-
Iceland2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Maendeleo Katika Kazi ya Kutafsiri
Mara nyingi imekuwa vigumu kwa wale wahubiri wachache nchini Iceland kutafsiri vitabu vyote kutoka kwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” katika lugha ya Iceland. (Mt. 24:45) Katika miaka ya kwanzakwanza, vichapo vingi vilitafsiriwa na Mashahidi kutoka Iceland walioishi Kanada. Hatimaye kazi hiyo ilifanywa nchini Iceland. Wamishonari wa kwanza walipofika mwaka wa 1947, walipata kufahamiana na mshairi mzee aliyekuwa jirani yao. Alijua Kiingereza na aliwasaidia wamishonari hao kujifunza lugha ya Iceland. Alijitolea pia kuwasaidia kutafsiri. Hivyo, ndugu wakamwajiri kutafsiri kitabu, “Mungu na Awe wa Kweli” na kijitabu kimoja (The Joy of All the People). Jambo la kusikitisha ni kwamba alitumia maneno mengi ya kale na ya kishairi, na ijapokuwa mmoja wa wamishonari wapya na Ndugu Lindal waliisahihisha tafsiri hiyo na kuichapa upya, bado kitabu hicho hakikufaa kwa kuongoza mafunzo ya Biblia kama ilivyotarajiwa. Hata hivyo, kilisambazwa sana tangu kichapwe kwa mara ya kwanza, na jumla ya nakala 14,568 zilichapwa. Zaidi ya nakala 20,000 za kile kijitabu zilichapwa katika mwaka wa 1949. Baadaye, ndugu walimwajiri mtafsiri mwingine atafsiri kitabu kuhusu dini mbalimbali (What Has Religion Done for Mankind?)
Katika miaka hiyo, ndugu wachache walitafsiri vijitabu kadhaa. Kimojawapo ni “Habari Njema Hizi za Ufalme,” kilichotolewa mwaka wa 1959. Kijitabu hicho kiliwasaidia ndugu kuanzisha mafunzo mengi ya Biblia. Baada ya kijitabu hicho kuchapishwa, idhini ya kuchapisha Mnara wa Mlinzi katika lugha ya Iceland ilitolewa.
Vitabu vingi vizuri vilitafsiriwa na kutolewa katika miaka iliyofuata, kama vile: “This Means Everlasting Life” ambacho kilitolewa mwaka wa 1962; Kutoka Paradiso Iliyopotea Mpaka Paradiso Iliyopatikana, mwaka wa 1966; Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, mwaka wa 1970; Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, mwaka wa 1984; na Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, mwaka wa 1996. Gazeti la Amkeni! limetolewa mara nne kwa mwaka katika lugha ya Iceland tangu mwaka wa 1982.
Kwa miaka mingi ndugu hawakuwa na kitabu cha nyimbo katika lugha ya Iceland. Nyimbo nne zilitafsiriwa na kuchapishwa mwaka wa 1960 kwa ajili ya kusanyiko. Na kwenye kusanyiko la wilaya mnamo Novemba 1963, ndugu walifurahi sana kupata kijitabu chenye nyimbo 30.
Kabla ya wakati huo, ndugu walikuwa wakiimba katika lugha mbalimbali mikutanoni. Günther na Rut Haubitz, mapainia wa pekee kutoka Ujerumani, walifika Iceland mwaka wa 1958. Rut bado anakumbuka kwamba ndugu kutoka nchi za kigeni walitumia vitabu vya nyimbo katika lugha yao kama vile Kidenishi, Kifini, Kiingereza, Kijerumani, Kinorway, au Kiswidi. Ndugu na dada wa Iceland waliimba katika lugha yoyote ile waliyoijua vizuri. Anasema, “Ilikuwa kwaya ya mchanganyiko kwelikweli!” Hatua kwa hatua, nyimbo nyingine za Ufalme zilitafsiriwa, na mwishowe kitabu chenye nyimbo zote 225 kikatolewa katika lugha ya Iceland mwaka wa 1999. Ndugu wanathamini sana zawadi hiyo bora kwa ajili ya kumsifu Yehova!
Kusanyiko la wilaya lililofanywa Agosti 1999 lilikuwa na jambo jipya kwa ndugu wa Iceland. Kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli! katika lugha ya Iceland kilitolewa sambamba na kile cha Kiingereza. Msemaji alipokitangaza katika Kiingereza, wasikilizaji wote walipiga makofi. Lakini badala ya kuwaambia ndugu kwamba kitabu hicho kitatolewa baadaye katika lugha ya Iceland, aliwaonyesha nakala ya kitabu hicho katika lugha hiyo, akisema kwamba tayari kilikuwa kimetafsiriwa katika lugha ya Iceland! Wote walisisimka sana. Kitabu cha kwanza na cha pili cha Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote, pia kilitolewa sambamba na kile cha Kiingereza.
-
-
Iceland2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Ofisi ya tawi ilirekebishwa mwaka wa 1998. Makao ya Wanabetheli yalinunuliwa ng’ambo ya barabara ili kuwe na nafasi kubwa zaidi kwenye ofisi hiyo kwa ajili ya Idara ya Tafsiri. Katika miaka ya majuzi watafsiri wamefaidika kutokana na ziara za ndugu kutoka makao makuu huko New York. Ndugu hao wamewafundisha jinsi ya kutumia programu za kompyuta zilizotayarishwa na Mashahidi wa Yehova kwa ajili ya kazi ya kutafsiri.
Hivi majuzi, wawakilishi kutoka makao makuu walikuja ili kuongoza shule ya kuwasaidia watafsiri kuelewa lugha ya Kiingereza vizuri zaidi. Shule hiyo imewasaidia watafsiri kuelewa habari za Kiingereza vizuri zaidi kabla ya kuanza kuzitafsiri.
Ofisi ya tawi inaandika hivi: “Tunapofikiria miaka ambayo imepita, tunafurahi kwamba kulikuwa na watu ambao hawakuogopa kuanza kutafsiri katika lugha ya Iceland, ingawa hawakuwa na vifaa vya kutosha na hawakujua lugha hiyo vizuri. Ijapokuwa tafsiri hizo hazikuwa nzuri kama za leo, ‘hatudharau siku ya mambo madogo.’ (Zek. 4:10) Tunafurahi kuona kwamba jina la Yehova na Ufalme wake umejulikana nchini Iceland, na kwamba wengi wameijua kweli.”
-