-
Jinsi Ulimwengu Huu Utakavyofikia Mwisho WakeMnara wa Mlinzi—2012 | Septemba 15
-
-
Jinsi Ulimwengu Huu Utakavyofikia Mwisho Wake
“Hamko gizani, hivi kwamba siku hiyo iwafikie ninyi kama vile ambavyo ingewafikia wezi.”—1 THE. 5:4.
1. Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kukesha na kuvumilia majaribu?
MATUKIO yenye kushtua yataitikisa dunia hivi karibuni. Kutimizwa kwa unabii mbalimbali wa Biblia kunathibitisha jambo hilo hakika, kwa hiyo tunahitaji kuendelea kukesha. Ni nini kitakachotusaidia kufanya hivyo? Mtume Paulo anatuhimiza ‘tuendelee kukaza macho yetu juu ya vitu visivyoonekana.’ Naam, tunahitaji kufikiria thawabu yetu ya uzima wa milele, iwe ni mbinguni au duniani. Kama muktadha unavyoonyesha, Paulo aliandika maneno hayo ili kuwatia moyo waamini wenzake wakazie fikira furaha watakayopata kwa sababu ya maisha yao ya uaminifu. Kufanya hivyo kungewasaidia pia kuvumilia majaribu na mateso.—2 Kor. 4:8, 9, 16-18; 5:7.
2. (a) Ni lazima tufanye nini ili tuendelee kuwa na tumaini thabiti? (b) Tutazungumzia nini katika makala hii na ile inayofuata?
2 Himizo la Paulo lina kanuni hii muhimu: Ili tuendelee kuwa na tumaini thabiti, ni lazima tukazie fikira mambo yatakayotukia hivi karibuni. Tunahitaji kukazia fikira matukio muhimu ambayo hayaonekani sasa. (Ebr. 11:1; 12:1, 2) Kwa hiyo, acheni tuchunguze matukio kumi ya wakati ujao ambayo yanahusiana sana na tumaini letu la uzima wa milele.a
NI MAMBO GANI YATAKAYOTUKIA KABLA TU YA ULE MWISHO?
3. (a) Ni jambo gani litakalotukia wakati ujao ambalo linatajwa katika 1 Wathesalonike 5:2, 3? (b) Viongozi wa kisiasa watafanya nini, na ni nani watakaojiunga nao?
3 Paulo aliandika kuhusu moja kati ya matukio hayo ya wakati ujao katika barua yake kwa Wathesalonike. (Soma 1 Wathesalonike 5:2, 3.) Anavuta uangalifu juu ya “siku ya Yehova.” Katika andiko hilo, maneno “siku ya Yehova” yanarejelea kipindi kitakachoanza wakati dini ya uwongo itakapoharibiwa na kufikia kilele chake katika vita vya Har–Magedoni. Hata hivyo, kabla tu ya siku ya Yehova kuanza, viongozi wa ulimwengu watakuwa wakisema “Amani na usalama!” Huenda hilo likarejelea tukio moja au mfuatano wa matukio. Huenda mataifa yakafikiri kwamba yako karibu kusuluhisha baadhi ya matatizo yao makubwa. Namna gani kuhusu viongozi wa kidini? Wao ni sehemu ya ulimwengu, kwa hiyo inawezekana kwamba watajiunga na viongozi wa kisiasa. (Ufu. 17:1, 2) Kwa kufanya hivyo, viongozi hao wa kidini watakuwa wanawaiga manabii waongo wa kale wa Yuda. Yehova alisema hivi kuhusu manabii hao: ‘Wanasema, “Kuna amani! Kuna amani!” wakati hakuna amani.’—Yer. 6:14; 23:16, 17.
4. Tofauti na watu wengi, sisi tunatambua nini?
4 Haidhuru ni nani watakaoshiriki kusema “Amani na usalama!” tukio hilo litaonyesha kwamba siku ya Yehova iko karibu kuanza. Ndiyo sababu Paulo alisema hivi: “Akina ndugu, hamko gizani, hivi kwamba siku hiyo iwafikie ninyi kama vile ambavyo ingewafikia wezi, kwa maana ninyi nyote ni wana wa nuru.” (1 The. 5:4, 5) Tofauti na watu wengi, sisi tunatambua maana ya Kimaandiko ya matukio ya sasa. Unabii huu kuhusu tangazo la “Amani na usalama!” utatimia jinsi gani hasa? Ni lazima tungoje ili tuone jinsi itakavyokuwa. Kwa hiyo, acheni tuazimie ‘kukaa macho na kutunza akili zetu.’—1 The. 5:6; Sef. 3:8.
“MALKIA” AMBAYE HAJUI KWAMBA ATAHARIBIWA
5. (a) “Dhiki kuu” itaanzaje? (b) Ni “malkia” yupi ambaye hajui kwamba ataharibiwa?
5 Ni tukio gani lisiloonekana litakalofuata baadaye? Paulo alisema hivi: “Wakati watakapokuwa wakisema: ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa juu yao mara moja.” Sehemu ya kwanza ya ‘uharibifu huo wa ghafula’ ni shambulio dhidi ya “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, inayojulikana pia kuwa “yule kahaba.” (Ufu. 17:5, 6, 15) Shambulio hilo dhidi ya aina zote za dini ya uwongo, kutia ndani dini zinazodai kuwa za Kikristo, litakuwa mwanzo wa “dhiki kuu.” (Mt. 24:21; 2 The. 2:8) Tukio hilo litawashtua watu wengi. Kwa nini? Kwa sababu kufikia wakati huo, kahaba huyo atajiona kwa uhakika kuwa “malkia” ambaye ‘hataona maombolezo kamwe.’ Lakini atagundua kwa ghafla kwamba hakujua kuwa ataharibiwa. Hata hivyo, ataharibiwa haraka sana kana kwamba ni “katika siku moja.”—Ufu. 18:7, 8.
6. Ni nani atakayeiharibu dini ya uwongo?
6 Neno la Mungu linamtambulisha mshambuliaji wa kahaba huyo kuwa “mnyama-mwitu” mwenye “pembe kumi.” Uchunguzi wa kitabu cha Ufunuo unaonyesha kwamba huyo mnyama-mwitu anafananisha Umoja wa Mataifa (UM). “Zile pembe kumi” zinafananisha serikali zote za kisiasa zilizopo sasa zinazomuunga mkono ‘mnyama-mwitu huyo mwenye rangi nyekundu.’b (Ufu. 17:3, 5, 11, 12) Shambulio hilo litakuwa kubwa kadiri gani? Mataifa ya UM yatapora utajiri wa kahaba huyo, yatafunua jinsi alivyo mwovu kikweli, yatamrarua, na “kumteketeza kabisa kwa moto.” Uharibifu wake utakuwa wa milele.—Soma Ufunuo 17:16.
7. Ni nini kitakachosababisha shambulio la “mnyama-mwitu”?
7 Unabii wa Biblia unaonyesha pia kile kitakachosababisha shambulio hilo. Kwa njia fulani, Yehova atatia wazo hilo ndani ya mioyo ya watawala wa kisiasa “ili kutekeleza wazo lake,” yaani, kumharibu kahaba huyo. (Ufu. 17:17) Dini inachochea vita na kuendelea kusababisha mvurugo ulimwenguni; kwa hiyo, huenda mataifa yakahisi kwamba yatanufaika yakimharibu kahaba huyo. Kwa kweli, watawala watakaposhambulia, watafikiri kwamba wanatimiza “wazo lao moja.” Hata hivyo, ukweli ni kwamba Mungu atawatumia kama vyombo vya kuharibu kabisa dini yote ya uwongo. Hivyo, katika hali isiyotarajiwa, sehemu moja ya mfumo wa Shetani itaishambulia ile sehemu nyingine, na Shetani hatakuwa na uwezo wa kuzuia jambo hilo.—Mt. 12:25, 26.
SHAMBULIO DHIDI YA WATU WA MUNGU
8. Shambulio la “Gogu wa nchi ya Magogu” ni nini?
8 Baada ya dini ya uwongo kuharibiwa, bado watumishi wa Mungu wataonekana kuwa ‘wanakaa kwa usalama’ na “bila ukuta.” (Eze. 38:11, 14) Ni nini kitakachotukia kwa kikundi hicho cha watu wanaoonekana kuwa bila ulinzi na wanaoendelea kumwabudu Yehova? Inaelekea kwamba watakuwa shabaha ya shambulio la “vikundi vingi vya watu.” Neno la Mungu linasema kwamba tukio hilo litakuwa shambulio la “Gogu wa nchi ya Magogu.” (Soma Ezekieli 38:2, 15, 16.) Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu shambulio hilo?
9. (a) Hangaiko kuu la Mkristo ni nini? (b) Ni hatua zipi tunazopaswa kuchukua sasa ili kuimarisha imani yetu?
9 Kujua kimbele kuhusu shambulio hilo dhidi ya watu wa Mungu hakutufanyi tuwe na wasiwasi kupita kiasi. Badala yake, hangaiko letu kuu si wokovu wetu, bali ni kutakaswa kwa jina la Yehova na kutetewa kwa enzi yake kuu. Kwa kweli, Yehova alitangaza hivi zaidi ya mara 60: “Mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.” (Eze. 6:7) Hivyo, tunatazamia kwa hamu sana kutimizwa kwa sehemu hiyo muhimu ya unabii wa Ezekieli, huku tukiwa na uhakika wa kwamba “Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu.” (2 Pet. 2:9) Kwa sasa, tunahitaji kutumia kila fursa kuimarisha imani yetu ili tuendelee kushika utimilifu wetu kwa Yehova licha ya matatizo tutakayokabili. Tunapaswa kufanya nini? Tunapaswa kusali, kujifunza na kutafakari Neno la Mungu, na kuwahubiria wengine ujumbe wa Ufalme. Kwa kufanya hivyo, tunaendelea kuwa na tumaini la uzima wa milele ambalo ni thabiti kama “nanga.”—Ebr. 6:19; Zab. 25:21.
MATAIFA YATALAZIMIKA KUMTAMBUA YEHOVA
10, 11. Ni nini itakayokuwa ishara ya kuanza kwa Har–Magedoni, na ni nini kitakachotukia wakati huo?
10 Ni tukio gani lenye kushtua litakalosababishwa na shambulio dhidi ya watumishi wa Yehova? Yehova, kupitia Yesu na majeshi ya kimbingu, ataingilia kati kwa ajili ya watu Wake. (Ufu. 19:11-16) Hatua hiyo ya kuingilia kati ndiyo itakayokuwa “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote,” yaani, Har–Magedoni.—Ufu. 16:14, 16.
11 Kuhusu vita hivyo, Yehova anatangaza hivi kupitia Ezekieli: “‘Nitaita upanga juu [ya Gogu] kotekote katika eneo langu lote lenye milima,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. ‘Upanga wa kila mmoja utakuwa juu ya ndugu yake.’ ” Wale walio upande wa Shetani wataingiwa na hofu kubwa na kuanza kuuana wenyewe kwa wenyewe, yaani, mpiganaji dhidi ya mpiganaji mwenzake. Hata hivyo, Shetani pia atashambuliwa. Yehova anasema hivi: “Nitanyesha . . . moto na kiberiti juu [ya Gogu] na juu ya vikosi vyake na juu ya vikundi vingi vya watu vitakavyokuwa pamoja naye.” (Eze. 38:21, 22) Kutakuwa na matokeo gani Mungu atakapochukua hatua hiyo?
12. Mataifa yatalazimika kutambua nini?
12 Mataifa yatalazimika kutambua kwamba Yehova ndiye aliyetoa amri ili yapondwe na kushindwa. Kisha, kama jeshi la kale la Misri lililowafuatilia Waisraeli kwenye Bahari Nyekundu lilivyolia, huenda majeshi ya Shetani yakalia hivi kwa kukata tamaa: “Hakika Yehova anawapigania”! (Kut. 14:25) Naam, mataifa yatalazimika kumtambua Yehova. (Soma Ezekieli 38:23.) Tuko karibu kadiri gani kuona mwanzo wa mfuatano wa matukio hayo?
HAKUNA SERIKALI NYINGINE KUU YA ULIMWENGU ITAKAYOTOKEA
13. Tunajua nini kuhusu sehemu ya tano ya sanamu ambayo Danieli anafafanua?
13 Unabii mmoja katika kitabu cha Danieli unatuwezesha kujua tuko wapi katika mkondo wa wakati. Danieli anafafanua sanamu ya umbo la kibinadamu ambayo inafanyizwa kutokana na madini mbalimbali. (Dan. 2:28, 31-33) Sanamu hiyo inafananisha mfuatano wa serikali kuu za ulimwengu ambazo zilikuwa na uvutano mkubwa juu ya watu wa Mungu, zamani na sasa. Serikali hizo ni Babiloni, Umedi na Uajemi, Ugiriki, Roma, na serikali kuu ya mwisho ambayo inatawala sasa. Uchunguzi wa unabii wa Danieli unaonyesha kwamba serikali hii kuu ya mwisho ya ulimwengu inafananishwa na miguu na vidole vya sanamu hiyo. Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, Uingereza na Marekani zilianzisha ushirikiano wa pekee. Naam, sehemu ya tano ya sanamu ya Danieli ni Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Miguu ndiyo sehemu ya mwisho ya sanamu hiyo, na hilo linaonyesha kwamba hakuna serikali nyingine kuu ya kibinadamu itakayotokea baada ya serikali hiyo. Miguu na vidole vimefanyizwa kwa chuma na udongo, kuonyesha kwamba Muungano wa Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani umedhoofika.
14. Ni serikali gani kuu ya ulimwengu itakayokuwa ikitawala vita vya Har–Magedoni vitakapoanza?
14 Unabii huohuo unaonyesha kwamba Ufalme wa Mungu, unaofananishwa na jiwe kubwa, ulikatwa kutoka kwenye mlima wa enzi kuu ya Yehova katika mwaka wa 1914. Jiwe hilo sasa linasonga kwa kasi sana ili kugonga shabaha yake, yaani, miguu ya sanamu hiyo. Katika vita vya Har–Magedoni, miguu na sehemu nyingine za sanamu hiyo zitapondwa kabisa. (Soma Danieli 2:44, 45.) Kwa hiyo, Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani bado itakuwa serikali kuu wakati vita vya Har–Magedoni vitakapoanza. Itasisimua kama nini kuona unabii huo ukitimizwa kikamili!c Hata hivyo, Yehova atamchukulia Shetani hatua gani?
HATUA AMBAYO MUNGU ATAMCHUKULIA ADUI YAKE MKUU
15. Baada ya Har–Magedoni, itakuwaje kwa Shetani na roho wake waovu?
15 Kwanza, Shetani atashuhudia tangu mwanzo hadi mwisho tengenezo lake lote duniani likiangamizwa. Kisha, Shetani mwenyewe ataelekezewa fikira. Mtume Yohana anaripoti kinachofuata. (Soma Ufunuo 20:1-3.) Yesu Kristo, ambaye ni “malaika . . . mwenye ufunguo wa abiso,” atamshika Shetani na roho wake waovu na kuwatupa ndani ya abiso, kisha atawafungia humo kwa miaka elfu moja. (Luka 8:30, 31; 1 Yoh. 3:8) Tendo hilo ni hatua ya kwanza ya kukiponda kichwa cha yule nyoka.d—Mwa. 3:15.
16. Itamaanisha nini kwa Shetani kuwa ndani ya “abiso”?
16 “Abiso” ambamo Shetani na roho wake waovu watatupwa ni nini? Neno la Kigiriki aʹbys·sos linalotumiwa na Yohana linamaanisha “-enye kina sana au kina kisicho cha kawaida.” Linatafsiriwa pia kuwa “shimo lisilo na mwisho,” “lisilo na mipaka,” na “lisilo na kikomo.” Kwa hiyo, ni mahali ambapo hapawezi kufikiwa na mtu yeyote yule isipokuwa Yehova tu na malaika wake aliyewekwa rasmi “mwenye ufunguo wa abiso.” Humo, Shetani atakuwa katika hali ya kutotenda kama ya mfu ili “asipotoshe mataifa tena.” Kwa kweli, ‘simba huyo anayenguruma’ atanyamazishwa!—1 Pet. 5:8.
MATUKIO YANAYOONGOZA KWENYE KIPINDI CHA AMANI
17, 18. (a) Kufikia hapa, tumezungumzia matukio gani ambayo hayajaonekana? (b) Baada ya matukio hayo, tutafurahia kipindi gani cha wakati?
17 Matukio muhimu yatakayoitikisa dunia yako mbele yetu. Tunatazamia kuona jinsi tangazo la “Amani na usalama! ” litakavyotolewa. Kisha, tutashuhudia uharibifu wa Babiloni Mkubwa, shambulio la Gogu wa Magogu, vita vya Har–Magedoni, na kutupwa kwa Shetani na roho wake waovu ndani ya abiso. Baada ya matukio hayo, na uovu wote utakapokuwa umetoweka, tutaingia katika kipindi kipya cha maisha, yaani, Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo, wakati tutakapofurahia “wingi wa amani.”—Zab. 37:10, 11.
18 Zaidi ya matukio hayo matano ambayo tumechunguza kufikia hapa, bado kuna ‘vitu vingine visivyoonekana’ ambavyo tunapaswa ‘kuendelea kuvikazia macho.’ Matukio hayo yatazungumziwa katika makala inayofuata.
a Matukio hayo kumi yanazungumziwa katika makala hii na ile inayofuata.
b Tazama kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu! ukurasa wa 251-258.
c Maneno “kuzikomesha falme hizi zote” yaliyo katika Danieli 2:44 yanarejelea falme, au serikali kuu za ulimwengu, zinazofananishwa na sehemu mbalimbali za sanamu hiyo. Hata hivyo, unabii mwingine wa Biblia kama huo unaonyesha kwamba “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa” watajipanga dhidi ya Yehova katika “siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” (Ufu. 16:14; 19:19-21) Kwa hiyo, si falme zinazofananishwa na sanamu hiyo tu zitakazoharibiwa kwenye Har–Magedoni bali pia falme nyingine zote za ulimwengu huu.
d Kichwa cha yule nyoka kitapondwa kwa mara ya mwisho baada ya ile miaka miaka elfu moja wakati Shetani na roho wake waovu wanapotupwa ndani ya “lile ziwa la moto na kiberiti.”—Ufu. 20:7-10; Mt. 25:41.
-
-
Amani Kwa Muda Wa Miaka Elfu Moja Na Kuendelea!Mnara wa Mlinzi—2012 | Septemba 15
-
-
Amani Kwa Muda Wa Miaka Elfu Moja Na Kuendelea!
“Ili Mungu awe vitu vyote kwa kila mtu.”—1 KOR. 15:28.
1. Ni tarajio gani lenye kusisimua ambalo “umati mkubwa” unangojea?
JE, UNAWEZA kuwazia mambo yote mazuri ambayo serikali yenye nguvu chini ya uongozi wa mtawala mwenye haki na huruma inaweza kuwafanyia raia wake kwa muda wa miaka elfu moja? “Umati mkubwa” usio na hesabu, yaani, waokokaji wa “ile dhiki kuu,” wanangojea matukio mazuri yatakayokomesha kabisa mfumo huu mwovu wa mambo wa sasa.—Ufu. 7:9, 14.
2. Wanadamu wamepatwa na nini kwa muda wa miaka 6,000 iliyopita?
2 Kwa muda wa miaka 6,000 iliyopita, wanadamu wamejaribu kujitegemea na kujitawala wenyewe, na jambo hilo limewaletea maumivu na mateso makali. Biblia ilisema hivi zamani: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.” (Mhu. 8:9) Tunaona nini leo? Mbali na vita na machafuko ya kijamii, kuna matatizo makubwa ya umaskini, magonjwa, uharibifu wa mazingira, mabadiliko ya hali ya hewa, na kadhalika. Maofisa wa serikali wameonya kwamba tusipobadili mtazamo wetu wa kutojali, matokeo yatakuwa mabaya sana.
3. Utawala wa ile Miaka Elfu Moja utaleta nini?
3 Chini ya uongozi wa Mfalme wa Kimasihi Yesu Kristo na wale 144,000 ambao watatawala pamoja naye, Ufalme wa Mungu utaondoa hatua kwa hatua madhara yote ambayo wanadamu wamepata na kurekebisha makao yao, Dunia. Wakati wa Utawala wa ile Miaka Elfu Moja, ahadi hii ya Yehova Mungu yenye kuchangamsha moyo itatimia: “Mimi ninaumba mbingu mpya na dunia mpya; na mambo ya zamani hayatakumbukwa akilini, wala hayataingia moyoni.” (Isa. 65:17) Hata hivyo, ni matukio gani mazuri ajabu yasiyoonekana tunayongojea? Kwa msaada wa Neno la Mungu la kinabii, acheni tupate picha ya mambo hayo mazuri ajabu ambayo ‘hayajaonekana.’—2 Kor. 4:18.
‘WATAJENGA NYUMBA NA KUPANDA MASHAMBA YA MIZABIBU’
4. Watu wengi leo wanaishi katika nyumba za aina gani?
4 Ni nani hangependa kuwa na nyumba yake mwenyewe, ambamo yeye na familia yake wangehisi wakiwa salama salimini? Hata hivyo, katika ulimwengu wa leo, ni vigumu sana kupata makao mazuri. Watu wanasongamana katika majiji yaliyojaa watu. Wengi wanaishi katika makao ya muda ya watu maskini na mitaa ya mabanda. Ni ndoto tu kwa watu hao kuwa na nyumba yao wenyewe.
5, 6. (a) Maandiko ya Isaya 65:21 na Mika 4:4 yatatimiaje? (b) Tunawezaje kupata baraka hizo?
5 Chini ya utawala wa Ufalme, tamaa ya kila mkaaji ya kuwa na nyumba yake mwenyewe itatoshelezwa, kwa kuwa ilitabiriwa hivi kupitia Isaya: “Hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake.” (Isa. 65:21) Hata hivyo, mbali na mtu kuwa na nyumba yake mwenyewe kuna matarajio mengine. Baadhi ya watu leo wanaishi katika nyumba zao wenyewe, wachache hata wana nyumba za kifahari. Lakini sikuzote wana wasiwasi kwamba wataipoteza nyumba yao kwa sababu ya kuporomoka kwa thamani ya pesa au wanaogopa kwamba wataibiwa. Kila kitu kitakuwa tofauti kama nini chini ya utawala wa Ufalme! Nabii Mika aliandika hivi: “Wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, wala hakutakuwa na mtu yeyote anayewatetemesha.”—Mika 4:4.
6 Tukiwa na tarajio hilo zuri ajabu akilini, tunapaswa kufanya nini? Bila shaka, sisi sote tunahitaji nyumba nzuri. Hata hivyo, badala ya kujitahidi kupata nyumba tunayotamani sasa, labda kwa kuchukua mikopo mikubwa, je, halingekuwa jambo la hekima kwetu kukazia fikira ahadi ya Yehova? Kumbuka yale ambayo Yesu alisema kujihusu: “Mbweha wana mapango na ndege wa mbinguni wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake.” (Luka 9:58) Yesu alikuwa na uwezo na nguvu za kujenga au kupata nyumba nzuri sana kuliko mtu mwingine yeyote. Kwa nini hakufanya hivyo? Ni wazi kwamba Yesu alitaka kuepuka jambo lolote ambalo lingemkengeusha fikira na kumsonga na hivyo kumzuia asitangulize Ufalme. Je, tunaweza kufuata mfano wake na kuendelea kuwa na jicho rahisi, yaani, kutojiruhusu tusongwe na upendo wa vitu vya kimwili na mahangaiko?—Mt. 6:33, 34.
“MBWA-MWITU NA MWANA-KONDOO WATALISHA KAMA KITU KIMOJA”
7. Mwanzoni Yehova alikusudia kuwe na uhusiano gani kati ya wanadamu na wanyama?
7 Alipokuwa akiumba, Yehova aliwaumba wanadamu mwisho na walikuwa ndio uumbaji bora zaidi kati ya kazi zake za kidunia. Yehova alimwambia Stadi wake wa Kazi, Mwanawe mzaliwa wa kwanza, kusudi lake hususa: “Na tufanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu, nao watawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na wanyama wa kufugwa na dunia yote na kila mnyama anayetembea juu ya dunia.” (Mwa. 1:26) Kwa hiyo, Adamu na Hawa, na hatimaye wanadamu wote, waliamriwa watawale wanyama.
8. Kwa kawaida wanyama wanaonyesha tabia gani leo?
8 Je, kweli wanadamu wanaweza kuwatiisha wanyama wote na kuishi nao kwa amani? Watu wengi wana uhusiano wa karibu sana na wanyama wanaowapenda, kama vile mbwa na paka. Hata hivyo, namna gani kuhusu wanyama-mwitu? Ripoti moja inasema hivi: “Wanasayansi ambao wameishi kwa ukaribu pamoja na wanyama-mwitu na ambao wamejifunza kuwahusu, wamegundua kwamba wanyama wote wana hisia.” Bila shaka, tunaona wanyama wakiogopa au kukasirika wanapotishwa, lakini je, wanaweza kuonyesha hisia nyororo? Ripoti hiyo inaendelea kusema hivi: “Wanyama hufunua sifa yao kuu zaidi, yaani, uwezo wao mkubwa wa kuonyesha upendo mchangamfu hasa wanapowalea watoto wao.”
9. Tunaweza kutazamia mabadiliko gani kuhusiana na wanyama?
9 Kwa hiyo, hatupaswi kushangaa tunaposoma katika Biblia kwamba kutakuwa na amani kati ya wanadamu na wanyama. (Soma Isaya 11:6-9; 65:25.) Kwa nini? Kumbuka kwamba Noa na familia yake walipotoka ndani ya safina baada ya Gharika, Yehova aliwaambia hivi: “Kila kiumbe hai cha dunia na kila kiumbe kinachoruka cha mbinguni kitawahofu.” Kwa hiyo, wanyama walipaswa kuwahofu wanadamu ili kujilinda. (Mwa. 9:2, 3) Je, Yehova hataweza kuondoa kwa kiasi fulani hofu na woga huo ili uhusiano kati ya wanadamu na wanyama uwe kama alivyokusudia mwanzoni? (Hos. 2:18) Wote watakaookoka na kuishi duniani watafurahia maisha kama nini!
“ATAFUTA KILA CHOZI”
10. Kwa nini mara nyingi wanadamu hutokwa na machozi?
10 Sulemani alipoona “matendo yote ya uonevu yanayofanywa chini ya jua,” aliomboleza hivi: “Tazama! machozi ya wale wanaokandamizwa, lakini hawakuwa na mtu wa kuwafariji.” (Mhu. 4:1) Leo mambo yako vivyo hivyo, au ni mabaya hata zaidi. Ni nani kati yetu hajawahi kutokwa na machozi kwa sababu fulani? Ni kweli kwamba nyakati nyingine machozi hayo yanaweza kuwa ya shangwe. Hata hivyo, kwa ujumla, tunatokwa na machozi kwa sababu mioyo yetu imejaa huzuni.
11. Ni simulizi gani la Biblia ambalo hasa linakugusa moyo?
11 Kumbuka masimulizi mengi yenye kugusa moyo na hisia tunayosoma katika Biblia. Sara alipokufa akiwa na umri wa miaka 127, ‘Abrahamu aliingia ndani kumwombolezea Sara na kumlilia.’ (Mwa. 23:1, 2) Naomi alipowaaga mabinti-wakwe zake wawili wajane, “wakaanza kupaaza sauti zao na kulia,” na kisha “wakapaaza sauti zao na kulia tena.” (Rut. 1:9, 14) Mfalme Hezekia alipokuwa mgonjwa na kujua kwamba hakika angekufa, alisali kwa Mungu na “akaanza kulia sana,” jambo lililomgusa moyo Yehova. (2 Fal. 20:1-5) Na ni nani asiyeguswa moyo na simulizi kuhusu mtume Petro akimkana Yesu? Aliposikia jogoo akiwika, Petro “akaenda nje akalia kwa uchungu.”—Mt. 26:75.
12. Utawala wa Ufalme utawaleteaje wanadamu kitulizo cha kweli?
12 Kwa sababu ya matukio yenye kuhuzunisha yanayotupata, makubwa na madogo, wanadamu wanahitaji sana faraja na kitulizo. Hayo ndiyo mambo ambayo Utawala wa Miaka Elfu Moja utawaletea raia wake: “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufu. 21:4) Ni jambo zuri ajabu kujua kwamba maombolezo, kilio, na maumivu hayatakuwapo tena. Mungu anaahidi pia kuondoa kabisa adui mkuu wa wanadamu, yaani, kifo. Hilo litatukiaje?
‘WALE WOTE WALIOMO NDANI YA MAKABURI YA UKUMBUSHO WATATOKA’
13. Kifo kimewaathirije wanadamu tangu Adamu atende dhambi?
13 Tangu Adamu atende dhambi, kifo kimetawala kama mfalme juu ya wanadamu. Kifo kimekuwa adui asiyeshindwa, mwisho usioepukika wa wanadamu wenye dhambi, chanzo cha majonzi na huzuni isiyo na kifani. (Rom. 5:12, 14) Kwa kweli, kwa sababu ya “kuogopa kifo,” mamilioni ya watu “wametiishwa chini ya utumwa katika maisha yao yote.”—Ebr. 2:15.
14. Ni nini kitakachotukia kifo kitakapoondolewa?
14 Biblia inataja kwamba wakati utakuja ambapo “adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.” (1 Kor. 15:26) Tunaweza kutaja vikundi viwili vitakavyofaidika na jambo hilo. Wale wa “umati mkubwa,” wanaoishi sasa wataweza kuokoka na kuingia katika ulimwengu mpya ulioahidiwa wakitarajia kupata uzima usio na mwisho. Na mabilioni ya watu ambao tayari wamekufa, wataweza kufufuliwa. Je, unaweza kuwazia shangwe na msisimuko utakaokuwapo wakati “umati mkubwa” utakapowakaribisha wale wanaofufuliwa? Kuchunguza kwa makini baadhi ya masimulizi ya Biblia kuhusu ufufuo kunaweza kutusaidia kuelewa jinsi hali itakavyokuwa wakati huo.—Soma Marko 5:38-42; Luka 7:11-17.
15. Inaelekea utatendaje ukimwona mpendwa wako akifufuliwa na kuishi tena?
15 Fikiria maneno “wakawa na shangwe kubwa” na “wakaanza kumtukuza Mungu.” Ikiwa ungekuwepo wakati huo, labda ungehisi vivyo hivyo. Kwa kweli, tutasisimuka sana kwa shangwe na furaha tutakapoona wapendwa wetu waliokufa wakifufuliwa na kuishi tena. Yesu alisema hivi: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.” (Yoh. 5:28, 29) Hakuna yeyote kati yetu aliyewahi kuona jambo kama hilo likitendeka; bila shaka litakuwa mojawapo ya mambo makubwa zaidi kati ya “vitu visivyoonekana.”
MUNGU ATAKUWA “VITU VYOTE KWA KILA MTU”
16. (a) Kwa nini tunapaswa kuzungumzia kwa shauku baraka ambazo bado hatujaziona? (b) Paulo alisema nini ili kuwatia moyo Wakristo wa Korintho?
16 Naam, wakati ujao wenye utukufu unawangojea wale ambao ni waaminifu kwa Yehova katika nyakati hizi ngumu! Hata ingawa bado hatujaziona baraka hizo kubwa za wakati ujao, kuendelea kuzifikiria kutatusaidia kukazia akili mambo yaliyo muhimu kwelikweli na kuepuka kukengeushwa na mambo ya muda tu yanayovutia ya mfumo huu wa mambo. (Luka 21:34; 1 Tim. 6:17-19) Wakati wa funzo na ibada ya familia, katika mazungumzo pamoja na waamini wenzetu, na katika mazungumzo pamoja na wanafunzi wa Biblia na wale wanaopendezwa, acheni tuzungumzie kwa shauku tumaini na tarajio letu zuri ajabu. Kufanya hivyo kutafanya mambo hayo yawe wazi katika akili na mioyo yetu. Mtume Paulo alifanya vivyo hivyo alipowatia moyo Wakristo wenzake. Maneno yake yaliwasaidia kupiga picha akilini mambo ambayo yangetukia mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo. Jaribu kuwazia maana kamili ya maneno ya Paulo katika 1 Wakorintho 15:24, 25, 28.—Soma.
17, 18. (a) Ni katika njia gani Yehova alikuwa “vitu vyote kwa kila mtu” mwanzoni mwa historia ya wanadamu? (b) Yesu atafanya nini ili kurudisha umoja na upatano?
17 Hakuna maneno yanayoweza kueleza kwa njia bora zaidi jinsi maisha yatakavyokuwa mwishoni mwa ile miaka elfu moja kuliko haya: “Ili Mungu awe vitu vyote kwa kila mtu.” Hilo linamaanisha nini? Fikiria jinsi mambo yalivyokuwa katika Edeni wakati wanadamu wakamilifu, Adamu na Hawa, walipokuwa sehemu ya familia ya Yehova ya ulimwenguni pote yenye amani na upatano. Yehova, Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, alitawala moja kwa moja juu ya uumbaji wake wote, malaika na wanadamu. Waliweza kuwasiliana naye kibinafsi na kumwabudu, naye aliwabariki. Mungu alikuwa “vitu vyote kwa kila mtu.”
18 Uhusiano huo mzuri uliharibika wakati ambapo wanadamu, wakichochewa na Shetani, waliasi enzi kuu ya Yehova. Hata hivyo, tangu mwaka wa 1914, Ufalme wa Kimasihi umekuwa ukipiga hatua ili kurudisha tena amani na upatano. (Efe. 1:9, 10) Wakati wa ule Utawala wa Miaka Elfu Moja, mambo mazuri ajabu ambayo sasa ‘hayaonekani’ yatakuwa halisi. Kisha “ule mwisho” utakuja, yaani, mwisho wa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo. Baadaye kutatokea nini? Ingawa amepewa “mamlaka yote mbinguni na duniani,” Yesu hataki makuu. Hana nia ya kunyakua cheo cha Yehova. Kwa unyenyekevu, ‘anamkabidhi ufalme Mungu wake ambaye pia ni Baba yake.’ Atatumia cheo chake cha pekee na mamlaka “kwa utukufu wa Mungu.”—Mt. 28:18; Flp. 2:9-11.
19, 20. (a) Raia wote wa Ufalme wataonyeshaje kwamba wanaikubali enzi kuu ya Yehova? (b) Ni tarajio gani kubwa ambalo tunangojea?
19 Wakati huo, raia wa kidunia wa Ufalme watakuwa wamefanywa kuwa wakamilifu. Watafuata mfano wa Yesu na watatambua kwa unyenyekevu na kwa hiari enzi kuu ya Yehova. Watakuwa na fursa ya kuonyesha tamaa yao ya kutambua enzi kuu ya Yehova kwa kufanikiwa kupita lile jaribu la mwisho. (Ufu. 20:7-10) Kisha, waasi wote, yaani, wanadamu na roho waovu, wataharibiwa milele. Huo utakuwa wakati wenye shangwe na furaha kama nini! Familia ya Yehova ya ulimwenguni pote itamsifu kwa furaha, kwa sababu Yehova atakuwa “vitu vyote kwa kila mtu.”—Soma Zaburi 99:1-3.
20 Je, mambo hayo mazuri ajabu ambayo Ufalme utaleta hivi karibuni yatakuchochea kukazia fikira mapenzi ya Mungu na kujitahidi kuyafanya? Je, unaweza kuepuka kukengeushwa fikira na faraja na tumaini la uwongo ambalo ulimwengu wa Shetani unatoa? Je, utaimarisha azimio lako la kuunga mkono na kuitegemeza enzi kuu ya Yehova? Matendo yako na yathibitishe kwamba unatamani kufanya hivyo milele. Kisha, utakuwa na pendeleo la kufurahia amani na ufanisi kwa muda wa miaka elfu moja na kuendelea!
-