Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ‘Lo! Kina cha Hekima ya Mungu!’
    Mkaribie Yehova
    • Uthibitisho wa Hekima ya Mungu

      9, 10. (a) Yehova ana hekima ya aina gani, naye ameionyeshaje? (b) Chembe huthibitishaje hekima ya Yehova?

      9 Je, umewahi kustaajabia ustadi wa fundi anayetengeneza vifaa maridadi vinavyofanya kazi vizuri? Hekima hiyo inavutia sana. (Kutoka 31:1-3) Yehova mwenyewe ndiye chanzo hasa cha hekima hiyo. Mfalme Daudi alisema hivi kumhusu Yehova: “Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, na nafsi yangu yajua sana.” (Zaburi 139:14) Kwa kweli, kadiri tunavyojifunza kuhusu mwili wa mwanadamu, ndivyo tunavyozidi kutiwa kicho na hekima ya Yehova.

      10 Kwa mfano: Uhai wako ulianza kwa chembe moja—mbegu ya mama yako iliungana na mbegu ya baba yako. Baada ya muda, chembe hiyo ilianza kugawanyika. Mwishowe mwili wako ukawa na chembe ndogo sana zipatazo trilioni 100. Chembe 10,000 hivi zenye ukubwa wa wastani zinaweza kutoshea kwenye kichwa kidogo sana cha pini. Lakini, kila chembe ina umbo tata sana. Chembe moja ni tata sana kushinda kiwanda au mashine yoyote iliyotengenezwa na mwanadamu. Wanasayansi wanasema kwamba chembe moja ni kama jiji lililozingirwa na ukuta—lenye malango yanayolindwa, lenye mfumo wa usafiri, mfumo wa mawasiliano, mitambo ya nguvu, viwanda, mifumo ya kuondoa na kusafisha maji machafu, walinzi, na hata kuna aina fulani ya makao makuu ya serikali katika kiini chake. Isitoshe, chembe inaweza kutengeneza chembe nyingine pacha kwa saa chache tu!

      11, 12. (a) Ni nini kinachofanya chembe za kiini-tete kinachokua zigawanyike, na hilo linapatanaje na Zaburi 139:16? (b) Ubongo wa mwanadamu unaonyeshaje kwamba ‘tumeumbwa kwa jinsi ya ajabu’?

      11 Bila shaka chembe zote hazifanani. Chembe za kiini-tete zinapoendelea kugawanyika, chembe mpya zinafanya kazi mbalimbali. Baadhi yake zitakuwa chembe za neva; nyingine zitakuwa chembe za mifupa, misuli, damu, au za macho. Utaratibu huo wa kugawanyika kwa chembe umehifadhiwa kiasili katika “maktaba” yenye ramani za chembe za urithi, DNA. Inastaajabisha kwamba Daudi aliongozwa kumwambia Yehova hivi: “Wewe uliniona hata kabla sijazaliwa, uliandika kila kitu kitabuni mwako.”—Zaburi 139:16, BHN.

      12 Viungo fulani vya mwili ni tata kupindukia. Kwa mfano, fikiria ubongo wa mwanadamu. Baadhi ya watu wamesema kwamba ubongo ndicho kitu tata zaidi katika ulimwengu wote. Una chembe za neva zipatazo bilioni 100—idadi hiyo inakaribia idadi ya nyota katika kundi letu la nyota. Kila moja ya chembe hizo inaungana na maelfu ya chembe nyingine. Wanasayansi wanasema kwamba ubongo wa mwanadamu unaweza kuhifadhi habari zilizo katika maktaba zote ulimwenguni na kwamba uwezo wake haupimiki. Licha ya kuchunguza kwa miaka mingi sana ubongo ‘ulioumbwa kwa jinsi ya ajabu,’ wanasayansi wanakubali kwamba huenda wasifaulu kamwe kufahamu kikamili jinsi unavyofanya kazi.

      13, 14. (a) Chungu na viumbe wengine wanaonyeshaje kwamba wana “akili nyingi sana,” na hilo linatufundisha nini kumhusu Muumba? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba vitu vilivyoumbwa kama vile utando wa buibui vimefanywa “kwa hekima”?

      13 Lakini wanadamu ni mojawapo tu ya mambo yanayoonyesha hekima ya Yehova ya uumbaji. Zaburi 104:24 yasema hivi: “Ee, BWANA, jinsi yalivyo mengi matendo yako! Kwa hekima umevifanya vyote pia. Dunia imejaa mali zako.” Kila kiumbe kinadhihirisha hekima ya Yehova. Kwa mfano, chungu ana “akili nyingi sana.” (Mithali 30:24) Kwa kweli, makundi ya chungu yana utaratibu wa hali ya juu sana. Makundi fulani ya chungu hutunza, hufuga, na kupata chakula kutoka kwa wadudu fulani kana kwamba ni mifugo. Chungu wengine ni kama wakulima, wanapanda “mimea” ya kuvu. Viumbe wengine wengi wanafanya mambo yenye kustaajabisha kwa kutumia hekima ya kisilika. Nzi wa kawaida huruka kwa njia za kustaajabisha sana ambazo ndege bora ya kisasa iliyobuniwa na mwanadamu haiwezi. Ndege wanaohama huongozwa na nyota, nguvu za sumaku za dunia, au aina fulani ya ramani iliyo akilini mwao. Wanabiolojia hujifunza kwa miaka mingi tabia tata za kisilika za viumbe hao. Mungu aliyeumba viumbe hao ana hekima iliyoje!

      14 Wanasayansi wamejifunza mengi kutokana na hekima ya Yehova ya uumbaji. Hata kuna elimu fulani ya uhandisi inayojaribu kuiga ubuni wa maumbile inayoitwa biomimetics. Kwa mfano, labda umewahi kustaajabia umaridadi wa utando wa buibui. Lakini mhandisi anaona kwamba utando huo umebuniwa kwa njia ya pekee sana. Tando fulani nyembamba ni ngumu kuliko chuma, ni ngumu kushinda nyuzi za mavazi yasiyopenywa na risasi. Ni ngumu kadiri gani? Hebu wazia utando wa buibui uliorefushwa kufikia ukubwa wa wavu unaovutwa na mashua ya uvuvi. Utando wa aina hiyo ungeweza kusimamisha ndege ya abiria inayosafiri kwa kasi angani! Naam, Yehova amefanya vitu hivyo vyote “kwa hekima.”

      Ubuni na hekima ya kisilika iliyo katika viumbe wa Mungu: utando wa buibui, chungu wenye utaratibu wakibeba vipande vya majani, bata-bukini wakihama pamoja

      Ni nani aliyeumba viumbe hawa ambao wana “akili nyingi sana”?

      Hekima ya Vitu Visivyo Duniani

      15, 16. (a) Nyota zinatoa uthibitisho gani kuhusu hekima ya Yehova? (b) Wadhifa wa Yehova akiwa Amiri Mkuu wa malaika wengi sana unaonyesha nini kuhusu hekima yake akiwa Msimamizi?

      15 Hekima ya Yehova inaonekana wazi katika kazi zake ulimwenguni pote. Nyota ambazo tulizungumzia kwa undani katika Sura ya 5, hazijatapakaa kiholela-holela angani. Yehova amepanga nyota kwa njia maridadi sana katika magalaksi, kwa kutumia hekima yake ya “sheria za angani.” Magalaksi hayo yamepangwa katika makundi makubwa, ambayo huungana na kufanyiza makundi mengine makubwa hata zaidi. (Ayubu 38:33, The New Jerusalem Bible) Si ajabu Yehova anasema kwamba nyota zilizo mbinguni ni kama “jeshi”! (Isaya 40:26) Hata hivyo, kuna jeshi jingine ambalo linaonyesha wazi zaidi hekima ya Yehova.

  • ‘Lo! Kina cha Hekima ya Mungu!’
    Mkaribie Yehova
Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki