-
Unaweza Kufanikiwa!Amkeni!—2012 | Novemba
-
-
Unaweza Kufanikiwa!
“Mimi hufurahi sana binti zangu wawili wanaponikumbatia bila mimi kutazamia na kuniambia, ‘Tunakupenda, Mama.’”—ANNA, MAMA ASIYE NA MWENZI, POLAND.
“Mara nyingi mimi hufurahi ninapoona watoto wangu wakinishukuru kwa mambo ninayowafanyia. Nyakati nyingine wao hunipa zawadi ndogo, kama vile picha waliyochora. Wanapofanya hivyo mimi huhisi kana kwamba jitihada zangu zote zimethaminiwa.”—MASSIMO, BABA ASIYE NA MWENZI, ITALIA.
“Nyakati nyingine ninapohisi nimeshuka moyo, mmoja wa wana wangu hunikumbatia, na kunibusu, kisha ananiambia kwamba ananipenda sana.”—YASMIN, MAMA ASIYE NA MWENZI, AFRIKA KUSINI.
HAYO ni baadhi ya mambo ambayo wazazi wengi wasio na wenzi walimwambia mwandishi wa Amkeni! katika uchunguzi uliofanywa sehemu mbalimbali ulimwenguni. Wazazi wengi wasio na wenzi, hasa akina mama, walisema kwamba walitamani kuwa na mwenzi mwenye upendo ambaye angewasaidia.a Hata hivyo, maelezo yao yaliyotolewa kwa unyoofu yanaonyesha pia kwamba wamefaulu kubadilikana kulingana na hali yao.
Ni nini ambacho kimewasaidia wazazi hao wasio na wenzi wabadilikane kulingana na hali na wafaulu kutimiza jukumu lao gumu? Katika makala zifuatazo, tutachunguza baadhi ya mapendekezo yao na maelezo yao ya unyoofu, na pia tutachunguza kanuni muhimu ambazo zimewasaidia. Ikiwa wewe ni mzazi asiye na mwenzi, tunatumaini kwamba makala hizi zitakusaidia ufanikiwe kutimiza jukumu lako gumu kwa shangwe na pia kwa njia inayoridhisha. Kwa kweli, hilo linaweza kuwa jambo gumu katika ulimwengu wa leo ulio na msukosuko na unaobadilika haraka.b
Makala hizi zitakazia fikira maeneo sita. Jinsi ambavyo wazazi wasio na wenzi wanaweza
Kutafuta msaada kutoka kwa watu wengine
Kuwasiliana kwa njia inayofaa zaidi na watoto wao
Kutanguliza mambo yanayofaa
Kuweka mipaka iliyo wazi kuhusu mwenendo
Kufundisha maadili yanayofaa
Kuhakikisha kwamba Mungu ni sehemu ya familia yao
-
-
2 Jifunze Kuwasiliana VizuriAmkeni!—2012 | Novemba
-
-
2 Jifunze Kuwasiliana Vizuri
Jaribu kuwa tayari kumsikiliza mtoto wako anapokuwa tayari kuzungumza
“Nimejifunza kusikiliza kwa makini sana. Haidhuru nimechoka kiasi gani.”—MIRANDA, AFRIKA KUSINI.
Tatizo.
“Tatizo langu,” anasema Cristina, “si tu kupata wakati wa kuwa pamoja na binti yangu, bali pia ni kujihusisha kabisa kiakili na kihisia licha ya uchovu na majukumu yangu mengi.”
Mapendekezo.
Fanya iwe rahisi kwa watoto kuzungumza nawe kwa uhuru. “Mimi hujaribu kuwawekea watoto wangu mfano mzuri,” anasema Elizabeth, mama ya watoto watano, “na watoto wangu hujihisi huru kuzungumza nami. Mimi pia huwatia moyo wazungumze pamoja na pia wasiende kulala wakiwa wamekasirikiana. Isitoshe, wanajua kwamba siwezi kuvumilia tabia ya kunyamaziana.”
Usiwapuuze watoto wako wanapoongea. “Mwana wangu alipokuwa mchanga,” anaandika Lyanne, “alikuwa akizungumza kama kasuku na nilimpuuza mara nyingi. Kisha alipokuwa tineja, aliacha kuzungumza, nami nikatambua kwamba nilikuwa nimefanya kosa kubwa kumpuuza awali. Nilifanya kazi ngumu, ngumu sana, ya kumlazimisha azungumze nami. Nilizungumza na mzee fulani katika kutaniko letu kuhusu jambo hilo. Alinishauri nitulie na nizungumze na mwana wangu pole kwa pole. Nilifuata shauri lake, na pole kwa pole mambo yakaanza kubadilika.”
Uwe na subira. Andiko la Mhubiri 3:7 linasema kuna “wakati wa kukaa kimya na wakati wa kusema.” Dulce, mama ya watoto watatu anasema, “Wakati watoto wangu walipokataa kuzungumza, niliwaambia kwamba niko tayari kuwasikiliza watakapokuwa tayari kuzungumza.” Badala ya kuwalazimisha watoto wazungumze, kwa subira, waache wajihisi huru kufanya hivyo. Hivyo ndivyo Biblia inavyopendekeza. “Fikra za mtu zimefichika kama kilindi cha maji; lakini mtu mwenye busara ajua kuzichota humo.”—Methali 20:5, Biblia Habari Njema.
Uwe “mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.” (Yakobo 1:19) Lizaan, aliyenukuliwa katika makala iliyotangulia, anasema hivi: “Nilijifunza kudhibiti ulimi wangu watoto waliponieleza matatizo yao. Pia ilinibidi nijizuie kutoa mashauri haraka-haraka bali nizungumze kwa utulivu niliposhughulikia mambo yanayowasumbua.” Leasa, mama ya wavulana wawili, anaandika hivi: “Haijawa rahisi kwangu kuwa msikilizaji mzuri. Nyakati nyingine hata niliyaona matatizo ya wana wangu kuwa ya kipuuzi, kwa hiyo ilinibidi nijifunze kuonyesha fadhili zaidi.”
“Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote.” (Wakolosai 4:6) “Ili nisizuie mazungumzo,” anasema Lyanne, “nimejitahidi sana kuwa mtulivu hata wakati ambapo mambo mazito yanatokea.”
Ikiwa hutajitahidi kuwa mtulivu, huenda ukapandwa na hasira na kufoka, na hilo litafanya mambo yawe mabaya hata zaidi! (Waefeso 4:31) Kwa mfano, kumfokea mtoto kunaweza kukatiza mawasiliano na kutokeza matatizo zaidi.
Wajue watoto wako. “Wana wangu wawili wanatofautiana kabisa,” anasema Yasmin, aliyenukuliwa hapo awali. “Mmoja ni mzungumzaji; na yule mwingine ni mnyamavu. Ninaposhughulika na yule mnyamavu, nimejifunza kwamba ni afadhali nisimwulize jambo moja kwa moja. Badala yake, mimi huzungumza naye tunapokuwa tukifanya jambo fulani pamoja kama vile kucheza mchezo fulani, au anapozungumza kuhusu jambo linalompendeza. Tunapofanya mambo pamoja, kwa busara mimi humwuliza maoni yake kuhusu jambo fulani.”
Namna gani ikiwa mvulana hajihisi huru kuzungumza na mama yake kuhusu mambo fulani ya kibinafsi, kama vile alivyohisi mwana anayebalehe wa Misao? Kijana huyo alisema, “Wewe hunielewi hata kidogo.” Mama huyo alitafuta msaada kutoka kwa mwanamume mkomavu, anayetegemeka katika kutaniko lake. Misao anasema hivi: “Mwanamume huyo amekuwa mshauri wa mwana wangu, na sasa mwana wangu ana moyo mtulivu.”
Usisahau kwamba wewe ni mzazi, si rafiki tu. “Nilimfanya binti yangu tineja kuwa msiri wangu,” anasema Iwona, mama ya watoto wawili. “Ingawa nilijua si sawa kufanya hivyo, nilifanya kosa hilo na ilibidi nirekebishe hali hiyo.” Ingawa unataka kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na mtoto wako, kumbuka kwamba wewe ukiwa mzazi, wewe ndiye uliye na mamlaka. Unapodumisha hadhi yako na kuonyesha ukomavu na uimara, unafanya iwe rahisi kwa watoto wako kukuheshimu na kutii amri hii ya Biblia: “Enyi watoto, watiini wazazi wenu.”—Waefeso 6:1, 2.
‘Wapende watoto wako.’ (Tito 2:4) Watoto wanahitaji upendo kama vile tu wanavyohitaji chakula na kinywaji! Kwa hiyo, kila mara, kwa maneno na matendo, wahakikishie kwamba unawapenda! Ukifanya hivyo, watajihisi wakiwa salama na pia watakuwa tayari kuzungumza nawe na kukutii.
-
-
3 Tanguliza Mambo YanayofaaAmkeni!—2012 | Novemba
-
-
3 Tanguliza Mambo Yanayofaa
Mle angalau mlo mmoja pamoja kila siku
“Kila wakati nilijihisi mchovu—nilijaribu kusawazisha mambo kama vile kazi ya kuajiriwa, kuwalea watoto, ratiba ya ibada, kazi za nyumbani, na kupumzika.”—YOKO, JAPANI.
Tatizo.
Miranda, mama ya wavulana wawili anasema: “Tatizo langu kuu ni kuwa mama anayefanya kazi ya kuajiriwa ambaye anapaswa kuiandalia familia mahitaji yake yote—ya kimwili, kiakili, kihisia, na kiroho—bila msaada wa mwenzi wa ndoa.”
Mapendekezo.
Amua ni mambo gani yaliyo muhimu kwako na kwa watoto wako, kisha tanguliza mambo hayo.
Zingatia mambo hayo na ujifunze kutumia wakati na pesa vizuri. Kwa mfano: Afya ya watoto wako ni muhimu, kwa hiyo tumia pesa ulizochuma kwa jasho kununua vyakula vyenye lishe. Ni afadhali kufanya hivyo kuliko kutumia pesa zako kulipia gharama za hospitali. Kabla ya kufanya ununuzi, andika orodha ya vitu unavyohitaji. Hilo litakuzuia kununua vitu ambavyo huhitaji au huwezi kugharamia. Roberto, baba anayeishi Marekani pamoja na watoto wake wanne anasema, “Mimi hupenda kupika.” Kisha anaongezea hivi, “Nilijifunza kukazia fikira mahitaji yetu badala ya vitu tulivyotaka, na si mahitaji yetu kwa ujumla tu, bali mambo tuliyohitaji siku hiyo.”
Tumia pesa ulizochuma kwa jasho kununua vyakula vyenye lishe. Ni afadhali kufanya hivyo kuliko kutumia pesa zako kulipia gharama za hospitali
Ondoa nyumbani kwako vitu kama vile vitabu, nguo, na vifaa ambavyo hutumii. Mama mmoja asiye na mwenzi alisema hivi: “Kuwa na vitu vingi huleta mkazo. Kadiri ulivyo na vitu vingi ndivyo unavyokuwa na vitu vingi vya kusafisha, kurekebisha, na kudumisha. Siri ya kurahisisha maisha yako ni kuwa na vitu vichache.”
Wazoeze watoto wako kuacha kila kitu kikiwa nadhifu kabla ya kulala. Usiache nyumba yako iwe shaghalabaghala. Mazoezi hayo yanawafundisha watoto wako kutunza vyumba vyao na pia nyumba yenu. Bila shaka, mfano wako mzuri utafanya iwe rahisi kwa watoto kutii.
Ingawa huenda ukawa na shughuli nyingi, lazima utenge wakati wa kuwa pamoja na watoto wako, na si tu vipindi vifupi-vifupi vya wakati, bali wakati mwingi iwezekanavyo. Watoto wako wanahitaji uwape wakati na uwakazie fikira.—Kumbukumbu la Torati 6:7.
Mle angalau mlo moja pamoja kila siku, na mfanye pindi hiyo iwe yenye kufurahisha. Colette, mama ya watoto watatu anasema hivi: “Kwa kuwa kila mtu huwa nyumbani wakati wa chakula cha jioni, tuliamua kwamba tutatumia pindi hiyo kujengana kihisia na kiroho. Mlo huo umekuwa wa pekee kwa familia yetu hadi leo.”
-
-
4 Weka Mipaka Iliyo WaziAmkeni!—2012 | Novemba
-
-
4 Weka Mipaka Iliyo Wazi
Uwe thabiti, na usiwe kigeugeu
“Kulea watoto ukiwa peke yako si jambo rahisi—hasa wanapofikia umri wa kubalehe na kutaka kuasi wazazi wao kama vijana wengine wengi.”—DULCE, AFRIKA KUSINI.
Tatizo.
Biblia ilitabiri kwamba “katika siku za mwisho,” watoto kwa ujumla wangekuwa “wasiotii wazazi.”—2 Timotheo 3:1, 2.
Mapendekezo.
Tambua kwamba “ili wakue vizuri, watoto wanahitaji kujua sheria na matarajio ya wazazi.” (The Single Parent Resource, cha Brook Noel) Barry G. Ginsberg ambaye ni mwanasaikolojia wa watoto na familia anasema hivi: “Mahusiano huwa mazuri na yasiyo na mkazo kunapokuwa na mipaka iliyo wazi.” Aliongezea hivi: “Mipaka hiyo inapokuwa ya wazi na inapoeleweka vizuri, inakuwa rahisi kufanya familia iwe na furaha.” Unaweza kuwekaje mipaka iliyo wazi?
Uwe thabiti. Uchunguzi mmoja uliofanywa nchini Australia ulionyesha kwamba watoto huwa watundu wazazi wao wanaposhindwa kuwakataza jambo fulani na wanapowaruhusu wafanye watakavyo. Kama Biblia inavyosema: “Mvulana [au msichana] aliyeachiliwa atamletea mama yake aibu.”—Methali 29:15.
Usiache hisia za hatia kuhusu hali yako ukiwa mzazi mmoja zikufanye uwaendekeze watoto wako. Yasmin, aliyenukuliwa hapo awali anasema: “Nyakati nyingine, mimi huanza kuwahurumia wana wangu wawili kwa sababu wanalelewa na mzazi mmoja.” Lakini kama tutakavyoona, hakuruhusu hisia hizo, ambazo hazikuwa na ubaya wowote, zimfanye abatilishe uamuzi wake.
Usibadili-badili sheria, na usiwe kigeugeu. (Mathayo 5:37) “Watoto wanapojua kwamba bila shaka watatiwa nidhamu kwa sababu ya tabia fulani isiyofaa, hilo litawazuia wasiwe na matatizo ya kihisia na tabia zisizofaa,” linasema jarida American Journal of Orthopsychiatry. Yasmin anasema: “Niliketi pamoja na wavulana wangu na tukazungumza kuhusu nidhamu. Wakifanya makosa, ninajaribu kutoa nidhamu bila kubadilika-badilika. Hata hivyo, nimejifunza kwanza kuwasikiliza na kisha kuwaeleza kwa utulivu jinsi ambavyo jambo walilofanya limeathiri familia yetu. Baada ya kufanya hivyo, mimi hutoa nidhamu kama nilivyosema.”
Uwe na usawaziko; usitoe nidhamu ukiwa na hasira. Ingawa unahitaji kuwa thabiti kwa lililo sawa, unahitaji pia kubadilikana kulingana na hali inapohitajika. “Hekima inayotoka juu”—yaani, kutoka kwa Mungu—ni “yenye usawaziko,” linasema andiko la Yakobo 3:17. Watu wenye usawaziko hawafanyi mambo bila kufikiri au kwa hasira. Wala hawashikilii sheria kupita kiasi. Badala yake, wao hufikiri kwanza, huenda hata wakasali kuhusu jambo hilo, kisha wanaweza kutenda kwa utulivu na kwa njia inayofaa.
Kutobadili-badili sheria, kuwa thabiti, na kuwa na usawaziko, pamoja na kuweka mfano mzuri, kutakusaidia kuweka mipaka ambayo itafanya nyumba yako iwe kimbilio la kweli kwa ajili ya watoto wako.
-
-
5 Wafundishe Viwango Bora vya MaadiliAmkeni!—2012 | Novemba
-
-
5 Wafundishe Viwango Bora vya Maadili
Wazazi wenye hekima huwafundisha watoto wao viwango bora vya maadili vinavyopatikana katika Biblia
“Mapema maishani, sikuishi kulingana na viwango vya Biblia na ilikuwa vigumu kwangu kuwafundisha watoto wangu. Lakini sasa ni rahisi kufanya hivyo kwa sababu nina msaada wa Biblia.”—ELIZABETH, AFRIKA KUSINI.
Tatizo.
Kushinikizwa na marafiki shuleni na kuzorota kwa maadili ulimwenguni pote kunaathiri sana familia. Watoto wanahitaji viwango bora vya maadili ili kupinga uvutano huo mbaya. La sivyo, huenda hawatakuwa watu wazima wenye kutegemeka, wenye maadili yanayofaa, na wenye adabu.
Mapendekezo.
Wazazi wengi wasio na wenzi, kutia ndani wale walionukuliwa katika mfululizo huu, hutafuta mwongozo kutoka katika Biblia, kwa kuwa wanatambua kwamba ina hekima isiyo na kifani kutoka kwa Mungu. Kwa mfano, chunguza yale ambayo Biblia inasema kuhusu kanuni muhimu zaidi kuliko zote—kuonyesha upendo wa kweli.
“Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. Haushangilii juu ya ukosefu wa uadilifu, bali hushangilia pamoja na kweli. Huhimili mambo yote, . . . hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.”—1 Wakorintho 13:4-8.
Wazazi wanapoonyesha upendo wa aina hiyo, watoto wao hufaulu kutokeza sifa nzuri. Colette, aliyetajwa awali, anayeishi Ufaransa, aliandika hivi: “Mara nyingi niliwaambia watoto wangu kwamba ninawapenda. Pia niliwaambia kwamba wao ni zawadi kutoka kwa Mungu na kwa sababu hiyo walihitaji kutunzwa vizuri. Kwa upande wao, walipaswa kuwa wenye adabu na kuniheshimu mimi na baba yao [ambaye hakuwa na haki kisheria ya kuwalea]. Kanuni hizo zimefanya tuaminiane na kuheshimiana.”—Zaburi 127:3.
Anna, anayeishi nchini Poland, aliandika hivi: “Watoto wangu wanapogombana, mimi huwakumbusha maneno ya Yesu kwamba mambo tunayotaka watu watutendee, tunapaswa kuwatendea vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Roberto, aliyetajwa hapo awali, anakabiliana na tatizo ambalo huwakumba wazazi wengi wasio na mwenzi. Anasema: “Watoto wanakabili viwango vya aina mbili—vyako na vya yule mzazi mwingine. Ninaposisitiza kwamba lazima watii viwango vya Biblia, ninajua kwamba wakati huo wanamwona yule mzazi mwingine kuwa mzuri kuliko mimi.” Zaidi ya hayo, anasema: “Huenda yule mzazi mwingine akawapa watoto zawadi ili wampende. Ni vigumu kukabiliana na hali kama hiyo, lakini kuwasiliana kwa njia nzuri na watoto kunasaidia.”
Si rahisi sikuzote kuishi kupatana na viwango vya Biblia, lakini unapofanikiwa unafurahia jitihada zako! Sarah, mzazi asiye na mwenzi anayeishi Afrika Kusini anasema: “Ninafurahi kwamba watoto wangu wamelelewa kwa mwongozo wa Yehova. Ni kweli kwamba tumekuwa na matatizo, lakini sikuzote Mungu ametusaidia.”
-
-
6 Mwombe Mungu MsaadaAmkeni!—2012 | Novemba
-
-
6 Mwombe Mungu Msaada
Je, unamwomba Mungu akusaidie kulea watoto wako?
“Mume wangu aliponiacha mimi na watoto, nilimsihi Mungu atusaidie. Alijibu sala yangu. Hatujawahi kukosa mahitaji yetu. Ametusaidia na kutuongoza.”—MAKI, JAPANI
KATIKA ulimwengu wa leo unaopenda vitu vya kimwili, watu kwa ujumla hawamfikirii Mungu. Hata hivyo, Muumba wetu anapendezwa na sisi na anataka tufanikiwe maishani. Andiko la Isaya 41:10 linaeleza vizuri hisia zake: “Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. . . . Nitakusaidia kwelikweli.”
Katika makala iliyotangulia, tulizungumzia jinsi Mungu anavyotusaidia kupitia viwango bora vya maadili vinavyopatikana katika Biblia. (2 Timotheo 3:16) Lakini Biblia si kitabu kinachotoa tu mwongozo. Kinatufunulia pia sifa zenye kupendeza za Mungu na kutuonyesha kwamba anatupenda. Kwa hiyo, wazazi wengi Wakristo—iwe wana wenzi au hawana—wametambua kwamba tunapofuata mafundisho ya Biblia, tunaona wema wa Mungu.
Robert, Austria: “Yehova Mungu ndiye baba au mama bora kuliko yeyote kati yetu. Anajua mahitaji ya watoto wetu, na anajua jinsi ya kuwalinda. Kwa hiyo, mimi husali kwake mara nyingi nikiwa na binti yangu.”
Ayusa, Japani: “Mimi hufurahi sana ninapomwona mwana wangu akiwa na uhakika kwamba Yehova atatutegemeza anaposema, ‘Yehova yuko pamoja nasi, kwa hiyo kila kitu kitakuwa shwari.’”
Cristina, Italia: “Ninapoona kwamba siwezi kutatua tatizo fulani, mimi husali kwa Yehova, na kuliacha mikononi mwake. Mara moja mimi huwa na amani ya akili kwa kuwa ninajua kwamba tatizo hilo litatatuliwa kwa njia inayofaa kabisa.”
Laurentine, Ufaransa: “Ninaweza kuthibitisha kwamba Yehova amenibariki nikiwa mzazi asiye na mwenzi. Kwa kweli yeye huwaokoa wanaoteseka na wasio na baba au mama.”
Keiko, Japani: “Mungu hana ubaguzi. Anataka kutunza familia zote kwa upendo, iwe zina wazazi wawili au mzazi mmoja.”—Matendo 10:34.
Akionyesha kwamba Mungu anatuonyesha huruma na kutuhangaikia, Yesu Kristo alisema: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi . . . , kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.” (Mathayo 11:28-30) Kwa kweli, Yesu pamoja ya Baba yake wa mbinguni, Yehova Mungu, wanataka tuhisi tukiwa salama chini ya utunzaji wao wenye upendo. Tunasoma hivi kwenye Zaburi 34:8: “Onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema.” Ndiyo, Mungu anataka ujionee mwenyewe kwamba mashauri yake hufanya kazi, kwamba anataka ufanikiwe maishani. Je, utakubali mwaliko wake?
-