-
Kuna Tumaini Gani kwa Maskini?Amkeni!—2007 | Mei
-
-
Mungu Anapendezwa na Maskini
Muumba wa wanadamu, Yehova Mungu, hapendezwi na hali hiyo. Yehova anawahurumia maskini. Tunasoma hivi katika Biblia: “[Mungu] hatakisahau kilio cha wenye kuteseka.” (Zaburi 9:12) Yehova ni Mungu anayewajali maskini.
Kumhusu Yehova, Biblia inasema: “Mtu mwenye taabu, mvulana asiye na baba, anajikabidhi kwako. Wewe mwenyewe umekuwa msaidizi wake.” (Zaburi 10:14) Ona jinsi mstari huo wa Biblia unavyowataja wanaoteseka kama mtu mmoja-mmoja.a Naam, Mungu humtazama kila mtu na kufikiria mahitaji yake. Kwake kila mtu ana thamani na anastahili uangalifu. Yehova anawaalika watu wote wajifunze kumhusu na wafurahie urafiki wake haidhuru hali yao ya kiuchumi.
Jambo moja ambalo watu hujifunza kutoka kwa Mungu ni kuonyesha wengine huruma na hisia-mwenzi. Mashahidi wa Yehova hujiona kuwa familia kubwa ya kiroho. Wao huthaminiana, na kati yao kuna upendo wa kweli wa Kikristo. Wakati mmoja Bwana Yesu Kristo aliwaambia hivi wafuasi wake: “Ninyi nyote ni ndugu.” (Mathayo 23:8) Kwa hiyo, wote wanaokubali ibada ya kweli wanakuwa sehemu ya undugu usiobaguana kwa misingi ya utajiri. Kila mmoja humjali mwenzake, nao hutiana moyo nyakati za taabu.
Biblia ina kanuni zinazoweza kumsaidia mtu kupunguza madhara ya umaskini. Maandiko yanaonyesha kwamba Mungu hushutumu kuchafua mwili, kama vile kwa kutumia tumbaku na kutumia kileo vibaya. (Methali 20:1; 2 Wakorintho 7:1) Mtu anayeishi kupatana na kanuni hizo huweka akiba ya pesa ambazo zingepotezwa kupitia mazoea mabaya. Yeye huepuka magonjwa yanayosababishwa na uvutaji wa sigara na ulevi, na gharama ya matibabu ambayo ingesababishwa na magonjwa hayo. Pia Biblia inawafundisha watu kukataa kufikiri kwa njia ya kimwili na pupa. (Marko 4:19; Waefeso 5:3) Mtu anapoheshimu Neno la Mungu kuhusiana na mambo hayo, yeye huepuka pia kupoteza pesa zake kwa kucheza kamari.
Biblia hutoa kanuni zinazotusaidia kuishi vizuri hata tukiwa maskini. Ona mfano ufuatao:
Katika nchi ambayo watu wengi sana hawana kazi, mwanamke anayefanya kazi katika kiwanda fulani alihatarisha kazi yake kwa kuomba ruhusa ya kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Msimamizi wake angemwachisha kazi mara moja. Badala yake, alimshangaza mwanamke huyo na wafanyakazi wenzake kwa kumpa ruhusa. Isitoshe, msimamizi huyo alimwambia angependa aendelee kufanya kazi katika kiwanda chake na akamsifu kwa kuwa “mfanyakazi mzuri.” Kwa nini?
Mfanyakazi huyo ambaye ni Shahidi wa Yehova, anaishi kulingana na kanuni za Biblia. Akitamani “kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote,” hakusema uwongo au kuiba na hivyo akawa na sifa nzuri ya unyoofu. (Waebrania 13:18) Kupatana na kanuni iliyoongozwa kwa roho inayopatikana katika Wakolosai 3:22, 23, alifanya kazi yake “kwa nafsi yote.” Hilo linamaanisha alimtii mwajiri wake, na alihakikisha kwamba kila siku alifanya kazi kwa bidii ili astahili kulipwa.
Bila shaka, tunaishi katika mfumo wa kiuchumi ambao unaongozwa na ubinafsi na jambo kuu ni kupata faida. Huenda wengine ambao wanaheshimu sana kanuni za Biblia wakahitaji kung’ang’ana ili kupata chakula, mavazi, na makao wanayohitaji. Lakini wana dhamiri safi mbele za Muumba nao wanatazamia kwa uhakika kwamba kutakuwa na wakati ujao mzuri, kwa sababu Yehova ni “Mungu anayetoa tumaini.”—Waroma 15:13.
-
-
Kuna Tumaini Gani kwa Maskini?Amkeni!—2007 | Mei
-
-
a Mistari mingine miwili ya Biblia inayozungumzia jinsi Mungu anavyowahangaikia watu wanaoteseka ni Zaburi 35:10 na Zaburi 113:7.
-