-
‘Kuleta Habari Njema za Jambo Bora’Mnara wa Mlinzi—2005 | Julai 1
-
-
‘Kuleta Habari Njema za Jambo Bora’
“Jinsi inavyopendeza juu ya milima miguu ya yeye . . . anayeleta habari njema za jambo bora.”—ISAYA 52:7.
1, 2. (a) Ni mambo gani yenye kutisha yanayotukia kila siku? (b) Watu wengi huhisije wanapopata habari mbaya kila siku?
LEO watu wanapokea habari nyingi mbaya ulimwenguni pote. Wanapowasha redio, wanasikia habari zenye kutisha kuhusu magonjwa hatari yanayoikumba dunia. Wanapotazama habari kwenye televisheni wanaona picha zenye kusikitisha sana za watoto wenye njaa wakiomba msaada. Wanasoma katika magazeti kuhusu mabomu yanayolipua majengo na kuwaua watu wengi wasio na hatia.
2 Naam, mambo yenye kutisha yanatukia kila siku. Tamasha ya ulimwengu huu kwa hakika inabadilika na kuwa mbaya zaidi. (1 Wakorintho 7:31) Gazeti moja huko Ulaya Magharibi lilisema, nyakati nyingine ni kama ulimwengu wote “unakaribia kuteketea.” Si ajabu kwamba watu wengi wanafadhaika! Mtu mmoja aliyenukuliwa katika uchunguzi wa habari za televisheni nchini Marekani alitoa maoni ambayo bila shaka ni sawa na ya mamilioni ya watu wengine aliposema hivi: ‘Baada ya kutazama habari, mimi hushuka moyo sana. Zote ni habari mbaya. Zinanihuzunisha sana.’
Habari Ambazo Kila Mtu Anahitaji Kusikia
3. (a) Biblia inatangaza habari gani njema? (b) Kwa nini unathamini habari njema za Ufalme?
3 Je, habari njema zinaweza kupatikana katika ulimwengu huu wenye kuhuzunisha? Bila shaka zinaweza kupatikana! Inafariji kujua kwamba Biblia inatangaza habari njema. Hizo ni habari za kwamba Ufalme wa Mungu utakomesha magonjwa, njaa, uhalifu, vita, na kila namna ya ukandamizaji. (Zaburi 46:9; 72:12) Je, hizo si habari ambazo kila mtu anahitaji kusikia? Mashahidi wa Yehova wanaamini hivyo. Kwa hiyo, wanajulikana kila mahali kwa sababu wanajitahidi daima kuwahubiria watu wa mataifa yote habari njema za Ufalme wa Mungu.—Mathayo 24:14.
4. Ni mambo gani kuhusu huduma yetu tutakayozungumzia katika makala hii na katika ile inayofuata?
4 Basi, tunaweza kufanya nini ili tuendelee kuhubiri habari njema kwa bidii na kuridhika tunapofanya hivyo—hata katika maeneo ambayo watu wengi hawataki ujumbe wetu? (Luka 8:15) Bila shaka tutafaidika tukipitia kifupi mambo matatu muhimu kuhusu kazi yetu ya kuhubiri. Tunaweza kuchunguza (1) nia yetu, au kwa nini tunahubiri; (2) ujumbe wetu, au kile tunachohubiri; na (3) njia zetu, au jinsi tunavyohubiri. Tunapokuwa na nia inayofaa, ujumbe ulio wazi, na kutumia njia zenye matokeo, tutawapa watu wa kila namna nafasi ya kusikia habari bora kabisa—habari njema za Ufalme wa Mungu.a
Kwa Nini Tunahubiri Habari Njema?
5. (a) Ni sababu gani kuu inayotuchochea kuhubiri? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba kutii amri ya Biblia ya kuhubiri huonyesha kwamba tunampenda Mungu?
5 Hebu tuzungumzie jambo la kwanza, yaani, nia yetu. Kwa nini tunahubiri habari njema? Sababu yetu ni kama ya Yesu. Alisema: “Ninampenda Baba.” (Yohana 14:31; Zaburi 40:8) Kwa hiyo, kumpenda Mungu ndiyo sababu kuu inayotuchochea kuhubiri. (Mathayo 22:37, 38) Biblia inahusianisha kumpenda Mungu na huduma, kwa kuwa inasema hivi: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake.” (1 Yohana 5:3; Yohana 14:21) Je, amri za Mungu zinatia ndani ile amri ya ‘kwenda kufanya wanafunzi’? (Mathayo 28:19) Ndiyo. Ingawa maneno hayo yalisemwa na Yesu, kwa kweli yalitoka kwa Yehova. Jinsi gani? Yesu alieleza hivi: “Sifanyi jambo lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe; bali kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema mambo haya.” (Yohana 8:28; Mathayo 17:5) Kwa hiyo, tunapotii amri ya kuhubiri, tunamwonyesha Yehova kwamba tunampenda.
6. Kumpenda Mungu hutuchochea katika njia zipi kuhubiri?
6 Pia, kumpenda Yehova hutuchochea kuhubiri kwa sababu tunataka kupinga uwongo ambao Shetani anaeneza kumhusu. (2 Wakorintho 4:4) Shetani ametilia shaka uadilifu wa utawala wa Mungu. (Mwanzo 3:1-5) Tukiwa Mashahidi wa Yehova tunatamani sana kushiriki katika kufunua uchongezi wa Shetani na kulitakasa jina la Mungu mbele ya wanadamu. (Isaya 43:10-12) Isitoshe, tunashiriki katika huduma kwa sababu tumejua sifa za Yehova na njia zake. Tunahisi tukiwa karibu naye na tunatamani sana kuwaeleza wengine kumhusu Mungu wetu. Kwa kweli, wema wa Yehova na njia zake za uadilifu hutuletea shangwe kubwa sana hivi kwamba hatuwezi kuacha kuongea juu yake. (Zaburi 145:7-12) Moyo wetu unatusukuma kumsifu na kutangaza ‘sifa zake bora’ kwa wale ambao watasikiliza.—1 Petro 2:9; Isaya 43:21.
7. Mbali na kumpenda Mungu, ni sababu gani nyingine muhimu inayotufanya tuhubiri?
7 Kuna sababu nyingine muhimu inayotufanya tuendelee kuhubiri: Tunataka kwa moyo wote kuwafariji wale wanaofadhaishwa na habari nyingi mbaya na wale wanaoteseka kwa sababu mbalimbali. Tunajitahidi kumwiga Yesu tunapowafariji wengine. Kwa mfano, angalia simulizi la Marko sura ya 6.
8. Simulizi la Marko sura ya 6 linaonyesha nini kuhusu hisia za Yesu kuwaelekea watu?
8 Mitume wametoka kuhubiri na wanamsimulia Yesu mambo yote ambayo wamefanya na kufundisha. Yesu anaona kwamba mitume wamechoka, kwa hiyo anawaambia waende pamoja naye ili ‘wapumzike kidogo.’ Kwa hiyo wanapanda mashua na kwenda mahali patulivu. Watu wanawafuata, wakikimbia kando ya bahari, na muda si muda wanawafikia. Yesu anafanya nini? Biblia inasema hivi: “Akaona umati mkubwa, lakini akawasikitikia, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji. Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.” (Marko 6:31-34) Kwa sababu anawasikitikia watu, Yesu anaendelea kuhubiri habari njema ajapokuwa mchovu. Ni wazi kwamba Yesu anawasikitikia sana watu hao. Anawahurumia.
9. Simulizi la Marko sura ya 6 linatufunza nini kuhusu nia inayofaa ya kuhubiri?
9 Tunajifunza nini kutokana na simulizi hilo? Tukiwa Wakristo tunahisi tuna wajibu wa kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi. Tunatambua jukumu letu la kutangaza habari njema, kwa kuwa mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe.” (1 Timotheo 2:4) Hata hivyo, hatuhubiri ili kutimiza wajibu tu, bali pia tunahubiri kwa sababu ya huruma. Ikiwa kama Yesu tunawahurumia watu sana, moyo wetu utatuchochea kufanya yote tuwezayo kuwahubiria habari njema. (Mathayo 22:39) Kuwa na nia nzuri ya kushiriki katika huduma kutatuchochea tuhubiri habari njema bila kuacha.
Ujumbe Wetu Ni Habari Njema za Ufalme wa Mungu
10, 11. (a) Isaya anaelezaje ujumbe ambao tunahubiri? (b) Yesu aliletaje habari njema za jambo bora, na watumishi wa Mungu katika nyakati zetu wameigaje kielelezo cha Yesu?
10 Tuchunguze jambo la pili kuhusu huduma yetu, yaani, ujumbe wetu. Tunahubiri nini? Nabii Isaya alitoa maelezo haya mazuri sana kuhusu ujumbe ambao tunatangaza: “Jinsi inavyopendeza juu ya milima miguu ya yeye anayeleta habari njema, yeye anayetangaza amani, yeye anayeleta habari njema za jambo bora, yeye anayetangaza wokovu, yeye anayeuambia Sayuni: ‘Mungu wako amekuwa mfalme!’”—Isaya 52:7.
11 Maneno makuu katika andiko hilo, “Mungu wako amekuwa mfalme,” yanatukumbusha ujumbe ambao tunapaswa kutangaza, yaani, habari njema za Ufalme wa Mungu. (Marko 13:10) Ona pia kwamba mstari huo unakazia ubora wa ujumbe wetu. Isaya anatumia maneno kama vile “wokovu,” “habari njema,” “amani,” na “jambo bora.” Katika karne ya kwanza W.K., miaka mingi baada ya siku za Isaya, Yesu Kristo alitimiza unabii huo kwa njia ya pekee alipoweka kielelezo katika kutangaza kwa bidii habari njema za jambo bora, yaani, kuja kwa Ufalme wa Mungu. (Luka 4:43) Katika nyakati zetu, hasa tangu mwaka wa 1919, Mashahidi wa Yehova wameiga kielelezo cha Yesu kwa kutangaza kwa bidii habari njema za Ufalme wa Mungu uliosimamishwa na baraka ambazo utaleta.
12. Habari njema za Ufalme zina matokeo gani kwa wale wanaozikubali?
12 Habari njema za Ufalme zina matokeo gani kwa wale wanaozikubali? Leo habari njema zinawafariji watu na kuwapa tumaini kama ilivyokuwa katika siku za Yesu. (Waroma 12:12; 15:4) Zinawapa watu wanyoofu tumaini kwa sababu wanajifunza kwamba kuna sababu nzuri za kutarajia hali bora wakati ujao. (Mathayo 6:9, 10; 2 Petro 3:13) Tumaini hilo huwasaidia sana watu wanaomwogopa Mungu waendelee kuwa na mtazamo mzuri. Mtunga-zaburi anasema kwamba ‘hawataogopa hata habari mbaya.’—Zaburi 112:1, 7.
Ujumbe “Unaofunga Majeraha ya Waliovunjika Moyo”
13. Nabii Isaya anataja baraka gani ambazo wale wanaokubali habari njema wanapata sasa?
13 Zaidi ya hayo, wale wanaokubali habari njema tunazohubiri hupata kitulizo na baraka sasa. Jinsi gani? Nabii Isaya alitaja baadhi ya baraka hizo alipotabiri hivi: “Roho ya Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova iko juu yangu, kwa sababu Yehova amenitia mafuta niwatangazie wapole habari njema. Amenituma kufunga majeraha ya waliovunjika moyo, kutangaza uhuru kwa wale waliochukuliwa mateka na kufunguliwa kabisa kwa macho hata kwa walio wafungwa; kutangaza mwaka wa nia njema upande wa Yehova na siku ya kisasi upande wa Mungu wetu; kuwafariji wote wanaoomboleza.”—Isaya 61:1, 2; Luka 4:16-21.
14. (a) Maneno “kufunga majeraha ya waliovunjika moyo” yanaonyesha nini kuhusu ujumbe wa Ufalme? (b) Tunamwigaje Yehova katika kuwajali waliovunjika moyo?
14 Unabii huo unaonyesha kwamba kwa kuhubiri habari njema, Yesu ‘angefunga majeraha ya waliovunjika moyo.’ Isaya anatumia mfano mzuri kama nini! Kamusi moja ya Biblia inasema kwamba neno la Kiebrania linalotafsiriwa ‘funga majeraha’ “mara nyingi linatumiwa kuhusu ‘kufunga’ bendeji, na hivyo kutibu au kuponya waliojeruhiwa.” Muuguzi mwenye kujali anaweza kufunga bendeji au kitambaa kwenye kiungo cha mwili kilichojeruhiwa ili kukitegemeza. Vivyo hivyo, wahubiri wenye kujali wanapohubiri ujumbe wa Ufalme, wanawategemeza wale wote wanaokubali ujumbe huo ambao wanateseka kwa njia fulani. Na wanapowategemeza wenye uhitaji, wanamwiga Yehova katika kuwajali watu wengine. (Ezekieli 34:15, 16) Mtunga-zaburi anasema hivi kumhusu Mungu: “Anawaponya wenye mioyo iliyovunjika, naye anafunga sehemu zao zenye maumivu.”—Zaburi 147:3.
Jinsi Ujumbe wa Ufalme Unavyobadili Maisha ya Watu
15, 16. Simulia mambo yaliyoonwa yanayoonyesha jinsi ujumbe wa Ufalme unavyowategemeza na kuwaimarisha wenye uhitaji.
15 Mambo mengi yaliyoonwa yanaonyesha jinsi ujumbe wa Ufalme unavyowategemeza na kuwaimarisha wale waliovunjika moyo. Fikiria kisa cha Oreanna, mwanamke mzee kutoka Amerika Kusini ambaye alikuwa amepoteza kabisa hamu ya kuishi. Shahidi mmoja wa Yehova alianza kumtembelea Oreanna na kumsomea Biblia na Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia.b Mwanzoni, mwanamke huyo aliyeshuka moyo alisikiliza usomaji huo akiwa amelala kitandani huku akiwa amefumba macho yake, naye alikuwa akishusha pumzi kwa nguvu mara kwa mara. Hata hivyo, baada ya muda alianza kujitahidi kuketi kitandani wakati wa usomaji huo. Baadaye, alianza kuketi kwenye kiti sebuleni na kumngoja mwalimu wake wa Biblia. Halafu, mwanamke huyo akaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo katika Jumba la Ufalme. Alitiwa moyo na yale aliyojifunza kwenye mikutano hiyo, naye akaanza kuwapa vichapo vya Biblia watu wote waliopita karibu na nyumba yake. Kisha, Oreanna akabatizwa akiwa na umri wa miaka 93 na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Ujumbe wa Ufalme ulimsaidia kupata tena na hamu ya kuishi.—Methali 15:30; 16:24.
16 Ujumbe wa Ufalme unawategemeza sana hata wale ambao wanajua kwamba maisha yao yatakatishwa na ugonjwa. Kwa mfano, fikiria kisa cha Maria kutoka Ulaya Magharibi. Alikuwa na ugonjwa unaosababisha kifo na hakuwa na matumaini yoyote. Alikuwa ameshuka moyo kabisa alipotembelewa na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, alipojifunza kuhusu makusudi ya Mungu, maisha yake yakawa na maana tena. Alibatizwa na akawa mwenye bidii sana katika kazi ya kuhubiri. Katika miaka miwili ya mwisho ya maisha yake, alikuwa mwenye shangwe nyingi na tumaini. Maria alikufa akiwa na tumaini thabiti la ufufuo.—Waroma 8:38, 39.
17. (a) Ujumbe wa Ufalme unabadilije maisha ya wale wanaoukubali? (b) Wewe binafsi umejionea kwa njia gani kwamba Yehova “anawainua wote ambao wameinama chini”?
17 Mambo hayo yanathibitisha kwamba ujumbe wa Ufalme unaweza kubadili maisha ya watu ambao wanataka kujua kweli za Biblia. Watu ambao wanaomboleza kifo cha mpendwa hupata nguvu tena wanapojifunza kuhusu tumaini la ufufuo. (1 Wathesalonike 4:13) Watu maskini ambao hujitahidi sana kulisha familia zao hupata tena heshima na ujasiri wanapojifunza kwamba Yehova hatawaacha kamwe ikiwa watakuwa washikamanifu kwake. (Zaburi 37:28) Kwa msaada wa Yehova, watu wengi walioshuka moyo hupata nguvu hatua kwa hatua ili kukabiliana na ugonjwa huo na hata baadhi yao hupona. (Zaburi 40:1, 2) Kwa kweli, hivi sasa Yehova anatumia nguvu za Neno lake ‘kuwainua wote ambao wameinama chini.’ (Zaburi 145:14) Tunapoona jinsi habari njema za Ufalme zinavyowafariji waliovunjika moyo katika eneo letu na katika kutaniko la Kikristo, jambo hilo hutukumbusha tena na tena kwamba tuna habari bora zaidi leo!—Zaburi 51:17.
“Dua Yangu kwa Mungu kwa Ajili Yao”
18. Paulo alihisije Wayahudi walipokataa habari njema, na kwa nini?
18 Watu wengi hukataa ujumbe wetu licha ya kwamba una habari bora zaidi. Itikio lao linaweza kutufanya tuhisije? Tunaweza kuhisi kama mtume Paulo. Aliwahubiria Wayahudi mara nyingi, lakini wengi wao wakakataa ujumbe wa wokovu. Paulo aliumia sana moyoni walipokataa. Alikiri hivi: “Nina huzuni kubwa na maumivu yasiyokoma moyoni mwangu.” (Waroma 9:2) Paulo aliwahurumia Wayahudi ambao aliwahubiria. Alihuzunika sana kuona wakikataa habari njema.
19. (a) Kwa nini ni jambo linaloeleweka kwamba nyakati nyingine tunaweza kuhisi tumevunjika moyo? (b) Ni nini kilichomsaidia Paulo kuendelea na kazi yake ya kuhubiri?
19 Sisi pia tunahubiri habari njema kwa sababu ya huruma. Kwa hiyo, ni jambo linaloeleweka kwamba tunaweza kuvunjika moyo watu wengi wanapokataa ujumbe wa Ufalme. Tunahisi hivyo kwa sababu tunahangaikia kikweli hali ya kiroho ya wale tunaowahubiria. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka mfano wa mtume Paulo. Ni nini kilichomsaidia kuendelea na kazi yake ya kuhubiri? Ingawa alihuzunika na kuumia moyoni Wayahudi walipokataa habari njema, Paulo hakukata tamaa na kufikiri kwamba Wayahudi wote hawangeweza kusaidiwa. Alitumaini kwamba baadhi yao wangemkubali Kristo. Kwa hiyo, Paulo alieleza hisia zake kuhusu Myahudi mmoja-mmoja aliposema hivi: “Nia njema ya moyo wangu na dua yangu kwa Mungu kwa ajili yao, kwa kweli, ni kwa ajili ya wokovu wao.”—Waroma 10:1.
20, 21. (a) Tunawezaje kumwiga Paulo katika huduma yetu? (b) Makala inayofuata itazungumzia jambo gani kuhusu huduma yetu?
20 Ona mambo mawili ambayo Paulo alikazia. Nia ya moyo wake ilikuwa kwamba watu fulani wapate wokovu, naye alimwomba Mungu kwa ajili yao. Leo tunamwiga Paulo. Tunadumisha nia ya moyoni ya kumtafuta mtu yeyote ambaye huenda akawa na mwelekeo unaofaa kuelekea habari njema. Tunasali daima kwa Yehova tupate watu wa aina hiyo ili tuweze kuwasaidia wafuate njia ya wokovu.—Methali 11:30; Ezekieli 33:11; Yohana 6:44.
21 Hata hivyo, ili kuwapelekea watu wengi iwezekanavyo ujumbe wa Ufalme, hatupaswi kukazia tu uangalifu kwa nini tunahubiri na kile tunachohubiri, bali pia jinsi tunavyohubiri. Makala inayofuata itazungumzia jambo hilo.
[Maelezo ya Chini]
a Makala hii itazungumzia mambo mawili ya kwanza. Makala ya pili itazungumzia jambo la tatu.
b Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-
-
Habari Njema Kwa Watu wa Mataifa YoteMnara wa Mlinzi—2005 | Julai 1
-
-
Habari Njema Kwa Watu wa Mataifa Yote
“Mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”—MATENDO 1:8.
1. Tunazingatia nini tukiwa walimu wa Biblia, na kwa nini?
WALIMU stadi hawazingatii tu mambo wanayowafundisha wanafunzi wao bali pia jinsi wanavyowafundisha. Tunafanya vivyo hivyo tukiwa walimu wa kweli ya Biblia. Tunazingatia ujumbe tunaohubiri na njia tunazotumia. Ujumbe wetu, yaani, habari njema ya Ufalme wa Mungu, haubadiliki, lakini sisi hubadili njia zetu kulingana na hali. Kwa nini? Ili tufikie watu wengi iwezekanavyo.
2. Tunamwiga nani tunapobadili njia zetu za kuhubiri?
2 Tunapobadili njia zetu za kuhubiri, tunawaiga watumishi wa zamani wa Mungu. Kwa mfano, fikiria mtume Paulo. Alisema hivi: “Kwa Wayahudi nilikuwa kama Myahudi . . . Kwa wale wasio na sheria nilikuwa kama asiye na sheria . . . Kwa walio dhaifu nilikuwa dhaifu, ili niwapate walio dhaifu. Nimekuwa mambo yote kwa watu wa namna zote, ili kwa vyovyote niwaokoe wengine.” (1 Wakorintho 9:19-23) Paulo alipata matokeo alipobadili njia zake za kuhubiri. Sisi pia tutapata matokeo tukibadili utangulizi wetu ili uwafae watu tunaozungumza nao.
Kufikia “Miisho ya Dunia”
3. (a) Tunakabili tatizo gani katika kazi yetu ya kuhubiri? (b) Maneno ya Isaya 45:22 yanatimizwaje leo?
3 Tatizo kubwa linalowakabili wale wanaohubiri habari njema ni ukubwa wa eneo, yaani, “dunia yote inayokaliwa.” (Mathayo 24:14) Katika karne iliyopita, watumishi wengi wa Yehova walijitahidi sana kwenda katika nchi nyingine ili kueneza habari njema. Matokeo yalikuwa nini? Ongezeko kubwa ajabu ulimwenguni pote. Mwanzoni mwa karne ya 20, kazi ya kuhubiri ilifanywa katika nchi chache tu, lakini leo Mashahidi wa Yehova wanahubiri kwa bidii katika nchi 235! Kwa kweli, habari njema ya Ufalme inatangazwa hata kufikia “miisho ya dunia.”—Isaya 45:22.
4, 5. (a) Ni nani ambao wametimiza jukumu muhimu katika kueneza habari njema? (b) Baadhi ya ofisi za tawi zilisema nini kuhusu wageni wanaotumika katika maeneo yaliyo chini ya ofisi hizo?
4 Kwa nini kuna ongezeko kubwa hivyo? Sababu ni nyingi. Wamishonari waliozoezwa katika Shule ya Gileadi na, hivi karibuni, wanafunzi zaidi ya 20,000 waliofuzu katika Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, wamechangia sehemu kubwa. Vilevile Mashahidi wengi ambao wamehamia nchi zenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme kwa gharama yao wamechangia pia ongezeko hilo. Wakristo hao wenye kujitolea, wanaume kwa wanawake, vijana kwa wazee, waseja na waliofunga ndoa, hutimiza sehemu muhimu sana katika kuhubiri ujumbe wa Ufalme duniani pote. (Zaburi 110:3; Waroma 10:18) Wanathaminiwa sana. Baadhi ya ofisi za tawi ziliandika hivi kuhusu wahubiri kutoka nchi nyingine waliojitolea kutumika katika maeneo yenye uhitaji mkubwa yaliyo chini ya ofisi hizo.
5 “Mashahidi hawa wapendwa huongoza katika kuhubiri maeneo ya mbali, husaidia kuanzisha makutaniko mapya, na huwasaidia ndugu na dada kukua kiroho.” (Ekuado) “Ikiwa mamia ya wageni wanaotumika huku wangeondoka, makutaniko hayangekuwa thabiti. Ni baraka kuwa nao.” (Jamhuri ya Dominika) “Katika mengi ya makutaniko yetu, kuna idadi kubwa ya akina dada, na hata katika makutaniko fulani asilimia 70 ya wahubiri ni akina dada. (Zaburi 68:11) Wengi wa dada hao ni wapya katika kweli, lakini dada waseja mapainia ambao wametoka nchi nyingine hutimiza jukumu muhimu sana la kuwazoeza. Dada hao kutoka nchi nyingine wanatusaidia sana!” (Nchi moja ya Ulaya Mashariki) Je, umewahi kufikiria kutumika katika nchi nyingine?a—Matendo 16:9, 10.
“Watu Kumi Kutoka Katika Lugha Zote”
6. Andiko la Zekaria 8:23 linaonyeshaje kwamba tungekabili tatizo la lugha katika kazi yetu ya kuhubiri?
6 Tatizo lingine kubwa tunalokabili ni lugha nyingi ambazo zinazungumzwa duniani. Neno la Mungu lilitabiri hivi: “Itakuwa katika siku hizo kwamba watu kumi kutoka katika lugha zote za mataifa watashika, ndiyo, wataushika upindo wa nguo ya mtu aliye Myahudi, wakisema: ‘Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.’” (Zekaria 8:23) Katika utimizo wa leo wa unabii huo, wale watu kumi wanawakilisha umati mkubwa, uliotabiriwa katika Ufunuo 7:9. Hata hivyo, ona kwamba kulingana na unabii wa Zekaria, hao “watu kumi” hawangetoka tu katika mataifa yote bali pia wangetoka “katika lugha zote za mataifa.” Je, tumeona sehemu hiyo muhimu ya unabii huo ikitimizwa? Bila shaka.
7. Takwimu zinaonyeshaje kwamba watu “kutoka katika lugha zote” wanahubiriwa habari njema?
7 Fikiria takwimu zifuatazo. Miaka 50 iliyopita vichapo vyetu vilichapishwa katika lugha 90. Leo, vinachapishwa katika lugha zaidi ya 400. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” amefanya yote awezayo kutayarisha vichapo hata katika lugha ambazo zinazungumzwa na watu wachache. (Mathayo 24:45) Kwa mfano, vichapo vya Biblia sasa vinapatikana katika lugha ya Greenland (inayozungumzwa na watu 47,000), lugha ya Palau (inayozungumzwa na watu 15,000), na Yapese (inayozungumzwa na watu wasiozidi 7,000).
“Mlango Mkubwa” Unaotokeza Nafasi Mpya
8, 9. Ni jambo gani limetufungulia “mlango mkubwa,” na maelfu ya Mashahidi wamekabilianaje na hali hiyo?
8 Siku hizi si lazima twende nchi nyingine ili tuwahubirie watu wa lugha zote habari njema. Katika miaka ya karibuni, mamilioni ya wakimbizi na wahamiaji wanaozungumza lugha mbalimbali wamehamia nchi zilizoendelea kiuchumi. Kwa mfano, huko Paris, Ufaransa, lugha 100 hivi zinazungumzwa. Huko Toronto, Kanada, kuna lugha 125; na London, Uingereza, lugha zaidi ya 300 za kigeni zinazungumzwa! Watu hao kutoka nchi nyingine wanaishi katika maeneo mengi ya makutaniko na hilo limefungua “mlango mkubwa” unaotokeza nafasi mpya za kuwahubiria habari njema watu kutoka katika mataifa yote.—1 Wakorintho 16:9.
9 Maelfu ya Mashahidi wanakabiliana na hali hiyo kwa kujifunza lugha nyingine. Si rahisi kwa wengi wao. Hata hivyo, jitihada zao si za bure kwani wanapata shangwe wanapowasaidia wakimbizi na wahamiaji kujifunza kweli ya Neno la Mungu. Katika mwaka mmoja wa hivi karibuni, asilimia 40 hivi ya wote waliobatizwa kwenye makusanyiko ya wilaya katika nchi moja ya Ulaya Magharibi walikuwa wahamiaji kutoka nchi nyingine.
10. Umekitumiaje kijitabu Habari Njema kwa Watu wa Mataifa Yote? (Ona sanduku “Yaliyomo Katika Kijitabu Habari Njema kwa Watu wa Mataifa Yote,” kwenye ukurasa wa 26.)
10 Ni kweli kwamba wengi wetu hatuwezi kujifunza lugha ya kigeni. Hata hivyo, tunaweza kuwasaidia wahamiaji kwa kutumia vizuri kijitabu kipya cha Habari Njema kwa Watu wa Mataifa Yote (Kiingereza na Kifaransa),b ambacho kina ujumbe wa Biblia wenye kuvutia katika lugha mbalimbali. (Yohana 4:37) Je, unakitumia kijitabu hicho katika huduma?
Watu Wanapokataa Habari Njema
11. Ni tatizo gani lingine tunalokabili katika maeneo fulani?
11 Uvutano wa Shetani unapoongezeka duniani, mara nyingi tunakabili tatizo lingine—katika maeneo fulani watu wengi wanakataa habari njema. Bila shaka, hatushangazwi na hali hiyo kwa kuwa Yesu alitabiri kwamba ingekuwa hivyo. Alisema hivi kuhusu siku zetu: “Upendo wa walio wengi zaidi utapoa.” (Mathayo 24:12) Kwa kweli, imani ya wengi katika Mungu na heshima yao kuelekea Biblia imepungua. (2 Petro 3:3, 4) Ndiyo sababu katika sehemu fulani za ulimwengu ni watu wachache sana wanaokuwa wanafunzi wa Kristo. Lakini hilo halimaanishi kwamba jitihada za ndugu na dada zetu Wakristo wapendwa ambao wanahubiri kwa uaminifu katika maeneo kama hayo magumu ni za bure. (Waebrania 6:10) Kwa nini? Fikiria mambo yafuatayo.
12. Kazi yetu ya kuhubiri inatimiza makusudi gani mawili?
12 Injili ya Mathayo inakazia makusudi mawili makuu ya kazi yetu ya kuhubiri. Kusudi moja ni ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mathayo 28:19) Kusudi la pili ni kwamba ujumbe wa Ufalme unatolewa kuwa “ushahidi.” (Mathayo 24:14) Makusudi yote mawili ni muhimu, lakini kusudi la pili ni la pekee. Kwa nini?
13, 14. (a) Ni sehemu gani kuu ya ishara ya kuwapo kwa Kristo? (b) Tunapaswa kukumbuka nini hasa tunapohubiri katika maeneo magumu?
13 Mwandishi wa Biblia, Mathayo, aliandika swali hili ambalo mitume walimuuliza Yesu: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3) Yesu aliwajibu kwamba kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote ingekuwa sehemu kuu ya ishara hiyo. Je, alimaanisha kufanya wanafunzi? Hapana. Alisema: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14) Kwa hiyo, Yesu alionyesha kwamba kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme ingekuwa sehemu muhimu ya ishara hiyo.
14 Basi, tunapohubiri habari njema ya Ufalme, tunakumbuka kwamba hata ikiwa nyakati nyingine hatufaulu kufanya wanafunzi, tunafaulu kutoa “ushahidi.” Iwe watu wanakubali au la, wao wanajua kazi tunayofanya, hivyo tunashiriki kutimiza unabii wa Yesu. (Isaya 52:7; Ufunuo 14:6, 7) Shahidi mmoja kijana kutoka Ulaya Magharibi anayeitwa Jordy alisema hivi: “Mimi hufurahi sana kujua kwamba Yehova ananitumia kutimiza Mathayo 24:14.” (2 Wakorintho 2:15-17) Hapana shaka kwamba unahisi vivyo hivyo.
Ujumbe Wetu Unapopingwa
15. (a) Yesu aliwaonya wafuasi wake kimbele kuhusu nini? (b) Ni nini hutuwezesha kuhubiri licha ya upinzani?
15 Tatizo lingine ni upinzani mkali kuelekea kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme. Yesu aliwaonya kimbele wafuasi wake hivi: “Mtachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.” (Mathayo 24:9) Kama Wakristo wa mapema, wafuasi wa Yesu leo wamechukiwa, wamepingwa, na kuteswa. (Matendo 5:17, 18, 40; 2 Timotheo 3:12; Ufunuo 12:12, 17) Katika nchi fulani, wamepigwa marufuku na serikali. Hata hivyo, Wakristo wa kweli katika nchi hizo wanaendelea kuhubiri habari njema ya Ufalme kwa sababu wanataka kumtii Mungu. (Amosi 3:8; Matendo 5:29; 1 Petro 2:21) Ni nini kinachowawezesha Wakristo hao na Mashahidi wengine ulimwenguni pote kuendelea kuhubiri? Yehova huwatia nguvu kwa roho yake takatifu.—Zekaria 4:6; Waefeso 3:16; 2 Timotheo 4:17.
16. Yesu alionyeshaje uhusiano uliopo kati ya kazi ya kuhubiri na roho ya Mungu?
16 Yesu alikazia uhusiano uliopo kati ya roho ya Mungu na kazi ya kuhubiri alipowaambia wafuasi wake hivi: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8; Ufunuo 22:17) Mfuatano wa matukio katika andiko hilo ni muhimu. Kwanza, wanafunzi walipokea roho takatifu, kisha wakaanza kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote. Wangeweza tu kuvumilia katika kazi ya kutoa “ushahidi kwa mataifa yote” kwa msaada wa roho ya Mungu. (Mathayo 24:13, 14; Isaya 61:1, 2) Ndiyo sababu Yesu alisema kwamba roho takatifu ni “msaidizi.” (Yohana 15:26) Alisema kwamba roho ya Mungu ingewafundisha na kuwaongoza wanafunzi wake.—Yohana 14:16, 26; 16:13.
17. Roho takatifu hutusaidiaje tunapopingwa vikali?
17 Roho ya Mungu inatusaidiaje leo wakati kazi yetu ya kuhubiri habari njema inapopingwa vikali? Roho ya Mungu hutuimarisha, nayo huwapinga wale wanaotutesa. Ili kuelewa hilo, fikiria tukio moja katika maisha ya Mfalme Sauli.
Apingwa na Roho ya Mungu
18. (a) Sauli alibadilikaje akawa mbaya sana? (b) Sauli alimtesa Daudi katika njia zipi?
18 Sauli alianza vyema akiwa mfalme wa kwanza wa Israeli, lakini baadaye akamwasi Yehova. (1 Samweli 10:1, 24; 11:14, 15; 15:17-23) Kwa hiyo roho ya Mungu ikaacha kumtegemeza mfalme huyo. Sauli alimkasirikia sana Daudi, ambaye alitiwa mafuta kuwa mfalme anayefuata wa Israeli na aliyetegemezwa na roho ya Mungu. (1 Samweli 16:1, 13, 14) Daudi alionekana kuwa anaweza kushambuliwa kwa urahisi kwa sababu alikuwa na kinubi tu hali Sauli alikuwa na mkuki. Kwa hiyo, siku moja Daudi alipokuwa akipiga kinubi, ‘Sauli aliutupa mkuki na kusema: “Nitampigilia Daudi ukutani!” lakini Daudi akakwepa kutoka mbele yake, mara mbili.’ (1 Samweli 18:10, 11) Baadaye, Sauli alimsikiliza mwanaye Yonathani, rafiki ya Daudi, na kuapa hivi: “Kama Yehova anavyoishi, [Daudi] hatauawa.” Lakini Sauli ‘akatafuta tena kumpigilia Daudi ukutani kwa mkuki.’ Hata hivyo, Daudi “akakwepa kutoka mbele ya Sauli, hivi kwamba akaupigilia mkuki ule ndani ya ukuta.” Daudi alikimbia, lakini Sauli akamfuata. Wakati huo hatari, roho ya Mungu ilimpinga Sauli. Jinsi gani?—1 Samweli 19:6, 10.
19. Roho ya Mungu ilimlindaje Daudi?
19 Daudi alikimbia hadi kwa nabii Samweli, lakini Sauli akawatuma wajumbe wake wakamkamate Daudi. Hata hivyo, walipofika mahali ambapo alikuwa amejificha, ‘roho ya Mungu ikaja juu ya wajumbe hao wa Sauli, nao pia wakaanza kutenda kama manabii.’ Walilemewa sana na roho ya Mungu hivi kwamba walisahau kabisa sababu iliyowaleta hapo. Sauli aliwatuma wajumbe mara mbili zaidi ili wamlete Daudi, nao pia wakalemewa na roho ya Mungu. Mwishowe, Mfalme Sauli mwenyewe alienda kumtafuta Daudi, lakini Sauli pia akashindwa kustahimili roho ya Mungu. Kwa kweli, roho takatifu ilimfanya alale chini “mchana huo wote na usiku huo wote,” hivyo Daudi akawa na wakati wa kutosha wa kukimbia.—1 Samweli 19:20-24.
20. Tunajifunza nini kutokana na simulizi la jinsi Sauli alivyomtesa Daudi?
20 Simulizi hilo kuhusu Sauli na Daudi linatufundisha jambo lenye kutia moyo sana: Watu wanaowatesa watumishi wa Mungu hawawezi kufaulu wanapopingwa na roho ya Mungu. (Zaburi 46:11; 125:2) Yehova alikusudia Daudi awe mfalme wa Israeli. Hakuna mtu yeyote angeweza kubadili kusudi hilo. Katika siku zetu, Yehova amekusudia kwamba “habari njema ya ufalme itahubiriwa.” Hakuna mtu yeyote anayeweza kuzuia kazi hiyo.—Matendo 5:40, 42.
21. (a) Baadhi ya wapinzani leo hutendaje? (b) Tuna uhakika gani?
21 Viongozi fulani wa kidini na wa kisiasa hutumia uwongo na hata jeuri kujaribu kutuzuia kufanya kazi hiyo. Hata hivyo, Yehova atawalinda watu wake leo kama alivyomlinda Daudi kiroho. (Malaki 3:6) Kwa hiyo, tunasema hivi kwa uhakika kama Daudi: “Nimeweka tegemeo langu katika Mungu. Sitaogopa. Mtu wa udongo anaweza kunitenda nini?” (Zaburi 56:11; 121:1-8; Waroma 8:31) Kwa msaada wa Yehova, na tuendelee kukabiliana na matatizo yote tunapotekeleza kazi aliyotukabidhi ya kuwahubiria watu wa mataifa yote habari njema ya Ufalme.
[Maelezo ya Chini]
a Ona sanduku “Ninaridhika Sana,” kwenye ukurasa wa 22.
b Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-