-
Utawala wa Shetani Utashindwa KabisaMnara wa Mlinzi—2010 | Januari 15
-
-
Utawala wa Shetani Utashindwa Kabisa
“Mambo hayatakuwa mema kwa mwovu.”—MHU. 8:13.
1. Kwa nini hukumu inayokuja ya waovu ni habari yenye kufariji?
PUNDE si punde, waovu watahukumiwa. Wataadhibiwa kwa sababu ya makosa yao. (Met. 5:22; Mhu. 8:12, 13) Hiyo ni habari yenye kufariji, hasa kwa wale ambao wanapenda uadilifu na ambao wametendewa isivyo haki na kuteswa na waovu. Atakayekuwa wa kwanza kabisa kuhukumiwa kati ya waovu, ni baba ya uovu Shetani Ibilisi.—Yoh. 8:44.
2. Kwa nini muda ulihitajiwa ili kutatua suala ambalo lilitokezwa katika Edeni?
2 Katika bustani ya Edeni, Shetani alijiona kuwa mtu wa maana sana, akawafanya wanadamu wakatae utawala wa Mungu. Kwa hiyo, wazazi wetu wa kwanza walijiunga na Shetani katika kutilia shaka haki ya Yehova ya kutawala na hivyo wakawa watenda-dhambi. (Rom. 5:12-14) Bila shaka, Yehova alijua matokeo ya kumwasi na kutomheshimu. Hata hivyo, viumbe wote wenye akili walipaswa kuona wazi matokeo hayo ambayo hayangeweza kuepukika. Basi, muda ulihitajiwa ili suala hilo litatuliwe na kuthibitisha kwa uhakika kwamba waasi hao walikuwa wamekosea kabisa.
3. Tuna maoni gani kuhusu serikali za wanadamu?
3 Kwa kuwa wanadamu walikuwa wamekataa kuongozwa na Yehova, walilazimika kuanzisha serikali zao wenyewe. Mtume Paulo alipokuwa akiwaandikia waamini wenzake huko Roma, aliziita serikali hizo za wanadamu “mamlaka zilizo kubwa.” Katika siku za Paulo, mamlaka kubwa ilikuwa hasa serikali ya Roma iliyoongozwa na Maliki Nero, ambaye alitawala kuanzia mwaka wa 54-68 W.K. Paulo alisema kwamba mamlaka kama hizo zilizo kubwa “zimesimamishwa na Mungu katika vyeo vyao vya kadiri.” (Soma Waroma 13:1, 2.) Je, hilo linamaanisha kwamba Paulo alikuwa akitetea utawala wa wanadamu kuwa ni bora kuliko utawala wa Mungu? Bila shaka hapana. Badala yake, alikuwa akisema kwamba maadamu Yehova anaruhusu utawala wa wanadamu uendelee kuwapo, Wakristo wanapaswa kuheshimu “mpango wa Mungu” na kuwatii watawala hao.
Njia Inayoongoza Kwenye Msiba
4. Eleza ni kwa nini utawala wa wanadamu utashindwa kwa hakika.
4 Bila shaka, utawala wa wanadamu unaoongozwa na Shetani utashindwa. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba utawala huo hautegemei hekima ya Mungu. Yehova peke yake ndiye aliye na hekima kamilifu. Hivyo basi, yeye ndiye chanzo pekee cha mwongozo unaotegemeka kuhusu utawala wenye mafanikio. (Yer. 8:9; Rom. 16:27) Sikuzote, Yehova anajua njia bora zaidi ya kufanya mambo, tofauti na wanadamu ambao mara nyingi wanajifunza kwa kukisia-kisia tu. Serikali yoyote ambayo haifuati mwongozo wa Mungu haiwezi kufanikiwa. Kwa sababu hiyo na kwa sababu ya mwelekeo mwovu wa Shetani, njia yake ya kuongoza kupitia utawala wa wanadamu haingefanikiwa tangu mwanzoni.
5, 6. Inaelekea ni nini kilichomwongoza Shetani amwasi Yehova?
5 Kwa kawaida, mtu mwenye busara hawezi kuanza kufanya jambo ambalo halitafanikiwa. Ikiwa atasisitiza kufanya jambo hilo, atalazimika kutambua makosa yake. Historia imethibitisha tena na tena kwamba hakuna faida yoyote inayotokana na kumpinga Muumba mweza-yote. (Soma Methali 21:30.) Hata hivyo, Shetani alimwasi Yehova kwa kuwa alipofushwa na kiburi chake, naye alijiona kuwa mtu wa maana sana. Hivyo, Ibilisi alichagua kimakusudi kufuata njia ambayo ingemwongoza kwenye msiba tu.
6 Mtazamo wa Shetani wa kimbelembele ulionyeshwa baadaye na mtawala wa Babiloni ambaye Biblia inasema alijigamba hivi: “Nitaenda juu mbinguni. Nitakiinua kiti changu cha ufalme juu ya nyota za Mungu, nami nitaketi juu ya mlima wa mkutano, katika sehemu za mbali zaidi za kaskazini. Nitaenda juu ya mahali palipo juu pa mawingu; mimi nitajifananisha na Aliye Juu Zaidi.” (Isa. 14:13-15) Jitihada za mtawala huyo asiye na busara hazikufanikiwa, na kwa aibu utawala wa Babiloni ulishindwa. Hivi karibuni, Shetani atashindwa kabisa vivyo hivyo pamoja na ulimwengu wake.
Kwa Nini Mungu Aliruhusu Hali Hiyo?
7, 8. Wanadamu wamefaidika jinsi gani kwa sababu ya Yehova kuruhusu uovu uendelee kuwapo kwa muda?
7 Huenda watu fulani wakauliza kwa nini Yehova hakuwazuia wanadamu wajiunge na Shetani na kufuata utawala ambao kwa hakika ungeshindwa. Akiwa Mungu Mweza-Yote, bila shaka angeweza kuwazuia. (Kut. 6:3) Hata hivyo, hakuwazuia. Kwa sababu ya hekima yake, alitambua kwamba ikiwa angewaruhusu wanadamu waendelee na uasi wao kwa muda fulani, mwishowe matokeo yangekuwa mazuri. Hatimaye, Yehova angethibitika kuwa Mtawala mwadilifu na mwenye upendo, na wanadamu waaminifu wangefaidika kutokana na uamuzi wa Mungu.
8 Familia ya wanadamu ingeepuka mateso mengi ikiwa wanadamu wangekataa kudanganywa na Shetani na kama hawangeasi utawala wa Mungu! Hata hivyo, uamuzi wa Yehova wa kuwaruhusu wanadamu wajitawale kwa muda fulani umekuwa na faida. Hatua hiyo imewasaidia sana watu wenye mioyo minyoofu kuona kwamba ni jambo la hekima kumsikiliza Mungu na kumtegemea. Kwa karne nyingi, wanadamu wamejaribu aina mbalimbali za serikali, lakini hakuna hata moja ambayo imethibitika kuwa inafaa kabisa. Jambo hilo la hakika limefanya waabudu wa Mungu wasadiki kabisa kwamba utawala wa Yehova ndio utawala bora zaidi. Ni kweli kwamba kwa sababu Yehova ameruhusu utawala mwovu wa Shetani uendelee kuwapo, wanadamu wote wameteseka, kutia ndani wale ambao wanamwabudu Mungu kwa uaminifu. Hata hivyo, waabudu hao waaminifu wamefaidika kwa sababu Yehova ameruhusu uovu uendelee kuwapo kwa muda.
Uasi Ambao Umefanya Yehova Atukuzwe
9, 10. Eleza jinsi ambavyo utawala wa Shetani umefanya Yehova atukuzwe.
9 Uhakika wa kwamba Yehova amewaruhusu wanadamu washawishiwe na Shetani na kujitawala, hauthibitishi kamwe kwamba utawala wa Yehova haufai. Badala yake, historia inathibitisha ukweli wa maneno ya Yeremia ambayo alisema akiongozwa na roho ya Mungu kwamba wanadamu hawawezi kujitawala. (Soma Yeremia 10:23.) Kwa kuongezea, uasi wa Shetani umempa Yehova nafasi ya kuonyesha sifa Zake nzuri kwa njia iliyo wazi zaidi. Jinsi gani?
10 Matokeo mabaya ya utawala wa Shetani yamefunua waziwazi zaidi sifa kamilifu za Yehova ambazo huenda hatungeziona. Kwa hiyo, ametukuzwa machoni pa wale ambao wanampenda. Ndiyo, ingawa huenda likaonekana kuwa jambo la kushangaza, kwa kweli utawala wa Shetani umefanya Mungu atukuzwe. Hilo limeonyesha wazi kwamba Yehova ameshughulika na upinzani huo kuelekea enzi yake kuu kwa njia bora zaidi. Ili kuthibitisha ukweli huo, acheni tuchunguze kwa ufupi sifa fulani za Yehova na tuone jinsi ambavyo utawala mwovu wa Shetani umemfanya Yehova aonyeshe sifa hizo kwa njia nyingine nyingi.
11. Yehova ameonyesha upendo jinsi gani?
11 Upendo. Maandiko yanatuambia kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yoh. 4:8) Kwanza kabisa, Mungu alionyesha upendo wake kwa kuwaumba wanadamu. Kwa kuongezea, miili yetu iliyoumbwa kwa njia ya ajabu na yenye kustaajabisha inathibitisha pia upendo wa Mungu. Pia, kwa upendo Yehova aliwapa wanadamu makao mazuri sana ambayo yalikuwa na kila kitu walichohitaji ili kuwa na furaha. (Mwa. 1:29-31; 2:8, 9; Zab. 139:14-16) Lakini familia ya wanadamu ilipotumbukia katika dhambi, Yehova alionyesha upendo wake kwa njia nyingine mpya. Jinsi gani? Mtume Yohana ananukuu maneno haya ya Yesu: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yoh. 3:16) Mungu aliwaonyesha wanadamu upendo wake kwa njia kubwa zaidi alipomtuma Mwana wake mzaliwa-pekee aje duniani kuwakomboa watenda-dhambi. (Yoh. 15:13) Uthibitisho huo mkubwa wa upendo uliwawekea pia wanadamu mfano wa kuiga, na umewapa nafasi ya kuonyesha upendo wa Mungu wa kujidhabihu katika maisha yao ya kila siku, kama Yesu alivyofanya.—Yoh. 17:25, 26.
12. Nguvu za Yehova zinaonekana jinsi gani?
12 Nguvu. “Mungu, Mweza-Yote” ndiye peke yake aliye na nguvu za kuumba uhai. (Ufu. 11:17; Zab. 36:9) Mwanadamu anapozaliwa anaweza kulinganishwa na karatasi ambayo haina maandishi yoyote. Wakati wa kifo, anakuwa amejaza kwenye karatasi hiyo maamuzi, matendo, na mambo mbalimbali aliyopitia maishani ambayo yalifinyanga utu wake. Habari hiyo inaweza kuhifadhiwa katika kumbukumbu ya Yehova. Wakati ukifika, Yehova anaweza kumfufua mtu huyo, akiwa na utu wake wa pekee. (Yoh. 5:28, 29) Kwa hiyo, ingawa hapo mwanzoni Mungu hakukusudia wanadamu wafe, kifo kimempa Yehova nafasi ya kuonyesha kwamba ana nguvu za kuwafufua wafu. Kwa kweli, Yehova ni “Mungu, Mweza-Yote.”
13. Dhabihu ya Yesu ilionyesha jinsi gani haki kamilifu ya Yehova?
13 Haki. Yehova hasemi uwongo; wala hatendi kamwe isivyo haki. (Kum. 32:4; Tito 1:2) Sikuzote anashikamana na viwango vya juu zaidi vya kweli na haki, hata ikiwa inaonekana kwamba kufanya hivyo kutamgharimu sana. (Rom. 8:32) Bila shaka, Yehova alihisi uchungu sana alipomwona Mwana wake mpendwa akifa kwenye mti wa mateso kana kwamba Yesu alikuwa mwasi aliyekuwa amekufuru. Hata hivyo, akichochewa na upendo kuelekea wanadamu wasio wakamilifu, Yehova alikuwa tayari kuruhusu tukio hilo lenye kuumiza litendeke ili ashikamane na viwango vyake vikamilifu vya haki. (Soma Waroma 5:18-21.) Ulimwengu uliojaa ukosefu wa haki ulimpa Yehova nafasi ya kuthibitisha kwamba yeye ndiye mfano bora zaidi katika kuonyesha haki.
14, 15. Yehova ameonyesha subira na hekima yake isiyo na kifani kwa njia gani mbalimbali?
14 Hekima. Mara tu baada ya Adamu na Hawa kufanya dhambi, Yehova alifunua jinsi ambavyo angeondoa madhara yote yaliyosababishwa na uasi wao. (Mwa. 3:15) Yehova alionyesha wazi kabisa hekima yake kwa kuchukua hatua ya haraka na kufunua hatua kwa hatua kusudi lake kuelekea watumishi wake. (Rom. 11:33) Hakuna jambo lolote linaloweza kumzuia Yehova asitimize makusudi yake. Katika ulimwengu uliojaa watu wenye maadili mapotovu, wanaopenda vita, wasio na usawaziko, wasiotii, wasio na rehema, wenye ubaguzi, na wanafiki, Yehova amekuwa na nafasi ya kutosha ya kuwaonyesha viumbe wake hekima ya kweli. Mwanafunzi Yakobo alisema hivi: “Hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili, kisha yenye kufanya amani, yenye usawaziko, tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema, haifanyi tofauti zenye ubaguzi, si ya kinafiki.”—Yak. 3:17.
15 Subira na Ustahimilivu. Sifa za Yehova za subira na ustahimilivu hazingeonekana wazi zaidi ikiwa hangelazimika kushughulika na wanadamu wasio wakamilifu, wenye dhambi, na wanaokosea. Kwa kukubali kushughulika na wanadamu kwa maelfu ya miaka, Yehova ameonyesha kwamba ana sifa hizo nzuri ajabu kwa kiwango kikamilifu, na hivyo tunapaswa kumshukuru sana. Kwa kufaa, mtume Petro alisema kwamba tunapaswa ‘kuiona subira ya Bwana wetu kuwa wokovu.’—2 Pet. 3:9, 15.
16. Kwa nini utayari wa Yehova wa kusamehe unatuletea shangwe nyingi sana?
16 Yuko Tayari Kusamehe. Sisi sote ni watenda-dhambi na tunajikwaa mara nyingi. (Yak. 3:2; 1 Yoh. 1:8, 9) Tunapaswa kushukuru sana kwamba Yehova yuko tayari kusamehe “kwa njia kubwa”! (Isa. 55:7) Fikiria pia ukweli huu: Kwa sababu tumezaliwa tukiwa watenda-dhambi wasio wakamilifu, tunaweza kupata shangwe nyingi sana Mungu anapotusamehe makosa yetu. (Zab. 51:5, 9, 17) Sifa hiyo ya Yehova yenye kugusa moyo inatuchochea sisi binafsi kumpenda zaidi na inatutia moyo kuiga mfano wake tunaposhughulika na wengine.—Soma Wakolosai 3:13.
Kwa Nini Ulimwengu Una Ugonjwa?
17, 18. Utawala wa Shetani umeshindwa jinsi gani?
17 Kwa karne nyingi, mfumo wote wa ulimwengu wa Shetani ambao unatokana na utawala wake, umeshindwa kufanikiwa. Mwaka wa 1991, gazeti moja (The European) lilisema hivi: “Je, ulimwengu una ugonjwa? Bila shaka ndiyo, lakini . . . ugonjwa huo haujasababishwa na Mungu, ugonjwa wa ulimwengu umesababishwa na wakaaji wake.” Hilo ni kweli kabisa! Wakichochewa na Shetani, wazazi wetu wa kwanza walichagua utawala wa wanadamu badala ya utawala wa Yehova. Kwa kufanya hivyo, walianzisha utawala ambao bila shaka ungeshindwa. Maumivu na mateso ambayo wanadamu wanapata ulimwenguni pote ni ishara ya kwamba utawala wa wanadamu umeshikwa na ugonjwa hatari.
18 Utawala wa Shetani unachochea uchoyo. Hata hivyo, uchoyo au ubinafsi hauwezi kamwe kuushinda upendo, ambao ni msingi wa utawala wa Yehova. Utawala wa Shetani umeshindwa kuleta amani, furaha, na usalama. Ni wazi kwamba utawala wa Yehova ndio utawala bora kabisa! Je, leo kuna uthibitisho wowote unaoonyesha hivyo? Ndiyo, kama tutakavyoona katika habari inayofuata.
-
-
Utawala wa Yehova Umethibitika Kuwa Bora!Mnara wa Mlinzi—2010 | Januari 15
-
-
Utawala wa Yehova Umethibitika Kuwa Bora!
“Aliye Juu Zaidi ni Mtawala katika ufalme wa wanadamu.”—DAN. 4:17.
1, 2. Taja sababu fulani ambazo zimefanya utawala wa wanadamu ushindwe.
UTAWALA wa wanadamu umeshindwa! Hakuna shaka yoyote kuhusu hilo. Sababu kuu ambayo imefanya ushindwe ni kwamba wanadamu hawana hekima ya kutawala kwa mafanikio. Leo ni wazi zaidi kwamba utawala wa wanadamu umeshindwa kwa kuwa watawala wengi ‘wanajipenda wenyewe, wanapenda pesa, wanajidai, wana majivuno, si washikamanifu, hawataki makubaliano yoyote, ni wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, na wenye kujivuna kwa kiburi.’—2 Tim. 3:2-4.
2 Hapo zamani, wazazi wetu wa kwanza walikataa utawala wa Mungu. Walipofanya hivyo, huenda walifikiri kwamba wanachagua uhuru. Hata hivyo, ukweli ni kwamba walikuwa wanajitiisha chini ya utawala wa Shetani. Utawala mbaya wa wanadamu ambao umekuwapo kwa miaka elfu sita chini ya uvutano wenye nguvu wa “mtawala wa ulimwengu huu,” Shetani, umesababisha hali iliyopo leo ambayo ni mbaya zaidi katika historia yote ya wanadamu. (Yoh. 12:31) Kikizungumza kuhusu hali ya wanadamu leo, kitabu kimoja (The Oxford History of the Twentieth Century) kinasema kwamba, ni kazi bure “kutafuta ulimwengu ulio mkamilifu.” Kinaeleza hivi: “Mbali na kwamba hauwezi kupatikana, jitihada hizo zinasababisha misiba, utawala wa kimabavu, na vita vibaya zaidi.” Maelezo hayo manyoofu yanaonyesha wazi kwamba utawala wa wanadamu umeshindwa!
3. Tunaweza kusema Mungu angetawala jinsi gani ikiwa Adamu na Hawa hawangefanya dhambi?
3 Basi, inasikitisha kwamba wazazi wetu wa kwanza walikataa utawala pekee ambao unafaa, yaani, utawala wa Mungu! Bila shaka, hatujui vizuri kabisa jinsi ambavyo Yehova angeitawala dunia ikiwa Adamu na Hawa wangeendelea kuwa waaminifu kwake. Hata hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba utawala wa Mungu ambao ungekubaliwa na wanadamu wote ungetawala kwa upendo na haungekuwa na ubaguzi. (Mdo. 10:34; 1 Yoh. 4:8) Kwa sababu Mungu ana hekima isiyo na kifani, tunaweza pia kuwa na hakika kwamba ikiwa wanadamu wangeendelea kujitiisha chini ya utawala wa Yehova, makosa yote ambayo yamefanywa na watu ambao wameunga mkono utawala wa wanadamu yangeepukwa. Utawala wa Mungu, yaani, theokrasi, ungefanikiwa “kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.” (Zab. 145:16) Kwa ufupi, ungekuwa utawala mkamilifu. (Kum. 32:4) Inasikitisha kwamba wanadamu walikataa utawala huo!
4. Shetani ameruhusiwa kutawala kwa kadiri gani?
4 Hata hivyo, ni vizuri kukumbuka kwamba hata ingawa Yehova aliwaruhusu wanadamu wajitawale, hakupoteza kamwe haki yake ya kuwatawala viumbe wake. Hata mfalme mwenye nguvu wa Babiloni alilazimika kukiri kwamba kwa hakika “Aliye Juu Zaidi ni Mtawala katika ufalme wa wanadamu.” (Dan. 4:17) Mwishowe, Ufalme wa Mungu utafanya mapenzi ya Mungu yatendeke. (Mt. 6:10) Ni kweli kwamba Yehova amemruhusu Shetani awe “mungu wa mfumo huu wa mambo” kwa kipindi kifupi ili masuala ambayo yalitokezwa na mpinzani huyo yajibiwe kikamili. (2 Kor. 4:4; 1 Yoh. 5:19) Hata hivyo, Shetani hana uwezo wa kuvuka mipaka ambayo amewekewa na Yehova. (2 Nya. 20:6; linganisha na Ayubu 1:11, 12; 2:3-6.) Sikuzote kumekuwa na watu ambao wamechagua kujitiisha kwa Mungu hata ingawa wameishi katika ulimwengu ambao unatawaliwa na Adui mkuu wa Mungu.
Mungu Atawala Israeli
5. Waisraeli walimwahidi Mungu nini?
5 Kuanzia wakati wa Abeli mpaka wakati taifa la Israeli lilipoanzishwa, watu fulani waaminifu walimwabudu Yehova na kutii amri zake. (Ebr. 11:4-22) Katika siku za Musa, Yehova alifanya agano na wazao wa mzee Yakobo, nao wakawa taifa la Israeli. Mwaka wa 1513 K.W.K., Waisraeli pamoja na wazao wao walimkubali Yehova awe Mtawala wao, wakasema hivi: “Yote ambayo Yehova amesema tuko tayari kuyafanya.”—Kut. 19:8.
6, 7. Utawala wa Mungu katika Israeli ulionyesha nini?
6 Yehova aliwachagua Waisraeli wawe watu wake kwa kusudi fulani. (Soma Kumbukumbu la Torati 7:7, 8.) Yehova hakuwachagua Waisraeli kwa faida yao. Jina la Mungu na enzi yake kuu ilihusika pia, na hayo yalikuwa mambo ya maana zaidi. Waisraeli wangetumiwa kutoa ushahidi kwamba Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli. (Isa. 43:10; 44:6-8) Kwa hiyo, Yehova aliliambia hivi taifa hilo: “Ninyi ni watu watakatifu kwa Yehova Mungu wenu, naye Yehova amewachagua ninyi muwe watu wake, mali ya pekee, kutoka kati ya vikundi vyote vya watu vilivyo kwenye uso wa nchi.”—Kum. 14:2.
7 Yehova alipowatawala Waisraeli alikumbuka kwamba hawakuwa wakamilifu. Wakati huohuo, sheria zake zilikuwa kamilifu na zilionyesha sifa za yule Aliyezitoa. Amri za Yehova ambazo Musa alipewa zilionyesha utakatifu wa Mungu, jinsi anavyopenda haki, jinsi alivyo tayari kusamehe, na subira yake. Baadaye, katika siku za Yoshua na kizazi kilichoishi wakati huo, taifa hilo lilitii amri za Yehova na likapata amani na baraka za kiroho. (Yos. 24:21, 22, 31) Kipindi hicho cha historia ya taifa la Israeli kilionyesha mafanikio ya utawala wa Yehova.
Matokeo Mabaya ya Utawala wa Wanadamu
8, 9. Ni ombi gani lisilo la hekima ambalo Waisraeli walitoa, na lilikuwa na matokeo gani?
8 Hata hivyo, baada ya muda, Waisraeli waliasi tena na tena utawala wa Mungu na wakapoteza ulinzi wake. Mwishowe, kupitia nabii Samweli, Waisraeli waliomba wawe na mfalme wa kibinadamu ambaye wangeweza kumwona. Yehova alimwambia Samweli awape mfalme kama walivyoomba. Hata hivyo, Yehova aliongezea hivi: “Hawakukukataa wewe, bali wamenikataa mimi nisiwe mfalme juu yao.” (1 Sam. 8:7) Ingawa Yehova aliwaruhusu Waisraeli wawe na mfalme ambaye wangeweza kumwona, aliwaonya kwamba utawala wa mfalme wa kibinadamu ungekuwa na matokeo mabaya.—Soma 1 Samweli 8:9-18.
9 Historia ilionyesha ukweli wa onyo ambalo Yehova alitoa. Waisraeli walipata matatizo makubwa walipotawaliwa na mfalme wa kibinadamu, hasa mfalme alipokosa kuwa mwaminifu. Tukifikiria mfano huo wa Waisraeli, haishangazi kwamba katika historia yote serikali zinazoongozwa na wanadamu ambao hawamjui Yehova zimeshindwa kuleta mafanikio yenye kudumu. Ni kweli kwamba wanasiasa fulani wanamwomba Mungu abariki jitihada zao za kupata amani na usalama, lakini Mungu anaweza jinsi gani kuwabariki wale ambao hawajitiishi chini ya utawala wake?—Zab. 2:10-12.
Taifa Jipya Chini ya Utawala wa Mungu
10. Kwa nini Yehova aliwakataa Waisraeli wasiwe taifa lake lililochaguliwa?
10 Taifa la Israeli halikutaka kumtumikia Mungu kwa uaminifu. Mwishowe, walimkataa Masihi aliyechaguliwa na Mungu, naye Yehova akawakataa na kuchagua kikundi kingine ambacho kingekuwa taifa jipya na kuchukua nafasi ya taifa la Israeli. Hivyo, kutaniko la Kikristo la waabudu wa Yehova waliotiwa mafuta lilianzishwa mwaka wa 33 W.K. Kwa kweli, kutaniko hilo lilikuwa taifa jipya ambalo lilitawaliwa na Yehova. Paulo aliliita taifa hilo “Israeli wa Mungu.”—Gal. 6:16.
11, 12. Taifa la Israeli linafanana jinsi gani na “Israeli wa Mungu” katika usimamizi?
11 Kuna mambo fulani yanayotofautiana na mengine yanayofanana kati ya taifa la Israeli na taifa jipya la “Israeli wa Mungu.” Tofauti na Israeli la kale, kutaniko la Kikristo halina mfalme wa kibinadamu na halihitaji kutoa dhabihu za wanyama kwa ajili ya watenda-dhambi. Mpango wa kuwa na wazee au wanaume wazee, ambao ulikuwapo katika taifa la Israeli upo pia katika kutaniko la Kikristo. (Kut. 19:3-8) Wazee hao Wakristo hawatawali kundi. Badala yake, wanalichunga kutaniko na wanajitoa kabisa katika kuongoza utendaji wa Kikristo. Wanashughulika kwa upendo na kila mtu kutanikoni, nao wanawaheshimu wote.—2 Kor. 1:24; 1 Pet. 5:2, 3.
12 Wanapotafakari kuhusu jinsi Mungu alivyoshughulika na taifa la Israeli, washiriki wa “Israeli wa Mungu” na waandamani wao, “kondoo wengine,” wanachochewa kumthamini zaidi Yehova na utawala wake. (Yoh. 10:16) Kwa mfano, historia inaonyesha kwamba watawala katika Israeli walikuwa na uvutano mkubwa sana juu ya raia wao, iwe ni uvutano mzuri au uvutano mbaya. Hilo linapaswa kuwakumbusha wale wanaoongoza kati ya Wakristo kwamba ingawa wao si watawala kama wafalme wa zamani, ni lazima sikuzote waweke mfano mzuri katika kuonyesha imani.—Ebr. 13:7.
Jinsi Yehova Anavyotawala Leo
13. Ni jambo gani la maana sana lililotukia mwaka wa 1914?
13 Leo, Wakristo wanautangazia ulimwengu kwamba utawala wa wanadamu unakaribia kukoma. Mwaka wa 1914, Yehova aliusimamisha Ufalme wake mbinguni chini ya Mfalme aliyemweka rasmi, Yesu Kristo. Wakati huo, alimpa Yesu mamlaka ya kwenda “akishinda na kukamilisha ushindi wake.” (Ufu. 6:2) Mfalme huyo mpya aliyetawazwa aliambiwa hivi: “Nenda ukitiisha katikati ya adui zako.” (Zab. 110:2) Inasikitisha kwamba mataifa yameendelea kukataa kujitiisha chini ya utawala wa Yehova. Yameendelea kutenda kana kwamba “hakuna Yehova.”—Zab. 14:1.
14, 15. (a) Ufalme wa Mungu unatutawala jinsi gani leo, na hivyo, tunapaswa kujiuliza maswali gani? (b) Ubora wa utawala wa Mungu unaonekana jinsi gani hata leo?
14 Leo, kuna washiriki wachache waliotiwa mafuta wa “Israeli wa Mungu,” na wakiwa ndugu za Yesu, wanaendelea kutenda wakiwa “mabalozi walio badala ya Kristo.” (2 Kor. 5:20) Wamewekwa rasmi kuwa jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara ili kutunza na kuwaandalia chakula cha kiroho watiwa-mafuta na umati unaoongezeka wa mamilioni ya Wakristo walio na tumaini la kuishi milele duniani. (Mt. 24:45-47; Ufu. 7:9-15) Ufanisi wa kiroho ambao waabudu wa kweli wanafurahia leo unaonyesha kwamba Yehova amebariki mpango huo.
15 Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, ninajua vizuri madaraka ambayo ninapaswa kutimiza katika kutaniko la Kikristo? Je, ninaunga mkono inavyofaa utawala wa Yehova? Je, ninajivunia kuwa raia wa Ufalme wa Yehova unaotawala? Je, nimeazimia kuendelea kuwaambia wengine kuhusu Ufalme wa Mungu kwa kadiri ninayoweza?’ Tukiwa kikundi, tunajitiisha kwa kupenda chini ya mwongozo unaotolewa na Baraza Linaloongoza na kushirikiana na wazee waliowekwa rasmi kutanikoni. Tunapofanya hivyo, tunaonyesha kwamba tunakubali utawala wa Mungu. (Soma Waebrania 13:17.) Kujitiisha kwa kupenda kunatokeza umoja wa ulimwenguni pote ambao ni wa pekee sana katika ulimwengu huu uliogawanyika. Pia, kunatokeza amani na uadilifu na kunamletea Yehova utukufu, na hivyo kuonyesha kwamba utawala wake ndio utawala bora kabisa.
Utawala wa Yehova Utashinda
16. Ni uamuzi gani ambao kila mtu anapaswa kufanya leo?
16 Wakati unakaribia sana ambapo masuala yaliyotokezwa katika Edeni yatatatuliwa. Kwa hiyo, huu ndio wakati wa watu kufanya uamuzi. Ni lazima kila mtu aamue ikiwa atakubali utawala wa Yehova au ataendelea kuunga mkono utawala wa wanadamu. Tuna pendeleo la kuwasaidia watu wapole wafanye uamuzi unaofaa. Hivi karibuni, wakati wa Har–Magedoni, utawala wa Yehova utaondoa kabisa serikali za wanadamu ambazo zinaongozwa na Shetani. (Dan. 2:44; Ufu. 16:16) Utawala wa wanadamu utakoma, na Ufalme wa Mungu utaitawala dunia yote. Bila shaka, kwa njia kamilifu kabisa, utawala wa Yehova utakuwa umethibitika kuwa bora.—Soma Ufunuo 21:3-5.
17. Ni mambo gani ya hakika ambayo yanawasaidia wapole wafanye uamuzi mzuri kuhusu utawala?
17 Wale ambao bado hawajaamua kuwa upande wa Yehova wanapaswa kusali na kufikiria faida ambazo utawala wa Mungu utawaletea wanadamu. Utawala wa wanadamu umeshindwa kusuluhisha tatizo la uhalifu, kutia ndani ugaidi. Utawala wa Mungu utaondoa waovu wote duniani. (Zab. 37:1, 2, 9) Utawala wa wanadamu umesababisha vita visivyokoma, lakini utawala wa Mungu ‘utakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.’ (Zab. 46:9) Zaidi ya hayo, utawala wa Mungu utarudisha pia amani kati ya wanadamu na wanyama! (Isa. 11:6-9) Umaskini na njaa ni mambo ya kawaida chini ya utawala wa wanadamu, lakini utawala wa Mungu utayaondoa. (Isa. 65:21) Hata watawala wa kibinadamu wenye nia nzuri wameshindwa kuondoa magonjwa na kifo, lakini chini ya utawala wa Mungu, wazee na wagonjwa watafurahi kurudishiwa nguvu za ujana. (Ayu. 33:25; Isa. 35:5, 6) Kwa kweli, dunia itakuwa paradiso na hata wafu watafufuliwa.—Luka 23:43; Mdo. 24:15.
18. Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunaamini kuwa utawala wa Mungu ndio utawala bora?
18 Ndiyo, utawala wa Mungu utaondoa madhara yote ambayo Shetani alisababisha alipowashawishi wazazi wetu wa kwanza wamwasi Muumba wao. Hebu wazia, Shetani amekuwa akisababisha madhara kwa miaka 6,000 hivi, lakini Mungu, kupitia Kristo, ataondoa madhara hayo katika kipindi cha miaka 1,000! Hilo linathibitisha kwa njia kubwa kama nini kwamba utawala wa Mungu ndio utawala bora zaidi! Tukiwa Mashahidi wa Mungu wetu, tunamkubali kuwa Mtawala wetu. Kwa hiyo, acheni tuonyeshe kila siku, ndiyo, kila saa ya maisha yetu kwamba sisi ni waabudu wa Yehova, raia wa Ufalme wake, na tunajivunia kuwa Mashahidi wake. Na acheni tutumie kila nafasi kumwambia kila mtu ambaye atatusikiliza kwamba utawala wa Yehova ndio utawala bora kabisa.
-