-
Iceland2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Makusanyiko ya Kimataifa Yaleta Shangwe
Kwa miaka mingi, ndugu wa Iceland wamefurahia kuhudhuria makusanyiko katika nchi nyingine. Ndugu watano kutoka Iceland walikuwa na pendeleo la kuhudhuria kusanyiko la kimataifa la Mapenzi ya Mungu huko New York mwaka wa 1958. Wengi walihudhuria Makusanyiko ya Waabudu Wenye Umoja huko Ulaya mwaka wa 1961, na mwaka wa 1963 wakahudhuria Makusanyiko ya “Habari Njema za Milele.” Wengine walifurahia kushirikiana na ndugu kutoka nchi nyingi kwenye Makusanyiko ya Kimataifa ya “Ushindi wa Kimungu” mwaka wa 1973. Zaidi ya wahubiri 100 kutoka Iceland walihudhuria Kusanyiko la Kimataifa la “Amani Duniani” huko Copenhagen, Denmark, Agosti 5-10, 1969. Hicho ndicho kikundi kikubwa zaidi kutoka Iceland kuhudhuria kusanyiko la kimataifa katika nchi nyingine. Mwaka huohuo, asilimia 80 ya wahubiri wa Iceland walihudhuria kusanyiko hilo katika nchi nyingine.
Ndugu wengi kutoka Iceland walikuwa wamepanga kuhudhuria kusanyiko hilo la mwaka wa 1969, kwa hiyo ofisi ya tawi ya Denmark ilipanga ndugu hao waketi pamoja. Kila asubuhi, kabla ya vipindi vya kusanyiko kuanza, ndugu kutoka Iceland walikusanyika kwenye sehemu yao ambako walielezwa mambo makuu ya programu katika lugha yao.
Mmoja wa wale waliohudhuria kusanyiko hilo ni kijana anayeitwa Bjarni Jónsson. Yeye ni mwana wa wakili aliyemiliki jengo lililokodiwa na ndugu kwa ajili ya makao ya wamishonari na ofisi ya tawi huko Reykjavík. Bjarni hakujua mengi kuhusu kweli, na hakukusudia kuhudhuria kusanyiko aliposafiri pamoja na ndugu hadi Copenhagen. Kwa nini basi alihudhuria kusanyiko hilo?
Kjell Geelnard, aliyekuwa msimamizi wa ofisi ya tawi wakati huo, alikuwa na mambo kadhaa ya kuzungumzia pamoja na baba ya Bjarni. Kjell alimweleza kuhusu kusanyiko la kimataifa huko Copenhagen na kuwahusu ndugu waliopanga kuhudhuria. Wakili huyo aliposikia jambo hilo aliuliza kama mwanaye mkubwa angeweza kuandamana na ndugu hao. Alimwambia Ndugu Geelnard kwamba mwanaye alikuwa amemaliza shule, na angependa kumlipia safari ya kwenda ng’ambo, kwa hiyo huenda safari ya Copenhagen ikamfaa. Kjell aliona wazo hilo kuwa zuri naye akamwambia wakili huyo kwamba ikiwa Bjarni angetaka kuhudhuria kusanyiko ili ajionee jinsi mambo yalivyo kwenye kusanyiko, angeweza kupanga ili apate mahali pa kulala huko Copenhagen. Wakili huyo alifurahi kusikia jambo hilo na kumwuliza mwanaye kama angetaka kujiunga na Mashahidi wa Yehova waliopanga kwenda kusanyikoni. Mwana huyo alikubali mara moja.
Ndugu waliwasiliana na Idara ya Mahali pa Kulala huko Copenhagen ili kumtafutia Bjarni mahali pa kulala. Walipata nafasi katika nyumba ya familia moja ya Mashahidi. Ndugu mmoja kutoka Marekani, ambaye alikuwa amepangiwa kukaa pamoja na ndugu kutoka Iceland anayeitwa Jakob, alikuwa amefuta ombi lake, kwa hiyo Bjarni akapata mahali pake. Hata hivyo, Jakob hakufika kwa sababu fulani. Kwa hiyo, Bjarni peke yake ndiye aliyeenda kwa familia hiyo. Ndugu kwenye Idara ya Mahali pa Kulala hawakuwaeleza watu wa familia hiyo kwamba Bjarni angekuja badala ya yule ndugu kutoka Marekani, kwa hiyo walifikiri kwamba mgeni wao ni Jakob.
Kwa kawaida, ndugu kutoka sehemu mbalimbali wanapokutana wao husimulia mambo yaliyoonwa. Ndugu wa Denmark walishangaa kwamba “Jakob” hakuwa na mengi ya kueleza. Kwa upande mwingine, Bjarni alivurugika kidogo wakati ndugu na dada waliomkaribisha walipomwita Jakob. Kwa kuwa Jakob ni jina linalotajwa katika Biblia, alifikiri kwamba huenda Mashahidi wa Yehova wana desturi ya kutumia majina yanayotajwa katika Biblia wanapoongea na waamini wenzao. Hali hiyo ya kutoelewana ilirekebishwa wakati ndugu mmoja aliyeishi katika nyumba ambayo Bjarni alikaa, alipokutana na ndugu kutoka Denmark aliyekuwa painia huko Iceland. Alimwuliza ndugu huyo kama “Jakob” alikuwa mpya katika kweli, kwa sababu alijua mambo machache sana kuhusu kazi ya kuhubiri huko Iceland. Painia huyo alimweleza kwamba mgeni wao si Jakob bali ni Bjarni, mwanafunzi wa shule kutoka Iceland aliyekuwa amesafiri pamoja na akina ndugu hadi Copenhagen. Ndugu na dada waliomkaribisha Bjarni walionyesha ukarimu na kumwalika akae nao kwa juma lingine ili atembelee sehemu mbalimbali za Denmark. Bjarni aliguswa moyo na fadhili hiyo.
Bjarni alihudhuria kusanyiko. Na ijapokuwa hakufaidika kikamili na programu kwa sababu hakujua mengi kuhusu kweli, yale aliyojionea na kusikia yalimvutia sana. Mara tu aliporudi Iceland, yeye na familia yao walianza kujifunza Biblia. Bjarni alifanya maendeleo makubwa katika kweli na kubatizwa mwaka wa 1971. Ametumikia katika Halmashauri ya Ofisi ya Tawi nchini Iceland tangu mwaka wa 1979.
Svanberg Jakobsson amekuwa mtafsiri kwenye ofisi ya tawi ya Iceland kwa miaka mingi na sasa yeye ndiye mwangalizi wa Idara ya Tafsiri. Alipokuwa mhubiri kijana, alihudhuria Kusanyiko la Kimataifa la “Ushindi wa Kimungu” huko London, Uingereza, mwaka wa 1973. Anasema hivi: “Ninakumbuka jinsi nilivyosisimuka nilipowatazama maelfu ya ndugu na dada wakimiminika kwenye uwanja wa kusanyiko. Nilishangaa kuwaona ndugu na dada wengi kutoka Afrika, wote wakiwa wamevalia mavazi ya kitamaduni yenye rangi mbalimbali. Siwezi kamwe kusahau furaha ya kuwa pamoja na makumi ya maelfu ya ndugu, kusikiliza programu pamoja nao, kuimba pamoja nao, kusali pamoja nao, na kula pamoja nao.”
Sólborg Sveinsdóttir, aliyebatizwa mwaka wa 1958, alisafiri kwa meli kwa muda wa siku sita, pamoja na watoto wanne, ili kuhudhuria kusanyiko huko Copenhagen, Denmark, mwaka wa 1961. Sólborg alikuwa katika kikundi kidogo kilichokuwa mbali sana huko Keflavík. Alihisije baada ya kuhudhuria kusanyiko kubwa la kimataifa? Anasema hivi: “Nilivutiwa sana kusikia zaidi ya ndugu 30,000 wakiimba nyimbo za Ufalme katika lugha tano. Jambo hilo lilinigusa moyo sana. Mambo yote yalikuwa yamepangwa vizuri sana.”
Ijapokuwa iliwagharimu pesa nyingi, ndugu waliona inafaa kuhudhuria makusanyiko hayo ya kimataifa. Ilikuwa baraka kuhudhuria karamu hizo nzuri za kiroho zilizoandaliwa na Yehova, na kuwa pamoja na maelfu ya waamini wenzao.
-
-
Iceland2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 227]
Zaidi ya wahubiri 100 kutoka Iceland walihudhuria Kusanyiko la Kimataifa la “Amani Duniani” huko Copenhagen, Denmark, mwaka wa 1969
-