Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Bado “Agano la Kale” Linafaa?
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Septemba 1
    • Je, Bado “Agano la Kale” Linafaa?

      MWAKA wa 1786, daktari mmoja Mfaransa alichapisha kitabu kinachoitwa Mazungumzo Kuhusu Viungo na Fisiolojia (Traité d’anatomie et de physiologie). Wakati huo kitabu hicho kilionwa kuwa kitabu sahihi zaidi kuhusu neva, na hivi majuzi nakala moja kati ya nakala chache zilizopo za kitabu hicho iliuzwa kwa zaidi ya dola 27,000! Hata hivyo, wagonjwa wengi hawawezi kumtumaini daktari anayetegemea utafiti wa kitiba uliofanywa karne zilizopita ulio katika kitabu hicho. Ingawa ni chenye thamani ya kihistoria na ya kimaandishi, kitabu hicho hakiwezi kumsaidia mgonjwa leo.

      Wengi wanahisi vivyo hivyo kuhusu kitabu kinachoitwa Agano la Kale. Wanathamini masimulizi yake ya historia ya Waisraeli na wanavutiwa na mashairi yake mazuri. Hata hivyo, hawaoni kuwa ni jambo la hekima kufuata mwongozo uliotolewa miaka zaidi ya 2,400 iliyopita. Ujuzi wa kisayansi, biashara, na hata maisha ya familia leo yanatofautiana sana na jinsi ilivyokuwa wakati Biblia ilipoandikwa. Philip Yancey, aliyekuwa msimamizi wa maandishi wa gazeti moja (Christianity Today), aliandika hivi katika kitabu chake (The Bible Jesus Read): “Kitabu hicho hakipatani na akili kila mara, na kinapopatana na akili kinawaudhi watu wa leo. Kwa sababu hiyo na nyinginezo, mara nyingi watu hawasomi Agano la Kale ambalo ni robo tatu ya Biblia.” Maoni hayo si mapya.

      Miaka isiyozidi 50 baada ya kifo cha mtume Yohana kilichotokea mwaka wa 100 W.K., kijana tajiri aliyeitwa Marcion alidai waziwazi kwamba Wakristo wanapaswa kukataa Agano la Kale. Kulingana na mwanahistoria Mwingereza, Robin Lane Fox, Marcion alisema kwamba “‘Mungu’ katika Agano la Kale alikuwa ‘mkatili kabisa’ naye aliwapendelea waporaji na magaidi kama vile Mfalme Daudi wa Israeli. Kinyume naye, Kristo alifunua Mungu mpya aliyekuwa tofauti na bora zaidi.” Fox anaandika kwamba maoni hayo “yakawa ‘Imani ya Marcioni,’ nayo iliendelea kuwavutia watu mpaka kufikia karne ya nne, hasa katika maeneo ya Mashariki ambako watu walizungumza Kisiria.” Watu fulani bado wanafuata imani hiyo. Kwa sababu hiyo, miaka zaidi ya 1,600 baadaye, anaandika Philip Yancey, “ujuzi wa Agano la Kale unadidimia haraka kati ya Wakristo nao unaelekea kutoweka kabisa katika jamii ya leo.”

      Je, agano lingine limechukua mahali pa Agano la Kale? Tunaweza kupatanisha jinsi gani ujuzi wetu kuhusu “Yehova wa majeshi” katika Agano la Kale na “Mungu wa upendo na amani” katika Agano Jipya? (Isaya 13:13; 2 Wakorintho 13:11) Je, Agano la Kale linaweza kukufaidi leo?

  • “Yaliandikwa Ili Kutufundisha Sisi”
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Septemba 1
    • “Yaliandikwa Ili Kutufundisha Sisi”

      “HAKUNA mwisho wa kutungwa kwa vitabu vingi.” (Mhubiri 12:12) Wingi wa habari iliyochapishwa leo unafanya maneno hayo yawe ya kweli kama tu yalivyokuwa yalipoandikwa. Hivyo basi, msomaji mwenye utambuzi anaweza jinsi gani kuamua kitabu kinachomfaa?

      Wanapofikiria ikiwa watasoma au hawatasoma kitabu fulani, wasomaji wengi wanataka kujua mambo fulani kumhusu mtungaji wa kitabu hicho. Huenda wachapishaji wakatia ndani habari fupi iliyo na jina la mji anakotoka mtungaji, kiwango chake cha elimu, na vitabu vyake vingine. Ni jambo la maana kumtambulisha mtungaji, kwa kuwa katika karne za mapema, watungaji wanawake walitumia majina bandia ya kiume ili watu wasikate kauli kwamba vitabu vyao ni vya kiwango cha chini kwa sababu tu viliandikwa na wanawake.

      Inasikitisha kwamba kama ilivyoonyeshwa katika habari iliyotangulia, watu fulani wanapuuza Maandiko ya Kiebrania kwa sababu wanaamini kwamba Mungu anayetajwa humo ni mungu mkatili aliyewaangamiza maadui wake bila rehema.a Acheni tuchunguze yale ambayo Maandiko ya Kiebrania na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanatuambia kumhusu Mtungaji wa Biblia.

      Habari Kumhusu Mtungaji

      Kulingana na Maandiko ya Kiebrania, Mungu aliliambia taifa la Israeli: “Mimi ni Yehova; sikubadilika.” (Malaki 3:6) Miaka 500 hivi baadaye, Yakobo, mwandikaji wa Biblia aliandika hivi kumhusu Mungu: “Naye habadiliki, kama kugeuka kwa kivuli.” (Yakobo 1:17) Kwa nini basi, watu fulani wanahisi kwamba Mungu anayefunuliwa katika Maandiko ya Kiebrania anatofautiana na Mungu wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo?

      Jibu ni kwamba sifa mbalimbali za Mungu zinafunuliwa katika sehemu tofauti-tofauti za Biblia. Katika kitabu kimoja tu cha Mwanzo, inasemekana kwamba Mungu ‘anaumia moyoni mwake,’ anaitwa “Mtokezaji wa mbingu na dunia,” na “Mwamuzi wa dunia yote.” (Mwanzo 6:6; 14:22; 18:25) Je, maelezo hayo yanayotofautiana yanamhusu Mungu yuleyule? Bila shaka.

      Kwa mfano: Huenda hakimu wa eneo fulani akajulikana na watu ambao amewahukumu mahakamani kuwa mtekelezaji wa sheria aliye thabiti. Kwa upande mwingine, huenda watoto wake wakamwona kuwa baba mwenye upendo na mkarimu. Marafiki wake wa karibu wanaweza kumwona kuwa rafiki anayependa ucheshi. Mtu yuleyule mmoja ni hakimu, baba, na rafiki. Ukweli ni kwamba sifa zake mbalimbali zinaonekana chini ya hali tofauti-tofauti.

      Vivyo hivyo, Maandiko ya Kiebrania yanamfafanua Yehova kuwa “Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo na kweli.” Lakini, tunasoma pia kwamba “kwa vyovyote hatakosa kuadhibu.” (Kutoka 34:6, 7) Sehemu hizo mbili zinaonyesha maana ya jina la Mungu. Kihalisi “Yehova” linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.” Yaani, Mungu anakuwa chochote anachohitaji kuwa ili atimize ahadi zake. (Kutoka 3:13-15) Lakini bado yeye ni Mungu yuleyule. Yesu alisema: “Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja.”—Marko 12:29.

      Je, Kitabu Kingine Kimechukua Mahali pa Maandiko ya Kiebrania?

      Leo utafiti mpya unapofanywa au mitazamo ya watu inapobadilika, ni jambo la kawaida kuandika vitabu vipya na kuachana na vya zamani. Je, hivyo ndivyo Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yalivyochukua mahali pa Maandiko ya Kiebrania? Hapana.

      Ikiwa Yesu alikusudia masimulizi ya huduma yake na maandishi ya wanafunzi wake yachukue mahali pa Maandiko ya Kiebrania, bila shaka angeonyesha jambo hilo waziwazi. Hata hivyo, masimulizi ya Luka kumhusu Yesu kabla tu hajaenda mbinguni, yanasema hivi: “Akaanzia Musa na Manabii wote [katika Maandiko ya Kiebrania] akawafasiria [wanafunzi wake wawili] mambo yanayomhusu yeye mwenyewe katika Maandiko yote.” Baadaye, Yesu aliwatokea mitume wake waaminifu na vilevile watu wengine. Masimulizi hayo yanaendelea hivi: “Sasa akawaambia: ‘Haya ndiyo maneno yangu niliyowaambia nilipokuwa ningali pamoja nanyi, kwamba mambo yote yaliyoandikwa katika sheria ya Musa na katika Manabii na Zaburi juu yangu lazima yatimizwe.’” (Luka 24:27, 44) Kwa nini Yesu aliendelea kunukuu Maandiko ya Kiebrania mwishoni mwa huduma yake ya kidunia ikiwa yalikuwa yamepitwa na wakati?

      Baada ya kuanzishwa kwa kutaniko la Kikristo, wafuasi wa Yesu waliendelea kutumia Maandiko ya Kiebrania kukazia unabii mbalimbali ambao ungetimizwa, kanuni za Sheria ya Musa zenye masomo muhimu, na masimulizi ya watumishi wa Mungu wa zamani ambao mifano yao mizuri iliwatia moyo Wakristo waendelee kuwa waaminifu. (Matendo 2:16-21; 1 Wakorintho 9:9, 10; Waebrania 11:1–12:1) “Andiko lote,” akaandika mtume Paulo, “limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida.”b (2 Timotheo 3:16) Maandiko ya Kiebrania yamekuwa yenye faida kwa njia gani leo?

      Mashauri Kuhusu Maisha ya Kila Siku

      Fikiria tatizo la ubaguzi wa rangi leo. Katika jiji moja la Ulaya Mashariki, mwanamume mmoja Mwethiopia aliye na umri wa miaka 21 anasema hivi: “Tukitaka kwenda mahali popote lazima tuwe kikundi. Labda hawatatushambulia tukiwa kikundi.” Anaongezea: “Hatuwezi kwenda nje baada ya saa 12 jioni, hasa kwenye njia za gari la moshi la chini ya ardhi. Watu wanapotutazama wanaona tu rangi yetu.” Je, Maandiko ya Kiebrania yanazungumzia tatizo hilo kubwa?

      Waisraeli wa kale waliambiwa hivi: “Ikiwa mkaaji mgeni anakaa pamoja nawe akiwa mgeni katika nchi yenu, msimtendee vibaya. Yule mkaaji mgeni anayekaa akiwa mgeni pamoja nanyi atakuwa kwenu kama mwenyeji wenu; nawe utampenda kama wewe mwenyewe, kwa maana mlikuwa wakaaji wageni katika nchi ya Misri.” (Mambo ya Walawi 19:33, 34) Ndiyo, kulingana na sheria, Waisraeli wa kale walipaswa kuwaheshimu wahamiaji, au “wakaaji wageni,” na sheria hiyo imo katika Maandiko ya Kiebrania. Je, hukubali kwamba kanuni hiyo inayotegemea sheria inaweza kumaliza tatizo la ubaguzi wa rangi leo?

      Ingawa hayatoi mashauri mengi ya kibiashara, Maandiko ya Kiebrania yanatoa mwongozo unaofaa wa kushughulikia pesa kwa hekima. Kwa mfano, tunasoma hivi katika Methali 22:7: “Mkopaji ni mtumishi wa mtu anayemkopesha.” Leo, washauri wengi wa masuala ya kifedha wanakubali kwamba kununua vitu bila hekima kwa njia ya mkopo kunaweza kutokeza hasara kubwa ya kiuchumi.

      Kwa kuongezea, kutafuta mali bila kujali matokeo yoyote yale, kama watu wengi wanavyofanya katika ulimwengu wa leo unaopenda mali, kulifafanuliwa vizuri na Mfalme Sulemani, mmoja wa matajiri wakubwa zaidi katika historia ya wanadamu. Aliandika: “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato. Hilo pia ni ubatili.” (Mhubiri 5:10) Hilo ni onyo lenye hekima kama nini!

      Tumaini la Wakati Ujao

      Biblia nzima ina kichwa kimoja: Mungu atatumia Ufalme ulio mikononi mwa Yesu Kristo kutetea enzi Yake kuu na kulitakasa jina Lake.—Danieli 2:44; Ufunuo 11:15.

      Katika Maandiko ya Kiebrania, tunajifunza mengi kuhusu maisha chini ya Ufalme wa Mungu, mambo ambayo yanatufariji na kutuwezesha kumkaribia zaidi yule aliye Chanzo cha faraja hiyo, Yehova Mungu. Kwa mfano, nabii Isaya alitabiri kwamba kutakuwa na amani kati ya wanyama na wanadamu: “Mbwa-mwitu kwa kweli atakaa pamoja na mwana-kondoo kwa muda fulani, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi, na ndama na mwana-simba mwenye manyoya shingoni na mnyama aliyelishwa vizuri wote pamoja; na mvulana mdogo atakuwa kiongozi juu yao.” (Isaya 11:6-8) Hilo ni tarajio zuri kama nini!

      Na namna gani wale ambao wanataabika kwa sababu ya ubaguzi wa rangi au chuki ya kijamii, magonjwa, au matatizo ya kiuchumi wasiyoweza kuyashinda? Maandiko ya Kiebrania yanatoa unabii huu kumhusu Kristo Yesu: “Atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. Atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataziokoa nafsi za maskini.” (Zaburi 72:12, 13) Ahadi kama hizo zinafaa kwa sababu zinawawezesha wale ambao wanaziamini watarajie wakati ujao wakiwa na tumaini na uhakika.—Waebrania 11:6.

      Haishangazi kwamba mtume Paulo aliongozwa na roho kuandika hivi: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini”! (Waroma 15:4) Ndiyo, Maandiko ya Kiebrania yangali sehemu ya maana sana ya Neno la Mungu lililoongozwa na roho, yaani, Biblia. Yana faida kubwa sana kwetu leo. Tunatumaini kwamba utajitahidi kujifunza mengi zaidi kuhusu yale ambayo Biblia nzima inafundisha hasa, na hivyo kumkaribia zaidi Mtungaji wake, Yehova Mungu.—Zaburi 119:111, 112.

      [Maelezo ya Chini]

      a Katika habari hii, tunaliita Agano la Kale Maandiko ya Kiebrania. (Ona sanduku “Ni Agano la Kale au Ni Maandiko ya Kiebrania?” katika ukurasa wa 6.) Vivyo hivyo, kwa kawaida Mashahidi wa Yehova wanaliita Agano Jipya, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

      b Maandiko ya Kiebrania yana kanuni nyingi zenye faida kubwa leo. Hata hivyo, tunapaswa kutambua kwamba Wakristo hawako chini ya Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli kupitia Musa.

      [Sanduku katika ukurasa wa 6]

      NI AGANO LA KALE AU NI MAANDIKO YA KIEBRANIA?

      Maneno “agano la kale” yanapatikana katika 2 Wakorintho 3:14 katika tafsiri za Kiswahili. Katika mstari huo neno la Kigiriki di·a·theʹke limetafsiriwa kuwa “agano.”

      Mtungaji wa kamusi Edward Robinson alisema hivi: “Kwa kuwa agano la kale limo katika vitabu vya Musa, [di·a·theʹke] linamaanisha kitabu cha agano, maandishi ya Musa, yaani, ile sheria.” Katika 2 Wakorintho 3:14, mtume Paulo alikuwa akizungumzia Sheria ya Musa, ambayo inafanyiza sehemu tu ya Maandiko ya kabla ya Ukristo.

      Hivyo basi, ni jina gani linalofaa zaidi kutumiwa kuhusu vile vitabu 39 vya kwanza vya Biblia Takatifu? Badala ya kudokeza kwamba sehemu hiyo ya Biblia imepitwa na wakati au ni ya kale, Yesu Kristo na wafuasi wake waliiita “Maandiko” na pia “Maandiko matakatifu.” (Mathayo 21:42; Waroma 1:2) Hivyo, kupatana na maneno hayo yaliyoongozwa na roho, Mashahidi wa Yehova wanaliita Agano la Kale Maandiko ya Kiebrania, kwa sababu sehemu hiyo ya Biblia iliandikwa mwanzoni katika Kiebrania hasa. Vivyo hivyo, wanaliita Agano Jipya Maandiko ya Kigiriki, kwa sababu Kigiriki ndiyo lugha iliyotumiwa na watu walioongozwa na roho ya Mungu kuandika sehemu hiyo ya Biblia.

      [Picha katika ukurasa wa 4]

      Mtu anaweza kuwa hakimu thabiti, baba mwenye upendo, na rafiki

      [Picha katika ukurasa wa 5]

      Yesu alitumia Maandiko ya Kiebrania katika huduma yake yote

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Ni kanuni gani za Biblia zinazoweza kumsaidia mtu afanye maamuzi mazuri?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki