-
Ahadi ya Mkuu wa AmaniUnabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
Nchi ‘Yadharauliwa’
13. “Galilaya ya mataifa” ni nini, nayo yajaje “kudharauliwa”?
13 Isaya sasa agusia tukio moja kati ya matukio yenye maafa makubwa zaidi yanayowakumba wazao wa Abrahamu: “Yeye aliyekuwa katika dhiki hatakosa changamko. Hapo kwanza aliiingiza nchi ya Zabuloni na nchi ya Naftali katika hali ya kudharauliwa, lakini zamani za mwisho ameifanya kuwa tukufu, karibu na njia ya bahari; ng’ambo ya Yordani, Galilaya ya mataifa.” (Isaya 9:1) Galilaya ni eneo katika ufalme wa kaskazini wa Israeli. Katika unabii wa Isaya eneo hilo latia ndani “nchi ya Zabuloni na nchi ya Naftali” na pia “njia ya bahari,” ambayo ni njia ya zamani iliyokuwa kandokando ya Bahari ya Galilaya na kufika kwenye Bahari ya Mediterania. Katika siku ya Isaya, eneo hilo laitwa “Galilaya ya mataifa,” labda kwa sababu wakazi katika mengi ya majiji yake ni watu wasio Waisraeli.c Nchi hiyo ‘yadharauliwaje’? Waashuri wapagani waishinda, wawapeleka Waisraeli uhamishoni, na kuleta wakazi wapagani katika eneo hilo, ambao si wazao wa Abrahamu. Basi ufalme wa kaskazini wa makabila kumi watoweka katika historia, na kutokuwa taifa dhahiri tena!—2 Wafalme 17:5, 6, 18, 23, 24.
14. “Dhiki” ya Yuda itakuwaje nyepesi kuliko ile ya ufalme wa makabila kumi?
14 Yuda pia imesongwa na Waashuri. Je, itatokomea katika “dhiki” kama ule ufalme wa makabila kumi uliowakilishwa na Zabuloni na Naftali? La. Katika “zamani za mwisho,” Yehova ataleta baraka katika eneo la ufalme wa kusini wa Yuda na hata katika nchi ambayo hapo awali ilitawaliwa na ufalme wa kaskazini. Jinsi gani?
15, 16. (a) Wakati unaoitwa “zamani za mwisho” ambapo hali itabadilika kwa “wilaya za Zebuloni na Naftali” ni upi? (b) Nchi iliyodharauliwa yapata kuheshimiwaje?
15 Mtume Mathayo ajibu swali hilo katika rekodi yake iliyopuliziwa ihusuyo huduma ya Yesu duniani. Akifafanua siku za mwanzo za huduma hiyo, Mathayo asema: “Baada ya kuondoka Nazareti, [Yesu] alikuja na kufanya makao katika Kapernaumu kando ya bahari katika wilaya za Zebuloni na Naftali, ili kupate kutimizwa lile lililosemwa kupitia Isaya nabii, akisema: ‘Ewe nchi ya Zebuloni na nchi ya Naftali, kando ya barabara ya bahari, katika upande ule mwingine wa Yordani, Galilaya ya mataifa! watu wenye kuketi katika giza waliona nuru kubwa, na kwa habari ya wale wenye kuketi katika mkoa wa kivuli cha kifo, nuru iliwazukia.’”—Mathayo 4:13-16.
16 Naam, “zamani za mwisho” alizotabiri Isaya ni wakati wa huduma ya Kristo duniani. Yesu alitumia wakati mwingi wa maisha yake duniani akiwa Galilaya. Alianza huduma yake katika wilaya ya Galilaya na kutangaza: “Ufalme wa mbingu umekaribia.” (Mathayo 4:17) Huko Galilaya, alitoa Mahubiri ya Mlimani yaliyo maarufu sana, akawachagua mitume wake, akafanya mwujiza wake wa kwanza, na kuonekana kwa wafuasi wapatao 500 baada ya ufufuo wake. (Mathayo 5:1–7:27; 28:16-20; Marko 3:13, 14; Yohana 2:8-11; 1 Wakorintho 15:6) Hivyo, Yesu alitimiza unabii wa Isaya kwa kuitukuza “nchi ya Zabuloni na nchi ya Naftali.” Bila shaka, Yesu hakuhudumia watu wa Galilaya peke yao. Kwa kuhubiri habari njema nchini kote, Yesu ‘alilifanya kuwa tukufu’ taifa lote la Israeli, kutia ndani Yuda.
“Nuru Kuu”
17. “Nuru kuu” yaangazaje katika Galilaya?
17 Hata hivyo, namna gani kuhusu mtajo wa Mathayo juu ya “nuru kubwa” katika Galilaya? Huo pia ulinukuliwa katika unabii wa Isaya. Isaya aliandika: “Watu wale waliokwenda katika giza wameona nuru kuu; wale waliokaa katika nchi ya uvuli wa mauti, nuru imewaangaza.” (Isaya 9:2) Kufikia karne ya kwanza W.K., nuru ya ile kweli ilikuwa imefichwa na mambo ya kipagani yasiyo ya kweli. Wayahudi waliokuwa viongozi wa kidini walikuwa wamelizidisha tatizo hilo kwa kushikilia mapokeo yao ya kidini ‘yaliyolibatilisha neno la Mungu.’ (Mathayo 15:6) Wanyenyekevu walionewa na kutatanishwa, huku wakifuata “viongozi vipofu.” (Mathayo 23:2-4, 16) Yesu Mesiya alipokuja, macho ya watu wengi wanyenyekevu yalifunguliwa kiajabu. (Yohana 1:9, 12) Kazi ya Yesu akiwa duniani na baraka zilizotokana na dhabihu yake zafananishwa ipasavyo na “nuru kuu” katika unabii wa Isaya.—Yohana 8:12.
18, 19. Kwa nini wale walioitikia nuru walikuwa na shangwe kuu?
18 Wale walioitikia nuru hiyo walikuwa na sababu nyingi za kufurahi. Isaya aliendelea: “Umeliongeza taifa, umezidisha furaha yao; Wanafurahi mbele zako, kama furaha ya wakati wa mavuno, kama watu wafurahivyo wagawanyapo nyara.” (Isaya 9:3) Kuhubiri kwa Yesu na kule kwa wafuasi wake kulitokeza wenye moyo wa haki, walioonyesha hamu ya kumwabudu Yehova kwa roho na kweli. (Yohana 4:24) Katika muda unaopungua miaka minne, umati ulikubali Ukristo. Elfu tatu walibatizwa katika siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K. Muda mfupi baadaye, “idadi ya wanaume ikawa karibu elfu tano.” (Matendo 2:41; 4:4) Wanafunzi walipozidi kudhihirisha nuru kwa bidii, “idadi ya wanafunzi ikafuliza kuzidi sana katika Yerusalemu; na umati mkubwa wa makuhani ukaanza kuwa mtiifu kwa imani.”—Matendo 6:7.
19 Sawa na wale wanaoshangilia kupata mavuno mengi au wanaofurahia kugawanya nyara yenye thamani baada ya ushindi mkubwa wa kijeshi, wafuasi wa Yesu walishangilia kwa sababu ya ongezeko. (Matendo 2:46, 47) Baadaye, Yehova aliifanya nuru ing’ae katika mataifa. (Matendo 14:27) Kwa hiyo watu wa jamii mbalimbali wakashangilia kwa sababu njia ya kumkaribia Yehova ilikuwa imefunguliwa kwao.—Matendo 13:48.
“Kama Katika Siku ya Midiani”
20. (a) Wamidiani walithibitikaje kuwa adui za Israeli, na Yehova alikomeshaje tisho lao? (b) Yesu atakomeshaje tisho la adui za watu wa Mungu “katika siku ya Midiani” ya wakati ujao?
20 Matokeo ya utendaji wa Mesiya ni ya kudumu, kama tuonavyo katika maneno yafuatayo ya Isaya: “Umeivunja nira ya mzigo wake, na gongo la bega lake, na fimbo yake yeye aliyemwonea, kama katika siku ya Midiani.” (Isaya 9:4) Karne kadhaa kabla ya siku ya Isaya, Wamidiani walipanga njama na Wamoabi ili kushawishi Israeli watende dhambi. (Hesabu 25:1-9, 14-18; 31:15, 16) Baadaye, Wamidiani waliwatisha Waisraeli kwa kuvamia na kupora vijiji na mashamba yao kwa miaka saba. (Waamuzi 6:1-6) Ndipo Yehova, kupitia Gideoni mtumishi wake, akayashinda kabisa majeshi ya Midiani. Baada ya “siku [hiyo] ya Midiani,” hakuna uthibitisho uonyeshao kuwa watu wa Yehova waliteseka tena mikononi mwa Wamidiani. (Waamuzi 6:7-16; 8:28) Katika wakati ujao ulio karibu, Yesu Kristo, Gideoni mkuu, atawatwanga na kuwaua adui za watu wa Yehova leo. (Ufunuo 17:14; 19:11-21) Kisha, “kama katika siku ya Midiani,” ushindi kamili na udumuo milele utapatikana kwa nguvu za Yehova, wala si kwa uwezo wa binadamu. (Waamuzi 7:2-22) Watu wa Mungu hawatateseka tena kamwe chini ya nira ya uonevu!
21. Unabii wa Isaya waonyesha nini juu ya wakati ujao wa vita?
21 Wonyesho wa nguvu za Mungu si utukuzaji wa vita. Yesu aliyefufuliwa ndiye Mkuu wa Amani, naye ataleta amani ya milele kwa kuwaharibu adui zake. Isaya sasa asema juu ya zana za kijeshi kuharibiwa kabisa kwa moto: “Silaha zote za mtu mwenye silaha wakati wa mshindo [“kila buti ya akanyagaye kwa mtetemo,” “NW”], na mavazi yaliyofingirishwa katika damu, yatakuwa tayari kuteketezwa, yatakuwa kuni za kutiwa motoni.” (Isaya 9:5) Mitetemo inayosababishwa na kukanyaga kwa buti za wanajeshi walio mwendoni haitasikika tena kamwe. Yunifomu zenye damu za askari waliozoea vita hazitaonekana tena. Vita havitakuwapo tena kamwe!—Zaburi 46:9.
“Mshauri wa Ajabu”
22. Katika kitabu cha Isaya, Yesu apewa jina gani la unabii lenye maana nyingi?
22 Wakati wa kuzaliwa kwake kimwujiza, yeye aliyezaliwa ili awe Mesiya alipewa jina Yesu, limaanishalo “Yehova Ni Wokovu.” Lakini anayo majina mengine pia, majina ya unabii yanayoonyesha jukumu lake muhimu na cheo chake cha juu. Jina moja kati ya hayo ni Imanueli, limaanishalo “Pamoja Nasi Yuko Mungu.” (Isaya 7:14; linganisha Mathayo 1:23.) Isaya sasa afafanua jina jingine la unabii: “Kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, tumepewa mtoto mwanamume; na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; naye ataitwa jina lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme [“Mkuu,” “NW”] wa amani.” (Isaya 9:6) Fikiria maana kamili ya jina hilo la unabii lenye sehemu nyingi.
23, 24. (a) Yesu ni “Mshauri wa ajabu” kwa njia gani? (b) Washauri Wakristo leo waweza kuigaje kielelezo cha Yesu?
23 Mshauri ni mtu anayetoa shauri. Yesu Kristo alitoa mashauri ya ajabu alipokuwa duniani. Twasoma katika Biblia kuwa “umati ulishangaa juu ya njia yake ya kufundisha.” (Mathayo 7:28) Yeye ni Mshauri mwenye hekima na hisia-mwenzi, anayeelewa hali ya binadamu kwa njia ya pekee. Shauri lake si la kukemea na kutia adabu tu. Mara nyingi, hilo hutolewa kwa namna ya mafundisho na shauri lenye upendo. Shauri la Yesu ni la ajabu kwa sababu sikuzote lina hekima, ni kamilifu, nalo halina makosa. Lifuatwapo, huongoza kwenye uhai udumuo milele.—Yohana 6:68.
24 Shauri la Yesu halitokani tu na akili zake nyingi. Badala yake, asema: “Kile nifundishacho si changu, bali ni chake yeye aliyenituma.” (Yohana 7:16) Kama ilivyokuwa kwa habari ya Solomoni, Yehova Mungu ndiye Chanzo cha hekima ya Yesu. (1 Wafalme 3:7-14; Mathayo 12:42) Kielelezo cha Yesu chapasa kuwachochea walimu na washauri katika kutaniko la Kikristo kutegemeza mafundisho yao kwa Neno la Mungu sikuzote.—Mithali 21:30.
“Mungu Mwenye Nguvu” na “Baba wa Milele”
25. Jina “Mungu mwenye nguvu” latufahamisha nini juu ya Yesu wa mbinguni?
25 Yesu pia ni “Mungu mwenye nguvu” na “Baba wa milele.” Haimaanishi kuwa ananyakua mamlaka na cheo cha Yehova, aliye “Mungu Baba yetu.” (2 Wakorintho 1:2) Yesu “hakufikiria upokonyaji, yaani, kwamba yeye awe sawa na Mungu.” (Wafilipi 2:6) Yeye anaitwa Mungu Mwenye Nguvu, wala si Mungu Mweza Yote. Yesu hakujifanya kamwe kuwa Mungu Mweza Yote, kwa maana alisema kuhusu Baba yake kuwa “Mungu pekee wa kweli,” yaani, Mungu pekee apaswaye kuabudiwa. (Yohana 17:3; Ufunuo 4:11) Katika Maandiko, neno “mungu” laweza kumaanisha “mwenye uweza” au “mwenye nguvu.” (Kutoka 12:12; Zaburi 8:5; 2 Wakorintho 4:4) Kabla hajaja duniani, Yesu alikuwa “mungu,” “akiwako katika umbo la Mungu.” Baada ya ufufuo wake, alirudi kwenye cheo cha juu hata zaidi huko mbinguni. (Yohana 1:1; Wafilipi 2:6-11) Isitoshe, jina “mungu” lina maana nyingine zaidi. Waamuzi katika Israeli waliitwa “miungu”—wakati mmoja Yesu mwenyewe aliwaita hivyo. (Zaburi 82:6; Yohana 10:35) Yehova amemteua Yesu kuwa Hakimu, ambaye “akusudiwa kuhukumu walio hai na wafu.” (2 Timotheo 4:1; Yohana 5:30) Kwa wazi, yeye aitwa ipasavyo Mungu Mwenye Nguvu.
26. Kwa nini Yesu aweza kuitwa “Baba wa milele”?
26 Jina la cheo “Baba wa milele” larejezea nguvu na mamlaka ya Mfalme wa Kimesiya ya kuwapa binadamu tazamio la uhai wa milele duniani. (Yohana 11:25, 26) Urithi wa mzazi wetu wa kwanza, Adamu, ulikuwa kifo. Yesu, Adamu wa mwisho, “akawa roho ipayo uhai.” (1 Wakorintho 15:22, 45; Waroma 5:12, 18) Kama vile Yesu, Baba wa Milele, atakavyoishi milele, ndivyo wanadamu watiifu watakavyofurahia milele manufaa ya ubaba wake.—Waroma 6:9.
‘Mkuu wa Amani’
27, 28. Raia za ‘Mkuu wa amani’ wanapata manufaa gani za ajabu wakati huu na hata wakati ujao pia?
27 Mbali na uhai udumuo milele, mwanadamu pia huhitaji amani, pamoja na Mungu na vilevile pamoja na mwanadamu mwenzake. Hata leo, wale wanaojitiisha kwa utawala wa ‘Mkuu wa amani’ ‘wamefua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu.’ (Isaya 2:2-4) Wao hawaweki chuki kwa sababu ya tofauti za kisiasa, kijamii, kiuchumi, au za maeneo. Wameungana katika ibada ya Mungu mmoja wa kweli, Yehova, nao hujitahidi kudumisha uhusiano wa amani pamoja na jirani zao, ndani na vilevile nje ya kutaniko.—Wagalatia 6:10; Waefeso 4:2, 3; 2 Timotheo 2:24.
28 Kwa wakati wa Mungu uliowekwa, Kristo ataleta amani thabiti, yenye kudumu na kuenea kotekote duniani. (Matendo 1:7) “Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe, katika kiti cha enzi cha Daudi na ufalme wake; kuuthibitisha na kuutegemeza kwa hukumu na kwa haki, tangu sasa na hata milele.” (Isaya 9:7a) Yesu hatatumia njia za kimabavu ili kudhihirisha mamlaka yake akiwa Mkuu wa Amani. Raia zake hawatanyang’anywa hiari yao na kukandamizwa. Badala yake, yote atakayotekeleza yatakuwa “kwa hukumu na kwa haki.” Ni badiliko lenye kuburudisha kama nini!
29. Twapaswa kufanya nini iwapo twataka kufurahia baraka ya amani idumuyo milele?
29 Kwa kuzingatia maana ya ajabu ya jina la Yesu la unabii, umalizio wa Isaya kwa sehemu hii ya unabii wake unasisimua kwelikweli. Aandika: “Wivu [“Bidii,” “NW”] wa BWANA wa majeshi ndio utakaotenda hayo.” (Isaya 9:7b) Naam, Yehova hutenda kwa bidii. Hafanyi jambo lolote shingo upande. Twaweza kuwa na hakika ya kwamba lolote aahidilo, atalitimiza kikamili. Iwapo yeyote atamani kufurahia amani idumuyo milele, basi na amtumikie Yehova kwa moyo wote. Sawa na Yehova Mungu na Yesu, Mkuu wa Amani, watumishi wote wa Mungu na wawe “wenye bidii kwa kazi zilizo bora.”—Tito 2:14.
-
-
Ahadi ya Mkuu wa AmaniUnabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
c Wengine wamedokeza kuwa labda wakazi wa yale majiji 20 ya Galilaya ambayo Mfalme Solomoni alimpa Hiramu mfalme wa Tiro hawakuwa Waisraeli.—1 Wafalme 9:10-13.
-
-
Ahadi ya Mkuu wa AmaniUnabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
[Picha katika ukurasa wa 127]
Yesu alikuwa nuru nchini
-
-
Ole Wao Waasi!Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
Sura ya 11
Ole Wao Waasi!
1. Yeroboamu alifanya kosa gani kubwa?
WATU wa Yehova wa agano walipogawanyika na kuwa falme mbili, ufalme wa kaskazini wa makabila kumi ukawa chini ya utawala wa Yeroboamu. Mfalme huyo mpya alikuwa mtawala mwenye uweza na nguvu. Lakini hakuwa na imani kamili katika Yehova. Kwa sababu hiyo alifanya kosa kubwa lililoathiri vibaya historia yote ya ufalme wa kaskazini. Sheria ya Kimusa iliwaamuru Waisraeli wafunge safari mara tatu kwa mwaka ya kwenda hekaluni huko Yerusalemu, jiji ambalo sasa lilikuwa katika ufalme wa kusini wa Yuda. (Kumbukumbu la Torati 16:16) Akihofia kuwa safari hizo za kawaida zingewafanya raia zake wafikirie kuhusu kuungana tena na ndugu zao wa kusini, Yeroboamu “a[li]fanyiza ng’ombe wawili wa dhahabu, akawaambia watu, Ni vigumu kwenu kupanda kwenda Yerusalemu; tazama, hii ndiyo miungu yenu, enyi Israeli, iliyowapandisha kutoka nchi ya Misri. Akamweka mmoja katika Betheli, na wa pili akamweka katika Dani.”—1 Wafalme 12:28, 29.
2, 3. Kosa la Yeroboamu liliathirije Israeli?
2 Kwa muda fulani, ilionekana kwamba mpango wa Yeroboamu umefanikiwa. Hatua kwa hatua watu wakaacha kwenda Yerusalemu nao wakaanza kuabudu mbele ya ng’ombe hao wawili. (1 Wafalme 12:30) Hata hivyo, zoea hilo la kidini la uasi lilifisidi ufalme wa kaskazini wa makabila kumi. Miaka iliyofuata, hata Yehu, aliyekuwa amefanya bidii yenye kustahili pongezi ya kuondolea mbali ibada ya Baali katika Israeli, aliendelea kuinamia ndama hao wa dhahabu. (2 Wafalme 10:28, 29) Uamuzi mbaya sana wa Yeroboamu ulisababisha mambo gani mengine? Misukosuko ya kisiasa na watu kuteseka.
3 Kwa sababu ya uasi wa Yeroboamu, Yehova alisema kuwa uzao wake haungetawala katika nchi hiyo, na mwishowe msiba mbaya sana ungeukumba ufalme wa kaskazini. (1 Wafalme 14:14, 15) Neno la Yehova likatimia kweli. Wafalme saba kati ya wafalme wa Israeli walitawala kwa miaka miwili au kwa muda usiozidi huo—baadhi yao kwa siku chache tu. Mfalme mmoja alijiua, na sita wakauawa na watu wenye tamaa ya makuu walionyakua kiti cha ufalme. Hasa baada ya utawala wa Yeroboamu wa Pili, uliokwisha karibu mwaka wa 804 K.W.K. huku Uzia akitawala katika Yuda, Israeli ilikumbwa na ghasia, jeuri, na mauaji. Kwa sababu ya hali hizo, Yehova apeleka onyo, au “neno,” la moja kwa moja kupitia Isaya kwa ufalme wa kaskazini. “Bwana alimpelekea Yakobo neno, likamfikilia Israeli.”—Isaya 9:8.a
Kiburi na Kujisifu Hutokeza Hasira ya Kisasi ya Mungu
4. Yehova apeleka “neno” gani dhidi ya Israeli, na kwa nini?
4 “Neno” la Yehova halitapuuzwa. “Watu wote watajua, yaani, Efraimu na yeye akaaye Samaria, wasemao kwa kiburi na kwa kujisifu nafsi zao.” (Isaya 9:9) “Yakobo,” “Israeli,” “Efraimu,” na “Samaria” yote hurejezea ufalme wa kaskazini wa Israeli, ambapo Efraimu ndilo kabila kubwa na Samaria ni jiji kuu. Neno la Yehova dhidi ya ufalme huo ni taarifa kali ya hukumu, kwa kuwa Efraimu imekuwa kaidi katika uasi nayo imeshupaa katika kujisifu mbele za Yehova. Mungu hatawalinda watu hao wasipate matokeo ya njia zao mbovu. Watalazimika kusikia, au kuzingatia, neno la Mungu.—Wagalatia 6:7.
5. Waisraeli wakosaje kuathiriwa na hukumu za Yehova?
5 Hali ziendeleapo kuwa mbaya, watu wapata hasara kubwa, kutia ndani nyumba zao—ambazo kwa kawaida hujengwa kwa matofali ya udongo na mbao zisizo ghali. Je, hali hiyo yafanya mioyo yao inyenyekee? Je, watatii manabii wa Yehova na kumrudia Mungu wa kweli?b Isaya arekodi jibu la watu hao wenye kujisifu: “Matofali yameanguka, lakini sisi tutajenga kwa mawe yaliyochongwa; mikuyu imekatwa lakini sisi tutaweka mierezi badala yake.” (Isaya 9:10) Waisraeli wamkaidi Yehova na kuwakataa manabii wake, wanaowaeleza sababu ya kupatwa na magumu hayo. Ni kana kwamba watu hao wanasema: ‘Huenda tukapoteza nyumba zilizojengwa kwa matofali ya udongo ziharibikazo upesi na mbao zisizo ghali, ila tutalipia hasara hiyo kwa kujenga upya kwa vifaa bora—mawe yaliyochongwa na mierezi!’ (Linganisha Ayubu 4:19.) Yehova hana jingine ila kuzidi kuwatia nidhamu.—Linganisha Isaya 48:22.
6. Yehova adhoofishaje mbinu za mwungano wa Siria na Israeli dhidi ya Yuda?
6 Isaya aendelea: “BWANA atawainua adui wa Resini juu yake.” (Isaya 9:11a) Mfalme Peka wa Israeli na Mfalme Resini wa Siria wameungana. Wanapanga njama ya kuvamia ufalme wa Yuda wa makabila mawili na kumtawaza mfalme fulani kibaraka—“mwana wa Tabeeli”—kwenye kiti cha ufalme cha Yehova katika Yerusalemu. (Isaya 7:6) Lakini njama hiyo itaambulia patupu. Resini anao adui wenye nguvu, na Yehova “atawainua” adui hao dhidi “yake,” Israeli. Neno “atawainua” lamaanisha kuwaruhusu wapige vita vya ushindi vitakavyoharibu mwungano huo na malengo yake.
7, 8. Ushindi wa Ashuru dhidi ya Siria una matokeo gani kwa Israeli?
7 Kuvunjika kwa mwungano huo kwaanza Ashuru ishambuliapo Siria. “Mfalme wa Ashuru akapanda juu ya Dameski [jiji kuu la Siria], akautwaa, akawahamisha watu wake mateka mpaka Kiri, akamwua Resini.” (2 Wafalme 16:9) Baada ya kupoteza mshirika wake mwenye nguvu, Peka atambua kwamba mbinu zake dhidi ya Yuda zimekomeshwa. Kwa hakika, muda mfupi baada ya kifo cha Resini, Hoshea amwua Peka, na kunyakua kiti cha ufalme huko Samaria.—2 Wafalme 15:23-25, 30.
8 Siria, mshirika wa awali wa Israeli, sasa ni kibaraka wa Ashuru, utawala wenye nguvu zaidi katika eneo hilo. Isaya atabiri kuhusu namna Yehova atakavyoutumia mwungano huo mpya wa kisiasa: “[Yehova] atawachochea adui zake [Israeli]; Waashuri [“Wasiria,” “NW”] upande wa mbele, na Wafilisti upande wa nyuma, nao watamla Israeli kwa kinywa kilicho wazi. Pamoja na hayo yote hasira yake haikugeukia mbali, lakini mkono wake umenyoshwa hata sasa.” (Isaya 9:11b, 12) Naam, Siria sasa ni adui ya Israeli, lazima Israeli ijitayarishe kushambuliwa na Ashuru na Siria. Uvamizi huo wafanikiwa. Ashuru yamfanya Hoshea mnyakuzi kuwa mtumishi wake, na kutoza ushuru mkubwa mno. (Makumi kadhaa ya miaka mapema, Ashuru ilipokea kiasi kikubwa cha ushuru kutoka kwa Mfalme Menahemu wa Israeli.) Maneno ya nabii Hosea ni barabara kabisa: “Wageni wamekula nguvu zake [za Efraimu]”!—Hosea 7:9; 2 Wafalme 15:19, 20; 17:1-3.
9. Kwa nini twaweza kusema kuwa Wafilisti washambulia “upande wa nyuma”?
9 Je, Isaya hasemi pia kwamba Wafilisti watavamia “upande wa nyuma”? Ndiyo. Kabla ya siku za dira zenye kutegemea uvutano wa sumaku, Waebrania waliashiria upande kwa kutegemea macheo ya jua. Kwa hiyo, “upande wa mbele” ulikuwa mashariki, ilhali magharibi, makao ya pwani ya Wafilisti, ilikuwa “upande wa nyuma.” Kwa habari hii, huenda “Israeli” inayotajwa katika Isaya 9:12 ikatia ndani Yuda kwa sababu Wafilisti walivamia Yuda wakati wa utawala wa Ahazi, aliyetawala siku za Peka, na kutwaa majiji na ngome kadhaa za Yudea na kuzifanya makazi yao. Sawa na Efraimu iliyo kaskazini, Yuda yastahili nidhamu hiyo kutoka kwa Yehova, kwa sababu Yuda pia imejaa uasi.—2 Mambo ya Nyakati 28:1-4, 18, 19.
Toka ‘Kichwa Hata Mkia’—Taifa la Waasi
10, 11. Yehova ataleta adhabu gani dhidi ya Israeli kwa sababu ya uasi wao wenye kuendelea?
10 Licha ya mateso yake yote—na licha ya matangazo makali ya manabii wa Yehova—ufalme wa kaskazini waendelea kuasi dhidi ya Yehova. “Watu hao hawakumwelekea yeye aliyewapiga, wala kumtafuta BWANA [“Yehova,” “NW”] wa majeshi.” (Isaya 9:13) Basi, nabii huyo asema: “BWANA atakata katika Israeli kichwa na mkia, kuti na nyasi, katika siku moja. Mzee mwenye kuheshimiwa ndiye kichwa, na nabii afundishaye uongo ndiye mkia. Kwa maana wawaongozao watu hawa ndio wawakoseshao, na hao walioongozwa na watu hao wameangamia.”—Isaya 9:14-16.
11 “Kichwa” na “kuti” zawakilisha “mzee mwenye kuheshimiwa”—viongozi wa taifa. “Mkia” na “nyasi” zarejezea manabii wa uwongo wanaotamka maneno yawapendezayo viongozi wao. Msomi mmoja wa Biblia aandika: “Manabii wasio wa kweli waitwa mkia, kwa maana walikuwa watu wenye utovu mkubwa zaidi wa kiadili, na kwa maana walikuwa wafuasi vibaraka na waungaji mkono wa watawala waovu.” Profesa Edward J. Young asema hivi kuhusu manabii hao wasio wa kweli: “Hawakuwa viongozi hata kidogo bali walifuata tu waendako viongozi na kusifu-sifu na kujipendekeza, kama mkia wa mbwa unaotikiswa-tikiswa.”—Linganisha 2 Timotheo 4:3.
Hata ‘Wajane na Mayatima’ Ni Waasi
12. Ufisadi umepenya kadiri gani katika jamii ya Israeli?
12 Yehova ndiye Mtetezi wa wajane na mayatima. (Kutoka 22:22, 23) Ijapokuwa hivyo, sikia asemayo Isaya sasa: “Bwana hatawafurahia vijana wao, wala hatawahurumia yatima zao wala wajane wao; maana kila mtu ni mnajisi, dhalimu, na kila ulimi hunena upumbavu. Pamoja na hayo yote hasira yake haikugeukia mbali, lakini mkono wake umenyoshwa hata sasa.” (Isaya 9:17) Uasi umefisidi tabaka zote za jamii, kutia ndani wajane na mayatima! Yehova awatuma manabii wake kwa saburi, akitumaini kuwa watu hao watabadili njia zao. Kwa kielelezo, “Ee Israeli, mrudie BWANA, Mungu wako; maana umeanguka kwa sababu ya uovu wako,” asihi Hosea. (Hosea 14:1) Hapana budi Mtetezi wa wajane na mayatima ahuzunika sana kwa kulazimika kutekeleza hukumu dhidi yao pia!
13. Twaweza kujifunza nini kutokana na ile hali katika siku ya Isaya?
13 Sawa na Isaya, twaishi katika nyakati za hatari kabla ya siku ya hukumu ya Yehova dhidi ya waovu. (2 Timotheo 3:1-5) Basi, ni muhimu kwa Wakristo wa kweli, haidhuru hali yao maishani, wadumu wakiwa safi kiroho, kiadili, na kiakili ili waendelee kupata upendeleo wa Mungu. Kila mmoja na alinde kwa bidii uhusiano wake na Yehova. Yeyote aliyeponyoka kutoka katika “Babiloni Mkubwa” na ‘asishiriki pamoja naye dhambi zake’ tena.—Ufunuo 18:2, 4.
Ibada Isiyo ya Kweli Hutokeza Jeuri
14, 15. (a) Ibada ya roho waovu huleta nini? (b) Isaya atabiri kwamba Israeli itapata mateso gani yanayoendelea?
14 Ibada isiyo ya kweli kwa hakika ni kuabudu roho waovu. (1 Wakorintho 10:20) Kama ilivyodhihirika kabla ya Furiko, uvutano wa roho waovu husababisha jeuri. (Mwanzo 6:11, 12) Basi, haishangazi kwamba Israeli inapoasi na kuanza kuabudu roho waovu, jeuri na uovu wajaa nchini.—Kumbukumbu la Torati 32:17; Zaburi 106:35-38.
15 Kwa maneno yenye nguvu, Isaya afafanua kuenea kwa uovu na jeuri katika Israeli: “Uovu huteketeza kama moto; huila mibigili na miiba, naam, huwaka katika vichaka vya mwitu, nao hupaa juu katika mawingu mazito ya moshi. Kwa sababu ya hasira ya BWANA wa majeshi nchi hii inateketea kabisa; watu hawa nao ni kama kuni zitiwazo motoni; hapana mtu amhurumiaye ndugu yake. Hupokonya upande wa mkono wa kuume, nao huona njaa! hula upande wa mkono wa kushoto, wala hawashibi! watakula kila mtu nyama ya mkono wake mwenyewe. Manase anamla Efraimu, naye Efraimu anamla Manase; nao wawili pamoja watakuwa juu ya Yuda. Pamoja na hayo yote hasira yake haikugeukia mbali, lakini mkono wake umenyoshwa hata sasa.”—Isaya 9:18-21.
16. Maneno ya Isaya 9:18-21 yatimizwaje?
16 Kama moto usambaao kichaka kwa kichaka, jeuri yasambaa haraka isiweze kudhibitiwa nayo upesi yavifikia “vichaka vya mwitu,” ikisababisha moto mkubwa wa mwituni wa jeuri. Waelezaji wa Biblia Keil na Delitzsch wasema kwamba kiwango cha jeuri ni cha “kujiangamiza kikatili sana wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe vyenye vurugu. Huku wakiwa hawana hisia zozote, walinyafuana pasipo kuridhika.” Labda makabila ya Efraimu na Manase yatajwa hapa kwa sababu hayo ndiyo wawakilishi wakuu wa ufalme wa kaskazini na, wakiwa wazao wa wana wawili wa Yosefu, ndio wenye udugu wa karibu zaidi kati ya yale makabila kumi. Hata hivyo, licha ya hayo, hawakomeshi jeuri yao ya kuuana ndugu kwa ndugu ila tu wapiganapo vita na Yuda iliyo kusini.—2 Mambo ya Nyakati 28:1-8.
-
-
Ole Wao Waasi!Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
a Isaya 9:8–10:4 ina beti nne (mafungu ya shairi), kila mmoja ukimalizika kwa kibwagizo chenye kutisha: “Pamoja na hayo yote hasira yake haikugeukia mbali, lakini mkono wake umenyoshwa hata sasa.” (Isaya 9:12, 17, 21; 10:4) Mtindo huo wa kifasihi huunganisha Isaya 9:8–10:4 kuwa “neno” moja kuu. (Isaya 9:8) Pia ona kwamba “mkono [wa Yehova] umenyoshwa hata sasa,” si kwa ajili ya kuleta upatanisho, bali kuhukumu.—Isaya 9:13.
b Manabii wa Yehova waliotumwa kwa ufalme wa kaskazini wa Israeli ni pamoja na Yehu (siye yule mfalme), Eliya, Mikaya, Elisha, Yona, Odedi, Hosea, Amosi, na Mika.
-