Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kuna Habari Njema Ambayo Watu Wote Wanahitaji
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Juni 15
    • Kuna Habari Njema Ambayo Watu Wote Wanahitaji

      “Habari njema . . . kwa kweli, hiyo ni nguvu za Mungu kwa ajili ya wokovu.”—ROM. 1:16.

      1, 2. Kwa nini unahubiri “habari njema ya ufalme,” na unakazia mambo gani kuhusu habari hiyo?

      ‘NINAFURAHI kuwahubiria watu habari njema kila siku.’ Inaelekea kwamba umewahi kusema au kufikiria maneno hayo. Ukiwa Shahidi wa Yehova ambaye amejitoa, unajua jinsi lilivyo jambo la maana kuhubiri “hii habari njema ya ufalme.” Labda unaweza kusema kutoka akilini unabii wa Yesu kuhusu kufanya kazi hiyo.—Mt. 24:14.

      2 Unapohubiri “habari njema ya ufalme,” unaendelea kufanya kazi ambayo Yesu alianzisha. (Soma Luka 4:43.) Bila shaka, jambo moja ambalo unakazia ni kwamba hivi karibuni Mungu ataingilia kati ya mambo ya wanadamu. Kupitia ile “dhiki kuu,” atamaliza dini ya uwongo na kuondoa uovu wote duniani. (Mt. 24:21) Huenda pia unakazia kwamba Ufalme wa Mungu utarudisha tena Paradiso duniani ili amani na furaha isitawi. Kwa kweli, “habari njema ya ufalme” ni sehemu ya “habari njema [iliyotangazwa] kimbele kwa Abrahamu, yaani: ‘Kupitia kwako mataifa yote yatabarikiwa.’”—Gal. 3:8.

      3. Kwa nini tunaweza kusema kwamba mtume Paulo alikazia habari njema katika kitabu cha Waroma?

      3 Je, inawezekana kwamba huenda hatukazii sana jambo fulani la maana kuhusu habari njema ambalo watu wanahitaji? Katika barua yake kwa Waroma, mtume Paulo alitumia neno “ufalme” mara moja tu, lakini alitumia maneno “habari njema” mara 12. (Soma Waroma 14:17.) Ni jambo gani kuhusu habari njema ambalo Paulo alitaja mara nyingi katika kitabu hicho? Kwa nini jambo hilo kuhusu habari njema ni la maana sana? Na kwa nini tunapaswa kukumbuka jambo hilo tunapowahubiria watu “habari njema ya Mungu” katika eneo letu?—Marko 1:14; Rom. 15:16; 1 The. 2:2.

      Jambo Ambalo Watu Walioishi Huko Roma Walihitaji

      4. Paulo alihubiri kuhusu nini alipokuwa amefungwa kwa mara ya kwanza huko Roma?

      4 Tunajifunza mengi tunapochunguza mambo ambayo Paulo alizungumzia alipofungwa kwa mara ya kwanza huko Roma. Tunasoma kwamba alipotembelewa na kikundi cha Wayahudi, ‘alitoa ushahidi kamili kuhusiana na (1) ufalme wa Mungu na kutumia ushawishi kwao kuhusu (2) Yesu.’ Matokeo yalikuwa nini? “Wengine wakaanza kuamini mambo yaliyosemwa; wengine hawakuamini.” Baada ya hapo, Paulo alikuwa ‘akiwakaribisha kwa fadhili wale wote walioingia ndani kwake, akiwahubiria (1) ufalme wa Mungu na kufundisha mambo yanayohusu (2) Bwana Yesu Kristo.’ (Mdo. 28:17, 23-31) Ni wazi kwamba Paulo alikazia Ufalme wa Mungu. Lakini ni jambo gani lingine ambalo alikazia? Jambo fulani la msingi kuhusiana na Ufalme, yaani, daraka la Yesu katika kusudi la Mungu.

      5. Ni uhitaji gani hasa ambao Paulo alizungumzia katika kitabu cha Waroma?

      5 Watu wote wanahitaji kumjua Yesu na kumwamini. Katika kitabu cha Waroma, Paulo alizungumzia uhitaji huo. Kabla ya hapo, aliandika kuhusu “Mungu, ambaye ninamtolea utumishi mtakatifu kwa roho yangu kuhusiana na ile habari njema juu ya Mwana wake.” Aliongezea hivi: “Siionei aibu habari njema; kwa kweli, hiyo ni nguvu za Mungu kwa ajili ya wokovu kwa kila mtu aliye na imani.” Baadaye alizungumza kuhusu wakati “Mungu anapohukumu kupitia Kristo Yesu mambo ya siri ya wanadamu, kulingana na habari njema ninayoitangaza.” Na akasimulia hivi: “Kutoka Yerusalemu na kuzunguka mpaka Ilirikamu nimehubiri kikamili habari njema juu ya Kristo.”a (Rom. 1:9, 16; 2:16; 15:19) Unafikiri ni kwa nini Paulo alikazia habari kuhusu Yesu Kristo alipowaandikia Waroma?

      6, 7. Tunaweza kusema nini kuhusu kuanzishwa kwa kutaniko la Roma na kuhusu watu waliokuwa katika kutaniko hilo?

      6 Hatujui jinsi kutaniko la Roma lilivyoanzishwa. Je, Wayahudi au watu waliogeuzwa imani ambao walikuwapo wakati wa Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. walirudi Roma wakiwa Wakristo? (Mdo. 2:10) Au je, wafanyabiashara na wasafiri waliokuwa Wakristo ndio walioeneza kweli huko Roma? Kwa vyovyote vile, Paulo alipoandika kitabu hicho, karibu mwaka wa 56 W.K., tayari kutaniko hilo lilikuwa limeanzishwa muda mrefu kabla ya mwaka huo. (Rom. 1:8) Kutaniko hilo lilikuwa na watu wa aina gani?

      7 Wengine wao walikuwa na asili ya Kiyahudi. Paulo anawasalimu Androniko na Yunia akiwaita “jamaa zangu,” inaelekea anamaanisha watu wa ukoo ambao walikuwa Wayahudi wenzake. Akila aliyekuwa akitengeneza mahema huko Roma pamoja na mke wake Prisila, alikuwa pia Myahudi. (Rom. 4:1; 9:3, 4; 16:3, 7; Mdo. 18:2) Lakini inaelekea kwamba ndugu na dada wengi ambao Paulo aliwatumia salamu walikuwa Watu wa Mataifa. Huenda wengine wao walikuwa watu “wa nyumbani mwa Kaisari,” labda ikimaanisha watumwa na maofisa wa cheo cha chini wa Kaisari.—Flp. 4:22; Rom. 1:6; 11:13.

      8. Watu waliokuwa huko Roma walikuwa katika hali gani ngumu?

      8 Kila Mkristo huko Roma alikuwa katika hali ngumu na kila mmoja wetu pia yuko katika hali hiyo. Paulo alieleza hivi hali hiyo: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Rom. 3:23) Ni wazi kwamba watu wote ambao Paulo aliwaandikia walihitaji kutambua kwamba walikuwa watenda-dhambi na walipaswa kuwa na imani katika njia ya Mungu ya kutimiza uhitaji huo.

      Kutambua Tatizo la Dhambi

      9. Paulo alikazia matokeo gani ambayo yanaweza kuletwa na habari njema?

      9 Mapema katika barua kwa Waroma, Paulo alitaja kuhusu matokeo mazuri ajabu ambayo yangetokana na habari njema ambayo alitaja mara nyingi: “Siionei aibu habari njema; kwa kweli, hiyo ni nguvu za Mungu kwa ajili ya wokovu kwa kila mtu aliye na imani, kwa Myahudi kwanza na pia kwa Mgiriki.” Ndiyo, watu wangeweza kuokolewa. Hata hivyo, imani ilihitajiwa, kulingana na kweli muhimu inayotegemea Habakuki 2:4: “Mwadilifu—ataishi kwa njia ya imani.” (Rom. 1:16, 17; Gal. 3:11; Ebr. 10:38) Lakini hiyo habari njema, ambayo inaweza kufanya mtu aokolewe, inahusiana jinsi gani na ukweli wa kwamba “wote wamefanya dhambi”?

      10, 11. Kwa nini jambo linalotajwa katika Waroma 3:23 si jipya kwa watu fulani lakini ni jipya kwa wengine?

      10 Kabla mtu hajasitawisha imani inayoweza kuokoa uhai wake, ni lazima akubali kwamba yeye ni mtenda-dhambi. Hilo si wazo jipya kwa wale ambao tangu utotoni wamemwamini Mungu na kujua Biblia kwa kiasi fulani. (Soma Mhubiri 7:20.) Iwe wanakubali au wana mashaka, hata hivyo, wanajua kwa kadiri fulani Paulo alimaanisha nini aliposema: “Wote wamefanya dhambi.” (Rom. 3:23) Lakini, tunapoendelea kutimiza huduma yetu, tunaweza kukutana na watu ambao hawaelewi maneno hayo.

      11 Katika nchi fulani, tangu utotoni mtu wa kawaida hafundishwi kwamba alizaliwa akiwa mwenye dhambi, na kwamba alirithi dhambi. Ni kweli kwamba huenda akatambua kuwa anakosea, ana tabia zisizopendeza, na huenda amefanya mambo fulani mabaya. Na anaona kwamba watu wengine wako katika hali kama yake. Hata hivyo, kwa sababu ya malezi yake, haelewi kwa kweli ni kwa nini yeye na wengine wako hivyo. Hata katika lugha fulani, ukisema kwamba mtu ni mtenda-dhambi, huenda wengine wakafikiri unasema kwamba mtu huyo ni mhalifu au amevunja sheria fulani. Bila shaka, huenda isiwe rahisi kwa mtu anayelelewa katika mazingira kama hayo kufikiri kwamba yeye ni mtenda-dhambi kwa njia ambayo Paulo alimaanisha.

      12. Kwa nini watu wengi hawaamini kwamba wanadamu wote ni watenda-dhambi?

      12 Hata katika nchi zinazodai kuwa za Kikristo, watu wengi hawaamini kwamba wao ni watenda-dhambi. Kwa nini? Hata kama wanaenda kanisani mara kwa mara, wanaona simulizi la Biblia kuhusu Adamu na Hawa kuwa hadithi tu. Wengine wanalelewa katika mazingira ambayo watu hawaamini kwamba kuna Mungu. Hivyo, wana shaka kuhusu kuwapo kwa Mungu na hawaelewi kwamba Mtu Mkuu Kuliko Wote aliwawekea wanadamu viwango vya maadili na kwamba kutofuata viwango hivyo ni dhambi. Kwa njia fulani, wao ni kama watu walioishi katika karne ya kwanza ambao Paulo alisema kwamba ‘hawakuwa na tumaini’ na ‘walikuwa bila Mungu katika ulimwengu.’—Efe. 2:12.

      13, 14. (a) Ni sababu gani moja inayofanya wale wasioamini kwamba kuna Mungu na pia dhambi wasiweze kujitetea? (b) Kutoamini kwamba kuna Mungu na pia dhambi kumewaongoza watu wengi kufanya nini?

      13 Katika barua kwa Waroma, Paulo alitoa sababu mbili zinazoonyesha kwa nini malezi kama hayo hayawezi kuwa kisingizio leo na hata wakati wa zamani. Sababu ya kwanza ni kuwa uumbaji wenyewe unatoa ushahidi wa kwamba kuna Muumba. (Soma Waroma 1:19, 20.) Hilo linapatana na maneno ambayo Paulo alisema alipowaandikia Waebrania akiwa huko Roma: “Kila nyumba hujengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.” (Ebr. 3:4) Hata hivyo, sababu aliyotoa inaonyesha kwamba kuna Muumba aliyeujenga, au kuutokeza, ulimwengu wote mzima.

      14 Kwa hiyo, Paulo alikuwa na sababu nzuri ya kuwaandikia Waroma kwamba mtu yeyote ‘hakuwa na sababu ya kujitetea,’ kutia ndani Waisraeli wa kale ambao waliabudu sanamu zisizo na uhai. Inaweza kusemwa hivyo pia kuhusu wale ambao walijiingiza katika mwenendo mpotovu kingono kinyume cha matumizi ya asili ya mwili wa mwanamume na mwanamke. (Rom. 1:22-27) Akirejelea sababu kama hizo, kwa kufaa Paulo alikata kauli kwamba “Wayahudi na vilevile Wagiriki wote wako chini ya dhambi.”—Rom. 3:9.

      ‘Mtoa Ushahidi’

      15. Ni nani ambao wana dhamiri, na hilo lina matokeo gani?

      15 Kitabu cha Waroma kinataja sababu nyingine ambayo inapaswa kuwafanya watu watambue kwamba wao ni watenda-dhambi na wanahitaji msaada ili watoke katika hali hiyo ngumu. Kuhusu sheria ambazo Mungu aliwapa Waisraeli wa kale, Paulo aliandika hivi: “Wale wote waliofanya dhambi chini ya sheria watahukumiwa kwa sheria.” (Rom. 2:12) Akiendelea kutoa sababu zake, anasema kwamba mara nyingi vikundi vya jamii au watu wa mataifa ambao hawajui sheria za Mungu ‘wanafanya kwa asili mambo ya sheria.’ Kwa nini watu kama hao kwa kawaida wanapinga ngono kati ya watu wa ukoo, kuua, na kuiba? Paulo alitaja sababu: Wana dhamiri.—Soma Waroma 2:14, 15.

      16. Kwa nini kuwa na dhamiri hakumaanishi kwamba mtu ataepuka dhambi?

      16 Hata hivyo, inaelekea umeona kwamba kuwa na dhamiri inayofanya kazi kama mtoa ushahidi ndani yetu hakumaanishi kwamba mtu atafuata mwongozo wa dhamiri hiyo. Mfano wa Waisraeli wa kale unaonyesha jambo hilo. Ingawa Waisraeli walikuwa na dhamiri waliyopewa na Mungu na sheria zilizo wazi kutoka kwa Mungu ambazo zilikataza kuiba na kufanya uzinzi, mara nyingi walipuuza dhamiri zao na wakavunja Sheria ya Yehova. (Rom. 2:21-23) Walikuwa na hatia mara mbili na hivyo bila shaka wakawa watenda-dhambi, na kushindwa kufuata viwango vya Mungu na mapenzi yake. Hilo liliharibu kabisa uhusiano wao na Muumba wao.—Law. 19:11; 20:10; Rom. 3:20.

      17. Tunatiwa moyo jinsi gani na kitabu cha Waroma?

      17 Huenda mambo ambayo tumechunguza katika kitabu cha Waroma yakafanya mtu afikiri kwamba wanadamu wana hali yenye kuhuzunisha sana mbele za Mweza-Yote, kutia ndani sisi. Hata hivyo, Paulo hakuachia hapo. Akitaja maneno ya Daudi katika Zaburi 32:1, 2, mtume huyo aliandika hivi: “Wenye furaha ni wale ambao matendo yao ya kuasi sheria yamesamehewa na ambao dhambi zao zimefunikwa; mwenye furaha ni mtu ambaye Yehova hatahesabu dhambi yake kamwe.” (Rom. 4:7, 8) Ndiyo, Mungu amepanga njia nzuri ya kisheria ya kusamehe dhambi.

      Habari Njema Iliyokazia Yesu

      18, 19. (a) Katika katibu cha Waroma, Paulo alikazia fikira jambo gani kuhusu habari njema? (b) Tunapaswa kutambua nini ili tupate baraka za Ufalme?

      18 Kwa kufaa huenda ukasema hivi: “Kwa kweli hiyo ni habari njema!” Bila shaka hiyo ni habari njema, na hilo linaturudisha kwenye jambo fulani kuhusu habari njema ambalo Paulo alikazia katika kitabu cha Waroma. Kama ilivyotajwa, Paulo aliandika hivi: “Siionei aibu habari njema; kwa kweli, hiyo ni nguvu za Mungu kwa ajili ya wokovu.”—Rom. 1:15, 16.

      19 Hiyo habari njema ilikazia daraka la Yesu katika kutimiza kusudi la Mungu. Paulo alitazamia ‘siku ambayo Mungu atahukumu kupitia Kristo Yesu mambo ya siri ya wanadamu, kulingana na habari njema.’ (Rom. 2:16) Aliposema hivyo, hakuwa akipunguza uzito wa “ufalme wa Kristo na wa Mungu” au mambo ambayo Mungu atafanya kupitia Ufalme. (Efe. 5:5) Lakini alionyesha kwamba ili tuishi na kufurahia baraka ambazo zitaletwa na Ufalme wa Mungu, ni lazima tutambue (1) hali yetu tukiwa watenda-dhambi machoni pa Mungu na (2) kwa nini tunahitaji kuwa na imani katika Yesu Kristo ili dhambi zetu zisamehewe. Mtu anapoelewa na kukubali mambo hayo kuhusu kusudi la Mungu na kuona hali ambazo atafurahia wakati ujao, anaweza kwa kufaa kusema hivi: “Kwa kweli, hiyo ni habari njema!”

      20, 21. Katika huduma yetu, kwa nini tunapaswa kukumbuka habari njema inayokaziwa katika kitabu cha Waroma, na tunaweza kupata matokeo gani?

      20 Bila shaka, tunapaswa kukumbuka jambo hilo kuhusu habari njema tunapoendelea na huduma yetu ya Kikristo. Akizungumza kuhusu Yesu, Paulo alinukuu maneno ya Isaya: “Yeyote anayemwamini hatakata tamaa.” (Rom. 10:11; Isa. 28:16) Huenda ujumbe wa msingi kumhusu Yesu usiwe mpya kwa wale ambao wanaelewa mambo ambayo Biblia inasema kuhusu dhambi. Hata hivyo, kwa wengine, ujumbe huo ni mpya kabisa, jambo ambalo halijulikani au ambalo kwa kawaida watu hawaliamini katika jamii zao. Watu kama hao wanapomwamini Mungu na kuamini Maandiko, tutahitaji kueleza daraka la Yesu. Habari inayofuata itazungumzia jinsi Waroma sura ya 5 inavyoeleza jambo hilo kuhusu habari njema. Huenda utaona kwamba funzo hilo litakusaidia katika huduma yako.

      21 Ni jambo lenye kuthawabisha kama nini kuwasaidia watu wenye mioyo minyoofu kuelewa habari njema inayotajwa tena na tena katika kitabu cha Waroma, habari njema ambayo ‘kwa kweli, ni nguvu za Mungu kwa ajili ya wokovu kwa kila mtu aliye na imani.’ (Rom. 1:16) Mbali na kuthawabishwa kwa njia hiyo, tutaona wengine wakikubaliana na maneno ambayo Paulo alinukuu katika Waroma 10:15: “Jinsi ilivyo yenye kupendeza miguu ya wale wanaotangaza habari njema ya mambo mema!”—Isa. 52:7.

      [Maelezo ya Chini]

      a Maneno kama hayo yanapatikana katika vitabu vingine vilivyoandikwa chini ya mwongozo wa roho ya Mungu.—Marko 1:1; Mdo. 5:42; 1 Kor. 9:12; Flp. 1:27.

  • Mungu Anapendekeza Upendo Wake Kwetu
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Juni 15
    • Mungu Anapendekeza Upendo Wake Kwetu

      “Fadhili zisizostahiliwa [zitatawala] kama mfalme kupitia uadilifu kwa tazamio la uzima wa milele.”—ROM. 5:21.

      1, 2. Tunaweza kufikiria zawadi gani mbili, lakini ni zawadi gani ambayo ina thamani kubwa zaidi?

      “ZAWADI kubwa zaidi ambayo Waroma . . . waliwapatia wale waliotawala baada yao ni sheria yao na wazo la kwamba watu wanapaswa kuishi kulingana na sheria.” (Dakt. David J. Williams wa Chuo Kikuu cha Melbourne, Australia) Hata iwe jambo hilo ni la kweli kadiri gani, kuna zawadi ambayo ina thamani kubwa hata zaidi. Zawadi hiyo ni mpango wa Mungu wa kutuwezesha kuwa na msimamo unaokubalika na wenye uadilifu mbele zake na tumaini la kuokolewa na kupata uzima wa milele.

      2 Katika njia fulani, kulikuwa na mambo ya kisheria ambayo yalihusu jinsi Mungu alivyotoa zawadi hiyo. Katika Waroma sura ya 5, mtume Paulo hakutaja mambo hayo kana kwamba ni makubaliano ya kisheria ambayo hayategemei hisia zozote. Badala yake alianza kwa kutoa uhakikisho huu wenye kusisimua: “Tumetangazwa kuwa waadilifu kutokana na imani, [basi] na tufurahie amani pamoja na Mungu kupitia Bwana wetu Yesu Kristo.” Wale wanaopokea zawadi hiyo kutoka kwa Mungu wanachochewa kumpenda pia. Paulo alikuwa mmoja wa watu hao. Aliandika hivi: “Upendo wa Mungu umemiminwa ndani ya mioyo yetu kupitia roho takatifu.”—Rom. 5:1, 5.

      3. Ni maswali au maulizo gani ambayo yanajitokeza?

      3 Hata hivyo, kwa nini zawadi hiyo ya upendo ilihitajiwa? Mungu angeweza kuitoa jinsi gani kwa njia ya haki, na kwa usawaziko? Na watu wanapaswa kufanya nini ili wastahili kuipokea? Acheni tutafute majibu yenye kuridhisha na tuone jinsi yanavyokazia upendo wa Mungu.

      Upendo wa Mungu Unashinda Dhambi

      4, 5. (a) Yehova alionyesha upendo wake katika njia gani kubwa? (b) Ni ujuzi kuhusu mambo gani ambao unatuwezesha kuelewa Waroma 5:12?

      4 Katika tendo ambalo lilionyesha upendo mkubwa, Yehova alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee ili kuwasaidia wanadamu. Paulo alieleza jambo hilo hivi: “Mungu hupendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.” (Rom. 5:8) Fikiria jambo moja la hakika ambalo limetajwa hapo: “Tulipokuwa tungali watenda-dhambi.” Wote wanapaswa kujua jinsi hali hiyo ilivyotokea.

      5 Paulo alieleza hali hiyo, alipoanza kwa kutaja jambo hili: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Rom. 5:12) Tunaweza kuelewa jambo hilo kwa sababu Mungu aliongoza mambo ili masimulizi yaandikwe ambayo yanaonyesha jinsi maisha ya mwanadamu yalivyoanza. Yehova aliwaumba wanadamu wawili, Adamu na Hawa. Muumba ni mkamilifu, na wanadamu hao wa kwanza ambao ni wazazi wetu, walikuwa pia wakamilifu. Mungu aliwapa sheria moja tu ambayo walipaswa kufuata na akawaambia kwamba kutotii sheria hiyo kungeleta adhabu ya kifo. (Mwa. 2:17) Hata hivyo, walichagua kuasi, huku wakipuuza mwongozo wa Mungu uliokuwa wenye usawaziko, na hivyo wakamkataa Mungu kuwa Mpaji-Sheria na Mwenye Enzi Kuu.—Kum. 32:4, 5.

      6. (a) Kwa nini wazao wa Adamu walikufa kabla Mungu hajatoa Sheria ya Musa na baada ya hapo? (b) Ni hali gani ambayo inaweza kulinganishwa na ugonjwa kama wa damu kutoganda?

      6 Adamu alipata watoto baada ya kutenda dhambi, na hivyo akawapitishia wote dhambi na matokeo yake mabaya. Bila shaka, watoto hao hawakuwa wamevunja sheria ya Mungu kama Adamu alivyofanya, kwa hiyo hawakushtakiwa kwa dhambi hiyohiyo; na pia hakukuwa na sheria yoyote iliyokuwa imeandikwa wakati huo. (Mwa. 2:17) Hata hivyo, bado wazao wa Adamu walirithi dhambi. Hivyo, dhambi na kifo vilitawala mpaka wakati Mungu alipowapa Waisraeli sheria iliyoandikwa, ambayo ilionyesha wazi kwamba walikuwa watenda-dhambi. (Soma Waroma 5:13, 14.) Matokeo mabaya ya dhambi tuliyorithi yanaweza kufananishwa na magonjwa na kasoro fulani zinazorithiwa kama vile upungufu wa damu, au hemofilia yaani, ugonjwa wa damu kutoganda. Huenda umewahi kusoma kwamba Alexis, mwana wa Alexandra na Nicholas wa Pili mtawala wa Urusi, alirithi ugonjwa wa damu kutoganda unaoitwa hemofilia. Ni kweli kwamba katika familia kama hiyo, watoto fulani hawasumbuliwi na magonjwa kama hayo, lakini huenda wakawa na magonjwa hayo mwilini. Lakini hali ni tofauti kabisa kuhusu dhambi. Matokeo mabaya ya dhambi ya Adamu hayangeweza kuepukika. Wote wanapatwa na matokeo hayo. Sikuzote yanasababisha kifo. Na watoto wote wanarithi matokeo hayo. Je, matokeo hayo mabaya yangeweza kuondolewa?

      Mpango Ambao Mungu Alifanya Kupitia Yesu Kristo

      7, 8. Maisha ya wanaume wawili wakamilifu yalileta jinsi gani matokeo tofauti?

      7 Kwa upendo, Mungu alifanya mpango ili wanadamu wawe huru kutokana na dhambi waliyorithi. Paulo alieleza kwamba hilo liliwezekana kupitia mwanadamu mwingine, mwanamume mkamilifu aliyeishi baadaye, yaani, Adamu wa pili. (1 Kor. 15:45) Lakini maisha ya kila mmoja wa wanaume hao wawili wakamilifu yameleta matokeo yaliyo tofauti kabisa. Jinsi gani?—Soma Waroma 5:15, 16.

      8 Paulo aliandika hivi: “Sivyo ilivyo kwa ile zawadi kama ilivyokuwa kwa lile kosa.” Adamu alikuwa na hatia ya kosa hilo, na kwa haki alipokea adhabu kali, alikufa. Hata hivyo, hangekufa peke yake. Tunasoma hivi: “Kwa kosa la mtu [huyo] mmoja wengi walikufa.” Hukumu ya haki iliyotolewa kwa Adamu ilitaka kwamba wazao wake wote wasio wakamilifu wapate adhabu hiyohiyo, kutia ndani sisi. Lakini bado tunaweza kufarijiwa kwa kujua kwamba mwanamume mkamilifu, Yesu, angeweza kuleta matokeo yaliyo kinyume kabisa. Matokeo gani? Tunapata jibu katika maneno haya ya Paulo: “Kutangazwa [kwa watu wa namna zote] kuwa waadilifu kwa ajili ya uzima.”—Rom. 5:18.

      9. Mungu alikuwa akifanya nini alipotangaza wanadamu kuwa waadilifu, kama inavyotajwa katika Waroma 5:16, 18?

      9 Ni nini maana ya maneno ya Kigiriki yanayotafsiriwa kuwa “tangazo la uadilifu” na “kutangazwa kuwa waadilifu”? Mtafsiri mmoja wa Biblia aliandika hivi kuhusu wazo hilo: “Ni maneno ya mfano ya kisheria ambayo yanaonyesha jambo halali kisheria. Yanaonyesha badiliko la msimamo wa mtu mbele za Mungu, si badiliko linalofanyika ndani ya mtu . . . Maneno hayo ya mfano yanaonyesha kwamba Mungu ni hakimu au mwamuzi ambaye amefanya uamuzi ambao unampendelea mshtakiwa, ambaye ameletwa mbele ya mahakama ya Mungu, kwa njia ya mfano, akiwa ameshtakiwa kwa kosa la kutokuwa mwadilifu. Lakini Mungu anamwondolea mshtakiwa huyo hatia.”

      10. Yesu alifanya jambo gani ambalo liliweka msingi wa wanadamu kutangazwa kuwa waadilifu?

      10 Ni kwa msingi gani ‘Mwamuzi mwadilifu wa dunia yote’ angeweza kumtangaza mtu asiye mwadilifu kuwa mwadilifu? (Mwa. 18:25) Kwa upendo, Mungu aliweka msingi kwa kumtuma duniani Mwana wake mzaliwa-pekee. Yesu alifanya mapenzi ya Baba yake kikamili, ingawa alishawishiwa, alitukanwa, na kudhihakiwa vikali sana. Alishika utimilifu wake mpaka kufikia hatua ya kufa kwenye mti wa mateso. (Ebr. 2:10) Kwa kuudhabihu uhai wake mkamilifu wa kibinadamu, Yesu alitoa fidia au dhabihu ya ukombozi ambayo ingewaachilia huru, au kuwakomboa, wazao wa Adamu kutoka katika dhambi na kifo.—Mt. 20:28; Rom. 5:6-8.

      11. Fidia au dhabihu ya ukombozi inategemea ulinganifu gani?

      11 Katika andiko lingine Paulo alisema hiyo ni “fidia inayolingana.” (1 Tim. 2:6) Ililingana katika maana gani? Adamu aliwaletea mabilioni ya wazao wake hali ya kutokamilika na kifo. Ni kweli kwamba Yesu, akiwa mwanadamu mkamilifu, angetokeza mabilioni ya wazao wakamilifu.a Hivyo, ilieleweka kwamba maisha ya Yesu pamoja na maisha ya wale wote ambao wangekuwa wazao wake wakamilifu yangetokeza dhabihu inayolingana na maisha ya Adamu na wazao wake wasio wakamilifu. Hata hivyo, Biblia haisemi kwamba wote ambao wangeweza kuwa wazao wa Yesu walikuwa sehemu ya dhabihu ya ukombozi. Andiko la Waroma 5:15-19 linaonyesha kwamba kifo cha “mtu mmoja” tu ndicho kilichowawezesha wanadamu wawekwe huru. Ndiyo, uhai mkamilifu wa Yesu ulilingana na uhai wa Adamu. Jambo ambalo linakaziwa, na ambalo linapaswa kukaziwa ni, Yesu Kristo peke yake. Sasa iliwezekana kwa watu wa namna zote kupokea zawadi ya bure na uzima kwa sababu ya “tendo moja la kutetewa kuwa haki” la Yesu, maisha yake ya utii na kushika utimilifu mpaka kifo. (2 Kor. 5:14, 15; 1 Pet. 3:18) Jambo hilo liliwezekana jinsi gani?

      Kuwekwa Huru kwa Msingi wa Fidia

      12, 13. Kwa nini wale ambao wanatangazwa kuwa waadilifu wanahitaji rehema na upendo wa Mungu?

      12 Yehova Mungu alikubali fidia au dhabihu ya ukombozi ambayo Mwana wake alitoa. (Ebr. 9:24; 10:10, 12) Lakini wanafunzi wa Yesu waliokuwa duniani, kutia ndani mitume wake waaminifu waliendelea kuwa na hali ya kutokamilika. Ingawa walijitahidi kuepuka makosa, nyakati nyingine hawakufaulu. Kwa nini? Kwa sababu walikuwa wamerithi dhambi. (Rom. 7:18-20) Lakini Mungu angeweza na alifanya jambo fulani kuhusiana na hilo. Aliikubali “fidia inayolingana” na alikuwa tayari kuitumia kwa ajili ya watumishi wake wa kibinadamu.

      13 Si kwamba Mungu alikuwa chini ya wajibu wa kutumia dhabihu ya ukombozi kwa ajili ya mitume na wengine kwa sababu walikuwa wamefanya mambo fulani mazuri. Badala yake, Mungu alitumia dhabihu ya ukombozi kwa ajili yao kwa sababu ya rehema na upendo wake mwingi sana. Alichagua kuwaweka huru mitume na wengine kutoka kwa hukumu waliyopewa, na kuwaona kuwa wameondolewa hatia ambayo walikuwa wamerithi. Paulo alieleza hilo waziwazi hivi: “Kwa fadhili hizi zisizostahiliwa, kwa kweli, ninyi mmeokolewa kupitia imani; na hiyo si kutokana na ninyi, ni zawadi ya Mungu.”—Efe. 2:8.

      14, 15. Ni thawabu gani ambayo wale wanaotangazwa na Mungu kuwa waadilifu waliahidiwa, lakini bado walihitaji kufanya nini?

      14 Hebu fikiria zawadi kubwa ajabu kutoka kwa Mweza-Yote ya kusamehe dhambi ambazo mtu alirithi kutia ndani makosa aliyofanya! Huwezi kuhesabu dhambi ambazo watu mmoja-mmoja walitenda kabla ya kuwa Wakristo; hata hivyo, kwa msingi wa dhabihu ya ukombozi, Mungu anaweza kusamehe dhambi hizo. Paulo aliandika hivi: “Zawadi ilitokana na makosa mengi katika tangazo la uadilifu.” (Rom. 5:16) Mitume na watu wengine ambao walipokea zawadi hiyo yenye upendo (kutangazwa kuwa waadilifu) walipaswa kuendelea kumwabudu Mungu wa kweli wakiwa na imani. Wangepata thawabu gani wakati ujao? ‘Wale wanaopokea wingi wa fadhili zisizostahiliwa na zawadi ya bure ya uadilifu watatawala wakiwa wafalme katika uzima kupitia mtu mmoja, Yesu Kristo.’ Kwa kweli, zawadi ya uadilifu ina matokeo yaliyo tofauti kabisa. Zawadi hiyo inatokeza uzima.—Rom. 5:17; soma Luka 22:28-30.

      15 Wale wanaopokea zawadi hiyo, yaani, kutangazwa kuwa waadilifu, wanakuwa wana wa kiroho wa Mungu. Wakiwa warithi wenzi pamoja na Kristo, wana tumaini la kufufuliwa na kwenda mbinguni ili kuwa wana halisi wa kiroho na ‘kutawala wakiwa wafalme’ pamoja na Yesu Kristo.—Soma Waroma 8:15-17, 23.

      Watu Wengine Wanaonyeshwa Upendo wa Mungu

      16. Wale walio na tumaini la kuishi duniani wanaweza kupokea zawadi jinsi gani?

      16 Si wote wanaomwamini Mungu na kumtumikia kwa ushikamanifu wana tumaini la ‘kutawala wakiwa wafalme’ pamoja na Kristo mbinguni. Wengi wao wana tumaini linalotegemea Biblia kama lile la watumishi wa Mungu walioishi kabla ya Ukristo. Wanatumaini kuishi milele katika paradiso duniani. Je, wanaweza hata sasa kupokea zawadi ya upendo kutoka kwa Mungu na kuonwa kuwa waadilifu wakiwa na tumaini la kuishi duniani? Kulingana na yale ambayo Paulo aliwaandikia Waroma, bila shaka jibu ni ndiyo!

      17, 18. (a) Mungu alimwona Abrahamu jinsi gani kwa sababu ya imani yake? (b) Ni kwa njia gani Yehova angeweza kumwona Abrahamu kuwa mwadilifu?

      17 Paulo alizungumza kuhusu mfano mkuu zaidi, Abrahamu, mwanamume mwenye imani aliyeishi kabla Yehova hajawapa Waisraeli sheria iliyoandikwa na muda mrefu kabla Kristo hajafungua njia ya kupata uzima mbinguni. (Ebr. 10:19, 20) Tunasoma hivi: “Kwa maana ahadi ile kwamba awe mrithi wa ulimwengu hakuipata Abrahamu au uzao wake kupitia sheria, bali ilikuwa kupitia uadilifu kwa njia ya imani.” (Rom. 4:13; Yak. 2:23, 24) Kwa hiyo, Mungu alimhesabu Abrahamu ambaye alikuwa mwaminifu kuwa mwadilifu.—Soma Waroma 4:20-22.

      18 Hilo halimaanishi kwamba Abrahamu hakuwa na dhambi alipokuwa akimtumikia Yehova kwa makumi mengi ya miaka. Hapana, hakuwa mwadilifu katika njia hiyo. (Rom. 3:10, 23) Hata hivyo, kwa sababu ya hekima yake isiyo na mipaka, Yehova alifikiria kuhusu imani ya Abrahamu iliyokuwa ya pekee na matendo yake yaliyotegemea imani hiyo. Abrahamu aliweka imani hasa katika “uzao” ulioahidiwa ambao ungekuja kupitia ukoo wake. Uzao huo ulithibitika kuwa yule Masihi, au Kristo. (Mwa. 15:6; 22:15-18) Kwa kufaa, kwa msingi wa “fidia ambayo Kristo Yesu alilipa,” Mungu ambaye ni Hakimu anaweza kusamehe dhambi ambazo zilifanywa zamani. Hivyo, Abrahamu na watu wengine wenye imani walioishi kabla ya Ukristo wana tumaini la kufufuliwa.—Soma Waroma 3:24, 25; Zab. 32:1, 2.

      Furahia Msimamo wa Uadilifu Leo

      19. Kwa nini maoni ya Mungu kuhusu Abrahamu yanapaswa kuwatia moyo watu wengi leo?

      19 Ukweli wa kwamba Mungu mwenye upendo alimhesabu Abrahamu kuwa mwadilifu unapaswa kuwachochea Wakristo wa kweli leo. Yehova hakumtangaza kuwa mwadilifu kama anavyowatangaza kuwa waadilifu wale anaowatia mafuta kuwa “warithi pamoja na Kristo.” Washiriki wa kikundi hicho kidogo ‘wanaitwa wawe watakatifu’ na wanakubaliwa kuwa “wana wa Mungu.” (Rom. 1:7; 8:14, 17, 33) Kinyume na hilo, Abrahamu alikuja kuwa “rafiki ya Yehova,” na jambo hilo lilitukia kabla ya kutolewa kwa dhabihu ya ukombozi. (Yak. 2:23; Isa. 41:8) Basi, namna gani kuhusu Wakristo wa kweli ambao wana tumaini la kuishi katika dunia iliyorudishwa kuwa Paradiso?

      20. Leo Mungu anawatazamia wale anaowaona kuwa waadilifu kama Abrahamu wafanye nini?

      20 Watu hao hawapokei “zawadi ya bure ya uadilifu” wakiwa na tumaini la kuishi mbinguni “kupitia kuachiliwa huru kwa njia ya fidia ambayo Kristo Yesu alilipa.” (Rom. 3:24; 5:15, 17) Hata hivyo, wanamwamini kabisa Mungu na maandalizi yake, na wanaonyesha imani yao kupitia matendo mazuri. Moja kati ya matendo hayo ni ‘kuhubiri kuhusu ufalme wa Mungu na kufundisha mambo yanayohusu Bwana Yesu Kristo.’ (Mdo. 28:31) Hivyo, Yehova anaweza kuwaona watu hao kuwa waadilifu kama vile alivyomwona Abrahamu. Zawadi ambayo watu hao wanapokea, yaani, urafiki pamoja na Mungu, ni tofauti na “zawadi ya bure” ambayo watiwa mafuta wanapokea. Hata hivyo, bila shaka wanapokea zawadi hiyo kwa shukrani nyingi.

      21. Ni faida gani ambazo tunaweza kupata kwa sababu ya upendo na haki ya Yehova?

      21 Ikiwa unatazamia kufurahia uzima wa milele duniani, unapaswa kutambua kwamba umepata nafasi hiyo si kwa sababu ya tendo la mtawala fulani wa kibinadamu. Badala yake, mpango huo unaonyesha kusudi lenye hekima la Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Yehova anatimiza kusudi lake hatua kwa hatua. Hatua hizo zinalingana na haki ya kweli. Zaidi ya hilo, hatua hizo zimeonyesha upendo mkubwa wa Mungu. Ndiyo sababu Paulo alisema: “Mungu hupendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.”—Rom. 5:8.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kwa mfano, maoni hayo kuhusu wazao yalitiwa ndani ya Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 736, fungu la 4 na 5 (Étude perspicace des Écritures, Buku la 2, ukurasa wa 728 fungu la 1 na 2).

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki