-
Kuhubiri na Kufundisha Duniani Kote2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Fiji
[Picha katika ukurasa wa 63]
Kijana anayeitwa Viliame, alikuwa mchezaji stadi wa mpira wa raga naye alitamani sana kuchezea timu ya taifa. Ndugu yake, anayeitwa Leone, alitaka pia kuwa mchezaji wa raga, lakini baada ya kukubali kujifunza Biblia na painia mmoja wa pekee, akaona kwamba hawezi kutumikia mabwana wawili. Alianza kuhudhuria mikutano naye akaacha kucheza raga. Mama yake ambaye ni Shahidi, alimnunulia nguo za mikutano, lakini walipozozana, Viliame alichukua nguo hizo za Leone na kuzirarua. Leone alivunjika moyo sana, lakini hakulipiza kisasi. Baadaye, Leone alienda kuuza matikiti sokoni, naye akatumia kiasi fulani cha pesa alizopata kununua nguo za mkutano, Biblia na kalamu. Alimnunulia Viliame pia. Akikumbuka jinsi alivyomtendea ndugu yake, Viliame aliguswa moyo sana na matendo ya fadhili ya ndugu yake. Alivaa nguo zake mpya na kumshangaza ndugu yake kwa kuhudhuria mkutano. Pia, Viliame alikubali kujifunza Biblia, nao ndugu hao wawili wakafanya maendeleo ya kiroho. Walipokuwa wakijiandaa kwa ajili ya ubatizo, Viliame alipewa nafasi nzuri ya kucheza raga Ulaya, nafasi ambayo vijana wengi huitamani, kwa sababu ina donge nono na umaarufu mkubwa. Hata hivyo, miradi yake ilikuwa imebadilika naye akaamua kujiweka wakfu kwa Yehova. Viliame na Leone walitumikia wakiwa mapainia wasaidizi kwa miezi sita baada tu ya kubatizwa. Alipoona mwenendo mzuri wa watoto wake, Waisea, baba yao aliamua pia kujifunza Biblia. Waisea alifanya mabadiliko makubwa akabatizwa pamoja na binti zake wawili kwenye kusanyiko la siku ya pekee.
-
-
Kuhubiri na Kufundisha Duniani Kote2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 64]
Walikataa kazi ya kucheza raga yenye donge nono nao wakaamua kumtumikia Yehova
-