Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Wasaidie Wengine Wakubali Ujumbe wa Ufalme
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Novemba 15
    • Wasaidie Wengine Wakubali Ujumbe wa Ufalme

      “Agripa akamwambia Paulo: ‘Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.’”—MATENDO 26:28.

      1, 2. Kwa nini mtume Paulo alisimama mbele ya Gavana Festo na Mfalme Agripa wa Pili?

      KATIKA mwaka wa 58 W.K., Mfalme Herode Agripa wa Pili na dada yake Bernike walimtembelea Gavana Mroma, Porkio Festo, huko Kaisaria. Walikuwa wamealikwa na Gavana huyo, nao ‘wakaingia kwa fahari nyingi katika chumba cha baraza pamoja na viongozi wa kijeshi na vilevile wanaume waheshimiwa katika jiji.’ Ndipo Festo akaamuru mtume Mkristo Paulo aletwe mbele zao. Kwa nini mfuasi huyo wa Yesu Kristo alisimama mbele ya kiti cha hukumu cha Gavana Festo?—Matendo 25:13-23.

      2 Mambo ambayo Festo aliwaeleza wageni wake yanajibu swali hilo. Alisema: “Mfalme Agripa na ninyi wanaume wote mliopo pamoja nasi, ninyi mnaona mtu huyu ambaye kuhusu yeye umati wote wa Wayahudi ukiwa pamoja umepeleka ombi kwangu katika Yerusalemu na hapa pia, ukipaaza sauti kwamba hapaswi kuishi tena kamwe. Lakini mimi nikaona hakuwa amefanya jambo lolote linalostahili kifo. Kwa hiyo mwanamume huyu mwenyewe alipokata rufani kwa Mheshimiwa, niliamua kumpeleka. Lakini kuhusu yeye sina jambo hakika la kumwandikia Bwana wangu. Kwa hiyo nikamleta mbele yenu, na hasa mbele yako wewe, Mfalme Agripa, ili, baada ya kumhoji kihukumu, nipate jambo fulani la kuandika. Kwa maana linaonekana kuwa jambo lisilo la akili kwangu kumpeleka mfungwa bila kuonyesha mashtaka juu yake.”—Matendo 25:24-27.

      3. Kwa nini viongozi wa kidini walimshtaki Paulo?

      3 Maneno ya Festo yanaonyesha kwamba Paulo alikuwa ameshtakiwa kwa uwongo kwamba alikuwa mchochezi, kosa ambalo lilistahili hukumu ya kifo. (Matendo 25:11) Lakini Paulo hakuwa na hatia. Mashtaka hayo yalitokana na wivu wa viongozi wa kidini wa Yerusalemu. Walipinga kazi ya Paulo ya kutangaza Ufalme nao walichukizwa sana kuona kwamba aliwasaidia wengine wawe wafuasi wa Yesu Kristo. Chini ya ulinzi mkali, Paulo alisafirishwa kutoka Yerusalemu hadi jiji la bandarini la Kaisaria, ambako alikata rufani kwa Kaisari. Kutoka hapo angepelekwa Roma.

      4. Mfalme Agripa alisema maneno gani yenye kushangaza?

      4 Wazia Paulo akiwa katika jumba la gavana mbele ya watu ambao walitia ndani mtawala wa eneo muhimu la Miliki ya Roma. Mfalme Agripa anamgeukia Paulo na kusema: “Unaruhusiwa kujitetea.” Paulo anapozungumza, jambo la kustaajabisha linatukia. Mfalme anaanza kuguswa moyo na mambo ambayo Paulo anasema. Naam, Mfalme Agripa anasema: “Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.”—Matendo 26:1-28.

      5. Kwa nini maneno ya Paulo kwa Agripa yalikuwa yenye matokeo sana?

      5 Hebu wazia! Kwa sababu Paulo alijitetea kwa njia ya ustadi, mtawala huyo aliguswa moyo na nguvu zenye kupenya za Neno la Mungu. (Waebrania 4:12) Kwa nini njia ya Paulo ya kujitetea ilikuwa yenye matokeo sana? Nasi tunaweza kujifunza jambo gani kutoka kwa Paulo ambalo linaweza kutusaidia katika kazi yetu ya kufanya wanafunzi? Tunapochanganua njia yake ya kujitetea, mambo mawili makuu yanadhihirika: (1) Paulo alikuwa mwenye ushawishi katika mazungumzo yake. (2) Alitumia ujuzi wake wa Neno la Mungu kwa ustadi, kama vile msanii hutumia kifaa fulani kwa njia yenye matokeo.

  • Wasaidie Wengine Wakubali Ujumbe wa Ufalme
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Novemba 15
    • Ushawishi Unaochochea Moyo

      10. Paulo alianzishaje mazungumzo yake ya kujitetea mbele ya Agripa?

      10 Sasa na tuchunguze kwa makini maneno ambayo Paulo alitumia kujitetea katika Matendo sura ya 26. Ona jinsi alivyoanza mazungumzo yake. Katika utangulizi wake, Paulo alitafuta sababu nzuri ya kumpongeza Agripa, hata ingawa mfalme huyo alikuwa na uhusiano wenye aibu pamoja na dada yake Bernike. Paulo alisema: “Kuhusu mambo yote ninayoshtakiwa na Wayahudi, Mfalme Agripa, ninajihesabu mwenyewe kuwa mwenye furaha kwamba ninajitetea mbele yako leo, hasa kwa kuwa wewe una ujuzi juu ya desturi zote na vilevile mabishano kati ya Wayahudi. Kwa hiyo ninakuomba unisikie kwa subira.”—Matendo 26:2, 3.

      11. Maneno ya Paulo kwa Agripa yalionyeshaje heshima, nayo yalikuwa na manufaa gani?

      11 Je, umeona kwamba Paulo alitambua cheo cha juu cha Agripa kwa kumwita Mfalme, jina lake la cheo? Kwa kufanya hivyo na pia kwa kuchagua maneno yake kwa hekima, Paulo alimwonyesha Agripa heshima. (1 Petro 2:17) Mtume huyo alikiri kwamba Agripa alijua desturi na sheria za raia zake Wayahudi ambazo zilikuwa ngumu kueleweka, na kusema kwamba alikuwa mwenye furaha kwa kuwa aliweza kujitetea mbele ya mtawala kama huyo mwenye ujuzi. Paulo, aliyekuwa Mkristo, hakutenda kana kwamba alikuwa mtu bora kuliko Agripa ambaye hakuwa Mkristo. (Wafilipi 2:3) Badala yake, Paulo alimwomba mfalme huyo amsikilize kwa subira. Hivyo, Paulo akatokeza hali ambayo yaelekea ingemfanya Agripa, na pia wasikilizaji wengine, wakubali mambo aliyotaka kusema. Alikuwa anaweka msingi wa kutegemeza hoja zake kwa kuzungumzia mambo ambayo wote walikubaliana.

      12. Tunawezaje kuchochea mioyo ya wasikilizaji wetu tunapofanya kazi ya kutangaza Ufalme?

      12 Acheni tuchochee mioyo ya wasikilizaji wetu tangu mwanzo hadi mwisho wa mazungumzo yetu kuhusu ujumbe wa Ufalme kama vile Paulo alivyofanya mbele ya Agripa. Tunaweza kufanya hivyo kwa kuonyesha tunamheshimu kikweli mtu tunayemhubiria na kwamba tunapendezwa kikweli na malezi na maoni yake.—1 Wakorintho 9:20-23.

      Tumia Neno la Mungu kwa Ustadi

      13. Unawezaje kuwachochea wasikilizaji wako kama Paulo?

      13 Paulo alitamani kuwachochea wasikilizaji wake watende kupatana na habari njema. (1 Wathesalonike 1:5-7) Ili kutimiza hilo, aliuchochea moyo wao wa mfano ambao ni chanzo cha msukumo wa kutenda. Tunapochunguza zaidi namna Paulo alivyojitetea mbele ya Agripa, ona jinsi Paulo ‘alivyotumia neno la Mungu sawasawa’ kwa kurejelea mambo yaliyosemwa na Musa na manabii.—2 Timotheo 2:15.

      14. Eleza jinsi Paulo alivyotumia ushawishi alipokuwa mbele ya Agripa.

      14 Paulo alijua kwamba Agripa alikuwa Myahudi kwa jina tu. Alitaja ujuzi wa Agripa kuhusu Dini ya Kiyahudi na kusema kwamba mahubiri yake yalihusu hasa ‘kutosema lolote ila mambo ambayo Manabii na vilevile Musa walisema yatatukia’ kuhusu kifo na ufufuo wa Masihi. (Matendo 26:22, 23) Akizungumza na Agripa moja kwa moja, Paulo aliuliza: “Je, wewe, Mfalme Agripa, unawaamini Manabii?” Agripa alitatanika. Kama angesema kwamba hakuwaamini manabii, sifa yake akiwa mwamini Myahudi ingeharibika. Na kama angekubaliana na hoja ya Paulo, angekuwa anakiri hadharani kwamba anakubaliana na maoni ya mtume huyo na hivyo kuitwa Mkristo, jambo ambalo lilikuwa hatari. Paulo alijibu swali lake mwenyewe kwa hekima, akisema: “Ninajua unawaamini.” Moyo wa Agripa ulimchochea kujibuje? Alijibu: “Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.” (Matendo 26:27, 28) Ingawa Agripa hakupata kuwa Mkristo, ni wazi kwamba Paulo alimgusa moyo kwa kadiri fulani kwa ujumbe wake.—Waebrania 4:12.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki