-
Matatizo ya Pekee ya Familia za KamboAmkeni!—2012 | Aprili
-
-
Matatizo ya Pekee ya Familia za Kambo
● Mtaalamu wa masuala ya familia za kambo, Dakt. Patricia Papernow, anasema kwamba haingefaa kutatua matatizo ya familia za kambo kwa kutumia mashauri yaleyale yanayopewa familia za kawaida. Kufanya hivyo ni kama kujaribu kutafuta njia katika barabara ya jiji moja ukitumia ramani ya jiji lingine.
Ukweli ni kwamba zaidi ya kuwa na matatizo ya pekee, familia za kambo zina matatizo mengi kuliko yale ya familia za kawaida. Mwanasaikolojia William Merkel, anasema kuwa familia ya kambo ndio “uhusiano tata, usio wa asili na mgumu zaidi kati ya mahusiano yote ya wanadamu.”
Ikiwa hali ni ngumu hivyo, familia ya kambo inawezaje kufanikiwa? Mahusiano katika familia za kambo yanaweza kufananishwa na kitambaa kikubwa kilichoshonwa kwa kutumia vitambaa vidogo-vidogo tofauti. Vinapoanza kushonwa pamoja, huenda mshono huo ukawa dhaifu, lakini unapokamilika, unakuwa na nguvu—ikiwa vitambaa hivyo vilishonwa kwa uangalifu.
Acheni tuchunguze baadhi ya matatizo ya kawaida ambayo hukumba familia za kambo na hatua ambazo zimesaidia wengi kuunganisha maisha yao. Kisha tutasoma kuhusu familia nne za kambo ambazo zimefanikiwa.
TATIZO LA 1: MATARAJIO YASIYOTIMIZWA
“Nilitarajia kwamba nikiwapenda na kuwajali sana watoto wangu wa kambo, watanikubali, lakini hata baada ya miaka minane, bado ninasubiri.”—Gloria.a
FAMILIA nyingi za kambo huanza zikiwa na matarajio makubwa. Wazazi hutarajia kwamba wataepuka au kurekebisha makosa yaliyofanywa katika ndoa zao za kwanza na watapata upendo na usalama ambao ulikosekana katika ndoa hizo. Ingawa huenda matarajio mengine yasiwe halisi, bado yanaweza kumfanya mtu afadhaike yasipotimia. Biblia inasema: “Tarajio lililocheleweshwa linafanya moyo uwe mgonjwa.” (Methali 13:12) Ufanye nini ikiwa matarajio uliyokuwa nayo hayajatimizwa na yanafanya moyo wako uwe mgonjwa?
UNACHOWEZA KUFANYA
Usipuuze hisia zako ukidhani kwamba utaacha kukata tamaa. Badala yake, chunguza ni matarajio gani yasiyotimizwa yanayokufanya utamauke. Kisha chunguza ni kwa nini ulitarajia jambo hilo ili uelewe ni kwa nini unashikamana nalo. Mwishowe, jaribu kutafuta jambo linaloweza kutimizwa kwa sasa. Ona mifano ifuatayo:
1. Tangu mwanzo, nitawapenda watoto wangu wa kambo, nao watanipenda.
Kwa nini? Sikuzote nimetamani kuwa na familia changamfu yenye uhusiano wa karibu.
Tarajio halisi: Baada ya muda, upendo wetu unaweza kukua. Jambo muhimu kwa sasa ni kwamba tujihisi tukiwa salama na tuheshimiane katika familia.
2. Kila mtu katika familia mpya atazoea hali haraka.
Kwa nini? Tuko tayari kuanza maisha mapya.
Tarajio halisi: Familia za kambo huchukua kati ya miaka minne hadi saba kuimarika. Matatizo yetu ni ya kawaida.
3. Hatutazozana kuhusu pesa.
Kwa nini? Upendo utatusaidia tusibishanie mambo madogo.
Tarajio halisi: Masuala ya kifedha yanayohusiana na ndoa zetu za awali ni mazito. Huenda isiwe rahisi kushirikiana katika matumizi ya pesa.
TATIZO LA 2: KUELEWA HISIA ZA WENGINE
“Tulibadilikana haraka kulingana na hali—kila mtu katika familia mpya ya kambo alizoea hali mara moja.”—Yoshito.
“Ni baada ya miaka kumi tu ndipo nilipoamua kuunga mkono mambo katika familia yetu ya kambo na kuisaidia ifanikiwe.”—Tatsuki, mwana wa kambo wa Yoshito.
KAMA Yoshito na Tatsuki, huenda watu katika familia za kambo wasielewe kabisa maoni ya wengine katika familia yao. Kwa nini hilo ni muhimu? Matatizo yanapotokea, huenda ukataka kuyatatua haraka. Lakini ili ufanikiwe kuyatatua, lazima kwanza uwaelewe watu wa familia yako.
Ni muhimu kufikiria jinsi unavyozungumza, kwa kuwa maneno yanaweza kubomoa au kujenga. Kama Biblia inavyosema: “Kifo na uzima viko katika nguvu za ulimi.” (Methali 18:21) Unawezaje kuutumia ulimi wako ili kuwasaidia wote waweze kuelewana?
UNACHOWEZA KUFANYA
• Pendezwa na wengine na uwe na hisia-mwenzi badala ya kuhukumu. Kwa mfano:
Mwana wako akisema, “Ninamkosa baba yangu,” kubaliana naye. Badala ya kusema, “Lakini baba yako wa kambo anakupenda na kukujali kuliko baba yako mzazi,” unaweza kumwambia: “Lazima iwe unapitia hali ngumu. Hebu nieleze, ni nini hasa kinachokufanya umkose baba yako?”
Badala ya kumlaumu mwenzi wako mpya wa ndoa kwa kusema, “Ikiwa ungekuwa mzazi mzuri mwana wako angekuwa na adabu zaidi,” mweleze hisia zako. Unaweza kumwambia: “Tafadhali mkumbushe Luke awe akinisalimu anapokuja nyumbani. Hilo litanifanya nihisi vizuri.”
• Jaribuni kufahamiana zaidi wakati mnapokula, wakati wa tafrija, na wakati wa ibada.
• Muwe na mikutano ya familia kwa ukawaida, na kila mtu awepo. Mruhusu kila mtu katika familia aeleze maoni yake bila kumkatiza, akianza na mambo mazuri kuhusu familia mpya kisha aeleze mahangaiko yake. Mheshimiane hata mnapokosa kupatana, na uwaruhusu wote katika familia watoe mapendekezo ya jinsi mambo yanavyoweza kushughulikiwa.
TATIZO LA 3: KUMFANYA KILA MTU AHISI YEYE NI SEHEMU YA FAMILIA
“Mke wangu na watoto wake hujadiliana mambo kisiri kisha wananiletea malalamiko yao. Najihisi kuwa mgeni asiyetakikana.”—Walt.
HOFU ya kuwa mgeni katika familia yako mwenyewe inaweza kuwa chanzo cha matatizo mengine. Kwa mfano:
• Watoto ambao walikuwa na uhusiano mzuri na mtu kabla ya ndoa huwa na matatizo baadaye mtu huyo anapokuwa mzazi wa kambo.
• Mzazi wa kambo anamwonea wivu mtoto aliye na umri wa miaka sita.
• Ugomvi mkubwa unatokea kwa sababu ya mambo madogo-madogo ya nyumbani.
Tatizo hilo huwaathiri pia wazazi halisi wa watoto kwa kuwa wanahisi mkazo familia ya kambo inapokosa umoja. Carmen anasema, “Kujaribu kuwa mpatanishi kati ya mume wangu na watoto wangu wawili ni jambo gumu sana.”
Ile Kanuni Bora inaweza kusaidia kutatua tatizo hilo. Yesu alisema: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Familia za kambo zinawezaje kumfanya kila mtu ahisi yeye ni sehemu ya familia?
UNACHOWEZA KUFANYA
• Tanguliza ndoa yako. (Mwanzo 2:24) Tenga wakati wa kuwa pamoja na mwenzi wako mpya, na uhakikishe kwamba watoto wako wanajua wazi fungu lake katika familia. Kwa mfano, baba anaweza kuwaambia watoto wake hivi kabla hajaoa tena: “Ninampenda Anna, naye atakuwa mke wangu. Najua kwamba mtamtendea kwa njia inayofaa.”
• Tenga wakati wa kuwa pamoja na kila mmoja wa watoto wako. Kutenga wakati hususa kunaonyesha kwamba wao ni muhimu kwako na kutawahakikishia kwamba unawapenda.
• Tenga wakati wa kuwa pamoja na kila mtoto wa kambo ili ujenge uhusiano mzuri naye bila mzazi halisi kuwa mpatanishi.
• Waruhusu watoto wawe sehemu ya familia bila kuwatazamia wapuuze familia yao ya zamani. Usiwalazimishe watoto wa kambo wakuite “Baba” au “Mama.” Mwanzoni, huenda watoto wenye umri mkubwa wasijihisi huru kutumia maneno kama “familia” au “sisi” wanapozungumza kuhusu familia ya kambo.
• Mpe kila mtoto kazi za kufanya nyumbani, mahali pa kuketi kwenye meza ya kulia, na sehemu yake nyumbani. Hilo linatia ndani watoto ambao huja nyumbani mara kwa mara.
• Mnaweza kuhamia nyumba nyingine au mbadili mpangilio wa nyumba ya zamani ili washiriki wapya wasijihisi kuwa ni wageni.
TATIZO LA 4: KUWATIA WATOTO NIDHAMU
“Ninapowatia nidhamu watoto wa Carmen, yeye huwambembeleza badala ya kuniunga mkono.”—Pablo.
“Mimi huhisi uchungu sana Pablo anapowatendea watoto wangu kwa ukali.”—Carmen.
KWA nini suala la kuwalea watoto linaweza kusababisha mgogoro katika familia ya kambo? Huenda watoto hawakuwa wakitiwa nidhamu walipokuwa katika familia ya mzazi mmoja. Mzazi wa kambo anapojiunga na familia, huenda ikamchukua muda kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na watoto. Matokeo yatakuwa nini? Mzazi wa kambo anaweza kufikiri kwamba mzazi halisi anawaendekeza watoto wake, naye mzazi halisi anaweza kufikiri kwamba mzazi wa kambo ni mkali mno.
Biblia inapendekeza kuwe na usawaziko katika kuwalea watoto: “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova [Mungu].” (Waefeso 6:4) Jambo linalokaziwa hapa ni kuzoeza akili ya mtoto badala ya kudhibiti tabia yake. Lakini wazazi wanatiwa moyo wawe wenye fadhili na upendo ili nidhamu yao isiwakasirishe watoto.
UNACHOWEZA KUFANYA
• Weka sheria za nyumbani na uhakikishe kwamba zile ambazo tayari zipo zinafuatwa. Fikiria faida za kuwa na sheria hizo katika hali ifuatayo:
Mama wa kambo: Jennifer, sheria katika familia hii ni kwamba hupaswi kutuma ujumbe kupitia simu mpaka umalize kazi za shule.
Jennifer: Wewe si mama yangu.
Mama wa kambo: Ni kweli kwamba mimi si mama yako lakini kwa leo uko chini yangu, na sheria ni kwamba hupaswi kutuma ujumbe mpaka umalize kazi za shule.
• Usiweke sheria nyingi mno au kubadili ratiba haraka sana. Huenda ombi linaloonekana kuwa rahisi kwa mzazi wa kambo likawa mzigo kwa mtoto ambaye anahisi maisha yake yamebadilika ghafula. Bila shaka, huenda ikafaa kuweka sheria fulani mpya kama vile kuhusu faragha na mavazi, hasa ikiwa kuna watoto wenye umri mkubwa katika familia ya kambo.
• Ikiwa mna maoni yanayotofautiana kuhusu kuwatia watoto nidhamu, zungumzieni jambo hilo faraghani, si mbele ya watoto. Kazia fikira tabia hususa ya mtoto badala ya makosa fulani katika malezi yake ya awali.
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina katika mfululizo huu yamebadilishwa.
[Picha katika ukurasa wa 3]
Huenda kuwa na familia ya kambo iliyo na umoja ikaonekana kuwa ndoto
[Picha katika ukurasa wa 4]
Sikilizeni kwa makini ili kuelewa hisia na mahangaiko ya yule mwingine
[Picha katika ukurasa wa 6]
Ikiwa wazazi wana maoni yanayotofautiana, wanapaswa kuyazungumzia faraghani
-
-
Familia Za Kambo ZilizofanikiwaAmkeni!—2012 | Aprili
-
-
Familia Za Kambo Zilizofanikiwa
HATUISHI TU KATIKA NYUMBA MOJA
Binti ya Philip, Elise, mwenye umri wa miaka 20 aliyekuwa akiishi na baba yake alikuwa amejichukulia jukumu la kutunza nyumba yao. Baada ya Philip kumwoa Louise, je, mama huyo wa kambo na binti wa kambo wangekuwa na uhusiano mzuri?
Louise: Mwanzoni mambo yalikuwa magumu sana. Mimi hupenda kukaa nyumbani na kufanya kazi za nyumba na nilitaka kutimiza madaraka yangu nikiwa mke.
Elise: Louise alipanga upya kila kitu na kutupa baadhi ya vitu vyetu. Wakati mmoja, nilikuwa nikipanga nyumba na kwa makosa nikaweka vitu fulani mahali pasipofaa kwa kuwa mpangilio ulikuwa umebadilika. Jambo hilo lilimkasirisha Louise, na tukatupiana maneno makali, na sikuzungumza naye kwa juma moja.
Louise: Pindi moja nilimwambia Elise, “Sijui itakuwaje, lakini siwezi kuvumilia uhasama tulio nao.” Jioni hiyo alinijia na kuniomba msamaha. Nilimkumbatia na sote tukalia.
Elise: Louise aliacha baadhi ya picha zangu ukutani, na Baba hakuondoa taa nilizokuwa nimeweka sebuleni. Huenda jambo hilo likaonekana kuwa dogo, lakini hilo lilinisaidia kuhisi kwamba nyumba yetu haijabadilika kabisa. Ninathamini jinsi ambavyo Louise humtunza ndugu yangu mdogo anapokuja kututembelea. Miaka miwili imepita, na sasa nimeanza kumwona Louise kuwa sehemu ya familia yetu.
Louise: Ninahisi kwamba sisi si watu wanaoishi tu katika nyumba moja, mimi na Elise tumekuwa marafiki wa karibu.
‘UMOJA NI MUHIMU ZAIDI’
Anton na Marelize walikuwa na watoto watatu kila mmoja walipooana miaka sita iliyopita.
Anton: Sisi hufanya mambo tukiwa familia kama vile kwenda kuishi katika hema wakati wa likizo, nasi hutenga wakati wa kuwa pamoja na kila mtoto akiwa peke yake. Ilituchukua miaka kadhaa kuhisi kwamba sisi ni familia, lakini kufikia sasa tumetatua matatizo mengi ya familia.
Marelize: Ni muhimu kwetu kuwaona watoto wote kuwa “wetu” si “wako” au “wangu.” Nakumbuka siku moja nilikasirika kwa kuwa nilihisi Anton alimtia nidhamu mmoja wa wana wangu isivyofaa na akamruhusu binti yake aketi kwenye kiti cha mbele katika gari. Nilijifunza kwamba umoja wa familia ni muhimu zaidi kuliko mambo mengine kama vile, kuketi katika kiti cha mbele. Sisi hujaribu kuwatendea wote kwa usawa ingawa hatuwezi kumtendea kila mtu kwa njia ileile.
Pia mimi huepuka kuzungumzia pindi zenye furaha tulizokuwa nazo katika familia yetu ya zamani kwa kuwa wale ambao hawakuwepo wakati huo watahisi kwamba tunaipenda zaidi familia ya zamani. Badala yake, mimi hushukuru kwa familia yetu ya sasa.
‘TOA PONGEZI KWANZA’
Francis na Cecelia walifunga ndoa miaka minne iliyopita. Familia yao inatia ndani watoto watatu wa Cecelia ambao ni watu wazima na kijana wa Francis.
Francis: Mimi hujaribu kuwa mwenye kufikika nami huepuka kukasirika upesi. Sisi hula milo pamoja kwa ukawaida, nasi hutumia fursa hiyo kuzungumza tukiwa familia. Pia, mimi huwatia moyo watoto wote washiriki kufanya kazi za nyumbani, kwa kuwa hilo linafaidi familia nzima.
Cecelia: Mimi hutenga wakati wa kuwa na kila mtoto na kusikiliza mahangaiko yao na mambo yanayowakasirisha. Tunapokuwa na mkutano wa familia, sisi hujaribu kutoa pongezi kwanza na kisha kuwatia moyo warekebishe mambo fulani. Na ninapokosea, mimi hukubali kosa langu na kuomba msamaha kutoka moyoni.
NILILELEWA NA WAZAZI WAWILI WA KAMBO
Yuki, mwenye umri wa miaka 20, hajamwona baba yake tangu alipokuwa na umri wa miaka mitano. Baadaye, mama yake aliolewa tena na Tomonori. Lakini Yuki alipokuwa na umri wa miaka kumi, mama yake alikufa. Miaka mitano baadaye, Yuki alijipata akiishi na wazazi wawili wa kambo, wakati ambapo Tomonori alimwoa Mihoko.
Yuki: Baba yangu wa kambo alipoamua kuoa tena, nilijiambia, “Singependa kuwa na mama wa kambo. Tayari kumekuwa na mabadiliko mengi maishani mwangu.” Hali hiyo haikunifurahisha hata kidogo, nami nilimtendea mama wa kambo kwa ubaridi.
Mihoko: Hata ingawa mume wangu hakunishinikiza nimpende mwana wake wa kambo kama alivyompenda, niliazimia kujaribu kuwa na uhusiano mzuri na Yuki. Tulijitahidi sana kufanya mambo aliyozoea kama vile kushiriki katika utendaji wa kiroho, tafrija, na kula mlo wa jioni pamoja halafu kuwa na mazungumzo baadaye. Nilielewa hisia zake vizuri zaidi tulipozungumza kuhusu kifo cha mama yake.
Nilipopata mimba, tulikuwa na wasiwasi kuhusu Yuki na tulitaka ahisi kwamba bado yeye ni sehemu ya familia yetu. Tulimruhusu Yuki amlishe na kumwosha mtoto na pia kumbadili nepi, na tulimpongeza mbele ya watu kwa msaada wake. Mtoto huyo anayeitwa Itsuki anampenda sana Yuki. Hata kabla ya kujifunza maneno “baba” na “mama,” alijifunza kusema niinii, yaani, kaka.
Yuki: Ukiwa mtoto wa kambo, ni kawaida kujihisi mpweke na kuwa wewe si sehemu ya familia. Unapojaribu kuwaeleza wengine hisia zako, hawaelewi. Hata hivyo, ninafurahi kusema kwamba Wakristo wenzangu wamenitegemeza kikweli. Wasiwasi niliokuwa nao kumwelekea mama yangu wa kambo umekwisha. Yeye hunipa mashauri mazuri, na ninaweza kumwambia yaliyo moyoni.
[Blabu katika ukurasa wa 9]
Uwe na subira! Familia za kambo zinaweza kufanikiwa na kuwa na furaha
-