Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Walijaribu Kuwazuia Watu Wasilipate Neno la Mungu
    Amkeni!—2011 | Desemba
    • Baadaye, Kilatini kiliacha kuwa lugha ya kawaida. Ni watu wenye elimu tu walioendelea kutumia Kilatini, na Kanisa Katoliki lilipinga mbinu za kutafsiri Biblia katika lugha nyingine. Viongozi wa kidini walisisitiza kwamba Biblia ilifaa tu kuwa katika lugha ya Kiebrania, Kigiriki, na Kilatini.a

      Migawanyiko Katika Kanisa na Kutafsiriwa kwa Biblia

      Katika karne ya tisa W.K., Methodius na Cyril, wamishonari Wathesalonike waliokuwa wametumwa na Kanisa la Mashariki huko Byzantium, walipendekeza kwamba Kislavonia kitumiwe katika kanisa. Kusudi lao lilikuwa kuwawezesha watu wa Slavonia wa Ulaya Mashariki kujifunza kumhusu Mungu katika lugha yao wenyewe kwa kuwa hawakuelewa Kigiriki au Kilatini.

      Hata hivyo, wamishonari hao walikabili upinzani mkali kutoka kwa makasisi Wajerumani, ambao walijaribu kulazimisha kwamba Kilatini kitumiwe ili kuzuia Ukristo wa Byzantium usienee. Kwa wazi, siasa zilikuwa muhimu kwao kuliko watu kupata elimu ya kidini. Mizozo kati ya sehemu ya Magharibi na ya Mashariki ya dini zinazodai kuwa za Kikristo ulifanya Kanisa Katoliki na Kanisa la Othodoksi la Mashariki zigawanyike katika mwaka wa 1054.

      Kuzuia Biblia Isitafsiriwe

      Mwishowe, Kanisa Katoliki likaanza kuona Kilatini kuwa lugha takatifu. Kwa sababu hiyo, katika mwaka wa 1079 Vratislaus, dyuki wa Bohemia, alipoandika barua akiomba ruhusa ya kutumia Kislavonia katika ibada kanisani, Papa Gregory wa Saba alimjibu hivi: “Hatuwezi kwa njia yoyote kukubali ombi hili.” Kwa nini?

      “Kwa wale wanaochunguza jambo hili kwa uangalifu,” akasema Gregory, “ni wazi kwamba ilimpendeza Mungu kufanya sehemu fulani ya Maandiko Matakatifu isieleweke kabisa kwa sababu, ikiwa kila mtu angeelewa kila kitu, basi [Maandiko] yangefanywa kuwa ya kawaida tu na kuvunjiwa heshima au watu wasio na akili nyingi wangeyaelewa vibaya na hivyo waasi.”

      Watu wa kawaida hawangeweza kupata Biblia kwa urahisi, na ilipaswa kuwa hivyo. Msimamo huo uliwafanya makasisi waendelee kuwa na mamlaka juu ya watu wa kawaida. Hawakutaka watu wa kawaida wachunguze mambo ambayo waliona kuwa ni ya makasisi tu.

      Mnamo 1199, Papa Innocent wa Tatu aliandika kuhusu watu walioonwa kuwa wazushi ambao walitafsiri Biblia katika Kifaransa na wakaamua kuwa na mazungumzo kati yao kuihusu. Innocent alitumia maneno haya ya Yesu kuwahusu: “Msiwape mbwa kitu kitakatifu, wala msitupe lulu zenu mbele ya nguruwe.” (Mathayo 7:6) Kwa nini alikuwa na maoni hayo? “Ili mtu wa kawaida na ambaye hana elimu asiwe na kimbelembele cha kujifunza Maandiko matakatifu yaliyotukuka, au kuwahubiria watu kuyahusu.” Mara nyingi, wale waliopinga amri ya papa walipelekwa kwa watesaji ambao waliwalazimisha waungame kwamba wao ni wazushi. Wale waliokataa kukana msimamo wao waliteketezwa wakiwa hai.

      Wakati wa kile kipindi kirefu cha kuwazuia watu wasiipate na kuisoma Biblia, barua ya Papa Innocent ilitumiwa mara nyingi ili kutetea wazo la kwamba Biblia haipaswi kutumiwa wala kutafsiriwa katika lugha nyingine. Punde tu baada ya amri yake kutolewa, Biblia katika lugha nyingine zikaanza kuteketezwa, na pia watu fulani waliomiliki Biblia waliteketezwa. Katika karne zilizofuata, maaskofu na watawala wa nchi za Ulaya zilizokuwa chini ya udhibiti wa Kanisa Katoliki walitumia njia yoyote waliyoweza ili kuhakikisha kwamba marufuku yaliyowekwa na Papa Innocent wa Tatu yalifuatwa.

      Viongozi wa Kanisa Katoliki walijua kwamba mafundisho mengi ya dini hiyo hayakutegemea Biblia bali yalitegemea mapokeo ya kanisa. Bila shaka, hiyo ilikuwa sababu moja iliyowafanya wawazuie waumini wao wasiipate Biblia. Iwapo wangeisoma basi wangetambua kwamba mafundisho ya kanisa yalipingana na Maandiko.

  • Walijaribu Kuwazuia Watu Wasilipate Neno la Mungu
    Amkeni!—2011 | Desemba
    • a Inaonekana kwamba wazo hilo lilitokana na maandishi ya askofu Mhispania, Isidore wa Seville (560-636 W.K.), aliyesema hivi: “Kuna lugha tatu takatifu, Kiebrania, Kigiriki, na Kilatini, na hizo ndizo lugha kuu ulimwenguni pote. Sababu ni kwamba shtaka dhidi ya Bwana lililoandikwa juu ya msalaba na Pilato lilikuwa katika lugha hizo tatu.” Bila shaka, uamuzi wa kuandika shtaka hilo katika lugha hizo tatu ulifanywa na Waroma wapagani. Uamuzi huo haukutoka kwa Mungu.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki