Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Kiongozi Wenu Ni Mmoja, Kristo”
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Septemba 15
    • “Kiongozi Wenu Ni Mmoja, Kristo”

      “Msiitwe ‘viongozi,’ kwa maana Kiongozi wenu ni mmoja, Kristo.”—MT. 23:9, 10.

      1. Mashahidi wa Yehova wanamtambua nani kuwa Kiongozi wao, na kwa nini?

      MAKANISA yanayodai kuwa ya Kikristo yana viongozi wa kibinadamu, kama vile papa wa Roma, wazee na makasisi wa majimbo wa makanisa ya Othodoksi ya Mashariki, na viongozi wa dini nyingine. Mashahidi wa Yehova hawamtambui mwanadamu yeyote kuwa kiongozi wao. Wao si wanafunzi au wafuasi wa mwanadamu yeyote. Hilo linapatana na maneno haya ya kinabii ya Yehova kumhusu Mwana wake: “Tazama! Nimemtoa kuwa shahidi kwa vikundi vya mataifa, kuwa kiongozi na kamanda kwa vikundi vya mataifa.” (Isa. 55:4) Kutaniko la kimataifa la Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao, “kondoo wengine,” hawataki kiongozi mwingine ila tu yule ambaye Yehova amewapa. (Yoh. 10:16) Wanatii maneno haya ya Yesu: “Kiongozi wenu ni mmoja, Kristo.”—Mt. 23:10.

      Mkuu wa Kiroho wa Israeli

      2, 3. Mwana wa Mungu alifanya kazi gani katika Israeli?

      2 Karne nyingi kabla ya kuanzishwa kwa kutaniko la Kikristo, Yehova alimtumia malaika kuwaongoza watu wake wa taifa la Israeli. Baada ya kuwatoa Waisraeli Misri, Yehova aliwaambia hivi: “Tazama, ninamtuma malaika mbele yako ili akuongoze barabarani na kukuingiza mahali ambapo nimetayarisha. Jiangalie kwa sababu yake na kuitii sauti yake. Usijiendeshe kwa kumwasi yeye, kwa maana hatawasamehe kosa lenu; kwa sababu jina langu limo ndani yake.” (Kut. 23:20, 21) Ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba malaika huyo ambaye ‘jina la Yehova lilikuwa ndani yake,’ alikuwa Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu.

      3 Kabla ya kuzaliwa akiwa mwanadamu, inaonekana kwamba Mwana wa Mungu aliitwa Mikaeli. Katika kitabu cha Danieli, Mikaeli anaitwa ‘yule mkuu wa watu wa Danieli,’ Israeli. (Dan. 10:21) Mwanafunzi Yuda anaonyesha kwamba Mikaeli alihusika katika shughuli za Waisraeli kabla ya siku za Danieli. Baada ya kifo cha Musa, inaonekana kwamba Shetani alikusudia kuutumia mwili wa Musa ili kuendelea kwa njia fulani kujitafutia faida zake mwenyewe. Huenda alitaka kufanya hivyo kwa kuwachochea Waisraeli waabudu sanamu. Mikaeli aliingilia kati ili kuzuia jambo hilo lisitokee. Yuda anasema hivi: “Wakati Mikaeli, yule malaika mkuu alipokuwa na tofauti na Ibilisi na kubishana naye juu ya mwili wa Musa, yeye hakuthubutu kumhukumu kwa matukano, bali alisema: ‘Yehova na akukemee.’” (Yuda 9) Muda mfupi baadaye, kabla ya kuzingirwa kwa Yeriko, bila shaka Mikaeli, yule “mkuu wa jeshi la Yehova,” ndiye aliyemtokea Yoshua na kumhakikishia kwamba Mungu alikuwa pamoja naye. (Soma Yoshua 5:13-15.) Wakati roho mmoja mwovu mkuu alipojaribu kumzuia malaika kwenda kumpelekea nabii Danieli ujumbe fulani wa maana, Mikaeli, yule malaika mkuu, alimsaidia malaika huyo.—Dan. 10:5-7, 12-14.

      Kiongozi Aliyetabiriwa Anafika

      4. Ni unabii gani ambao ulitolewa kuhusu kuja kwa yule Masihi?

      4 Kabla ya tukio hilo, Yehova alikuwa amemtuma malaika wake Gabrieli kwa nabii Danieli ili ampe unabii kuhusu kuja kwa “Masihi aliye Kiongozi.” (Dan. 9:21-25)a Kwa wakati unaofaa kabisa, mwishoni mwa mwaka wa 29 W.K., Yesu alibatizwa na Yohana. Roho takatifu ilimiminwa juu ya Yesu, na hivyo kumfanya kuwa Mtiwa-Mafuta, yaani, Kristo, yule Masihi. (Mt. 3:13-17; Yoh. 1:29-34; Gal. 4:4) Akiwa Masihi, Yesu angekuja kuwa Kiongozi asiye na kifani.

      5. Kristo alitenda jinsi gani akiwa Kiongozi wakati wa huduma yake duniani?

      5 Tangu mwanzo wa huduma yake duniani, Yesu alijithibitisha kuwa “Masihi aliye Kiongozi.” Baada ya siku chache tu, Yesu alianza kuwakusanya wanafunzi, na akafanya muujiza wake wa kwanza. (Yoh. 1:35–2:11) Wanafunzi wake walimfuata aliposafiri kotekote nchini, akihubiri habari njema ya Ufalme. (Luka 8:1) Aliwazoeza katika kazi ya kuhubiri na akawaongoza katika kuhubiri na kufundisha, na hivyo akawawekea mfano mzuri. (Luka 9:1-6) Wazee Wakristo leo wanapaswa kumwiga katika jambo hilo.

      6. Kristo alijithibitisha katika njia gani kuwa Mchungaji na Kiongozi?

      6 Yesu alionyesha sifa yake nyingine akiwa kiongozi kwa kujilinganisha na mchungaji mwenye upendo. Wachungaji wa mashariki wanawaongoza kihalisi wanyama wao. Katika kitabu kimoja (The Land and the Book), W. M. Thomson aliandika hivi: “Mchungaji anaenda mbele, si kuonyesha njia tu, bali kuona ikiwa njia hiyo inafaa na ni salama. . . . Akiwa na fimbo [yake] anawaongoza na kuwaelekeza wanyama kwenye malisho mazuri, naye anawalinda kutokana na maadui.” Akionyesha kwamba yeye ni Mchungaji wa kweli na Kiongozi, Yesu alisema hivi: “Mimi ndiye mchungaji mwema; mchungaji mwema huitoa nafsi yake kwa ajili ya kondoo. Kondoo wangu huisikiliza sauti yangu, nami ninawajua, nao wananifuata.” (Yoh. 10:11, 27) Kupatana na maneno yake, Yesu alikufa kifo cha kidhabihu kwa ajili ya kondoo wake, lakini Yehova “alimfufua ili awe kiongozi na Mwokozi.”—Mdo. 5:31, New Jerusalem Bible; Ebr. 13:20.

      Mwangalizi wa Kutaniko la Kikristo

      7. Yesu analiongoza kutaniko la Kikristo kupitia nini?

      7 Muda mfupi kabla ya kupanda mbinguni, Yesu aliyefufuliwa aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” (Mt. 28:18) Kwa uwezo wa Yehova, Yesu aliwapa wanafunzi wake roho takatifu ili iwatie nguvu katika kweli ya Kikristo. (Yoh. 15:26) Yesu aliwamiminia roho hiyo Wakristo wa mapema siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. (Mdo. 2:33) Kutaniko la Kikristo lilianzishwa wakati huo ambao roho takatifu ilimiminwa. Huko mbinguni, Yehova alimweka Mwana wake kuwa kiongozi juu ya kutaniko lote duniani. (Soma Waefeso 1:22; Kol. 1:13, 18.) Yesu analiongoza kutaniko la Kikristo kupitia roho takatifu ya Yehova, na ana malaika ambao ‘walitiishwa kwake.’—1 Pet. 3:22.

      8. Katika karne ya kwanza, Kristo alitumia nani duniani ili kuwaongoza wanafunzi wake, na anatumia nani leo?

      8 Pia, kupitia roho takatifu, Kristo alitoa “zawadi katika wanadamu,” wengine ‘wakiwa wachungaji na walimu’ katika kutaniko. (Efe. 4:8, 11) Mtume Paulo aliwahimiza hivi waangalizi Wakristo: “Jiangalieni ninyi wenyewe na kundi lote, ambalo roho takatifu imewaweka ninyi rasmi kuwa waangalizi kati yake, kulichunga kutaniko la Mungu.” (Mdo. 20:28) Kutaniko la Kikristo lilipoanza, waangalizi hao wote walikuwa wanaume waliotiwa mafuta kwa roho. Mitume na wazee wa kutaniko la Yerusalemu walikuwa baraza linaloongoza. Kristo aliwatumia kuongoza kundi lote la “ndugu” zake watiwa-mafuta duniani. (Ebr. 2:11; Mdo. 16:4, 5) Katika wakati huu wa mwisho, Kristo amemkabidhi “mali zake zote,” yaani, faida zake zote za Ufalme duniani, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” na mwakilishi wa mtumwa huyo, Baraza Linaloongoza, ambacho ni kikundi cha wanaume Wakristo watiwa-mafuta. (Mt. 24:45-47) Watiwa-mafuta na waandamani wenzao, kondoo wengine, wanatambua kwamba wanapofuata uongozi wa Baraza Linaloongoza la siku zetu, kwa kweli wanamfuata Kiongozi wao, Kristo.

      Kristo Anaanzisha Kazi ya Kuhubiri

      9, 10. Kristo aliongoza mambo jinsi gani katika kueneza habari njema ya Ufalme?

      9 Tangu mwanzoni, Yesu mwenyewe aliongoza kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri na kufundisha. Aliweka utaratibu ambao ungefuatwa katika kuhubiri habari njema ya Ufalme kwa wakaaji wa dunia. Wakati wa huduma yake, aliwaagiza hivi mitume wake: “Msiende katika barabara ya mataifa, na msiingie katika jiji la Wasamaria; bali, badala ya hivyo, nendeni kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli. Mnapoenda, hubirini, mkisema, ‘Ufalme wa mbinguni umekaribia.’” (Mt. 10:5-7) Walihubiri ujumbe huo kwa bidii kati ya Wayahudi na watu waliogeuzwa imani, hasa baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K.—Mdo. 2:4, 5, 10, 11; 5:42; 6:7.

      10 Baadaye, kupitia roho takatifu, Yesu alieneza kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme kwa Wasamaria na kisha kwa watu wengine wasio Wayahudi. (Mdo. 8:5, 6, 14-17; 10:19-22, 44, 45) Akiwa na nia ya kueneza habari njema katikati ya mataifa, Yesu mwenyewe alimchochea Sauli wa Tarso kuwa Mkristo. Yesu alimwagiza hivi mwanafunzi wake Anania: “Ondoka, uende kwenye barabara inayoitwa Nyoofu, na kwenye nyumba ya Yuda tafuta mtu anayeitwa jina Sauli, kutoka Tarso. . . . Ondoka uende, kwa sababu mtu huyu ni chombo kilichochaguliwa kwangu ili kupeleka jina langu kwa mataifa na vilevile kwa wafalme na wana wa Israeli.” (Mdo. 9:3-6, 10, 11, 15) “Mtu huyu” alikuja kuwa mtume Paulo.—1 Tim. 2:7.

      11. Kristo alipanua jinsi gani kazi ya kuhubiri akitumia roho takatifu?

      11 Wakati ulipofika wa kupanua kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme katikati ya mataifa yasiyo ya Kiyahudi, Paulo alipata mwongozo kutoka mbinguni wa kwenda katika Asia Ndogo na Ulaya kwa ajili ya safari za umishonari. Simulizi la Luka katika Matendo linasema hivi: “Walipokuwa [manabii na walimu Wakristo katika kutaniko la Antiokia ya Siria] wakimhudumia Yehova hadharani na kufunga, roho takatifu ikasema: ‘Kati ya watu wote wekeni kando Barnaba na Sauli kwa ajili yangu kwa kazi ambayo nimewaitia wao.’ Ndipo wakafunga na kusali na kuweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.” (Mdo. 13:2, 3) Yesu mwenyewe alimwita Sauli wa Tarso kuwa “chombo [Chake] kilichochaguliwa” ili kulipeleka jina Lake kwa mataifa; hivyo, nguvu hiyo mpya kwa kazi ya kutoa ushahidi ilitoka kwa Kristo, ambaye ni Kiongozi wa kutaniko. Wakati wa safari ya pili ya Paulo ya umishonari ilikuwa wazi kwamba Yesu alikuwa akitumia roho takatifu ili kuongoza kazi ya kuhubiri. Simulizi hilo linasema kwamba “roho ya Yesu,” yaani, Yesu alimwongoza Paulo na wasafiri wenzake kupitia roho takatifu, kuamua wakati na mahali ambapo wangeenda, na walipata maono ambayo yaliwaelekeza Ulaya.—Soma Matendo 16:6-10.

      Uongozi wa Yesu Juu ya Kutaniko Lake

      12, 13. Kitabu cha Ufunuo kinaonyesha jinsi gani kwamba Kristo anachunguza kwa makini mambo yanayotendeka katika kila kutaniko?

      12 Yesu alichunguza kwa makini mambo yaliyokuwa yakitendeka katika makutaniko ya wafuasi wake watiwa-mafuta katika karne ya kwanza W.K. Alijua vizuri sana hali ya kiroho ya kila kutaniko. Jambo hilo linaonekana wazi hasa tunaposoma Ufunuo sura ya 2 na ya 3. Anataja makutaniko saba yaliyo katika Asia Ndogo. (Ufu. 1:11) Tuna kila sababu ya kuamini kwamba alijua pia hali ya kiroho ya makutaniko mengine ya wafuasi wake yaliyokuwa duniani wakati huo.—Soma Ufunuo 2:23.

      13 Yesu aliyapongeza makutaniko mengine kwa sababu ya uvumilivu wao, uaminifu chini ya majaribu, ushikamanifu kwa neno lake, na kwa kuwakataa waasi-imani. (Ufu. 2:2, 9, 13, 19; 3:8) Kwa upande mwingine, alitoa mashauri makali kwa makutaniko fulani kwa sababu upendo wao kumwelekea ulikuwa umepoa, pia yaliruhusu ibada ya sanamu, uasherati, na madhehebu kati yao. (Ufu. 2:4, 14, 15, 20; 3:15, 16) Akiwa mwangalizi wa kiroho mwenye upendo, hata kwa wale ambao aliwashauri kwa ukali, Yesu alisema hivi: “Wale wote ninaowapenda, mimi huwakaripia na kuwatia nidhamu. Kwa hiyo uwe mwenye bidii na utubu.” (Ufu. 3:19) Ingawa alikuwa mbinguni, Yesu alikuwa akiyaongoza makutaniko ya wanafunzi wake duniani kupitia roho takatifu. Mwishoni mwa ujumbe mbalimbali kwa makutaniko hayo, alisema hivi: “Yeye aliye na sikio na asikie yale ambayo roho inayaambia makutaniko.”—Ufu. 3:22.

      14-16. (a) Yesu amejithibitisha jinsi gani kuwa Kiongozi mwenye ujasiri wa watu wa Yehova duniani? (b) Kumekuwa na matokeo gani kwa sababu ya Yesu kuwa “pamoja” na wanafunzi wake “siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo”? (c) Tutazungumzia nini katika habari inayofuata?

      14 Tumeona kwamba Mikaeli (Yesu) alijithibitisha kuwa Kiongozi wa Israeli ambaye ni malaika mwenye nguvu. Baadaye, Yesu alikuwa Kiongozi mwenye ujasiri na Mchungaji mwenye upendo wa wanafunzi wake wa mapema. Wakati wa huduma yake duniani, aliongoza katika kazi ya kuhubiri. Na baada ya kufufuliwa, aliongoza moja kwa moja kazi ya kueneza habari njema ya Ufalme.

      15 Kupitia roho takatifu, mwishowe Yesu angepanua kazi ya kutoa ushahidi mpaka kwenye miisho ya dunia. Kabla ya kupanda mbinguni, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8; soma 1 Petro 1:12.) Chini ya mwongozo wa Kristo, ushahidi mkubwa ulitolewa katika karne ya kwanza.—Kol. 1:23.

      16 Lakini Yesu mwenyewe alionyesha kwamba kazi hiyo ingeendelea mpaka wakati wa mwisho. Baada ya kuwaamuru wafuasi wake wahubiri na kufanya wanafunzi kutoka katika mataifa yote, Yesu aliwaahidi hivi: “Mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:19, 20) Tangu apewe mamlaka ya kifalme mwaka wa 1914, Kristo yupo “pamoja” na wanafunzi wake kuliko wakati mwingine wowote naye anatenda akiwa Kiongozi wao. Habari inayofuata itazungumzia utendaji wake mwingi tangu mwaka wa 1914.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kwa habari zaidi kuhusu unabii huo, ona sura ya 11 ya kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli!

  • Kiongozi Wetu Anayetenda kwa Bidii Leo
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Septemba 15
    • Kiongozi Wetu Anayetenda kwa Bidii Leo

      “Akaenda akishinda na kukamilisha ushindi wake.”—UFU. 6:2.

      1, 2. (a) Utendaji wa kifalme wa Kristo tangu mwaka wa 1914 unaonyeshwa jinsi gani katika Biblia? (b) Ni hatua gani ambazo Kristo amechukua tangu awekwe rasmi kuwa mfalme?

      KRISTO aliwekwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Kimasihi wa Yehova mwaka wa 1914. Tunawazia yeye ni nani leo? Je, tunawazia yeye ni mfalme mwenye kutafakari ambaye ameketi juu ya kiti chake cha ufalme, akitazama chini mara kwa mara ili kuona jinsi kutaniko lake linavyoendelea? Ikiwa tunawazia hivyo, tunapaswa kubadili maoni yetu. Katika Zaburi na katika kitabu cha Ufunuo anaonyeshwa akiwa mfalme mwenye nguvu aliye juu ya farasi, naye anaenda “akishinda na kukamilisha ushindi wake,” akiendelea ‘kufanikiwa’ mpaka mwisho.—Ufu. 6:2; Zab. 2:6-9; 45:1-4.

      2 Hatua ya kwanza ya kifalme ambayo Kristo alichukua baada ya kuwekwa rasmi kuwa mfalme ni kumshinda yule “joka mkubwa na malaika zake.” Akiwa malaika mkuu Mikaeli, na akiongoza malaika wake, Kristo alimtupa Shetani na roho wake waovu kutoka mbingu takatifu na kuwazuilia kwenye ujirani wa dunia. (Ufu. 12:7-9) Kisha, katika daraka lake akiwa ‘mjumbe wa Yehova wa agano,’ Yesu alikuja pamoja na Baba yake kukagua hekalu la kiroho. (Mal. 3:1) Alizihukumu dini zinazodai kuwa za Kikristo, sehemu yenye kulaumika zaidi ya “Babiloni Mkubwa,” akazipata na hatia ya kumwaga damu na kufanya uzinzi wa kiroho pamoja na mfumo wa kisiasa wa ulimwengu huu.—Ufu. 18:2, 3, 24.

      Kumsafisha Mtumwa Wake Aliye Duniani

      3, 4. (a) Kristo alitimiza kazi gani akiwa “mjumbe” wa Yehova? (b) Ukaguzi wa hekalu ulifunua nini, na akiwa Kichwa cha kutaniko, Yesu alimweka nani rasmi?

      3 Ukaguzi uliofanywa na Yehova na “mjumbe” wake ulifunua pia kwamba katika ua wa kidunia wa hekalu hilo la kiroho kuna kikundi cha Wakristo wa kweli, ambao hawakuwa sehemu ya dini zinazodai kuwa za Kikristo. Lakini, hata Wakristo hao watiwa-mafuta, au “wana wa Lawi,” walihitaji pia kusafishwa. Ilikuwa tu kama vile nabii Malaki alivyokuwa ametabiri: “[Yehova] ataketi kama msafishaji na mtakasaji wa fedha naye atawatakasa wana wa Lawi; naye atawasafisha kama dhahabu na kama fedha, nao watakuwa kwa Yehova watu wanaotoa toleo la zawadi katika uadilifu.” (Mal. 3:3) Yehova alimtumia ‘mjumbe wake wa agano,’ Kristo Yesu, kuwasafisha Waisraeli hao wa kiroho.

      4 Hata hivyo, Kristo aliwakuta Wakristo haohao waaminifu waliotiwa mafuta wakifanya yote wawezayo ili kuwaandalia watu wa nyumba ya imani chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. Kuanzia mwaka wa 1879 na kuendelea, katika hali zinazofaa na zisizofaa, walikuwa wakitangaza kweli za Biblia kuhusu Ufalme wa Mungu kupitia gazeti hili. Yesu alikuwa ametabiri kwamba wakati ambapo ‘angefika’ kuwakagua watumishi wake wa nyumbani wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo,” angemkuta mtumwa fulani akiwaandalia watumishi hao “chakula chao kwa wakati unaofaa.” Angemtangaza mtumwa huyo kuwa mwenye furaha na ‘angemweka juu ya mali zake zote’ duniani. (Mt. 24:3, 45-47) Akiwa Kichwa cha kutaniko la Kikristo, Kristo amemtumia ‘mtumwa huyo mwaminifu na mwenye busara’ kusimamia mambo ya Ufalme Wake duniani. Ameandaa mwongozo kwa ‘watumishi wa nyumbani,’ watiwa-mafuta na waandamani wao, “kondoo wengine,” kupitia Baraza Linaloongoza.—Yoh. 10:16.

      Kuvuna Dunia

      5. Ni utendaji gani wa kifalme ambao mtume Yohana aliona katika maono?

      5 Katika maono, mtume Yohana aliona jambo lingine ambalo Mfalme wa Kimasihi angefanya katika “siku ya Bwana,” baada ya kuwekwa kuwa mfalme mwaka wa 1914. Yohana aliandika hivi: “Nikaona, na, tazama! wingu jeupe, na mtu fulani kama mwana wa binadamu ameketi juu ya wingu lile, mwenye taji la dhahabu juu ya kichwa chake na mundu mkali mkononi mwake.” (Ufu. 1:10; 14:14) Yohana alimsikia malaika mmoja kutoka kwa Yehova akimwambia Mvunaji huyo atie ndani mundu wake kwa sababu “mavuno ya dunia yameiva kabisa.”—Ufu. 14:15, 16.

      6. Yesu alisema ni hali gani ambayo ingetokea katika wakati wa mwisho?

      6 ‘Mavuno hayo ya dunia’ yanatukumbusha mfano wa Yesu wa ngano na magugu. Yesu alijifananisha na mtu mmoja aliyepanda mbegu za ngano katika shamba lake akitazamia kuvuna ngano nzuri iliyokomaa, ambayo inafananisha “wana wa ufalme,” yaani, Wakristo wa kweli watiwa-mafuta ambao watatawala pamoja naye katika Ufalme wake. Lakini usiku, adui mmoja, “Ibilisi,” alikuja na kupanda magugu katika shamba hilo, “wana wa yule mwovu.” Mpandaji aliwaagiza wafanyakazi wake waache ngano na magugu yakue pamoja mpaka wakati wa mavuno, kwenye “umalizio wa mfumo wa mambo.” Wakati huo, angewatuma malaika wake watenganishe ngano na magugu.—Mt. 13:24-30, 36-41.

      7. Kristo anatimiza jinsi gani kazi ya “mavuno ya dunia”?

      7 Katika kutimiza maono ambayo Yohana alipewa, Yesu amekuwa akiongoza kazi ya mavuno ya ulimwenguni pote. “Mavuno ya dunia” yalianza na kukusanywa kwa mabaki ya wale “wana wa ufalme” 144,000 ambao ni “ngano” inayotajwa katika mfano wa Yesu. Tofauti kati ya Wakristo wa kweli na Wakristo wa uwongo ilionekana wazi zaidi baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, na jambo hilo limechangia kutimizwa kwa sehemu ya pili ya “mavuno ya dunia,” yaani, kukusanywa kwa kondoo wengine. Hao kondoo wengine si “wana wa ufalme,” badala yake, ni “umati mkubwa” wa raia wanaojitiisha kwa kupenda chini ya Ufalme huo. Wanavunwa kutoka kati ya “vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha.” Wanajitiisha chini ya Ufalme wa Kimasihi, ambao unafanyizwa na Kristo Yesu na wale “watakatifu” 144,000 ambao watakuwa pamoja naye katika serikali hiyo ya kimbingu.—Ufu. 7:9, 10; Dan. 7:13, 14, 18.

      Uongozi Katika Makutaniko

      8, 9. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Kristo haoni tu mwenendo wa kutaniko lote kwa ujumla, bali pia anaona mwenendo wa kila mshiriki wa kutaniko? (b) Kama inavyoonyeshwa kwenye ukurasa wa 26, ni ‘mambo gani mazito ya Shetani’ ambayo tunapaswa kuepuka?

      8 Tuliona katika habari iliyotangulia jinsi ambavyo Kristo alikuwa akichunguza kwa makini hali ya kiroho ya kila kutaniko katika karne ya kwanza W.K. Katika siku zetu, akiwa Mfalme anayetawala ambaye amepewa “mamlaka yote mbinguni na duniani,” Kristo Kiongozi wetu anatenda kwa bidii akiwa kichwa cha makutaniko ulimwenguni pote na cha waangalizi wa makutaniko hayo. (Mt. 28:18; Kol. 1:18) Yehova ‘amemfanya kuwa kichwa juu ya vitu vyote kuhusiana na kutaniko’ la watiwa-mafuta. (Efe. 1:22) Akiwa kichwa cha kutaniko, hakuna jambo linalotokea katika kutaniko lolote kati ya makutaniko zaidi ya 100,000 ya Mashahidi wa Yehova ambalo haoni.

      9 Yesu alituma ujumbe huu kwa wazee wa kutaniko la kale la Thiatira: “Haya ndiyo mambo ambayo Mwana wa Mungu anasema, yeye ambaye macho yake ni kama mwali wa moto, . . . ‘Mimi nayajua matendo yako.’” (Ufu. 2:18, 19) Aliwakemea washiriki wa kutaniko hilo kwa sababu ya maisha yao mapotovu na ya anasa kwa kuwaambia hivi: “Mimi ndiye ninayechunguza figo na mioyo, nami nitawapa ninyi mmoja-mmoja kulingana na matendo yenu.” (Ufu. 2:23) Maneno hayo yanaonyesha kwamba Kristo haoni tu mwenendo wa kutaniko lote kwa ujumla, bali pia anaona mwenendo wa kila mshiriki wa kutaniko. Yesu aliwapongeza Wakristo katika Thiatira “ambao hawakujua ‘mambo mazito ya Shetani.’” (Ufu. 2:24) Leo pia anawathamini vijana na wazee, ambao hawajiingizi ndani ya “mambo mazito ya Shetani” kupitia Intaneti au michezo ya video yenye jeuri au kufuata mawazo mapotovu ya wanadamu. Anafurahi kama nini kuona Wakristo wengi leo wakijitahidi na kujidhabihu kadiri wanavyoweza ili kufuata mwongozo wake katika sehemu zote za maisha yao!

      10. Ni nini kinachoonyesha kwamba Kristo anawaongoza wazee wa kutaniko, lakini ni mpango gani ambao wanahitaji kutambua?

      10 Kristo anaongoza kwa upendo makutaniko yake duniani kupitia wazee waliowekwa rasmi. (Efe. 4:8, 11, 12) Katika karne ya kwanza, waangalizi wote walikuwa wanaume waliozaliwa kwa roho. Katika kitabu cha Ufunuo wanafananishwa na nyota zilizo katika mkono wa kuume wa Kristo. (Ufu. 1:16, 20) Leo, wazee wa makutaniko mengi ni washiriki wa kondoo wengine. Wanawekwa rasmi baada ya sala na chini ya mwongozo wa roho takatifu, hivyo tunaweza kusema kwamba wao pia wanaongozwa na Kristo, au wako chini ya mkono wake ambao unaongoza. (Mdo. 20:28) Hata hivyo, wanatambua kwamba Kristo anatumia kikundi kidogo cha wanaume Wakristo watiwa-mafuta wakiwa Baraza Linaloongoza ili kuwaongoza na kuwaelekeza wanafunzi wake duniani.—Soma Matendo 15:6, 28-30.

      “Njoo, Bwana Yesu”

      11. Kwa nini tuna hamu ya kuona Kiongozi wetu akija upesi?

      11 Katika ufunuo ambao mtume Yohana alipewa, Yesu alisema mara nyingi kwamba alikuwa akija upesi. (Ufu. 2:16; 3:11; 22:7, 20) Bila shaka, alikuwa akisema kuhusu kuja kwake ili kutekeleza hukumu juu ya Babiloni Mkubwa na sehemu inayobaki ya mfumo mwovu wa mambo wa Shetani. (2 The. 1:7, 8) Akiwa na hamu ya kuona matukio yote mazuri ajabu yaliyotabiriwa yakitimia, mtume Yohana aliyezeeka alisema hivi: “Amina! Njoo, Bwana Yesu.” Sisi ambao tunaishi mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo tunatamani pia kuona Kiongozi na Mfalme wetu akija katika mamlaka ya Ufalme kulitakasa jina la Baba yake na kuitetea enzi Yake kuu.

      12. Ni kazi gani ambayo Kristo atakamilisha kabla ya pepo za uharibifu kuachiliwa?

      12 Kabla ya Yesu kuja kuliharibu tengenezo linaloonekana la Shetani, watiwa-mafuta wanaobaki kati ya wale 144,000 ambao ni washiriki wa Israeli wa kiroho watatiwa muhuri wa mwisho. Biblia inasema waziwazi kwamba pepo za uharibifu juu ya mfumo wa Shetani hazitaachiliwa kabla ya kazi hiyo ya kuwatia muhuri wale 144,000 kukamilika.—Ufu. 7:1-4.

      13. Kristo ataonyesha wazi jinsi gani kuwapo kwake wakati wa sehemu ya kwanza ya ile “dhiki kuu”?

      13 “Kuwapo” kwa Kristo tangu mwaka wa 1914 hakujatambuliwa na wakaaji wengi wa dunia. (2 Pet. 3:3, 4) Hata hivyo, hivi karibuni ataonyesha wazi kuwapo kwake atakapotekeleza hukumu za Yehova juu ya sehemu mbalimbali za mfumo wa mambo wa Shetani. Uharibifu wa “yule mtu wa uasi-sheria,” yaani, makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo, utakuwa uthibitisho ulio wazi kabisa wa “ufunuo wa kuwapo kwake.” (Soma 2 Wathesalonike 2:3, 8.) Utakuwa uthibitisho ulio wazi kwamba Kristo anatenda akiwa Hakimu au Mwamuzi aliyewekwa rasmi na Yehova. (Soma 2 Timotheo 4:1.) Kuharibiwa kwa sehemu yenye kulaumika zaidi ya Babiloni Mkubwa kutakuwa ndio mwanzo wa uharibifu kamili wa hiyo milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo yenye uovu. Yehova atatia ndani ya mioyo ya viongozi wa kisiasa wazo la kumharibu kahaba huyo wa kiroho. (Ufu. 17:15-18) Hiyo itakuwa sehemu ya kwanza ya ile “dhiki kuu.”—Mt. 24:21.

      14. (a) Kwa nini sehemu ya kwanza ya ile dhiki kuu itafupishwa? (b) “Ishara ya Mwana wa binadamu” itamaanisha nini kwa watu wa Yehova?

      14 Yesu alisema kwamba siku za dhiki hiyo zitafupishwa “kwa sababu ya wale waliochaguliwa,” yaani, mabaki ya Wakristo watiwa-mafuta ambao bado wako duniani. (Mt. 24:22) Yehova hataruhusu shambulizi hilo la kuiharibu dini ya uwongo liwafagilie mbali Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao, kondoo wengine. Yesu aliongeza kwamba “baada ya ile dhiki ya siku hizo,” kutakuwa na ishara katika jua, mwezi, na nyota, “ndipo ishara ya Mwana wa binadamu itakapoonekana mbinguni.” Hilo litafanya mataifa ya dunia ‘yajipige-pige yenyewe kwa kuomboleza.’ Haitakuwa hivyo kwa watiwa-mafuta, ambao wana tumaini la kuishi mbinguni, na waandamani wao, ambao wana tumaini la kuishi duniani. Wao ‘watasimama wima na kuinua vichwa vyao, kwa sababu ukombozi wao utakuwa umekaribia.’—Mt. 24:29, 30; Luka 21:25-28.

      15. Ni kazi gani ambayo Kristo atafanya anapokuja?

      15 Kabla ya kukamilisha ushindi wake, Mwana wa binadamu anakuja kwa njia nyingine. Alitabiri hivi: “Wakati Mwana wa binadamu atakapofika katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye, ndipo atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu. Na mataifa yote yatakusanyika mbele yake, naye atawatenganisha watu, mmoja kutoka kwa mwenzake, kama vile mchungaji anavyotenganisha kondoo na mbuzi. Naye atawaweka kondoo kwenye mkono wake wa kuume, lakini mbuzi kwenye mkono wake wa kushoto.” (Mt. 25:31-33) Unabii huo unahusu kuja kwa Kristo akiwa Hakimu ili kuwatenganisha watu wa “mataifa yote” katika vikundi viwili: “kondoo,” yaani, wale ambao watakuwa wamewaunga mkono kwa bidii ndugu wa kiroho wa Kristo (Wakristo watiwa-mafuta walio duniani) na “mbuzi,” yaani, wale “wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.” (2 The. 1:7, 8) Kondoo, wanaosemwa kuwa “waadilifu,” watapata “uzima wa milele” duniani, lakini mbuzi “watakatiliwa mbali milele,” yaani, wataharibiwa.—Mt. 25:34, 40, 41, 45, 46.

      Yesu Anakamilisha Ushindi Wake

      16. Kristo Kiongozi wetu atakamilisha ushindi wake jinsi gani?

      16 Baada ya hesabu kamili ya wafalme-makuhani wenzake kutiwa muhuri na kondoo kutambuliwa na kuwekwa kwenye mkono wake wa kuume wa wokovu, Kristo anaweza kuendelea “kukamilisha ushindi wake.” (Ufu. 5:9, 10; 6:2) Akiongoza jeshi lenye nguvu la malaika na, bila shaka, akiwa pamoja na ndugu zake waliofufuliwa, Kristo atauharibu mfumo wote wa Shetani wa kisiasa, kijeshi, na kibiashara duniani. (Ufu. 2:26, 27; 19:11-21) Ushindi wa Kristo utakamilika wakati atakapouharibu mfumo mwovu wa Shetani. Kisha atamtupa Shetani na roho waovu ndani ya abiso kwa muda wa miaka elfu moja.—Ufu. 20:1-3.

      17. Wakati wa Utawala wa ile Miaka Elfu Moja, Kristo atawaongoza kondoo wengine kwenye nini, na tunapaswa kuazimia kufanya nini?

      17 Akizungumza kuhusu “umati mkubwa” wa kondoo wengine, ambao wataokoka ile dhiki kuu, mtume Yohana alitabiri kwamba “Mwana-Kondoo, aliye katikati ya kile kiti cha ufalme, atawachunga, na kuwaongoza kwenye chemchemi za maji ya uzima.” (Ufu. 7:9, 17) Ndiyo, wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu Moja, Kristo ataendelea kuwaongoza kondoo wengine, ambao wanasikiliza kwelikweli sauti yake, naye atawaongoza kwenye uzima wa milele. (Soma Yohana 10:16, 26-28.) Na tuazimie kuendelea kumfuata kwa uaminifu Kiongozi wetu na mfalme sasa na mpaka katika ulimwengu mpya wa Yehova ulioahidiwa!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki