Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Jinsi ya Kusitawisha Tamaa ya Kujifunza
    Amkeni!—2004 | Agosti 8
    • Jinsi ya Kusitawisha Tamaa ya Kujifunza

      “Mfunze mtoto namna ya kuishi vizuri, naye hatasahau njia hiyo hata uzeeni.”—METHALI 22:6, BIBLIA HABARI NJEMA.

      JE, UMEWAHI kuwaambia watoto walale wakati jambo la kupendeza linapotukia? Ijapokuwa wamechoka, wanalia, na hata kukasirika, watajitahidi juu chini kukaa macho na kushiriki jambo hilo. Mwandishi John Holt aliandika hivi: “Uhitaji [wao] wa kutaka kufahamu mambo na kuwa na ustadi wa kuyafanya ni mkubwa sana kama vile uhitaji wao wa kula, kupumzika, au kulala. Nyakati nyingine, uhitaji huo unaweza kuwa mkubwa hata zaidi.”

      Tatizo ni kwamba ni vigumu kwa watoto kudumisha tamaa ya kujifunza katika maisha yao yote, kutia ndani miaka yao ya shule. Ingawa hakuna siri hususa ya mafanikio, kuna njia kadhaa ambazo zimefaulu zinazoweza kutumiwa na wazazi, walimu, na watoto. Hata hivyo, jambo muhimu zaidi ni upendo.

      Upendo Utaboresha Uwezo wa Kujifunza

      Watoto hutamani kupendwa na wazazi wao. Upendo huo huwafanya wahisi wakiwa salama na kuwa tayari zaidi kuwasiliana, kuuliza maswali, na kuchunguza mambo. Upendo huwachochea wazazi kuzungumza na watoto wao kwa ukawaida na kupendezwa na elimu yao. Kulingana na kitabu Eager to Learn—Helping Children Become Motivated and Love Learning, utafiti unaonyesha kwamba “inaonekana wazazi hasa ndio wanaowachochea watoto kujifunza.” Matokeo mazuri zaidi hupatikana wazazi wanaposhirikiana na walimu. Kitabu hicho kinasema: “Tamaa ya watoto ya kujifunza huchochewa sana kunapokuwa na ushirikiano kati ya wazazi na walimu.”

      Wazazi pia huchochea uwezo wa watoto wa kujifunza. Katika uchunguzi wa familia 43, uliofanywa kwa muda mrefu na kuripotiwa katika kitabu Inside the Brain, watafiti “waligundua kwamba watoto waliozungumziwa mara nyingi [katika miaka yao mitatu ya kwanza], walikuwa na akili sana kuliko wale ambao hawakuzungumziwa na wazazi wao mara nyingi.” Kitabu hicho kinaongeza kwamba “wazazi wanaozungumza na watoto wao mara nyingi huwasifu kwa mafanikio yao, hujibu maswali yao, huwapa mwongozo badala ya kuwaamuru, na hutumia maneno mengi kwa njia mbalimbali.” Ikiwa wewe ni mzazi, je, unazungumza na watoto wako kwa ukawaida na kwa njia yenye kujenga?

      Upendo Ni Wenye Fadhili na Wenye Kuelewa

      Uwezo na vipawa vya watoto hutofautiana. Bila shaka, haitafaa wazazi waruhusu tofauti hizo ziathiri upendo wao kwa watoto wao. Hata hivyo, katika ulimwengu wa leo, watu hutambuliwa kwa sababu ya uwezo wao, na hilo linaweza kuwafanya watoto fulani “wafikiri kwamba ili watambuliwe, ni lazima wafanye mambo vizuri kuliko wengine,” chasema kitabu Thinking and Learning Skills. Licha ya kuwafanya watoto “waogope sana kutofanikiwa,” maoni hayo yanaweza pia kuwafanya wahangaike na kufadhaika bila sababu. Gazeti India Today linasema kwamba visa vya vijana kujiua huko India vimeongezeka mara tatu katika miaka 25 iliyopita, hasa kwa sababu ya mahangaiko yanayotokana na mkazo wa kufanya vizuri shuleni na kutotegemezwa na familia.

      Pia watoto wanaweza kuathiriwa kihisia wanapoitwa “wapumbavu” au “wajinga.” Maneno hayo ya ukatili huwavunja moyo kujifunza. Hata hivyo, mzazi anapaswa kuonyesha upendo wenye fadhili nyakati zote na kuendeleza tamaa ya mtoto ya kiasili ya kujifunza kulingana na uwezo wake, bila kumfanya aogope kuaibishwa. (1 Wakorintho 13:4) Ikiwa mtoto ana tatizo la kujifunza, wazazi wenye upendo hujaribu kusaidia bila kumfanya mtoto ahisi kwamba yeye ni mjinga au hafai. Ni kweli kwamba hilo linahitaji subira na busara, lakini matokeo huwa mazuri. Upendo huo unaweza kusitawishwaje? Hatua ya kwanza muhimu ni kuwa na mtazamo wa kiroho.

      Mtazamo wa Kiroho Hutokeza Usawaziko

      Hali ya kiroho inayotokana na Biblia ni muhimu kwa sababu mbalimbali. Kwanza, inatusaidia kuwa na maoni yanayofaa kuhusu elimu ya kilimwengu, yaani, kuiona kuwa muhimu lakini si muhimu zaidi. Kwa mfano, hesabu ina matumizi mengi, lakini haiwezi kumfanya mtu awe na maadili.

      Biblia pia hututia moyo tuwe wenye usawaziko kuhusu wakati tunaotumia katika elimu ya kilimwengu, inaposema hivi: “Hakuna mwisho wa kutungwa kwa vitabu vingi, na kushughulika navyo sana huuchosha mwili.” (Mhubiri 12:12) Ni kweli kwamba watoto wanahitaji elimu nzuri ya msingi, lakini haipaswi kuchukua muda wao wote. Pia wanahitaji wakati wa kufanya mambo mengine yanayofaa, hasa mambo ya kiroho yanayoboresha utu wao.

      Sifa nyingine ya kiroho inayotajwa katika Biblia ni kiasi. (Mika 6:8) Watu wenye kiasi hutambua mipaka yao, nao hawaathiriwi na tamaa ya makuu na mashindano ya ukatili yanayoonekana katika taasisi nyingi za elimu. Gazeti India Today linasema kwamba sifa hizo mbaya “huwafanya watu washuke moyo.” Tuwe vijana au wazee, sisi hufanikiwa zaidi tunapotii mashauri haya ya Biblia yaliyoongozwa na Mungu: “Na tusiwe wenye kujisifu, wenye kuchochea mashindano juu ya mtu na mwenzake, tukioneana wivu.” “Lakini kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine.”—Wagalatia 5:26; 6:4.

      Wazazi wanawezaje kutumia kanuni hizo katika elimu ya watoto wao? Njia moja ni kumtia moyo kila mtoto ajiwekee miradi ya kibinafsi na kuchunguza maendeleo yake mwenyewe. Kwa mfano, ikiwa hivi karibuni mwana wako alifanya mtihani wa hesabu au wa kuandika maneno kwa usahihi, mwombe alinganishe matokeo yake na ya mtihani wa awali. Kisha msifu au umtie moyo inapofaa. Kwa kufanya hivyo, utamsaidia kujiwekea miradi anayoweza kutimiza, kuchunguza maendeleo yake, na kushughulikia udhaifu wowote bila kumlinganisha na wengine.

      Hata hivyo, siku hizi vijana wengi wenye vipawa huamua kutofanya vizuri shuleni kwa sababu ya kuogopa kudhihakiwa. Vijana wengine husema: “Kufanya vizuri shuleni ni ushamba.” Je, mtazamo wa kiroho unaweza kusaidia katika hali hiyo? Bila shaka! Fikiria andiko la Wakolosai 3:23, linalosema: “Kila mfanyacho, fanyeni kwa moyo wote, kwa sababu ya Bwana na si kwa ajili ya mtu.” (BHN) Je, kweli kuna sababu nyingine kubwa zaidi ya kutuchochea kufanya kazi kwa bidii kuliko kumpendeza Mungu? Mtazamo huo mzuri humwezesha mtu kushinda uvutano usiofaa wa marika.

      Wafundishe Watoto Wapende Kusoma

      Kusoma na kuandika ni mambo ya msingi yanayohitajiwa ili kupata elimu nzuri ya kilimwengu na pia ya kiroho. Wazazi wanaweza kuwachochea watoto wao wapende vitabu kwa kuwasomea tangu utotoni. Daphne, anayefanya kazi ya kusahihisha makala zilizoandikwa, anashukuru kwamba wazazi wake walimsomea kwa ukawaida alipokuwa mtoto. Anasema hivi: “Walinisaidia kupenda kusoma. Kwa hiyo, nilijua kusoma kabla sijaanza shule. Wazazi wangu pia walinifundisha kufanya utafiti ili nijitafutie majibu ya maswali yangu. Mpaka sasa mazoezi hayo yananisaidia sana.”

      Kwa upande mwingine, Holt, aliyenukuliwa awali, anaonya kwamba kuwasomea watoto tu “hakutoshi.” Anaongeza hivi: “Ikiwa mzazi na mtoto hawafurahii usomaji huo, basi mtoto hatafaidika. . . . Hata watoto wanaopenda kusomewa kwa sauti . . . hawawezi kufurahia usomaji ikiwa mzazi hafurahii kuwasomea.” Hivyo, Holt anapendekeza kwamba wazazi wachague vitabu wanavyovipenda pia, huku wakikumbuka kwamba huenda watoto wakataka kusomewa vitabu hivyo mara nyingi! Mamilioni ya wazazi ulimwenguni pote hufurahia kuwasomea watoto wao vitabu hivi viwili, Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu na Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Vimeandikwa hasa kwa ajili ya watoto na vina picha nyingi, vinawachochea kufikiri, na kuwafundisha kanuni za Mungu.

      Timotheo, Mkristo wa karne ya kwanza, alibarikiwa kuwa na mama na nyanya waliopendezwa sana na elimu yake, hasa ya kiroho. (2 Timotheo 1:5; 3:15) Timotheo akawa mwenye kuwajibika na kutegemeka—sifa ambazo haziwezi kutokezwa na elimu ya kilimwengu pekee. (Wafilipi 2:19, 20; 1 Timotheo 4:12-15) Leo, katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote kuna vijana wengi wa kiume na wa kike walio kama Timotheo kwa sababu wamezoezwa na wazazi wa kiroho wenye upendo.

      Fundisha kwa Uchangamfu!

      Kitabu Eager to Learn kinasema kwamba mwalimu anayetaka kuwasaidia wengine kupenda kujifunza anapaswa kuwa na “sifa moja, yaani uchangamfu. Walimu wenye uchangamfu huwaonyesha wanafunzi kwamba wanafurahia yale wanayofundisha na jambo hilo huonekana wazi kabisa.”

      Hata hivyo, ni wazi kwamba si wazazi au walimu wote walio wachangamfu. Kwa hiyo, wanafunzi wenye hekima hujaribu kujichochea kwa kuona kujifunza kuwa daraka lao. Kitabu kilichotajwa mapema kinasema, “hakuna mtu atakayekuwa na watoto wetu daima ili kuwasaidia kujifunza, kufanya kazi vizuri, kufikiri, na kujitahidi kuboresha stadi zao.”

      Kwa mara nyingine tena, hilo linakazia kwamba maadili ambayo watoto hujifunza nyumbani ni muhimu kuliko wanayojifunza shuleni. Je, wazazi mnafurahia kujifunza? Je, hali za nyumbani zinawawezesha watoto kujifunza na kukazia mambo ya kiroho? (Waefeso 6:4) Kumbuka kwamba mfano wako na mafundisho yako yatawachochea watoto wako muda mrefu baada ya wao kumaliza shule na kuondoka nyumbani.—Ona sanduku “Familia Zinazofaulu Kujifunza,” kwenye ukurasa wa 7.

      Tambua Kwamba Watu Hujifunza kwa Njia Tofauti

      Ubongo wa kila mtu hufanya kazi kwa njia tofauti; kila mtu ana njia yake ya kujifunza. Mtu mmoja anaweza kufanikiwa anapotumia njia fulani, na huenda mwingine asifanikiwe anapoitumia. Hivyo, Dakt. Mel Levine anasema hivi katika kitabu chake A Mind at a Time: “Tukishughulika na watoto kwa njia ileile, hatuwatendei vizuri. Kila mtoto ana mahitaji yake ya kujifunza; na ana haki ya kutimiziwa mahitaji hayo.”

      Kwa mfano, watu fulani huelewa na kukumbuka mambo vizuri wanapoona picha au michoro. Wengine hupendelea maandishi au mazungumzo, au yote mawili. Levine anasema: “Njia bora ya kukumbuka habari fulani ni kuibadilisha kwa njia fulani. Ikiwa ni picha, ieleze kwa maneno, ikiwa ni maneno, piga picha akilini.” Njia hiyo hufanya kujifunza kunufaishe na kufurahisha pia.

  • Jinsi ya Kusitawisha Tamaa ya Kujifunza
    Amkeni!—2004 | Agosti 8
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

      Familia Zinazofaulu Kujifunza

      Mambo yafuatayo yanaweza kuisaidia familia yako kufaulu kujifunza:

      ◼ Wajulishe watoto wako mara nyingi na kwa upendo kwamba unawatarajia wajiendeshe vyema na kufanya vizuri shuleni

      ◼ Watoto wanapaswa kufahamu kwamba mafanikio yanatokana na kufanya kazi kwa bidii

      ◼ Kujishughulisha wala si kukaa kitako tu

      ◼ Watoto watumie wakati mwingi kila juma kujifunza nyumbani na vilevile kufanya kazi za shule, kusoma ili kujifurahisha, kufanya mambo wanayopenda, kufanya kazi pamoja na familia, kuzoezwa kazi za nyumbani, na kupewa migawo

      ◼ Watoto wanapaswa kuiona familia yao kuwa mahali ambapo wanaweza kutegemezwa na kupata suluhisho la matatizo yao

      ◼ Watoto waelezwe sheria za nyumbani waziwazi na zitekelezwe kwa uthabiti

      ◼ Wazazi wawasiliane na walimu mara nyingi

      ◼ Wazazi wahangaikie hasa maendeleo ya kiroho ya watoto wao

      [Picha]

      Wazazi, je, mnawafundisha watoto kufurahia kujifunza?

      [Hisani]

      Mapendekezo haya yametolewa katika kitabu Eager to Learn—Helping Children Become Motivated and Love Learning.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki