-
Acha Yehova Akuongoze Kupata Uhuru wa KweliMnara wa Mlinzi—2012 | Julai 15
-
-
Acha Yehova Akuongoze Kupata Uhuru wa Kweli
‘Chunguza ndani ya sheria kamilifu iliyo ya uhuru.’—YAK. 1:25.
JE, UNAWEZA KUELEZA?
Ni sheria gani inayoongoza kwenye uhuru wa kweli, na ni nani wanaofaidika kutokana na sheria hiyo?
Ni nini siri ya kupata uhuru wa kweli?
Wote wanaoendelea kutembea kwenye njia ya uzima watapata uhuru gani?
1, 2. (a) Unaweza kusema nini kuhusu uhuru wa watu leo, na kwa nini hali iko hivyo? (b) Ni uhuru gani ambao watumishi wa Yehova watapata wakati ujao?
TUNAISHI wakati ambapo mambo kama vile pupa, uasi-sheria, na jeuri yanazidi kuongezeka. (2 Tim. 3:1-5) Ili kukabiliana na matatizo hayo, serikali zinatunga sheria zaidi, zinaimarisha vikosi vya polisi, na kutumia vifaa vya kielektroniki vya ulinzi. Katika nchi fulani, raia wanajaribu kuongeza usalama wao kwa kuweka ving’ora katika nyumba zao, na pia kufunga milango yao kwa makufuli mengi zaidi na hata kuweka nyua za umeme. Watu wengi hawatoki nje usiku au kuwaruhusu watoto wao wacheze nje peke yao iwe mchana au usiku. Ni wazi kwamba watu wanazidi kupoteza uhuru wao na inaelekea kwamba hali hiyo itazidi kuwa mbaya.
2 Katika bustani ya Edeni, Shetani alidai kwamba siri ya kupata uhuru wa kweli ni kutomtegemea Yehova. Dai hilo limethibitika kuwa la uwongo na la uovu kama nini! Kwa kweli, kadiri watu wanavyopuuza mipaka ya maadili na ya kiroho ambayo Mungu ameweka, ndivyo wanadamu kwa ujumla wanavyozidi kuteseka. Hali hiyo inayozidi kuwa mbaya inatuathiri sisi pia tukiwa watumishi wa Yehova. Hata hivyo, tunatumaini kuona wanadamu wakiwekwa huru kutoka katika utumwa wa dhambi na uharibifu na kufurahia ule ambao Biblia inauita “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Rom. 8:21) Kwa kweli, tayari Yehova ameanza kuwatayarisha watumishi wake ili wafurahie uhuru huo. Kwa njia gani?
3. Yehova amewapa wafuasi wa Kristo sheria gani, na ni maswali gani tutakayochunguza?
3 Jibu linategemea ile sheria ambayo mwandikaji wa Biblia, Yakobo, aliiita “sheria kamilifu iliyo ya uhuru.” (Soma Yakobo 1:25.) Tafsiri nyingine za Biblia zinatafsiri hivi maneno hayo, “sheria ambayo inatufanya tuwe huru” (The New English Bible) na “sheria kamilifu ya uhuru” (The New American Bible). Bila shaka, kwa kawaida watu wanaposikia neno “sheria” wanalihusianisha na vizuizi, bali si uhuru. Basi, ni nini “sheria kamilifu iliyo ya uhuru”? Na sheria hiyo inatuwekaje huru?
SHERIA INAYOTUWEKA HURU
4. “Sheria kamilifu iliyo ya uhuru” ni nini, na ni nani wanaofaidika nayo?
4 “Sheria kamilifu iliyo ya uhuru” si Sheria ya Musa, kwa sababu Sheria ya Musa ilifanya makosa yawe wazi na ilitimizwa na Kristo. (Mt. 5:17; Gal. 3:19) Hivyo basi, Yakobo alikuwa akizungumza kuhusu sheria gani? Alikuwa akizungumza kuhusu “sheria ya Kristo,” ambayo pia inaitwa “sheria ya imani” na “sheria ya watu huru.” (Gal. 6:2; Rom. 3:27; Yak. 2:12) Kwa hiyo, “sheria kamilifu” inatia ndani kila jambo ambalo Yehova anataka tufanye. Wakristo watiwa-mafuta na “kondoo wengine” wanafaidika na sheria hiyo.—Yoh. 10:16.
5. Kwa nini sheria ya uhuru si mzigo mzito?
5 Tofauti na sheria za nchi nyingi, “sheria kamilifu” si ngumu kueleweka wala si mzigo mzito bali inatia ndani amri rahisi na kanuni za msingi. (1 Yoh. 5:3) Yesu alisema hivi: “Nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mt. 11:29, 30) Zaidi ya hayo, “sheria kamilifu” haihitaji kuwa orodha ndefu ya vizuizi, au adhabu, kwa sababu inategemea upendo na imeandikwa katika akili na mioyo, si kwenye mabamba ya mawe.—Soma Waebrania 8:6, 10.
JINSI “SHERIA KAMILIFU” INAVYOTUWEKA HURU
6, 7. Tunaweza kusema nini kuhusu viwango vya Yehova, na kwa nini sheria ya uhuru inatuweka huru?
6 Mipaka ambayo Yehova amewawekea viumbe wake wenye akili inawanufaisha na kuwalinda. Kwa mfano, fikiria sheria za kiasili ambazo zinadhibiti nishati na vitu mbalimbali. Watu hawalalamiki kwamba sheria hizo zinawakandamiza. Badala yake, wanazithamini, na kutambua kwamba sheria za kiasili ni muhimu kwa ajili ya hali yao njema. Vivyo hivyo, viwango vya Yehova vya maadili na vya kiroho, tunavyojifunza kupitia ile “sheria kamilifu” ya Kristo, vimewekwa kwa faida ya wanadamu.
7 Mbali na kwamba inatulinda, sheria ya uhuru inaturuhusu kutosheleza tamaa zetu zote zinazofaa bila kujiumiza au kuingilia uhuru na haki ya wengine. Basi siri ya kuwa huru kikweli, yaani, kuweza kufanya mambo tunayotamani, ni kusitawisha tamaa zinazofaa, ambazo zinapatana na utu wa Yehova na viwango vyake. Kwa maneno mengine, tunapaswa kujifunza kupenda mambo ambayo Yehova anapenda na kuchukia yale anayochukia, na sheria ya uhuru inatusaidia kufanya hivyo.—Amo. 5:15.
8, 9. Wale wanaoshikamana na sheria ya uhuru wanapata faida gani? Toa mfano.
8 Kwa sababu ya hali yetu ya kutokamilika, tunapambana na mwili wetu ili kushinda tamaa zisizofaa. Hata hivyo, tunapofuata kwa ushikamanifu sheria ya uhuru, tunafurahia kwa kadiri fulani uwezo wa sheria hiyo wa kutuweka huru hata sasa. Kwa mfano, mwanafunzi mpya wa Biblia anayeitwa Jay alizoea kuvuta tumbaku. Alipojifunza kwamba zoea hilo halimpendezi Mungu, alilazimika kufanya uamuzi. Je, angeendelea kuutii mwili wake au angejitiisha chini ya Yehova? Kwa hekima, alichagua kumtumikia Mungu, hata ingawa mwili wake ulitamani sana tumbaku. Alihisije baada ya kushinda zoea hilo? Baadaye alisema hivi: “Nilifurahi sana na kujihisi nikiwa huru kabisa.”
9 Jay alijifunza kupitia mambo aliyokabili kwamba uhuru wa ulimwengu, ambao unawaruhusu watu ‘kukaza akili juu ya mwili,’ kwa kweli unawafanya wawe watumwa, lakini uhuru wa Yehova, ambao unamaanisha “kukaza akili juu ya roho,” unawaweka watu huru na kuwawezesha kupata “uzima na amani.” (Rom. 8:5, 6) Jay alipata wapi nguvu za kushinda zoea lake ambalo lilimfanya awe mtumwa? Nguvu hizo zilitoka kwa Mungu; hazikuwa nguvu zake mwenyewe. Alisema hivi: “Nilijifunza Biblia kwa ukawaida, nilisali ili nipate roho takatifu, na kutafuta msaada wenye upendo ambao nilipewa kwa hiari na kutaniko la Kikristo.” Maandalizi hayohayo yanaweza kutusaidia sisi sote kupata uhuru wa kweli. Acheni tuone jinsi yanavyoweza kutusaidia.
CHUNGUZA NENO LA MUNGU
10. “Kuchunguza” ndani ya sheria ya Mungu kunamaanisha nini?
10 Andiko la Yakobo 1:25 linasema hivi kwa sehemu: “Yeye anayechunguza ndani ya sheria kamilifu iliyo ya uhuru na ambaye hudumu katika hiyo . . . atakuwa mwenye furaha katika kuitenda.” Neno la awali la Kigiriki ambalo linatafsiriwa kuwa “anayechunguza” linamaanisha “kuinama ili kuangalia kwa makini,” na linatoa wazo la kujitahidi kwa bidii. Naam, ikiwa tunataka sheria ya uhuru iguse akili na moyo wetu, ni lazima tutimize sehemu yetu kwa kujifunza Biblia kwa bidii, kusali, na kutafakari kuhusu yale tunayosoma.—1 Tim. 4:15.
11, 12. (a) Yesu alikaziaje uhitaji wa kufanya kweli iwe njia yetu ya maisha? (b) Kulingana na mfano ulio katika fungu, ni hatari gani ambayo vijana hasa wanapaswa kuepuka?
11 Wakati huohuo, ni lazima ‘tudumu,’ au tuendelee, kufuata Neno la Mungu, na hivyo kufanya kweli iwe njia yetu ya maisha. Yesu alitoa wazo hilohilo alipowaambia hivi watu fulani waliomwamini: “Mkikaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, nanyi mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.” (Yoh. 8:31, 32) Kitabu kimoja kinasema kwamba neno “kujua,” katika andiko hilo linamaanisha pia kuthamini kwa sababu “jambo ‘linalojulikana’ ni lenye thamani au ni muhimu kwa yule anayelijua.” Kwa hiyo, ‘tunajua’ kweli katika maana kamili tunapoifanya kweli hiyo iwe njia yetu ya maisha. Hapo ndipo tunapoweza kwa kufaa kusema kwamba “neno la Mungu” “linafanya kazi” ndani yetu, likifinyanga utu wetu ili tumwige kwa ukaribu zaidi Baba yetu wa mbinguni.—1 The. 2:13.
12 Jiulize hivi: ‘Je, kwa hakika ninaijua kweli? Je, nimeifanya iwe njia yangu ya maisha? Au bado ninatamani “uhuru” wa ulimwengu?’ Akifikiria miaka yake ya utineja, dada mmoja ambaye alilelewa na wazazi Wakristo aliandika hivi: “Unapolelewa katika familia inayofuata kweli, ni kana kwamba Yehova yuko daima katika familia yenu. Lakini mimi kwa kweli sikumjua kamwe. Sikujifunza kamwe kuchukia mambo anayochukia. Sikuamini kamwe kwamba alijali mambo niliyofanya. Na sikujifunza kamwe kuzungumza naye katika sala nilipokuwa na matatizo. Nilitegemea uelewaji wangu mwenyewe, lakini sasa ninajua kwamba lilikuwa jambo la upumbavu kutegemea uelewaji wangu kwa sababu sikujua chochote.” Inafurahisha kwamba baadaye dada huyo alitambua kwamba alifikiri kwa njia isiyofaa kabisa, na hivyo akafanya mabadiliko makubwa. Hata alianza kutumikia akiwa painia wa kawaida.
ROHO TAKATIFU INAWEZA KUKUSAIDIA UWE HURU
13. Roho takatifu ya Mungu inatusaidiaje kuwa huru?
13 Katika andiko la 2 Wakorintho 3:17, tunasoma hivi: “Mahali palipo na roho ya Yehova, pana uhuru.” Roho takatifu inatusaidiaje kuwa huru? Kati ya mambo mengine, inasitawisha ndani yetu sifa muhimu ambazo zinatuwezesha kuwa huru—“upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.” (Gal. 5:22, 23) Bila sifa hizo, hasa upendo, watu hawawezi kuwa huru kikweli, na jambo hilo linaonekana wazi ulimwenguni leo. Inapendeza kujua kwamba baada ya kutaja sifa za tunda la roho, mtume Paulo aliongezea hivi: “Hakuna sheria juu ya mambo hayo.” Alimaanisha nini? Hakuna sheria yoyote inayoweza kulizuia tunda la roho ya Mungu lisiendelee kukua. (Gal. 5:18) Kwa wazi, sheria ya aina hiyo ingekuwa na faida gani? Ni mapenzi ya Yehova kwamba tusitawishe sifa kama za Kristo milele na kuonyesha sifa hizo bila kuzuiwa.
14. Ni katika njia gani roho ya ulimwengu inawafanya watu wanaojitiisha chini yake kuwa watumwa?
14 Wale ambao ni watumwa wa roho ya ulimwengu na ambao wanatosheleza tamaa zao za kimwili bila kujali huenda wakafikiri kwamba wako huru. (Soma 2 Petro 2:18, 19.) Hata hivyo, ukweli ni kwamba wao ni watumwa. Ni lazima maagizo na sheria nyingi sana zitungwe ili kudhibiti tamaa na tabia zao zenye kudhuru. Paulo anasema kwamba “sheria huwekwa, si kwa ajili ya mtu mwadilifu, bali kwa ajili ya watu wenye kuasi sheria na watundu.” (1 Tim. 1:9, 10) Watu hao pia ni watumwa wa dhambi, wanachochewa kufanya “mambo yanayopendwa na mwili,” mwili ambao ni bwana mkatili. (Efe. 2:1-3) Kwa njia fulani, watu hao ni kama wadudu wanaotambaa na kuingia ndani ya bakuli la asali. Wanasukumwa na tamaa yao, na kwa ghafula wanajikuta wamenaswa.—Yak. 1:14, 15.
KUWEKWA HURU KATIKA KUTANIKO LA KIKRISTO
15, 16. Ushirika wetu katika kutaniko ni muhimu kadiri gani, na tunafurahia uhuru gani?
15 Ulipoanza kushirikiana na kutaniko la Kikristo, hukujiunga na kutaniko kana kwamba unajiunga na chama cha kijamii. Badala yake, uliingia katika kutaniko kwa sababu Yehova alikuvuta. (Yoh. 6:44) Ni nini kilichomchochea Yehova akuvute? Je, ni kwa sababu aliona wewe ni mtu mwadilifu anayemwogopa Mungu? Huenda ukajibu, “La, hasha!” Basi, Mungu aliona nini? Aliona kwamba una moyo ambao utakubali sheria yake inayowaweka watu huru, moyo ambao utajitiisha chini ya mwongozo wake wenye fadhili. Katika kutaniko, Yehova ameujenga moyo wako kwa kukulisha kiroho, kukuweka huru kutokana na uwongo wa kidini, ushirikina, na kukufundisha kusitawisha utu kama wa Kristo. (Soma Waefeso 4:22-24.) Matokeo ni kwamba umepata pendeleo la kuwa kati ya watu pekee ulimwenguni ambao wanaweza kwa kufaa kuitwa “watu huru.”—Yak. 2:12.
16 Fikiria jambo hili: Je, unaogopa unapokuwa pamoja na watu wanaompenda Yehova kwa moyo wao wote? Je, unajikuta kila mara ukitazama huku na huku kwa wasiwasi? Unapoongea na ndugu na dada zako katika Jumba la Ufalme, je, unaogopa kwamba huenda wakaiba vitu vyako? Huogopi kamwe! Unatulia na kuhisi ukiwa huru. Je, ungehisi hivyo katika mkutano wa kilimwengu? Inaelekea kwamba hungehisi hivyo! Zaidi ya hayo, uhuru ambao unafurahia miongoni mwa watu wa Mungu ni kionjo tu cha uhuru ambao utafurahia wakati ujao.
“UHURU WENYE UTUKUFU WA WATOTO WA MUNGU”
17. Uhuru wa wanadamu unahusianaje na “kufunuliwa kwa wana wa Mungu”?
17 Paulo alipokuwa akizungumza kuhusu uhuru ambao Yehova atawapa watumishi wake duniani, aliandika hivi: “Uumbaji unangojea na kutazamia kwa hamu kufunuliwa kwa wana wa Mungu.” Kisha akaongezea hivi: “Uumbaji wenyewe pia utawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Rom. 8:19-21) “Uumbaji” unarejelea wanadamu ambao wana tumaini la kuishi milele duniani, wale ambao watafaidika wakati wa “kufunuliwa” kwa wana wa Mungu waliotiwa mafuta kwa roho. Kufunuliwa huko kutaanza wakati “wana” hao, ambao watakuwa wamefufuliwa na kuingia katika makao ya roho, watakaposhirikiana na Kristo katika kuondoa kabisa uovu duniani na kuokoa “umati mkubwa” ili uingie katika mfumo mpya wa mambo.—Ufu. 7:9, 14.
18. Uhuru utaongezekaje kwa wanadamu watiifu, na ni uhuru gani ambao watafurahia mwishowe?
18 Wakati huo, wanadamu waliokombolewa watapata uhuru mpya kabisa, uhuru kutokana na uvutano wa Shetani na roho waovu. (Ufu. 20:1-3) Jambo hilo litaleta kitulizo kama nini! Kisha, wale 144,000 ambao watakuwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo wataendelea kutumia faida za dhabihu ya fidia kuwaweka wanadamu huru hatua kwa hatua mpaka dhambi na hali ya kutokamilika iliyosababishwa na Adamu itakapokuwa imeondolewa kabisa. (Ufu. 5:9, 10) Baada ya kubaki waaminifu hata chini ya jaribu, wanadamu watakuwa wamepata uhuru kamili ambao Yehova alikusudia wawe nao, “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” Hebu fikiria jambo hilo! Hutahitaji tena kupambana na mwili wako ili kufanya mambo yanayofaa machoni pa Mungu kwa sababu mwili wako wote utakuwa mkamilifu na utu wako utakuwa umebadilika kabisa kulingana na utu wa Mungu.
19. Ni lazima tuendelee kufanya nini leo ili tupate uhuru wa kweli wakati ujao?
19 Je, unatamani kupata “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu”? Ikiwa ndivyo, acha akili na moyo wako uendelee kuongozwa na “sheria kamilifu iliyo ya uhuru.” Naam, jifunze Maandiko kwa bidii. Ishi kupatana na kweli, na uifanye iwe mali yako. Sali ili upate roho takatifu. Nufaika kikamili kwa kushirikiana na kutaniko la Kikristo na kula chakula cha kiroho ambacho Yehova anaandaa. Usimruhusu Shetani akudanganye, kama alivyomdanganya Hawa, kufikiri kwamba matakwa ya Mungu yanatubana sana. Kwa kweli, Ibilisi ni mjanja sana. Lakini kama tutakavyoona katika makala inayofuata, hakuna sababu ya ‘Shetani kutushinda akili, kwa maana tunazijua mbinu zake.’—2 Kor. 2:11.
-
-
Mtumikie Mungu wa UhuruMnara wa Mlinzi—2012 | Julai 15
-
-
Mtumikie Mungu wa Uhuru
“Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.”—1 YOH. 5:3.
JE, UNAWEZA KUJIBU?
Shetani hujaribu jinsi gani kufanya sheria za Mungu zionekane kuwa mzigo mzito?
Kwa nini ni lazima tuwe waangalifu sana tunapochagua marafiki wetu?
Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kuwa washikamanifu kwa Mungu wa uhuru?
1. Yehova ana maoni gani kuhusu uhuru, na alionyeshaje hivyo aliposhughulika na Adamu na Hawa?
YEHOVA peke yake ndiye aliye na uhuru kamili. Hata hivyo, hautumii vibaya kamwe uhuru huo; wala kuwanyima uhuru watumishi wake kwa kuingilia kila jambo wanalofanya. Badala yake, amewapa watumishi wake uhuru wa kuchagua, ambao unawaruhusu kutumia uwezo wao kutosheleza tamaa zao zote zinazofaa. Kwa mfano, Mungu aliwapa Adamu na Hawa amri moja tu iliyowakataza kula matunda ya “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” (Mwa. 2:17) Walikuwa na uhuru mwingi ajabu wa kutimiza mapenzi ya Muumba wao!
2. Kwa nini wazazi wetu wa kwanza walipoteza uhuru ambao Mungu aliwapa?
2 Kwa nini Mungu aliwapa wazazi wetu wa kwanza uhuru mwingi hivyo? Aliwaumba kwa mfano wake na kuwapa dhamiri, na hivyo alitarajia kwamba upendo wao kumwelekea akiwa Muumba wao ungewaongoza katika njia inayofaa. (Mwa. 1:27; Rom. 2:15) Inahuzunisha kwamba Adamu na Hawa hawakumthamini Muumba wao mzuri ajabu na hawakuthamini uhuru ambao alikuwa amewapa. Badala yake, walichagua uhuru usiofaa ambao Shetani aliwaahidi, yaani, uhuru wa kimaadili. Lakini badala ya kupata uhuru zaidi, wazazi wetu wa kwanza walijiuza wenyewe na wazao wao wa baadaye katika utumwa wa dhambi, na hivyo matokeo yakawa mabaya sana.—Rom. 5:12.
3, 4. Shetani anajaribu kutudanganya jinsi gani kuhusiana na viwango vya Yehova?
3 Ikiwa Shetani alifaulu kuwashawishi wanadamu wawili wakamilifu, pamoja na viumbe wengi wa roho, wakatae enzi kuu ya Mungu, anaweza pia kutudanganya. Bado anatumia mbinu hiyohiyo leo. Anajaribu kutupotosha kwa kutufanya tufikiri kwamba viwango vya Mungu ni mzigo mzito, na vinatunyima raha na shangwe. (1 Yoh. 5:3) Kufikiri kwa njia hiyo kunaweza kuwa na uvutano mkubwa juu yetu ikiwa tutashirikiana kwa ukawaida na watu wanaofikiri kwa njia hiyo. Dada mmoja mwenye umri wa miaka 24 ambaye alifanya uasherati alisema hivi: “Marafiki wabaya walikuwa na uvutano mkubwa sana juu yangu, hasa kwa sababu niliogopa kuwa na maoni tofauti na vijana wenzangu.” Huenda wewe pia umekabili msongo kama huo wa marafiki.
4 Inahuzunisha kwamba nyakati nyingine kunaweza pia kuwa na uvutano wa marafiki wabaya katika kutaniko la Kikristo. Kijana mmoja Shahidi alisema hivi: “Ninajua vijana fulani ambao walikuwa na uhusiano wa kimahaba na watu ambao si waamini. Hata hivyo, mwishowe niligundua kwamba kadiri nilivyoshirikiana nao, ndivyo nilivyozidi kuwa kama wao. Hali yangu ya kiroho ikaanza kuharibika. Sikuwa nikifurahia chakula cha kiroho katika mikutano, na sikushiriki kwa ukawaida katika utumishi. Hapo ndipo nilipotambua kwamba nilihitaji kukatisha urafiki huo, na ndivyo nilivyofanya!” Je, unajua uvutano wenye nguvu ambao marafiki wako wanaweza kuwa nao juu yako? Fikiria mfano fulani katika Biblia ambao unatuhusu leo.—Rom. 15:4.
ALIIBA MIOYO YAO
5, 6. Absalomu aliwadanganya wengine jinsi gani, na je, njama yake ilifanikiwa?
5 Biblia ina mifano mingi ya watu ambao walikuwa na uvutano mbaya juu ya wengine. Mfano mmoja mbaya ni Absalomu, mwana wa Mfalme Daudi. Absalomu alikuwa mwanamume mwenye sura nzuri sana. Hata hivyo, baada ya muda, aliruhusu pupa ya mambo makuu ijae katika moyo wake, kama Shetani, kwa kuwa alianza kutamani kiti cha ufalme cha baba yake, ambacho hakuwa na haki ya kuchukua.a Ili kujaribu kuchukua ufalme kwa hila, Absalomu alijifanya kwamba anawajali sana Waisraeli wenzake huku akionyesha kwa ujanja kwamba mfalme hakuwajali. Naam, kama tu Ibilisi alivyofanya katika bustani ya Edeni, Absalomu alijifanya kwamba anawasaidia, na wakati huohuo alikuwa akieneza uwongo mbaya kuhusu baba yake mwenyewe.—2 Sam. 15:1-5.
6 Je, njama ya werevu ya Absalomu ilifanikiwa? Naam, ilifanikiwa kwa kadiri fulani kwa sababu simulizi la Biblia linasema hivi: “Absalomu akaendelea kuiba mioyo ya watu wa Israeli.” (2 Sam. 15:6) Hata hivyo, mwishowe Absalomu alishindwa kwa sababu ya kiburi chake. Na inasikitisha kwamba jambo hilo lilisababisha kifo chake na vifo vya maelfu ya watu ambao aliwashawishi kumfuata.—2 Sam. 18:7, 14-17.
7. Ni mambo gani tunayoweza kujifunza kutokana na simulizi kumhusu Absalomu? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 14.)
7 Kwa nini Waisraeli hao walidanganywa kwa urahisi sana? Labda walitamani vitu ambavyo Absalomu aliwaahidi. Au huenda walidanganywa na sura yake nzuri. Kwa vyovyote vile, tunaweza kuwa na hakika kuhusu jambo hili: Walikosa kuwa washikamanifu kwa Yehova na kwa mfalme aliyemweka rasmi. Leo, Shetani anaendelea kuwatumia “akina Absalomu wa mfano” ili kujaribu kuiba mioyo ya watumishi wa Yehova. Huenda watu hao wakasema, ‘viwango vya Yehova vinatubana sana. Hebu watazame watu wote ambao hawamtumikii Yehova. Wanaponda raha kabisa!’ Je, utatambua kwamba madai hayo ni uwongo wenye kuchukiza na hivyo kuendelea kuwa mshikamanifu kwa Mungu? Je, utatambua kwamba “sheria kamilifu” ya Yehova, yaani, sheria ya Kristo, ndiyo tu inayoweza kukuongoza kupata uhuru wa kweli? (Yak. 1:25) Ikiwa ndivyo, thamini sheria hiyo, na usijaribu kamwe kuutumia vibaya uhuru wako wa Kikristo.—Soma 1 Petro 2:16.
8. Ni mifano gani ya watu halisi inayoonyesha kwamba kupuuza viwango vya Yehova hakuleti furaha?
8 Shetani anawalenga hasa vijana. Ndugu ambaye sasa ana umri wa miaka 30 na kitu alisema hivi kuhusu miaka yake ya utineja: “Niliona kwamba viwango vya Yehova vya maadili vinanibana sana, wala si ulinzi.” Kwa sababu hiyo, akafanya uasherati. Lakini hakupata furaha kwa kufanya hivyo. Alisema hivi: “Kwa miaka mingi nilisumbuliwa sana na hisia nyingi za hatia na majuto.” Dada mmoja aliandika hivi kuhusu miaka yake ya utineja: “Baada ya kufanya uasherati, unahuzunika sana na kujiona hufai. Hata sasa baada ya miaka 19 kupita, bado ninaumia ninapokumbuka jambo hilo.” Dada mwingine alisema hivi: “Nilipofikiria jinsi mwenendo wangu ulivyowavunja moyo watu ninaowapenda sana nilivurugika sana kiakili, kiroho, na kihisia. Ni jambo baya sana kuishi bila kibali cha Yehova.” Shetani hataki ufikirie matokeo hayo mabaya ya dhambi.
9. (a) Ni maswali gani yanayoweza kutusaidia kuchunguza maoni yetu kumhusu Yehova, sheria na kanuni zake? (b) Kwa nini ni muhimu kumjua Mungu vizuri?
9 Inahuzunisha kama nini kwamba vijana wengi katika kweli, hata watu wenye umri mkubwa, wamelazimika kujifunza kwa majonzi kwamba mara nyingi kufurahia dhambi kunasababisha madhara makubwa sana! (Gal. 6:7, 8) Kwa hiyo, jiulize hivi: ‘Je, ninatambua kwamba kwa kweli mbinu za Shetani ni za udanganyifu na zenye kuumiza? Je, ninamwona Yehova kuwa Rafiki yangu wa karibu zaidi, ambaye sikuzote ananiambia ukweli na anataka niwe na maisha mazuri? Je, ninasadiki kabisa kwamba Yehova hawezi kamwe kuninyima jambo ambalo kwa kweli ni zuri na litakaloniletea furaha kubwa zaidi?’ (Soma Isaya 48:17, 18.) Ili ujibu ndiyo kutoka moyoni, unahitaji kufanya mengi zaidi ya kuwa tu na ujuzi wa kijuu-juu kumhusu Yehova. Unahitaji kumjua kwa undani na kutambua kwamba sheria na kanuni za Biblia zinaonyesha kwamba anakupenda, na si kwamba anataka kukunyima uhuru.—Zab. 25:14.
SALI ILI UWE NA MOYO WENYE HEKIMA NA MTIIFU
10. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kumwiga Mfalme Sulemani alipokuwa kijana?
10 Alipokuwa angali kijana, Sulemani alisali hivi kwa unyenyekevu: ‘Mimi ni mvulana mdogo tu. Sijui jinsi ya kutoka na jinsi ya kuingia.’ Kisha akasali ili apewe moyo wenye hekima na mtiifu. (1 Fal. 3:7-9, 12) Yehova alijibu ombi hilo la unyoofu, na atajibu ombi lako pia, iwe wewe ni kijana au mzee. Bila shaka, Yehova hatakupa ufahamu na hekima kimuujiza. Lakini atakufanya uwe mwenye hekima ukijifunza kwa bidii Neno lake, ukisali ili akupe roho takatifu, na kunufaika kikamili na maandalizi ya kiroho ambayo anatoa kupitia kutaniko la Kikristo. (Yak. 1:5) Kwa kweli, Yehova anatumia njia hizo kuwafanya hata watumishi wake vijana wawe na hekima zaidi kuliko wale wote wanaopuuza mashauri yake, hata wale wanaoitwa eti “wenye hekima na walio na akili” katika ulimwengu huu.—Luka 10:21; soma Zaburi 119:98-100.
11-13. (a) Ni mambo gani muhimu tunayoweza kujifunza kutokana na Zaburi 26:4, Methali 13:20, na 1 Wakorintho 15:33? (b) Unaweza kutumiaje kanuni hizo za Kimaandiko?
11 Kwa mfano, ili uone umuhimu wa kujifunza Biblia na kutafakari kuhusu mambo tunayosoma ili tumjue Yehova kwa undani, fikiria maandiko yafuatayo. Kila andiko lina kanuni muhimu kuhusu marafiki tunaochagua: “Sikuketi na watu wasiosema kweli; wala siingii pamoja na wale wanaoficha jinsi walivyo.” (Zab. 26:4) “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” (Met. 13:20) “Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.”—1 Kor. 15:33.
12 Ni mambo gani muhimu tunayoweza kujifunza kutokana na maandiko hayo? (1) Yehova anataka tuchague marafiki wetu kwa uangalifu. Anataka kutulinda kimaadili na kiroho. (2) Watu tunaoshirikiana nao wanaweza kuwa na uvutano mzuri au mbaya juu yetu; hilo ni jambo la hakika maishani. Maandiko hayo yameandikwa kwa njia inayoonyesha kwamba Yehova anajaribu kugusa mioyo yetu. Jinsi gani? Ona kwamba hakuna andiko lolote kati ya maandiko hayo ambalo linaweka sheria, kwa kusema “hupaswi . . .” Badala yake, maandiko hayo yameandikwa kwa njia rahisi inayoonyesha ukweli. Ni kana kwamba Yehova anatuambia hivi: ‘Huu ndio ukweli wa mambo. Utaitikiaje? Ni nini kilicho moyoni mwako?’
13 Mwishowe, kwa sababu maandiko hayo matatu yametolewa yakiwa kweli za msingi, yanatumika hata sasa na yanaweza kutumika katika hali nyingi mbalimbali. Kwa mfano, jiulize maswali kama vile: Ninaweza kuepuka jinsi gani kushirikiana na watu “wanaoficha jinsi walivyo”? Ninaweza kukutana na watu wa aina hiyo katika hali gani? (Met. 3:32; 6:12) “Watu wenye hekima” ambao Yehova anataka nishirikiane nao ni nani? “Wajinga” ambao anataka niwaepuke ni nani? (Zab. 111:10; 112:1; Met. 1:7) Ni ‘tabia gani nzuri’ ambazo nitaharibu nikichagua marafiki wabaya? Je, ninaweza kupata marafiki wabaya katika ulimwengu tu? (2 Pet. 2:1-3) Ungejibuje maswali hayo?
14. Mnawezaje kuboresha jioni yenu ya Ibada ya Familia?
14 Baada ya kuchanganua Maandiko hayo, kwa nini usichunguze maandiko mengine ya Biblia ambayo yanafunua maoni ya Mungu kuhusu mambo ambayo yanakuhusu wewe au familia yako?b Wazazi, pangeni kuzungumzia mambo hayo wakati wa jioni ya Ibada yenu ya Familia. Mnapofanya hivyo, kumbukeni kwamba mradi wenu ni kumsaidia kila mshiriki wa familia kuthamini kikamili zaidi kina cha upendo wa Mungu kutuelekea kama unavyofunuliwa katika sheria na kanuni zake. (Zab. 119:72) Kwa kweli, funzo kama hilo linapaswa kuwasaidia wote katika familia wamkaribie Yehova na kuwa na uhusiano wa karibu kati yao.
15. Utajuaje ikiwa unasitawisha moyo wenye hekima na mtiifu?
15 Utajuaje ikiwa unasitawisha moyo wenye hekima na mtiifu? Njia moja ni kulinganisha njia yako ya kufikiri na ile ya watu waaminifu walioishi zamani, kama vile Mfalme Daudi, aliyeandika hivi: “Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu.” (Zab. 40:8) Pia, mwandikaji wa Zaburi 119 alisema hivi: “Jinsi ninavyoipenda sheria yako! Ndiyo ninayoihangaikia mchana kutwa.” (Zab. 119:97) Upendo wa aina hiyo haukui kwenye udongo usio na kina. Badala yake, unatokana na kujifunza kwa undani, kusali, kutafakari, na uzoefu, yaani, kuhesabu baraka nyingi sana ambazo umepata maishani kwa sababu ya kushikamana na viwango vya Mungu.—Zab. 34:8.
PIGANIA UHURU WAKO WA KIKRISTO!
16. Ni lazima tutambue nini ikiwa tunataka kushinda vita vyetu vya kupata uhuru wa kweli?
16 Katika historia yote, mataifa yamepigana vita vya kikatili yakitafuta uhuru. Basi, ni muhimu hata zaidi kwako kuwa tayari kupigana kiroho kwa ajili ya uhuru wako wa Kikristo! Tambua kwamba maadui wako si Shetani tu, ulimwengu, na roho yake yenye sumu. Ni lazima pia upigane na hali yako ya kutokamilika, kutia ndani moyo wenye hila. (Yer. 17:9; Efe. 2:3) Hata hivyo, kwa msaada wa Yehova, unaweza kushinda vita hivyo. Isitoshe, kila mara unaposhinda, iwe ni katika jambo dogo au kubwa, kuna angalau faida mbili. Kwanza, utaufanya moyo wa Yehova ushangilie. (Met. 27:11) Pili, unapoona jinsi “sheria kamilifu iliyo ya uhuru” ilivyo na nguvu za kuweka huru, utaazimia hata zaidi kuendelea kutembea katika ‘barabara nyembamba’ inayoongoza kwenye uzima wa milele. Baadaye, utafurahia uhuru mwingi zaidi ambao washikamanifu wa Yehova watapata wakati ujao.—Yak. 1:25; Mt. 7:13, 14.
17. Kwa nini hatupaswi kuvunjika moyo kwa sababu ya hali yetu ya kutokamilika, na Yehova anatusaidiaje?
17 Bila shaka, nyakati nyingine sote tunakosea. (Mhu. 7:20) Unapokosea, usivunjike moyo kupita kiasi au kuhisi kwamba hufai. Ukijikwaa, kwa njia ya mfano, simama na usonge mbele, hata ikiwa hilo linamaanisha kuwaomba msaada wazee wa kwenu. ‘Sala yao ya imani,’ akaandika Yakobo, ‘itamponya mtu asiyejisikia vizuri, na Yehova atamwinua. Pia, ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.’ (Yak. 5:15) Naam, usisahau kamwe kwamba Mungu ni mwenye rehema kwelikweli na kwamba alikuvuta katika kutaniko kwa sababu aliona sifa zako nzuri. (Soma Zaburi 103:8, 9.) Kwa hiyo, maadamu unaendelea kumtumikia Yehova kwa moyo kamili, hatakutupa kamwe.—1 Nya. 28:9.
18. Tunaweza kutendaje kupatana na sala ya Yesu katika Yohana 17:15?
18 Alipokuwa akisali usiku wake wa mwisho pamoja na mitume wake waaminifu 11, Yesu alisema maneno haya yasiyosahaulika kwa niaba yao: “Uwalinde kwa sababu ya yule mwovu.” (Yoh. 17:15) Yesu hakuwahangaikia tu mitume wake, bali pia wafuasi wake wote. Kwa hiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atajibu sala ya Yesu kwa kutulinda katika nyakati hizi za hatari. “[Yehova] ni ngao kwa wale wanaotembea kwa utimilifu . . . Atailinda njia ya washikamanifu wake.” (Met. 2:7, 8) Naam, njia ya utimilifu ina matatizo yake, lakini ndiyo njia pekee inayoongoza kwenye uzima wa milele na uhuru wa kweli. (Rom. 8:21) Usimruhusu mtu yeyote akushawishi uiache njia hiyo!
[Maelezo ya Chini]
a Ilikuwa baada ya kuzaliwa kwa Absalomu, ndipo Mungu alipompa Daudi ahadi kuhusu “uzao” ambao ungetokea wakati ujao na kurithi kiti chake cha ufalme. Kwa hiyo, bila shaka Absalomu alijua kwamba Yehova hakuwa amemchagua yeye kurithi kiti cha ufalme cha Daudi.—2 Sam. 3:3; 7:12.
b Mifano mizuri ya maandiko mnayoweza kutumia ni 1 Wakorintho 13:4-8, ambamo Paulo anafafanua upendo, na Zaburi 19:7-11, ambayo inataja baraka nyingi tunazopata tunapotii sheria za Yehova.
-