-
Iceland2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Majumba Mawili Yajengwa kwa Siku Nne
Ujenzi wa Majumba mawili ya Ufalme mwezi wa Juni ulikuwa tukio la kipekee sana kwa ndugu wa Iceland katika mwaka wa utumishi wa 1995. Moja lilijengwa Keflavík, na lile lingine huko Selfoss. Hayo ni Majumba ya kwanza kujengwa kwa muda mfupi nchini Iceland. Ujenzi wa yote mawili ulichukua siku nne tu na ulifaulu kwa msaada wa ndugu kutoka Norway. Ofisi ya tawi ya Norway ilituma vifaa vingi vya ujenzi, na ndugu na dada zaidi ya 120 kutoka nchi hiyo wakaja kusaidia kujenga. Maneno haya yalisikiwa mara nyingi mahali pa ujenzi: “Hili ni jambo la ajabu kabisa.” Ndugu nchini Iceland walikuwa wamesoma na kusikia kuhusu Majumba ya Ufalme yanayojengwa kwa muda mfupi, lakini sasa walijionea jambo hilo. Bila shaka, lilikuwa jambo la kustaajabisha kwamba kwa muda wa siku chache tu idadi ya Majumba ya Ufalme iliongezeka maradufu nchini Iceland!
Ndugu wa Iceland walipata Majumba mawili mapya ya Ufalme, na pia wakatiwa moyo kwa kushirikiana na ndugu na dada kutoka Norway waliojilipia nauli na kutumia siku zao za likizo ili kusaidia kujenga majumba hayo. Bila shaka, huo ni uthibitisho wa undugu wetu wa ulimwenguni pote! Ndugu wa Iceland pia walisaidia katika ujenzi huo. Wahubiri wenyeji 150 hivi walisaidia pia. Idadi hiyo ni karibu nusu ya wahubiri nchini Iceland.
Watu wa eneo hilo walipata ushahidi pia kupitia ujenzi wa Majumba hayo ya Ufalme. Vituo viwili vya televisheni vinavyorusha matangazo nchini kote vilizungumzia ujenzi huo katika vipindi vya habari na kuonyesha picha za majumba hayo mawili yaliyokuwa yakijengwa. Ujenzi huo ulizungumziwa pia katika vituo kadhaa vya redio na katika magazeti ya kila siku. Kasisi mmoja wa kanisa la Selfoss hakufurahi kwamba Mashahidi walitajwa mara nyingi katika vyombo vya habari. Kwa hiyo, katika gazeti la kila siku la eneo hilo, kasisi huyo alichapisha makala ya kuonya juu ya mafundisho hatari na ya uwongo ya Mashahidi wa Yehova. Alisema kwamba watu waliopungukiwa akili na wanaoweza kushawishika kwa urahisi walipaswa kujihadhari sana. Alipohojiwa kwenye redio alirudia maonyo hayo. Lakini maneno ya kasisi huyo hayakuwa na matokeo aliyotarajia. Badala yake, watu wengi walistaajabia ujenzi wa Majumba hayo ya Ufalme, na wengi ambao ndugu walikutana nao katika kazi ya kuhubiri walisema kwamba walishangaa kusikia maoni ya kasisi huyo.
Juma moja hivi baada ya onyo la kasisi huyo kuchapishwa, gazeti la kila siku lilikuwa na picha ya kuchekesha iliyochorwa. Katika sehemu ya mbele ya picha hiyo kuna kanisa, na nyuma kuna Jumba la Ufalme. Kuna mto kati ya majengo hayo mawili, na ndugu kadhaa wanaotabasamu na waliovalia vizuri wanatembea kwenye daraja kutoka kwenye Jumba la Ufalme wakielekea kanisani, wakiwa na mikoba yao ya utumishi. Nje ya kanisa, mwanamke anaruka kwa woga kutoka katika kiti chake cha magurudumu. Mtu aliyevunjika mguu na mwingine kipofu, wanatimua mbio huku wakipaaza sauti: “Kimbieni, kimbieni, Mashahidi wanakuja!” Yule kasisi amesimama kwenye ngazi ya kuingia kanisani, naye anaonekana kuwa ameshangaa. Wengi walipenda picha hiyo. Mhariri wa gazeti hilo na wafanyakazi wenzake walichagua picha hiyo kuwa picha bora ya kuchekesha ya mwaka huo, nao wakaikuza na kuibandika ukutani katika ofisi yao. Ilibaki hapo kwa miaka kadhaa.
-
-
Iceland2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 249]
Juu: Ujenzi wa Jumba la Ufalme huko Selfoss, mwaka wa 1995
[Picha katika ukurasa wa 249]
Kulia: Jumba la Ufalme la Selfoss
-