-
‘Nendeni Mkafanye Wanafunzi, Mkiwabatiza’Mnara wa Mlinzi—2006 | Aprili 1
-
-
‘Nendeni Mkafanye Wanafunzi, Mkiwabatiza’
“Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza . . . , na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”—MATHAYO 28:19, 20.
1. Taifa la Israeli lilifanya uamuzi gani chini ya Mlima Sinai?
YAPATA miaka 3,500 iliyopita, taifa zima liliweka nadhiri kwa Mungu. Wakiwa wamekusanyika chini ya Mlima Sinai, Waisraeli walitangaza hivi waziwazi: “Yote ambayo Yehova amesema tuko tayari kuyafanya.” Kuanzia wakati huo, Waisraeli wakawa watu waliowekwa wakfu kwa Mungu, “mali [yake] ya pekee.” (Kutoka 19:5, 8; 24:3) Walitazamia kupata ulinzi wake, na vizazi vyao vyote vingeishi katika nchi “inayotiririka maziwa na asali.”—Mambo ya Walawi 20:24.
2. Watu wanaweza kuwa na uhusiano gani pamoja na Mungu leo?
2 Hata hivyo, kama mtunga-zaburi Asafu alivyotaja, Waisraeli ‘hawakulishika agano la Mungu, nao walikataa kutembea katika sheria yake.’ (Zaburi 78:10) Hawakutimiza nadhiri ambayo mababu zao waliweka kwa Yehova. Mwishowe, taifa hilo lilipoteza uhusiano wa pekee ambao mababu zao walikuwa nao pamoja na Mungu. (Mhubiri 5:4; Mathayo 23:37, 38) Hivyo, Mungu ‘alielekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake.’ (Matendo 15:14) Na katika siku hizi za mwisho, Mungu anakusanya “umati mkubwa, ambao hakuna mtu [anayeweza] kuuhesabu, kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha,” na umati huo unasema hivi kwa shangwe: “Wokovu unatoka kwa Mungu wetu, anayeketi juu ya kiti cha ufalme, na Mwana-Kondoo.”—Ufunuo 7:9, 10.
3. Ni hatua gani ambazo mtu anahitaji kuchukua ili awe na uhusiano pamoja na Mungu?
3 Ili kuwa miongoni mwa wale walio na uhusiano huo wenye thamani pamoja na Mungu, ni lazima mtu ajiweke wakfu kwa Yehova na kuonyesha wakfu huo hadharani kwa kubatizwa ndani ya maji. Kufanya hivyo ni kutii amri hii ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20) Waisraeli walisikiliza wakati “kitabu cha agano” kiliposomwa. (Kutoka 24:3, 7, 8) Hivyo, walielewa yale ambayo Yehova alitaka wafanye. Vivyo hivyo leo, kabla mtu hajachukua hatua ya kubatizwa, anahitaji kupata ujuzi sahihi kuhusu mapenzi ya Mungu ambao unapatikana katika Neno lake, Biblia.
4. Ni lazima mtu afanye nini ili astahili kubatizwa? (Tia ndani sanduku lililo hapa juu.)
4 Ni wazi kwamba Yesu alitaka wanafunzi wake wawe na msingi thabiti wa imani kabla ya kubatizwa. Aliwaagiza wafuasi wake waende na kufanya wanafunzi na vilevile kuwafundisha ‘kushika mambo yote ambayo aliamuru.’ (Mathayo 7:24, 25; Waefeso 3:17-19) Hivyo, kwa kawaida wale wanaostahili kubatizwa huwa wamejifunza Biblia kwa miezi kadhaa au hata kwa mwaka mmoja au miwili ili wasifanye uamuzi haraka au bila kufikiri. Wakati wa ubatizo, wale wanaotaka kubatizwa huulizwa maswali mawili ya msingi, nao hujibu kwa kusema ndiyo. Kwa kuwa Yesu alikazia kwamba ‘neno letu Ndiyo linapaswa kumaanisha Ndiyo, na Siyo yetu, Siyo,’ inafaa sote tuchunguze kwa makini maana ya maswali hayo mawili ya ubatizo.—Mathayo 5:37.
Toba na Wakfu
5. Swali la kwanza la ubatizo linakazia hatua gani mbili muhimu?
5 Katika swali la kwanza la ubatizo, yule anayetaka kubatizwa huulizwa ikiwa ametubu kuhusiana na mambo aliyofanya zamani na ikiwa amejiweka wakfu kwa Yehova ili kufanya mapenzi yake. Swali hilo linakazia hatua mbili muhimu ambazo mtu anahitaji kuchukua kabla ya kubatizwa, yaani, toba na wakfu.
6, 7. (a) Kwa nini ni lazima wote wanaotaka kubatizwa watubu? (b) Ni lazima mtu afanye mabadiliko gani baada ya kutubu?
6 Kwa nini ni lazima mtu atubu kabla ya kubatizwa? Mtume Paulo anaeleza hivi: “Wakati fulani sisi sote tulijiendesha . . . kupatana na tamaa za mwili wetu.” (Waefeso 2:3) Kabla ya kupata ujuzi sahihi wa mapenzi ya Mungu, tuliishi kupatana na ulimwengu, kulingana na maadili yake na viwango vyake. Maisha yetu yaliongozwa na mungu wa mfumo huu, Shetani. (2 Wakorintho 4:4) Hata hivyo, baada ya kujua mapenzi ya Mungu, tunaazimia kuishi “si kwa ajili ya tamaa za wanadamu tena, bali kwa ajili ya mapenzi ya Mungu.”—1 Petro 4:2.
7 Maisha hayo mapya huleta faida nyingi. Kwanza kabisa, yanatuwezesha kuwa na uhusiano wenye thamani pamoja na Yehova, ambao Daudi aliulinganisha na mwaliko wa kuingia katika “hema” la Mungu na “mlima [wake] mtakatifu.” Hilo ni pendeleo kubwa ajabu! (Zaburi 15:1) Yehova hamkaribishi mtu yeyote bali anawakaribisha wale tu ‘wanaotembea bila kosa na kuzoea kutenda uadilifu na kusema kweli katika moyo wao.’ (Zaburi 15:2) Kwa kuwa tulikuwa katika hali mbalimbali kabla ya kujifunza kweli, ili tutimize matakwa hayo huenda tukalazimika kufanya mabadiliko fulani katika mwenendo na utu wetu. (1 Wakorintho 6:9-11; Wakolosai 3:5-10) Kile kinachomchochea mtu afanye mabadiliko hayo ni toba, yaani, kujutia kabisa maisha yetu ya zamani na kuazimia kwa bidii kumpendeza Yehova. Toba humwongoza mtu ageuke kabisa, yaani, aache maisha ya kilimwengu ya ubinafsi na kufuata njia inayompendeza Mungu.—Matendo 3:19.
8. Sisi hujiwekaje wakfu, na kujiweka wakfu kunahusianaje na ubatizo?
8 Katika sehemu ya pili ya swali la kwanza la ubatizo, wale wanaotaka kubatizwa huulizwa ikiwa wamejiweka wakfu kwa Yehova ili wafanye mapenzi yake. Wakfu ni hatua muhimu ambayo inapaswa kutangulia ubatizo. Hatua hiyo hufanywa kupitia sala, na katika sala hiyo tunaeleza tamaa yetu ya kutoa maisha yetu kwa Yehova kupitia Kristo. (Waroma 14:7, 8; 2 Wakorintho 5:15) Kisha, Yehova anakuwa Bwana wetu na Mmiliki wetu, nasi tunafurahia kufanya mapenzi ya Mungu kama Yesu. (Zaburi 40:8; Waefeso 6:6) Ahadi hiyo nzito inayotolewa kwa Yehova hufanywa mara moja tu. Hata hivyo, kwa kuwa tunajiweka wakfu faraghani, siku ya ubatizo tunafanya tangazo la hadharani ili kuwaonyesha watu wote kwamba tumechukua hatua hiyo nzito ya kujiweka wakfu kwa Baba yetu wa mbinguni.—Waroma 10:10.
9, 10. (a) Mapenzi ya Mungu yanahusisha nini? (b) Maofisa wa Nazi walitambuaje kwamba tumejiweka wakfu?
9 Kuiga kielelezo cha Yesu cha kufanya mapenzi ya Mungu kunahusisha nini? Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuuchukua mti wake wa mateso na kunifuata sikuzote.” (Mathayo 16:24) Hapa Yesu alitaja mambo matatu ambayo ni lazima tuyafanye. Kwanza, ‘tunajikana’ wenyewe, yaani, tunaacha mielekeo yetu ya ubinafsi ya kutokamilika, na badala yake tunakubali shauri na mwongozo wa Mungu. Pili, ‘tunauchukua mti wetu wa mateso.’ Katika siku za Yesu, mti wa mateso uliwakilisha aibu na kuteseka. Kwa kuwa sisi ni Wakristo, tunakubali kuteseka kwa ajili ya habari njema. (2 Timotheo 1:8) Ingawa watu katika ulimwengu wanaweza kutudhihaki au kutushutumu, sisi ‘hudharau aibu’ kama Kristo, nasi tunapata furaha kwa kujua kwamba tunampendeza Mungu. (Waebrania 12:2) Mwishowe, tunamfuata Yesu “sikuzote.”—Zaburi 73:26; 119:44; 145:2.
10 Inapendeza kwamba hata wapinzani fulani hutambua kuwa Mashahidi wa Yehova wamejiweka wakfu kwa Mungu ili wamtumikie kwa moyo wote. Kwa mfano, katika kambi ya mateso ya Buchenwald wakati wa utawala wa Nazi huko Ujerumani, Mashahidi waliokataa kukana imani yao walipaswa kutia sahihi taarifa hii iliyochapishwa: “Bado mimi ni Mwanafunzi wa Biblia mwaminifu, nami sitavunja kamwe kiapo changu mbele za Yehova.” Bila shaka, maneno hayo yanaonyesha wazi mtazamo wa watumishi wote waaminifu wa Mungu waliojiweka wakfu!—Matendo 5:32.
Kutambulishwa Kuwa Mmoja wa Mashahidi wa Yehova
11. Mtu anayebatizwa anapata pendeleo gani?
11 Katika sehemu ya kwanza ya swali la pili, yule anayetaka kubatizwa huulizwa ikiwa anaelewa kwamba ubatizo wake unamtambulisha kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Baada ya kubatizwa, anakuwa mhudumu aliyewekwa rasmi ambaye anatambulishwa kwa jina la Yehova. Hilo ni pendeleo kubwa na daraka zito. Isitoshe, linamwezesha yule anayebatizwa awe na tazamio la kupata wokovu wa milele, maadamu anabaki mwaminifu kwa Yehova.—Mathayo 24:13.
12. Heshima ya kutambulishwa kwa jina la Yehova huleta daraka gani?
12 Bila shaka, ni heshima kubwa sana kutambulishwa kwa jina la Mungu mweza-yote, Yehova. Nabii Mika alisema hivi: “Vikundi vyote vya watu vitatembea kila kimoja katika jina la mungu wake; bali sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.” (Mika 4:5) Hata hivyo, heshima hiyo huleta daraka fulani. Tunahitaji kuishi kwa njia inayoleta heshima kwa Yehova, yule ambaye tunatambulishwa kwa jina lake. Paulo aliwakumbusha Wakristo huko Roma kwamba ikiwa mtu hatendi yale anayohubiri, jina la Mungu “linafanyiwa makufuru,” au kuchafuliwa.—Waroma 2:21-24.
13. Kwa nini watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu wana daraka la kutoa ushahidi kuhusu Mungu wao?
13 Mtu anapokuwa Shahidi wa Yehova, anakubali pia daraka la kutoa ushahidi kuhusu Mungu wake. Yehova aliwaalika watu wa taifa la Israeli waliojiweka wakfu wawe mashahidi wake, ili watoe ushahidi kuhusu Uungu wake wa milele. (Isaya 43:10-12, 21) Lakini taifa hilo lilishindwa kutimiza daraka hilo, na mwishowe likapoteza kabisa kibali cha Yehova. Leo, Wakristo wa kweli wanajivunia pendeleo la kutoa ushahidi kumhusu Yehova. Tunafanya hivyo kwa sababu tunampenda na tunatamani jina lake litakaswe. Je, kweli tunaweza kunyamaza huku tukijua ukweli kuhusu Baba yetu wa mbinguni na kusudi lake? Tunahisi kama mtume Paulo, wakati aliposema: “Nimewekewa sharti. Kwa kweli, ole wangu mimi ikiwa sitangazi habari njema!”—1 Wakorintho 9:16.
14, 15. (a) Tengenezo la Yehova hutusaidiaje kufanya maendeleo ya kiroho? (b) Ni maandalizi gani yanayotusaidia kiroho?
14 Katika swali la pili, yule anayetaka kubatizwa anakumbushwa pia kuhusu daraka lake la kushirikiana na tengenezo la Yehova linaloongozwa kwa roho. Hatuwezi kujitenga na wengine tunapomtumikia Mungu, nasi tunahitaji kusaidiwa, kutegemezwa, na kutiwa moyo na “ushirika mzima wa akina ndugu.” (1 Petro 2:17; 1 Wakorintho 12:12, 13) Tengenezo la Mungu linatimiza daraka muhimu katika maendeleo yetu ya kiroho. Linaandaa habari nyingi za Biblia zilizochapishwa ambazo zinatusaidia kuongeza ujuzi sahihi, kutenda kwa hekima tunapokabili matatizo, na kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Kama mama anayehakikisha kwamba mtoto wake amelishwa vizuri na kutunzwa, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” huandaa chakula tele cha kiroho kwa wakati unaofaa ili tufanye maendeleo ya kiroho.—Mathayo 24:45-47; 1 Wathesalonike 2:7, 8.
15 Kwenye mikutano ya kila juma, watu wa Yehova huzoezwa na kutiwa moyo wawe Mashahidi wa Yehova waaminifu. (Waebrania 10:24, 25) Shule ya Huduma ya Kitheokrasi hutufundisha kuzungumza mbele ya watu, na Mkutano wa Utumishi hutuzoeza kutangaza ujumbe wetu kwa njia yenye matokeo. Tunapohudhuria mikutano yetu na kujifunza kibinafsi habari za Biblia zilizochapishwa, tunaona roho ya Yehova ikifanya kazi ili kuongoza tengenezo lake. Kupitia maandalizi hayo yanayotolewa kwa ukawaida, Mungu hutuonyesha hatari, hutuzoeza kuwa wahudumu stadi, na kutusaidia tuendelee kukesha kiroho.—Zaburi 19:7, 8, 11; 1 Wathesalonike 5:6, 11; 1 Timotheo 4:13.
Nia ya Kufanya Uamuzi wa Kubatizwa
16. Ni nini kinachotuchochea kujiweka wakfu kwa Yehova?
16 Kwa hiyo, yale maswali mawili ya ubatizo yanawakumbusha wale wanaotaka kubatizwa maana ya ubatizo wa maji na madaraka yanayotokana na hatua hiyo. Basi, wanapaswa kuwa na nia gani wanapofanya uamuzi wa kubatizwa? Tunakuwa wanafunzi waliobatizwa, si kwa sababu mtu ametulazimisha, bali kwa sababu Yehova ‘anatuvuta.’ (Yohana 6:44) Kwa kuwa “Mungu ni upendo,” anatawala kwa upendo, wala si kwa mabavu. (1 Yohana 4:8) Sisi huvutwa kwa Yehova kwa sababu ya sifa zake nzuri na jinsi anavyotutendea. Yehova alimtoa Mwana wake mzaliwa-pekee kwa ajili yetu, naye anatuahidi maisha bora wakati ujao. (Yohana 3:16) Hivyo, tunachochewa kumpa maisha yetu, naam, kuyaweka wakfu kwake.—Methali 3:9; 2 Wakorintho 5:14, 15.
17. Hatukujiweka wakfu kwa mambo gani?
17 Sisi hujiweka wakfu, si kwa lengo fulani wala kwa kazi fulani, bali kwa Yehova mwenyewe. Kazi ambayo Mungu amewapa watu wake itabadilika, lakini wakfu wao kwake hauwezi kubadilika. Kwa mfano, mgawo ambao Yehova alimpa Abrahamu ni tofauti sana na ule aliompa Yeremia. (Mwanzo 13:17, 18; Yeremia 1:6, 7) Lakini, watu hao wawili walitimiza kazi hususa ambayo Mungu aliwapa kwa sababu walimpenda Yehova na walitaka kufanya mapenzi yake kwa uaminifu. Katika wakati huu wa mwisho, wafuasi wote wa Kristo waliobatizwa hujitahidi kutimiza amri ya Kristo ya kuhubiri habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Kufanya kazi hiyo kwa moyo wote ni njia nzuri ya kuonyesha kwamba tunampenda Baba yetu wa mbinguni na kwamba tumejiweka wakfu kwake.—1 Yohana 5:3.
18, 19. (a) Tunapobatizwa, sisi hutoa taarifa gani hadharani? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?
18 Bila shaka, ubatizo humwezesha mtu kupata baraka nyingi, lakini hiyo ni hatua inayopaswa kufikiriwa kwa uzito. (Luka 14:26-33) Inaonyesha azimio ambalo linapaswa kutangulizwa kabla ya madaraka mengine yote. (Luka 9:62) Tunapobatizwa, tunatoa taarifa hii hadharani: “Mungu huyu ni Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele. Yeye mwenyewe atatuongoza mpaka tufe.”—Zaburi 48:14.
19 Makala inayofuata itazungumzia maswali mengine yanayoweza kutokea kuhusiana na ubatizo wa maji. Je, mtu anaweza kuwa na sababu nzuri za kuepuka kubatizwa? Je, umri unapaswa kufikiriwa? Sote tunaweza kufanya nini ili kufanya pindi ya ubatizo iwe yenye kuheshimika?
-
-
Kutimiza Matakwa ya Ubatizo wa KikristoMnara wa Mlinzi—2006 | Aprili 1
-
-
Kutimiza Matakwa ya Ubatizo wa Kikristo
“Ni nini kinachonizuia nisibatizwe?”—MATENDO 8:36.
1, 2. Filipo alianzishaje mazungumzo pamoja na ofisa mmoja Mwethiopia, na nini kinachoonyesha kwamba mtu huyo alipendezwa na mambo ya kiroho?
MWAKA mmoja au miwili hivi baada ya kifo cha Yesu, ofisa mmoja wa serikali alikuwa akisafiri kuelekea kusini kwenye barabara iliyotoka Yerusalemu mpaka Gaza. Bado alihitaji kusafiri kilometa 1,500 hivi akitumia gari la kukokotwa. Hiyo ilikuwa safari yenye kuchosha kweli! Mtu huyo aliyemwogopa Mungu alikuwa amesafiri mbali sana, kutoka Ethiopia hadi Yerusalemu, ili kumwabudu Yehova. Alipokuwa katika safari ndefu ya kurudi, alitumia vizuri wakati wake kwa kusoma Neno la Mungu. Naam, alikuwa na imani kwelikweli. Yehova alimtambua mtu huyo mnyoofu, na kupitia malaika, Akamwongoza mwanafunzi Filipo amhubirie.—Matendo 8:26-28.
2 Ilikuwa rahisi kwa Filipo kuanzisha mazungumzo kwa kuwa ofisa huyo Mwethiopia alikuwa akisoma kwa sauti kubwa, kama ilivyokuwa desturi wakati huo. Hivyo, Filipo alimsikia akisoma kitabu cha kukunjwa cha Isaya. Filipo aliamsha upendezi wa mtu huyo kwa kuuliza swali moja rahisi: “Je, wewe kwa kweli unaelewa unayoyasoma?” Kisha, mazungumzo kuhusu Isaya 53:7, 8 yakaanza. Mwishowe, Filipo “akamtangazia habari njema juu ya Yesu.”—Matendo 8:29-35.
3, 4. (a) Kwa nini Filipo alimbatiza Mwethiopia huyo bila kukawia? (b) Tutachunguza maswali gani?
3 Kwa muda mfupi tu, Mwethiopia huyo alielewa daraka la Yesu katika kusudi la Mungu na vilevile uhitaji wa kuwa mwanafunzi aliyebatizwa wa Kristo. Mwethiopia huyo alipoona mahali penye maji karibu, alimuuliza Filipo hivi: “Ni nini kinachonizuia nisibatizwe?” Bila shaka, hizo zilikuwa hali za pekee. Tayari mtu huyo mwenye imani alikuwa akimwabudu Mungu akiwa mgeuzwa-imani. Kama hangebatizwa wakati huo, basi huenda hangepata nafasi nyingine ya kubatizwa kwa muda mrefu sana. Zaidi ya yote, mtu huyo alielewa matakwa ya Mungu, na alitaka kuyatimiza kwa moyo wote. Filipo alikubali ombi lake kwa furaha, naye Mwethiopia huyo alipobatizwa “aliendelea kwenda zake akishangilia.” Inaelekea alienda kuwa mhubiri mwenye bidii wa habari njema katika nchi yao.—Matendo 8:36-39.
4 Ingawa hatua za wakfu na ubatizo hazipaswi kuchukuliwa kimchezo wala haraka-haraka, mfano wa ofisa huyo Mwethiopia unaonyesha kwamba kuna nyakati ambazo watu fulani wamebatizwa muda mfupi tu baada ya kusikia kweli ya Neno la Mungu.a Basi, inafaa kuchunguza maswali haya: Mtu anapaswa kujitayarishaje kwa ajili ya ubatizo? Ni wakati gani ambapo umri unapaswa kufikiriwa? Ni maendeleo gani ya kiroho ambayo yanapaswa kuonekana kabla mtu hajabatizwa? Zaidi ya yote, kwa nini Yehova anataka watumishi wake wachukue hatua hiyo?
Mapatano Mazito
5, 6. (a) Watu wa Mungu wa kale walionyeshaje kwamba wanathamini upendo wa Yehova? (b) Tunaweza kuwa na uhusiano gani wa karibu pamoja na Mungu baada ya kubatizwa?
5 Baada ya kuwakomboa Waisraeli kutoka Misri, Yehova alikuwa tayari kuwakubali kuwa “mali [yake] ya pekee,” kuwapenda na kuwalinda na kuwafanya kuwa “taifa takatifu.” Hata hivyo, ili wapate baraka hizo, iliwabidi watu hao waonyeshe waziwazi kwamba wanathamini upendo wa Mungu. Walifanya hivyo kwa kukubali kufanya ‘yote ambayo Yehova alisema’ na kufanya agano pamoja naye. (Kutoka 19:4-9) Katika karne ya kwanza, Yesu aliwaamuru wafuasi wake wafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, na wale waliokubali mafundisho yake wakabatizwa. Uhusiano mzuri pamoja na Mungu ulitegemea kumwamini Yesu Kristo kisha kubatizwa.—Mathayo 28:19, 20; Matendo 2:38, 41.
6 Masimulizi hayo ya Biblia yanaonyesha kwamba Yehova huwabariki wale wanaofanya na kutimiza mapatano mazito ya kumtumikia. Kwa Wakristo, wakfu na ubatizo ni hatua ambazo mtu anapaswa kuchukua ili apate baraka za Yehova. Tunaazimia kufuata njia zake na kutafuta mwongozo wake. (Zaburi 48:14) Tunapofanya hivyo, Yehova hushika mkono wetu na kutuongoza katika njia tunayopaswa kutembea ndani yake.—Zaburi 73:23; Isaya 30:21; 41:10, 13.
7. Kwa nini wakfu na ubatizo unapaswa kuwa uamuzi wa kibinafsi?
7 Nia yetu ya kuchukua hatua hizo inapaswa kuwa upendo kwa Yehova na tamaa ya kumtumikia. Mtu hapaswi kubatizwa eti kwa sababu mwingine amemwambia kwamba amejifunza kwa muda mrefu au kwa sababu rafiki zake wanabatizwa. Ni kweli kwamba wazazi na Wakristo wengine waliokomaa wanaweza kumhimiza mtu afikirie wakfu na ubatizo. Hata mtume Petro aliwasihi wale waliomsikiliza wakati wa Pentekoste ‘wabatizwe.’ (Matendo 2:38) Hata hivyo, kujiweka wakfu ni jambo la kibinafsi, na hakuna mtu mwingine yeyote anayeweza kufanya hivyo kwa niaba yetu. Sisi wenyewe ndio tunaopaswa kujiamulia kufanya mapenzi ya Mungu.—Zaburi 40:8.
Kujitayarisha Vizuri kwa Ajili ya Ubatizo
8, 9. (a) Kwa nini ubatizo wa watoto wachanga haupatani na Maandiko? (b) Kabla ya kubatizwa, vijana wanapaswa kufanya maendeleo gani ya kiroho?
8 Je, watoto wanaweza kuwa na hekima ya kufanya uamuzi wa kujiweka wakfu? Maandiko hayataji umri hususa wa kubatizwa. Lakini, ni wazi kwamba watoto wachanga hawawezi kuwa waamini, hawawezi kuwa na imani, wala hawawezi kujiweka wakfu kwa Mungu. (Matendo 8:12) Kuhusu Wakristo wa karne ya kwanza, mwanahistoria Augustus Neander alisema hivi katika kitabu chake (General History of the Christian Religion and Church): “Mwanzoni ni watu wazima tu waliokuwa wakibatizwa, kwa kuwa kwa kawaida watu walielewa kwamba ubatizo unahusiana sana na imani.”
9 Vijana wengine husitawisha hali ya kiroho wakiwa na umri mdogo, huku wengine hufanya hivyo baada ya muda mrefu. Hata hivyo, kabla ya kubatizwa, kijana anapaswa kuwa na uhusiano pamoja na Yehova, kuelewa kwa usahihi mafundisho ya msingi ya Maandiko, na kufahamu kabisa maana ya wakfu, kama ilivyo kwa watu wazima pia.
10. Ni hatua gani zinazopaswa kutangulia wakfu na ubatizo?
10 Yesu aliwaagiza wanafunzi wake kuwafundisha wapya mambo yote aliyoamuru. (Mathayo 28:20) Kwa hiyo, kwanza kabisa, wapya wanahitaji kupata ujuzi sahihi kuhusu kweli, kisha ujuzi huo utawawezesha kumwamini Yehova na Neno lake. (Waroma 10:17; 1 Timotheo 2:4; Waebrania 11:6) Halafu, kweli ya Biblia inapogusa moyo wa mtu, inamchochea kutubu na kugeuka kwa kuacha maisha yake ya zamani. (Matendo 3:19) Mwishowe, mtu huyo hutamani kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa, kama vile Yesu alivyoamuru.
11. Kwa nini ni muhimu tushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri kabla ya ubatizo?
11 Hatua nyingine muhimu ya kufanya maendeleo ili kufikia ubatizo ni kuhubiri habari njema ya Ufalme. Hiyo ndiyo kazi muhimu zaidi ambayo Yehova amewapa watu wake katika siku hizi za mwisho. (Mathayo 24:14) Hivyo, wahubiri ambao hawajabatizwa wanaweza kupata shangwe kwa kuwaeleza wengine yale wanayoamini. Kufanya kazi hiyo huwatayarisha pia kushiriki kwa ukawaida na kwa bidii katika huduma ya shambani baada ya ubatizo.—Waroma 10:9, 10, 14, 15.
Je, Kuna Jambo Linalokuzuia Usibatizwe?
12. Ni mambo gani ambayo huenda yakawazuia wengine wasibatizwe?
12 Huenda wengine wakasita kubatizwa kwa sababu hawataki madaraka yanayoambatana na hatua hiyo. Wanatambua kwamba ili watimize viwango vya Yehova, itawabidi wafanye mabadiliko makubwa maishani mwao. Au huenda wakaogopa kwamba itakuwa vigumu kwao kutimiza matakwa ya Mungu baada ya ubatizo. Huenda wengine wakafikiri hivi, “Labda siku moja nitafanya kosa na kutengwa na ushirika wa kutaniko.”
13. Katika siku za Yesu, ni nini kilichowazuia watu fulani wasiwe wafuasi wake?
13 Katika siku za Yesu, watu fulani waliruhusu mapendezi yao wenyewe na uhusiano wa kifamilia uwazuie wasiwe wanafunzi wake. Mwandishi fulani alisema kwamba angemfuata Yesu popote ambapo Yesu angeenda. Lakini Yesu akamwambia kwamba mara nyingi hata hana mahali pa kulala usiku. Yesu alipomwalika mtu mwingine amfuate, mtu huyo alijibu kwamba anahitaji kwanza ‘kumzika’ baba yake. Labda, alitaka kukaa nyumbani na kungoja mpaka wakati ambapo baba yake angekufa badala ya kumfuata Yesu na kushughulikia daraka hilo la kifamilia wakati ambapo lingetokea. Mwishowe, mtu wa tatu alisema kwamba kabla ya kumfuata Yesu, anahitaji kwanza ‘kuwaaga’ watu wa nyumbani mwake. Yesu alisema kwamba kuahirisha mambo kwa njia hiyo ni “kutazama mambo yaliyo nyuma.” Hivyo, inaonekana kwamba wale wanaosita kuamua hawatakosa visingizio vya kuepuka daraka lao la Kikristo.—Luka 9:57-62.
14. (a) Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana walitendaje wakati Yesu alipowaalika wawe wavuvi wa watu? (b) Kwa nini hatupaswi kusita-sita kukubali nira ya Yesu?
14 Mfano wa Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana ni tofauti sana. Yesu alipowaalika wamfuate na kuwa wavuvi wa watu, Biblia inasema hivi: “Mara moja wakaziacha nyavu, wakamfuata.” (Mathayo 4:19-22) Kwa kufanya uamuzi huo bila kusitasita, walijionea ukweli wa maneno ambayo Yesu aliwaambia baadaye: “Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mathayo 11:29, 30) Ingawa ubatizo huleta nira ya daraka, Yesu anatuhakikishia kwamba hiyo ni nira laini inayoweza kubebwa ambayo itatuburudisha sana.
15. Mfano wa Musa na Yeremia unaonyeshaje kwamba tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atatutegemeza?
15 Bila shaka, si ajabu kwa mtu kuhisi kwamba hawezi kutimiza madaraka yanayotokana na ubatizo. Mwanzoni, Musa na Yeremia walihisi kwamba hawawezi kushughulikia migawo ambayo Yehova alikuwa amewapa. (Kutoka 3:11; Yeremia 1:6) Mungu aliwapa uhakikisho gani? Alimwambia Musa hivi: “Nitakuwa pamoja nawe.” Pia, alimwahidi Yeremia hivi: “Mimi niko pamoja nawe ili kukukomboa.” (Kutoka 3:12; Yeremia 1:8) Sisi pia tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatutegemeza. Kumpenda Mungu na kumtegemea kunaweza kutusaidia kuondoa shaka kwamba hatuwezi kutimiza wakfu wetu. Mtume Yohana aliandika hivi: “Hakuna woga katika upendo, lakini upendo mkamilifu hutupa woga nje.” (1 Yohana 4:18) Mvulana mdogo anaweza kuogopa anapotembea peke yake, lakini anakuwa na uhakika anapotembea akiwa ameushika mkono wa baba yake. Vivyo hivyo, tukimtegemea Yehova kwa moyo wetu wote, anatuahidi kwamba ‘atanyoosha mapito yetu’ tunapoendelea kutembea pamoja naye.—Methali 3:5, 6.
Pindi Inayostahili Heshima
16. Kwa nini ubatizo unahusisha kumzamisha mtu kabisa ndani ya maji?
16 Kwa kawaida, hotuba ya Kimaandiko inayoeleza maana ya ubatizo wa Kikristo hutolewa kabla ya ubatizo. Mwishoni mwa hotuba hiyo, wale wanaotaka kubatizwa huombwa wafanye tangazo la hadharani la imani yao kwa kujibu yale maswali mawili ya ubatizo. (Waroma 10:10; ona sanduku kwenye ukurasa wa 22.) Kisha, wale wanaotaka kubatizwa huzamishwa ndani ya maji, kwa kufuata mfano uliowekwa na Yesu. Biblia inasema kwamba baada ya Yesu kubatizwa, ‘alipanda kutoka katika maji’ au “kutoka majini.” (Mathayo 3:16; Marko 1:10) Ni wazi kwamba Yohana Mbatizaji alimzamisha Yesu kabisa.b Kuzamishwa kabisa huonyesha badiliko kubwa ambalo tumefanya maishani, yaani, ni kana kwamba tunakufa kuhusiana na maisha yetu ya zamani na kuanza maisha mapya ya kumtumikia Mungu.
17. Watazamaji na wale wanaotaka kubatizwa wanaweza kuonyeshaje heshima wakati wa ubatizo?
17 Ubatizo ni pindi nzito na ya shangwe. Biblia inaonyesha kwamba Yesu alikuwa akisali wakati Yohana alipombatiza katika Mto Yordani. (Luka 3:21, 22) Kupatana na mfano huo, wale wanaotaka kubatizwa wanapaswa kujiendesha kwa njia inayofaa wakati wa ubatizo. Kwa kuwa Biblia inatuhimiza tuvalie kwa kiasi kila siku, tunapaswa kutii shauri hilo hata zaidi siku ya ubatizo wetu! (1 Timotheo 2:9) Pia, watazamaji wanaweza kuonyesha heshima kwa kusikiliza kwa makini hotuba ya ubatizo na kutazama ubatizo kwa utaratibu.—1 Wakorintho 14:40.
Baraka Ambazo Wanafunzi Waliobatizwa Hupata
18, 19. Ubatizo huleta mapendeleo na baraka gani?
18 Tunapojiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa, tunakuwa sehemu ya familia ya pekee. Kwanza kabisa, Yehova anakuwa Baba yetu na Rafiki yetu. Kabla ya ubatizo, tulikuwa tumetenganishwa na Mungu, lakini baada ya ubatizo tunapatanishwa naye. (2 Wakorintho 5:19; Wakolosai 1:20) Kupitia dhabihu ya Kristo, tumemkaribia Mungu naye anatukaribia. (Yakobo 4:8) Nabii Malaki anaeleza jinsi Yehova anavyowasikiliza wale wanaolitumia jina lake na kutambulishwa kwa jina hilo, naye anaingiza majina yao katika kitabu chake cha kumbukumbu. Mungu anasema hivi: “Nao watakuwa wangu, . . . Nami nitawaonyesha huruma, kama vile mwanamume anavyomwonyesha huruma mwana wake ambaye anamtumikia.”—Malaki 3:16-18.
19 Pia, ubatizo hutuwezesha kuwa sehemu ya undugu wa ulimwenguni pote. Mtume Petro alipouliza baraka ambazo wanafunzi wa Kristo watapata kwa sababu ya kujidhabihu, Yesu aliahidi hivi: “Kila mtu ambaye ameacha nyumba au ndugu au dada au baba au mama au watoto au mashamba kwa ajili ya jina langu atapokea mara nyingi zaidi naye atarithi uzima wa milele.” (Mathayo 19:29) Miaka mingi baadaye, Petro aliandika kuhusu “ushirika mzima wa akina ndugu” ambao ulikuwa umesitawi “ulimwenguni.” Petro mwenyewe alijionea utegemezo na baraka zinazotokana na undugu wenye upendo, nasi pia tunaweza kujionea mambo hayo.—1 Petro 2:17; 5:9.
20. Tunapobatizwa tunapata tumaini gani zuri?
20 Isitoshe, Yesu alionyesha kwamba wale wanaomfuata ‘watarithi uzima wa milele.’ Naam, wakfu na ubatizo hutupa tumaini la ‘kuushika imara uzima ulio wa kweli,’ yaani, uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu. (1 Timotheo 6:19) Hakuna msingi mwingine bora kuliko huo ambao tunaweza kujiwekea sisi wenyewe pamoja na familia zetu kwa ajili ya wakati ujao! Tumaini hilo zuri litatuwezesha ‘kutembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.’—Mika 4:5.
[Maelezo ya Chini]
a Vivyo hivyo, Wayahudi na wageuzwa-imani 3,000 waliosikiliza hotuba ya Petro wakati wa Pentekoste, walibatizwa bila kukawia. Bila shaka, kama yule towashi Mwethiopia, tayari walijua mafundisho ya msingi na kanuni za Neno la Mungu.—Matendo 2:37-41.
b Kulingana na kitabu kimoja (Expository Dictionary of New Testament Words cha Vine), neno la Kigiriki baʹpti·sma (ubatizo) linamaanisha “hatua ya kuingizwa ndani ya maji, kuzamishwa na kuinuliwa.”
-