Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ndoa—Zawadi Kutoka kwa Mungu Mwenye Upendo
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
    • KUCHAGUA MWENZI WA NDOA ANAYEFAA

      9, 10. (a) Paulo alionyesha jinsi gani hatari ya kuwa na urafiki wa karibu pamoja na wasioamini? (b) Mara nyingi kupuuza shauri la Mungu la kutofunga ndoa na mtu asiyeamini huwa na matokeo gani?

      9 Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika kanuni ya maana ambayo mtu anapaswa kutumia anapochagua mwenzi wa ndoa: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini.” (2 Wakorintho 6:14) Mfano aliotumia unatokana na maisha ya ukulima. Wanyama wawili wanaotofautiana sana kwa ukubwa au nguvu wakifungwa nira pamoja, wote wawili wataumia. Vivyo hivyo, mwamini na mtu asiyeamini wanapofungwa nira pamoja katika ndoa, bila shaka watakwaruzana na kugongana-gongana. Ikiwa mmoja wao anataka kuendelea kukaa katika upendo wa Yehova naye yule mwingine hajali hata kidogo, mambo wanayotanguliza maishani yatatofautiana na huenda hilo likatokeza mkazo mwingi. Hivyo, Paulo aliwasihi Wakristo wafunge ndoa “katika Bwana tu.”—1 Wakorintho 7:39.

      10 Nyakati nyingine, Wakristo fulani ambao hawajafunga ndoa wanaona kwamba ni afadhali kufungwa nira isivyo sawa kuliko kuishi maisha ya upweke. Wengine wanaamua kupuuza shauri la Biblia na kufunga ndoa na mtu ambaye hamtumikii Yehova. Mara nyingi matokeo yamekuwa yenye kusikitisha. Watu hao hujikuta wamefunga ndoa na mtu ambaye hawawezi kuzungumza pamoja naye mambo ya maana zaidi maishani. Wanakuwa wapweke hata zaidi kuliko walivyokuwa kabla ya kufunga ndoa. Inafurahisha kwamba kuna maelfu ya Wakristo waseja wanaotegemea na kushikamana na mashauri ya Mungu kuhusu jambo hilo. (Zaburi 32:8) Ingawa wanatarajia kwamba siku moja watafunga ndoa, wanaendelea kuwa waseja mpaka watakapopata mwenzi kati ya wale wanaomwabudu Yehova Mungu.

      11. Ni nini kinachoweza kukusaidia kuchagua mwenzi wa ndoa kwa hekima? (Ona pia sanduku “Ninatafuta Mwenzi wa Aina Gani?”)

      11 Hata hivyo, haimaanishi kwamba kila mtumishi wa Yehova anaweza kuwa mwenzi wa ndoa anayefaa. Ikiwa unafikiria kufunga ndoa, tafuta mtu ambaye utu na miradi yake ya kiroho inapatana na yako, na anampenda Mungu kama wewe. Jamii ya mtumwa mwaminifu imechapisha habari nyingi kuhusu jambo hilo, na ingefaa ufikirie kwa uzito na kusali kuhusu mashauri hayo ya Kimaandiko, na kuwa tayari kuongozwa nayo unapofanya uamuzi huo muhimu.a—Zaburi 119:105.

      12. Ni desturi gani kuhusu ndoa inayofuatwa katika nchi nyingi, na ni mfano gani wa Biblia unaotoa mwongozo?

      12 Katika nchi nyingi, wazazi humchagulia mtoto wao mwenzi. Kulingana na utamaduni wa watu katika maeneo hayo, wazazi huonwa kuwa wana hekima na uzoefu mwingi zaidi ambao unahitajiwa ili kufanya uamuzi huo wa maana. Mara nyingi ndoa hizo zinafaulu, kama ilivyokuwa nyakati za Biblia. Mfano wa Abrahamu wa kumtuma mtumishi wake akamtafutie Isaka mke unaweza kuwasaidia wazazi walio katika hali kama hiyo leo. Abrahamu hakuhangaikia pesa wala umaarufu. Badala yake, alifanya juu chini kumtafutia Isaka mke kati ya watu wanaomwabudu Yehova.b—Mwanzo 24:3, 67.

      NINATAFUTA MWENZI WA AINA GANI?

      Kanuni: “Wawili watakuwa mwili mmoja.”—Mathayo 19:5.

      Jiulize

      • Kwa nini ingefaa ‘kupita upeo wa ujana’ kabla ya kufunga ndoa?—1 Wakorintho 7:36; 13:11; Mathayo 19:4, 5.

      • Ijapokuwa nina umri wa kutosha kufunga ndoa, kuna faida gani nikiendelea kuwa mseja kwa kipindi fulani?—1 Wakorintho 7:32-34, 37, 38.

      • Nikiamua kufunga ndoa, kwa nini ni jambo la maana kwamba yule atakayekuwa mwenzi wangu wa ndoa awe amemtumikia Yehova kwa uaminifu kwa muda? —1 Wakorintho 7:39.

      • Ni kwa njia gani maandiko yanayofuata yanaweza kumsaidia dada aone sifa ambazo mwenzi wa ndoa anapaswa kuwa nazo?—Zaburi 119:97; 1 Timotheo 3:1-7.

      • Andiko la Methali 31:10-31 linaweza kumsaidia jinsi gani ndugu achague mwenzi wa ndoa kwa hekima?

  • Ndoa—Zawadi Kutoka kwa Mungu Mwenye Upendo
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki