Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kukosa Subira Kunaweza Kuleta Madhara
    Amkeni!—2012 | Desemba
    • Kukosa Subira Kunaweza Kuleta Madhara

      FIKIRIA mfano huu: Mwanamume fulani anaendesha gari lake kwenye barabara ambayo ni kinyume cha sheria kulipita gari lililo mbele yako. Mwanamke aliye mbele yake anaendesha gari kwa mwendo wa chini kidogo kuliko ule uliowekwa. Mwanamume huyo asiye na subira anaona kwamba mwanamke huyo anaendesha gari polepole sana. Baada ya kumfuata kwa ukaribu sana kwa dakika chache, anakosa subira kabisa na kuendesha gari kwa mwendo wa kasi na kumpita. Kwa kufanya hivyo anavunja sheria na pia anaweza kusababisha aksidenti.

      Namna gani mwanamke ambaye hana subira anapofanya kazi na watu ambao hawafanyi kazi haraka na si werevu kama yeye? Au mwanamume asiye na subira ambaye kila wakati anabonyeza kidude cha kufanya lifti ije? Je, mara nyingi wewe hushindwa kuwa na subira unaposhughulika na wazazi wako waliozeeka? Au je, wewe ni mzazi ambaye hukosa subira haraka unaposhughulika na watoto wako wachanga? Je, wewe hukasirishwa haraka na makosa ya wengine?

      Yaelekea kila mtu atakosa kuwa na subira pindi fulani. Lakini huenda kukawa na matokeo mabaya ikiwa ni jambo la kawaida kwa mtu kukosa subira.

      Madhara kwa afya:

      [Picha katika ukurasa wa 5]

      Imesemekana kwamba kukosa subira humfanya mtu akate tamaa, audhike, na hata apandwe na hasira. Hisia hizo zinaweza kutufanya tuwe na mkazo zaidi, na hilo linaweza kudhuru afya yetu. Uchunguzi wa hivi karibuni uliochapishwa na Chama cha Kitiba cha Marekani ulitaja kihususa kwamba kukosa subira huongeza hatari ya kupanda kwa shinikizo la damu, hata miongoni mwa vijana.

      Kuna matatizo mengine ya afya yanayohusianishwa na kukosa subira. Uchunguzi wa hivi karibuni unaonyesha kwamba kukosa subira kunaweza kutokeza tatizo la kunenepa kupita kiasi. “Watafiti waligundua kwamba watu ambao hawana subira wana uwezekano mkubwa wa kuwa wanene kupita kiasi kuliko watu wenye subira,” linaripoti gazeti Washington Post. Katika maeneo fulani, vyakula visivyo na lishe ambavyo hupikwa haraka vinapatikana kwa urahisi na kwa bei nafuu wakati wote, jambo ambalo huwavutia watu wasio na subira.

      Kuahirisha mambo:

      [Picha katika ukurasa wa 6]

      Utafiti uliofanywa na Kituo cha Utafiti wa Sera za Kiuchumi huko London ulionyesha kwamba watu wasio na subira wana mazoea ya kuahirisha mambo yanayopaswa kufanywa. Je, inawezekana kwamba wao huahirisha kazi ambazo zitachukua wakati mwingi kwa sababu hawana subira ya kufanya kazi hizo hadi wazikamilishe? Vyovyote vile, mazoea ya kuahirisha mambo yanaweza kuwa na matokeo mabaya kwa mwenye kuahirisha na kwa uchumi. Kulingana na gazeti The Telegraph, linalochapishwa huko Uingereza, mtafiti Ernesto Reuben alisema kwamba “kuahirisha mambo huathiri sana kazi na kuwagharimu watu pesa nyingi [watu wasio na subira] wanapoahirisha kufanya kazi kwa muda mrefu.”

      Kutumia vibaya kileo na matendo ya jeuri:

      [Picha katika ukurasa wa 6]

      Gazeti la Uingereza, South Wales Echo linasema kwamba “watu wasio na subira wana uwezekano mkubwa wa kujihusisha katika jeuri baada ya kunywa kileo hadi usiku wa manane.” Watafiti katika Chuo Kikuu cha Cardiff walithibitisha hilo baada ya kuwachunguza mamia ya wanaume na wanawake.

      Kufanya maamuzi yasiyofaa:

      [Picha katika ukurasa wa 6]

      Kikundi cha wachanganuzi katika Kituo cha Utafiti cha Pew huko Washington, D.C., kiligundua kwamba kwa sababu ya kukosa subira watu “mara nyingi hufanya haraka maamuzi yasiyo na hekima.” Dakt. Ilango Ponnuswami, ambaye ni profesa na msimamizi wa Idara ya Huduma za Jamii katika Chuo Kikuu cha Bharathidasan, India, alifikia mkataa huohuo. Anaeleza hivi: “Kukosa subira kutakugharimu. Kutakugharimu pesa na marafiki, kutakuletea maumivu na kuteseka au madhara mengine, kwa kuwa mara nyingi watu wasio na subira hufanya maamuzi mabaya.”

      Matatizo ya kifedha:

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Gazeti Research Review, linalochapishwa na Benki ya Federal Reserve ya Boston linasema kwamba kukosa subira kumehusianishwa na “kuwa na madeni mengi.” Kwa mfano, huenda wenzi wa ndoa ambao wameoana hivi karibuni wakakosa subira na kutaka kuwa na vitu vyote vya nyumba mara tu baada ya kufanya harusi licha ya kwamba hawana pesa za kuvinunua. Kwa hiyo, wananunua nyumba, fanicha, gari, na vitu vingine kwa mkopo. Jambo hilo linaweza kuleta mzozo katika ndoa. Watafiti katika Chuo Kikuu cha Arkansas, Marekani wanasema kwamba “wenzi wa ndoa ambao wameoana hivi karibuni wanaoanza maisha yao kwa madeni hawana furaha kama wenzi ambao huwa na madeni machache sana au hawana madeni yoyote wanapoanza maisha ya ndoa.”

      Watu fulani wanasema kwamba kukosa subira ndiko kulikosababisha kuporomoka kwa uchumi wa Marekani hivi karibuni. Gazeti Forbes ambalo huzungumzia mambo ya kiuchumi linadai kwamba “hali iliyopo sasa katika soko la ulimwengu ilisababishwa na kukosa subira na pupa. Ukosefu wa subira uliwafanya watu wengi sana wa kawaida wanunue nyumba kwa bei ya juu zaidi kuliko pesa walizokuwa nazo katika benki. Kwa hiyo, waliamua kukopa pesa nyingi sana ambazo ingewachukua miaka mingi kuzilipa—na hata katika visa fulani, hawangeweza kuzilipa maisha yao yote.”

      Kupoteza marafiki:

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Kukosa subira kunaweza kutufanya tupoteze uwezo wetu wa kuwasiliana. Ikiwa mtu hana subira ya kujihusisha katika mazungumzo yanayojenga, yaelekea atazungumza bila kufikiri. Huenda pia akakasirika watu wengine wanapozungumza. Mtu wa aina hiyo hana subira ya kungoja hadi mtu aseme anachotaka kusema. Kwa hiyo, msikilizaji asiye na subira anaweza kuwaharakisha wengine wamalize wanachosema kwa kuwamalizia sentensi zao au kujaribu kutumia njia nyingine kuharakisha mazungumzo.

      Ukosefu huo wa subira unaweza kumfanya mtu apoteze marafiki. Dakt. Jennifer Hartstein, mtaalamu wa magonjwa ya akili aliyenukuliwa katika makala iliyotangulia anaeleza hivi: “Ni nani anayetaka kuwa na mtu ambaye kila mara anagongesha-gongesha miguu yake chini kwa kukosa subira [au] anatazama saa yake kila mara?” Kwa kweli kukosa subira si sifa nzuri. Kutafanya usiwe na marafiki.

      Hayo ni baadhi tu ya mambo ambayo huenda yakatokea kwa sababu ya kukosa subira. Makala inayofuata itazungumzia jinsi ya kusitawisha sifa ya subira na kuidumisha.

  • Jinsi ya Kuwa Mwenye Subira Zaidi
    Amkeni!—2012 | Desemba
    • Jinsi ya Kuwa Mwenye Subira Zaidi

      [Picha katika ukurasa wa 8, 9]

      Hakuna faida ya kuwa na wasiwasi kuhusu mambo ambayo huwezi kudhibiti

      BAADA ya kusoma makala zilizotangulia, huenda ukakubali kwamba kadiri ulivyo mwenye subira ndivyo unavyokuwa na afya nzuri, unavyofanya maamuzi mazuri, na kuwa na marafiki wazuri. Kwa hiyo, unawezaje kuwa mwenye subira zaidi? Chunguza mapendekezo yafuatayo.

      Tambua visababishi:

      Kuna mambo au hali mbalimbali zinazoweza kumfanya mtu akose subira. Ni nini hasa hukufanya wewe ukose subira? Je, ni watu fulani hususa? Huenda mwenzi wa ndoa, wazazi, au watoto wako wakawa ndio hasa wanaokufanya ukose subira maishani. Au je, wewe hukosa subira kwa sababu ya wakati? Kwa mfano, je, wewe hukosa subira unapolazimika kuwangoja wengine au ikiwa umechelewa? Je, wewe hukosa subira unapokuwa umechoka, una njaa, una usingizi, au uko chini ya mkazo fulani? Je, wewe hukosa subira hasa unapokuwa nyumbani au kazini?

      Kujua mambo yanayokufanya ukose subira kutakusaidiaje? Zamani za kale, Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Mtu mwangalifu huona hatari akajificha, lakini wajinga hujitokeza mbele wakaumia.” (Methali 22:3, Biblia Habari Njema) Kupatana na methali hiyo ya kale ya Biblia, ikiwa utaona kimbele kwamba jambo fulani litakufanya ukose subira, huenda ukazuia hilo lisitokee. Huenda mwanzoni ikakubidi ujitahidi sana kuwa mwenye subira zaidi, lakini baada ya muda, kuwa na subira kunaweza kuwa jambo la kawaida kwako.

      Rahisisha maisha yako:

      Profesa Noreen Herzfeld, ambaye hufundisha sayansi ya kompyuta katika Chuo Kikuu cha Saint John’s huko Minnesota, Marekani anasema kwamba “watu hawawezi kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja. Ubongo hauwezi kukazia fikira mambo mbalimbali wakati uleule.” Anaongezea hivi: “Baada ya muda, kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja hupunguza uwezo wetu wa kukaza fikira, kuwa makini, na mwishowe hilo huharibu sifa nzuri kama vile subira, uthabiti, uwezo wa kufanya maamuzi mazuri, na kutatua matatizo.”

      Ni vigumu kuwa mwenye subira unapokuwa na mkazo kwa sababu ya kuwa na mambo mengi ya kufanya, sehemu nyingi unazotazamiwa kwenda, na watu wengi wa kuwasiliana nao. Dakt. Jennifer Hartstein, aliyetajwa hapo awali katika mfululizo huu anaonya hivi: “Kimsingi, mkazo ndicho kisababishi cha ukosefu wa subira.”

      Msemo unaojulikana sana unasema, “subira huvuta heri.” Kwa hiyo, tenga wakati wa kufurahia maisha. Tenga wakati wa kuanzisha urafiki wa karibu na watu wachache badala ya kuwa na urafiki wa kijuujuu na watu wengi. Pangia wakati wako na ufahamu mambo ya kutanguliza. Jihadhari na vifaa vya kiteknolojia na mambo mengine yanayopoteza wakati.

      Ili kurahisisha maisha yako, huenda ikafaa kuchunguza ratiba yako ya kila siku. Ni utendaji gani unaopaswa kupunguza au kuondoa? Methali moja ya Biblia inasema: “Kuna wakati uliowekwa wa kila kitu . . . , wakati wa kuweka na wakati wa kutupa.” (Mhubiri 3: 1, 6) Huenda sasa ndio wakati wa kuondoa mambo yanayochukua wakati mwingi hivi kwamba unakuwa na shughuli nyingi zinazokufanya ukose subira.

      Ona mambo kihalisi:

      Ona maisha kwa njia halisi. Kwanza kabisa, katika maisha ya kila siku, mambo hayafanyiki haraka kama tunavyotaka. Huwezi kutarajia mambo yatendeke wakati ambapo wewe unataka yatendeke. Unahitaji subira.

      Pili, kumbuka kwamba si kila wakati unaweza kudhibiti hali zako. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Si wenye mbio wanaoshinda katika mbio, wala wenye nguvu wanaoshinda katika pigano, wala pia wenye hekima wanaopata chakula, wala pia wenye uelewaji wanaokuwa na utajiri, wala wenye ujuzi wanaopata kibali; kwa sababu wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote. Kwa maana mwanadamu pia hajui wakati wake.”​—Mhubiri 9:11, 12.

      Badala ya kukosa subira kwa sababu ya hali ambazo huwezi kudhibiti, jaribu kutambua mambo ambayo wewe unaweza kudhibiti. Kwa mfano, badala ya kukasirika kwa sababu basi limechelewa, tafuta njia nyingine ya usafiri. Huenda hata ikawa afadhali kutembea badala ya kukosa subira na kukasirika. Ikiwa ni lazima ungojee, tumia wakati huo kufanya jambo la maana, kama vile kusoma kitu fulani au kuandika mambo unayopanga kufanya.

      Ukweli wa mambo ni kwamba hakuna faida ya kuwa na wasiwasi kuhusu mambo ambayo huwezi kudhibiti. Biblia inasema hivi kwa kufaa: “Ni nani miongoni mwenu ambaye kwa kusumbuka anaweza kujiongeza maisha yake hata kwa saa moja?”​—Luka 12:25, Neno—​Biblia Takatifu.

      Sitawisha urafiki pamoja na Mungu:

      Watu wengi wanaoiamini Biblia wamegundua kwamba wanaweza kuwa na subira wanapofuata kanuni zake. Biblia inasema kwamba mtu aliye na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu ana mwelekeo wa kuonyesha subira pamoja na sifa nyingine muhimu kama vile upendo, shangwe, amani, upole, na kujizuia. (Wagalatia 5:22, 23) Biblia inaahidi hivi: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.” (Wafilipi 4:6, 7) Soma Biblia na ujifunze jinsi unavyoweza kuwa mwenye subira zaidi na kuishi bila mahangaiko.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki