Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kuona Ni Kuamini
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Mei 1
    • Kwa nini Paulo alikuwa na uhakika kwamba kuna Mungu na kwamba anapendezwa na wanadamu ambao Aliumba? Paulo alionyesha sababu moja alipowaandikia Wakristo wenzake katika jiji la Roma. Alisema hivi kumhusu Mungu: “Sifa zake ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa.”—Waroma 1:20.

      Kurasa zinazofuata zinazungumzia sifa tatu za Mungu ambazo zinaweza kuonekana waziwazi katika vitu alivyoumba. Unapochunguza mifano hiyo, jiulize hivi: ‘Ninahisi jinsi gani ninapojifunza kuhusu sifa hizi za Mungu?’

  • Uumbaji Unathibitisha Hekima ya Mungu
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Mei 1
    • Uumbaji Unathibitisha Hekima ya Mungu

      “Ni Yeye anayetufundisha sisi kuliko wanyama wa dunia, naye anatufanya tuwe na hekima kuliko hata viumbe vinavyoruka vya mbinguni.”—AYUBU 35:11.

      NDEGE ni viumbe wenye uwezo mbalimbali wenye kustaajabisha. Watu wanaotengeneza ndege (eropleni) wanavutiwa sana kuona jinsi ndege wanavyoruka angani bila tatizo lolote. Aina fulani ya ndege wanaweza kuruka maelfu ya kilomita juu ya bahari na kufika mahali wanapokwenda bila kukosea na pasipo mwongozo wowote.

      Jambo lingine lenye kustaajabisha kuhusu ndege—ambalo linafunua mengi zaidi juu ya hekima ya Muumba wao—ni uwezo wao wa kuwasiliana kwa milio na nyimbo. Fikiria mifano fulani.

      Jinsi Ndege Wanavyowasiliana

      Ndege wa aina fulani wanaanza kuwasiliana hata kabla ya kutoka ndani ya yai. Kwa mfano, kware wa kike anataga mayai manane, yai moja kila siku. Ikiwa mayai yote yangekomaa kwa kadiri ileile, yangetokeza vifaranga kwa kipindi cha siku nane. Hivyo, kware wa kike angekuwa na kazi ngumu ya kutunza vifaranga wa juma moja, huku akiendelea kulalia yai ambalo halijakomaa. Hata hivyo, vifaranga vyote vinane vya kware vitatoka ndani ya yai katika muda wa saa sita. Hilo linawezekana jinsi gani? Sababu moja kuu ambayo watafiti wametoa ni kwamba kifaranga cha kware ambacho bado kingali ndani ya yai kinawasiliana na vifaranga vingine vilivyo ndani ya mayai na kwa njia moja au nyingine vinafanya mipango ili vitoke wakati mmoja.

      Ndege wanapokomaa, kwa kawaida ni ndege wa kiume anayeimba. Anafanya hivyo hasa wakati wa kujamiiana ili kuweka mipaka ya eneo lake au kuvutia ndege wa kike. Ni kana kwamba kila moja ya maelfu ya jamii za ndege ina lugha yake na hilo linawasaidia ndege wa kike kutambua ndege wa kiume wa jamii yao.

      Kuna sababu nzuri inayofanya ndege waimbe hasa asubuhi na mapema na jua linapotua. Nyakati hizo hakuna upepo wala kelele nyingi. Wachunguzi wamegundua kwamba asubuhi na jioni nyimbo za ndege zinasikika vizuri zaidi mara 20 kuliko zinavyosikika mchana.

      Ingawa mara nyingi ndege wa kiume ndio wanaoimba, ndege wa kike na wa kiume wanatoa milio mbalimbali au sauti za chini ambazo zina maana tofauti. Kwa mfano, ndege wa aina ya Chaffinch wana milio tisa. Wanatoa mlio fulani ili kuonya kuhusu hatari iliyo angani—kama vile ndege anayetafuta mawindo—lakini wanatoa mlio tofauti ili kuonya kuhusu hatari iliyo ardhini.

      Zawadi Kubwa Zaidi

      Kwa kweli, hekima ya kisilika ya ndege inastaajabisha. Lakini wanadamu wana uwezo mbalimbali wa kuwasiliana ambao unastaajabisha hata zaidi. Andiko la Ayubu 35:11 linasema kwamba Mungu amewafanya wanadamu kuwa wenye “hekima kuliko hata viumbe vinavyoruka vya mbinguni.” Wanadamu wana uwezo wa pekee wa kueleza mambo magumu kupitia ishara au sauti zinazotokezwa na misuli ya koo.

      Tofauti na viumbe wengine, inaelekea watoto wachanga wa kibinadamu wanazaliwa wakiwa na uwezo wa kujifunza lugha ngumu. Gazeti moja kwenye Intaneti (American Scientist) linasema hivi: “Watoto wanajifunza lugha ambayo hata wazazi wao hawazungumzi nao moja kwa moja; watoto ambao ni viziwi hata wanaanzisha lugha yao ya ishara ikiwa hawafundishwi lugha ya ishara nyumbani.”

  • Uumbaji Unathibitisha Hekima ya Mungu
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Mei 1
    • Unahisi Jinsi Gani?

      Unahisi jinsi gani unaposikia nyimbo tamu za ndege au mtoto anapojifunza kutamka maneno yake ya kwanza? Je, unaona hekima ya Mungu katika vitu ambavyo amefanya?

      Baada ya kutafakari kuhusu jinsi alivyoumbwa, mtunga-zaburi Daudi alichochewa kumwambia Mungu: “Nitakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha. Kazi zako ni za ajabu, kama vile nafsi yangu inavyojua vema.” (Zaburi 139:14) Unapochunguza kwa uthamini uthibitisho wa hekima ya Mungu katika uumbaji, bila shaka imani yako katika uwezo wake wa kukupa mwongozo mzuri itakua.

  • Nyota Zinafunua Nguvu za Mungu
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Mei 1
    • Nyota Zinafunua Nguvu za Mungu

      “Inueni macho yenu juu, mwone. Ni nani ameviumba vitu hivi? Ni Yeye anayelileta jeshi lake kulingana na hesabu, ambaye zote anaziita kwa jina. Kutokana na wingi wa nguvu zenye msukumo, yeye pia akiwa hodari katika nguvu, hakuna hata moja kati ya hizo inayokosekana.”—ISAYA 40:26.

      JUA letu ni nyota yenye ukubwa wa kadiri tu. Hata hivyo, ukubwa wake unazidi ukubwa wa dunia kwa mara 330,000. Nyota nyingi ambazo ziko karibu na dunia ni ndogo zaidi kuliko jua. Hata hivyo, nyota nyingine, kama ile inayoitwa V382 Cygni, ni kubwa angalau mara 27 kuliko jua letu.

      Jua letu linatoa nishati au nguvu nyingi kadiri gani? Fikiria joto ambalo ungehisi ikiwa ungekuwa umbali wa kilomita 15 kutoka kwenye moto. Kwa wastani, jua liko umbali wa kilomita milioni 150 kutoka duniani. Hata hivyo, siku yenye jua kali, joto lake linaweza kuchoma ngozi! Inashangaza kwamba yapata sehemu moja tu ya bilioni ya nishati ya jua ndiyo inayofika duniani. Hata hivyo, sehemu hiyo ndogo ya nguvu za jua inatosha kutegemeza uhai kwenye sayari yetu.

      Wanasayansi wamegundua kwamba jumla ya nishati inayotoka kwenye jua letu tu inatosha kutegemeza sayari zipatazo trilioni 31 zilizo kama dunia. Au tukihesabu nguvu hizo kwa njia nyingine: Ikiwa nguvu zote ambazo jua linatoa kwa sekunde moja tu zingekusanywa, Marekani ingepata “nishati ya kutosha, kwa ajili ya miaka 9,000,000 ijayo,” kinasema kituo kimoja cha Intaneti (cha Space Weather Prediction Center, SWPC).

      Nishati ya jua inatoka kwenye kiini cha jua, yaani, ndani kabisa ya tanuru ya nyuklia ambayo inagonganisha atomi na kutokeza nguvu. Jua ni kubwa sana na kiini chake ni kizito sana hivi kwamba inachukua mamilioni ya miaka ili nishati iliyo ndani ya kiini hicho itokee nje. “Ikiwa Jua lingeacha kutoa nishati leo,” kinasema kituo cha Intaneti kilichotajwa juu, “ingechukua miaka 50,000,000 ili kuhisi mabadiliko makubwa duniani!”

      Sasa fikiria uhakika huu: Unapoinua macho yako juu usiku usiokuwa na mawingu, unaweza kuona maelfu ya nyota, kila moja ikitoa nishati nyingi sana, kama jua letu. Wanasayansi wanakadiria kwamba kuna mabilioni na mabilioni ya nyota katika ulimwengu wote!

      Nyota zote hizo zilitoka wapi? Watafiti wengi sasa wanaamini kwamba kwa sababu ambazo hawajaelewa, ulimwengu wote ulitokea ghafula miaka bilioni 14 hivi iliyopita. Biblia inasema hivi kwa ufupi: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” (Mwanzo 1:1) Bila shaka, inaweza kusemwa kwamba Yule ambaye aliumba mashini hizo kubwa za nishati ambazo tunaita nyota ni “hodari katika nguvu.”—Isaya 40:26.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki