-
Ulimwengu Usio na Umaskini UnakaribiaMnara wa Mlinzi—2005 | Mei 15
-
-
Yehova Mungu huwajali maskini. (Ona sanduku lenye kichwa “Mungu Huwaonaje Maskini?”) Kwa upendo, ameandaa mipango ya kuwasaidia watu walio kama Tukiso na Maseiso wajifunze mengi zaidi juu yake. Na katika Neno lake, ametoa mashauri yanayoweza kutumiwa maishani.
Mipango Yenye Manufaa
Sikuzote, Mashahidi wa Yehova wamejitahidi kuiga mfano wa Mungu wa kuwajali maskini. (Wagalatia 2:10) Wakristo wa kweli wanapoathiriwa na msiba katika nchi fulani, mara nyingi mipango hufanywa ili kuwasaidia. Jambo la maana zaidi ni kwamba Mashahidi huhangaikia mahitaji ya kiroho ya watu wote, kutia ndani maskini. (Mathayo 9:36-38) Katika miaka 60 iliyopita, maelfu ya wahudumu waliozoezwa wamejitolea kuwa wamishonari katika nchi nyingine. Kwa mfano, mume na mke wamishonari kutoka Ufini walijifunza Kisotho na hivyo wakawafundisha Tukiso na Maseiso wawe wanafunzi wa Yesu. (Mathayo 28:19, 20) Mara nyingi wamishonari hujinyima maisha ya starehe katika nchi zenye ufanisi na kuhamia nchi zenye umaskini.
Wakristo wa kweli hawapaswi kuiba ili kupata riziki. Badala yake, wanaamini kwamba Yehova Mungu anaweza kutosheleza mahitaji yao. (Waebrania 13:5, 6) Njia moja ambayo Yehova hutumia kutosheleza mahitaji ya watu wake ni undugu wa ulimwenguni pote wa waabudu wake ambao hutunzana.
Pia, Yehova huwasaidia maskini kwa kuwapa mashauri wanayoweza kutumia maishani. Kwa mfano, Biblia inaamuru hivi: “Mwizi asiibe tena, bali afanye kazi ya bidii, akifanya kwa mikono yake kazi iliyo njema, ili awe na kitu cha kumgawia mtu aliye na uhitaji.” (Waefeso 4:28) Watu wengi wasioajiriwa wameamua kuanzisha kazi zao na kufanya kazi ngumu, kama vile kupanda mboga katika bustani. Isitoshe, Biblia huwasaidia maskini kuweka akiba ya pesa kwa kuwafundisha kuepuka mazoea mabaya, kama vile ulevi.—Waefeso 5:18.
-
-
Ulimwengu Usio na Umaskini UnakaribiaMnara wa Mlinzi—2005 | Mei 15
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6, 7]
MUNGU HUWAONAJE MASKINI?
Biblia inamfafanua Muumba wa wanadamu kuwa “Yeye anayewapa wenye njaa mkate.” (Zaburi 146:7) Ina mistari zaidi ya mia moja inayoonyesha kwamba Mungu anawajali maskini.
Kwa mfano, Yehova alipowapa Waisraeli wa kale Sheria yake, aliwaamuru wakulima Waisraeli wasivune kabisa kingo za mashamba yao. Hawakupaswa kukusanya matunda yaliyosalia kwa kupitia tena mzeituni au mzabibu. Sheria hizo zilikuwa maandalizi yenye upendo kwa wageni, mayatima, wajane, na watu wengine walioteseka.—Mambo ya Walawi 19:9, 10; Kumbukumbu la Torati 24:19-21.
Zaidi ya hayo, Mungu aliwaamuru Waisraeli hivi: “Msimtese mjane yeyote wala mvulana asiye na baba. Mkimtesa hata kidogo, naye anililie hata kidogo, sitakosa kukisikia kilio chake; nayo hasira yangu itawaka kwelikweli, nami hakika nitawaua kwa upanga, na wake zenu watakuwa wajane, nao wana wenu watakuwa wavulana wasio na baba.” (Kutoka 22:22-24) Kwa kusikitisha, matajiri wengi Waisraeli walipuuza maneno hayo. Kwa sababu ya kosa hilo na makosa mengineyo, Yehova Mungu aliwaonya Waisraeli kupitia manabii wake. (Isaya 10:1, 2; Yeremia 5:28; Amosi 4:1-3) Hatimaye, Mungu aliwafanya Waashuru na baadaye Wababiloni watwae maeneo ya Waisraeli. Waisraeli wengi waliuawa, na waokokaji wakapelekwa katika mataifa mengine wakiwa mateka.
Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, aliwahangaikia maskini kwa upendo kama Baba yake. Yesu alisema hivi kuhusu kusudi la huduma yake: “Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta kuwatangazia maskini habari njema.” (Luka 4:18) Hiyo haimaanishi kwamba Yesu aliwahudumia maskini tu. Aliwasaidia matajiri pia. Lakini, alipofanya hivyo, mara nyingi alionyesha kwamba anawahangaikia maskini. Kwa mfano, alimshauri hivi mtawala mmoja tajiri: “Uza vitu vyote ulivyo navyo uwagawie maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha uje uwe mfuasi wangu.”—Luka 14:1, 12-14; 18:18, 22; 19:1-10.
Yehova Mungu na Mwana wake huwajali sana maskini. (Marko 12:41-44; Yakobo 2:1-6) Yehova anaonyesha kwamba anawajali maskini kwa kuwakumbuka mamilioni ya maskini waliokufa. Wote hao watafufuliwa katika ulimwengu mpya usio na umaskini.—Matendo 24:15.
-