-
Kujenga Pamoja Duniani PoteMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Majumba ya Ufalme
Kama ilivyokuwa kwa Wakristo wa karne ya kwanza, mwanzoni makutaniko mengi ya Mashahidi wa Yehova yalitumia makao ya faragha kwa mikutano yao mingi. Katika Stockholm, Sweden, wale wachache wa kwanza waliofanya mikutano ya ukawaida huko walitumia duka la useremala, ambalo walikodi ili walitumie baada ya kazi ya siku kufanywa. Kwa sababu ya mnyanyaso, kikundi kidogo katika mkoa wa La Coruña, Hispania, kilifanya mikutano yao ya kwanza katika bohari, au ghala ndogo.
Wakati nafasi zaidi ilipohitajiwa, katika nchi zilizokuwa na uhuru wa kufanya hivyo, makutaniko ya mahali ya Mashahidi wa Yehova yangekodi mahali pa mikutano. Hata hivyo, ikiwa jumba hilo lilikuwa likitumiwa pia na matengenezo mengine, ilibidi kusafirisha vifaa au kuviandaa kwa matumizi kwa ajili ya kila mkutano, na mara nyingi kulikuwako harufu ya tumbako iliyobakia. Mahali ilipowezekana, akina ndugu wangekodi duka lisilotumiwa au chumba cha orofa ambacho kingetumiwa na kutaniko pekee. Lakini, baada ya wakati, katika mahali pengi gharama za juu za kukodi na kutopatikana kwa mahali pafaapo kulifanya iwe lazima kufanya mipango mingine. Katika visa fulani majengo yalinunuliwa na kurekebishwa upya.
Kabla ya Vita ya Ulimwengu 2, yalikuwako makutaniko machache yaliyojenga mahali pa kukutana palipokusudiwa hasa kwa matumizi yao. Hata mapema sana kama 1890, kikundi cha Wanafunzi wa Biblia katika Marekani katika Mount Lookout, West Virginia, kilijenga mahali pacho chenyewe pa kukutanikia.a Hata hivyo, ujenzi wa Majumba ya Ufalme wenye kuenea haukuanza mpaka miaka ya 1950.
Jina Jumba la Ufalme lilidokezwa katika 1935 na J. F. Rutherford, aliyekuwa wakati huo msimamizi wa Watch Tower Society. Kuhusiana na vifaa vya tawi la Sosaiti katika Honolulu, Hawaii, alipanga ndugu wajenge jumba ambamo mikutano ingefanyiwa. Wakati James Harrub alipouliza Ndugu Rutherford angeliitaje jengo hilo, yeye alijibu: “Waonaje tukiliita kwa jina ‘Jumba la Ufalme,’ kwa kuwa ndivyo tunavyofanya, kuhubiri habari njema za Ufalme?” Baada ya hapo, ilipowezekana, majumba yaliyokuwa yakitumiwa kwa ukawaida na Mashahidi yakaanza hatua kwa hatua kutambulishwa kwa ishara zilizosema “Jumba la Ufalme.” Hivyo, wakati London Tabernacle liliporekebishwa upya katika 1937-1938, lilipewa jina jipya Jumba la Ufalme. Baada ya wakati, mahali pakuu pa mikutano pa makutaniko ulimwenguni pote pakaja kuitwa Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova.
Njia Zaidi ya Moja za Kujenga
Maamuzi juu ya kama watakodi au kujenga Majumba ya Ufalme hufanywa na makutaniko yenyewe mojamoja. Pia hayo hulipia gharama zozote za ujenzi na udumishaji. Ili kuokoa fedha, makutaniko mengi yamejitahidi kufanya kazi nyingi ya ujenzi kadiri inavyowezekana bila kuajiri wafanyakazi wa mkataba wa kulipwa.
Majumba yenyewe yaweza kujengwa kwa matufali, mawe, na mbao, au vifaa vingine, ikitegemea gharama pamoja na vifaa vinavyopatikana katika eneo. Katika Katima Mulilo, Namibia, nyasi ndefu zilitumiwa kwa ajili ya paa, na udongo kutoka vichuguu (ambao hukauka na kuwa imara sana) ulifinyangwa kuwa ukuta na sakafu. Mashahidi katika Segovia, Kolombia, walitengeneza matufali ya saruji yao wenyewe ya kujengea. Mawe ya volkano kutoka Mlima Lasen yalitumiwa katika Colfax, California.
Hudhurio la mikutano mara nyingi likiwa linazidi 200 katika 1972, kutaniko katika Maseru, Lesotho, lilijua kwamba walihitaji kujenga Jumba la Ufalme lifaalo. Kila mtu alisaidia katika mradi huo. Ndugu wazee-wazee walitembea kufikia kilometa 32 ili kushiriki. Watoto walivingirisha mapipa ya maji kuyaleta kwenye mahali pa ujenzi. Dada waliandaa milo. Pia walitumia nyayo zao kutwanga ardhi, ili kuiimarisha katika kuitayarisha kwa ajili ya kumwagwa kwa bamba la zege, wakati wote wakiimba nyimbo za Ufalme na kukanyagakanyaga chini kwa kufuatana na mwendo wa muziki. Changarawe, iliyogharimu kuisafirisha tu kutoka milima ya karibu, ilitumiwa kwa ajili ya kuta. Tokeo likawa Jumba la Ufalme ambalo lingeweza kutoshea watu kama 250.
Nyakati nyingine, Mashahidi kutoka makutaniko ya karibu walisaidia kazi ya ujenzi. Hivyo, katika 1985, wakati Mashahidi wa Yehova katika Imbali, mji wa weusi katika Afrika Kusini, walipojenga jumba ambalo lingeweza kutoshea watu 400 vizuri, Mashahidi wenzao kutoka majiji ya karibu ya Pietermaritzburg na Durban walikuja kusaidia. Je, waweza kuwazia jinsi majirani walivyoshangaa wakati, katika pindi ya siku hizo za msukosuko wa tofauti za rangi katika Afrika Kusini, walipoona vikundi vya Mashahidi weupe, Machotara, na Wahindi wakimiminika katika mji na kufanya kazi bega kwa bega pamoja na ndugu zao Waafrika weusi? Kama vile meya mwenyeji alivyojulisha: “Laweza kufanywa kwa upendo tu.”
Hata roho ya kupenda iweje, makutaniko yaliona kwamba hali za mahali zilizuia yale ambayo ndugu wangeweza kufanya. Wanaume kutanikoni walikuwa na familia za kuruzuku na kwa kawaida wangeweza kufanya kazi kwenye mradi huo wakati wa miisho-juma tu na labda kidogo jioni. Makutaniko mengi yalikuwa na mafundi wa ujenzi wachache tu. Hata hivyo, jengo ambalo kidogo ni rahisi, lililo wazi kidogo lifaalo hali za tropiki lingeweza kujengwa kwa siku chache au labda majuma machache. Kwa msaada wa Mashahidi katika makutaniko ya karibu, majengo imara zaidi yangeweza kukamilishwa kwa miezi mitano au sita. Katika visa vingine ilitaka mwaka mmoja au miwili.
Hata hivyo, walipokuwa wakisonga kuingia katika miaka ya 1970, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote walikuwa wakiongezeka kwa kadiri ya makutaniko mawili au matatu mapya kila siku. Kufikia miaka ya mapema ya 1990, kadiri ya ongezeko ilifikia makutaniko tisa kwa siku. Je, uhitaji wao mkubwa wa Majumba ya Ufalme mapya ungeweza kutimizwa?
Kusitawisha Mbinu za Ujenzi wa Haraka
Mapema katika miaka ya 1970, katika Marekani, Mashahidi zaidi ya 50 kutoka makutaniko ya karibu walikuja pamoja ili kusaidia kujenga Jumba la Ufalme jipya katika Carterville, Missouri, kwa ajili ya kikundi kilichokuwa kikikutana katika Jiji la Webb. Katika mwisho-juma mmoja walijenga kiunzi kikuu na kufanya kazi kubwa kwenye paa. Kulikuwa kungali na mengi ya kufanywa, na ilichukua miezi kadhaa kumaliza kazi; lakini sehemu ya maana yalo ilikuwa imekamilishwa kwa kipindi kifupi.
Wakati wa mwongo uliofuata, kadiri akina ndugu walivyofanya kazi pamoja kujenga majumba kama 60, vizuizi vilishindwa, na njia zenye matokeo zaidi zikasitawishwa. Baada ya wakati, walipata kuona kwamba baada ya kazi ya msingi kufanywa, wangeweza kukaribia kukamilisha Jumba la Ufalme lote kwa mwisho-juma mmoja.
Waangalizi kadhaa wa makutaniko—wote kutoka magharibi-kati mwa Marekani—walianza kujitahidi kufikia mradi huo. Wakati makutaniko yalipoomba msaada wa kujenga Jumba la Ufalme lao, mmoja au zaidi wa akina ndugu hao angezungumzia mradi huo pamoja nao na kuandaa mambo mengi madogomadogo kuhusu matayarisho ambayo lazima yashughulikiwe na wenyeji kabla ya kazi kuanza kufanywa. Miongoni mwa mambo mengine, ilibidi ruhusa za ujenzi zipatikane, ilibidi msingi na bamba la sakafu la zege vimwagwe, ilibidi umeme uwe unafanya kazi, ilibidi mabomba ya maji ya chini ya ardhi yawe yamewekwa mahali payo, na ilibidi ifanywe mipango yenye kutegemeka ya kuleta vifaa vya ujenzi. Kisha tarehe ingeweza kuwekwa ya ujenzi wa Jumba la Ufalme lenyewe. Jengo hilo halingekuwa limetangulia kuundwa; lingejengwa toka chini hadi juu mahali papo hapo pa ujenzi.
Ni nani wangefanya hasa kazi ya ujenzi? Kwa kadiri ilivyowezekana, ilifanywa na wafanyakazi wa kujitolea, wasiolipwa. Familia nzimanzima mara nyingi zilishiriki. Wale wenye kupanga mradi huo waliwasiliana na Mashahidi waliokuwa mafundi na ambao walikuwa wameeleza nia yao ya kushiriki katika miradi hiyo. Wengi wao walitazamia kwa hamu kila mradi mpya wa ujenzi. Mashahidi wengine waliopata kujua juu ya miradi hiyo walitaka kushiriki; mamia kutoka eneo la karibu—na kutoka sehemu za mbali zaidi—walimiminika kwenye mahali pa ujenzi, wakiwa na hamu ya kutoa utumishi wao mbalimbali katika njia yoyote waliyoweza. Walio wengi wao hawakuwa wajenzi stadi, lakini hakika walitoa ithibati kwamba wao walifaana na maelezo ya wale ambao wangekuwa waungaji mkono wa Mfalme wa Kimesiya wa Yehova kama ilivyoandikwa kwenye Zaburi 110:3, ambalo husema: “Watu wako wanajitoa kwa hiari.”
Alhamisi jioni kabla ya ile jitihada kubwa kuanza, wale waliokuwa wakisimamia ujenzi walikutana ili kupanga mambo madogomadogo ya mwisho. Jioni iliyofuata, wafanyakazi walionyeshwa slaidi juu ya utaratibu ili waelewe jinsi ambavyo kazi ingefanywa. Mkazo ulitiwa juu ya umaana wa sifa za kimungu. Ndugu walitiwa moyo wafanye kazi pamoja kwa upendo, wawe wenye fadhili, na kuonyesha saburi na ufikirio. Kila mtu alitiwa moyo afanye kazi kwa mwendo wa taratibu lakini asiharakishe na asisite kuchukua dakika chache kushiriki pamoja na mwingine jambo lililoonwa lenye kujenga. Mapema asubuhi iliyofuata, ujenzi ulianza.
Katika wakati uliopangwa mapema Jumamosi asubuhi, kila mtu angeacha kufanya alilokuwa akifanya ili kusikiliza mazungumzo ya Andiko la siku. Sala ilitolewa, maana ilifahamiwa vema kwamba fanikio la mradi wote lilitegemea baraka ya Yehova.—Zab. 127:1.
Kazi ilipoanza, hiyo ilisonga mbele kasi. Katika muda wa saa moja kuta zilikuwa zimesimama. Farasi za paa zilifuata. Kufunika kuta kukamalizwa. Mafundi wa umeme wakaanza kuzungusha waya. Vitundu vya visawazishahewa vikawekwa. Kabati zikajengwa pahali pazo. Nyakati nyingine kulinyesha mwisho-juma wote, au halihewa iligeuka kuwa baridi sana au joto sana, lakini kazi ilisonga mbele. Hakukuwa na mashindano au ushindani miongoni mwa mafundi.
Mara nyingi, kabla ya jua kushuka katika siku ya pili, Jumba la Ufalme lilikuwa limekamilishwa—limepambwa vizuri ndani, labda hata kupambwa mandhari ya nje. Ilipofaa zaidi, kazi ziliratibiwa ziendelee kwa siku tatu, au labda miisho-juma miwili. Mwishoni mwa mradi, walio wengi kati ya wafanyakazi wangebaki, wakiwa wamechoka lakini wenye furaha sana, wafurahie mkutano wa kwanza wa kawaida wa kutaniko, funzo la Mnara wa Mlinzi.
Wakitia shaka kwamba kazi nzuri ingeweza kufanywa kwa haraka sana jinsi hiyo, watu kadhaa katika Guymon, Oklahoma, Marekani, waliita mkaguzi wa ujenzi wa jiji. “Niliwaambia kwamba kama walitaka kuona jambo lililofanywa sawasawa, yawapasa kuzuru jumba hilo!” akasema mkaguzi huyo baadaye alipokuwa akisimulia Mashahidi kisa hicho. “Nyinyi watu hata mnafanya sawasawa yale yaliyofichika na yasiyoonekana!”
Kadiri uhitaji wa Majumba ya Ufalme ulivyoongezeka, ndugu waliokuwa wamesitawisha zile njia nyingi za ujenzi wa haraka walizoeza wengine. Ripoti za yale yaliyokuwa yakifanywa zilienea kwenye nchi nyinginezo. Je, njia hizo za ujenzi zingeweza kutumiwa huko pia?
Ujenzi wa Haraka Wafanywa Kuwa wa Kimataifa
Ujenzi wa Majumba ya Ufalme katika Kanada ulikuwa ukiachwa nyuma sana na mahitaji ya makutaniko. Mashahidi katika Kanada walialika wale waliokuwa wakipanga miradi ya ujenzi wa haraka katika Marekani waje wawaeleze jinsi walivyoufanya. Mwanzoni, Wakanada walikuwa na shaka kidogo kwamba wangeweza kujenga hivyo katika Kanada, lakini waliamua kujaribu. Jumba la Ufalme la kwanza lililojengwa kwa njia hiyo katika Kanada lilijengwa katika Elmira, Ontario, katika 1982. Kufikia 1992, kulikuwa Majumba ya Ufalme 306 katika Kanada yaliyokuwa yamejengwa kwa njia hiyo.
Mashahidi katika Northampton, Uingereza, walifikiri kuwa wangeweza kufanya hivyo pia. Mradi wao, katika 1983, ulikuwa ndio wa kwanza katika Ulaya. Ndugu wenye ujuzi katika namna hiyo ya ujenzi walisafiri kutoka Marekani na Kanada ili kusimamia mradi huo na kusaidia Mashahidi wenyeji wajifunze jinsi ya kuufanya. Wenye kujitolea wengine walikuwapo kutoka mbali sana kama vile Japani, India, Ufaransa, na Ujerumani. Walikuwapo wakiwa wenye kujitolea, si ili kulipwa. Yote yaliwezekanaje? Kama vile mwangalizi wa kikundi kimoja cha Mashahidi wa Ireland kilichofanya kazi katika mradi kama huo alivyosema, ‘Yanafanikiwa kwa sababu ndugu na dada wote hushirikiana chini ya uvutano wa roho ya Yehova.’
Hata wakati sheria za ujenzi za mahali zinapoonekana zikifanya miradi kama hiyo isiwezekane, Mashahidi wamepata kwamba, mara nyingi, wakati maofisa wa jiji wanapoelezwa mambo kirefu, wanakuwa na furaha kushirikiana.
Baada ya mradi wa ujenzi wa haraka katika Norway, kaskazini mwa Mzingo wa Aktiki, gazeti Finnmarken lilieleza kwa mshangao hivi: “Ajabu kabisa. Hayo ndiyo maneno pekee tuwezayo kupata ya kuelezea waliyofanya Mashahidi wa Yehova mwisho-juma uliopita.” Vivyo hivyo, wakati Mashahidi katika Kisiwa cha Kaskazini cha New Zealand walipojenga Jumba la Ufalme lenye kuvutia kwa siku mbili na nusu, kichwa kikuu cha habari kwenye ukurasa wa mbele katika gazeti la mahali hapo kilijulisha: “Mradi Wakaribia Kuwa Muujiza.” Makala hiyo iliongeza: “Labda sehemu ya mradi huo yenye kuduwaza akili zaidi ni upangaji mzuri wa mambo na uendeshaji-mambo wenye utulivu kabisa.”
Umbali wa mahali panapohitaji Jumba la Ufalme hauthibitiki kuwa kizuizi kisichoshindika. Katika Belize mradi wa ujenzi wa haraka ulifanywa, hata ingawa ilimaanisha kusafirisha kila kipande cha kifaa cha ujenzi hadi kwenye kisiwa kilometa 60 kutoka Jiji la Belize. Wakati Jumba la Ufalme lenye kifaa cha kusawazisha hewa lilipojengwa katika Port Hedland, Australia Magharibi, mwisho-juma mmoja, lilijengwa kwa vifaa na wafanyakazi ambao karibu wote walikuja kutoka umbali wa kilometa 1,600 au zaidi. Wafanyakazi wenyewe walijilipia nauli zao wenyewe. Walio wengi kati ya wale walioshiriki sehemu katika mradi huo hawakujua kibinafsi Mashahidi katika Kutaniko la Port Hedland, na ni wachache sana kati yao ambao wangepata kuhudhuria mikutano humo wakati wowote. Lakini hiyo haikuwazuia kuonyesha upendo wao katika njia hiyo.
Hata kukiwa na idadi ndogo ya Mashahidi mahali fulani, hilo halizuii utumizi wa njia hizo za kujenga majumba. Mashahidi kama 800 kutoka Trinidad walijitolea kusafiri hadi Tobago ili kusaidia ndugu na dada zao Wakristo 84 wa huko wajenge jumba katika Scarborough katika 1985. Wale Mashahidi 17 (wengi wao wakiwa wanawake na watoto) katika Goose Bay, Labrador, bila shaka walihitaji msaada ikiwa wangeweza wakati wowote kupata Jumba la Ufalme lao wenyewe. Katika 1985, Mashahidi kutoka sehemu nyingine za Kanada walikodi ndege tatu ili kusafirisha 450 kati yao hadi Goose Bay ili kufanya kazi hiyo. Baada ya siku mbili za kazi ya bidii, walikuwa na programu ya kuwekwa wakfu katika jumba lililokamilika jioni ya Jumapili.
Hiyo haimaanishi kwamba Majumba ya Ufalme yote sasa yanajengwa kwa njia za ujenzi wa haraka, lakini idadi yayo inayozidi kukua yanajengwa hivyo.
Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa
Kufikia katikati ya 1986 kadiri ambayo Majumba ya Ufalme yalihitajiwa ilikuwa imeongezeka sana. Wakati wa mwaka uliotangulia, makutaniko mapya 2,461 yalikuwa yameundwa ulimwenguni pote; 207 kati ya hayo yalikuwa katika Marekani. Baadhi ya Majumba ya Ufalme yalikuwa yakitumiwa na makutaniko matatu, manne, au hata matano. Kama vile Maandiko yalivyokuwa yametabiri, kwelikweli Yehova alikuwa akiharakisha kazi ya kukusanya kuleta ndani.—Isa. 60:22.
Ili kuhakikisha utumizi bora zaidi wa wafanyakazi na kuwezesha wote waliokuwa wakijenga Majumba ya Ufalme wanufaike kutokana na ujuzi uliokuwa umepatikana, Sosaiti ilianza kuratibu utendaji wao. Ukiwa mwanzo, katika 1987 Marekani iligawanywa miongoni mwa Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa 60. Kulikuwa mengi ya kufanywa na hizo zote; upesi baadhi yazo zilikuwa na miradi iliyopangwa kwa mwaka mmoja au zaidi. Wale waliowekwa kutumikia kwenye halmashauri hizo walikuwa wanaume ambao, kwanza kabisa, walikuwa wamestahili kiroho, wazee katika makutaniko, walio vielelezo vizuri katika kudhihirisha matunda ya roho ya Mungu. (Gal. 5:22, 23) Wengi wao pia walikuwa na ujuzi katika kushughulikia mambo ya mashamba na nyumba, uhandisi, ujenzi, usimamizi wa biashara, usalama, na nyanja zinazohusiana.
Makutaniko yalitiwa moyo yashauriane na Halmashauri ya Ujenzi ya Kimkoa kabla ya kuchagua mahali pa kujenga Jumba la Ufalme jipya. Mahali mlimokuwa na zaidi ya kutaniko moja jijini, walihimizwa pia kushauriana na mwangalizi au waangalizi wa mizunguko, mwangalizi wa jiji, na wazee kutoka makutaniko ya karibu. Makutaniko yaliyokuwa yakipanga urekebishaji mkubwa wa jengo la zamani au ujenzi wa Jumba la Ufalme jipya yalishauriwa yanufaike na ujuzi wa ndugu wa Halmashauri ya Ujenzi ya Kimkoa ya eneo lao na kwa miongozo ambayo Sosaiti ilikuwa imewatolea. Kupitia halmashauri hiyo, mipango ingeratibiwa ili kukusanya wafanyakazi stadi waliohitajiwa kutoka miongoni mwa ndugu na dada katika kazi za ufundi 65 waliokuwa tayari wamejitolea kusaidia kwenye miradi hiyo.
Kadiri taratibu zilivyofanywa kuwa bora zaidi, iliwezekana kupunguza idadi ya wafanyakazi waliohusika katika ujenzi wowote ule mmoja. Badala ya kuwa na maelfu penye ujenzi ama wakitazama ama wakitoa utumishi wao mbalimbali, ni mara chache sana walipokuwapo zaidi ya 200 penye ujenzi kwa wakati wowote ule mmoja. Badala ya kutumia mwisho-juma wote pale, wafanyakazi walikuwapo wakati tu stadi zao hususa zilipohitajiwa. Hivyo walikuwa na wakati zaidi wa kutumia pamoja na familia zao na wa kufanya utendaji pamoja na makutaniko ya kwao. Wakati ndugu wenyeji walipokuwa wanaweza kufanya kazi fulani kwa wakati mzuri, mara nyingi ilionekana kuwa yafaa zaidi kuleta kikundi cha ujenzi wa haraka wakati tu wa zile kazi ambazo walihitajiwa sana kufanya.
Ijapokuwa kazi yote ilisonga mbele kwa mwendo wenye kushangaza, hilo halikuwa ndilo jambo muhimu. Jambo muhimu zaidi lilikuwa kuandaa ujenzi bora wa Majumba ya Ufalme yenye kiasi yaliyokusudiwa kutimiza mahitaji ya mahali. Upangaji-mambo wa uangalifu ulifanywa ili kutimiza jambo hilo huku gharama zikiwa chini iwezekanavyo. Hatua zilichukuliwa kuhakikisha kwamba usalama ulifikiriwa zaidi—usalama wa wafanyakazi, majirani, wapita njia, na watumiaji wa wakati ujao wa Jumba la Ufalme.
Ripoti kuhusu mpango huo wa kujenga Majumba ya Ufalme zilipofikia nchi nyinginezo, ofisi za tawi za Sosaiti ambazo ziliamini kwamba ungekuwa wenye kufaidi katika maeneo yazo ziliandaliwa habari kamili zilizohitaji. Kufikia 1992, Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa zilizowekwa rasmi na Sosaiti zilikuwa zikisaidia ujenzi wa Majumba ya Ufalme katika nchi kama vile Afrika Kusini, Argentina, Australia, Japani, Kanada, Mexico, Ufaransa, Hispania, Uingereza, na Ujerumani. Njia za ujenzi zilipatanishwa na hali za mahali. Msaada ulipohitajiwa kutoka kwa tawi jingine kwa ajili ya ujenzi wa Jumba la Ufalme, huo ulipangwa kupitia ofisi ya makao makuu ya Sosaiti. Katika sehemu fulani za ulimwengu, majumba mapya yalikuwa yakijengwa kwa siku kadhaa; kwingineko, kwa majuma kadhaa au labda miezi michache. Kwa kupanga mambo kwa uangalifu na jitihada zilizoratibiwa, bila shaka wakati uliotakwa ili kuandaa Jumba la Ufalme jipya ulikuwa ukipunguzwa.
-
-
Kujenga Pamoja Duniani PoteMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 320, 321]
Kufanya Kazi Pamoja ili Kujenga Haraka Majumba ya Ufalme
Maelfu ya makutaniko mapya huundwa kila mwaka. Katika visa vingi, Majumba ya Ufalme mapya hujengwa na Mashahidi wenyewe. Picha hizi zilipigwa wakati wa ujenzi wa Jumba la Ufalme katika Connecticut, Marekani, katika 1991
Ijumaa, saa 1:40 asubuhi
Ijumaa, saa 6 adhuhuri
Jumamosi, saa 1:41 jioni
Kazi kubwa yakamilika, Jumapili, saa 12:10 jioni
Wamtegemea Yehova kwa baraka yake, na huchukua wakati kuzungumzia shauri kutoka Neno lake
Wote ni wenye kujitolea wasiolipwa, wenye furaha kufanya kazi mmoja kando ya mwenzake
[Picha katika ukurasa wa 327]
Majumba ya Ufalme Katika Nchi Mbalimbali
Mahali pa mikutano patumiwapo na Mashahidi wa Yehova kwa kawaida huwa penye kiasi. Ni safi, penye starehe, katika mazingira yenye kuvutia
Peru
Filipino
Ufaransa
Jamhuri ya Korea
Japani
Papua New Guinea
Ireland
Kolombia
Norway
Lesotho
-