-
Mkono wa Yehova WainuliwaUnabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
Wimbo wa Wokovu
13, 14. Watu wa Mungu leo wana ‘mji gani ulio na nguvu,’ na ni nani wanaoruhusiwa kuingia humo?
13 Namna gani watu wa Mungu? Huku wakifurahia kupata upendeleo na ulinzi wa Yehova, wapaza sauti zao kwa wimbo. “Siku ile wimbo huu utaimbwa katika nchi ya Yuda; Sisi tunao mji ulio na nguvu; ataamuru wokovu kuwa kuta na maboma. Wekeni wazi malango yake, taifa lenye haki, lishikalo kweli, liingie.” (Isaya 26:1, 2) Ingawa hapana shaka maneno hayo yalitimia kwa njia fulani nyakati za kale, hayo pia yatimizwa waziwazi leo. “Taifa lenye haki” la Yehova, Israeli wa kiroho, limeandaliwa tengenezo lenye nguvu, lifananalo na mji. Hiyo ni sababu iliyoje ya kushangilia na kuimba!
14 Ni watu wa aina gani wanaokuja katika “mji” huo? Wimbo huo wajibu: “[Mungu] utamlinda yeye ambaye moyo wake umekutegemea katika amani kamilifu, kwa kuwa anakutumaini. Mtumainini BWANA siku zote maana BWANA [“Yah” “NW”] YEHOVA ni mwamba wa milele.” (Isaya 26:3, 4) “Moyo” ambao Yehova autegemeza ni ile tamaa ya kutii kanuni zake zenye uadilifu na kumtumaini yeye, wala si kuitumaini mifumo ya ulimwengu ya kibiashara, kisiasa, na kidini inayotapatapa. “Yah Yehova” ndiye Mwamba pekee wa usalama unaotegemeka. Wale wanaomtumaini Yehova kwa ukamili hupata ulinzi wake na kufurahia “amani kamilifu.”—Mithali 3:5, 6; Wafilipi 4:6, 7.
15. ‘Mji ulioinuka’ umeshushwaje leo, na “miguu yao walio maskini” imeukanyagiaje chini?
15 Jambo hilo ni tofauti kama nini na mambo yanayowakumba adui za watu wa Mungu! “Amewashusha wakaao juu, mji ule ulioinuka, aushusha, aushusha hata nchi, auleta hata mavumbini. Mguu utaukanyaga chini, naam, miguu yao walio maskini, na hatua zao walio wahitaji.” (Isaya 26:5, 6) Mara nyingine tena, huenda hapo Isaya aurejezea “mji ule ulioinuka” katika Moabu, au labda anamaanisha mji mwingine tofauti, kama vile Babiloni, ambao bila shaka umeinuka katika kiburi. Vyovyote vile, Yehova ameushinda “mji ule ulioinuka,” na watu wake ‘walio maskini na wahitaji’ waukanyagia chini. Leo unabii huo wafaa kabisa Babiloni Mkubwa, hasa Jumuiya ya Wakristo. Mwaka wa 1919, ‘mji huo ulioinuka’ ulilazimika kuwaachilia watu wa Yehova—anguko lenye aibu—wao nao wamechukua hatua ya kumkanyagia chini mtekaji wao wa awali. (Ufunuo 14:8) Wamefanyaje hivyo? Kwa kutangaza hadharani kisasi cha Yehova kinachokuja juu yake.—Ufunuo 8:7-12; 9:14-19.
Kutamani Uadilifu na “Ukumbusho” wa Yehova
16. Isaya aweka kielelezo gani chema cha ujitoaji?
16 Baada ya wimbo huo wa ushindi, Isaya afunua kina cha ujitoaji wake mwenyewe na thawabu za kumtumikia Mungu mwenye uadilifu. (Soma Isaya 26:7-9.) Nabii huyo aweka kielelezo chema cha ‘kumngojea Yehova’ na cha kuwa na tamaa nyingi kwa ajili ya “jina” na “ukumbusho” wa Yehova. Ukumbusho wa Yehova ni nini? Andiko la Kutoka 3:15 lasema: “BWANA [“Yehova,” NW] . . . ndilo jina langu hata milele, nalo ni kumbukumbu langu [“ukumbusho wangu,” NW] hata vizazi vyote.” Isaya alipenda sana jina la Yehova na maana yake yote, kutia ndani viwango na njia Zake za uadilifu. Wale wanaositawisha upendo kama huo kwa Yehova wanahakikishiwa kupata baraka yake.—Zaburi 5:8; 25:4, 5; 135:13; Hosea 12:5.
17. Wabaya watanyimwa mapendeleo gani?
17 Hata hivyo, sio watu wote wanaompenda Yehova na viwango vyake bora. (Soma Isaya 26:10.) Wabaya, wajapoalikwa, hukataa kwa kichwa kigumu kujifunza uadilifu ili wapate kuingia katika “nchi ya unyofu,” nchi inayokaliwa na watumishi wa Yehova walio wanyofu kiadili na kiroho. Kwa hiyo, wabaya ‘hawatauona utukufu wa BWANA.’ Hawataishi ili wapate baraka zitakazowajia wanadamu baada ya kutukuzwa kwa jina la Yehova. Hata katika ulimwengu mpya, dunia yote itakapokuwa “nchi ya unyofu,” huenda watu fulani wakashindwa kuzikubali fadhili-upendo za Yehova. Majina ya watu hao hayataandikwa katika kitabu cha uhai.—Isaya 65:20; Ufunuo 20:12, 15.
18. Watu fulani katika siku ya Isaya wameamuaje kuwa vipofu, nao watalazimika ‘kumwona’ Yehova lini?
18 “BWANA, mkono wako umeinuliwa, lakini hawaoni; lakini watauona wivu wako kwa ajili ya watu wako, nao watatahayari; naam, moto utawala adui zako.” (Isaya 26:11) Katika siku ya Isaya, mkono wa Yehova umethibitika kuinuliwa Yehova awalindapo watu wake kwa kuchukua hatua dhidi ya adui zao. Lakini wengi hawajatambua hilo. Watu hao, ambao wameamua wenyewe kuwa vipofu kiroho, hatimaye watalazimika ‘kumwona,’ au kumkiri, Yehova, moto wa wivu wake uwachomapo. (Sefania 1:18) Baadaye Mungu amwambia Ezekieli: “Nao watajua ya kuwa mimi ndimi BWANA.”—Ezekieli 38:23.
“Ambaye Yehova Ampenda Humtia Nidhamu”
19, 20. Kwa nini Yehova amewatia watu wake nidhamu, naye amewatiaje nidhamu hiyo, na ni nani ambao wamenufaika kutokana nayo?
19 Isaya afahamu kwamba amani na ufanisi wowote ambao wananchi wenzake wafurahia hutokana na baraka ya Yehova. “BWANA, utatuamuria amani; maana ni wewe pia uliyetutendea kazi zetu zote.” (Isaya 26:12) Licha ya hayo na licha ya kwamba Yehova aliweka mbele ya watu wake fursa ya kuwa “ufalme wa makuhani, na taifa takatifu,” Yuda imekuwa na historia yenye mawaa. (Kutoka 19:6) Mara kwa mara, watu wake wamegeukia ibada ya miungu isiyo ya kweli. Kwa hiyo, wametiwa nidhamu mara nyingi. Hata hivyo, nidhamu hiyo ni uthibitisho wa upendo wa Yehova kwa maana mtu “ambaye Yehova ampenda humtia nidhamu.”—Waebrania 12:6.
20 Mara kwa mara, Yehova awatia watu wake nidhamu kwa kuyaruhusu mataifa mengine, “mabwana wengine,” wawatawale. (Soma Isaya 26:13.) Mwaka wa 607 K.W.K., awaruhusu Wababiloni wawapeleke uhamishoni. Je, hilo lawanufaisha? Mateso peke yake hayamfaidi mtu. Hata hivyo, iwapo mwenye kuteseka ajifunza kutokana na mateso hayo, atubu, na kumpa Yehova ujitoaji usiohusisha wengine, ndipo anaponufaika. (Kumbukumbu la Torati 4:25-31) Je, kuna Wayahudi wowote waonyeshao toba ya kimungu? Ndiyo! Isaya atabiri: “Kwa msaada wako peke yako tutalitaja jina lako.” Baada ya kurudi kutoka uhamishoni mwaka wa 537 K.W.K., mara nyingi Wayahudi wahitaji nidhamu kwa sababu ya dhambi nyinginezo, lakini hawanaswi tena katika mtego wa kuabudu miungu ya mawe.
21. Ni nini litakalowapata wale ambao wamewakandamiza watu wa Mungu?
21 Vipi juu ya watekaji wa Yuda? “Wamekufa, hawataishi; wamekwisha kufariki, hawatafufuka; kwa sababu hiyo umewajilia, na kuwaangamiza, na kuupoteza ukumbusho wao.” (Isaya 26:14) Babiloni litateseka kwa sababu ya ukatili wake juu ya taifa teule la Yehova. Kwa kutumia Wamedi na Waajemi, Yehova atalipindua Babiloni lenye kiburi na kuwaachilia huru watu Wake waliopelekwa uhamishoni. Jiji hilo kubwa, Babiloni, litafifia, kana kwamba limeuawa. Hatimaye, halitakuwapo kabisa.
22. Watu wa Mungu wamebarikiwaje leo?
22 Katika utimizo wa leo, mabaki ya Israeli wa kiroho waliotiwa nidhamu waliachiliwa huru kutoka Babiloni Mkubwa nao wakarudishwa kwenye utumishi wa Yehova mwaka wa 1919. Huku wakiwa wametiwa nguvu upya, Wakristo watiwa-mafuta walijitolea kwa bidii kutimiza kazi yao ya kuhubiri. (Mathayo 24:14) Yehova naye amewabariki kwa kuwapa ongezeko, hata akauleta umati mkubwa wa “kondoo wengine” watumikie pamoja nao. (Yohana 10:16) “Umeliongeza hilo taifa, BWANA, umeliongeza taifa; wewe umetukuzwa, umeipanua mipaka yote ya nchi hii. BWANA, katika taabu zao walikwenda kwako; waliomba maombi mengi wakati adhabu yako ilipokuwa juu yao.”—Isaya 26:15, 16.
‘Watafufuka’
23. (a) Kunatukia wonyesho gani mkubwa wa nguvu za Yehova mwaka wa 537 K.W.K.? (b) Kulitukia wonyesho gani kama huo mwaka wa 1919 W.K.?
23 Isaya airudia hali inayoikabili Yuda inapokuwa ingali utekwani huko Babiloni. Alilinganisha taifa hilo na mwanamke ambaye ana uchungu wa kuzaa ijapokuwa hawezi kuzaa pasipo msaada. (Soma Isaya 26:17, 18.) Msaada huo wapatikana mwaka wa 537 K.W.K., na watu wa Yehova warudi nchini kwao, wakiwa na hamu ya kujenga upya hekalu na kuirudisha ibada ya kweli. Ni kana kwamba taifa hilo lafufuliwa kutoka kwa wafu. “Wafu wako wataishi, maiti zangu zitafufuka; amkeni, kaimbeni, ninyi mnaokaa mavumbini, kwa maana umande wako ni kama umande wa mimea, nayo ardhi itawatoa waliokufa.” (Isaya 26:19) Huo ni wonyesho ulioje wa nguvu za Yehova! Isitoshe, ulikuwa wonyesho mkubwa kama nini maneno hayo yalipotimizwa kiroho mwaka wa 1919! (Ufunuo 11:7-11) Nasi twatazamia kama nini wakati maneno hayo yatakapotimizwa kihalisi katika ulimwengu mpya na wale waliokufa ‘watakapoisikia sauti ya Yesu na kutoka’ katika makaburi ya ukumbusho!—Yohana 5:28, 29.
24, 25. (a) Huenda Wayahudi walitiije amri ya Yehova ya kujificha katika mwaka wa 539 K.W.K.? (b) Huenda “vyumba” vikarejezea nini leo, na inatupasa tusitawishe mtazamo gani kuvielekea?
24 Hata hivyo, iwapo watu waaminifu wataka kufurahia baraka za kiroho zilizoahidiwa kupitia Isaya, ni sharti watii amri za Yehova: “Njoni, watu wangu, ingia wewe ndani ya vyumba vyako, ukafunge mlango nyuma yako ujifiche kitambo kidogo, mpaka ghadhabu hii itakapopita. Kwa maana, tazama, BWANA anakuja kutoka mahali pake, ili kuwaadhibu wakaao duniani, kwa sababu ya uovu wao; ardhi nayo itafunua damu yake, wala haitawafunika tena watu wake waliouawa.” (Isaya 26:20, 21; linganisha Sefania 1:14.) Huenda maneno hayo yakatimizwa mara ya kwanza wakati Wamedi na Waajemi, wakiongozwa na Mfalme Koreshi, washindapo Babiloni mwaka wa 539 K.W.K. Kwa mujibu wa mwanahistoria Mgiriki aitwaye Xenophon, Koreshi aingiapo Babiloni, aamuru kila mtu akae nyumbani kwake kwa sababu jeshi lake la wapanda-farasi “limeamriwa kumwua mtu yeyote watakayemkuta nje ya nyumba.” Leo, “vyumba” katika unabii huo huenda vikahusianishwa kwa ukaribu na makumi ya maelfu ya makutaniko ya watu wa Yehova ulimwenguni kote. Makutaniko hayo yataendelea kutimiza fungu muhimu maishani mwetu, hata wakati wa “dhiki kubwa.” (Ufunuo 7:14) Basi ni muhimu kama nini kwamba tuendelee kuwa na mtazamo unaofaa kuelekea kutaniko nasi tushirikiane nalo kwa ukawaida!—Waebrania 10:24, 25.
25 Mwisho wa ulimwengu wa Shetani utakuja hivi karibuni. Kwa sasa hatujui jinsi Yehova atakavyowalinda watu wake katika kipindi hicho chenye kuhofisha. (Sefania 2:3) Hata hivyo, tujuacho ni kwamba wokovu wetu utategemea imani, uaminifu-mshikamanifu na utii wetu kwa Yehova.
-
-
Mkono wa Yehova WainuliwaUnabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
[Picha katika ukurasa wa 278]
“Ingia wewe ndani ya vyumba vyako”
-