-
Iceland2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Makao ya Wamishonari na Majumba ya Ufalme Yahitajiwa
Ndugu Nathan H. Knorr kutoka makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova alipotembelea Iceland mwaka wa 1968, aliona uhitaji wa kuwa na jengo linalofaa kwa ajili ya ofisi ya tawi na makao ya wamishonari. Kabla ya hapo, walikuwa wamekodi nyumba mbalimbali. Ndugu walianza kutafuta kiwanja ambapo wangeweza kujenga jengo moja lenye Jumba la Ufalme, makao ya wamishonari, na ofisi ya tawi. Wakati huohuo, ndugu walikodi nyumba nzuri kwenye barabara ya Hrefnugata, namba 5, mjini Reykjavík, na wale wamishonari sita wakahamia nyumba hiyo Oktoba 1, 1968. Nyumba hiyo ilikuwa kituo cha kazi nchini Iceland kwa miaka mitano iliyofuata. Baadaye, ndugu walinunua kiwanja kilichofaa kwenye barabara ya Sogavegur, namba 71, huko Reykjavík. Ujenzi wa ofisi ya tawi ulianza mapema mwaka wa 1972. Hiyo ilikuwa kazi ngumu kwa ndugu hao wachache wa Iceland kwa sababu hawakujua mengi kuhusu ujenzi. Hakuna ndugu aliyekuwa fundi wa ujenzi wala mwenye kampuni ya ujenzi, kwa hiyo iliwabidi kukodi kampuni ya ujenzi na kuwaajiri mafundi wasiokuwa Mashahidi. Wenye kampuni hizo walikuwa tayari kufanya kazi pamoja na ndugu. Ili wawe na mahali pa kulia chakula, ndugu walikodi sehemu ya nyumba kuukuu iliyokuwa karibu na kiwanja. Dada walipika chakula kwa zamu nyumbani kwao na kuwapelekea wafanyakazi.
Kupitia ujenzi huo, watu wengi walipata kuwajua Mashahidi katika eneo hilo. Watu wenye kampuni za ujenzi na wenye mamlaka mjini walikuwa na nafasi nzuri ya kuwajua Mashahidi wa Yehova. Nao wengine walipopita karibu na uwanja huo, walisimama ili waone jinsi ujenzi ulivyoendelea. Walipokuwa tayari kupiga plasta ndani, ndugu mmoja kutoka Denmark, ambaye ni fundi wa ujenzi, alikuja kusaidia. Pia, dada walisaidia sana katika kazi hiyo. Wenye mamlaka walipotembelea eneo la ujenzi, waliwaona dada wakiendesha mashine ya kuchanganya saruji. Mmoja wao alisema hivi: “Ninafikiri wanawake wa kanisa letu wanaweza kujifunza jambo fulani hapa. Bila shaka, makanisa yangejengwa kwa mafanikio zaidi kwa kufanya kazi badala ya kuzunguka-zunguka na kuomba pesa.” Jengo hilo liliwekwa wakfu Mei 1975, ndugu Milton G. Henschel alipotembelea Iceland na kutoa hotuba ya kuweka wakfu. Kwa miaka mingi jengo hilo lilitumiwa kama makao ya wamishonari na vilevile Jumba la Ufalme kwa makutaniko ya Reykjavík. Sasa jengo hilo ni ofisi ya tawi.
Jumba la Ufalme jipya na makao ya wamishonari huko Akureyri yalijengwa mwaka wa 1987. Umoja na undugu wa ulimwenguni pote wa watu wa Yehova ulionekana wazi wakati ndugu na dada 60 hivi kutoka Finland na Sweden walipokuja kuwasaidia ndugu wa Iceland katika ujenzi huo.
-
-
Iceland2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 243]
Kulia: Jumba la Ufalme na makao ya wamishonari huko Akureyri
-