-
Ulimwengu Mzima Waharibiwa!Mnara wa Mlinzi—2002 | Machi 1
-
-
Ulimwengu Mzima Waharibiwa!
Unapotazama ulimwengu huu wenye majiji, utamaduni, mafanikio ya kisayansi, na mabilioni ya watu, ni rahisi kufikiri kwamba utadumu. Je, unafikiri kwamba siku moja ulimwengu huu unaweza kutoweka kabisa? Huenda ikawa vigumu kwako kuwazia jambo hilo. Hata hivyo, je unajua kwamba kulingana na chanzo chenye kutegemeka, kulikuwa na ulimwengu mwingine ambao uliharibiwa kabisa?
HATUZUNGUMZII ulimwengu wa makabila yasiyostaarabika. Ulimwengu ulioangamia ulikuwa umesitawi sana na ulikuwa na majiji, sanaa, na ujuzi wa kisayansi. Hata hivyo, rekodi ya Biblia hutuambia kwamba katika siku ya 17 ya mwezi wa 2, miaka 352 kabla ya kuzaliwa kwa mzee wa ukoo Abrahamu, gharika ilianza ghafula na kuangamiza ulimwengu mzima.a
Je, rekodi hiyo ni sahihi? Je, kweli gharika hiyo ilitokea? Je, kweli kulikuwa na ulimwengu wa kale kabla ya ulimwengu wa sasa ambao ulisitawi kisha ukaharibiwa? Ikiwa ndivyo, kwa nini uliharibiwa? Tatizo lilikuwa nini? Na tunaweza kujifunza chochote kutokana na kuharibiwa kwa ulimwengu huo?
Je, Kweli Kuna Ulimwengu wa Kale Ulioharibiwa?
Ikiwa kwa kweli msiba mkubwa kama huo ulitokea, basi haungeweza kusahaulika kamwe. Kwa hiyo, katika nchi nyingi kuna mambo yanayotukumbusha uharibifu huo. Kwa mfano, fikiria tarehe kamili iliyorekodiwa katika Maandiko. Mwezi wa pili wa kalenda ya kale ulianza katikati ya Oktoba na kumalizika katikati ya Novemba kulingana na kalenda ya siku hizi. Kwa hiyo siku ya 17 inakaribiana sana na siku ya kwanza ya mwezi wa Novemba. Hivyo, huenda haikutukia tu kwamba katika nchi nyingi watu hufanya sherehe kwa ajili ya wafu wakati huo wa mwaka.
Uthibitisho mwingine kwamba kulikuwa na Gharika wapatikana katika mapokeo ya wanadamu. Karibu watu wote wa kale wana hekaya zinazosema kwamba wazazi wao wa kale waliokoka furiko la ulimwenguni pote. Mbilikimo wa Afrika, Wainka wa Marekani, Waselti wa Ulaya—wote wana hekaya zinazofanana na za watu wa Alaska, Amerika Kaskazini, Australia, China, India, Lithuania, Mexico, Micronesia, na New Zealand, kwa kutaja nchi chache tu.
Bila shaka, kadiri wakati ulivyopita ndivyo hekaya hizo zilivyotiwa chumvi, lakini zote zina mambo kadhaa yanayoonyesha kwamba zilikuwa na chanzo kimoja: Mungu alichukizwa na uovu wa wanadamu. Akaleta furiko kubwa lililoangamiza wanadamu wote isipokuwa wachache tu waliokuwa waadilifu. Wanadamu hao waadilifu walijenga meli ambayo ilitumiwa kuwaokoa na kuokoa wanyama pia. Baadaye, ndege walitumwa kutafuta nchi kavu. Hatimaye meli ilitua juu ya mlima. Waliposhuka kutoka katika meli hiyo, waokokaji hao walitoa dhabihu.
Jambo hilo linathibitisha nini? Haiwezekani mambo hayo yanayofanana yawe yalitokea tu. Hekaya hizo zote zinathibitisha ushuhuda wa kale wa Biblia kwamba wanadamu wote ni wazao wa waokokaji wa furiko lililoangamiza wanadamu. Hivyo, hatuhitaji kutegemea hekaya au ngano kujua yaliyotokea. Tuna Maandiko ya Kiebrania ya Biblia yaliyohifadhiwa vizuri.—Mwanzo, sura ya 6-8.
Biblia ina historia iliyopuliziwa ambayo inataja jinsi uhai ulivyoanza. Hata hivyo, kuna uthibitisho unaoonyesha kwamba hiyo si historia tu. Unabii wake wenye kutegemeka na hekima yake nyingi huonyesha kwamba Biblia ni njia ya Mungu ya kuwasiliana na wanadamu. Tofauti na ngano, Biblia inataja majina, tarehe, nasaba, na maeneo ya kijiografia katika masimulizi yake ya kihistoria. Inatueleza jinsi maisha yalivyokuwa kabla ya Furiko na kufunua ni kwa nini ulimwengu mzima ulifikia kikomo kwa ghafula.
Ni nini kilichofanya watu hao walioishi kabla ya gharika waharibiwe? Makala inayofuata itajibu swali hilo. Hilo ni swali muhimu kwa wale ambao huenda wanataka kujua kama wakati ujao wa jamii ya leo ni salama.
[Maelezo ya Chini]
-
-
Kwa Nini Ulimwengu Huo wa Kale Uliangamia?Mnara wa Mlinzi—2002 | Machi 1
-
-
Kwa Nini Ulimwengu Huo wa Kale Uliangamia?
GHARIKA iliyokumba ulimwengu mzima haikuwa msiba wa kiasili. Ilikuwa hukumu kutoka kwa Mungu. Onyo lilitolewa, lakini wengi wakalipuuza. Kwa nini? Yesu alieleza hivi: “Katika siku hizo kabla ya furiko, [watu walikuwa] wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiozwa, hadi siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina; nao hawakujali mpaka furiko likaja na kuwafagilia mbali wote.”—Mathayo 24:38, 39.
Jamii Iliyositawi
Kwa njia fulani, jamii iliyoishi kabla ya Furiko ilifurahia hali bora kuliko sisi leo. Kwa mfano, wanadamu wote walizungumza lugha moja. (Mwanzo 11:1) Jambo hilo lingeleta mafanikio katika sanaa na sayansi ambazo zinahitaji juhudi za pamoja za watu wengi wenye ustadi mbalimbali. Pia, kwa kuwa watu waliishi kwa muda mrefu, wangeweza kuendelea kuongeza ujuzi wao katika mambo waliyokuwa wamejifunza kwa karne nyingi.
Wengine hudai kwamba maisha ya mwanadamu hayakuwa marefu sana wakati huo na kwamba miaka inayotajwa katika Biblia ni miezi tu. Je, jambo hilo ni kweli? Hebu fikiria Mahalaleli. Biblia inasema: “Mahalaleli akaishi miaka sitini na mitano, akamzaa Yaredi. . . . Siku zote za Mahalaleli ni miaka mia nane na tisini na mitano, akafa.” (Mwanzo 5:15-17) Ikiwa mwaka mmoja ni sawa na mwezi mmoja, basi Mahalaleli alimzaa mwanawe akiwa na umri wa miaka mitano tu! Watu wa wakati huo walikaribia ukamilifu wa mwanadamu wa kwanza, Adamu. Kwa kweli waliishi kwa karne nyingi. Walipata mafanikio gani?
Karne nyingi kabla ya Furiko, idadi ya watu duniani ilikuwa imekua sana hivi kwamba Kaini mwana wa Adamu aliweza kujenga mji aliouita Henoko. (Mwanzo 4:17) Viwanda mbalimbali vilisitawi katika enzi zilizotangulia Furiko. Watu walifua “kila chombo cha kukatia, cha shaba na cha chuma.” (Mwanzo 4:22) Bila shaka vyombo hivyo vilitumiwa katika ujenzi, useremala, ushonaji, na kilimo. Ufuaji huo unatajwa katika masimulizi juu ya wanadamu wa kwanza kabisa duniani.
Ujuzi wa miaka mingi ungewezesha vizazi vilivyofuatana visitawishe ustadi katika ufuaji vyuma, kilimo, ufugaji wa kondoo na ng’ombe, uandishi, na sanaa. Kwa mfano, Yubali alikuwa “baba yao wapigao kinubi na filimbi.” (Mwanzo 4:21) Jamii hiyo ilikuwa imesitawi sana. Hata hivyo, mambo yalikoma ghafula. Ni nini kilichotukia?
Tatizo Lilikuwa Nini?
Ingawa jamii iliyoishi kabla ya Furiko ilikuwa na mafanikio mengi, haikuwa na mwanzo mzuri. Mzazi wao wa kwanza Adamu alimwasi Mungu. Naye Kaini aliyejenga mji wa kwanza kabisa duniani, akamwua nduguye. Si ajabu kwamba uovu uliongezeka haraka! Watoto wa Adamu walirithi kasoro nyingi sana kutoka kwake.—Waroma 5:12.
Yaonekana uovu ulikuwa unakaribia kilele Yehova alipoamua kwamba angeuruhusu uendelee kwa miaka mingine 120 tu. (Mwanzo 6:3) Biblia inasema: ‘Maovu ya mwanadamu yalikuwa makubwa duniani na kila kusudi alilowaza moyoni mwake lilikuwa baya tu sikuzote. Dunia ilijaa dhuluma.’—Mwanzo 6:5, 11.
Hatimaye, Mungu alimwambia Noa waziwazi kwamba angeharibu wanadamu wote kwa gharika. (Mwanzo 6:13, 17) Ingawa Noa alikuwa “mhubiri wa uadilifu,” yaonekana ilikuwa vigumu kwa watu kuamini kwamba ulimwengu uliowazunguka ungefikia kikomo. (2 Petro 2:5) Watu wanane tu ndio waliotii onyo hilo na kuokolewa. (1 Petro 3:20) Kwa nini mambo hayo ni muhimu kwetu leo?
Yana Umuhimu Gani Kwetu?
Tunaishi katika nyakati zinazofanana na za Noa. Sisi husikia kwa ukawaida habari nyingi sana kuhusu vitendo vya ugaidi vyenye kuogofya, kampeni za kuangamiza jamii fulani, mauaji ya watu wengi yanayofanywa na majambazi bila sababu hususa, na jeuri katika familia. Kwa mara nyingine dunia imejaa jeuri, na kama zamani, watu wamejulishwa kwamba kuna hukumu inayokuja. Yesu mwenyewe alisema kwamba angekuja akiwa Hakimu aliyeteuliwa na Mungu na kutenganisha watu kama vile mchungaji atenganishavyo kondoo na mbuzi. Yesu alisema wale watakaopatikana kuwa hawastahili, “wataondoka kuingia katika kukatiliwa-mbali kudumuko milele.” (Mathayo 25:31-33, 46) Hata hivyo, Biblia inasema kwamba wakati huo kutakuwa na mamilioni ya watu watakaookoka—umati mkubwa unaomwabudu Mungu wa pekee wa kweli. Tofauti na wakati mwingine wowote, watu hao watafurahia maisha katika amani na usalama wenye kudumu katika ulimwengu unaokuja.—Mika 4:3, 4; Ufunuo 7:9-17.
Wengi hudhihaki taarifa na maonyo ya Biblia kuhusu hukumu ambayo itathibitisha kwamba taarifa hizo ni za kweli. Lakini mtume Petro alieleza kwamba wadhihaki hao wanapuuza mambo ya hakika. Aliandika: “Katika siku za mwisho watakuja wadhihaki . . . na kusema: ‘Kuko wapi kuwapo kwake huku kulikoahidiwa?’ . . . Kwa maana, kulingana na kutaka kwao, jambo hili huponyoka kujali kwao, kwamba mbingu zilikuwako tangu zamani za kale na dunia ikisimama kwa kutungamana kutoka katika maji na katikati ya maji kwa neno la Mungu; na kwa njia hizo ulimwengu wa wakati huo ulipatwa na uangamizo ulipogharikishwa kwa maji. Lakini kwa neno hilohilo mbingu na dunia zilizopo sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto na zinawekwa akiba hadi siku ya hukumu na ya uangamizo wa watu wasiomwogopa Mungu.”—2 Petro 3:3-7.
Onyo kuhusu siku hiyo ya hukumu inayokuja, na habari njema kuhusu amani itakayofuata, zinahubiriwa kwa bidii ulimwenguni pote leo, kwa kutii amri ya kiunabii ya Yesu. (Mathayo 24:14) Onyo hilo lapaswa kuchukuliwa kwa uzito kwa kuwa Mungu Mweza Yote hutimiza ahadi zake.
Ulimwengu Unaokuja
Wakati ujao wa wanadamu utakuwaje tunapofikiria badiliko kubwa linalokuja? Katika utangulizi wa Mahubiri yake maarufu ya Mlimani, Yesu aliahidi: “Wenye furaha ni wenye tabia-pole, kwa kuwa wao watairithi dunia.” Kisha akawafunza wanafunzi wake kusali kwa Mungu hivi: “Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.” (Mathayo 5:5; 6:10) Naam, Yesu mwenyewe alifundisha kwamba wakati ujao mzuri unawangojea wanadamu waaminifu hapa duniani. Aliuita “uumbaji-upya.”—Mathayo 19:28.
Kwa hiyo, unapofikiria wakati ujao, usiruhusu wadhihaki wakufanye utilie shaka onyo la Mungu. Ni kweli kwamba mazingira yetu yanaweza kuonekana kuwa yenye kudumu nao ulimwengu wa sasa umekuwapo kwa muda mrefu. Hata hivyo, hatupaswi kuutumainia. Ulimwengu wa wanadamu tayari umehukumiwa. Hivyo basi, maneno ya kumalizia ya barua ya mtume Petro na yakutie moyo:
“Kwa kuwa vitu vyote hivi vitafumuliwa hivyo, nyinyi mwapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu, mkingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova . . . Kwa kuwa mnangojea mambo haya, fanyeni kabisa yote mwezayo ili mwishowe mpatikane naye mkiwa bila doa na bila waa na katika amani. . . . Endeleeni kukua katika fadhili isiyostahiliwa na ujuzi juu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo.” (2 Petro 3:11, 12, 14, 18) Jifunze kutokana na mambo yaliyotokea wakati wa Noa. Mkaribie Mungu. Ongeza ujuzi juu ya Yesu Kristo. Sitawisha ujitoaji-kimungu, na uwe miongoni mwa mamilioni wanaochagua kuokoka mwisho wa ulimwengu huu na kuingia katika ulimwengu wenye amani unaokuja.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Watu walijua kufua vyuma hata kabla ya Furiko
[Picha katika ukurasa wa 7]
Tunatazamia wakati ujao mzuri ajabu
-