-
Acheni Wote Wamtukuze Yehova!Mnara wa Mlinzi—1997 | Januari 1
-
-
Acheni Wote Wamtukuze Yehova!
“Mtukuzeni BWANA [“Yehova,” “NW”] katika mashariki.”—ISAYA 24:15.
1. Jina la Yehova lilionwaje na manabii wake, kwa kutofautisha na mtazamo upi ulio katika Jumuiya ya Wakristo leo?
YEHOVA—jina tukufu la Mungu! Manabii waaminifu wa kale walishangilia kama nini kusema katika jina hilo! Walimtukuza kwa mchachawo Bwana wao Mwenye Enzi Kuu, Yehova, ambaye jina lake humtambulisha kuwa Mkusudiaji Mkuu. (Isaya 40:5; Yeremia 10:6, 10; Ezekieli 36:23) Hata waitwao isivyofaa manabii wadogo walisema mengi kwa kumpa Yehova utukufu. Mmoja wao alikuwa Hagai. Katika kitabu cha Hagai, chenye mistari 38 tu, jina la Mungu latumiwa mara 35. Unabii huo waonekana kuwa baridi jina la cheo “Bwana” litumiwapo badala ya lile jina lenye thamani Yehova, kama vile mitume bora kabisa wa Jumuiya ya Wakristo walitafsirivyo katika tafsiri zao za Biblia.—Linganisha 2 Wakorintho 11:5.
2, 3. (a) Unabii mmoja wenye kutokeza juu ya kurudishwa kwa Israeli ulitimizwaje? (b) Mabaki ya Wayahudi na waandamani wao walishiriki katika shangwe ipi?
2 Kwenye Isaya 12:2, aina mbili za jina hilo zatumiwa.a Huyo nabii atangaza hivi: “Tazama, Mungu ndiye wokovu wangu; nitatumaini wala sitaogopa, maana BWANA [“Yah,” NW] YEHOVA ni nguvu zangu na wimbo wangu; naye amekuwa wokovu wangu.” (Ona pia Isaya 26:4.) Hivyo, miaka ipatayo 200 kabla ya kuachiliwa kwa Israeli kutoka katika utekwa wa Kibabiloni, Yah Yehova kupitia nabii wake Isaya alikuwa akitoa uhakikishio kwamba yeye ndiye aliyekuwa Mwokozi wao mwenye uweza. Utekwa huo ulikusudiwa udumu tangu 607 hadi 537 K.W.K. Pia Isaya aliandika hivi: “Mimi ni BWANA [“Yehova,” NW], nifanyaye vitu vyote; . . . nimwambiaye Koreshi, Mchungaji wangu, naye atayatenda mapenzi yangu; hata ataunena Yerusalemu, Utajengwa; na hilo hekalu, Msingi wako utawekwa.” Koreshi huyo alikuwa nani? Kwa kutokeza, alithibitika kuwa Mfalme Koreshi wa Uajemi, aliyeshinda Babiloni katika 539 K.W.K.—Isaya 44:24, 28.
3 Katika kutimizwa kwa maneno ya Yehova yaliyorekodiwa na Isaya, Koreshi alitolea Israeli lililotekwa agizo hili: “Basi kila mtu katika ninyi nyote mlio watu wake, BWANA, Mungu wake, na awe pamoja naye, na akwee mpaka Yerusalemu, ulioko Yuda, akaijenge nyumba ya BWANA, Mungu wa Israeli, (yeye ndiye Mungu), iliyoko Yerusalemu.” Mabaki Wayahudi wenye furaha kuu pamoja na Wanethini wasio Waisraeli na wana wa watumishi wa Solomoni walirudi Yerusalemu. Walifika kwa wakati ili kuadhimisha Msherehekeo wa Vibanda katika 537 K.W.K. na kumtolea Yehova dhabihu madhabahuni pake. Mwaka uliofuata, mwezi wa pili, waliweka msingi wa hekalu la pili, kwa kuambatana na sauti kubwa za shangwe na sifa kwa Yehova.—Ezra 1:1-4; 2:1, 2, 43, 55; 3:1-6, 8, 10-13.
4. Isaya sura ya 35 na ya 55 zilipataje kuwa uhalisi?
4 Unabii wa kurudisha wa Yehova ulipaswa utimizwe kwa utukufu katika Israeli: “Nyika na mahali palipo ukiwa patafurahi; jangwa litashangilia na kuchanua maua kama waridi. . . . watauona utukufu wa BWANA, na ukuu wa Mungu wetu.” “Mtatoka kwa furaha, mtaongozwa kwa amani; mbele yenu milima na vilima vitatoa nyimbo; . . . Jambo hili litakuwa la kumpatia BWANA jina, litakuwa ishara ya milele isiyokatiliwa mbali.”—Isaya 35:1, 2; 55:12, 13.
5. Kwa nini shangwe ya Israeli ilikuwa ya muda mfupi?
5 Hata hivyo, shangwe hiyo ilikuwa ya muda mfupi tu. Majirani walijaribu kuwa na muungano wa imani mbalimbali kwa ujenzi wa hekalu. Mwanzoni Wayahudi walikuwa thabiti wakitangaza hivi: “Ninyi haiwahusu kushirikiana nasi katika kumjengea Mungu wetu nyumba; bali sisi wenyewe peke yetu tutamjengea BWANA, Mungu wa Israeli, nyumba, kama mfalme Koreshi, mfalme wa Uajemi alivyotuamuru.” Majirani hao wakawa wapinzani wakali sasa. Wao “wakaidhoofisha mikono ya watu wa Yuda, wakawasumbua, walipokuwa wakijenga.” Pia walimpasha mwandamizi wa Koreshi, Artashasta, aliyepiga marufuku ujenzi wa hekalu habari za uwongo juu ya hali ya mambo. (Ezra 4:1-24) Kwa miaka 17 kazi ilikoma. Kwa kuhuzunisha, Wayahudi walitumbukia katika njia ya maisha ya kufuatia vitu vya kimwili katika kipindi hicho.
“BWANA wa Majeshi” Asema
6. (a) Yehova aliitikiaje hali katika Israeli? (b) Kwa nini ile ionwayo kuwa maana ya jina la Hagai ni yenye kufaa?
6 Hata hivyo, Yehova alionyesha ‘nguvu zake na uweza wake’ kwa niaba ya Israeli kwa kutuma manabii, sanasana Hagai na Zekaria, ili wawaamshe Wayahudi wapate kurudia madaraka yao. Jina la Hagai lahusiana na msherehekeo, kwa kuwa laonekana kumaanisha “Kuzaliwa Siku ya Msherehekeo.” Kwa kufaa, alianza kutoa unabii siku ya kwanza ya mwezi wa Msherehekeo wa Vibanda, wakati ambapo Wayahudi walitakiwa wawe “katika kufurahi kabisa.” (Kumbukumbu la Torati 16:15) Kupitia Hagai, Yehova alitoa ujumbe nne katika kipindi cha siku 112.—Hagai 1:1; 2:1, 10, 20.
7. Maneno ya ufunguzi ya Hagai yatutieje moyo?
7 Akitolea unabii wake utangulizi, Hagai alisema hivi: “BWANA wa majeshi asema hivi.” (Hagai 1:2a) “Majeshi” hayo yaweza kuwa nani? Hayo ni majeshi ya malaika ya Yehova, nyakati nyingine yakirejezewa katika Biblia kuwa majeshi ya kivita. (Ayubu 1:6; 2:1; Zaburi 103:20, 21; Mathayo 26:53) Je, halitutii moyo leo kwamba Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe anatumia majeshi hayo ya kimbingu yasiyoshindika ili kuelekeza kazi yetu ya kurudisha ibada ya kweli duniani?—Linganisha 2 Wafalme 6:15-17.
8. Ni mtazamo gani uliokuwa umeathiri Israeli, na wenye tokeo jipi?
8 Ujumbe wa kwanza wa Hagai ulikuwa na habari gani? Watu walikuwa wamesema hivi: “Huu sio wakati utupasao kuja, huu sio wakati wa kujenga nyumba ya BWANA.” Ujenzi wa hekalu, uliowakilisha kurudishwa kwa ibada ya kimungu, haukuwa tena hangaiko lao la kwanza. Walikuwa wamegeukia kujijengea nyumba zenye utukufu. Mtazamo wa kufuatia vitu vya kimwili ulikuwa umedidimisha idili yao kwa ibada ya Yehova. Tokeo likawa, baraka yake ilikuwa imeondolewa. Mashamba yao hayakuwa na mazao tena, nao walikosa mavazi ya wakati wa kipupwe chenye baridi kali sana. Mapato yao yalikuwa yamepungua, na ilikuwa kana kwamba walikuwa wakiweka fedha zao katika mfuko uliotoboka-toboka.—Hagai 1:2b-6.
9. Yehova alitoa onyo gani la upole lenye nguvu na lenye kujenga?
9 Mara mbili, Yehova alitoa onyo hili la upole lenye nguvu: “Zitafakarini njia zenu.” Kwa wazi, Zerubabeli, liwali wa Yerusalemu, na kuhani wa cheo cha juu Yoshuab waliitikia nao wakawatia moyo watu wote kwa ujasiri ‘waitii sauti ya BWANA, Mungu wao, na maneno ya Hagai nabii, kama BWANA, Mungu wao alivyomtuma; nao watu wakaogopa mbele za BWANA.’ Waaidha, ‘Hagai mjumbe wa BWANA, katika ujumbe wa BWANA, akawaambia watu, akisema, Mimi nipo pamoja nanyi, asema BWANA.’—Hagai 1:5, 7-14.
10. Yehova alitumiaje nguvu zake kwa niaba ya Israeli?
10 Watu fulani wa zamani katika Yerusalemu huenda wakawa walidhani kwamba utukufu wa hekalu lililojengwa upya ungekuwa “si kitu” kwa kulinganishwa na ule wa hekalu la kwanza. Hata hivyo, siku 51 hivi baadaye, Yehova alimsukuma Hagai atangaze ujumbe wa pili: “Uwe hodari, Ee Zerubabeli, asema BWANA; nawe uwe hodari, Ee Yoshua, mwana wa Yehosadaki, kuhani mkuu, nanyi iweni hodari, enyi watu wote wa nchi hii, asema BWANA; mkafanye kazi, kwa kuwa mimi ni pamoja nanyi, asema BWANA wa majeshi; . . . msiogope.” Yehova, ambaye kwa wakati ufaao angetumia nguvu zake zenye uweza wote ili ‘kuzitikisa mbingu na nchi,’ alihakikisha kwamba upinzani wote, hata ile marufuku ya kifalme, ulishindwa. Katika kipindi cha miaka mitano ujenzi wa hekalu ulitimizwa kwa mafanikio matukufu.—Hagai 2:3-6.
11. Mungu alijazaje hekalu la pili kwa ‘utukufu mkubwa zaidi’?
11 Ahadi yenye kutokeza ilitimizwa wakati huo: “Vitu vinavyotamaniwa na mataifa yote vitakuja; nami nitaijaza nyumba hii utukufu, asema BWANA wa majeshi.” (Hagai 2:7) Hivyo “vitu vinavyotamaniwa” vilithibitika kuwa wasio Waisraeli waliokuja kuabudu hekaluni, kwa kuwa lilionyesha utukufu wa kuwapo kwake kwenye fahari. Hekalu hilo lililojengwa upya lililinganaje na lile lililojengwa katika siku ya Solomoni? Nabii wa Mungu alitangaza hivi: “Utukufu wa mwisho wa nyumba hii utakuwa mkuu kuliko utukufu wake wa kwanza, asema BWANA wa majeshi.” (Hagai 2:9) Katika utimizo wa kwanza wa huo unabii, hekalu lililojengwa upya liliendelea kuwapo kwa muda mrefu zaidi ya ile nyumba ya kwanza. Bado lilikuwapo Mesiya alipotokea katika 29 W.K. Zaidi, kabla adui zake waasi-imani hawajamwua kimakusudi katika 33 W.K., Mesiya mwenyewe alililetea utukufu alipohubiri kweli humo.
12. Mahekalu mawili ya kwanza yalifaa kusudi jipi?
12 Hekalu la kwanza na la pili katika Yerusalemu yalifaa kusudi muhimu katika kufananisha sehemu mbalimbali za maana za utumishi wa kikuhani wa Mesiya na katika kudumisha ibada safi ya Yehova duniani hadi kutokea kwenyewe kwa Mesiya.—Waebrania 10:1.
Hekalu la Kiroho Lililo Tukufu
13. (a) Ni matukio gani yaliyohusiana na hekalu la kiroho yaliyotukia kuanzia 29 hadi 33 W.K.? (b) Dhabihu ya fidia ya Yesu ilikuwa na fungu gani muhimu katika matukio hayo?
13 Je, unabii wa kurudishwa wa Hagai una maana ya pekee kwa nyakati za baadaye? Bila shaka! Hekalu lililojengwa upya katika Yerusalemu likapata kuwa kitovu cha ibada yote ya kweli duniani. Lakini lilionyesha kimbele hekalu la kiroho lililo tukufu zaidi. Hilo lilianza kutenda katika 29 W.K. wakati ambapo, kwenye ubatizo wa Yesu katika Mto Yordani, Yehova alimtia mafuta Yesu awe Kuhani wa Cheo cha Juu, huku roho takatifu ikishuka juu yake kama hua. (Mathayo 3:16) Baada ya Yesu kumaliza huduma yake ya kidunia katika kifo cha kidhabihu, alifufuliwa na kwenda mbinguni, palipofananishwa na Patakatifu Zaidi Sana pa hekalu, na humo alimtolea Yehova thamani ya dhabihu yake. Hiyo ilitumika kuwa fidia ikifunika dhambi za wanafunzi wake, nayo, ikafungua njia ya kuwatia mafuta, katika siku ya Pentekoste 33 W.K., wawe makuhani wa cheo cha chini katika hekalu la kiroho la Yehova. Huduma yao ya uaminifu mpaka kifo katika ua wa hekalu duniani ingeongoza kwenye ufufuo wa kimbingu wa wakati ujao, kwa utumishi wa kikuhani wenye kuendelea.
14. (a) Ni shangwe gani iliyoshirikishwa na utendaji wenye bidii wa kutaniko la Kikristo la mapema? (b) Kwa nini shangwe hiyo ilikuwa ya muda mfupi?
14 Maelfu ya Wayahudi wenye kutubu—na baadaye Wasio Wayahudi—walimiminikia kutaniko hilo la Kikristo na kushiriki katika kutangaza habari njema ya utawala ujao wa Ufalme wa Mungu juu ya dunia. Baada ya miaka ipatayo 30, mtume Paulo aliweza kutaarifu kwamba habari njema zilikuwa zimehubiriwa “katika viumbe vyote chini ya mbingu.” (Wakolosai 1:23) Lakini baada ya kifo cha mitume, uasi-imani mkubwa ulisitawi, na nuru ya kweli ikaanza kusinzia. Ukristo wa kweli ulifunikwa na ufarakano wa Jumuiya ya Wakristo wenye kutegemea mafundisho na falsafa za kipagani.—Matendo 20:29, 30.
15, 16. (a) Unabii ulitimizwaje katika 1914? (b) Ni kukusanywa kupi kulikotia alama mwisho wa karne ya 19 na mapema karne ya 20?
15 Karne kadhaa zilipita. Kisha katika miaka ya 1870, kikundi cha Wakristo wenye moyo mweupe kikaanza kushiriki katika funzo la Biblia lenye kupenya. Kutokana na Andiko, waliweza kutaja mwaka wa 1914 kwa usahihi kuwa wenye kutia alama umalizio wa “nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa.” Wakati huo ndipo “nyakati” saba za ufananisho (miaka 2,520 ya utawala wa kibinadamu ulio kama wa hayawani) zilipoisha kwa kutawazwa kwa kimbingu kwa Kristo Yesu—Yeye aliye na “haki ya kisheria” kuwa Mfalme wa Kimesiya wa dunia. (Luka 21:24; Danieli 4:25; Ezekieli 21:26, 27, NW) Hasa kuanzia mwaka wa 1919 na kuendelea, Wanafunzi wa Biblia hao, wajulikanao leo kuwa Mashahidi wa Yehova, wamekuwa wakishiriki katika kueneza kwa bidii duniani kote habari njema ya Ufalme ujao. Katika 1919 ndipo maelfu machache yao walipoitikia mwito wa kutenda uliotolewa kwenye mkusanyiko katika Cedar Point, Ohio, Marekani. Idadi yao iliongezeka kufikia mwaka wa 1935 wakati ambapo watu 56,153 waliripoti utumishi wa shambani. Mwaka huo, watu 52,465 walikuwa wameshiriki mifano ya mkate na divai kwenye Ukumbusho wa kila mwaka wa kifo cha Yesu, wakionyesha tumaini lao la kuwa makuhani pamoja na Kristo Yesu katika sehemu ya kimbingu ya hekalu kubwa la kiroho la Yehova. Wao pia watatumikia pamoja naye wakiwa wafalme-washiriki katika Ufalme wake wa Kimesiya.—Luka 22:29, 30; Waroma 8:15-17.
16 Hata hivyo, Ufunuo 7:4-8 na 14:1-4 yaonyesha kwamba idadi ya jumla ya Wakristo watiwa-mafuta hao ni 144,000 tu, ambao wengi wao walikusanywa katika karne ya kwanza kabla ya uasi-imani mkubwa kutokea. Kuanzia mwisho wa karne ya 19 na kuendelea hadi karne ya 20, Yehova amekuwa akimalizia kukusanya kwa kikundi hiki cha watu ambao wanasafishwa kwa maji ya Neno lake, wanatangazwa kuwa waadilifu kupitia imani katika dhabihu ya Yesu yenye kufunika, na hatimaye wanatiwa muhuri wawe Wakristo watiwa-mafuta ili kufanyiza idadi kamili ya 144,000.
17. (a) Ni kukusanywa kupi ambako kumeendelea tangu miaka ya 1930? (b) Kwa nini Yohana 3:30 ni lenye upendezi hapa? (Ona pia Luka 7:28.)
17 Ni nini kinachofuata idadi kamili ya watiwa-mafuta inapokuwa imechaguliwa? Katika 1935, kwenye mkusanyiko wa kipekee huko Washington, D.C., Marekani, ilijulishwa kwamba “umati mkubwa” wa Ufunuo 7:9-17 ulikuwa kikundi cha watu ambao wangetambuliwa waziwazi “baada ya” wale 144,000 na ambao tumaini lao ni uhai udumuo milele katika dunia iliyo paradiso. Baada ya kumtambulisha kwa wazi Yesu aliyetiwa mafuta, Yohana Mbatizaji, ambaye ufufuo wake utakuwa duniani kwa kuwa yeye ni mmoja wa wale “kondoo wengine,” alisema hivi juu ya Mesiya: “Lazima huyo aendelee kuongezeka, lakini mimi lazima niendelee kupungua.” (Yohana 1:29; 3:30; 10:16; Mathayo 11:11) Kazi ya Yohana Mbatizaji ya kumtayarishia Mesiya wanafunzi ilikuwa ikiisha Yesu alipokuwa akitwaa uteuzi wa idadi ya watu wenye kuongezeka ambao wangekuwa miongoni mwa wale 144,000. Katika miaka ya 1930 jambo lililo kinyume lilitukia. Idadi ya watu “walioitwa na waliochaguliwa” wawe miongoni mwa wale 144,000 ilipungua ilhali ongezeko kubwa lilianza katika idadi ya “umati mkubwa” wa “kondoo wengine.” Umati huo mkubwa waendelea kuongezeka huku mfumo mwovu wa ulimwengu ukikaribia mwisho wao kwenye Har–Magedoni.—Ufunuo 17:14b.
18. (a) Kwa nini twaweza kutarajia kwa uhakika kwamba “mamilioni wanaoishi sasa hawatakufa kamwe”? (b) Kwa nini tutii kwa bidii Hagai 2:4?
18 Mapema katika miaka ya 1920, hotuba ya watu wote iliyotolewa na Mashahidi wa Yehova ilikuwa na kichwa “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe.” Huenda ikawa hilo lilionyesha kutumainia mazuri kupita kiasi wakati huo. Lakini leo taarifa hiyo yaweza kutolewa na uhakika kamili. Nuru yenye kuongezeka juu ya unabii wa Biblia na pia mchafuko wa kiserikali wa ulimwengu huu unaoangamia waonyesha waziwazi kwamba mwisho wa mfumo wa Shetani u karibu sana, sana! Ripoti ya Ukumbusho ya 1996 yaonyesha kwamba watu 12,921,933 walihudhuria, ambao kati yao 8,757 tu (asilimia .068) walionyesha tumaini lao la kimbingu kwa kushiriki mifano. Kurudishwa kwa ibada ya kweli kwakaribia mwisho. Lakini acheni tusilegeze mkono katika kazi hiyo. Ndiyo, Hagai 2:4 lataarifu hivi: “Iweni hodari, enyi watu wote wa nchi hii, asema BWANA; mkafanye kazi, kwa kuwa mimi ni pamoja nanyi, asema BWANA wa majeshi.” Na tuazimie kwamba mikazo yoyote ya ufuatiaji vitu vya kimwili au ya ulimwengu haitapata kupunguza bidii yetu kwa kazi ya Yehova!—1 Yohana 2:15-17.
19. Twaweza kushirikije katika utimizo wa Hagai 2:6, 7?
19 Pendeleo letu la kushiriki katika utimizo wa Hagai 2:6, 7 katika siku ya kisasa ni lenye shangwe: “BWANA wa majeshi asema hivi, Mara moja tena ni kitambo kidogo tu, nami nitazitikisa hizo mbingu, na hii nchi, na bahari, na nchi kavu; nami nitatikisa mataifa yote, na vitu vinavyotamaniwa na mataifa yote vitakuja; nami nitaijaza nyumba hii utukufu, asema BWANA wa majeshi.” Pupa, ufisadi, na chuki zimeenea kotekote katika ulimwengu huu wa karne ya 20. Kwa kweli umo katika siku zao za mwisho, na Yehova ameanza tayari ‘kuutikisa’ kwa kuwaamuru Mashahidi wake ‘watangaze siku yake ya kisasi.’ (Isaya 61:2) Kutikisa huko kwa mwanzo kutafikia upeo kwa uharibifu wa ulimwengu kwenye Har–Magedoni, lakini kabla ya wakati huo, Yehova anakusanya “vitu vinavyotamaniwa na mataifa” kwa ajili ya utumishi wake—watu wa dunia walio wasikivu, wenye mfano wa kondoo. (Yohana 6:44) Sasa “umati mkubwa” huo ‘unatoa utumishi mtakatifu’ katika ua wa kidunia wa nyumba yake ya ibada.—Ufunuo 7:9, 15.
20. Hazina yenye thamani zaidi yaweza kupatikana wapi?
20 Utumishi katika hekalu la kiroho la Yehova huleta faida yenye thamani kuliko hazina yoyote ya kimwili. (Mithali 2:1-6; 3:13, 14; Mathayo 6:19-21) Waaidha, Hagai 2:9 lataarifu hivi: “Utukufu wa mwisho wa nyumba hii utakuwa mkuu kuliko utukufu wake wa kwanza, asema BWANA wa majeshi; na katika mahali hapa nitawapa amani, asema BWANA wa majeshi.” Maneno hayo yanamaanisha nini kwetu leo? Makala yetu inayofuata itafunua.
-
-
Utukufu Mkubwa Zaidi wa Nyumba ya YehovaMnara wa Mlinzi—1997 | Januari 1
-
-
Utukufu Mkubwa Zaidi wa Nyumba ya Yehova
“Nitaijaza nyumba hii utukufu, asema BWANA wa majeshi.”—HAGAI 2:7.
1. Roho takatifu yahusianaje na imani na kazi?
ALIPOKUWA akihubiri nyumba hadi nyumba, mmoja wa Mashahidi wa Yehova alikutana na bibi Mpentekoste aliyeeleza hivi, ‘Sisi tuna roho takatifu, lakini nyinyi ndio mnaofanya kazi.’ Kwa busara, alielezwa kwamba mtu aliye na roho takatifu hana budi kutiwa hamasa, kufanya kazi ya Mungu. Yakobo 2:17 lataarifu hivi: “Imani ikiwa haina kazi, imekufa ndani yayo yenyewe.” Kwa msaada wa roho ya Yehova, Mashahidi wake wamekuza imani yenye nguvu, naye ‘ameijaza nyumba yake utukufu’ kwa kuwaelekeza ili wafanye kazi zenye uadilifu—hasa ‘kuhubiri habari njema hii ya Ufalme katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote.’ Yehova aridhikapo na kufanywa kwa kazi hiyo, “ndipo mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.
2. (a) Kujitia wenyewe katika kazi ya Yehova kutaleta baraka ipi? (b) Kwa nini tufurahie hali yoyote ionekanayo kuwa ya ‘kukawia’?
2 Kutokana na maneno hayo ya Yesu, twafikia mkataa wa kwamba kazi yetu leo lazima ikaze fikira kuwahubiri wengine “habari njema yenye utukufu ya Mungu mwenye furaha,” ambayo tumekabidhiwa. (1 Timotheo 1:11) Kadiri tujihusishavyo kwa furaha katika utumishi wa Yehova, ndivyo itakavyoonekana kwamba ule mwisho waja haraka zaidi. Kwenye Habakuki 2:2, 3, twasoma maneno haya ya Yehova: “Iandike njozi ukaifanye iwe wazi sana katika vibao, ili aisomaye apate kuisoma kama maji. Maana njozi hii bado ni kwa wakati ulioamriwa, inafanya haraka ili kuufikilia mwisho wake, wala haitasema uongo; ijapokawia, ingojee; kwa kuwa haina budi kuja, haitakawia [“haitachelewa,” NW].” Ndiyo, ‘hiyo njozi’ itatimia “ijapokawia.” Mwaka huu wa 83 wa utawala wa Ufalme wa Yesu, huenda wengine wakahisi kwamba tuko katika kipindi cha kukawia sasa. Je, hatupaswi kufurahi, hata hivyo, kwamba mwisho haujaja bado? Katika mwongo wa miaka ya 1990, vizuizi dhidi ya kuhubiri habari njema vimeondolewa, kana kwamba ni muujiza, katika Ulaya Mashariki, sehemu mbalimbali za Afrika, na nchi nyingine. Hali ionekanayo kuwa ya ‘kukawia’ inaruhusu wakati ili “kondoo” wengi zaidi wapate kukusanywa kutoka maeneo hayo ambayo yamefunguliwa majuzi.—Yohana 10:16.
3. Kwa nini uelewevu wetu juu ya “kizazi hiki” uliofanywa uwe wa kisasa utuchochee kuwa katika kazi ya Mungu kwa hima?
3 “Haitachelewa,” huyo nabii asema. Yesu alisema kwamba kizazi kiovu kilichopo sasa hakitapita mpaka “mambo yote haya yatukie.” (Mathayo 24:34) Je, uelewevu wetu wa maneno yake, uliofanywa uwe wa kisasa, wamaanisha kwamba utendaji wetu wa kuhubiri si wa hima sana?a Mambo ya hakika yaonyesha kwamba sivyo kabisa! Kizazi cha wakati wetu kinatumbukia katika hali ya uovu na ufisadi isiyo na kifani katika historia yote iliyotangulia. (Linganisha Matendo 2:40.) Twapaswa kufanya kazi yetu kwa hima. (2 Timotheo 4:2) Unabii wote mbalimbali juu ya wakati wa dhiki kubwa waonyesha kwamba itakuja ghafula, hapohapo, kwa siri—kama mwizi. (1 Wathesalonike 5:1-4; Ufunuo 3:3; 16:15) “Kwa sababu hiyo nyinyi pia jithibitisheni wenyewe kuwa tayari, kwa sababu kwenye saa msiyoifikiri kuwa hiyo, Mwana wa binadamu anakuja.” (Mathayo 24:44) Kizazi hiki cha wanadamu kisichomcha Mungu kikaribiapo kuangamizwa, kwa kweli hatutaki kutupilia mbali tumaini letu lenye thamani la uhai wa milele kwa kurudi kwenye “kugaagaa katika matope” ya vikengeusha-fikira vya kilimwengu!—2 Petro 2:22; 3:10; Luka 21:32-36.
4. Ni hali gani ambayo imetaka magawio ya kuongezeka ya “chakula kwenye wakati ufaao,” na uhitaji huo umeshughulikiwaje?
4 Kwa kupatana na unabii wa Yesu, katika 1914 kulikuwa na “mwanzo wa maumivu makali ya ghafula ya taabu” huku wanadamu wakiingia katika “umalizio wa mfumo wa mambo.” Majonzi, matukio yenye msiba mkuu, na uasi-sheria umeongezeka kufikia leo. (Mathayo 24:3-8, 12) Wakati uo huo, jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara iliyotiwa mafuta imepewa utume na Yehova wa kuwaandalia watu wa nyumba ya Bwana-Mkubwa wayo, Kristo, ‘chakula cha kiroho kwa wakati ufaao.’ (Mathayo 24:45-47) Toka katika kiti chake cha ufalme mbinguni, Mfalme huyu wa Kimesiya sasa anaelekeza programu bora kabisa ya ulishaji wa kiroho kotekote duniani.
‘Magawio Tele ya Chakula’
5. “Chakula” cha msingi kinapata uangalifu upi?
5 Fikiria matayarisho ya “magawio ya chakula.” (Luka 12:42) Chakula cha msingi katika orodha ya vyakula vya Kikristo ni Neno la Mungu, Biblia. Ili kufundisha Biblia kwa matokeo, tafsiri yenye kusomeka, iliyo sahihi, ni uhitaji wa msingi. Kwa miaka mingi uhitaji huu umetoshelezwa hatua kwa hatua, hasa kuanzia mwaka wa 1950 wakati ambapo Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilipotolewa katika Kiingereza. Kufikia 1961 Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Biblia nzima ilipatikana, na chapa mbalimbali zilitokea upesi katika lugha nyingine kubwakubwa. Zile tafsiri 3 zilizotolewa mwaka wa utumishi wa 1996 zafanya jumla kuwa 27, ambazo kati yazo 14 ni Biblia nzima. Ili kushughulikia kazi hiyo inayohusu Biblia, pamoja na vichapo vya Biblia, Wakristo waliojiweka wakfu wapatao 1,174 sasa wanafanya kazi wakati wote wakitafsiri katika nchi 77.
6. Sosaiti imeshughulikiaje uhitaji wa vichapo vya Biblia?
6 Katika kusaidia kazi ya jeshi hilo la watafsiri, ofisi 24 za uchapaji za Watch Tower Society zimekuwa zikitokeza hesabu ya vichapo yenye kuongezeka daima. Ili kutimiza hilo, matbaa za rotari za ziada zenye mwendo wa kasi zaendelea kuwekwa katika ofisi kubwa-kubwa za tawi. Kutolewa kwa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kumeongezeka mwezi baada ya mwezi, na kufikia jumla kuu ya nakala 943,892,500, ongezeko la asilimia 13.4 mwaka huo. Jumla ya kutolewa kwa Biblia na vitabu vyenye jalada gumu katika Marekani, Brazili, Finland, Ujerumani, Italia, Japani, Korea, na Mexico, pekee imeongezeka asilimia 40 toka 1995 kufikia nakala 76,760,098 katika 1996. Ofisi nyingine za tawi pia zimechangia sana ongezeko la ujumla katika kutolewa kwa fasihi.
7. Andiko la Isaya 54:2 lakuwaje lenye hima zaidi leo?
7 Kumekuwa na ongezeko kubwa hasa kwa sababu ya kule kuondolewa kwa vizuizi dhidi ya Mashahidi wa Yehova katika Ulaya Mashariki na Afrika katika miaka ya 1990. Njaa ya chakula cha kiroho ni kubwa katika nchi hizo. Kwa hiyo, mwito huu watolewa kwa hima kubwa hata zaidi: “Panua mahali pa hema yako, na wayatandaze mapazia ya maskani yako; usiwakataze; ongeza urefu wa kamba zako; vikaze vigingi vya hema yako.”—Isaya 54:2.
8. Ni itikio gani lenye ukarimu linalosaidia kuandaa utegemezo wa kifedha?
8 Hivyo, imekuwa lazima kupanua majengo katika nyingi za zile ofisi za tawi 104 za Sosaiti. Kwa sababu ya hali ngumu za kiuchumi katika maeneo mengi yaliyofunguliwa karibuni, sehemu kubwa ya gharama ya upanuzi huo inalipiwa kwa michango itolewayo kwa kazi ya ulimwenguni pote katika nchi zenye utajiri zaidi. Kwa furaha, makutaniko na watu mmojammoja wamekuwa wakiitikia kwa moyo wote, katika roho ya Kutoka 35:21: “Wakaja kila mtu ambaye moyo wake ulimhimiza, na kila mtu ambaye roho yake ilimfanya kuwa apenda, nao wakaleta sadaka [“michango,” NW] za kumpa BWANA.” Twatwaa fursa hii kuwashukuru wale wote ambao wamekuwa wakishiriki katika utoaji huo wa ukarimu.—2 Wakorintho 9:11.
9. Andiko la Waroma 10:13, 18 linatimizwaje leo?
9 Katika mwaka wa 1996, vichapo vya Watch Tower Society kwa kweli vimetukuza jina la Yehova na makusudi yake hadi miisho ya dunia. Ni kama tu alivyotabiri mtume Paulo. Akinukuu unabii wa Yoeli na Zaburi ya 19, aliandika hivi: “‘Kila mtu aitiaye jina la Yehova ataokolewa.’ Hata hivyo nauliza, Wao hawakukosa kusikia, sivyo? Kwani, kwa kweli, ‘mvumo wao ulitoka ukaenda kuingia katika dunia yote, na matamko yao hadi ncha za mwisho za dunia inayokaliwa.’” (Waroma 10:13, 18) Kwa kulikweza hivyo lile jina lenye thamani Yehova, watu wake wamekuwa na sehemu ya maana katika kuijaza nyumba yake ya ibada utukufu. Hata hivyo, upigaji mbiu huo umefanikiwaje hasa katika mwaka wa 1996? Tafadhali chunguza chati inayofuata kwenye kurasa 18 hadi 21.
Kuvuna Ulimwenguni Pote
10. Waona mambo gani yenye kutokeza katika utendaji wa watu wa Yehova, kama ulivyofanyiwa muhtasari katika chati kwenye kurasa 18 hadi 21?
10 Maneno ya Yesu kwenye Luka 10:2 hayajapata kamwe kuwa na nguvu zaidi: “Kwa kweli, mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo mwombeni Bwana-mkubwa wa mavuno atume wafanyakazi katika mavuno yake.” Je, wewe waitikia mwito huo? Mamilioni ya watu ulimwenguni wanaitikia. Hilo laonyeshwa na kilele kipya cha watangazaji wa Ufalme 5,413,769 walioripoti utumishi wa shambani katika mwaka wa 1996. Zaidi, ndugu na dada wapya 366,579 walibatizwa. Jinsi tunavyothamini hawa walio “vitu vinavyotamaniwa na mataifa yote,” wanaoshiriki sasa katika ‘kuijaza nyumba ya ibada ya Yehova utukufu’!—Hagai 2:7, NW.
11. Kwa nini sisi sote tuna sababu ya kushangilia sana?
11 Ripoti za upanuzi katika maeneo yaliyofunguliwa karibuni ni zenye kutokeza. Je, wengine kati yetu wanawaonea wivu wale wanaofurahia ukuzi huo? Kinyume cha hilo, twashangilia pamoja nao. Nchi zote zilikuwa na mianzo midogo. Zekaria, nabii aliyeishi wakati mmoja na Hagai, aliandika hivi: “Ni nani aliyeidharau siku ya mambo madogo?” (Zekaria 4:10) Twashangilia sana kwamba katika nchi ambayo kazi ya kutoa ushahidi imeimarishwa vizuri, sasa kuna mamilioni ya watangazaji wa Ufalme, na eneo huhubiriwa mara nyingi, hata kila juma katika majiji makubwa mengi. Je, tuna sababu ya kulegeza mkono huku Yehova akitokeza sasa fursa ya wokovu katika maeneo ambayo zamani yalikuwa chini ya vizuizi. La hasha! “Shamba ndio ulimwengu,” akasema Yesu. (Mathayo 13:38) Ushahidi kamili lazima uendelee kutolewa, kama vile wanafunzi wa mapema walivyotoa ushahidi kikamili katika umalizio wa mfumo wa mambo wa Kiyahudi.—Matendo 2:40; 10:42; 20:24; 28:23.
Kusonga Mbele Sikuzote
12. Tuna kichocheo gani cha kujongea “kuelekea mbele”? (Ona pia sanduku, “Kuvuna ‘Kutoka Miisho ya Dunia.’”)
12 Ndiyo, lazima twende sambamba, tukijongea “kuelekea mbele” pamoja na gari la kimbingu la kimalaika la Yehova. (Ezekieli 1:12) Twakumbuka maneno haya ya Petro: “Yehova si wa polepole kwa habari ya ahadi yake, kama watu fulani waonavyo kuwa ni upolepole, bali yeye ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Acheni kielelezo cha bidii cha ndugu zetu katika nchi zilizo maskini kiuchumi kituchochee. Hali yoyote ionekanayo kuwa kuchelewa kwa kuja kwa Har–Magedoni inaruhusu mamia ya maelfu ya watu wakusanywe katika nchi hizo pamoja na watu wengi katika maeneo ambayo yamehubiriwa sana. Usidanganyike: “Hiyo siku ya BWANA iliyo kuu i karibu; i karibu, nayo inafanya haraka sana.” (Sefania 1:14) Kwapaswa kuwa na kuharakisha kutoa ushahidi kamili wa mwisho kwa upande wetu pia!
13, 14. (a) Ni nini liwezalo kusemwa juu ya ugawanyaji wa vichapo katika mwaka wa 1996? (b) Makutaniko yaweza kufanya mipango gani ya pekee kila mwaka, na unapangaje kushiriki?
13 Ingawa mambo madogo-madogo hayaonekani katika chati ya utumishi, kumekuwa na ongezeko lenye kustahili kuangaliwa katika kugawanywa kwa Biblia, vitabu, na magazeti katika mwaka uliopita. Kwa kielelezo, uangushaji wa magazeti ulimwenguni pote ulionyesha ongezeko la asilimia 19, jumla ya nakala 543,667,923 ziliangushwa. Magazeti yetu hurahisisha mahubiri ya kubadilikana-badilikana—barabarani, katika mabustani, kwenye vituo vya mabasi, katika maeneo ya biashara. Ripoti zaonyesha kwamba katika baadhi ya maeneo yanayohubiriwa Ufalme mara nyingi, watu wa kitaaluma wamevutiwa na ubora wa magazeti yetu na wanakubali mafunzo ya Biblia.
14 Kila mwaka katika mwezi wa Aprili, kwa kawaida makutaniko hupanga utendaji wa magazeti wa pekee, ambao ni kampeni ya siku nzima ya kuhubiri nyumba hadi nyumba na katika sehemu za umma. Je, kutaniko lenu litashiriki katika utendaji huo mwezi wa Aprili 1997? Matoleo ya Aprili yenye kutokeza ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yametayarishwa, na kutolewa kwayo kwa wakati uleule ulimwenguni pote bila shaka kwatazamiwa kuwe kwenye kuvutia! Katika kisiwa cha Saiprasi, makutaniko, yanapotumia maneno ya shime “fikia kila mtu awezaye kufikiwa kwa ujumbe wa Ufalme,” hata yaliyatimiza kila mwezi kwa kazi ya magazeti iliyoratibiwa hivyo, na kufikia kilele kipya cha 275,359 cha magazeti yaliyoangushwa huo mwaka, ongezeko la asilimia 54.
Ujumbe Mbalimbali wa Mwisho wa Hagai
15. (a) Kwa nini Yehova alituma ujumbe mbalimbali wa ziada kupitia Hagai? (b) Ujumbe wa tatu wa Hagai wapaswa kuwasilisha somo gani kwetu?
15 Siku 63 baada ya kujulisha ujumbe wake wa pili, Yehova alimtuma Hagai na mbiu ya tatu ambayo ni vema tuifikirie kwa uzito leo. Hagai alisema kana kwamba Wayahudi walikuwa wakiuweka msingi wa hekalu, ambao kwa kweli walikuwa wameweka miaka 17 mapema. Kwa mara nyingine tena Yehova aliona yafaa afanye usafishaji. Makuhani na watu walikuwa wamekuwa walegevu na hivyo walikuwa wasio safi machoni pa Yehova. Je, yawezekana kwamba baadhi ya watu wa Yehova wamelegeza mikono yao leo, hata kujihusisha katika njia za ulimwengu zenye uendekevu na za kufuatia vitu vya kimwili? Ni jambo la hima kwamba sisi sote tutafakari “tangu siku hii” juu ya kuletea jina la Yehova utukufu, na kuwa wenye uhakika katika ahadi yake: “Tangu siku hii ya leo nitawabariki.”—Hagai 2:10-19; Waebrania 6:11, 12.
16. Ni ‘kutikisa’ kupi kunakokaribia, na tokeo litakuwa nini?
16 Siku iyo hiyo, neno la “BWANA wa majeshi” lilimjia Hagai mara ya nne na ya mwisho. Alijulisha linalohusika katika ‘kutikisa Kwake mbingu na dunia’ akisema hivi: “Nitakipindua kiti cha enzi cha falme, nami nitaziharibu nguvu za falme za mataifa; nami nitayapindua magari, na hao wapandao ndani yake; farasi na hao wawapandao wataanguka chini; kila mtu kwa upanga wa ndugu yake.” (Hagai 2:6, 21, 22) Hivyo ‘kutikisa’ kutafikia upeo wako Yehova asafishapo dunia kabisa kwenye Har–Magedoni. Kufikia wakati huo “vitu vinavyotamaniwa na mataifa yote” vitakuwa vimeingia, ili kufanyiza kitovu cha jamii ya kibinadamu cha ulimwengu mpya. Ni sababu zilizoje za kushangilia na kumsifu Yehova!—Hagai 2:7; Ufunuo 19:6, 7; 21:1-4.
17. Yesu amewekwaje kuwa kama “pete yenye muhuri”?
17 Kwa kumalizia unabii wake, Hagai aandika hivi: “Katika siku ile, asema BWANA wa majeshi, nitakutwaa wewe, Ee Zerubabeli, . . . nami nitakufanya kuwa kama pete yenye muhuri; kwa kuwa nimekuchagua, asema BWANA wa majeshi.” (Hagai 2:23) Kristo Yesu, sasa ndiye kifanani cha uhalisi cha Mfalme wa Kimesiya na Kuhani wa Cheo cha Juu wa Yehova, akiunganisha mbinguni nyadhifa mbalimbali walizokuwa nazo Liwali Zerubabeli na Kuhani wa Cheo cha Juu Yoshua katika Yerusalemu la kidunia. Sawa na pete rasmi yenye muhuri kwenye mkono wa kuume wa Yehova, Yesu ndiye yule ambaye amekuwa “Ndiyo” akiwa chombo cha Yehova katika kutimiza ‘ahadi nyingi za Mungu.’ (2 Wakorintho 1:20; Waefeso 3:10,11; Ufunuo 19:10) Ujumbe wote wa kiunabii wa Biblia wakazia uandalizi wa Yehova yaani Kristo aliye Mfalme na Mfidi wa kikuhani.—Yohana 18:37; 1 Petro 1:18, 19.
18. ‘Usemi wa kumalizia wa BWANA wa majeshi’ utakuwaje na utimizo wenye kuburudisha?
18 Kwelikweli katika siku yetu, utukufu mkubwa zaidi unapatikana katika hekalu la kiroho la Yehova lenye kung’aa! Na upesi, baada ya Yehova kuufagilia mbali mfumo wote wa Shetani, Hagai 2:9 litakuwa na utimizo mwingine wenye kupendeza: “Katika mahali hapa nitawapa amani, asema BWANA wa majeshi.” Amani hatimaye!—amani ya ulimwengu wote mzima, yenye kudumu, ihakikishiwayo na “pete yenye muhuri” ya Yehova, Kristo Yesu, yule “Mfalme wa Amani,” ambaye kumhusu iliandikwa hivi: “Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe . . . Wivu wa BWANA wa majeshi ndio utakaotenda hayo.” (Isaya 9:6, 7) Kwa umilele wote utukufu wa nyumba ya ibada ya Yehova utaonyeshwa kotekote katika makao yenye amani ya enzi kuu yake ya ulimwengu wote mzima. Na tubaki sikuzote katika nyumba hiyo!—Zaburi 27:4; 65:4; 84:10.
-