Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ayubu Alilitukuza Jina la Yehova
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Aprili 15
    • Ayubu Alilitukuza Jina la Yehova

      “Jina la Yehova na liendelee kubarikiwa.”—AYU. 1:21.

      1. Huenda ni nani aliyeandika kitabu cha Ayubu, na alikiandika wakati gani?

      MUSA alikuwa na umri wa miaka 40 hivi alipokimbia kutoka Misri ili kuepuka ghadhabu ya Farao, akakimbilia Midiani. (Mdo. 7:23) Alipokuwa katika nchi hiyo, huenda alisikia habari kuhusu majaribu ya Ayubu, ambaye alikuwa akiishi karibu katika nchi ya Usi. Miaka mingi baadaye, Musa na taifa la Israeli walipokuwa karibu na Usi mwishoni mwa safari yao ya nyikani, huenda Musa alipata habari kuhusu miaka ya mwisho-mwisho ya maisha ya Ayubu. Kulingana na mapokeo ya Wayahudi, Musa aliandika kitabu cha Ayubu miaka michache baada ya kifo cha Ayubu.

      2. Kitabu cha Ayubu kinawatia moyo watumishi wa Yehova leo katika njia gani?

      2 Kitabu cha Ayubu kinatia nguvu imani ya watumishi wa Mungu leo. Katika njia gani? Masimulizi hayo yanatusaidia kuelewa mambo yaliyotukia mbinguni ambayo ni ya maana sana kwetu na yanakazia suala la maana sana la enzi kuu ya Mungu ya ulimwengu wote. Pia, masimulizi ya Ayubu yanapanua uelewaji wetu kuhusu mambo yanayohusika katika kudumisha utimilifu na yanatusaidia kuelewa kwa nini nyakati nyingine Yehova anaruhusu watumishi wake wateseke. Zaidi ya hayo, kitabu cha Ayubu kinamtambulisha Shetani Ibilisi kuwa Adui mkuu wa Yehova na wanadamu. Pia, kitabu hicho kinaonyesha kwamba wanadamu wasio wakamilifu kama Ayubu wanaweza kubaki washikamanifu kwa Yehova hata wakijaribiwa vikali. Acheni tuchunguze matukio fulani yanayoelezwa katika kitabu cha Ayubu.

      Ayubu Ajaribiwa na Shetani

      3. Tunajua nini kumhusu Ayubu, na kwa nini alikuwa shabaha ya Shetani?

      3 Ayubu alikuwa tajiri na mtu mashuhuri sana, mzee wa ukoo mwenye sifa nzuri. Alikuwa mshauri mwenye kuheshimiwa sana ambaye aliwasaidia watu wenye uhitaji. Jambo la maana hata zaidi ni kwamba Ayubu alimwogopa Mungu. Ayubu anaelezwa kuwa mtu ambaye ‘hakuwa na lawama na mnyoofu, na aliyemwogopa Mungu na kujiepusha na ubaya.’ Ayubu alikuwa shabaha ya mashambulizi ya Shetani Ibilisi kwa sababu ya kujitoa kwake kwa Mungu, bali si kwa sababu ya mali na umashuhuri wake.—Ayu. 1:1; 29:7-16; 31:1.

      4. Utimilifu ni nini?

      4 Utangulizi wa masimulizi ya kitabu cha Ayubu unaeleza kuhusu mkutano uliokuwa mbinguni ambapo malaika walisimama mbele za Yehova. Shetani pia alikuwepo, na alitoa mashtaka kumhusu Ayubu. (Soma Ayubu 1:6-11.) Ingawa Shetani alitaja mali za Ayubu, shabaha yake ilikuwa hasa kupinga utimilifu wa Ayubu. Neno “utimilifu” linamaanisha kuwa mnyoofu, asiye na lawama, mwadilifu, na bila kosa. Kulingana na Biblia, utimilifu wa wanadamu unamaanisha kujitoa kwa moyo kamili kwa Yehova.

      5. Shetani alidai nini kumhusu Ayubu?

      5 Shetani alidai kwamba Ayubu alimwabudu Mungu kwa sababu ya uchoyo, wala si kwa sababu ya utimilifu. Shetani alidai kwamba Ayubu angekuwa mshikamanifu kwa Yehova ikiwa tu Mungu angeendelea kumthawabisha na kumlinda. Ili kujibu dai la Shetani, Yehova alimruhusu Shetani amshambulie mwanamume huyo mwaminifu. Kwa hiyo, kwa siku moja tu, Ayubu alijulishwa kwamba mifugo yake iliibiwa au kuangamizwa, watumishi wake waliuawa, na watoto wake kumi wakafa. (Ayu. 1:13-19) Je, mashambulizi ya Shetani yalivunja utimilifu wa Ayubu? Maandiko yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanaeleza maoni ya Ayubu kuhusu misiba yake: “Yehova ametoa, na Yehova amechukua. Jina la Yehova na liendelee kubarikiwa.”—Ayu. 1:21.

      6. (a) Ni jambo gani lililotukia katika mkutano mwingine huko mbinguni? (b) Shetani alikuwa akimfikiria nani alipotilia shaka utimilifu wa Ayubu kwa Yehova?

      6 Baadaye, kulikuwa na mkutano mwingine mbinguni. Kwa mara nyingine tena Shetani alimshtaki Ayubu, akisema: “Ngozi kwa ngozi, na kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake. Ili kuwe na badiliko, tafadhali nyoosha mkono wako, uguse kufikia mfupa wake na nyama yake, uone kama hatakulaani wewe mbele za uso wako.” Ona kwamba Shetani alihusisha watu wengine katika mashtaka yake. Kwa kusema, “Kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake,” Ibilisi hakutilia shaka utimilifu wa Ayubu tu, bali pia wa “mtu” yeyote yule anayemwabudu Yehova. Baadaye, Mungu alimruhusu Shetani kumpiga Ayubu kwa ugonjwa wenye maumivu makali. (Ayu. 2:1-8) Lakini huo haukuwa mwisho wa majaribu ya Ayubu.

      Mambo Tunayojifunza Kutokana na Msimamo wa Ayubu

      7. Ayubu alisongwa sana katika njia gani na mke wake na pia wageni waliomtembelea?

      7 Mwanzoni, mke wa Ayubu aliumia moyoni kwa sababu ya mapigo yaliyompata mume wake. Bila shaka, alifadhaika kwa sababu ya vifo vya watoto wake na kupoteza mali ya familia yake. Inaonekana, aliumia moyoni kuona mume wake akikabiliana na ugonjwa wenye maumivu makali. Alimwambia Ayubu hivi: “Je, bado unashikilia sana utimilifu wako? Mlaani Mungu, ufe!” Kisha, wanaume watatu wakafika, yaani, Elifazi, Bildadi, na Sofari, inaelekea walikuja kumfariji Ayubu. Hata hivyo, walitumia mawazo ya udanganyifu na hivyo wakathibitika kuwa “wafariji wasumbufu.” Kwa mfano, Bildadi alidai kwamba watoto wa Ayubu walitenda dhambi na hivyo walistahili madhara yaliyowapata. Elifazi alidai kwamba mateso ya Ayubu yalikuwa adhabu kwa sababu ya dhambi alizotenda wakati uliopita. Hata alitilia shaka ikiwa wale wanaoshika utimilifu wana thamani yoyote machoni pa Mungu! (Ayu. 2:9, 11; 4:8; 8:4; 16:2; 22:2, 3) Chini ya hali hizo ngumu sana, Ayubu aliendelea kuwa mtimilifu. Ni kweli kwamba alikosea ‘alipoitangaza nafsi yake mwenyewe kuwa adilifu badala ya Mungu.’ (Ayu. 32:2) Hata hivyo, alibaki mwaminifu mpaka mwisho.

      8. Elihu aliwawekea mfano gani mzuri wale wanaotoa mashauri leo?

      8 Kisha, tunasoma kuhusu Elihu, ambaye pia alikuja kumtembelea Ayubu. Kwanza, Elihu alisikiliza hoja zilizotolewa na Ayubu na marafiki wake watatu. Ingawa alikuwa kijana kuliko wale wanaume wengine wanne, Elihu alionyesha hekima kubwa zaidi. Alizungumza na Ayubu kwa heshima, akitumia jina lake. Elihu alimpongeza Ayubu kwa unyoofu wake. Lakini pia alisema kwamba Ayubu alijaribu sana kuthibitisha kwamba hakuwa na kosa. Kisha, Elihu alimhakikishia Ayubu kwamba sikuzote ni jambo la maana sana kumtumikia Mungu kwa uaminifu. (Soma Ayubu 36:1, 11.) Ni mfano mzuri kama nini kwa wote wanaotoa mashauri leo! Elihu alionyesha subira, alisikiliza kwa makini, alipongeza ilipowezekana, na alitoa mashauri yenye kujenga.—Ayu. 32:6; 33:32.

      9. Yehova alimsaidia Ayubu jinsi gani?

      9 Mwishowe, Yehova aliongea na Ayubu! Masimulizi hayo yanasema hivi: “Yehova akaanza kumjibu Ayubu kutoka katika dhoruba ya upepo.” Akitumia mfululizo wa maswali, Yehova alimsaidia Ayubu kwa fadhili lakini kwa uthabiti kurekebisha mawazo yake. Ayubu alikubali kutoka moyoni karipio hilo, na akakiri hivi: “Nimekuwa kitu kisicho na maana . . . Ninatubu katika mavumbi na majivu.” Baada ya kuzungumza na Ayubu, Yehova aliwakaripia wale marafiki watatu wa Ayubu kwa sababu hawakusema “mambo ya kweli.” Ayubu alipaswa kusali kwa ajili yao. Kisha, “Yehova akaigeuza hali ya mateka ya Ayubu aliposali kwa ajili ya wale rafiki zake, na Yehova akaanza kumpa na kumwongezea Ayubu vyote vilivyokuwa vyake, kiasi cha mara mbili.”—Ayu. 38:1; 40:4; 42:6-10.

      Tunampenda Sana Yehova Kadiri Gani?

      10. Kwa nini Yehova hakumpuuza au kumharibu Shetani?

      10 Yehova ni Muumba wa ulimwengu wote, Mwenye Enzi Kuu ya uumbaji wote. Kwa nini hakupuuza tu mashtaka ya Ibilisi? Mungu alijua kwamba kumpuuza au kumharibu Shetani hakungesuluhisha suala ambalo lilitokezwa. Ibilisi alidai kwamba Ayubu, mtumishi mtimilifu wa Yehova, hangeendelea kuwa mshikamanifu ikiwa angepoteza mali yake yote. Ayubu alibaki mshikamanifu katika majaribu. Kisha, Shetani alidai kwamba mwanadamu yeyote angemwacha Mungu ikiwa angeteseka kimwili. Ayubu aliteseka, lakini utimilifu wake haukuvunjwa. Hivyo, Shetani alithibitika kuwa mwongo katika kisa cha mwanamume huyo mwaminifu, lakini asiye mkamilifu. Namna gani waabudu wengine wa Mungu?

      11. Yesu alionyesha waziwazi jinsi gani kwamba Shetani ni mwongo?

      11 Kwa kweli, kila mtumishi wa Mungu anayeendelea kushika utimilifu wake hata anapojaribiwa kwa njia yoyote ile na Shetani anaonyesha kibinafsi kwamba mashtaka ya adui huyo asiye na huruma ni ya uwongo. Yesu alikuja duniani na akaonyesha waziwazi kwamba Shetani ni mwongo. Yesu alikuwa mtu mkamilifu kama baba yetu wa kwanza, Adamu. Uaminifu wa Yesu mpaka kifo ulionyesha wazi kabisa kwamba Shetani ni mwongo na kwamba mashtaka yake ni ya uwongo.—Ufu. 12:10.

      12. Kila mtumishi wa Yehova ana nafasi na daraka gani?

      12 Hata hivyo, Shetani anaendelea kuwajaribu waabudu wa Yehova. Kupitia utimilifu wetu, kila mmoja wetu ana nafasi na daraka la kuonyesha kwamba anamtumikia Yehova kwa sababu anampenda, bali si kwa sababu za kichoyo. Tuna maoni gani kuhusu daraka hilo? Tunaona kwamba ni pendeleo kuwa washikamanifu kwa Yehova. Pia tunafarijiwa tunapojua kwamba Yehova anatupa nguvu za kuvumilia na, kama katika kisa cha Ayubu, Hataruhusu tujaribiwe kupita uwezo wetu.—1 Kor. 10:13.

      Shetani Ni Adui Mkaidi na Mwasi-Imani

      13. Kitabu cha Ayubu kinafunua mambo gani kumhusu Shetani?

      13 Maandiko ya Kiebrania yanaeleza kwa undani jinsi ambavyo Shetani amempinga Yehova bila aibu na kuwapotosha wanadamu. Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, tunapata habari zaidi kuhusu upinzani wa Shetani kumwelekea Yehova, na katika kitabu cha Ufunuo, tunajifunza kuhusu kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova, na kuharibiwa kwa Shetani milele. Kitabu cha Ayubu kinaongeza ujuzi wetu kuhusu uasi wa Shetani. Shetani alipohudhuria mikutano mbinguni, hakuhudhuria akiwa na kusudi la kumsifu Yehova. Ibilisi alikuwa na mtazamo mwovu na nia mbaya. Baada ya kumshtaki Ayubu na kuruhusiwa amjaribu, ‘Shetani aliondoka mbele za uso wa Yehova.’—Ayu. 1:12; 2:7.

      14. Shetani alionyesha mtazamo gani kumwelekea Ayubu?

      14 Hivyo, kitabu cha Ayubu kinamtambulisha Shetani kuwa adui wa wanadamu asiye na huruma. Kipindi cha wakati kisichojulikana kilipita kati ya mkutano wa mbinguni unaotajwa kwenye Ayubu 1:6 na ule unaotajwa kwenye Ayubu 2:1, na wakati huo Ayubu alijaribiwa kikatili. Uaminifu wa Ayubu ulimwezesha Yehova kumwambia Shetani: “Hata sasa bado [Ayubu] anashikilia sana utimilifu wake, ingawa wewe unanichochea juu yake nimmeze bila sababu.” Lakini Shetani hakukubali kwamba madai yake kumhusu Ayubu yalikuwa yamethibitishwa kuwa ya uwongo. Badala yake, aliomba kwamba Ayubu ajaribiwe tena vikali. Hivyo, Ibilisi alimjaribu Ayubu wakati alipokuwa tajiri na wakati ambapo hakuwa na chochote. Kwa wazi, Shetani hawahurumii watu wenye uhitaji au wale wanaopatwa na misiba. Anachukia watu watimilifu. (Ayu. 2:3-5) Hata hivyo, uaminifu wa Ayubu ulionyesha kwamba Shetani ni mwongo.

      15. Waasi-imani wa siku zetu wanafanana jinsi gani na Shetani?

      15 Shetani alikuwa kiumbe wa kwanza kuasi imani. Waasi-imani wa siku hizi wanaonyesha sifa mbaya kama zile za Ibilisi. Huenda wakawa na mwelekeo mbaya wa kuwachambua-chambua watu fulani katika kutaniko, wazee Wakristo, au Baraza Linaloongoza. Waasi-imani fulani wanapinga kutumiwa kwa jina la Mungu, Yehova. Hawataki kujifunza kumhusu Yehova au kumtumikia. Kama baba yao, Shetani, waasi-imani wanalenga watu watimilifu. (Yoh. 8:44) Haishangazi kwamba watumishi wa Yehova wanaepuka kabisa kushirikiana na waasi-imani!—2 Yoh. 10, 11.

      Ayubu Alilitukuza Jina la Yehova

      16. Ayubu alionyesha mtazamo gani kumwelekea Yehova?

      16 Ayubu alilitumia na kulisifu jina la Yehova. Hata alipoumia sana moyoni kwa sababu ya habari za vifo vya watoto wake, Ayubu hakumhesabia Mungu jambo lolote lisilofaa. Ingawa Ayubu alifikiri kimakosa kwamba Mungu ndiye aliyesababisha vifo hivyo, bado alilitukuza jina la Yehova. Baadaye, katika moja ya maneno yake ya kimethali, Ayubu alisema hivi: “Tazama! Kumwogopa Yehova—hiyo ndiyo hekima, na kuacha ubaya ni uelewaji.”—Ayu. 28:28.

      17. Ni nini kilichomsaidia Ayubu kudumisha utimilifu wake?

      17 Ni nini kilichomsaidia Ayubu kudumisha utimilifu wake? Ni wazi kwamba kabla ya kupatwa na misiba hiyo, alikuwa tayari amesitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Ingawa hatuna uthibitisho wa kwamba alijua kwamba Shetani alikuwa ametoa mashtaka fulani kumhusu Yehova, Ayubu aliazimia kubaki mshikamanifu. Alisema hivi: “Mpaka nitakapokata pumzi, sitajiondolea utimilifu wangu!” (Ayu. 27:5) Ayubu alidumisha jinsi gani uhusiano huo wa karibu pamoja na Mungu? Bila shaka, alithamini yale aliyosikia kuhusu jinsi Mungu alivyoshughulika na Abrahamu, Isaka, na Yakobo, ambao walikuwa watu wake wa ukoo. Na kwa kuchunguza uumbaji, Ayubu angeweza kutambua sifa nyingi za Yehova.—Soma Ayubu 12:7-9, 13, 16.

      18. (a) Ayubu alionyesha jinsi gani kwamba alijitoa kwa Yehova? (b) Tunaiga mfano mzuri wa Ayubu katika njia gani?

      18 Mambo ambayo Ayubu alijifunza yalimchochea kuwa na tamaa ya kumpendeza Yehova. Kwa kuwa huenda washiriki wa familia yake walifanya jambo fulani lisilompendeza Mungu au ‘walimlaani Mungu moyoni mwao,’ Ayubu alitoa dhabihu kwa ukawaida. (Ayu. 1:5) Hata akiwa chini ya majaribu makali, bado Ayubu alisema mambo mazuri kumhusu Yehova. (Ayu. 10:12) Anatuwekea mfano mzuri kama nini! Sisi pia tunapaswa kujifunza kwa ukawaida ili tupate ujuzi sahihi kumhusu Yehova na makusudi yake. Tunapaswa kuwa na mazoea mazuri ya kiroho, kama vile kujifunza, kuhudhuria mikutano, kusali, na kuhubiri habari njema. Zaidi ya hayo, tunafanya yote tunayoweza ili kulitangaza jina la Yehova. Na kama vile utimilifu wa Ayubu ulivyompendeza Yehova, ndivyo utimilifu wa watumishi wa Mungu leo unavyofanya moyo wa Yehova ushangilie. Habari hiyo itazungumziwa katika makala inayofuata.

  • Utimilifu Wako Unafanya Moyo wa Yehova Ushangilie
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Aprili 15
    • Utimilifu Wako Unafanya Moyo wa Yehova Ushangilie

      “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.”—MET. 27:11.

      1, 2. (a) Kitabu cha Ayubu kinaeleza dai gani la Shetani? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Shetani aliendelea kumdhihaki Yehova hata baada ya siku za Ayubu?

      YEHOVA alimruhusu Shetani ajaribu utimilifu wa Ayubu, mtumishi mshikamanifu wa Mungu. Kwa hiyo, Ayubu akapoteza mifugo yake, watoto wake, na afya yake nzuri. Lakini Shetani alipotilia shaka utimilifu wa Ayubu, hakuwa akimfikiria tu mwanamume huyo. Shetani alidai hivi: “Ngozi kwa ngozi, na kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake.” Dai hilo lilitokeza suala ambalo lilihusisha watu wengine mbali na Ayubu nalo limeendelea kwa muda mrefu hata baada ya kifo cha Ayubu.—Ayu. 2:4.

      2 Miaka 600 hivi baada ya Ayubu kujaribiwa, Sulemani aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.” (Met. 27:11) Kwa wazi, wakati huo bado Shetani alikuwa akimpinga Yehova. Zaidi ya hayo, katika maono ambayo mtume Yohana alipata, Shetani alionekana akiwashtaki watumishi wa Mungu baada ya yeye kufukuzwa kutoka mbinguni muda mfupi baada ya Ufalme wa Mungu kusimamishwa mwaka wa 1914. Ndiyo, hata leo hii, katika upeo wa siku za mwisho za mfumo huu mwovu, bado Shetani anatilia shaka utimilifu wa watumishi wa Mungu!—Ufu. 12:10.

      3. Ni mambo gani ya maana tunayoweza kujifunza kutokana na kitabu cha Ayubu?

      3 Hebu chunguza mambo matatu ya maana ambayo tunajifunza kutokana na kitabu cha Ayubu. Kwanza, majaribu ya Ayubu yanaonyesha wazi ni nani aliye adui mkuu wa wanadamu na yule anayesababisha upinzani kuelekea watu wa Mungu. Adui huyo ni Shetani Ibilisi. Pili, hata tukipatwa na majaribu ya aina gani, tukiwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu tutaweza kudumisha utimilifu wetu. Tatu, majaribu yanapotokea na tunapojaribiwa kwa njia moja au nyingine, Mungu anatusaidia kuvumilia kama alivyomsaidia Ayubu. Leo, Yehova anafanya hivyo kupitia Neno lake, tengenezo lake, na roho yake takatifu.

      Sikuzote Kumbuka Adui Yetu Mkuu Ni Nani

      4. Ni nani anayepaswa kulaumiwa kwa sababu ya hali za sasa za ulimwengu?

      4 Watu wengi hawaamini kwamba Shetani yuko. Hivyo, ingawa huenda wana wasiwasi kuhusu hali za ulimwengu, hawatambui yule hasa anayesababisha hali hizo, yaani, Shetani Ibilisi. Ni kweli kwamba wanadamu wenyewe ndio wanaopaswa kulaumiwa kwa sababu ya mateso mengi yanayowakumba. Wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, waliamua kutomtegemea Muumba wao. Na tangu wakati huo, vizazi ambavyo vimefuata vimetenda bila hekima. Hata hivyo, Ibilisi ndiye aliyemdanganya Hawa kumwasi Mungu. Yeye ndiye ametokeza kati ya wanadamu wasio wakamilifu na wanaokufa, mfumo wa ulimwenguni pote ulio chini ya uongozi wake. Kwa sababu Shetani ndiye “mungu wa mfumo huu wa mambo,” jamii ya wanadamu inaonyesha sifa zilezile mbaya kama za Shetani—kiburi, ugomvi, wivu, pupa, udanganyifu, na uasi. (2 Kor. 4:4; 1 Tim. 2:14; 3:6; soma Yakobo 3:14, 15.) Sifa mbaya kama hizo zimesababisha mizozo ya kisiasa na ya kidini, chuki, ufisadi, na machafuko, na zimechangia sana taabu ya wanadamu.

      5. Tunataka kuutumia jinsi gani ujuzi wenye thamani tulio nao?

      5 Ni ujuzi wenye thamani kama nini tulio nao sisi watumishi wa Yehova! Ndiyo, tunaelewa ni nani anayestahili kulaumiwa kwa sababu ya kuzorota kwa hali za ulimwengu. Hivyo basi, je, moyo wetu hautuchochei kushiriki katika utumishi wa shambani ili kuwajulisha watu ni nani aliye adui mkuu wa wanadamu? Je, hatufurahi kuwa upande wa Mungu wa kweli, Yehova, na kuwaeleza wengine jinsi atakavyomharibu Shetani na kukomesha taabu za wanadamu?

      6, 7. (a) Ni nani hasa anayesababisha mateso yanayowapata waabudu wa kweli? (b) Tunaweza kuiga jinsi gani mfano wa Elihu wa kale?

      6 Shetani ndiye chanzo cha huzuni nyingi ulimwenguni na pia upinzani ambao watu wa Mungu wanakabili leo. Ameazimia kutujaribu. Yesu Kristo alimwambia mtume Petro hivi: “Simoni, Simoni, tazama! Shetani amedai kuwapata ninyi ili awapepete kama ngano.” (Luka 22:31) Vivyo hivyo, kila mmoja wetu ambaye anafuata hatua za Yesu atapatwa na majaribu kwa njia moja au nyingine. Petro alimlinganisha Ibilisi na “simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” Na Paulo alisema: “Wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.”—1 Pet. 5:8; 2 Tim. 3:12.

      7 Mwamini mwenzetu anapopatwa na msiba, tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunakumbuka ni nani aliye adui yetu mkuu? Badala ya kujitenga na ndugu aliyepatwa na msiba, tunatenda kama Elihu wa kale, aliyezungumza na Ayubu kama rafiki wa kweli. Tunapaswa kumsaidia ndugu yetu kupigana na adui yetu, Shetani. (Met. 3:27; 1 The. 5:25) Kusudi letu ni kumsaidia mtumishi mwenzetu adumishe kwa vyovyote vile utimilifu wake, na hivyo kuufanya moyo wa Yehova ushangilie.

      8. Kwa nini Shetani hakufaulu kumfanya Ayubu aache kumheshimu Yehova?

      8 Kwanza, Shetani alisababisha Ayubu apoteze mifugo yake. Wanyama hao walikuwa wenye thamani kwa Ayubu, inaelekea walikuwa chanzo chake cha riziki. Lakini Ayubu aliwatumia pia katika ibada. Baada ya Ayubu kuwatakasa watoto wake, “aliamka asubuhi na mapema na kutoa dhabihu za kuteketezwa kulingana na hesabu yao wote; kwa kuwa Ayubu alisema, ‘labda wanangu wametenda dhambi nao wamemlaani Mungu moyoni mwao.’ Hivyo ndivyo Ayubu alivyofanya sikuzote.” (Ayu. 1:4, 5) Kwa hiyo, Ayubu alimtolea Yehova dhabihu za wanyama kwa ukawaida. Majaribu yalipoanza, hangeweza tena kufanya hivyo. Ayubu hakuwa tena na ‘vitu vyenye thamani’ ambavyo angetumia kumheshimu Yehova. (Met. 3:9) Lakini angeweza na alimheshimu Yehova kwa midomo yake!

      Sitawisha Uhusiano wa Karibu Pamoja na Yehova

      9. Ni kitu gani chenye thamani zaidi tulicho nacho?

      9 Tuwe matajiri au maskini, vijana au wazee, wenye afya nzuri au mbaya, tunaweza kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Hata tukikabili majaribu gani, tukiwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu tutaweza kudumisha utimilifu wetu na kuufanya moyo wa Yehova ushangilie. Hata watu fulani ambao hawakuwa na ujuzi mwingi wa kweli walisimama kwa ujasiri upande wa Mungu na kushika utimilifu wao.

      10, 11. (a) Dada yetu mmoja alipambana jinsi gani na majaribu ya utimilifu? (b) Ni jibu gani lenye nguvu ambalo dada huyo alimpa Shetani?

      10 Fikiria mfano wa Dada Valentina Garnovskaya, mmoja kati ya Mashahidi wengi wa Urusi ambao kama Ayubu mwaminifu, walishika utimilifu wao hata ingawa walijaribiwa vikali. Katika mwaka wa 1945, Valentina alipokuwa na umri wa miaka 20 hivi, ndugu mmoja alimhubiria. Ndugu huyo alimtembelea mara mbili ili kuzungumza naye kuhusu Biblia, lakini baada ya hapo Valentina hakumwona tena. Hata hivyo, Valentina alianza kuwahubiria majirani wake. Kwa hiyo, alikamatwa akahukumiwa kifungo cha miaka minane katika kambi moja. Katika mwaka wa 1953, aliachiliwa huru na papo hapo akaanza tena kazi yake ya kuhubiri. Kwa mara nyingine tena alikamatwa na kutupwa gerezani, wakati huo alifungwa miaka kumi. Baada ya kukaa katika kambi moja kwa miaka mingi, alihamishiwa kwenye kambi nyingine. Katika kambi hiyo, kulikuwa na dada fulani ambao walikuwa na nakala moja ya Biblia. Siku moja dada mmoja alimwonyesha Valentina Biblia hiyo. Ulikuwa wakati wenye kusisimua kama nini! Hebu wazia, kabla ya hapo, Valentina hakuwa ameona Biblia nyingine yoyote isipokuwa ile ambayo yule ndugu aliyemhubiria mwaka wa 1945 alikuwa nayo!

      11 Katika mwaka wa 1967, Valentina aliachiliwa huru na mwishowe akabatizwa katika maji ili kuonyesha wakfu wake kwa Yehova. Alitumia uhuru wake kwa kushiriki kwa bidii katika huduma mpaka mwaka wa 1969. Hata hivyo, mwaka huo, alikamatwa tena, na wakati huo alihukumiwa kifungo cha miaka mitatu gerezani. Lakini, Valentina aliendelea kuhubiri. Kabla ya kifo chake mwaka wa 2001, alikuwa amesaidia watu 44 kujifunza kweli. Alikaa gerezani na katika kambi mbalimbali kwa miaka 21. Alikuwa tayari kupoteza kila kitu, kutia ndani uhuru wake, ili kudumisha utimilifu wake. Mwishoni mwa maisha yake, Valentina alisema hivi: “Sikuwa na mahali pangu pa kuishi. Vitu vyangu vyote vilitoshea katika mfuko mmoja, lakini nilifurahi na kuridhika kwa kuwa nilimtumikia Yehova.” Ni jibu lenye nguvu kama nini ambalo Valentina alimpa Shetani, ambaye alidai kwamba wanadamu hawatabaki washikamanifu kwa Mungu wakijaribiwa! (Ayu. 1:9-11) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba aliufanya moyo wa Yehova ushangilie na kwamba Yehova anatazamia kwa hamu sana siku ambayo atamfufua Valentina na wengine wote ambao walikufa wakiwa waaminifu.—Ayu. 14:15.

      12. Upendo unatimiza nini katika uhusiano wetu pamoja na Yehova?

      12 Urafiki wetu pamoja na Yehova unategemea upendo wetu kwake. Tunavutiwa na sifa za Mungu na tunafanya yote tunayoweza ili kuishi kulingana na makusudi yake. Tofauti na madai ya Ibilisi, tunampenda Yehova kutoka moyoni na bila masharti yoyote. Upendo huo wa kutoka moyoni unatupa nguvu za kudumisha utimilifu chini ya majaribu. Kwa upande wake, Yehova “atailinda njia ya washikamanifu wake.”—Met. 2:8; Zab. 97:10.

      13. Yehova ana maoni gani kuhusu yale tunayofanya kwa ajili yake?

      13 Upendo unatuchochea kuliheshimu jina la Yehova, hata ikiwa tunahisi kwamba hatuwezi kutimiza mengi. Anaona nia yetu nzuri na hatuhukumu ikiwa hatutimizi yote ambayo tungependa kufanya. Jambo la maana si tu yale tunayofanya lakini pia kwa nini tunayafanya. Hata ingawa Ayubu alikuwa na huzuni nyingi na alikuwa amevumilia mambo mengi, aliwaambia washtaki wake jinsi alivyozipenda njia za Yehova. (Soma Ayubu 10:12; 28:28.) Katika sura ya mwisho ya kitabu cha Ayubu, Mungu alionyesha hasira yake kuelekea Elifazi, Bildadi, na Sofari kwa sababu hawakusema ukweli. Wakati huohuo, Yehova alionyesha kwamba alimkubali Ayubu kwa kumwita mara nne “mtumishi wangu” na kumwagiza asali kwa ajili ya wakosaji hao. (Ayu. 42:7-9) Acheni sisi pia tutende kwa njia inayomfanya Yehova atukubali.

      Yehova Anawategemeza Watumishi Wake Waaminifu

      14. Yehova alimsaidia jinsi gani Ayubu kurekebisha mawazo yake?

      14 Ayubu alidumisha utimilifu wake hata ingawa hakuwa mkamilifu. Nyakati nyingine, alipokabili hali ngumu sana, alikuwa na maoni yasiyofaa. Kwa mfano, alimwambia Yehova hivi: “Ninakulilia nipate msaada, lakini wewe hunijibu . . . Unadumisha uadui kwangu kwa nguvu kamili za mkono wako.” Zaidi ya hayo, Ayubu alijitetea sana aliposema hivi: “Mimi sina kosa,” na “hakuna jeuri mikononi mwangu, na sala yangu ni safi.” (Ayu. 10:7; 16:17; 30:20, 21) Hata hivyo, kwa fadhili Yehova alimsaidia Ayubu kwa kumuuliza maswali mengi ambayo yalimfanya Ayubu asijifikirie tu. Pia, yalimwezesha Ayubu kuona wazi zaidi ukuu wa Mungu na kwamba mwanadamu hawezi kamwe kulinganishwa na yeye. Ayubu alikubali mashauri naye akajirekebisha.—Soma Ayubu 40:8; 42:2, 6.

      15, 16. Yehova anawasaidia watumishi wake leo katika njia gani?

      15 Leo pia, kwa fadhili Yehova anawapa watumishi wake mashauri yaliyo thabiti. Kwa kuongezea, tunapata faida nyingi. Kwa mfano, Yesu Kristo alitoa fidia au dhabihu ya ukombozi na hivyo akaweka msingi wa msamaha wa dhambi. Kwa msingi wa dhabihu hiyo, tunaweza kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu hata ingawa hatujakamilika. (Yak. 4:8; 1 Yoh. 2:1) Tunapokabili majaribu, sisi pia tunasali ili roho takatifu ya Mungu itutegemeze na kututia nguvu. Kwa kuongezea, tuna Biblia kamili, na tukiisoma na kutafakari juu ya ujumbe wake, tunajitayarisha kwa ajili ya majaribu ya imani. Kujifunza kunatusaidia kuelewa suala la enzi kuu ya ulimwengu wote na suala la utimilifu wetu.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki