-
Iceland2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Mwaka wa 1952 iliamuliwa kwamba eneo la pwani ya kaskazini lilihitaji kuhubiriwa zaidi. Kwa hiyo, mnamo Juni mwaka huo, Oliver Macdonald na mkewe Sally, ambaye alikuja kutoka Uingereza mwaka wa 1949 ili aolewe naye, wakawekwa kuwa mapainia wa pekee na kutumwa Akureyri. Huko walipingwa sana na watu wa dini inayoitwa Ndugu wa Plymouth walioongozwa na balozi wa Uingereza mjini humo. Alikuwa na wafuasi wengi, na wengine walimsikiliza alipowashambulia Mashahidi katika hotuba zake, na katika makala alizoandika. Mapainia hao hawakuwa wamepatwa na upinzani kama huo walipokuwa Reykjavík, hata hivyo walipambana na shambulizi hilo bila woga, nao wakaendelea na kazi yao wakitumia kila nafasi kujibu mashtaka hayo ya uwongo. Baadhi ya magazeti yalichapisha majibu yao.
Mapainia hao walihubiri mjini humo, na vilevile mashambani, na kuwaachia watu vitabu. Kwa kawaida watu waliwakaribisha kwa chakula na kahawa, lakini hawakupata watu waliopendezwa kikweli na ujumbe wa Ufalme. Ndugu na Dada Macdonald walirudi Reykjavík mnamo Julai 1953, lakini kabla ya kuondoka Akureyri, walipanda mbegu za kweli, ambazo zilimea baadaye.
-
-
Iceland2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Hata hivyo, wamishonari na mapainia wote waliokuwa wamehubiri kwa bidii ili kweli itie mizizi nchini Iceland walikuwa wameondoka mwaka wa 1957, wengi wao kwa sababu ya matatizo ya afya.
Kwa hiyo, mwaka wa 1957, Dada Edith Marx, painia wa pekee kutoka Denmark ambaye alikuwa amekuja mwaka uliotangulia, alikabidhiwa madaraka ya kutunza lile kutaniko dogo. Wavunaji walihitajiwa ili kulisaidia kutaniko hilo dogo, ambalo lilijikuta limeachwa na ndugu waliokuwa wamewasaidia wale wapya kuijua kweli na kuwa imara. Muda si muda mapainia wa pekee kutoka Denmark, Sweden, na Ujerumani wakafika.
-