Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Imani Yako Katika Ufufuo Ni Yenye Nguvu Kadiri Gani?
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Julai 1
    • Maoni ya Jumuiya ya Wakristo Kuhusu Uhai Baada ya Kifo

      7. (a) Makanisa yaliyo mengi huamini nini? (b) Mwanatheolojia mmoja alifafanuaje fundisho la nafsi isiyoweza kufa?

      7 Licha ya tofauti zao nyingi, karibu madhehebu yote ya Jumuiya ya Wakristo hukubali kwamba wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa ambayo huendelea kuwa hai baada ya kufa kwa mwili. Walio wengi huamini kwamba mtu anapokufa, huenda nafsi yake ikaenda mbinguni. Wengine huhofu kwamba huenda nafsi yao ikaenda helo yenye moto au purgatori. Lakini wazo la nafsi isiyoweza kufa ni jambo kuu katika maoni yao juu ya uhai wa wakati ujao. Mwanatheolojia, Oscar Cullmann, alieleza juu ya hilo katika taarifa yake iliyochapishwa katika kitabu Immortality and Resurrection. Aliandika hivi: “Kama tungeuliza Mkristo wa kawaida leo . . . kulingana na mawazo yake, Agano Jipya hufundisha nini kuhusu kitakachompata mwanadamu baada ya kifo, walio wengi wangejibu hivi: ‘Kutoweza kufa kwa nafsi.’” Hata hivyo, Cullmann aliongeza kusema hivi: “Wazo hilo ambalo limekubaliwa na wengi ni mojawapo ya sababu za kutoelewana kukubwa zaidi kwa Ukristo.” Cullmann alisema kwamba alisababisha mfoko wa ghadhabu aliposema hivyo mara ya kwanza. Hata hivyo, hakukosea.

      8. Yehova alimwekea mwanamume na mwanamke wa kwanza taraja gani?

      8 Yehova Mungu hakuwaumba wanadamu waende mbinguni baada ya kufa. Awali, hakukusudia wafe kamwe. Adamu na Hawa waliumbwa wakiwa wakamilifu na walipewa fursa ya kuijaza dunia kwa uzao mwadilifu. (Mwanzo 1:28; Kumbukumbu la Torati 32:4) Wazazi wetu wa kwanza waliambiwa kwamba wangekufa iwapo tu wangekosa kumtii Mungu. (Mwanzo 2:17) Kama wangaliendelea kuwa watiifu kwa Baba yao wa kimbingu, wangaliendelea kuishi duniani milele.

      9. (a) Ni nini iliyo kweli kuhusu nafsi ya kibinadamu? (b) Ni nini hutukia kwa nafsi inapokufa?

      9 Ingawa hivyo, kwa kusikitisha Adamu na Hawa walishindwa kumtii Mungu. (Mwanzo 3:6, 7) Mtume Paulo anayafafanua matokeo yenye kuhuzunisha hivi: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikasambaa kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Badala ya kuishi milele duniani, Adamu na Hawa walikufa. Basi, ni nini kilichotukia? Je, walikuwa na nafsi zisizoweza kufa ambazo sasa zingeweza kupelekwa kwenye helo yenye moto kwa sababu ya dhambi yao? Kinyume cha hilo, Biblia husema kwamba, mapema alipoumbwa, Adamu ‘alikuwa nafsi hai.’ (Mwanzo 2:7) Mwanadamu hakupewa nafsi; alikuwa nafsi, mtu anayeishi. (1 Wakorintho 15:45) Kumbe, si Adamu tu aliyekuwa “nafsi hai,” bali kama vile ionyeshwavyo katika Kiebrania ambacho kilitumiwa kuandika kitabu cha Mwanzo, wanyama wa hali ya chini pia walikuwa “nafsi hai”! (Mwanzo 1:24) Adamu na Hawa walipokufa, walikuwa nafsi zilizokufa. Hatimaye, ilitukia kwao kama vile Yehova alikuwa amemwambia Adamu: “Kwa jasho la uso wako utakula chakula, hata utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.”—Mwanzo 3:19.

      10, 11. Kichapo New Catholic Encyclopedia hukubali nini kuhusu fundisho la Biblia juu ya nafsi, na hilo hulinganaje na yale Biblia husema?

      10 Kichapo New Catholic Encyclopedia hukubaliana kimsingi na jambo hilo. Katika makala yake “Nafsi (katika Biblia),” chasema hivi: “Katika AK [“Agano la Kale,” au Maandiko ya Kiebrania], mwili na nafsi hazigawanywi kuwa sehemu mbili.” Chaongeza kusema kwamba katika Biblia, neno “nafsi” “halimaanishi kamwe kwamba nafsi ni tofauti na mwili au na mtu mwenyewe.” Kwa kweli, nafsi mara nyingi “humaanisha kiumbe chenyewe, kiwe mnyama au kiwe mwanadamu.” Uwazi huo ni wenye kuburudisha, lakini mtu anaweza tu kushangaa ni kwa nini waenda-kanisani kwa ujumla hawajafahamishwa mambo hayo ya hakika.

      11 Waenda-kanisani wangaliepushwa na wasiwasi na hofu nyingi kama nini iwapo wangalijua kweli hii sahili ya Biblia: “Nafsi inayofanya zambi, itakufa,” wala si kuteseka katika moto wa helo! (Ezekieli 18:4, ZSB) Ingawa jambo hilo ni tofauti sana na yale Jumuiya ya Wakristo hufundisha, linapatana kabisa na yale ambayo Solomoni, mwanamume mwenye hekima alipuliziwa kusema: “Walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote, wala hawana ijara tena; maana kumbukumbu lao limesahauliwa. Lo lote mkono wako utakalolipata kulifanya, ulifanye kwa nguvu zako; kwa kuwa hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu [kaburi la kawaida la wanadamu] uendako wewe.”—Mhubiri 9:5, 10.

      12. Jumuiya ya Wakristo ilipata wapi fundisho lake kuhusu nafsi isiyoweza kufa?

      12 Kwa nini Jumuiya ya Wakristo hufundisha mambo tofauti na yale Biblia husema? Kichapo New Catholic Encyclopedia, katika makala yake ya “Kutoweza Kufa kwa Nafsi na kwa Binadamu,” chasema kwamba Waandishi wa Kanisa walitegemeza imani yao juu ya nafsi isiyoweza kufa, katika “washairi na wanafalsafa na dhana ya kimapokeo ya Kigiriki wala si katika Biblia . . . Baadaye, wasomi walipendelea kutumia imani ya Plato au kanuni za Aristotle.” Kichapo hicho chataarifu kwamba “uvutano wa dhana ya Uplato na Uplato mpya”—kutia na imani katika nafsi isiyoweza kufa—hatimaye ziliingizwa “katika mambo ya msingi ya theolojia ya Kikristo.”

      13, 14. Kwa nini si jambo la akili kutumaini kuelimishwa na wanafalsafa wapagani Wagiriki?

      13 Je, wanaodai kuwa Wakristo wangalipaswa kugeukia wanafalsafa wapagani Wagiriki kujifunza jambo la msingi kama vile tumaini la uhai baada ya kifo? Bila shaka la. Paulo alipowaandikia Wakristo walioishi Korintho, Ugiriki, alisema hivi: “Hekima ya ulimwengu huu ni upumbavu kwa Mungu; kwa maana imeandikwa: ‘Yeye hunasa wenye hekima katika ujanja wao wenyewe.’ Na tena: ‘Yehova ajua kwamba mawazowazo ya watu wenye hekima ni ya ubatili.’” (1 Wakorintho 3:19, 20) Wagiriki wa kale walikuwa waabudu-sanamu. Hivyo basi, wangeweza kuwaje chanzo cha ile kweli? Paulo aliwauliza Wakorintho hivi: “Hekalu la Mungu lina upatano gani na sanamu? Kwa maana sisi ni hekalu la Mungu aliye hai; kama vile Mungu alivyosema: ‘Mimi nitakaa miongoni mwao na kutembea miongoni mwao, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.’”—2 Wakorintho 6:16.

      14 Ufunuo wa kupata kweli takatifu ulitolewa mara ya kwanza kupitia taifa la Israeli. (Waroma 3:1, 2) Baada ya mwaka wa 33 W.K., ulitolewa kupitia kutaniko la Kikristo la watiwa-mafuta la karne ya kwanza. Akizungumza kuhusu Wakristo wa karne ya kwanza, Paulo alisema hivi: “Ni kwetu sisi Mungu ameyafunua [mambo yaliyotayarishwa kwa ajili ya wale wampendao] kupitia roho yake.” (1 Wakorintho 2:10; ona pia Ufunuo 1:1, 2.) Fundisho la Jumuiya ya Wakristo juu ya kutokufa kwa nafsi limetolewa katika falsafa za Kigiriki. Haikufunuliwa kupitia ufunuo mbalimbali wa Mungu kwa Waisraeli au kupitia kutaniko la karne ya kwanza la Wakristo watiwa-mafuta.

      Tumaini Halisi kwa Wafu

      15. Kulingana na Yesu, wafu wana tumaini gani halisi?

      15 Iwapo hakuna nafsi yoyote isiyoweza kufa, je, kuna tumaini gani halisi kwa wafu? Bila shaka kuna tumaini la ufufuo, ambalo ni fundisho kuu la Biblia, na ahadi ya Mungu ambayo kwa kweli ni ya ajabu. Yesu alimtolea rafiki yake Martha tumaini la ufufuo alipomwambia hivi: “Mimi ndio ufufuo na uhai. Yeye ambaye hudhihirisha imani katika mimi, hata ingawa afa, atakuja kwenye uhai.” (Yohana 11:25) Kumwamini Yesu kwamaanisha kuamini ufufuo, wala si kuamini nafsi isiyoweza kufa.

  • Imani Yako Katika Ufufuo Ni Yenye Nguvu Kadiri Gani?
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Julai 1
    • Mwili na Nafsi

      18. Wanafalsafa fulani Wagiriki waliitikiaje taarifa ya Paulo ya kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa, na kwa nini?

      18 Alipokuwa Athene, mtume Paulo alihubiri habari njema kwa umati uliotia ndani wanafalsafa Wagiriki. Walisikiliza mazungumzo hayo kuhusu Mungu mmoja wa kweli na mwito wake wa toba. Lakini ni nini kilichotukia baadaye? Paulo alimalizia hotuba yake kwa kusema hivi: “[Mungu] ameweka siku ambayo katika hiyo akusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kwa njia ya mwanamume ambaye ameweka rasmi, naye ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemfufua kutoka kwa wafu.” Maneno hayo yalitokeza mvurugo. “Waliposikia juu ya ufufuo wa wafu, wengine wao wakaanza kudhihaki.” (Matendo 17:22-32) Mwanatheolojia Oscar Cullmann asema hivi: “Kwa Wagiriki walioamini kwamba nafsi haiwezi kufa, huenda lilikuwa jambo gumu zaidi kwao kukubali yale Wakristo waliyohubiri kuhusu ufufuo kuliko ilivyokuwa kwa wengine. . . . Fundisho la Socrates na Plato, waliokuwa wanafalsafa wakuu, haliwezi kwa vyovyote kupatanishwa [kukubaliana] na fundisho la Agano Jipya.”

      19. Wanatheolojia wa Jumuiya ya Wakristo walijaribu kupatanishaje fundisho la ufufuo na fundisho la kwamba nafsi haiwezi kufa?

      19 Ijapokuwa hivyo, kufuatia uasi mkubwa baada ya kifo cha mitume, wanatheolojia walijitahidi kuunganisha fundisho la Wakristo juu ya ufufuo, na imani ya Plato katika nafsi isiyoweza kufa. Baada ya muda, baadhi yao walikubaliana juu ya utatuzi huu mpya: Wakati wa kufa, nafsi hutenganishwa (“huwekwa huru,” kama vile wengine husema) na mwili. Kisha kulingana na kichapo Outlines of the Doctrine of the Resurrection, cha R. J. Cooke, Siku ya Hukumu “kila mwili utaunganishwa tena na nafsi yake wenyewe, na kila nafsi na mwili wake yenyewe.” Kuunganishwa wakati ujao kwa mwili na nafsi yake isiyoweza kufa, kwasemekana kuwa ndio ufufuo.

      20, 21. Ni nani ambao wamefundisha kweli kuhusu ufufuo kwa upatano, na hilo limewanufaishaje?

      20 Nadharia hiyo bado ni fundisho rasmi la makanisa mashuhuri. Ingawa dhana hiyo yaweza kuonekana kuwa jambo la akili kwa mwanatheolojia, waenda-kanisani wengi hawaifahamu. Wao huamini tu kwamba wataenda mbinguni moja kwa moja watakapokufa. Kwa sababu hiyo, katika makala ya Mei 5, 1995, ya Commonweal, mwandishi John Garvey alidai kwamba: “Imani ya Wakristo walio wengi [kuhusu uhai baada ya kifo] yaonekana yakaribiana zaidi na ile imani ya Uplato mpya kuliko inavyokaribiana na imani yoyote ambayo kwa kweli ni ya Kikristo, na haina msingi wowote wa Biblia.” Kwa kweli, kwa kubadilisha Biblia na imani ya Plato, makasisi wa Jumuiya ya Wakristo walifuta tumaini la Biblia la ufufuo kwa makundi yao.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki