Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nyumba ya Yehova Yainuliwa Juu
    Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
    • Sura ya 4

      Nyumba ya Yehova Yainuliwa Juu

      Isaya 2:1-5

      1, 2. Ni maneno gani yameandikwa ukutani kwenye jengo la Umoja wa Mataifa, nayo yatoka wapi?

      “WATAFUA panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” Maneno hayo yameandikwa ukutani kwenye jengo la Umoja wa Mataifa huko New York City. Kwa makumi ya miaka, chanzo cha nukuu hilo hakikujulikana. Kwa kuwa lengo la UM ni kuleta amani duniani kote, ingeweza kuamuliwa kwa urahisi kuwa nukuu hilo lilibuniwa na waanzilishi wa UM, mwaka wa 1945.

      2 Hata hivyo, mwaka wa 1975, jina Isaya liliandikwa ukutani chini ya nukuu hilo. Ndipo ikawa dhahiri kuwa maneno hayo si ya juzijuzi. Kwa hakika, maneno hayo ni unabii uliorekodiwa zaidi ya miaka 2,700 iliyopita katika sura ya 2 ya kitabu cha Isaya. Kwa maelfu ya miaka, wapendao amani wametafakari juu ya wakati na jinsi ambavyo mambo yaliyotabiriwa na Isaya yangetukia. Hakuna haja ya kuhangaika tena. Leo twaona mbele yetu utimizo ulio wazi wa unabii huu wa kale.

      3. Mataifa wanaofua panga zao ziwe majembe ni nani?

      3 Mataifa yanayofua panga zao ziwe majembe ni nani? Kwa hakika hayo si mataifa na serikali za kisiasa za leo. Hadi sasa mataifa hayo yameunda panga, au silaha, za kupigana vita na vilevile za kulinda “amani” kwa nguvu. Kwa kawaida, sikuzote mataifa yamekuwa na mwelekeo wa kufua majembe yao yawe panga! Unabii wa Isaya hutimizwa na wawakilishi kutoka mataifa yote, watu wanaomwabudu Yehova, “Mungu wa amani.”—Wafilipi 4:9.

      Mataifa Yanayomiminika Kwenye Ibada Safi

      4, 5. Mistari ya kwanza ya Isaya sura ya 2 hutabiri nini, na ni nini kinachokazia kutegemeka kwa maneno hayo?

      4 Isaya sura ya 2 yaanza kwa maneno haya: “Hili ni neno aliloliona Isaya mwana wa Amozi katika habari za Yuda na Yerusalemu. Na itakuwa [“lazima itukie,” “NW”] katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya BWANA [“Yehova,” “NW”] utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote watauendea makundi makundi [“yatamiminika huko,” “BHN”].”—Isaya 2:1, 2.

      5 Ona kwamba Isaya hatabiri makisio tu. Isaya aagizwa arekodi mambo ambayo ni ‘lazima yatukie’—bila kushindwa. Lolote akusudialo Yehova lazima “litafanikiwa.” (Isaya 55:11) Yamkini ili kukazia kutegemeka kwa ahadi yake, Mungu alimpulizia nabii Mika, aliyeishi siku ya Isaya, arekodi katika kitabu chake unabii kama ule unaopatikana katika Isaya 2:2-4.—Mika 4:1-3.

      6. Unabii wa Isaya watimizwa lini?

      6 Unabii wa Isaya wapaswa kutimizwa lini? “Katika siku za mwisho.” Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yalitabiri mambo ambayo yangekitambulisha kipindi hicho. Baadhi ya mambo hayo ni vita, matetemeko ya dunia, magonjwa ya kuambukiza, upungufu wa chakula, na “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.”a (2 Timotheo 3:1-5; Luka 21:10, 11) Utimizo wa unabii mbalimbali kama huo hutoa uthibitisho mwingi unaoonyesha kuwa twaishi “katika siku za mwisho” za mfumo wa sasa wa ulimwengu. Kwa kufaa basi, tungetarajia kuona mambo aliyotabiri Isaya yakitimizwa wakati wetu.

      Mlima wa Kuabudia

      7. Isaya atoa mfano wa taswira gani ya unabii?

      7 Kwa maneno machache, Isaya atoa mfano wa taswira dhahiri ya unabii. Twaona mlima mrefu, ukiwa na nyumba tukufu kileleni, hekalu la Yehova. Mlima huo huinuka juu ya milima na vilima jirani. Ingawa hivyo, hauashirii mabaya wala hautishi; unavutia. Watu wa mataifa yote watamani sana kuupanda mlima wa nyumba ya Yehova; wanamiminika huko. Ni rahisi kuwazia mambo hayo, lakini yamaanisha nini?

      8. (a) Vilima na milima vyahusianishwa na nini katika siku ya Isaya? (b) Kumiminika kwa mataifa kwenye ‘nyumba ya Yehova’ hufananisha nini?

      8 Katika siku ya Isaya, mara nyingi vilima na milima vyahusianishwa na ibada. Kwa kielelezo, sehemu hizo zatumiwa kama mahali pa ibada ya sanamu na mahali patakatifu pa miungu isiyo ya kweli. (Kumbukumbu la Torati 12:2; Yeremia 3:6) Hata hivyo, nyumba, au hekalu, la Yehova lapamba kilele cha Mlima Moria jijini Yerusalemu. Waisraeli waaminifu wasafiri kwenda Yerusalemu mara tatu kwa mwaka nao wapanda Mlima Moria ili wamwabudu Mungu wa kweli. (Kumbukumbu la Torati 16:16) Kwa hiyo, kumiminika kwa mataifa kwenye ‘mlima wa nyumba ya Yehova’ hufananisha kukusanywa kwa vikundi vingi vya watu kwenye ibada ya kweli.

      9. ‘Mlima wa nyumba ya Yehova’ huwakilisha nini?

      9 Leo, pasipo shaka, watu wa Mungu hawakusanyiki katika mlima halisi wenye hekalu la mawe. Hekalu la Yehova huko Yerusalemu liliharibiwa na majeshi ya Waroma mwaka wa 70 W.K. Mbali na hayo, mtume Paulo alionyesha waziwazi kuwa hekalu huko Yerusalemu na tabenakulo iliyolitangulia vilikuwa vya ufananisho. Viliwakilisha uhalisi mkubwa zaidi, wa kiroho, “hema la kweli, ambalo Yehova alisimamisha, wala si mwanadamu.” (Waebrania 8:2) Hema hilo la kiroho ni mpango wa kumwendea Yehova katika ibada kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. (Waebrania 9:2-10, 23) Kupatana na hilo, ‘mlima wa nyumba ya Yehova’ unaotajwa katika Isaya 2:2 wawakilisha ibada safi iliyokwezwa ya Yehova katika wakati wetu. Wanaoikubali ibada ya kweli hawakusanyiki mahali popote halisi; wao hukusanyika katika umoja wa ibada.

      Kuinuliwa kwa Ibada Safi

      10, 11. Ibada ya Yehova imeinuliwaje katika siku yetu?

      10 Nabii huyo asema kuwa ‘mlima wa nyumba ya Yehova,’ au ibada safi, “u[nge]wekwa imara juu ya milima” nao “u[nge]inuliwa juu ya vilima.” Muda mrefu kabla ya wakati wa Isaya, Mfalme Daudi alipandisha sanduku la agano juu ya Mlima Moria huko Yerusalemu, jiji lililokuwa meta 760 juu ya usawa wa bahari. Sanduku hilo lilidumu hapo hadi lilipohamishwa kupelekwa katika hekalu lililomalizika kwenye Mlima Moria. (2 Samweli 5:7; 6:14-19; 2 Mambo ya Nyakati 3:1; 5:1-10) Basi, kufikia siku ya Isaya, sanduku takatifu lilikuwa tayari limeinuliwa kihalisi na kuwekwa katika hekalu, mahali palipo juu zaidi kuliko vilima jirani vilivyotumiwa kwa ajili ya ibada isiyo ya kweli.

      11 Hapana shaka kwamba sikuzote ibada ya Yehova, katika maana ya kiroho, imekuwa kuu kuliko mazoea ya kidini ya wale wanaotumikia miungu isiyo ya kweli. Hata hivyo, katika siku yetu, Yehova ameiinua ibada yake juu hadi mbinguni, juu kuliko namna zote za ibada isiyo safi, naam, juu zaidi kuliko “vilima” vyote na “juu ya milima.” Jinsi gani? Hasa kupitia kukusanywa pamoja kwa wale wanaotaka kumwabudu “kwa roho na kweli.”—Yohana 4:23.

      12. “Wana wa ufalme” ni nani, na kumekuwa na ukusanyaji gani?

      12 Kristo Yesu alirejezea “umalizio wa mfumo wa mambo” kuwa wakati wa mavuno ambapo malaika wangekusanya “wana wa ufalme”—wale wanaotumaini kutawala na Yesu katika utukufu wa mbinguni. (Mathayo 13:36-43) Tangu mwaka wa 1919, Yehova amewawezesha “waliobaki” kati ya wana hao washirikiane na malaika katika kazi ya kuvuna. (Ufunuo 12:17) Basi, mwanzoni kabisa, “wana wa ufalme,” ndugu za Yesu watiwa-mafuta, ndio hukusanywa. Kisha wao nao hushiriki katika kazi zaidi ya kukusanya.

      13. Yehova amewabarikije mabaki watiwa-mafuta?

      13 Wakati huu wa mavuno, Yehova amewasaidia hatua kwa hatua mabaki watiwa-mafuta walielewe na kulitumia Neno lake, Biblia. Hatua hiyo pia imechangia kuinuliwa kwa ibada safi. Ingawa ‘giza linaifunika dunia, na giza kuu linazifunika kabila za watu,’ watiwa-mafuta ‘wanang’aa wakiwa wamulikaji’ kati ya wanadamu, Yehova akiwa amewasafisha na kuwatakasa. (Isaya 60:2; Wafilipi 2:15) Wakiwa “[wame]jazwa ujuzi sahihi wa mapenzi yake katika hekima yote na ufahamivu wa kiroho,” hawa watiwa-mafuta kwa roho “wa[n]ang’aa kwa uangavu kama jua katika ufalme wa Baba yao.”—Wakolosai 1:9; Mathayo 13:43.

      14, 15. Mbali na kukusanywa kwa “wana wa ufalme,” ni kukusanya kupi kumetukia, na kukusanya huko kulitabiriwaje na Hagai?

      14 Isitoshe, wengine wamemiminika kwenye ‘mlima wa nyumba ya Yehova.’ Hao, ambao Yesu aliwaita “kondoo wengine,” wanatumaini kuishi milele katika dunia paradiso. (Yohana 10:16; Ufunuo 21:3, 4) Tangu miaka ya 1930, walikuja kwa maelfu, kisha kwa mamia ya maelfu, na sasa kwa mamilioni! Katika ono aliloonyeshwa mtume Yohana, wao hufafanuliwa kuwa “umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.”—Ufunuo 7:9.

      15 Nabii Hagai alitabiri kutokea kwa umati huu mkubwa. Aliandika: “Kwa maana BWANA wa majeshi asema hivi, Mara moja tena, ni kitambo kidogo tu, nami nitazitikisa hizo mbingu, na hii nchi, na bahari, na nchi kavu; nami nitatikisa mataifa yote, na vitu vinavyotamaniwa na mataifa yote [wale wanaojiunga na Wakristo watiwa-mafuta katika ibada safi] vitakuja; nami nitaijaza nyumba hii utukufu, asema BWANA wa majeshi.” (Hagai 2:6, 7) Kuwapo kwa “umati mkubwa” huo unaozidi kuongezeka na waandamani wake watiwa-mafuta huinua, naam, hutukuza, ibada safi katika nyumba ya Yehova. Haikuwahi kamwe kurekodiwa watu wengi namna hiyo wakiwa wameungana katika ibada ya Mungu wa kweli, na hilo humletea Yehova na Mfalme wake aliyetawazwa, Yesu Kristo, utukufu. Mfalme Solomoni aliandika: “Utukufu wa mfalme ni wingi wa watu wake.”—Mithali 14:28.

      Ibada Yakwezwa Maishani mwa Watu

      16-18. Watu fulani wamefanya mabadiliko gani ili wamwabudu Yehova kwa njia inayokubalika?

      16 Yehova astahili sifa zote kwa kuinuliwa kwa ibada safi wakati wetu. Na bado, wale wanaomkaribia wana pendeleo la kuishiriki kazi hii. Kama vile jitihada huhitajika ili kupanda mlima, vivyo hivyo jitihada huhitajika ili kujifunza na kuishi kupatana na viwango vya Mungu vya uadilifu. Sawa na Wakristo katika karne ya kwanza, watumishi wa Mungu leo wameachilia mbali mitindo ya maisha na mazoea yasiyopatana na ibada ya kweli. Waasherati, waabudu-sanamu, wazinzi, wezi, watu wenye pupa, walevi, na wengineo wamebadili njia zao nao ‘wameoshwa wakawa safi’ machoni pa Mungu.—1 Wakorintho 6:9-11.

      17 Mfano bora ni mambo yaliyompata mwanamke mmoja mchanga, aliyeandika hivi: “Wakati fulani nilikuwa nimepotea bila tumaini. Maisha yangu yalijaa ukosefu wa adili na ulevi. Nilipata magonjwa ya zinaa. Pia niliuza dawa za kulevya nami sikujali lolote.” Baada ya kujifunza Biblia, alifanya mabadiliko makubwa ili ajipatanishe na viwango vya Mungu. Sasa asema hivi: “Nafurahia amani ya akili, kujistahi, tumaini kwa wakati ujao, familia halisi, na zaidi ya yote, uhusiano na Baba yetu, Yehova.”

      18 Hata baada ya kupata msimamo unaokubaliwa mbele za Yehova, ni lazima wote waendelee kuinua ibada safi kwa kuitanguliza maishani mwao. Maelfu ya miaka iliyopita, Yehova alionyesha kupitia Isaya uhakika wake kwamba kungekuwako umati leo unaotamani kufanya ibada yake kuwa jambo muhimu zaidi maishani mwao. Je, wewe ni mmoja wao?

      Watu Waliofundishwa Njia za Yehova

      19, 20. Watu wa Mungu hufundishwa nini, nao hufundishiwa wapi?

      19 Isaya atuambia mengi zaidi juu ya wale wanaoikubali ibada safi leo. Asema hivi: “Mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa BWANA, nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la BWANA katika Yerusalemu.”—Isaya 2:3.

      20 Yehova hawaachilii watu wake wazurure kama kondoo waliopotea. Kupitia Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia, yeye huwapa “sheria” yake na “neno” lake ili wajifunze njia zake. Ujuzi huo huwaandaa ili ‘watembee katika mapito yake.’ Kutoka katika mioyo iliyojaa shukrani na kwa kupatana na mwelekezo wa Mungu, wao husemezana juu ya njia za Yehova. Wao hukusanyika pamoja kwenye mikusanyiko mikubwa na katika vikundi vidogo—kwenye Majumba ya Ufalme na katika nyumba za watu binafsi—ili kusikiliza na kujifunza njia za Mungu. (Kumbukumbu la Torati 31:12, 13) Kwa hiyo wao huiga kiolezo cha Wakristo wa mapema, waliokutana pamoja kwa ajili ya kutiana moyo na kuchocheana ili wajawe “kazi zilizo bora.”—Waebrania 10:24, 25.

      21. Watumishi wa Yehova hushiriki katika kazi gani?

      21 Wao huwaalika wengine ‘waende juu’ kwa ibada iliyoinuliwa ya Yehova Mungu. Jambo hili lapatana vema kama nini na amri aliyotoa Yesu kwa wanafunzi wake punde kabla ya kupaa mbinguni! Aliwaambia hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20) Kwa utegemezo wa Mungu, Mashahidi wa Yehova huenda kwa utiifu kotekote duniani, wakifundisha na kufanya wanafunzi, wakiwabatiza.

      Panga Zawa Majembe

      22, 23. Andiko la Isaya 2:4 hutabiri nini, na ofisa mmoja wa UM alisemaje kulihusu?

      22 Sasa twaingia katika mstari unaofuata, ambao sehemu yake imeandikwa ukutani kwenye jengo la UM. Isaya aandika: “Atafanya hukumu katika mataifa mengi, atawakemea watu wa kabila nyingi; nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”—Isaya 2:4.

      23 Haingekuwa rahisi kutimiza lengo hilo. Federico Mayor, mkurugenzi mkuu wa Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa, alisema hivi wakati mmoja: “Machukizo yote ya vita, tunayoyaona kupitia televisheni, hayaelekei kukomesha mfumo mkubwa wa mambo ya kivita ulioanzishwa na kudumishwa kwa karne nyingi. Vizazi vya leo vina kazi ya Kibiblia, inayoelekea kutowezekana ya ‘kuzifua panga zao ziwe majembe’ na kubadilika kutoka hali ya kupenda vita—iliyositawishwa tangu zamani za kale—kufikia hali ya kutaka amani. Kutekeleza hili kungekuwa ndiko tendo bora zaidi ambalo watu ulimwenguni kote wangeweza kutimiza, na urithi bora zaidi kwa wazao wetu.”

      24, 25. Ni nani wanaotimiza maneno ya Isaya, na kwa njia gani?

      24 Mataifa kwa jumla hayatapata kamwe kulifikia lengo hilo lililo juu sana. Hayana uwezo huo. Maneno ya Isaya yanatimizwa na watu mmoja-mmoja kutoka kwa mataifa mengi, ambao wameungana katika ibada safi. Yehova ‘amenyosha mambo’ miongoni mwao. Amewafundisha watu wake kuishi kwa amani. Kwa kweli, katika ulimwengu uliogawanyika na kujaa mizozo, kitamathali wao “wa[me]fua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu.” Jinsi gani?

      25 Kwanza, wao hawaungi mkono vita vya mataifa. Punde kabla ya kifo cha Yesu, watu wenye silaha walikuja kumkamata. Petro aliposhambulia kwa upanga ili kumtetea Bwana-Mkubwa wake, Yesu alimwambia hivi: “Rudisha upanga wako mahali pao, kwa maana wale wote wauchukuao upanga wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:52) Tangu wakati huo, wale wanaofuata hatua za Yesu wamefua panga zao ziwe majembe nao wamekataa kuchukua silaha ili kuwaua wanadamu wenzao au kuunga mkono harakati za vita kwa njia nyingine yoyote. Wao ‘hufuatia amani pamoja na watu wote.’—Waebrania 12:14.

      Kufuatia Njia za Amani

      26, 27. Watu wa Mungu ‘hutafutaje sana amani na kuifuatia’? Toa kielelezo.

      26 Amani ya watu wa Mungu haitokani tu na kukataa kupigana vita. Ingawa wamo katika nchi zaidi ya 230 nao hutoka katika jamii nyingi mbalimbali, wao hufurahia amani kati yao. Miongoni mwao mna utimizo wa maneno ya Yesu, aliyewaambia wanafunzi wake katika karne ya kwanza: “Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Wakristo leo ni “wenye kufanya amani.” (Mathayo 5:9) Wao “[hutafuta] sana amani na kuifuatia.” (1 Petro 3:11) Yehova, “Mungu apaye amani,” ndiye anayewategemeza.—Waroma 15:33.

      27 Kuna vielelezo vinavyovutia vya watu ambao wamejifunza kuwa wenye kufanya amani. Mwanamume kijana aandika hivi kuhusu maisha yake ya utotoni: “Magumu yaliyonipata yalinifundisha namna ya kujilinda. Yalinifanya mkali na mwenye hasira juu ya maisha. Sikuzote nilijikuta katika mapigano. Kila siku ningepigana na mtoto tofauti katika ujirani, wakati mmoja kwa ngumi, wakati mwingine kwa mawe au chupa. Nilikua nikiwa mjeuri sana.” Ingawa hivyo, hatimaye aliitikia mwaliko wa kwenda kwenye ‘mlima wa nyumba ya Yehova.’ Alijifunza njia za Mungu naye akawa mtumishi wa Mungu mwenye kufanya amani.

      28. Wakristo waweza kufanya nini ili kufuatia sana amani?

      28 Walio wengi wa watumishi wa Yehova hawakulelewa katika mazingira yenye jeuri hivyo. Ingawa hivyo, hata katika mambo madogo kwa kulinganisha—matendo ya fadhili, kusamehe, na hisia-mwenzi—wao hujitahidi kuendeleza amani pamoja na wengine. Ingawa si wakamilifu, wao hujitahidi kutumia shauri la Biblia juu ya “[kuendelea] kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika dhidi ya mwingine.”—Wakolosai 3:13.

      Wakati Ujao Wenye Amani

      29, 30. Kuna mataraja gani kwa dunia?

      29 Yehova amefanya jambo la ajabu katika hizi “siku za mwisho.” Amewakusanya watu wanaotaka kumtumikia kutoka katika mataifa yote. Amewafundisha kutembea katika njia zake, njia za amani. Hao ndio watakaookoka “dhiki kubwa” inayokuja na kuingia katika ulimwengu mpya wenye amani ambamo vita itakomeshwa milele.—Ufunuo 7:14.

      30 Panga, yaani, silaha, hazitakuwapo tena. Mtunga-zaburi aliandika hivi kuhusu wakati huo: “Njoni myatazame matendo ya BWANA, jinsi alivyofanya ukiwa katika nchi. Avikomesha vita hata mwisho wa dunia; avunja uta, akata mkuki, achoma moto magari.” (Zaburi 46:8, 9) Kwa mujibu wa mataraja hayo, himizo la Isaya linalofuata lafaa leo kama lilivyofaa alipoliandika: “Enyi wa nyumba ya Israeli, njoni, twende katika nuru ya BWANA [“Yehova,” “NW”].” (Isaya 2:5) Naam, nuru ya Yehova na iangaze njia yetu sasa, nasi tutatembea katika njia yake milele na milele.—Mika 4:5.

  • Yehova Huwafedhehesha Wenye Kiburi
    Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
    • Sura ya 5

      Yehova Huwafedhehesha Wenye Kiburi

      Isaya 2:6–4:1

      1, 2. Kwa nini twapendezwa na ujumbe wa unabii wa Isaya kwa Wayahudi wa siku yake?

      AKIWA amechukizwa na hali ya Yerusalemu na Yuda, nabii Isaya sasa amgeukia Yehova Mungu na kutangaza hivi: “Umewaacha watu wako, nyumba ya Israeli.” (Isaya 2:6a) Kwa nini Mungu amekasirika hata akawakataa watu aliochagua mwenyewe kama “miliki [yake] ya pekee”?—Kumbukumbu la Torati 14:2, NW.

      2 Sisi twapendezwa sana na shutuma ya Isaya dhidi ya Wayahudi wa wakati wake. Kwa nini? Kwa sababu hali ya Jumuiya ya Wakristo leo yafanana sana na ile ya watu wa Isaya, na ndivyo ilivyo hukumu ambayo Yehova atangaza. Kukazia fikira tangazo la Isaya kutatupa uelewevu ulio wazi juu ya mambo anayoshutumu Mungu nasi tutasaidiwa kuepuka mazoea anayoyakataa. Basi, tukiwa na hamu nyingi mno, na tulifikirie neno la unabii la Yehova kama lilivyorekodiwa katika Isaya 2:6–4:1.

      Wao Huinama Katika Kiburi

      3. Isaya atubu makosa gani ya watu wake?

      3 Isaya, akitubu makosa ya watu wake, asema hivi: “Wamejaa kawaida za mashariki, nao ni wapiga ramli kama Wafilisti, na wanapana mikono na wana wa wageni.” (Isaya 2:6b) Miaka ipatayo 800 mapema, Yehova aliwaamuru watu wake wachaguliwa: “Msijitie unajisi katika mambo hayo hata mojawapo; kwa maana hizo taifa nitakazozitoa mbele zenu zimekuwa najisi kwa mambo hayo yote.” (Mambo ya Walawi 18:24) Yehova alimlazimisha Balaamu aseme hivi kuhusu wale aliokuwa amechagua kuwa miliki yake ya pekee: “Kutoka kilele cha majabali namwona; na kutoka milimani namtazama; angalia, ni watu wakaao peke yao, wala hawatahesabiwa pamoja na mataifa.” (Hesabu 23:9, 12) Ingawa hivyo, kufikia siku ya Isaya wachaguliwa wa Yehova wametwaa mazoea yenye kuchukiza ya mataifa jirani, nao “wamejaa kawaida za mashariki.” Badala ya kuwa na imani katika Yehova na neno lake, wao wanapiga “ramli kama Wafilisti.” Nchi hiyo haijitengi na mataifa hata kidogo, nao “wanapana mikono” na “wana wa wageni”—yamkini, wageni wanaoanzisha mazoea yasiyomhofu Mungu miongoni mwa watu wake.

      4. Badala ya kuwafanya Wayahudi wamshukuru Yehova, mali na uwezo wa kijeshi zawaathirije?

      4 Akitaja ufanisi wa sasa wa kiuchumi na uwezo wa kijeshi wa Yuda chini ya Mfalme Uzia, Isaya ataarifu hivi: “Tena nchi yao imejaa fedha na dhahabu, wala hapana mwisho wa hazina zao; tena nchi yao imejaa farasi, wala hapana mwisho wa magari yao.” (Isaya 2:7) Je, watu hao wanamshukuru Yehova kwa ajili ya mali hizo na uwezo wa kijeshi? (2 Mambo ya Nyakati 26:1, 6-15) Hata! Badala yake, wao wazitumaini mali zenyewe na kumwachilia mbali aliye Chanzo chake, Yehova Mungu. Matokeo ni nini? “Nchi yao imejaa sanamu; huabudu kazi ya mikono yao, vitu vilivyofanywa kwa vidole vyao wenyewe. Mtu mnyonge huinama, na mtu mkubwa hujidhili; kwa hiyo usiwasamehe.” (Isaya 2:8, 9) Wao huzigeuzia mbali nyuso zao kutoka kwa Mungu aliye hai na kuinamia sanamu zisizo na uhai.

      5. Kwa nini kuinamia sanamu si tendo la unyenyekevu?

      5 Kuinama kwaweza kuwa ishara ya unyenyekevu. Lakini kuinamia vitu visivyo na uhai ni ubatili, kukimfanya mwabudu-sanamu ‘kujidhili,’ kujishusha cheo. Yehova awezaje kusamehe dhambi hiyo? Waabudu-sanamu hao watafanyaje Yehova atakapowataka watoe hesabu?

      ‘Macho Yaliyoinuka Yatashushwa Chini’

      6, 7. (a) Ni nini kinachowapata wenye kiburi katika siku ya hukumu ya Yehova? (b) Yehova adhihirisha hasira yake dhidi ya nini na nani, na kwa nini?

      6 Isaya aendelea: “Ingia ndani ya jabali; ukajifiche mavumbini mbele za utisho wa BWANA, mbele za utukufu wa enzi yake.” (Isaya 2:10) Lakini jabali lolote lile halitakuwa kubwa vya kutosha kuwalinda, wala hapana ficho lolote lile litakalokuwa kubwa vya kutosha kuwaficha, kutoka kwa Yehova, Mweza Yote. Ajapo kutekeleza hukumu yake, “macho ya mwanadamu yaliyoinuka yatashushwa chini, na kiburi cha mwanadamu kitainamishwa, naye BWANA, yeye peke yake, atatukuzwa siku hiyo.”—Isaya 2:11.

      7 “Siku ya BWANA [“Yehova,” “NW”] wa majeshi” inakuja. Itakuwa wakati wa Mungu kudhihirisha hasira yake “juu ya mierezi yote ya Lebanoni iliyo mirefu na kuinuka, na juu ya mialoni yote ya Bashani; na juu ya milima mirefu yote, na juu ya vilima vyote vilivyoinuka; na juu ya kila mnara mrefu, na juu ya kila ukuta ulio na boma; na juu ya merikebu zote za Tarshishi, na juu ya kila taswira ipendezayo.” (Isaya 2:12-16) Naam, kila shirika lililoundwa na mwanadamu kama ishara ya majivuno yake na kila mtu asiyemwogopa Mungu zitashughulikiwa katika siku ya hasira ya kisasi ya Yehova. Hivyo, “majivuno ya mwanadamu yatainamishwa, na kiburi cha watu kitashushwa; naye BWANA, yeye peke yake, atatukuzwa siku hiyo.”—Isaya 2:17.

      8. Siku ya hukumu iliyotabiriwa yajaje juu ya Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K.?

      8 Siku ya hukumu iliyotabiriwa yaja juu ya Wayahudi mwaka wa 607 K.W.K. Mfalme Nebukadreza wa Babiloni anapoharibu Yerusalemu. Wakazi waona jiji lao wanalolipenda likichomeka, majengo yake yenye fahari yakiwa yamebomolewa, ukuta wake wenye nguvu ukiwa umevunjwa-vunjwa. Hekalu la Yehova limebomolewa likawa vifusi. Hazina zao wala magari yao havifai chochote katika ‘siku ya Yehova wa majeshi.’ Namna gani sanamu zao? Ni kama tu Isaya anavyotabiri: “Sanamu zitatoweka kabisa.” (Isaya 2:18) Wayahudi—kutia ndani wakuu na watu wenye uwezo—wapelekwa uhamishoni huko Babiloni. Yerusalemu lapaswa kubaki ukiwa kwa miaka 70.

      9. Hali ya Jumuiya ya Wakristo yafananaje na ile ya Yerusalemu na Yuda katika siku ya Isaya?

      9 Kweli hali ya Jumuiya ya Wakristo inafanana kabisa na ile ya Yerusalemu na Yuda katika siku ya Isaya! Ni wazi kuwa Jumuiya ya Wakristo imesitawisha uhusiano wa karibu pamoja na mataifa ya ulimwengu huu. Hiyo hutegemeza Umoja wa Mataifa kwa bidii nayo imejaza nyumba yake sanamu na mazoea yasiyo ya Kimaandiko. Wafuasi wake ni wenye kufuatia vitu vya kimwili nao huutegemea uwezo wa kijeshi. Na je, wao hawaoni makasisi wao kuwa wanaostahili umashuhuri mkubwa, wakiwapa majina ya vyeo na sifa? Hapana shaka kiburi cha Jumuiya ya Wakristo kitabatilishwa. Lakini ni lini?

      “Siku ya Yehova” Inayokaribia

      10. Mitume Paulo na Petro huelekeza kwenye “siku [gani] ya Yehova”?

      10 Maandiko huelekeza kwenye “siku ya Yehova” itakayokuwa muhimu zaidi kuliko siku ya hukumu juu ya Yerusalemu na Yuda za kale. Mtume Paulo, chini ya upulizio, aliishirikisha “siku ya Yehova” inayokuja na kuwapo kwa Mfalme Yesu Kristo aliyetawazwa. (2 Wathesalonike 2:1, 2) Petro alizungumza kuhusu siku hiyo kwa kuhusiana na kuanzishwa kwa ‘mbingu mpya na dunia mpya ambamo uadilifu utakaa.’ (2 Petro 3:10-13) Hiyo ndiyo siku ambayo Yehova atatekeleza hukumu yake juu ya mfumo wote mwovu wa mambo, pamoja na Jumuiya ya Wakristo.

      11. (a) Ni nani ‘watakaoistahimili’ “siku ya Yehova” inayokuja? (b) Twaweza kumfanyaje Yehova awe kimbilio letu?

      11 “Ole wake siku hii!,” asema nabii Yoeli, “kwa maana siku ya BWANA [“Yehova,” NW] inakaribia, nayo itakuja kama uangamivu utokao kwake aliye Mwenyezi.” Kwa kuzingatia ukaribu wa “siku” hiyo, je, kila mtu hapaswi kuhangaikia usalama wakati wa kipindi hicho chenye kutia hofu? “Ni nani awezaye kuistahimili?” auliza Yoeli. Ajibu hivi: “BWANA atakuwa kimbilio la watu wake.” (Yoeli 1:15; 2:11; 3:16) Je, Yehova Mungu atakuwa kimbilio kwa wale wenye roho ya kiburi na wanaotumaini mali, uwezo wa kijeshi, na miungu iliyotengenezwa na wanadamu? Haiwezekani! Mungu aliwaacha hata watu wake waliochaguliwa walipotenda hivyo. Basi ni muhimu kama nini kwa watumishi wote wa Mungu ‘waitafute haki na kuutafuta unyenyekevu,’ na kuchunguza kwa uzito mahali ilipo ibada ya Yehova maishani mwao!—Sefania 2:2, 3.

      “Kwa Fuko na Popo”

      12, 13. Kwa nini yafaa kwa waabudu-sanamu kutupa miungu yao “kwa fuko na popo” katika siku ya Yehova?

      12 Waabudu-sanamu watazionaje sanamu zao wakati wa siku kuu ya Yehova? Isaya ajibu: “Watu wataingia ndani ya pango za majabali, na ndani ya mashimo ya nchi, mbele za utisho wa BWANA na utukufu wa enzi yake, atakapoondoka ili aitetemeshe mno dunia. Siku hiyo kila mtu atazitupilia mbali sanamu zake za fedha, na sanamu zake za dhahabu . . . kwa fuko na popo; ili aingie ndani ya pango za majabali, na ndani ya tundu za miamba iliyopasuka, mbele za utisho wa BWANA na utukufu wa enzi yake, atakapoondoka ili aitetemeshe mno dunia. Mwacheni mwanadamu ambaye pumzi yake i katika mianzi ya pua yake; kwa maana hudhaniwaje kuwa ni kitu?”—Isaya 2:19-22.

      13 Fuko huishi katika mashimo ardhini, na popo huishi katika mapango yenye ukiwa na giza. Na zaidi, mahali wanakoishi popo wengi pamoja, kuna harufu mbaya na mkusanyo mkubwa wa kinyesi. Kutupwa kwa sanamu mahali kama hapo kwafaa. Hizo zastahili kutupwa mahali penye giza na uchafu. Watu nao watatafuta kimbilio katika majabali na tundu za miamba iliyopasuka katika siku ya hukumu ya Yehova. Kwa hiyo, hatima ya sanamu na wenye kuziabudu itakuwa sawasawa. Kupatana kabisa na unabii wa Isaya, sanamu zisizo na uhai hazikuwaokoa waabudu wake wala Yerusalemu kutoka mikononi mwa Nebukadreza mwaka wa 607 K.W.K.

      14. Katika siku ya hukumu ya Yehova inayokuja juu ya milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli, watu walio na mtazamo wa kilimwengu watafanyaje?

      14 Watu watafanya nini katika siku ya hukumu ya Yehova juu ya Jumuiya ya Wakristo na juu ya sehemu nyingine za milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli? Yamkini wengi wao, wakikabiliwa na hali zinazozorota ulimwenguni kote, watang’amua kwamba sanamu zao hazifai chochote. Badala ya hizo, huenda wakatafuta kimbilio na ulinzi katika mashirika ya kidunia yasiyo ya kiroho, labda kutia ndani Umoja wa Mataifa, yule “hayawani-mwitu wa rangi-nyekundu-nyangavu” wa Ufunuo sura ya 17. “Pembe kumi” za hayawani-mwitu huyo wa ufananisho ndizo zitakazomharibu Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli, ambayo Jumuiya ya Wakristo ndiyo sehemu mashuhuri.—Ufunuo 17:3, 8-12, 16, 17.

      15. Yehova peke yake ‘atatukuzwaje’ katika siku yake ya hukumu?

      15 Ingawa kuangamizwa na kuchomwa kwa Babiloni Mkubwa huenda kukawa tendo la moja kwa moja la zile pembe kumi za ufananisho, huko, kwa kweli, ni utekelezaji wa hukumu ya Yehova. Kuhusu Babiloni Mkubwa, Ufunuo 18:8 hutaarifu hivi: “Hiyo ndiyo sababu katika siku moja tauni zake zitakuja, kifo na kuomboleza na njaa kali, naye atachomwa kabisa kwa moto, kwa sababu Yehova Mungu, aliyemhukumu, ni mwenye nguvu.” Basi Yehova Mungu, Mweza Yote, apewa sifa kwa kuwakomboa wanadamu kutoka katika mamlaka ya dini isiyo ya kweli. Kama anavyotaarifu Isaya, “BWANA [“Yehova,” NW], yeye peke yake, atatukuzwa siku hiyo. Kwa maana kutakuwa siku ya BWANA wa majeshi.”—Isaya 2:11b, 12a.

  • Yehova Huwafedhehesha Wenye Kiburi
    Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
    • [Picha katika ukurasa wa 50]

      Sanamu, mali, na uwezo wa kijeshi haviokoi Yerusalemu katika siku ya hukumu ya Yehova

      [Picha katika ukurasa wa 55]

      Katika “siku ya Yehova,” milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli itaangamizwa

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki