-
Mtumaini Yehova Kikamili Nyakati za TaabuMnara wa Mlinzi—2003 | Septemba 1
-
-
Unapopoteza Kazi au Mapato Yanapokuwa Kidogo
3. Watumishi wa Yehova wanaoishi katika ‘nyakati hizi za hatari’ wanakabili hali gani ngumu za kiuchumi, na tunajuaje kwamba Mungu yuko tayari kutusaidia?
3 Katika ‘nyakati hizi za hatari,’ sisi Wakristo hukabiliana na hali ngumu za kiuchumi kama watu wengine. (2 Timotheo 3:1) Kwa hiyo, huenda kwa ghafula tukajikuta tumepoteza kazi. Au huenda tukalazimika kufanya kazi kwa saa nyingi na kupata mshahara kidogo. Chini ya hali hizo, huenda tukaona ni vigumu ‘kuwaandalia kitu wale walio wetu wenyewe.’ (1 Timotheo 5:8) Je, Mungu Aliye Juu Zaidi yuko tayari kutusaidia nyakati hizo? Ndiyo kabisa! Kwa kweli, Yehova hatukingi na magumu yote ya maisha ya mfumo huu wa mambo. Hata hivyo, tukimtumaini, maneno ya Zaburi 46:1, BHN, yatatuhusu: “Mungu ni kimbilio letu na nguvu yetu; yeye ni msaada wetu daima wakati wa taabu.” Lakini tunaweza kuonyeshaje kwamba tunamtumaini Yehova kikamili kunapokuwa na taabu za kiuchumi?
4. Tunapokabili matatizo ya kiuchumi, tunaweza kusali juu ya nini, na Yehova huonaje sala hizo?
4 Njia moja ya kuonyesha kwamba tunamtumaini Yehova, ni kusali kwake. Lakini tunaweza kusali juu ya nini? Tunapokabili matatizo ya kiuchumi, huenda tukahitaji hekima sasa kuliko wakati mwingine wowote. Bila shaka tunapaswa kusali tupewe hekima! Neno la Yehova linatuhakikishia hivi: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, acheni afulize kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo.” (Yakobo 1:5) Naam, mwombe Yehova akupe hekima—uwezo wa kutumia vizuri ujuzi, uelewevu, na utambuzi—ili ufanye maamuzi ya busara na machaguo mazuri. Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo anatuhakikishia kwamba atasikiliza sala hizo. Yeye yuko tayari daima kunyoosha mapito ya wale wanaomtumaini kwa moyo wao wote.—Zaburi 65:2; Mithali 3:5, 6.
5, 6. (a) Kwa nini tunaweza kutegemea Neno la Mungu ili litusaidie kukabiliana na hali ngumu za kiuchumi? (b) Tunaweza kufanya nini ili kupunguza wasiwasi tunapopoteza kazi?
5 Njia nyingine ya kuonyesha kwamba tunamtumaini Yehova ni kutegemea mwongozo kutoka katika Neno lake. Vikumbusho vyake vyenye hekima vinavyopatikana katika Biblia vimekuwa “vyenye kutegemeka sana.” (Zaburi 93:5, NW) Ingawa kitabu hicho kilichoongozwa kwa roho ya Mungu kilikamilishwa zaidi ya miaka 1,900 iliyopita, kina mashauri yenye kutegemeka na ufahamu wenye kina unaoweza kutusaidia kukabiliana vizuri na hali ngumu za kiuchumi. Fikiria mifano fulani inayoonyesha hekima ya Biblia.
6 Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema hivi zamani: “Usingizi wake kibarua ni mtamu, kwamba amekula kidogo, au kwamba amekula kingi; lakini kushiba kwake tajiri hakumwachi kulala usingizi.” (Mhubiri 5:12) Wakati na pesa zinahitajika ili kurekebisha, kusafisha, kudumisha, na kulinda vitu vyetu vya kimwili. Hivyo tukipoteza kazi, huenda tukatumia nafasi hiyo kuchunguza tena mtindo wetu wa maisha na kujaribu kuamua vitu tunavyohitaji na vitu tusivyohitaji. Ili kupunguza wasiwasi, lingekuwa jambo la hekima kufanya mabadiliko fulani. Kwa mfano, je, inawezekana kufanya maisha yetu yawe sahili, labda kuhamia nyumba ndogo zaidi au kuondoa vitu vya kimwili tusivyohitaji?—Mathayo 6:22.
7, 8. (a) Yesu alionyeshaje kwamba anajua wanadamu wasio wakamilifu wana mwelekeo wa kuhangaikia vitu vya kimwili kupita kiasi? (Ona pia kielezi-chini.) (b) Yesu alitoa shauri gani lenye hekima kuhusu jinsi ya kuepuka kuwa na mahangaiko isivyofaa?
7 Katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu alishauri hivi: “Komeni kuhangaikia nafsi zenu kuhusu ni nini mtakula au ni nini mtakunywa, au juu ya miili yenu kuhusu ni nini mtavaa.”b (Mathayo 6:25) Yesu alijua kwamba kwa kawaida wanadamu wasio wakamilifu huhangaika kupata mahitaji ya lazima. Lakini tunawezaje ‘kukoma kuhangaikia’ vitu hivyo? Yesu alisema: “Fulizeni kutafuta kwanza ufalme.” Hata tuwe tunakabili matatizo gani, tunapaswa kuendelea kutanguliza ibada ya Yehova maishani. Tukifanya hivyo, Baba yetu wa mbinguni ‘atatuongezea’ mahitaji yetu yote ya kila siku. Kwa njia fulani, atatuandalia tunayohitaji.—Mathayo 6:33.
8 Yesu alitoa shauri hili lingine: “Msihangaike kamwe juu ya siku ifuatayo, kwa maana siku ifuatayo itakuwa na mahangaiko yayo yenyewe.” (Mathayo 6:34) Si jambo la hekima kuhangaikia isivyofaa mambo ambayo huenda yakatokea kesho. Msomi mmoja alisema hivi: “Wakati ujao si mbaya sana kama tunavyohofia.” Kutii kwa unyenyekevu shauri la Biblia kuhusu kuzingatia mambo muhimu na kutatua matatizo wakati yanapotokea kutatusaidia kuepuka kuwa na mahangaiko isivyofaa.—1 Petro 5:6, 7.
9. Tunapokabili taabu za kiuchumi, tunaweza kupata msaada gani katika vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”?
9 Tunapokabili taabu za kiuchumi, tunaweza pia kuonyesha kwamba tunamtumaini Yehova kwa kutafuta msaada kutoka katika vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45) Mara kwa mara, gazeti la Amkeni! limechapisha makala zilizo na mashauri na madokezo mazuri kuhusu jinsi ya kushughulika na magumu ya kiuchumi. Makala “Ukipoteza Kazi—Suluhisho Ni Nini?” katika toleo la Juni 8, 1992, iliorodhesha miongozo minane ambayo imewasaidia watu wengi kudumisha usawaziko wa kifedha na kihisia-moyo wanapopoteza kazi.c Bila shaka, pamoja na miongozo hiyo, tunapaswa kuwa na maoni yanayofaa kuhusu umuhimu wa pesa. Jambo hilo lilizungumziwa katika makala “Kitu Kingine cha Maana Sana Kuliko Pesa” iliyochapishwa katika toleo hilohilo.—Mhubiri 7:12.
-
-
Mtumaini Yehova Kikamili Nyakati za TaabuMnara wa Mlinzi—2003 | Septemba 1
-
-
c Miongozo hiyo minane ni: (1) Usiwe na hofu kuu; (2) fikiria kwa mwelekeo mzuri; (3) fungulia akili yako aina mpya za kazi; (4) ishi kwa mapato yako mwenyewe—si ya mwingine; (5) uwe mwangalifu na mkopo; (6) endeleza umoja katika familia; (7) endelea kujistahi; na (8) panga bajeti.
-