-
Lazima Watu wa Mungu Wapende FadhiliMnara wa Mlinzi—2004 | Aprili 15
-
-
Lazima Watu wa Mungu Wapende Fadhili
“Yehova anataka nini kutoka kwako ila kutenda haki na kupenda fadhili na kuwa na kiasi katika kutembea na Mungu wako?”—MIKA 6:8.
1, 2. (a) Kwa nini hatupaswi kushangaa kwamba Yehova anatazamia watu wake waonyeshe fadhili? (b) Tunapaswa kuchunguza maswali gani kuhusu fadhili?
YEHOVA ni Mungu wa fadhili. (Waroma 2:4; 11:22) Bila shaka, wenzi wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, walithamini sana fadhili za Mungu. Katika bustani ya Edeni, walizungukwa na uumbaji wenye kuonekana, jambo lililothibitisha kwamba Mungu ana fadhili kuelekea wanadamu, ambao wangeweza kuufurahia uumbaji huo. Naye Mungu anaendelea kuwa mwenye fadhili kwa wote, hata kwa watu waovu na wasio na shukrani.
2 Kwa kuwa wanadamu wameumbwa kwa mfano wa Mungu, wana uwezo wa kudhihirisha sifa za kimungu. (Mwanzo 1:26) Hivyo, haishangazi kwamba Yehova anatarajia tuonyeshe fadhili. Kama vile andiko la Mika 6:8 lisemavyo, ni lazima watu wa Mungu ‘wapende fadhili.’ Lakini fadhili ni nini? Nayo inahusianaje na sifa nyingine za kimungu? Kwa kuwa wanadamu wanaweza kuonyesha fadhili, kwa nini ulimwengu ni mahali penye ukatili hivyo? Kwa nini sisi tukiwa Wakristo tunapaswa kujitahidi kuonyesha fadhili tunaposhughulika na wengine?
Fadhili Ni Nini?
3. Ungefafanuaje fadhili?
3 Fadhili huonyeshwa kwa kuhangaikia hali njema ya wengine. Inaonyeshwa kwa kuwasaidia wengine na kuzungumza nao kwa ufikirio. Kuwa mwenye fadhili humaanisha kutenda mema badala ya kutenda mambo yenye kudhuru. Mtu mwenye fadhili ni mpole, mwenye urafiki, huruma, na neema. Yeye ni mkarimu na huwaonyesha wengine ufikirio. Mtume Paulo aliwashauri Wakristo hivi: “Jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu.” (Wakolosai 3:12) Hivyo basi, fadhili ni sehemu ya vazi la mfano la kila Mkristo wa kweli.
4. Yehova amechukuaje hatua ya kwanza katika kuonyesha wanadamu fadhili?
4 Yehova Mungu amechukua hatua ya kwanza katika kuonyesha fadhili. Kama Paulo alivyosema, wakati “Mwokozi wetu, Mungu, alipoonyesha fadhili na upendo kwa mwanadamu” ndipo ‘alipotuokoa kupitia kuoshwa kulikotuleta kwenye uzima na kupitia kutufanya sisi kuwa wapya kwa roho takatifu.’ (Tito 3:4, 5) Mungu ‘huwaosha,’ au huwasafisha, Wakristo watiwa-mafuta katika damu ya Yesu, akitumia manufaa ya dhabihu ya fidia ya Kristo kwa ajili yao. Wao pia hufanywa wapya kupitia roho takatifu na kuwa ‘viumbe wapya,’ wakiwa wana wa Mungu waliozaliwa kwa roho. (2 Wakorintho 5:17) Isitoshe, Mungu huonyesha upendo na fadhili kwa “umati mkubwa,” ambao ‘umefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo.’—Ufunuo 7:9, 14; 1 Yohana 2:1, 2.
5. Kwa nini wale wanaoongozwa na roho ya Mungu wanapaswa kuwaonyesha wengine fadhili?
5 Pia, fadhili ni sehemu ya matunda ya roho takatifu au nguvu za utendaji za Mungu. Paulo alisema: “Matunda ya roho ni upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia. Hakuna sheria juu ya mambo hayo.” (Wagalatia 5:22, 23) Hivyo basi, wale wanaoongozwa na roho ya Mungu wanapaswa kuwaonyesha wengine fadhili.
Fadhili ya Kweli Si Udhaifu
6. Ni wakati gani fadhili zinaweza kuwa udhaifu, na kwa nini?
6 Watu fulani huona fadhili kuwa udhaifu. Wanaona kwamba lazima nyakati nyingine mtu awe mgumu, na hata mjeuri ili wengine wamtambue. Hata hivyo, ukweli ni kwamba mtu anahitaji nguvu kwelikweli ili kuonyesha fadhili za kweli na kuepuka kuonyesha fadhili zisizofaa. Kwa kuwa fadhili za kweli ni sehemu ya matunda ya roho ya Mungu, fadhili hizo haziwezi kuwa mtazamo dhaifu wa kupuuza mwenendo mbaya. Kwa upande mwingine, fadhili zisizofaa ni udhaifu ambao humfanya mtu afumbie macho mwenendo mbaya.
7. (a) Eli alionyeshaje kwamba alikuwa mlegevu? (b) Kwa nini wazee wanapaswa kuwa waangalifu wasionyeshe fadhili zisizofaa?
7 Kwa mfano, fikiria Eli, kuhani mkuu wa Israeli. Alilegea katika kuwaadhibu wana wake, Hofni na Finehasi, waliokuwa wakitumikia wakiwa makuhani kwenye maskani. Kwa kuwa hawakuridhika na fungu la dhabihu ambalo Sheria ya Mungu iliagiza wapewe, walimwambia mtumishi adai kwa nguvu nyama mbichi kutoka kwa mwenye kutoa dhabihu kabla ya kufukiza moshi wa mafuta kwenye madhabahu. Pia wana wa Eli walifanya uasherati na wanawake waliotumikia kwenye mwingilio wa maskani. Hata hivyo, badala ya kuwaachisha Hofni na Finehasi kazi ya ukuhani, Eli aliwakemea tu kwa upole. (1 Samweli 2:12-29) Haishangazi kwamba “neno kutoka kwa Yehova lilikuwa limekuwa haba siku hizo”! (1 Samweli 3:1) Lazima wazee Wakristo wawe waangalifu ili wasionyeshe fadhili zisizofaa kwa wakosaji ambao wanaweza kuhatarisha hali ya kiroho ya kutaniko. Ukiwa na fadhili za kweli hutapuuza maneno na matendo maovu ambayo huvunja kanuni za Mungu.
8. Yesu alionyeshaje fadhili za kweli?
8 Yesu Kristo, ambaye ni Kielelezo chetu, hakuonyesha kamwe fadhili zisizofaa. Aliweka kielelezo bora sana katika kuonyesha fadhili za kweli. Kwa mfano, ‘aliwaonyesha watu upendo mwororo kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.’ Watu wanyoofu hawakuogopa kumfikia Yesu, hata walimletea watoto wao wadogo. Wazia fadhili na huruma alizoonyesha ‘alipowachukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki.’ (Mathayo 9:36; Marko 10:13-16) Ingawa Yesu alikuwa mwenye fadhili, alikuwa pia imara alipotetea yaliyo sawa machoni pa Baba yake wa mbinguni. Yesu hakuvumilia uovu kamwe; alikuwa na nguvu kutoka kwa Mungu za kuwashutumu viongozi wa kidini wanafiki. Kama inavyoonyeshwa katika Mathayo 23:13-26, alirudia mara kadhaa maneno haya: “Ole wenu ninyi, waandishi na Mafarisayo, wanafiki!”
Fadhili na Sifa Nyingine za Kimungu
9. Sifa ya fadhili inahusianaje na ustahimilivu na wema?
9 Sifa ya fadhili inahusiana na sifa nyingine zinazotokezwa na roho ya Mungu. Sifa hiyo imeorodheshwa katikati ya “ustahimilivu” na “wema.” Kwa kweli, mtu anayesitawisha sifa ya fadhili, huionyesha kwa kuwa mstahimilivu. Anakuwa mwenye subira hata kwa watu wasio na fadhili. Sifa ya fadhili inahusiana na wema katika maana ya kwamba, mara nyingi sifa hiyo huonyeshwa kwa kufanya mambo yanayowanufaisha wengine. Nyakati nyingine, neno la Kigiriki linalotumiwa katika Biblia kumaanisha “fadhili” linaweza kutafsiriwa kuwa “wema.” Wapagani walishangazwa sana na jinsi Wakristo wa mapema walivyoonyesha sifa hiyo hivi kwamba kulingana na Tertullian, waliwaita wafuasi hao wa Yesu ‘watu ambao wanaonyesha fadhili kwa kiwango cha juu zaidi.’
10. Fadhili na upendo zinahusianaje?
10 Kuna uhusiano kati ya fadhili na upendo. Yesu alisema hivi kuhusu wafuasi wake: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Na kuhusu upendo huo Paulo alisema: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili.” (1 Wakorintho 13:4) Sifa ya fadhili pia imehusianishwa na upendo katika maneno “fadhili zenye upendo,” ambayo yametumiwa mara nyingi katika Biblia. Hizi ni fadhili zinazotokana na upendo mshikamanifu. Nomino ya Kiebrania inayotafsiriwa “fadhili zenye upendo” inahusisha mengi zaidi ya upendo mwororo. Ni fadhili ambazo hushikamana kwa upendo na kitu fulani hadi kusudi la kitu hicho litimie. Fadhili zenye upendo za Yehova, au upendo mshikamanifu, huonyeshwa katika njia mbalimbali. Kwa mfano, sifa hiyo huonekana katika matendo yake ya kuokoa na kulinda.—Zaburi 6:4; 40:11; 143:12.
11. Fadhili zenye upendo za Mungu hutupa uhakikisho gani?
11 Fadhili zenye upendo za Yehova huwavuta watu kwake. (Yeremia 31:3) Watumishi waaminifu wa Mungu wanapohitaji kukombolewa au kusaidiwa, wanajua kwamba hakika atawaonyesha fadhili zenye upendo. Hatakosa kufanya hivyo. Hivyo, wanaweza kusali kwa imani kama mtunga-zaburi aliyesema: “Nami nimezitegemea fadhili zako zenye upendo; moyo wangu na ushangilie katika wokovu wako.” (Zaburi 13:5) Kwa kuwa upendo wa Mungu ni mshikamanifu, watumishi wake wanaweza kumtegemea kabisa. Wamehakikishiwa hivi: “Yehova hatawaacha watu wake, wala hatauacha urithi wake mwenyewe.”—Zaburi 94:14.
Kwa Nini Ulimwengu Una Ukatili Mwingi?
12. Utawala wenye kukandamiza ulianza lini na jinsi gani?
12 Jibu la swali hilo linahusiana na yale yaliyotukia katika bustani ya Edeni. Mapema katika historia ya wanadamu, kiumbe mmoja wa roho ambaye aligeuka kuwa mwenye ubinafsi na kiburi, alipanga njama ya kuwa mtawala wa ulimwengu. Kwa sababu hiyo, yeye akawa “mtawala wa ulimwengu huu,” mwenye kukandamiza kwelikweli. (Yohana 12:31) Mtawala huyo akaitwa Shetani Ibilisi, mpinzani mkuu wa Mungu na mwanadamu. (Yohana 8:44; Ufunuo 12:9) Njama yake yenye ubinafsi ya kuanzisha utawala wenye kupinga utawala wenye fadhili wa Yehova ilifichuliwa punde baada ya Hawa kuumbwa. Kwa hiyo, utawala mbaya ulianza wakati Adamu alipokataa utawala wa Mungu, na hivyo kukataa kabisa fadhili Zake. (Mwanzo 3:1-6) Badala ya kupata uhuru wa kweli, Adamu na Hawa walijikuta chini ya uvutano wa Ibilisi wenye ubinafsi na wenye kiburi, hivyo wakawa raia za utawala wake.
13-15. (a) Ni nini baadhi ya matokeo ya kukataa utawala mwadilifu wa Yehova? (b) Kwa nini ulimwengu huu ni mahali penye ukatili?
13 Na tufikirie baadhi ya matokeo ya utawala huo. Adamu na Hawa walifukuzwa kutoka eneo la dunia lililokuwa paradiso. Waliondoka katika bustani nzuri ambapo wangeweza kupata kwa urahisi mimea na matunda yenye kujenga afya, nao wakaenda kuishi maisha magumu nje ya bustani ya Edeni. Mungu alimwambia Adamu: “Kwa sababu uliisikiliza sauti ya mke wako ukala matunda ya mti ambao nilikupa amri hii kuuhusu, ‘Usile matunda yake,’ udongo umelaaniwa kwa sababu yako. Kwa maumivu utakula mazao yake siku zote za maisha yako. Nao utakuzalia miiba na mibaruti.” Laana iliyotolewa juu ya udongo ilimaanisha kwamba sasa ingekuwa vigumu sana kuulima. Wazao wa Adamu waliathiriwa sana na matokeo ya kulaaniwa kwa udongo, uliotokeza miiba na mibaruti, hivi kwamba Lameki, baba ya Noa, alitaja kuhusu ‘maumivu ya mikono yao yaliyoletwa na udongo ambao Yehova aliulaani.’—Mwanzo 3:17-19; 5:29.
14 Adamu na Hawa pia walipoteza utulivu na kuingia katika taabu. Mungu alimwambia Hawa hivi: “Nitazidisha sana maumivu ya mimba yako; kwa uchungu utazaa watoto, na tamaa yako itakuwa kwa mume wako, naye atakutawala.” Baadaye, Kaini, mzaliwa wa kwanza wa Adamu na Hawa, alitenda kitendo kikatili cha kumuua ndugu yake Abeli.—Mwanzo 3:16; 4:8.
15 “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu,” akasema mtume Yohana. (1 Yohana 5:19) Leo, ulimwengu unadhihirisha sifa mbovu kama za mtawala wake ambazo zinatia ndani ubinafsi na kiburi. Haishangazi kwamba umejaa ukatili! Lakini hali hazitakuwa hivyo milele. Yehova atahakikisha kwamba chini ya Ufalme wake watu wataonyesha fadhili na huruma nyingi badala ya ukatili.
Kutakuwa na Fadhili Nyingi Chini ya Ufalme wa Mungu
16. Kwa nini utawala wa Mungu kupitia Kristo Yesu ni wenye fadhili, na hilo hufanya tuwe na wajibu gani?
16 Yehova pamoja na Kristo Yesu, Mfalme wa Ufalme Wake aliyewekwa, wanataka raia zao wawe na sifa ya fadhili. (Mika 6:8) Yesu Kristo alituonyesha kimbele kwamba serikali aliyopewa na Baba yake ingekuwa yenye fadhili. (Waebrania 1:3) Tunaweza kuona hilo kutokana na maneno ya Yesu yaliyowafunua viongozi wa uwongo wa kidini, ambao waliwakandamiza watu kwa mizigo mizito. Alisema: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mathayo 11:28-30) Watawala wengi wa kidunia, wawe wa kidini au wengineo, huwachosha watu kwa sheria nyingi sana na kwa kuwafanyiza kazi bila shukrani. Hata hivyo, Yesu anawataka wafuasi wake wafanye mambo kulingana na mahitaji na uwezo wao. Nira ya Yesu ni yenye fadhili na yenye kuburudisha kwelikweli! Je, hatuchochewi kumwiga katika kuwaonyesha wengine fadhili?—Yohana 13:15.
17, 18. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba wale watakaotawala pamoja na Kristo mbinguni na wawakilishi wake duniani wataonyesha fadhili?
17 Maneno ya Yesu yenye kuvutia kwa mitume wake hukazia jinsi Ufalme wa Mungu ulivyo tofauti kabisa na utawala wa wanadamu. Biblia inasema: “Kukatokea pia bishano kali kati yao [wanafunzi] juu ya ni nani kati yao aliyeonekana kuwa mkuu zaidi ya wote. Lakini akawaambia: ‘Wafalme wa mataifa hupiga ubwana juu yao, na wale walio na mamlaka juu yao huitwa Wafadhili. Ingawa hivyo, ninyi hampaswi kuwa hivyo. Lakini acheni yule aliye mkuu zaidi ya wote kati yenu awe kama aliye mdogo zaidi ya wote, na yule anayetenda kama mkuu kama yule anayehudumu. Kwa maana ni nani aliye mkuu zaidi, yule anayeketi mezani au yule anayehudumu? Je, si yule anayeketi mezani? Lakini mimi nimo katikati yenu kama yule anayehudumu.’”—Luka 22:24-27.
18 Watawala wa kibinadamu hujaribu kuimarisha ukuu wao kwa ‘kupiga ubwana’ juu ya watu na kwa kutafuta majina makubwa ya vyeo kana kwamba majina hayo huwafanya wawe bora kuliko raia zao. Lakini Yesu alisema kwamba ukuu wa kweli hutokana na kuwahudumia wengine, ukifanya hivyo kwa bidii bila kuacha. Wote watakaotawala pamoja na Kristo mbinguni au watakaotumikia duniani wakiwa wawakilishi wake, lazima wajitahidi kufuata kielelezo chake cha unyenyekevu na fadhili.
19, 20. (a) Yesu alionyeshaje namna Yehova alivyo mwenye fadhili nyingi? (b) Tunawezaje kumwiga Yehova katika kuonyesha fadhili?
19 Na tuchunguze shauri lingine la upendo ambalo Yesu alitoa. Akionyesha namna Yehova alivyo mwenye fadhili nyingi, Yesu alisema: “Mkiwapenda wale wanaowapenda ninyi, hilo linawapa sifa gani? Kwa maana hata watenda-dhambi huwapenda wale wanaowapenda wao. Na mkiwatendea mema wale wanaowatendea ninyi mema, kwa kweli hilo linawapa sifa gani? Hata watenda-dhambi hufanya vivyo hivyo. Pia, mkikopesha bila faida wale ambao mnatumaini kupokea kutoka kwao, hilo linawapa sifa gani? Hata watenda-dhambi huwakopesha watenda-dhambi bila faida ili wapate kurudishiwa kwa kadiri ileile. Badala yake, endeleeni kuwapenda adui zenu na kutenda mema na kukopesha bila faida, bila kutumainia kurudishiwa chochote; na thawabu yenu itakuwa kubwa, nanyi mtakuwa wana wa Aliye Juu Zaidi, kwa sababu yeye ni mwenye fadhili kuwaelekea wasio na shukrani na waovu. Endeleeni kuwa wenye rehema, kama vile Baba yenu alivyo mwenye rehema.”—Luka 6:32-36.
20 Fadhili za kimungu hazina ubinafsi. Mungu hatarajii watu wamlipe au wampe kitu fulani ili awaonyeshe fadhili hizo. Kwa fadhili Yehova “hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mathayo 5:43-45; Matendo 14:16, 17) Kwa kumwiga Baba yetu wa mbinguni, sisi hatuepuki tu kuwadhuru watu wasio na shukrani bali huwatendea mema, hata wale ambao wametutendea kama maadui. Kwa kuonyesha fadhili, tunawadhihirishia Yehova na Yesu kwamba tunatamani kuishi chini ya Ufalme wa Mungu, wakati ambapo watu wataonyesha fadhili na sifa nyingine za kimungu katika mahusiano yao yote.
Kwa Nini Tuonyeshe Fadhili?
21, 22. Kwa nini tunapaswa kuonyesha fadhili?
21 Ni muhimu sana kwa Mkristo wa kweli kuonyesha fadhili. Hiyo huthibitisha kwamba tuna roho ya Mungu. Isitoshe, tunapoonyesha fadhili za kweli, tunamwiga Yehova Mungu na Kristo Yesu. Pia fadhili ni takwa kwa wale watakaokuwa raia za Ufalme wa Mungu. Basi, ni lazima tupende fadhili na kujizoeza kuionyesha.
22 Ni katika njia zipi tunaweza kuonyesha fadhili katika maisha yetu? Makala inayofuata itazungumzia habari hiyo.
-
-
Kujitahidi Kuonyesha Fadhili Katika Ulimwengu Wenye UaduiMnara wa Mlinzi—2004 | Aprili 15
-
-
Kujitahidi Kuonyesha Fadhili Katika Ulimwengu Wenye Uadui
“Kinachotamanika katika mtu wa udongo ni fadhili zake zenye upendo.”—METHALI 19:22.
1. Kwa nini inaweza kuwa vigumu kuonyesha fadhili?
JE, WEWE hujiona kuwa mtu mwenye fadhili? Ikiwa ndivyo, inaweza kuwa vigumu kuishi katika ulimwengu wa sasa. Kwa kweli, katika Biblia sifa ya fadhili inatajwa kuwa sehemu ya “matunda ya roho,” lakini kwa nini ni vigumu sana kuonyesha fadhili hata katika nchi zinazoitwa za Kikristo? (Wagalatia 5:22) Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, jibu hilo linaweza kupatikana kwa sehemu katika maneno ambayo mtume Yohana aliandika, yaani, ulimwengu mzima unatawaliwa na mtu fulani wa roho asiye na fadhili, Shetani Ibilisi. (1 Yohana 5:19) Yesu Kristo alimtambulisha Shetani kuwa “mtawala wa ulimwengu.” (Yohana 14:30) Hivyo, ulimwengu huu una mwelekeo kama wa mtawala wake mwasi na mkatili.—Waefeso 2:2.
2. Ni magumu gani yanayoweza kufanya tusionyeshe fadhili?
2 Maisha yetu huathiriwa sana wengine wanapotutendea kwa njia isiyo ya fadhili. Ukosefu huo wa fadhili unaweza kuonyeshwa na majirani wenye chuki, watu wenye ubaridi tusiowajua, na hata marafiki na watu wa familia ambao nyakati nyingine wanaweza kutenda bila kufikiri. Mara nyingi sisi huumizwa sana na mkazo wa kushughulika na watu wenye jeuri, ambao hupigiana kelele na kutukanana. Wengine wanapokosa kuonyesha fadhili, jambo hilo linaweza kutufanya tuwe na chuki, na huenda tukataka kulipiza kisasi kwa kuwatendea wengine bila fadhili. Huenda mtazamo huo hata ukasababisha matatizo ya afya ya kimwili au ya kiroho.—Waroma 12:17.
3. Watu hukabili matatizo gani makubwa ambayo hufanya iwe vigumu kwao kuonyesha fadhili?
3 Pia hali za ulimwengu zenye mkazo zinaweza kufanya iwe vigumu kwetu kuonyesha fadhili. Kwa mfano, wanadamu kwa ujumla hupatwa na mkazo kwa sababu ya vitisho na vitendo vya kigaidi, na pia uwezekano wa kutumiwa kwa silaha za kibiolojia au za nyuklia na vikundi mbalimbali vya mataifa. Isitoshe, mamilioni ya watu ni maskini, nao hupata chakula, makao, mavazi, na matibabu ya kuwawezesha tu kuendelea kuishi. Inakuwa vigumu kufuatia fadhili hali zinapoonekana kuwa zenye kukatisha tamaa.—Mhubiri 7:7.
4. Watu fulani wanaweza kufikia mkataa gani wenye makosa wanapofikiria kuwaonyesha wengine fadhili?
4 Mtu anaweza kufikia mkataa kwa urahisi kwamba si jambo muhimu sana kuonyesha fadhili na huenda hata akaona kufanya hivyo kuwa ishara ya udhaifu. Huenda akahisi ametendewa isivyo haki hasa wengine wanapomtendea bila kujali hisia zake. (Zaburi 73:2-9) Hata hivyo, Biblia inatutolea mwongozo ufaao inaposema: “Jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu, lakini neno linaloumiza hufanya hasira ipande.” (Methali 15:1) Upole na fadhili ni sehemu mbili za matunda ya roho yanayohusiana sana, na hizo ni sifa muhimu sana mtu anapokabili hali ngumu.
5. Tunahitaji kuonyesha fadhili katika sehemu zipi za maisha?
5 Kwa kuwa ni muhimu sana kuonyesha matunda ya roho takatifu ya Mungu tukiwa Wakristo, tunapaswa kufikiria jinsi tunavyoweza kuonyesha mojawapo ya sifa hizo, yaani, fadhili. Je, inawezekana kufuatia fadhili katika ulimwengu wenye uadui? Ikiwa ndivyo, ni katika njia zipi tunaweza kuonyesha kwamba haturuhusu uvutano wa Shetani utuzuie kuonyesha fadhili, hasa tunapokabili mikazo? Na tuone jinsi tunavyoweza kufuatia fadhili katika familia, katika huduma, kazini, shuleni, na pamoja na majirani na waamini wenzetu.
Fadhili Katika Familia
6. Kwa nini sifa ya fadhili ni muhimu sana katika familia, nayo inaweza kuonyeshwaje?
6 Ili kupata baraka na mwongozo wa Yehova, matunda ya roho ni muhimu, nayo yanahitaji kusitawishwa kikamili. (Waefeso 4:32) Na tuzungumzie uhitaji wa washiriki wa familia wa kuonyeshana fadhili. Katika shughuli zao za kila siku, mume na mke wanapaswa kuonyesha roho ya fadhili na ya kujali kati yao na kwa watoto wao. (Waefeso 5:28-33; 6:1, 2) Sifa hiyo ya fadhili inahitaji kuwa wazi katika njia ambayo washiriki wa familia huzungumziana, huku watoto wakiwaheshimu wazazi, nao wazazi wakiwatendea watoto wao ifaavyo. Usiwe mwepesi kushutumu, bali uwe mwepesi kupongeza.
7, 8. (a) Tunapaswa kuepuka mwenendo gani ili kuonyesha fadhili za kweli katika familia? (b) Mawasiliano mazuri husaidiaje kuwa na familia thabiti? (c) Unawezaje kuonyesha fadhili katika familia yako?
7 Ili tuwe wenye fadhili kwa washiriki wa familia yetu tunahitaji kufuata shauri hili la mtume Paulo: “Kwa kweli, yaondoleeni mbali mambo haya yote kutoka kwenu, ghadhabu, hasira, ubaya, matukano, na maneno machafu kutoka kinywani mwenu.” Familia za Wakristo zinapaswa kuwasiliana kila siku kwa heshima. Kwa nini? Kwa sababu mawasiliano mazuri ni muhimu ili familia ziwe thabiti. Ili kutuliza hali wakati kutoelewana kunapotokea, jaribu kutatua tatizo badala ya kujaribu kushinda mabishano. Washiriki wa familia wenye furaha hujitahidi sana kukuza fadhili na huruma kati yao.—Wakolosai 3:8, 12-14.
8 Fadhili ni sifa nzuri ambayo hutuchochea kuwatendea wengine mema. Hivyo, sisi hujitahidi kuwasaidia na kuwaonyesha ufikirio washiriki wengine wa familia katika njia yenye kupendeza. Jitihada ya kila mmoja na wote kwa ujumla inahitajiwa ili kuonyesha fadhili ambayo huiletea familia sifa. Kwa kufanya hivyo, watapata baraka za Mungu, nao watamheshimu Yehova, Mungu wa fadhili, kutanikoni na mahali wanapoishi.—1 Petro 2:12.
Fadhili Kazini
9, 10. Taja baadhi ya matatizo yanayoweza kutokea kazini, na eleza jinsi yanavyoweza kutatuliwa kwa fadhili.
9 Huenda ikawa vigumu kwa Mkristo kuwaonyesha fadhili wafanyakazi wenzake katika shughuli za kila siku kazini. Huenda mashindano kati ya wafanyakazi yakahatarisha kazi ya mtu pale mfanyakazi mwenzake anapotumia udanganyifu au hila ili amharibie sifa kwa mkubwa wa kazi. (Mhubiri 4:4) Si rahisi kuonyesha fadhili nyakati kama hizo. Hata hivyo, kwa kukumbuka kwamba kuonyesha fadhili ndilo jambo linalofaa, mtumishi wa Yehova anapaswa kujitahidi kadiri awezavyo ili awavute wale ambao ni vigumu kupatana nao. Kuonyesha kwamba tunawajali kunaweza kutusaidia kuwavuta. Labda unaweza kuonyesha kwamba unajali ikiwa mfanyakazi mwenzako ni mgonjwa au washiriki fulani wa familia yake ni wagonjwa. Hata kumjulia hali kunaweza kufanya awe na maoni yanayofaa. Naam, Wakristo wanapaswa kujitahidi kukuza upatano na amani kwa kadiri inavyowategemea. Nyakati nyingine neno la fadhili linaloonyesha kwamba unajali linaweza kuboresha hali hiyo.
10 Pindi nyingine, huenda mkubwa wa kazi akalazimisha wafanyakazi wake wakubali maoni yake ama akataka kila mtu ashiriki katika sherehe fulani za kutukuza taifa au sherehe nyingine isiyopatana na Maandiko. Huenda hali ya kutoelewana ikatokea iwapo dhamiri ya Mkristo haitamruhusu kushiriki katika sherehe hizo. Wakati huo huenda lisiwe jambo la hekima kumweleza kindani mkubwa wa kazi ubaya wa kukubaliana na mapendezi yake. Hiyo ni kwa sababu huenda watu wasioamini wasione ubaya wowote wa kushiriki katika sherehe hiyo. (1 Petro 2:21-23) Labda unaweza kueleza kwa fadhili sababu zako za kutoshiriki. Usilipize kisasi kwa kumdhihaki mtu anayekudhihaki. Inafaa Mkristo kufuata shauri hili zuri la Waroma 12:18: “Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”
Fadhili Shuleni
11. Vijana hukabili magumu gani wanapoonyesha fadhili kwa wanafunzi wenzao?
11 Inaweza kuwa vigumu sana kwa vijana kuwaonyesha wanafunzi wenzao fadhili. Mara nyingi vijana hutamani kukubaliwa na wanafunzi wenzao. Ili kuwavutia wanafunzi wengine, wavulana fulani hutenda kijeuri na hata huwadhulumu wengine shuleni. (Mathayo 20:25) Vijana wengine hupenda kujionyesha wao ni bora katika masomo, michezo, au katika mambo mengine. Ili kuonyesha ustadi wao, mara nyingi wao huwatendea wanadarasa na wanafunzi wengine kwa njia isiyo ya fadhili, wakifikiri kimakosa kwamba kufanya hivyo kutawafanya wawe bora kwa njia moja au nyingine. Kijana Mkristo anapaswa kujihadhari asiwaige vijana hao. (Mathayo 20:26, 27) Mtume Paulo alisema kwamba “upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili” na kwamba ‘haujigambi wala haujivuni.’ Hivyo, Mkristo anapaswa kufuata shauri la Kimaandiko anaposhughulika na wanafunzi wenzake badala ya kufuata kielelezo kibaya cha wale wanaotenda bila fadhili.—1 Wakorintho 13:4.
12. (a) Kwa nini inaweza kuwa vigumu kwa vijana kuwaonyesha walimu wao fadhili? (b) Vijana wanaweza kutafuta msaada wa nani wanapokazwa wasionyeshe fadhili?
12 Vijana wanapaswa pia kuwatendea walimu wao kwa fadhili. Wanafunzi wengi hufurahia kuwakasirisha walimu wao. Wao hujiona kwamba ni werevu wanapokosa kuwaheshimu walimu wao kwa vitendo vinavyovunja sheria za shule. Huenda wakawatisha wengine ili wawaunge mkono. Kijana Mkristo anapokataa kuwaunga mkono, huenda wakamdhihaki au kumtukana. Azimio la Mkristo la kuonyesha fadhili linaweza kujaribiwa anapokabili hali kama hizo kila mwaka shuleni. Hata hivyo, kumbuka kwamba ni muhimu kuwa mtumishi mshikamanifu wa Yehova. Uwe na hakika kwamba atakutegemeza kwa roho yake nyakati hizo ngumu maishani.—Zaburi 37:28.
Fadhili kwa Majirani
13-15. Ni nini kinachoweza kutuzuia tusiwaonyeshe majirani wetu fadhili, na tunawezaje kukabiliana na magumu hayo?
13 Uwe unaishi katika nyumba ya orofa, nyumba ya kawaida, au mahali pengine, unaweza kufikiria njia za kuonyesha kwamba una fadhili na unawajali majirani. Jambo hilo pia si rahisi.
14 Namna gani ikiwa unabaguliwa na majirani wako wa karibu kwa sababu ya rangi, taifa, au dini? Namna gani ikiwa nyakati nyingine ni wajeuri au wanakupuuza kabisa? Ukiwa mtumishi wa Yehova, utanufaika kwa kuonyesha fadhili kadiri uwezavyo. Utakuwa tofauti kwa njia yenye kuburudisha, na jambo hilo linamtukuza Yehova ambaye ni kielelezo bora cha fadhili. Huwezi kujua wakati ambapo jirani yako anaweza kubadili maoni yake kwa sababu ya fadhili zako. Huenda hata akawa msifaji wa Yehova.—1 Petro 2:12.
15 Fadhili zinaweza kuonyeshwaje? Njia moja ni kupitia mwenendo mzuri katika familia, huku wote wakionyesha matunda ya roho. Huenda majirani wakatambua jambo hilo. Nyakati nyingine unaweza kumtendea jirani yako kwa fadhili. Kumbuka kwamba fadhili humaanisha kupendezwa na wengine.—1 Petro 3:8-12.
Fadhili Katika Huduma Yetu
16, 17. (a) Kwa nini fadhili ni muhimu katika huduma yetu ya hadharani? (b) Tunawezaje kuonyesha fadhili tunaposhiriki sehemu mbalimbali za huduma yetu?
16 Tunapaswa kuonyesha fadhili katika huduma yetu ya Kikristo tunapojitahidi kuwatembelea watu makwao, kazini, na katika sehemu za umma. Tunapaswa kukumbuka kwamba tunamwakilisha Yehova, ambaye huonyesha fadhili sikuzote.—Kutoka 34:6.
17 Ni nini kinachohusika katika jitihada zako za kuonyesha fadhili katika huduma? Kwa mfano, unapohubiri barabarani, unaweza kuonyesha watu fadhili kwa kuwafikiria na kuongea nao kwa ufupi unapowafikia. Kwa kawaida njia za wanaotembea kwa miguu huwa na watu wengi, kwa hiyo uwe mwangalifu usifunge njia. Pia, unapohubiri katika eneo la biashara, onyesha fadhili kwa kuongea kwa ufupi, huku ukikumbuka kwamba wenye maduka wanahitaji kuwahudumia wateja.
18. Utambuzi hutimiza fungu gani katika kuonyesha fadhili katika huduma yetu?
18 Tumia busara katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Usikae sana katika nyumba moja, hasa ikiwa hali ya hewa si nzuri. Je, unaweza kutambua mtu anapoanza kukosa subira au hata kuudhiwa na ziara yako? Labda katika sehemu unayoishi ulimwenguni, Mashahidi wa Yehova hutembelea watu mara nyingi sana. Ikiwa ndivyo ilivyo, onyesha unafikiria hali za watu kwa njia ya pekee, sikuzote ukiwa mwenye fadhili na mchangamfu. (Methali 17:14) Jaribu kuonyesha kwamba unaelewa ni kwa nini mwenye nyumba hataki kusikiliza siku hiyo. Kumbuka kwamba huenda mmoja wa ndugu au dada zako Wakristo akatembelea nyumba hiyo karibuni. Ukikutana na mtu mjeuri, jitahidi sana kumwonyesha fadhili. Usizungumze kwa sauti kubwa au kukunja uso, bali zungumza kwa utulivu. Mkristo mwenye fadhili hangependa kuanzisha mabishano na mwenye nyumba. (Mathayo 10:11-14) Labda siku moja mtu huyo atasikiliza habari njema.
Fadhili Katika Mikutano ya Kutaniko
19, 20. Kwa nini fadhili zinahitajiwa kutanikoni, nazo zinaweza kuonyeshwaje?
19 Ni muhimu pia kuwaonyesha waamini wenzetu fadhili. (Waebrania 13:1) Kwa kuwa sisi ni sehemu ya undugu wa ulimwenguni pote, fadhili ni sifa muhimu tunaposhughulika na mmoja na mwenzake.
20 Ikiwa kutaniko linatumia Jumba la Ufalme pamoja na makutaniko mengine, ni muhimu kushughulika kwa fadhili na akina ndugu wa makutaniko hayo mengine, na kuwaonyesha heshima. Mashindano huharibu roho ya ushirikiano katika kupanga saa za mikutano, na mambo ya lazima kama vile usafi au urekebishaji. Uwe mwenye fadhili na mwenye kufikiria wengine hata ingawa huenda maoni yakatofautiana. Katika njia hiyo, fadhili zitashinda, naye Yehova atakubariki sana kwa kuonyesha kwamba unawajali wengine.
Endeleeni Kuonyesha Fadhili
21, 22. Kupatana na Wakolosai 3:12, azimio letu linapaswa kuwa nini?
21 Sifa ya fadhili inatia ndani mambo mengi sana hivi kwamba inagusa kila sehemu ya maisha yetu. Kwa hiyo, tunapaswa kuifanya iwe sehemu muhimu ya utu wetu wa Kikristo. Kuwaonyesha wengine fadhili kwapaswa kuwa zoea.
22 Sote na tuwaonyeshe wengine fadhili kila siku na hivyo kufuata maneno haya ya mtume Paulo: “Kama waliochaguliwa wa Mungu, watakatifu na wapendwa, jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu.”—Wakolosai 3:12.
-