-
Familia Zisizo na Baba Ni Tatizo LinaloongezekaAmkeni!—2004 | Agosti 22
-
-
Familia Zisizo na Baba Ni Tatizo Linaloongezeka
AKINA baba wengi wanaziacha familia zao. Katika miaka ya mwisho-mwisho ya 1990, gazeti USA Today lilisema kwamba Marekani ndiyo “nchi iliyo na idadi kubwa zaidi ya familia zisizo na baba.” Hata hivyo, familia zisizo na baba ni tatizo la ulimwenguni pote.
Ripoti ya idadi ya watu ya mwaka wa 2000 huko Brazili ilionyesha kwamba familia milioni 11.2 kati ya familia milioni 44.7, zinaongozwa na wanawake. Nchini Nikaragua, asilimia 25 ya watoto huishi na mama zao tu. Katika miaka ya 1990 huko Kosta Rika, idadi ya watoto wasiotambuliwa kisheria na baba zao iliongezeka kutoka asilimia 21.1 hadi asilimia 30.4.
Idadi hizo kutoka nchi tatu ni mfano tu wa hali ulimwenguni. Fikiria sehemu nyingine ya tatizo la familia zisizo na baba.
Akina Baba Wasiotimiza Madaraka Yao
Tafadhali ona sanduku “Baba, Utarudi Lini?” Nao, ambaye sasa ana umri wa miaka 23, anakubali hivi: “Nilimwona Baba mara chache sana kabla ya kuingia shule ya msingi. Siku moja alipokuwa akiondoka nyumbani, nilimsihi hivi, ‘Tafadhali usikose kurudi.’”
Mahusiano ya familia kama yale ya Nao na baba yake ndiyo yaliyomchochea Piotr Szczukiewicz, mwandishi kutoka Poland, kusema hivi: “Yaelekea baba ndiye mtu muhimu anayekosekana katika familia.” Ni kweli kwamba baba wengi huishi na familia zao na kuzitegemeza kiuchumi. Hata hivyo, kama vile gazeti Capital la Ufaransa lilivyoeleza, “baba wengi huridhika tu na kuandalia familia zao chakula huku wakipuuza kuwafundisha watoto wao.”
Mara nyingi kuna baba katika familia, lakini hajihusishi na maisha ya watoto wake. Anahangaikia mambo mengine. Jarida Famille chrétienne la Ufaransa linasema hivi: “[Baba] anaweza kuwepo kihalisi, lakini huenda asiwepo kiakili.” Kwa nini leo baba wengi wamejitenga na familia zao kiakili na kihisia?
Kulingana na jarida hilo, sababu kuu ni kwamba “yeye hukosa kuelewa daraka lake akiwa baba au mume.” Kulingana na maoni ya baba wengi, daraka la baba mzuri ni kuleta mshahara mnono. Kama alivyosema mwandishi Józef Augustyn, kutoka Poland, “baba wengi hufikiri wao ni wazazi bora kwa sababu wanachuma pesa kwa ajili ya familia.” Lakini hilo ni mojawapo tu ya madaraka ya baba.
Ukweli ni kwamba watoto hawawathamini baba zao kulingana na kiasi cha pesa wanazochuma au thamani ya zawadi wanazowapatia. Badala yake, watoto hutaka hasa upendo, wakati, na uangalifu kutoka kwa baba wala si zawadi. Hayo ndiyo mambo muhimu kwao.
Baba Wanahitaji Kujichunguza
Kulingana na ripoti ya Baraza Kuu la Elimu la Japani, “akina baba wanapaswa kuchunguza maisha yao kwa sababu wanatumia wakati mwingi kazini.” Swali ni, Je, baba yuko tayari kufanya marekebisho kwa faida ya watoto wake? Gazeti la Ujerumani Gießener Allgemeine, liliripoti uchunguzi fulani ulioonyesha kwamba baba wengi walikataa kuwatanguliza watoto wao badala ya kazi yao.
Watoto wanaweza kuumia sana kihisia wanapoona kwamba baba hawajali. Lidia, ambaye sasa ana umri wa miaka 21, anakumbuka vizuri jinsi baba yake alivyokuwa akifanya alipokuwa msichana mdogo huko Poland. Anasema: “Hakuzungumza nasi hata kidogo. Maisha yetu yalitofautiana kabisa. Hakujua kwamba nilikuwa nikienda disko.” Vilevile Macarena, msichana mwenye umri wa miaka 21 huko Hispania, anasema kwamba alipokuwa mtoto, baba yake “alizoea kwenda kujifurahisha na marafiki zake mwishoni mwa juma, na mara kwa mara hakurudi nyumbani kwa siku kadhaa.”
Kutanguliza Mambo Yanayofaa
Huenda baba wengi wakatambua kwamba hawatumii wakati wa kutosha pamoja na watoto wao. Baba ya kijana mmoja huko Japani alisema: “Ninatumaini kwamba mtoto wangu ataelewa hali yangu. Nyakati zote mimi humfikiria, hata ninapokuwa na shughuli nyingi.” Lakini je, tatizo hilo litasuluhishwa kwa kufikiri tu kwamba mtoto ataelewa kwa nini baba yake hapatikani?
Bila shaka, jitihada nyingi na kujinyima kunahitajiwa ili kutosheleza mahitaji ya mtoto. Ni kweli kwamba si rahisi kuwapa watoto kile wanachohitaji hasa, yaani upendo, wakati, na uangalifu. Yesu Kristo alisema: “Mwanadamu ataishi, si kwa mkate [au, chakula cha kimwili] tu.” (Mathayo 4:4) Pia, ni kweli kwamba watoto hawawezi kufanikiwa maishani kwa sababu tu ya vitu vya kimwili. Je, akina baba, mko tayari kudhabihu kitu chenye thamani zaidi kwenu, yaani, wakati au mafanikio yenu kazini ili kuwa pamoja na watoto wenu?
Gazeti Mainichi Daily News la Februari 10, 1986, lilieleza kuhusu baba mmoja aliyetambua kwamba watoto wake ni wenye thamani sana. Liliripoti hivi: ‘Ofisa mmoja wa cheo cha juu katika Shirika la Reli la Japani aliamua kuacha kazi badala ya kutenganishwa na familia yake.’ Kisha gazeti hilo likamnukuu ofisa huyo akisema: “Kazi ya mkurugenzi-mkuu inaweza kuchukuliwa na mtu yeyote. Lakini mimi peke yangu ndiye baba ya watoto wangu.”
Hatua ya kwanza ya kuwa baba mzuri ni kutambua mambo ambayo watoto wanahitaji kutoka kwa baba yao. Hebu tuchunguze kinachomaanishwa na kuwa baba mzuri.
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
“Baba, Utarudi Lini?”
Hilo ndilo swali ambalo Nao, msichana Mjapani mwenye umri wa miaka mitano, alimwuliza baba yake alipokuwa akienda kazini siku moja. Ingawa aliishi nyumbani, Nao alimwona mara chache sana. Kwa kawaida alifika nyumbani Nao akiwa amelala na kwenda kazini kabla hajaamka.
-
-
Baba Ambaye Watoto WanahitajiAmkeni!—2004 | Agosti 22
-
-
Baba Ambaye Watoto Wanahitaji
WATOTO wanahitaji baba ambaye anawapenda, aliye tayari kuwategemeza, na anayefanya kila anachoweza kuwasaidia kuwa watu wazima wanaotegemeka na kutumainika. Lakini watu wengi hawatambui kwamba watoto wanahitaji baba wa aina hiyo.
Ni kweli kwamba akina mama ndio wanaowazaa watoto, na mama mwenye upendo hutimiza daraka muhimu. Likionyesha kwamba baba pia ana daraka muhimu, jarida The Wilson Quarterly lilisema: “Kushindwa kwa akina baba kutimiza madaraka yao ndicho kisababishi kikuu cha matatizo mengi makubwa yanayoikumba jamii ya Marekani”—na tunaweza kuongezea kwamba ndicho kisababishi kikuu cha matatizo yanayokumba ulimwengu wote.
Gazeti la Brazili Jornal da Tarde linaripoti kuhusu uchunguzi ulioonyesha kwamba mara nyingi matatizo mengi ya kitabia ya vijana, kama vile kuwa wenye jeuri, kuwa watundu, kutofanya vizuri shuleni, na kutojali “husababishwa na kukosekana kwa akina baba.” Na kitabu cha Kiitaliano Gli imperfetti genitori (Wazazi Wasiokamilika) cha Marcello Bernardi kinakazia kwamba watoto wanahitaji kuwa na wazazi wawili ili wakue vizuri.
Maisha ya Familia Yanaweza Kuboreshwa
Hata ikiwa baba anayepuuza madaraka yake amechangia au kusababisha kwa kadiri kubwa matatizo katika familia, haimaanishi kwamba hali haiwezi kurekebishwa na maisha ya familia kuboreshwa. Hilo linawezekanaje? Baba anahitaji kufanya nini?
Hapana shaka kwamba watoto wanahitaji kuwa katika mpango mzuri wa familia, yaani, kuhisi kwamba mtu anayeongoza familia anawahangaikia. Uhitaji huo usipotoshelezwa, kama inavyotukia mara nyingi leo, maisha ya watoto huathiriwa sana. Hata hivyo, baba awepo au asiwepo, bado kuna tumaini. Katika Zaburi 68:5, Biblia inasema hivi: “Baba ya wavulana wasio na baba . . . ni Mungu katika makao yake matakatifu.”a
Jinsi ya Kupata Msaada
Kisa cha Lidia, yule msichana wa Poland aliyetajwa katika makala iliyotangulia, kinaonyesha kwamba msaada wa Mungu ni muhimu kwa ajili ya mafanikio na unaweza kupatikana. Maisha ya familia yao yalikuwaje? Familia hiyo ilipataje msaada wa Mungu?
Franciszek, baba ya Lidia, anakubali kwamba aliipuuza familia yake wakati watoto wake walipokuwa wachanga kama vile binti yake alivyosema. Anasema: “Sikujali kile ambacho watoto wetu walikuwa wakifanya. Sikuwaonyesha kwamba ninawapenda, na hatukuwa na uhusiano wa karibu.” Hivyo, hakujua kwamba wakati ambapo Lidia alikuwa na umri wa miaka 14, tayari yeye na ndugu na dada yake mdogo walikuwa wakienda kwenye karamu za ulevi, kuvuta sigara, kunywa pombe, na kupigana na wengine.
Hatimaye, Franciszek alitambua matatizo yaliyowakabili watoto wake, na aliudhika sana hivi kwamba akaamua kuchukua hatua. Anasema: “Nilimwomba Mungu msaada.” Inapendeza kwamba muda mfupi baadaye, Mashahidi wa Yehova waliwatembelea nyumbani, kisha yeye na mke wake wakakubali kujifunza Biblia. Muda si muda, wazazi hao wakaanza kutumia kanuni za Biblia maishani mwao. Hilo liliwasaidiaje watoto wao?
Franciszek anaeleza hivi: “Watoto wetu walianza kutambua kwamba nimeacha kunywa pombe na kuwa baba mzuri zaidi. Walitaka kuwafahamu vizuri Mashahidi wa Yehova. Walianza pia kujifunza Biblia na kuacha mashirika yao mabaya.” Rafał, mwana wake, anasema hivi kumhusu baba yake: “Nilianza kumpenda kama rafiki.” Kisha anaongeza hivi: “Sikuona tena umuhimu wa kushirikiana na genge la mitaani. Familia yetu ilijishughulisha sana na mambo ya kiroho.”
Sasa Franciszek ni mzee Mkristo katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova, naye anaendelea kuhangaikia familia yake na maendeleo ya kiroho ya kila mmoja wao. Mke wake na Lidia ni mapainia, yaani, waeneza-injili wa wakati wote. Rafał na dada yake mdogo Sylwia hushiriki kikamili katika funzo la Biblia, kutoa maelezo katika mikutano ya Kikristo, na kuwahubiria wengine.
Alitenda Yale Aliyofundisha
Fikiria pia yaliyompata Luis, baba ya Macarena. Huyo ni yule msichana mwenye umri wa miaka 21 wa Hispania aliyenukuliwa katika makala iliyotangulia. Luis alimwiga baba yake ambaye alikuwa mlevi. Kama Macarena alivyosema, baba yake alizoea kwenda na marafiki zake na kutorudi nyumbani kwa siku kadhaa. Isitoshe, alimtendea mke wake kama mtumwa badala ya kumtendea kama mwenzi anayethaminiwa. Ndoa yao ilikuwa karibu kuvunjika, na Macarena na ndugu na dada zake wadogo walisononeka sana.
Hatimaye, Luis alikubali kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Anasema: “Nilianza kutumia wakati pamoja na mke na watoto wangu. Tulianza kuzungumza, kula, na kujifunza Biblia pamoja. Pia tulishirikiana kufanya kazi za nyumbani na kufurahia burudani pamoja.” Macarena anasema: “Nilianza kuhisi kwamba nilikuwa na baba anayejali ambaye alipendezwa kabisa na familia yake.”
Zaidi ya kutia moyo familia yake kumtumikia Mungu, Luis alitenda yale aliyofundisha. Macarena anaeleza kwamba baba yake aliacha “biashara yenye mafanikio kwa kuwa ilichukua wakati wake mwingi, naye alitaka kutumia muda mwingi zaidi kushughulikia mambo ya familia.” Matokeo yalikuwa mazuri sana. Macarena anasema: “Mfano wake umenifundisha kuwa na jicho rahisi na kutanguliza mambo ya kiroho.” Sasa anatumikia akiwa painia, na mama yake na ndugu zake wadogo ni washiriki wenye bidii wa kutaniko la Kikristo.
Uamuzi wa Ofisa wa Reli
Bila shaka, watoto wanahitaji baba anayefanya maamuzi kwa kufikiria masilahi yao. Kijana wa Takeshi Tamura, yule ofisa Mjapani aliyetajwa katika makala iliyotangulia, alikuwa na marafiki wenye mwenendo mpotovu na alikuwa karibu kutumbukia katika matatizo makubwa. Hilo lilitukia mwaka wa 1986, mwaka ambao Takeshi aliamua kuacha cheo chake kikubwa katika Shirika la Reli la Japani. Takeshi anahisije sasa kuhusu uamuzi aliofanya miaka 18 iliyopita?
Hivi karibuni, alisema: “Labda huo ndio uamuzi bora zaidi ambao nimewahi kufanya. Kutumia wakati mwingi pamoja na mwanangu na kufanya mambo pamoja, kutia ndani kujifunza Biblia, kulikuwa na matokeo mazuri sana. Hilo lilituwezesha kuwa marafiki, naye alivunja uhusiano na marafiki zake wabaya na kuacha mwenendo usiofaa.”
Mke wa Takeshi alipata kuwa Shahidi wa Yehova miaka michache iliyotangulia, na mwenendo wake mzuri ndio uliomchochea mume wake kuichunguza Biblia na kujishughulisha zaidi na familia yake. Hatimaye Takeshi, mwana wake, na binti yake wakawa Mashahidi wa Yehova. Sasa, Takeshi na mwana wake ni wazee katika makutaniko wanayoshirikiana nayo, na mke wake na binti yake ni mapainia.
Akina Baba Wanahitaji Msaada
Ingawa baba wengi hutambua kwamba wanawapuuza watoto wao, hawajui la kufanya. Gazeti La Vanguardia la Hispania lilikuwa na kichwa hiki, “Asilimia 42 ya Wazazi [wa Hispania] Wanakubali Kwamba Hawajui Jinsi ya Kuwalea Vijana Wao.” Hilo ni kweli pia kuwahusu akina baba wenye watoto walio na umri wa chini ya miaka 13 na hata walio wachanga zaidi. Tofauti na maoni ya wengi, watoto hao pia wanahitaji baba anayetumia wakati pamoja nao na kuwahangaikia.
Ni mambo gani mengine ambayo akina baba wanaweza kujifunza ili wawe baba wazuri? Ni nani walio mifano bora kwa akina baba, na akina baba wanaweza kujifunza nini kutoka kwao? Makala yetu ya mwisho itashughulikia maswali hayo.
[Maelezo ya Chini]
a Tafadhali ona sura yenye kichwa “Familia za Mzazi Mmoja Zaweza Kufanikiwa!” katika kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Akina baba waliowapa watoto wao kile wanachohitaji
Franciszek na familia yake
Luis na familia yake
Takeshi na familia yake
-
-
Jinsi ya Kuwa Baba MzuriAmkeni!—2004 | Agosti 22
-
-
Jinsi ya Kuwa Baba Mzuri
MAKALA moja katika gazeti la Economist kuhusu kuzorota kwa maisha ya familia ilianza kwa taarifa hii yenye kuvuta fikira: “Kupata watoto ni rahisi, lakini kuwa baba mzuri si rahisi.”
Ijapokuwa ni vigumu kufanya mambo mengi maishani, mojawapo ya mambo magumu zaidi na muhimu zaidi maishani ni kuwa baba mzuri. Kila baba anapaswa kutamani kuwa baba mzuri, kwani hali njema na furaha ya familia yake inategemea jambo hilo.
Kwa Nini Si Rahisi Kuwa Baba Mzuri?
Kwa ufupi, mojawapo ya sababu kuu zinazofanya isiwe rahisi kuwa baba mzuri ni hali ya kutokamilika iliyorithiwa na wazazi na watoto wao pia. Biblia inasema: “Mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mbaya tangu ujana wake na kuendelea.” (Mwanzo 8:21) Ndiyo sababu mwandikaji mmoja wa Biblia alikubali hivi: “Mama yangu alinichukua mimba katika dhambi.” (Zaburi 51:5; Waroma 5:12) Lakini mwelekeo wa kufanya mabaya kwa sababu ya dhambi iliyorithiwa ni kizuizi kimoja tu kinachofanya iwe vigumu kuwa baba mzuri.
Kizuizi kingine kikubwa ni ulimwengu huu, yaani, mfumo wa mambo. Kwa nini? Kwa sababu kama vile Biblia inavyoeleza, “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu,” anayetambulishwa kuwa “yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani.” Vilevile Biblia inamwita Shetani “mungu wa mfumo huu wa mambo.” Si ajabu kwamba Yesu alisema wanafunzi wake hawapaswi kuwa “sehemu ya ulimwengu” kama vile ambavyo yeye si sehemu ya ulimwengu!—1 Yohana 5:19; Ufunuo 12:9; 2 Wakorintho 4:4; Yohana 17:16.
Ili kuwa baba mzuri ni muhimu sikuzote kutambua mambo haya: kutokamilika kwetu, Shetani Ibilisi, na ulimwengu huu unaoongozwa naye. Vizuizi hivyo si vya kuwaziwa. Ni halisi! Lakini mtu anaweza kujifunza wapi jinsi ya kuvishinda na jinsi ya kuwa baba mzuri?
Mfano wa Yehova na Yesu
Akina baba wanaweza kuichunguza Biblia ili kupata msaada wa kushinda vizuizi hivyo vilivyotajwa juu. Kuna mifano bora inayozungumziwa humo. Yesu alionyesha mfano bora zaidi alipowafundisha wanafunzi wake kusali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni.” Biblia humfafanua Baba yetu wa mbinguni kwa njia rahisi, inaposema: “Mungu ni upendo.” Baba ambaye ni mwanadamu anapaswa kutendaje anapofikiria mfano huo wenye upendo? Mtume Paulo alihimiza hivi: “Iweni waigaji wa Mungu . . . na endeleeni kutembea katika upendo.”—Mathayo 6:9, 10; 1 Yohana 4:8; Waefeso 5:1, 2.
Ikiwa wewe ni baba, fikiria jambo unaloweza kujifunza kutokana na tukio hili moja linaloonyesha jinsi Mungu alivyoshughulika na Mwana wake, Yesu. Andiko la Mathayo 3:17 linatueleza kwamba Yesu alipobatizwa katika maji, sauti ya Mungu ilisikika kutoka mbinguni, ikisema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” Tunaweza kujifunza nini kutokana na hilo?
Kwanza, fikiria jinsi mtoto anavyohisi wakati baba yake anapomwambia mtu fulani kwa furaha, ‘Huyu ni mwanangu’ au ‘Huyu ni binti yangu.’ Watoto hufanya maendeleo mazuri wazazi wanapowahangaikia na hasa wanapowapongeza. Yaelekea mtoto atachochewa kujitahidi zaidi ili apongezwe.
Pili, Mungu alieleza jinsi alivyohisi kumhusu Yesu alipomwita “mpendwa.” Bila shaka, taarifa hiyo ya upendo kutoka kwa baba yake ilimfurahisha Yesu sana. Watoto wako watatiwa moyo pia iwapo utawaonyesha kwamba unawapenda sana kwa maneno yako, na vilevile kwa kutumia wakati pamoja nao, kuwapa uangalifu, na kuwahangaikia.
Tatu, Mungu alimwambia Mwana wake: “Nimekukubali wewe.” (Marko 1:11) Hilo pia ni jambo muhimu ambalo mzazi anapaswa kufanya, yaani, kuwaambia watoto wake kwamba anapendezwa nao. Ni kweli kwamba mara nyingi mtoto atafanya makosa. Sisi sote hukosea. Lakini ukiwa baba, je, wewe hutafuta nafasi za kuwapongeza watoto wako kwa mambo wanayofanya na kusema?
Yesu alijifunza kwelikweli kutokana na Baba yake wa mbinguni. Akiwa duniani alionyesha waziwazi kwa maneno na matendo jinsi Baba yake anavyohisi kuwaelekea watoto Wake walio duniani. (Yohana 14:9) Hata Yesu alipokuwa na shughuli na mkazo mwingi, alitenga wakati wa kuketi na kuzungumza na watoto. Aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwazuia.” (Marko 10:14) Je, ninyi akina baba mnaweza kuiga mfano wa Yehova Mungu na wa Mwana wake kwa ukamili zaidi?
Ni Muhimu Kuwa Mfano Mzuri
Ni muhimu sana kuwa mfano mzuri kwa watoto wako. Yaelekea jitihada zako za ‘kuendelea kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova’ hazitafanikiwa usipokubali nidhamu kutoka kwa Mungu na kuiruhusu iongoze maisha yako. (Waefeso 6:4) Lakini kwa msaada wa Mungu, unaweza kushinda jambo lolote linalokuzuia kutii amri yake ya kuwatunza watoto wako.
Fikiria mfano wa Viktor Gutschmidt, Shahidi wa Yehova aliyeishi katika ule uliokuwa Muungano wa Sovieti. Mnamo Oktoba 1957, alihukumiwa kifungo cha miaka kumi kwa sababu ya kuhubiri kuhusu imani yake. Aliwaacha binti wawili wadogo na mke wake, Polina. Akiwa gerezani, aliruhusiwa kuandikia familia yake barua bila kutaja jambo lolote kumhusu Mungu au dini. Hata katika hali hiyo ngumu, Viktor aliazimia kuwa baba mzuri na alifahamu kwamba kuwafundisha watoto wake kumhusu Mungu ni jambo muhimu sana. Basi alifanya nini?
Viktor anaeleza hivi: “Nilipata habari za kuandika katika magazeti ya Young Naturalist na Nature ya Sovieti. Kisha nikachora picha za wanyama na watu kwenye kadi zinazotumwa kupitia posta na kuandika hadithi au simulizi kuhusu viumbe vya asili.”
Polina anasema hivi: “Mara tu tulipopokea kadi hizo tulizihusianisha na habari za Biblia. Kwa mfano, kadi hizo zilipoonyesha uzuri wa uumbaji, misitu, au mito, nilisoma Isaya sura ya 65,” inayozungumzia ahadi za Mungu za kufanya dunia kuwa paradiso.
Binti ya Viktor anayeitwa Yulia anasema: “Kisha Mama alisali pamoja nasi, na tulilia. Kadi hizo zilikuwa muhimu sana katika malezi yetu.” Polina anasema kwamba kutokana na kadi hizo “wasichana wangu walimpenda Mungu sana tangu utotoni.” Familia hiyo inaendeleaje sasa?
Viktor anaeleza hivi, “Sasa binti zangu wawili wameolewa na wazee Wakristo na wote wana familia zilizo imara kiroho pamoja na watoto wanaomtumikia Yehova kwa uaminifu.”
Zaidi ya ustadi, jitihada nyingi zinahitajiwa ili kuwa mfano mzuri. Yaelekea watoto watachochewa wanapoona baba yao akijitahidi sana kuwa mfano mzuri. Mwana mmoja aliyetumikia kwa miaka mingi katika utumishi wa wakati wote alisema hivi kwa uthamini kuhusu baba yake, “Nyakati nyingine baba alirudi nyumbani kutoka kazini akiwa amechoka sana hivi kwamba haikuwa rahisi kwake kukaa macho, lakini bado tulifanya funzo letu la Biblia, na hilo lilitusaidia kuchukua funzo hilo kwa uzito.”
Ni wazi kwamba kuwa mfano mzuri, katika maneno na matendo, ni muhimu sana ili uwe baba mzuri. Unahitaji kufanya hivyo ili uone ukweli wa methali hii ya Biblia inayosema: “Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa; hata atakapozeeka hatageuka kando na kuiacha.”—Methali 22:6.
Kwa hiyo, kumbuka kwamba jambo muhimu si yale unayosema tu, bali kilicho muhimu zaidi ni kile unachofanya, yaani, mfano wako. Mtaalamu Mkanada wa elimu ya watoto aliandika hivi: “Njia bora zaidi ya kuwachochea watoto wetu wajiendeshe [jinsi tutakavyo] ni kuweka mfano mzuri sisi wenyewe.” Kwa hakika, ukitaka watoto wako wathamini mambo ya kiroho ni lazima wewe mwenyewe uyathamini.
Tumia Wakati Pamoja na Watoto!
Watoto wako wanapaswa kuona mfano wako mzuri. Hilo linamaanisha kwamba unapaswa kutumia wakati mwingi sana pamoja nao wala si vipindi vifupi-vifupi tu. Kwa hekima, tii shauri la Biblia la ‘kujinunulia wakati,’ kwa kupuuza mambo yasiyo muhimu sana ili kuwa pamoja na watoto wako. (Waefeso 5:15, 16) Je, kweli kuna jambo muhimu kuliko watoto wako? Je, ni televisheni kubwa, michezo, nyumba nzuri, au kazi yako?
Akina baba wasipotumia wakati kuwashughulikia watoto wakiwa wachanga, watapata matokeo mabaya baadaye. Mara nyingi akina baba walio na watoto wenye mwenendo mpotovu au wasiojali mambo ya kiroho hujuta sana. Wao husikitika kwamba walishindwa kutumia wakati pamoja na watoto wao wachanga wakati walipowahitaji sana.
Kumbuka kwamba unahitaji kufikiria matokeo ya maamuzi yako watoto wakiwa wachanga. Biblia huwaita watoto wako “urithi kutoka kwa Yehova,” urithi ambao Mungu mwenyewe amekupa. (Zaburi 127:3) Hivyo, usisahau kamwe kwamba unawajibika mbele za Mungu kuhusiana na vile unavyowatendea!
Kuna Msaada
Baba mzuri hutamani kupata msaada utakaowafaidi watoto wake. Baada ya malaika kumwambia mke wa Manoa kwamba angepata mtoto, Manoa alimwomba Mungu hivi: “Tafadhali, . . . na arudi kwetu tena, atufundishe yale tunayopaswa kumtendea huyo mtoto atakayezaliwa.” (Waamuzi 13:8, 9) Manoa alihitaji msaada gani unaohitajiwa pia na wazazi leo? Hebu tuone.
Brent Burgoyne, mwalimu katika Chuo Kikuu cha Cape Town, Afrika Kusini, alisema: “Mojawapo ya zawadi kubwa ambazo mtu anaweza kumpa mtoto ni kumfundisha maadili bora.” Ukweli wa jambo hilo unaonyeshwa na ripoti moja katika gazeti Daily Yomiuri la Japani, iliyosema: “Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba asilimia 71 ya watoto Wajapani hawajawahi kukatazwa na baba zao wasiseme uwongo.” Jambo hilo linasikitisha, sivyo?
Ni nani anayeweza kufundisha maadili bora yenye kutegemeka? Ni yule aliyempa Manoa mwongozo, yaani, Mungu mwenyewe! Ili kutusaidia, Mungu alimtuma Mwana wake mpendwa, Yesu, akiwa Mwalimu—kama vile alivyoitwa na wengi. Kwa sasa, kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu, ambacho kina masomo yanayotegemea mafundisho ya Yesu, kinapatikana katika lugha nyingi ili kikusaidie kuwafundisha watoto.
Zaidi ya kufundisha kanuni zinazopatikana katika Neno la Mungu, kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu kina picha zaidi ya 160 zenye maswali muhimu. Kwa mfano, picha inayopatikana katika sura ya 22 yenye kichwa “Kwa Nini Hatupaswi Kusema Uwongo?” imeonyeshwa kwenye ukurasa wa 32 wa gazeti hili. Maelezo yaliyo kwenye ukurasa wenye picha hii yanasema hivi: “Labda mvulana anamwambia baba yake hivi: ‘La, sikupiga mpira ndani ya nyumba.’ Lakini namna gani ikiwa kwa kweli alifanya hivyo? Je, ni vibaya kusema kwamba hakupiga mpira?”
Pia kuna habari zenye kuchochea katika sura hizi: “Utii Unakulinda Wewe,” “Tuepuke Vishawishi,” “Jinsi ya Kuwa Mwenye Fadhili,” “Usiwe Mwizi Kamwe!,” “Je, Karamu Zote Zinampendeza Mungu?,” “Jinsi ya Kumfurahisha Mungu,” na “Kwa Nini Tufanye Kazi?” Hizo ni sura chache tu kati ya sura 48 za kitabu hicho.
Utangulizi wa kitabu hicho unamalizia kwa maneno haya: “Watoto wanahitaji zaidi kuelekezwa kwa Chanzo cha hekima yote, Baba yetu wa mbinguni, Yehova Mungu. Kila wakati Mwalimu Mkuu, Yesu, aliwaelekeza watu kwenye chanzo cha hekima yote, Muumba wetu. Kitabu hiki na kikusaidie sana pamoja na familia yako kumpendeza Yehova ili mpokee baraka za milele.”a
Hapana shaka kwamba kuwa baba mzuri kunatia ndani kuwa mfano mzuri kwa watoto wako, kutumia wakati mwingi pamoja nao, na kuwasaidia waishi kulingana na kanuni za Mungu ambazo ameonyesha katika Biblia.
[Maelezo ya Chini]
a Vitabu vingine ambavyo vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova ili kusaidia familia ni Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, Maswali Ambayo Vijana Huuliza−Majibu Yafanyayo Kazi, na Siri ya Kupata Furaha ya Familia.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Ajapokuwa gerezani, Viktor Gutschmidt alifanikiwa kuwa baba mzuri
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Alipofungwa gerezani kwa sababu ya imani yake, Viktor aliwachorea watoto wake picha hizi ili kuwafundisha
[Picha katika ukurasa wa 9]
Binti za Viktor katika mwaka wa 1965
[Picha katika ukurasa wa 10]
Akina baba wanapaswa kujitahidi sana kuwafundisha watoto wao
-