kushiriki pindi kwa pindi katika utumishi wa shambani. Kwa kutoa kielezi: Huenda kimwili mtu akawa nje ya Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli, lakini je, ameiacha kwa kweli? Je, bado anashikilia mambo yale yaonyeshayo roho ya Babiloni Mkubwa—roho ambayo hudharau viwango vya Mungu vya uadilifu? Je, yeye huchukua kivivi hivi adili na uaminifu katika ndoa? Je, yeye hukazia zaidi masilahi ya kibinafsi na ya vitu vya kimwili kuliko masilahi ya kiroho? Naam, je, amebaki kuwa bila kutiwa doa na ulimwengu?—Yakobo 1:27.

      Kunufaika na Imani Iliyojaribiwa

      13, 14. Wengine wamefanya nini baada ya kuanza kutembea katika njia ya ibada ya kweli?

      13 Ikiwa kwa kweli tumeikimbia Babiloni Mkubwa, na pia tumetoka katika ulimwengu, acheni tusitazame kwenye mambo yaliyo nyuma. Kwa kupatana na kanuni ipatikanayo kwenye Luka 9:62, kwa yeyote wetu kutazama nyuma, kungemaanisha kushindwa kuwa raia wa Ufalme wa Mungu. Yesu alisema hivi: “Hakuna mtu ambaye ameweka mkono wake kwenye plau naye atazama kwenye mambo yaliyo nyuma aufaaye sana ufalme wa Mungu.”

      14 Lakini wengine waliopata kuwa Wakristo wakati uliopita, wamejiruhusu tangu wakati huo wafanyizwe kulingana na mtindo wa mfumo huu wa mambo. Wao hawajakinza roho ya ulimwengu. (2 Petro 2:20-22) Vikengeusha-fikira vya kilimwengu vimefyonza mapendezi na wakati wao, hivyo vikizuia maendeleo yao. Badala ya kufuliza kuweka akili na mioyo yao ikiwa dhabiti kwenye Ufalme wa Mungu na uadilifu wake, wakitanguliza mambo hayo maishani, wamegeuka kufuatia miradi ya kimwili. Isipokuwa wasukumwe kukubali hali ya imani yao dhaifu na yenye uvuguvugu, na kubadili mwendo wao kwa kutafuta ushauri wa kimungu, wamo hatarini mwa kupoteza uhusiano wao wenye thamani na Yehova na tengenezo lake.—Ufunuo 3:15-19.

      15. Ni nini huhitajika ili kubaki tukiwa tumekubalika na Mungu?

      15 Kupatikana kwetu tukiwa wenye kukubalika na katika hali ya kuja kuokoka dhiki kubwa inayokuja upesi, kwategemea kufuliza kwetu kuwa safi, tukiwa ‘tumefua kanzu zetu katika damu ya Mwana-Kondoo.’ (Ufunuo 7:9-14; 1 Wakorintho 6:11) Ikiwa hatutadumisha msimamo safi na wenye uadilifu mbele ya Mungu, utumishi wetu mtakatifu hautakubalika. Bila shaka, kila mmoja wetu apaswa ang’amue kwamba ubora wa imani iliyojaribiwa utatusaidia kuvumilia na kuepuka kutompendeza Mungu.

      16. Ni katika njia zipi uwongo waweza kuthibitika kuwa jaribu la imani?

      16 Nyakati nyingine, vyombo vya habari na mamlaka za kilimwengu hutoa taarifa zisizo za kweli na zenye kushushia watu wa Mungu hadhi, zikiwakilisha isivyo kweli itikadi na njia yetu ya Kikristo ya maisha. Hilo halipaswi kutushangaza, kwa maana Yesu aonyesha waziwazi kwamba ‘ulimwengu ungetuchukia.’ (Yohana 17:14) Je, tutawaruhusu wale waliopofushwa na Shetani watuogofye na kutuvunja moyo na kutufanya tuaibikie habari njema? Je, tutaruhusu uwongo juu ya kweli uathiri kuhudhuria kwetu mikutano kwa kawaida, na utendaji wetu wa kuhubiri? Au tutasimama thabiti na kuwa wenye ujasiri na wenye kuazimia hata zaidi, kuendelea kutangaza kweli juu ya Yehova na Ufalme wake?

      17. Ni uhakikisho gani uwezao kutuchochea tuendelee kuonyesha imani?

      17 Kulingana na unabii wa Biblia ambao umetimizwa, sasa tunaishi kabisa katika wakati wa mwisho. Matarajio yetu yenye kuitegemea Biblia ya kuwa na ulimwengu mpya wenye uadilifu, kwa hakika yatakuwa mambo halisi, yenye kupendeza. Mpaka siku hiyo itakapofika, sote na tudhihirishe imani isiyotikisika katika Neno la Mungu, na kuthibitisha imani yetu kwa kutoacha kuhubiri habari njema za Ufalme ulimwenguni pote. Fikiria maelfu ya wanafunzi wapya wanaobatizwa kila juma. Je, hiyo si sababu ya kutosha kwetu kufahamu kwamba subira ya Yehova katika kutekelezwa kwa hukumu yake yaweza kutokeza wokovu wa watu wengi zaidi? Je, hatuoni shangwe kwamba Mungu ameruhusu utendaji wa kuhubiri Ufalme ambao ni wenye kuokoa uhai uendelee? Na je, hatupendezwi kwamba mamilioni ya watu wamekubali kweli na wanadhihirisha imani yao?

      18. Azimio lako ni nini kuhusiana na kumtumikia Yehova?

      18 Hatujui kujaribiwa kwa sasa kwa imani yetu kutaendelea mpaka lini. Lakini jambo hili ni hakika: Yehova ameweka siku yake isiyoweza kubadilika ya kutoza hesabu mbingu na dunia ya sasa yenye uovu. Wakati uleule, acheni tuazimie kuiga sifa ya hali ya juu ya imani iliyodhihirishwa na Yesu, Mkamilishaji wa imani yetu. Na acheni tufuate kielelezo cha mabaki watiwa-mafuta na wengineo wanaotumikia kwa ujasiri miongoni mwetu.

      19. Ni nini ambacho waweza kuwa na uhakika kwamba kitashinda ulimwengu huu?

      19 Yatupasa tuazimie kutangaza habari njema idumuyo milele bila kuacha kwa kila taifa, kabila, lugha, na watu, kwa kushirikiana na malaika arukaye katikati ya mbingu. Acheni wasikie tangazo hili la malaika: “Hofuni Mungu na kumpa utukufu, kwa sababu saa ya hukumu yake imewasili.” (Ufunuo 14:6, 7) Hukumu hiyo ya kimungu itakapotekelezwa, matokeo yatakuwa nini kwa habari ya ubora uliojaribiwa wa imani yetu? Je, huo hautakuwa ushindi wenye utukufu—ukombozi kutoka katika mfumo wa mambo wa sasa, kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu? Kwa kuvumilia majaribu ya imani yetu, tutaweza kusema, kama vile mtume Yohana alivyosema: “Huu ndio ushindi ambao umeshinda ulimwengu, imani yetu.”—1 Yohana 5:4.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki