Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nimeona Nguvu za Kweli ya Biblia
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Desemba 15
    • Kazi ya Umishonari

      Migawo ya kwanza miwili ambayo tulifanya tukiwa pamoja ni kuwa mapainia wa pekee huko Geneva na Norwich, New York. Mnamo Agosti 1948, tulipata pendeleo la kuhudhuria darasa la 12 la Gileadi. Kisha, tulitumwa huko Naples, Italia, pamoja na wenzi wengine wamishonari, Carl na Joanne Ridgeway. Wakati huo, wakaaji wa mji wa Naples walikuwa wanajitahidi kurudia hali yao ya kawaida ya maisha baada ya uharibifu wa vita. Ilikuwa vigumu kupata nyumba, kwa hiyo kwa miezi michache, tuliishi katika nyumba ndogo yenye vyumba viwili.

      Nilipokuwa mtoto nilizoea kuwasikia wazazi wangu wakizungumza Kiitaliano kwa matamshi ya Naples, basi nilizungumza Kiitaliano ambacho kilieleweka vizuri ingawa nilizungumza kwa matamshi ya Kimarekani. Fern alikuwa na matatizo ya kujifunza lugha hiyo. Lakini lazima nikubali kwamba alijifunza lugha hiyo na kuijua vizuri sana hata kuliko mimi.

      Mwanzoni, watu waliopendezwa na kweli ambao tuliwapata huko Naples, walikuwa wa familia moja tu yenye watu wanne. Walikuwa wakiuza sigara ambazo zilikuwa haramu. Kila siku ya kazi, mshiriki mmoja wa familia hiyo, Teresa, alibadilika umbo kwa njia ya ajabu. Asubuhi, alionekana mnene kwa sababu alijaza sigara ndani ya mifuko mingi ya nguo aliyokuwa amevaa. Kufikia jioni alionekana mwembamba kama sindano. Kweli ilibadili kabisa familia hiyo. Mwishowe, washiriki 16 wa familia hiyo wakawa Mashahidi. Sasa kuna Mashahidi karibu 3,700 katika jiji la Naples.

      Kazi Yetu Inapingwa

      Baada ya kukaa Naples kwa miezi tisa tu, wenye mamlaka walitulazimisha sisi wanne kuondoka katika mji huo. Tulienda Uswisi kwa mwezi mmoja hivi, kisha tukarudi Italia tukiwa na viza ya watalii. Mimi na Fern tulipewa mgawo wa kwenda Turin. Mwanzoni, tulikodi chumba kutoka kwa mwanamke fulani, na tulitumia chumba chake cha kuogea na chumba chake cha kupikia. Ndugu na Dada Ridgeway walipofika Turin, tuliishi pamoja katika nyumba ya kukodi. Baada ya muda, wenzi kumi wamishonari, yaani, waume watano na wake zao, waliishi katika nyumba hiyohiyo.

      Kufikia 1955, wenye mamlaka walipotufanya tuondoke Turin, tulikuwa tumeweka msingi wa makutaniko manne mpya. Sasa ndugu wenye uwezo katika eneo hilo wangeweza kutunza makutaniko hayo. Wenye mamlaka walituambia hivi: “Tuna hakika kwamba baada ya ninyi Wamarekani kuondoka, kazi yote ambayo mmefanya itaporomoka kabisa.” Lakini ongezeko ambalo lilitokea baadaye lilionyesha kwamba mafanikio ya kazi yetu yanategemea Mungu. Leo, kuna Mashahidi zaidi ya 4,600 na makutaniko 56 huko Turin.

      Florence—Mji Mzuri Ajabu

      Mgawo wetu uliofuata ulikuwa huko Florence. Tulikuwa tumesikia mara nyingi kuhusu mji huo, kwa kuwa dada yangu Carmela na mume wake, Merlin Hartzler walipewa mgawo wa kutumika wakiwa wamishonari katika mji huo. Hata hivyo, jiwazie ukiishi huko. Maeneo kama vile Piazza della Signoria, Ponte Vecchio, Piazzale Michelangelo, na Palazzo Pitti yalifanya uwe mji mzuri ajabu! Lilikuwa jambo lenye kufurahisha kuona jinsi wakaaji fulani wa Florence walivyoitikia habari njema.

      Tulijifunza na familia moja, na wazazi wakabatizwa. Hata hivyo, baba yao alikuwa mvutaji wa sigara. Mwaka wa 1973, gazeti la Mnara wa Mlinzi lilisema wazi kwamba kuvuta sigara ni zoea chafu na likawahimiza wasomaji waache zoea hilo. Watoto wakubwa wa familia hiyo walimsihi baba yao aache kuvuta sigara. Aliahidi kwamba angeacha, lakini hakuacha. Jioni moja, mke wake aliwaambia watoto wake mapacha wenye umri wa miaka tisa waende kulala kabla hajasali pamoja nao. Baadaye, alisikia vibaya na akaenda katika chumba chao. Tayari kila mmoja alikuwa ametoa sala yake mwenyewe. Mama akawauliza hivi: “Mlisali kuhusu nini?” Wakasema: “Yehova, tafadhali msaidie Baba aache kuvuta sigara.” Mke huyo akamwita mume wake, “Kuja usikilize sala ya watoto wako.” Alipokuja, alianza kulia akasema, “Sitavuta sigara tena kamwe!” Alitimiza ahadi yake, na sasa watu zaidi ya 15 wa familia hiyo ni Mashahidi.

  • Nimeona Nguvu za Kweli ya Biblia
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Desemba 15
    • Kurudi Italia

      Kwa sababu ya ukarimu wa marafiki, tuliweza kupanda meli inayosafirisha ndizi na kurudi Italia ili kuhudhuria kusanyiko la kimataifa huko Turin mwaka wa 1961. Tulipata habari kwamba tungepata mgawo mwingine. Mnamo Septemba (Mwezi wa 9) 1962, tulirudi Italia, ambako nilianza kutumika nikiwa mwangalizi wa mzunguko. Tulinunua gari dogo, ambalo tulitumia kwa miaka mitano kutembelea mizunguko miwili.

      Baada ya kuishi katika joto la Afrika, sasa tulihitaji kuvumilia baridi kali. Wakati wa majira ya kwanza ya baridi kali, tulipokuwa tukitembelea kutaniko fulani chini ya milima ya Alps, tulilala katika chumba kisicho na mfumo wa kupasha joto, juu ya ghala la nyasi kavu. Baridi ilikuwa kali sana hivi kwamba tulilala tukiwa tumevaa makoti yetu. Usiku huo, kuku wanne na mbwa wawili walikufa katika ujirani kwa sababu ya baridi hiyo!

      Baadaye, nilitumika pia nikiwa mwangalizi wa wilaya. Katika miaka hiyo, tulitembea katika nchi yote ya Italia. Tulitembelea maeneo fulani mara nyingi kama vile Calabria na Sicily. Tuliwatia moyo watoto wakue kiroho na kujitahidi kufikia mapendeleo ya kutumika wakiwa waangalizi wa makutaniko, wahudumu wanaosafiri, au Wanabetheli.

      Tumejifunza mengi kutokana na marafiki waaminifu ambao wamemtumikia Yehova kwa moyo wote. Tumethamini sifa zao, kama vile ushikamanifu wao kamili kwa Yehova, ukarimu wao, upendo wao kwa ndugu zao, na roho ya kubadilika kulingana na hali na kujidhabihu kwao. Tumehudhuria arusi katika Majumba ya Ufalme. Arusi hizo zilifanywa na Mashahidi ambao wanatambuliwa kisheria kuwa wahudumu wa kidini, jambo ambalo zamani lilionekana haliwezekani nchini Italia. Makutaniko hayakutani tena katika vyumba vya kupikia vya akina ndugu wala hayaketi kwenye mbao, kama yalivyokuwa yakifanya huko Turin. Badala yake, makutaniko mengi yana Majumba maridadi ya Ufalme ambayo yanamletea Yehova heshima. Hatufanyi makusanyiko tena katika majumba madogo machafu, badala yake, tunakusanyika katika Majumba makubwa ya Kusanyiko. Tumepata shangwe kama nini kuona idadi ya wahubiri ikipita 243,000. Tulipofika Italia kulikuwa na wahubiri 490 pekee.

      Tulifanya Maamuzi Yanayofaa

      Tumekabili matatizo mbalimbali, kutia ndani magonjwa na kutamani kurudi nyumbani. Fern alitamani kurudi nyumbani kila mara alipoona bahari. Pia, amefanyiwa upasuaji mkubwa mara tatu. Pindi moja, alipokuwa akienda kuongoza funzo la Biblia, mpinzani fulani alimshambulia kwa uma mkubwa wa kukusanya nyasi. Alilazwa tena hospitalini kwa sababu ya shambulizi hilo.

      Ingawa nyakati nyingine tunavunjika moyo, tumekuwa ‘tukimngojea Yehova,’ kama andiko la Maombolezo 3:24 linavyosema. Yeye ndiye Mungu wa faraja. Wakati fulani tulipokuwa tumeshuka moyo, Fern alipokea barua nzuri sana kutoka kwa Ndugu Nathan Knorr. Aliandika kwamba kwa kuwa alizaliwa karibu na Bethlehem, Pennsylvania, ambako Fern alianzia upainia, alijua vyema kwamba wanawake wa eneo hilo wa asili ya Ujerumani, kama Fern, wana nguvu na hawakati tamaa. Alisema kweli. Kadiri ambavyo miaka imepita, tumetiwa moyo kwa njia nyingi na watu wengi.

      Ingawa tumekabili matatizo, tumejitahidi kudumisha bidii yetu katika huduma. Akilinganisha roho ya bidii na divai ya Italia inayoitwa Lambrusco, ambayo ni tamu na yenye kumetameta, Fern anasema hivi kwa utani: “Hatupaswi kuruhusu roho yetu iache kumetameta.” Baada ya kusafiri kwa miaka zaidi ya 40 katika kazi ya mzunguko na wilaya, tulipata pendeleo jipya la kutembelea na kupanga vikundi na makutaniko katika lugha nyingine mbali na Kiitaliano. Vikundi hivyo vinawahubiria watu kutoka Bangladesh, China, Eritrea, Ethiopia, Ghana, India, Nigeria, Sri Lanka, Ufilipino, na nchi nyingine. Kitabu hakiwezi kutoshea masimulizi yetu kuhusu njia nzuri ajabu ambazo tumeona nguvu za Neno la Mungu zikibadili maisha ya wale ambao wameonja rehema ya Yehova.—Mika 7:18, 19.

      Tunasali kila siku ili Yehova aendelee kutupatia nguvu za kimwili na za kihisia ambazo tunahitaji ili kutimiza huduma yetu. Shangwe ya Bwana ni nguvu yetu. Inafanya macho yetu yang’ae na inatusadikisha kwamba tumefanya maamuzi yanayofaa maishani tunapoeneza kweli ya Biblia.—Efe. 3:7; Kol. 1:29.

  • Nimeona Nguvu za Kweli ya Biblia
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Desemba 15
    • 1948

      Nikiwa huko South Lansing kwa ajili ya darasa la 12 la Gileadi

      1949

      Mimi na Fern kabla ya kwenda Italia

      Capri, Italia

      1952

      Tukiwa na wamishonari wengine huko Turin na Naples

      1963

      Fern akiwa na baadhi ya wanafunzi wake wa Biblia

      “Hatupaswi kuruhusu roho yetu iache kumetameta”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki