Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Tufuate Imani Bila Kufikiri?
    Mnara wa Mlinzi—2002 | Aprili 1
    • Je, Tufuate Imani Bila Kufikiri?

      Mkuu wa kitivo cha theolojia katika chuo fulani huko Marekani aliandika: “Kuna watu wengi wanaodai kuwa na imani katika dini, wanaojiunga na dini hasa ili waepuke kutumia nguvu zao za kufikiri.” Kisha aongezea kusema: “Wanataka tu kuamini kila jambo bila kutaka uthibitisho.”

      HILI ladokeza kwamba watu wengi wanaodai kwamba wanaamini mafundisho ya dini hawafikirii ni kwa nini wana imani hiyo au kama imani yao ina msingi mzuri. Si ajabu kwamba wengi hawapendi kuzungumza kuhusu dini.

      Inasikitisha kwamba, mazoea kama yale ya kutumia mifano ya kidini na sala zinazokaririwa hufanya watu wasifikiri kwa njia ifaayo. Mazoea hayo, pamoja na majengo yenye kuvutia, madirisha ya vioo yenye rangi mbalimbali, na miziki yenye kusisimua, ndiyo mambo tu yapatikanayo katika dini nyingi. Ijapokuwa makanisa mengi yanadai kwamba imani yao ina msingi wa Biblia, ujumbe wao unaosema ‘amini katika Yesu nawe utaokolewa’ hauwachochei watu kujifunza Biblia kwa bidii. Wengine huhubiri gospeli ya kijamii au ya kisiasa. Matokeo yamekuwa nini?

      Mwandishi fulani wa dini alisema hivi kuhusu hali za kule Amerika Kaskazini: “Ukristo unaelekea kuwa wa kijuu-juu tu, na waumini hawafunzwi vizuri ile imani.” Msimamizi mmoja wa kura ya maoni alieleza kuwa Marekani ni “taifa la watu wasio na elimu ya Biblia.” Kwa hakika, maoni hayo yahusu pia nchi nyinginezo zinazodai kuwa za Kikristo. Pia dini nyingi zisizo za Kikristo haziwasaidii watu kufikiri badala yake zinatilia mkazo kukariri nyimbo, sala za kidesturi, na kutafakari kwa namna mbalimbali kunakohusisha mafumbo badala ya kufikiri kwa njia ifaayo.

      Hata hivyo, watu haohao wasiojali usahihi au ukweli wa imani yao ya kidini, mara nyingi hufikiria mambo mengine kwa makini sana katika maisha yao ya kila siku. Je, si jambo la kusikitisha kwamba mtu anayefanya utafiti mwingi ili anunue tu gari ambalo hatimaye litaharibika na kutupwa aweza kusema hivi kuhusu dini, ‘Ikiwa iliwaridhisha wazazi wangu, itaniridhisha pia.’

      Ikiwa kwa kweli twataka kumpendeza Mungu, je, hatupaswi kufikiria kwa uzito usahihi wa yale tunayoamini kumhusu? Mtume Paulo alizungumza kuhusu watu fulani wa kidini wa siku zake ambao walikuwa na “bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” (Waroma 10:2) Watu kama hao waweza kufananishwa na mpaka-rangi anayeajiriwa apake nyumba rangi lakini anatumia rangi zisizofaa kwa sababu hakusikiliza maagizo ya mwajiri wake. Huenda mpaka-rangi akapendezwa na kazi yake, lakini je, itakubaliwa na mwenye nyumba?

      Ni nini kinachokubaliwa na Mungu kuhusiana na ibada ya kweli? Biblia yajibu: “Hili ni bora na lenye kukubalika machoni pa Mwokozi wetu, Mungu, ambaye mapenzi yake ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:3, 4) Huenda wengine wakahisi kwamba haiwezekani kupata ujuzi wa aina hiyo miongoni mwa dini nyingi za siku hizi. Lakini fikiria—ikiwa ni mapenzi ya Mungu kwamba watu waje kwenye ujuzi sahihi wa kweli, je, angeweza kuuficha isivyo haki kutoka kwao? Sivyo kwa kuwa Biblia, inasema: “Ukimtafuta [Mungu], ataonekana nawe.”—1 Mambo ya Nyakati 28:9.

      Mungu anawezaje kupatikana kwa wale wanaomtafuta kwa unyofu? Makala ifuatayo itajibu swali hilo.

  • Mtafute Mungu kwa Moyo na Akili
    Mnara wa Mlinzi—2002 | Aprili 1
    • Mtafute Mungu kwa Moyo na Akili

      Ukristo wa kweli huwatia watu moyo watumie akili na kuchochewa na mioyo yao ili kujenga imani inayompendeza Mungu.

      KWA hakika mwanzilishi wa Ukristo, Yesu Kristo, alifunza kwamba ni lazima tumpende Mungu kwa ‘akili yote,’ au uwezo wetu wa kufikiri, na pia kwa ‘moyo wote’ na ‘nafsi yote.’ (Mathayo 22:37) Naam, uwezo wetu wa kufikiri una sehemu muhimu katika ibada yetu.

      Mara nyingi Yesu alisema hivi alipowakaribisha wasikilizaji wake wafikirie mafundisho yake: “Nyinyi mwafikiri nini?” (Mathayo 17:25; 18:12; 21:28; 22:42) Katika njia hiyohiyo, mtume Petro aliwaandikia waamini wenzake ili ‘aamshe uwezo wao mwangavu wa kufikiri.’ (2 Petro 3:1) Mtume Paulo, mishonari wa mapema aliyesafiri sana, aliwasihi Wakristo wenzake watumie ‘nguvu zao za kufikiri’ na “kujithibitishia [wenyewe] mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na matakatifu.” (Waroma 12:1, 2) Kwa kuchunguza tu kwa makini mambo wanayoamini, Wakristo wanaweza kujenga imani inayompendeza Mungu na inayowawezesha kukabiliana na majaribu yanayotokea maishani.—Waebrania 11:1, 6.

      Ili kuwasaidia wengine wajenge imani kama hiyo, Wakristo waeneza-evanjeli wa mapema ‘walijadiliana nao kwa kutoa sababu kutokana na Maandiko, wakieleza na kuthibitisha kwa marejezo’ mambo waliyofundisha. (Matendo 17:1-3) Mtazamo wa aina hiyo unaopatana na kufikiri kuzuri ulikuwa na matokeo mazuri kwa watu wenye mioyo minyofu. Kwa mfano, watu katika jiji la Beroya la Makedonia“walipokea neno [la Mungu] kwa hamu ya akili iliyo kubwa zaidi sana, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku juu ya kama mambo hayo [waliyoelezwa na Paulo na wenzake] yalikuwa hivyo.” (Matendo 17:11) Inafaa tukumbuke mambo mawili hapa. Kwanza, Waberoya walikuwa na hamu ya kusikia Neno la Mungu; pili, hawakuamini tu bila kufikiri kwamba yale waliyosikia yalikuwa kweli bali walihakikisha mambo hayo kwa kutumia Maandiko. Kwa sababu hiyo mishonari Mkristo Luka aliwapongeza Waberoya kwa heshima na kuwaita “wenye uelekevu bora.” Je, unaonyesha uelekevu wa namna hiyo unaposhughulikia mambo ya kiroho?

      Akili na Moyo Hushirikiana

      Kama ilivyotangulia kutajwa, ibada ya kweli huhusisha akili na moyo. (Marko 12:30) Fikiria ule mfano wa yule mpaka-rangi katika makala iliyotangulia ambaye alipaka nyumba rangi akitumia rangi zisizofaa. Kama angesikiliza kwa makini maagizo aliyopewa na mwajiri wake, angefanya kazi hiyo kwa moyo wote akiwa na uhakika kwamba ingekubaliwa na mwenye nyumba. Ndivyo ilivyo na ibada yetu.

      Yesu alisema, ‘waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli.’ (Yohana 4:23) Kwa sababu hiyo mtume Paulo aliandika hivi: “Hiyo ndiyo sababu pia sisi . . . hatujaacha kusali kwa ajili yenu na kuomba ili nyinyi mpate kujazwa ujuzi sahihi wa mapenzi yake katika hekima yote na ufahamivu wa kiroho, kusudi mtembee kwa kumstahili Yehova kwa madhumuni ya kumpendeza yeye.” (Wakolosai 1:9, 10) ‘Ujuzi huo sahihi’ huwawezesha watu wanyofu kuabudu kwa moyo na nafsi yote wakiwa na uhakika kamili kwa sababu ‘wanaabudu kile wajuacho.’—Yohana 4:22.

      Kwa sababu hizo, Mashahidi wa Yehova hawabatizi vitoto au watu wanaoanza tu kujifunza ambao hawajajifunza Maandiko kwa makini. Yesu aliwaagiza wafuasi wake hivi: “Mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20) Ni baada tu ya kupata ujuzi sahihi wa mapenzi ya Mungu ndipo wanafunzi wanyofu wa Biblia wanaweza kuamua kuhusu jinsi ya kuabudu wakitegemea ujuzi huo. Je, unajitahidi kupata ujuzi huo sahihi?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki